Saturday, January 19, 2019

Kitabu Changu Kutafsiriwa kwa kiSomali

Mara moja moja, katika miaka kadhaa iliyopita, nimekuwa nikiwazia kufanya mpango wa kutafsiriwa kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kwa kiSomali. Niliwazia lugha hiyo kwa kuwafikiria waSomali waishio Marekani. Hapa kuna waSomali wengi kuliko sehemu yoyote duniani ukiachilia mbali Somalia yenyewe. Jimbo hili la Minnesota ninapoishi linaongoza kwa kuwa na waSomali wengi.

Nimekuwa na mahusiano ya miaka mingi na waSomali wa Minnesota, hasa katika miji ya Faribault na Minneapolis. Nimehusika katika kuwashauri kuhusu maisha ya hapa Marekani, mifano ikiwa ni mihadhara yangu Mankato na Faribault.

WaSomali ambao wamesoma kitabu changu wanakipenda sana na wananikumbusha tunapokutana. Mmoja wao ni rafiki yangu Mohamed Dini. Huyu ndiye tumekubaliana akitafsiri kitabu hicho. Yeye ni mmoja wa waSomali wachache sana wanaotambulika katika fani hiyo hapa Minnesota. Kazi hiyo itaanza mwezi huu.

Ni faraja kubwa kwangu kwamba tafsiri hii itakapochapishwa itapunguza kwa kiasi kikubwa matatizo yanayowakabili waSomali Marekani, ambayo ni mara dufu kuliko yanayowakabili waAfrika wengine wengi. Tofauti na waAfrika wengi, waSomali wengi hawajui kiIngereza ambayo ndio lugha ya Marekani. Vile vile, waSomali ni waIslam, dini ambayo ni ya wachache hapa Marekani, na sehemu nyingi hakuna yale ambayo waIslam wanahitaji kwa mujibu wa dini yao. Kuna juhudi zinafanyika, lakini bado hazijatosheleza.

Ninangojea kwa hamu maendeleo ya shughuli hii hadi ifikie lengo.

Saturday, January 12, 2019

Mwongozo wa "Song of Lawino"

Nimechapisha kijitabu ambacho ni mwongozo wa Song of Lawino. Wanafunzi na wasomaji wa fasihi ya Afrika, angalau wa enzi za ujana wangu, wanafahamu kwamba Song of Lawino ni utungo maarufu wa Okot p'Bitek wa Uganda. Mwongozo wangu unaitwa Notes on Okot p'Bitek's Song of Lawino.

Huu ni mwongozo wangu wa pili kuuchapishwa, baada ya Notes on Acebe's Things Fall Apart, mwongozo ambao umekuwa ukitumiwa na wanafunzi na waalimu wa fasihi sehemu mbali mbali duniani kama nilivyowahi kugusia katika blogu hii.

Kila mwongozo unaongelea kazi tajwa lakini pia unagusia kazi zingine za fasihi ili kupanua uwanja wa ufahamu juu ya fasihi. Kila mwongozo unaingiza pia vipengele vya nadharia ya fasihi vinavyohusika katika kazi inayojadiliwa.  Kwa hiyo, kwa kusoma mwongozo moja, mtu anajifunza au anapata fursa ya kutafakri mambo mengi.

Nina nia ya kuandika miongozo mingine ya kazi muhimu za fasihi ya Afrika. Unaweza kujipatia mwongozo huu mpya na vitabu vyangu vingine katika duka la mtandaoni

Friday, January 11, 2019

Wanachuo wa Gustavus Adolphus Wameenda Tanzania

Tarehe 7, nilikwenda kukutana na wanachuo wa Gustavus Adolphus College ambao walikuwa wanaondoka kwenda Tanzania katika programu ya masomo. Hii ni programu ambayo imekuwepo miaka mingi. Wanafunzi wengi zaidi wanasomea uuguzi, na wanakwenda Tanzania ili kuelewa suala la uuguzi linakuwaje katika utamaduni tofauti na wa Marekani.

Nimekuwa nikialikwa kila mara kuongea nao kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni kutokana na kwamba wanasoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na tunapokutana wananiuliza maswali yatokanayo na niliyoandika au mengine. Maswali yalikuwa ya aina mbali mbali, yakiwemo kuhusu mtazamo wa waTanzania juu ya waMarekani na pia kuhusu hali ya kisiasa Tanzania.

Hapa kushoto ninaonekana na viongozi wa msafara, Profesa Barbara Zust na Mchungaji Todd Mattson. Profesa Zust ndiye mwaandaji wa kozi na kila mwaka anaweka kitabu changu kama muhimu kwa wanafunzi. Maelezo mafupi ya programu ya mwaka huu ni haya hapa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...