Saturday, December 17, 2022

Cross Cultural Conversation With an American Student

Sophia ni mwanafunzi wangu hapa katika Chuo cha St. Olaf. Ni mfuatiliaji wa maandishi na maongezi yangu YouTube kuhusu tofauti za tamaduni. Siku chache zilizopita, aliniambia kuwa amepata kitabu changu, Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences. Aliniambia kuwa angependa tufanye mahojiano. Leo, tarehe 17 Desemba, tumekutana ofisini mwangu tukaongelea mengi.

Monday, October 24, 2022

Mdau Amechapisha Mapitio ya Kitabu Changu

Tarehe 21 Oktoba, 2022, katika gazeti la The Citizen, Neelam Babul alichapisha mapitio ya kitabu changu. Nimevutiwa na mrejesho wake. Msomaji yeyote anayetoa maoni yake juu ya kitabu changu, yawe maoni ya ainna yoyote, nashukuru.

Saturday, October 1, 2022

Nimekutana na Wasomaji Wangu

Leo mjini Burnsville, Minnesota, nilikutana na wasomaji wangu wawili: Sarah B. Kamsin mwenye asili ya Sudan ya Kusini na Brighid McCarthy kutoka Marekani. Sarah ndiye aliyeandaa mkutano.

Sarah na mimi tumefahamiana tangu Julai 2019, aliponikuta kwenye maonesho ya vitabu mjini Blaine, Minnesota, akaipatia kitabu cha "Africans and Americans: Embracing Cultural Differences." 

Baadaye Sarah alichapisha kitabu cha mashairi yake kiitwacho  "Vita, Babel, Cauliflower," ambacho nilikisoma nikakifurahia, na kisha nikakiandikia uhakiki. Unaweza kuona kisehemu cha uhakiki wangu kwenye tovuti ya Amazon. Sarah ana kipaji kikubwa cha utunzi wa mashairi ya kiIngereza.

Katika maongezi yetu ya leo, nimefahamu kuwa baada ya kusoma kitabu changu cha "Africans and Americans: Embracing Cultural Differences," Sarah  alianza kumwelezea rafiki yake wa miaka mingi Brighid juu yangu na kitabu hiki..

Kutokana na hayo, Brighid alifurahi sana kukutana nami leo. Alikuwa na nakala ya kitabu, kikiwa kimepigiwa mistari kwenye vifungu na sentensi nyingi, kuashiria kuwa amekuwa akisoma kwa uangalifu na tafakuri tele. Nilishangaa anavyokumbuka hata mambo madogo yaliyomo kitabuni.

Tuliongea kwa masaa matatu, na muda mwingi tuliongelea tofauti za tanmadunni nilizozielezea kitabuni. Lakini pia tuliongelea uwezekano wa kushirikiana katika utatuzi wa mahitaji mbali mbali katika jamii za Afrika Mashariki, kama vile elimu na maji. Tumefurahi kugundua kuwa wote tayari tumekuwa tukifanya hayo. Brighid, kwa mfano amekuwa akifanya shughuli hizi Arusha. Tumehamasika kufanya zaidi.

Sunday, September 25, 2022

Mkutano na Mmiliki wa African Travel Seminars

Tarehe 22 Septemba, nilikutana na Georgina Martin Lorencz, mmiliki wa African Travel Seminars, kampuni ya utalii inayopeleka watu sehemu mbali mbali duniani. Huyu mama mwenye asili ya Ghana tunafanana kimtazamo kuhusu utalii. Tunataka utalii unaolinda heshima na utu, unaoboresha maelewano, na usio na hali yoyote ya udhalilishaji na ukoloni mamboleo. Tunataka manufaa ya utalii yaonekane katika jamii inayofikiwa na watalii.

Zaidi ya hayo, Georgina  ni kati ya wale wanaotumia kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika shughuli zao. Kuafiki kwao yale ninayosema kuhusu utamaduni wa waAfrika kunsnifanya nijisikie vizuri. Hiyo juzi nilimkabidhi kitabu changu kipya, Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences.

Kuna mambo muhimu tumepangia kufanya, ikiwemo kufungua njia mpya za utalii Tanzania, kuongezea programu iliyopo Tanzania ya African Travel Seminars. Taarifa zitapatikana kadiri muda unavyokwenda. 

Sunday, September 18, 2022

Tanga Watafakari Changamoto za Tofauti za Tamaduni


Tarehe 11 Juni, 2022, nilikuwa mgeni rasmi katika mkutano wa kwanza wa kikundi cha watu wa mataifa mbali mbali kilichoanzishwa Tanga kwa lengo la kutafakari na kuchambua changamoto za tofauti za tamaduni. Kikundi kinajulikana kama Cross Cultural Dialogue.

Mratibu wa kikundi, Georgina, alikuwa amesoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, wakati niko bado Marekani, akaamua kunialika kuongea nao.

Safari yangu kutoka Marekani nilitua Nairobi, nikapitiliza hadi Mombasa. Kutokea Mombasa, nilishuka Tanga. Nilipumzika siku moja nikisubiri mkutano. Mkutano tulifanyia Hashtag Cafe, na ulifana sana. Wadau walifurahia kunisikiliza, tukabadilishana uzoefu na mitazamo. Nilikuwa nimeleta nakala za vitabu vyangu: Matengo FolktalesAfricans and Americans: Embracing Cultural Differences, na Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences. Wadau walivinunua.

Kuanzishwa kwa Cross Cultural Dialogue ni jambo muhimu sana. Dunia inavyozidi kuwa kijiji, watu wa tamaduni mbali mbali, tupende tusipende, tunajikuta katika mahusiano ya kila aina ambayo huja na changamoto nyingi, ndogo na kubwa, kwa sababu ya tofauti za tamaduni. Tofauti hizi zinaweza kukwamisha au kuharibu mahusiano, iwe ni ya binafsi, biashara, diplomasia, na kadhalika.

Cross Cultural Dialogue wameendelea kukua. Nafurahi wanavyotumia vitabu vyangu kama dira na kichocheo cha tafakari. Mwamko wa aina ya Cross Cultural Dialogue unaleta matumaini kwa hatima ya Tanzania, katika ulimwengu wa leo wa ushindani mkubwa. Kwa wanaopenda, vitabu vinapatikana kwenye dula la A Novel Idea lililoko Slipway, Msasani, na pia katika TFA Center iliyopo Barabara ya Sokoine, Arusha.

Sunday, May 22, 2022

Huenda Nikaandika Kitabu Kingine Kuhusu Tamaduni

Tarehe 25 Agosti, 2021, nilichapisha kitabu, Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differe=-ians and Americans: Embracing Cultural Differences." Baada ya kuchapisha vitabu hivi, niliona sina haja ya kuandika kitabu kingine juu ya tamaduni.

Lakini, wiki kadhaa zilizopita, nilizindua programu ya mtandaoni, "Cross Cultural Conversations," ambayo naendesha kila Jumamosi. Ninaongea kupitia Zoom na kuwashirikisha wasikilizaji katika maongezi juu ya mada mbali mbali kuhusu tofauti baina utamaduni wa Afrika na wa Marekani.
Katika kufanya hivyo, nimejikuta nikizama zaidi katika masuala niliyoongelea katika vitabu vyangu, na ninaibua pia mengine au mitazamo ambayo haikuwemo vitabuni. Nikiendelea namna hii, nitachapisha kitabu kingine, labda kiitwe "Cross Cultural Conversations." Itachukua muda, bila shaka miaka kadhaa.

Friday, May 20, 2022

USHIRIKI WANGU KATIKA MATAMASHA

 

Mimi kama mwandishi, ninashiriki matamasha ya vitabu na tamaduni, kama inavyoonekana pichani. Hii ni fursa kwangu ya kufahamiana na watu, kuwajulisha kuhusu shughuli zangu kama mwalimi na mwandishi, na pia kusikia mawazo na mitazamo yao. Ni fursa pia ya watu kujipatia vitabu vyangu.

Ushiriki wangu kwenye shughuli hizi una manufaa kwangu na kwa jamii. Hayo huelezwa katika vyombo vya habari, na mfano ni huu hapa.

Mimi mwenyewe nimetamka mara kwa mara kuwa nayaona matamasha haya kama darasa, ambamo nafundisha na kujifunza.


Monday, May 16, 2022

VITABU VYANGU, NAFSI YANGU

Vitabu vyangu si vitu vilivyo nje yangu. Ni sehemu ya nafsi yangu, kama kilivyo kichwa changu au ulivyo moyo wangu. Haiwezekani kuvitenganisha na mimi mwenyewe.

Ninaandika vitabu si tu ili watu waifahamu mada, bali pia ili wanifahamu. Kwa hiyo, sielei angani kwa nadharia na hoja zisizofikika kirahisi. Ninaongelea mambo yanayomgusa binadamu. Vitabu hivi ni sauti yangu na pumzi yangu.

Nitakapokuwa siko diniani, vitabu hivi vitaendelea kuongea na walimwengu, vikiwasilisha sauti yangu. Kwa njia ya kazi zao, waandishi tangu kale wametamani na wamefanikiwa kuishi hata baada ya kufariki.

Gilgamesh, shujaa wa kale wa Mesopotamia, alitamani hivyo, akataka kuandika jina lake, lisitoweke. Akina Shakespeare na Shaaban Robert bado tunao, kadhalika akina Tolstoy, Muyaka, Achebe na wengine kwa maelfu.

Wednesday, May 11, 2022

Mpiga Debe Mpya

Nimeanzisha programu ya mazungumzo mtandaoni Zoom ninayoyaita "Cross Cultural Conversations." Nilianza tarehe 16 Aprili, na ninafanya kila Jumamosi, saa kumi na mbili jioni hadi saa moja na nusu kwa saa za Afrika Mashariki.

Siku mojawapo, baada ya mhadhara wangu juu ya "Money in African and American Culture," mhudhuriaji aitwaye Kelly aliweka picha ya vitabu vyangu kwenye ukurasa wake wa Facebook, pamoja na ujumbe huu:

Beautiful afternoon to sit in Miss Samantha's yard! I'm reading work from Joseph Mbele, suggested by my friend Anita. Joseph is leading a recurring Zoom call on Saturday mornings (10 to 11:30) with intriguing conversations, focusing on different topics. My inbox is always open, I'd be happy to share the next Eventbrite link.

Imetokea hivyo, kwamba tangu nianze programu hii, wahudhuriaji wamekuwa wapiga debe wangu wakuu. Wanawaambia wengine na kuwashawishi wahudhurie. Matangazo ya mada ninaweka Facebook siku chache kabla ya mhadhara. Yeyote anakaribishwa kujisajili kwa kutumia linki inayoambatishwa kwenye tangazo.

Monday, April 25, 2022

Mdau Wangu Makini Katutembelea

Leo hapa Chuoni St. Olaf alifika mama mmoja kutoka Togo ambaye anaishi kwenye mji wa mbali kiasi kutoka hapa nilipo. Alimleta binti yake kwenye programu fulani ya wanafunzi. 

Mama huyu ni mdau wangu hodari, kwa maana kwamba ni msomaji wa tangu zamani wa vitabu vyangu na maandishi mengine, na ni mfuatiliaji wa shughuli zangu za kuelimisha jamii. 

Kwenye haya matamasha, huwa sikosi kuwaona waAfrika  wa nchi kama vile Somalia,  Kenya, Ethiopia, Uganda, Sudani, Congo, Nigeria, Togo, Liberia au Ghana. Ninafurahi kuwa wadau kutoka nchi zote hizo wamenunua na wamevutiwa na kitabu changu kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.



Friday, March 18, 2022

Nimekutana na Mdau Wangu Mwingine

Leo nilienda Mall of America kukutana na Tanya, mjumbe wa bodi ya shule za Osseo District. Tulifahamiana miezi kadhaa iliyopita, siku nipotoa mhadhara kwa Rotary Club of Brooklyn Park. Alikuwa mmoja wa wahudhuriaji, na nilimfahamu siku hiyo kama mjumbe wa bodi ya shule za Osseo District.

Nilikuwa nimemwomba tukutane, kwa sababu nilikuwa na mambo ya kumwuliza. Moja ni kuhusu uwezekano wa kujenga uhusiano baina ya shule za Osseo District na shule ya Bukoba, Tanzania, ambayo uongozi wake uliniomba niwatafutie uwezekano huo hapa Marekani.. 

Jambo jingine nililotaka kuongea naye ni muendelezo wa yale machache tuliyogusia siku ya mhadhara wangu, ambao yanahusu kuzuia au kutatua migogoro inyotokea shuleni. Tulikuwa tumakubaliana kwamba tofauti za tamaduni zinachangia tatizo hilo.

Jambo la tatu ni kuwa nilitaka kumpa nakala ya Chickens in the Bus: Embracing Cultural differences. Nilishampa Africans and Americans: Embracing Cultural Differences baada kukutana mara ya kwanza. Ilikuwa ni furaha leo kusaini hiki kitabu na kumkabidhi. Huyu namhesabu kama mdau wangu muhimu.

Tumeongea mengi yanayohusu shule, kuhusu migogoro mashuleni itokanayo na tofauti au changamoto za tofauti za tamaduni na kadhalika. Tumegundua kuwa kwa ujumla tuna mitazamo inayofanana. Tumekubaliana kushirikiana kwa dhati siku zijazo katika kutafuta njia za kutatua changamoto zilizopo.
 

Saturday, March 12, 2022

 WADAU WA UTALII KWENYE MHADHARA WANGU ARUSHA

Tarehe 8 Januari, 2022, nilitoa mhadhara Arusha, mada ikiwa "challenges of cultural differences," yaani changamoto za tofauti za tamaduni. Hii ni mada ambayo naiongelea na kuiandikia sana. Mwandaaji wa mhadhara alikuwa mama Ama, mMarekani Mweusi. Walihudhuria watu wa mataifa mbali mbali, lakini zaidi kutoka Marekani na Tanzania. Tuilkaa kwa takriban saa tatu.
Baadhi ya waTanzania waliohudhuria ni vijana wa kampuni ya utalii iitwayo Rift Valley Cultural Tourism, ambayo makao yake ni Karatu. Kupitia kwa mkurugenzi wa kampuni, wote walikuwa wamepata nakala za kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences," na walikuwa wamekisoma. 

Waliposikia kuwa ninatoa mhadhara, waliamua kuhudhuria. Tulifurahi kukutana. Baada ya mhadhara, tulipiga hii picha inayoonekana hapa juu; baadhi yao wameshika kitabu changu. Wadau wa utalii ni wanufaika wa moja kwa moja wa kitabu hiki. Hii ilidhihirika mwaka 2007 wakati mkurugenzi wa J.M. Tours aliponunua nakala kadhaa akawapa madreva waongoza watalii wake wasome. 

Walikifurahia kwa msingi kwamba kiliwawezesha katika kushughulika na watalii. Niliandika kuhusu hilo kwenye makala yangu, "My Arusha Readers."
Ninawapongeza Rift Valley Cultural Tourism kwa kutambua fursa na kuitumia. Niko tayari kuwa nao bega kwa bega katika masuala ya utalii na utamaduni, kubadilishana uzoefu na kuelimishana. 

Mbali ya vitabu vyangu, ambavyo vinapatikana mtandaoni, nawakaribisha kwenye chaneli yangu ya YouTube.

Saturday, February 12, 2022

MTanzania Ughaibuni Aongelea Kitabu cha "Matengo Folktales"

 

Wiki za hivi karibuni nimepata kufahamiana na dada Corona Cormak, mTanzania aishiye Jamhuri ya Czech. Ni mwandishi mahiri wa vitabu vya watoto, ambavyo nimesoma nikavifurahia. Pia ni msimuliaji hodari wa hadithi.

Wiki hii, katika ukurasa wake wa Instagram, Coriona ameandika uchambuzi wake wa kitabu changu Matengo Folktales. Ameandika hivi:

I will start with a big smile. This book Matengo Folktales by John Mbele @africonexion. Took me way back into those days of story telling. Three stories in this book were so vividly. The Monster in the Rice, The Tale of two women and the Tale of Katigija. The sound of the songs in these stories is what I am still trying to remember. These songs were always sang with everyone when the stories were narrated. This is what is missing in story telling these days. We let our children just listen to the story without them taking part.

However, I am quite shocked with the amount of killing in every story. At least I don't remember the killing part. For example the Tale of two women, I remember this part when the woman was told to lick the wounds. And in Katigija Tale I remember the grandma singing when she brought the food to the child and the Monster in the Rice field, I remember how the children kept on disappearing.

My son was shocked when I told him The tale of Monster in the Rice. He was like, what a story, what a family 🙈🤣
Beautiful written and I like the comment section. This helps one to understand why these stories were what they were.
Now I need someone to sing those songs for me 🥳🤗
 
Tafsiri ya juu juu ya kiSwahili ni hivi:

Nitaanza na tabasamu kubwa. Kitabu ni "Matengo Folktales" cha [Joseph] Mbele. Kilinirudisha kwenye siku zile za usimuliaji hadithi. Hadithi tatu katika kitabu hiki zilisisimua: “Jitu Katika Shamba la Mpunga,” “Kisa cha Wanawake Wawili” na "Hadithi ya Katigija.” Najaribu kukumbuka sauti za nyimbo katika hadithi zile. Nyimbo hizi daima ziliimbwa na wote wakati hadithi zinasimuliwa. Hicho ndicho kinachokosekana katika usimulizi wa hadithi leo. Tunawafanya watoto wetu wasikilize tu bila wao kushiriki.

Lakini, nimeshtushwa na idadi ya mauaji katika kila hadithi. Sikumbuki sawasawa sehemu ambapo mauaji yenyewe yanatokea. Kwa mfano, "Kisa cha Wanawake Wawili," nakumbuka pale mwanamke anapoambiwa kulamba vidonds. Na katika “Hadithi ya Katigija” nakumbuka bibi anavyoimba wakati anamletea mtoto Katigija chakula, na katika “Jitu Katika Shamba la Mpunga” nakumbuka jinsi watoto walivyokuwa wanapotea. Mtoto wangu alishtuka nilipomsimulia “Kisa cha Jitu Katika Shamba la Mpunga.” Alishangaa ni hadithi gani hiyo, na ni familia gani hiyo.
 
Kitabu kimeandikwa vizuri na nilipendezwa na maelezo kuhusu hadithi. Yanasaidia kuelewa kwa nini hadithi ziko zilivyo. Sasa nahitaji mtu wa kuniimbia nyimbo zilozomo.

 

 

Wednesday, February 9, 2022

Vitabu Viko Chuoni Mbeya

 

Tarehe 27 hadi 29 Januari, 2022, nilikuwa mgeni wa Catholic University College of Mbeya. Nilikuwa nimealikwa kutoa mhadhara juu ya “Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.” Lakini nilijikuta katika shughuli zingine pia, ikiwemo mazungumzo na waalimu na pia mkuu wa chu

 

Katika mhadhara wangu, niliibua masuala ambayo nimeyaongelea katika vitabu vyangu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Chickens in the Bus: More Thoughts on Cultural Differences. Lengo langu kuu lilikuwa kuanzisha jadi ya kutafakari changamoto za tofauti za tamaduni katika ulimwengu wa utandawazi wa leo.

Tafakari hii inapaswa iwe endelevu. Kuchangia hilo, nilikabidhi nakala za hivi vitabu vyangu viwili kwa ajili ya maktaba ya chuo. Baadaye mkurugenzi  wa maktaba ameniandikia ujumbe wa shukrani kwa kupewa vitabu hivyo. 

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...