Friday, December 31, 2010

Mafisadi Wanaufurahia Mwaka Mpya

Mwaka unaoisha leo, mafisadi wanaoihujumu Tanzania walikuwa na sababu ya kukosa usingizi, kutokana na kampeni kali iliyofanyika dhidi yao.

Ingekuwa vipi, mwaka huu mpya ungekuwa ni mgumu kwa mafisadi, lakini moto uliowashwa dhidi yao umeendelea kuwa hafifu, kwa juhudi za zimamoto. Tumerudi katika amani na utulivu.

Thursday, December 30, 2010

Utamaduni na Utandawazi: Tunawafahamu wa-Turuki?


Wasomaji wa blogu zangu wanafahamu kuwa suala la utamaduni na utandawazi ni moja ya masuala ninayoyatafakari sana. Ninaelezea umuhimu wa suala hili kwa namna ya pekee katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Dhana ya utamaduni ina maana nyingi, na ni muhimu kwa mtumiaji wa dhana hii kuelezea anaitumia kwa maana ipi. Ili nieleweke vizuri na kiurahisi, singependa kuleta nadharia na mambo ya kufikirika. Badala yake, nimeamua kuuliza suali: Tunawafahamu wa-Turuki?

Leo hii, Tanzania na u-Turuki zinajenga uhusiano kwa kiwango ambacho hatujawahi kuona kabla, katika nyanja kama biashara, utalii, na elimu. Shirika la ndege la u-Turuki linapiga hatua katika kuimarisha safari baina ya Tanzania na u-Turuki. Ni wazi kuwa watu wa nchi hizi mbili wataendelea kuwa na mahusiano ya karibu katika nyanja mbali mbali.

Kama ninavyosema mara kwa mara, naamini kuwa mahusiano yoyote baina ya watu wa tamaduni mbali mbali yanaathiriwa moja kwa moja na tofauti za tamaduni hizo. Ndio maana ninauliza iwapo tunawafahamu wa-Turuki.

Sambamba na kuanzisha uhusiano na watu wa utamaduni tofauti na wetu, kuna umuhimu wa kujielimisha. Jambo moja ni kusoma vitabu. Nikiendelea na mfano huu wa u-Turuki, kuna waandishi maarufu wa ki-Turuki, kama vile Nazim Hikmet na Orhan Pamuk, ambaye alipata tuzo ya Nobel mwaka 2006. Kuna masimulizi ya kale, kama yale ambayo mhusika wake ni Nasreddin Hodja, maarufu kwa wa-Turuki na wasomaji wengine duniani.

Kwa miaka kadhaa nilifahamu kuhusu utungo maarufu unaojulikana kama The Book of Dede Korkut. Nilinunua nakala, lakini sikupata fursa ya kuisoma. Wiki hii nimeanza kuisoma, nikiwa nimesukumwa na hili suala la kukua kwa uhusiano baina ya Tanzania na u-Turuki. Lakini vile vile ni kwa sababu nimeamua kufundisha kitabu hiki katika kozi ya fasihi nitakayofundisha kuanzia wiki ijayo.

Kama nilivyotegemea, kitabu hiki ni hazina kubwa na njia nzuri ya kuwafahamu wa-Turuki: mtazamo wao wa maisha na mahusiano ya jamii, maadili yao na kadhalika. Kitabu hiki ni maarufu duniani. Wenzetu wa Brazil kwa mfano, ambao tunawaona kama rafiki zetu, wanakienzi kitabu hiki. Soma hapa.

Katika makala hii, juu ya kupokelewa kwa tafsiri ya The Book of Dede Korkut Brazil, tunaona wenzetu wanavyoelewa umuhimu wa kujisomea vitabu ili kujenga maelewano na watu wa nchi zingine na kuboresha mahusiano. Ni elimu ambayo inatufaa sote, kuanzia wafanya biashara, wadau wa elimu, diplomasia, utalii na kadhalika. Hayo ni baadhi ya mambo muhimu ninayomaanisha ninapoongelea suala la utamaduni na utandawazi.

Ingawa nimewataja wa-Turuki, siwaongelei wao tu. Tujiulize kama tunawafahamu wa-Hindi, wa-Australia, wa-China, wa-Marekani, wa-Rusi, na kadhalika. Jambo la kuzingatia ni kuwa dunia ya utandawazi wa leo inakuja na mitego na mitihani mingi, si ya kuivamia kichwa kichwa, bila elimu.

Sunday, December 19, 2010

Kitabu Kimetua St. Cloud, Minnesota

Wasomaji wa blogu zangu, hii na ile ya ki-Ingereza, wanafahamu ninavyopenda kujishughulisha na masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake katika ulimwengu wa leo.

Nafanya shughuli hizi si kwa ajili ya kutafuta umaarufu, bali naamini ni wajibu kwa wanadamu kusaidiana katika maisha na kuifanya dunia iwe bora kuliko ilivyo.

Miezi ya karibuni nimejishughulisha sana na matatizo yanayowapata wahamiaji wa ki-Somali katika jimbo la Minnesota, ambalo linaongoza kwa idadi ya wahamiaji wa ki-Somali. Wasomaji wa blogu zangu watakumbuka taarifa za shughuli zangu katika mji wa Faribault.

Matatizo kama haya ya Faribault yako pia katika miji mingine, kama vile St. Cloud. Kutokana uzoefu nilioupata Faribault, nimeanzisha mawasiliano na ndugu Mohamoud Mohamed, mkurugenzi wa SASSO, jumuia inayoshughulikia masuala ya wa-Somali mjini St. Cloud.

Nilimpelekea nakala ya kitabu cha Africans and Americans, kama mchango wangu na changamoto. Jana ameniambia kuwa kitabu amekipata, anaendelea kukisoma, na anakipenda. Atawaonyesha wadau wa St. Cloud: halmashauri ya mji, shule na vyuo, idara ya polisi, mahospitali, na kadhalika. Nami nilimhakikishia kuwa ni jambo bora. Badala ya watu kununiana tu au kugombana, ni vema wakaanza utaratibu wa kuzungumzia matatizo kama ilivyofanyika Faribault, na ikapokelewa vizuri.

Kama ninavyosema katika mihadhara, blogu na maandishi mengine, matatizo ya aina hii yanayoikumba miji ya Faribault na St. Cloud yanajitokeza katika miji na jamii nyingine duniani: Afrika, Asia, Australia, Marekani, Ulaya, na kwingineko, na yataongezeka, kutokana na mwenendo wa utandawazi wa leo. Ninapokuwa Dar es Salaam, kwa mfano, nasikiliza na kutafakari minong'ono na majungu kuhusu wa-China, ambao wanaendelea kuja katika mji ule. Niliwahi pia kuongelea tafrani iliyotokea Zanzibar. Kinachobaki ni sisi kujizatiti kwa kuelimishana kuhusu tofauti zetu na kutafuta namna ya kuishi bila matatizo.

Najiandaa kushiriki katika masuala ya St. Cloud. Mbali ya umuhimu wake kwa jinsi hali ilivyo, ni fursa ya mimi kujiongezea ujuzi na uzoefu nitakaoutumia katika kuwasaidia wengine.

Friday, December 17, 2010

Nimenunua Kitabu Kipya cha Chimamanda Ngozi Adichie

Leo nimenunua, The Thing Around Your Neck, kitabu kipya cha Chimamanda Ngozi Adichie. Huyu dada ni mwandishi wa ki-Nigeria, mwenye kipaji sana cha kuandika riwaya na hadithi fupi. Pia ana mawazo ya kusisimua na kufikirisha kuhusu simulizi. Umaarufu wake unakua kwa kasi. Amepata tuzo mbali mbali, ikiwemo ya Taasisi ya MacArthur

Riwaya yake ya kwanza, Purple Hibiscus, niliifundisha hapa chuoni St. Olaf. Inavutia sana kwa dhamira, maudhui, na matumizi ya lugha. Inaongelea maisha ya familia ya profesa wa chuo kikuu cha Nsukka, Nigeria, kwa namna ya kukufanya msomaji ujisikie uko sehemu hiyo. Matukio na migogoro baina ya wahusika imeelezwa kwa uhalisi wa kuvutia.

Mwaka 2006 nilipata bahati ya kumwona Chimamanda Ngozi Adichie, alipofika mjini Minneapolis kwenye tamasha la vitabu. Alikuja kuzindua kitabu chake cha pili, Half of a Yellow Sun. Nilinunua nakala, ambayo aliisaini, na tulipata muda wa kuzungumza kiasi, hata akaniambia kuhusu anavyoendesha blogu. Tulipiga picha inayoonekana hapa chini.
Bado sijapata muda wa kusoma Half of a Yellow Sun, ila ninayo hapa ofisini muda wote, na auala la kuisoma limo kwenye orodha yangu ya mambo muhimu ya kufanya.

The Thing Around Your Neck ni mkusanyo wa hadithi fupi. Nimeanza kusoma hadithi ya kwanza, ambayo inakumbusha Purple Hibiscus, kwa vile wahusika ni familia ya profesa katika chuo kikuu cha Nsukka. Lakini kwa kuangalia haraka haraka, nimeona kuwa kitabu hiki kina hadithi zinazohusu Nigeria na pia Marekani. Kwa maneno mengine, wahusika wa ki-Nigeria wako Nigeria na pia Marekani.

Hii imenikumbusha kitabu kingine cha hadithi kiitwacho Tropical Fish: Tales from Entebbe. Mwandishi ni Doreen Baingana wa Uganda, dada ambaye naye ana kipaji sana. Baadhi ya hadithi zilizomo katika kitabu hiki zinahusu matokeo yanayotokea Uganda na zingine zinahusu maisha ya wa-Ganda wakiwa Marekani.

Mpangilio huu wa hadithi za Adichie na Baingana unaendana na ukweli kwamba waandishi wote wawili wana uzoefu wa kuishi nchini kwao na pia Marekani. Ni katika kizazi kipya cha waandishi ambao wanailetea sifa sana Afrika.

Nina hamu ya kusoma The Thing Around Your Neck. Nina mategemeo ya kuandika makala katika blogu hii.

Friday, December 10, 2010

Laiti Ningekuwa Kama Hemingway

Laiti ningekuwa kama Hemingway, mwandishi maarufu sana duniani. Ningeandika kuhusu nchi yangu na watu wake kwa umakini, ubunifu, na ukweli wa kumgusa kila msomaji. Ningeandika kuhusu maziwa, mito, milima na mabonde. Ningeandika kuhusu fukwe, nyanda na visiwa. Ningeandika kuhusu miji na vijiji, mitaa na vitongoji.

Nimetamka hayo, na nimeanza kufanya mazoezi. Lakini bado njia ni ndefu mbele yangu.

Laiti ningekuwa kama Hemingway, aliyeangalia mazingira, matukio, na tabia za wanadamu kwa macho na akili yote, aliyejawa nidhamu ya kutumia lugha, akiangalia kila neno, tena na tena, akibadili na kusahihisha tena na tena, akitafuta namna ya kuandika sentensi sahihi yenye ukweli mtupu.

Laiti ningekuwa kama Hemingway, aliyetufundisha kuwa kazi ya mwandishi ni kujitoa mhanga ili nafsi yake yote ibakie katika kitabu tu, asibakishe hata chembe nje ya kitabu. Kila kitabu kiwe ni mauti ya mwandishi, vinginevyo kitabu hiki ni mzaha na udanganyifu. Je, nitayaweza hayo?

Hemingway aliandika kuhusu nchi mbali mbali alizozitembelea, ikiwemo nchi yangu. Nimekutana na watu wa nchi mbali mbali wanaomshukuru Hemingway kwa hilo. Tutalipaje fadhila, isipokuwa kwa kujijengea nidhamu ya kuyaangalia mazingira na maisha, nidhamu ya kuiheshimu lugha na sentensi, tuweze nasi kuandika mambo ya thamani? Tutalipaje fadhila kama hatuna ushujaa wa kuwa wakweli kama Hemingway?

Saturday, December 4, 2010

Nimekutana na Mratibu wa Chuo Kikuu cha Njombe

Tarehe 9 Oktoba nilipigiwa simu na mtu aliyejitambulisha kwa jina la Bill, akisema kuwa angependa kumleta kwangu mgeni kutoka Tanzania, kwa mazungumzo. Alimtaja mgeni kuwa ni Dr. Peter Kimilike.

Basi, tarehe 11 walifika hapa Chuoni St. Olaf. Tulifurahi kufahamiana. Dr. Kimilike ni mchungaji m-Tanzania ambaye anaratibu shughuli za kuanzisha Chuo Kikuu cha Njombe. Tulifurahi kutambua kuwa kuna watu maarufu ambao yeye na mimi tunafahamiana nao, kama vile Danford Mpumilwa, afisa habari wa Mahakama ya ki-Mataifa inayoshughulikia mauaji ya Rwanda (ICTR), na Rev. Dr. Anneth Munga, mkuu wa Chuo cha Sebastian Kolowa

Maongezi yetu yalilenga zaidi kwenye Chuo Kikuu cha Njombe. Nilimweleza Dr. Kimilike kuwa ninafuatilia kwa karibu maendeleo ya vyuo Tanzania. Kila ninapoenda kule, ninatembelea vyuo. Nikampa mifano ya vyuo nilivyotembelea: Tumaini (Iringa), Makumira (Arusha), na Sebastian Kolowa (Lushoto). Ninaelimika sana ninapoongea na walimu na wengine kuhusu hali halisi ya vyuo vyetu na mahitaji yaliyopo. Kwa mtu anayekaa ughaibuni, kuna fursa za kuchangia vitu kama vitabu.

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ninakitembelea mara kwa mara. Nilisoma na kufundisha hapo, na kila mwaka napita hapo kufanya utafiti, kuongea na walimu na pia wanafunzi. Napenda kutembelea shule za kila aina, kuanzia shule za msingi, kujielimisha kuhusu hali halisi.

Kuhusu Chuo Kikuu cha Njombe, nilimwambia kuwa nimefuatilia habari zake kwa miezi mingi, mtandaoni, kama vile Arusha Times. Alinieleza hatua iliyofikiwa na mipango inayoendelea. Kuna mahitaji mengi, kuanzia ya kukarabati majengo na kujenga mengine, kununua vitabu na majarida, vifaa vya maabara, kompyuta, na kuleta walimu.

Mwanzo ni mgumu, kama kawaida. Unahitajika mtandao wa wadau na washiriki wa aina mbali mbali. Cha kutia moyo ni kuwa msingi umeshajengwa kwa kutumia uwezo na nguvu za wananchi, ambao wamechanga chochote walicho nacho, iwe ni fedha, mazao, hata jogoo.

Chuo kina mikakati ya kujiendesha, kwa kuanzisha miradi kama ya kupanda miti kwa ajili ya mbao za kuuza, na pia kupanda mazao kama vile matunda. Dr. Kimilike anaelezea zaidi suala hili hapa.
Nimewekwa katika mtandao wa wahamasishaji wa Chuo Kikuu Cha Njombe. Nimelipokea jukumu hili kwa mikono miwili. Hizi picha tulipiga ndani ya uwanja wa ndege wa Minneapolis, Minnesota, wakati Mchungaji Kimilike alipokuwa anarudi Tanzania, Oktoba 24, baada ya ziara yake ya Marekani.

Tuesday, November 30, 2010

Asante, Joseph Mbele

Jioni hii, katika kuzurura mtandaoni, mitaa ya Google, nimekumbana na makala kwenye blogu fulani, ambayo inanitaja. Soma hapa.

Sikuwa nimeiona makala hii ambayo inataja ziara niliyofanya College of St. Benedict/St. John's University mwaka jana. Nilialikwa kutoa mihadhara. Katika darasa la Profesa Lisa Ohm, niliongelea hadithi na utamaduni, kufuatia maelezo yaliyomo katika kitabu cha Matengo Folktales, ambacho walikuwa wanakitumia. Soma hapa.

Mhadhara wa pili niliutoa kwa wanafunzi na walimu waliokuwa wanajiandaa kwenda Tanzania na Afrika ya Kusini, lakini ulihudhuriwa na wengi wengine. Lengo lilikuwa kuwaarifu kuhusu tofauti za msingi baina ya tamaduni wa mw-Afrika na ule wa m-Marekani, kama nilivyoeleza katika kitabu cha Africans and Americans.

Nakumbuka jinsi ukumbi ulivyojaa watu kwenye mhadhara huu, na kwenye meza nyuma ya umati walikuwa wameweka nakala nyingi za vitabu hivi viwili, kama ilivyo desturi hapa Marekani, wanapowaita waandishi kuzungumzia vitabu na uandishi. Soma hapa.

Nimefurahi kuona kuwa mazungumzo yangu kwa hao wa-Marekani yameelezwa kama ilivyoelezwa na mwandishi huyu. Nimefurahi jinsi anavyokiri kuwa yale niliyowaambia ndiyo aliyoyakuta Afrika Kusini. Huwa nakutana na wa-Marekani wengi wanaosema hivyo hivyo, wanaporudi kutoka Afrika. Nami nafanya juhudi nijielimishe zaidi kuhusu tofauti za tamaduni hizi, ili niweze kuboresha mafunzo na mawaidha ninayotoa.

Thursday, November 25, 2010

Kuendesha Blogu Mbili

Nina blogu mbili: ya ki-Swahili na ya ki-Ingereza. Kuendesha blogu moja ni kazi, blogu mbili ni zaidi. Kwa nini naendesha blogu mbili?

Nimewahi kuelezea kwa nini ninablogu. Labda nisisitize tu kuwa blogu yangu ya ki-Swahili inanipa fursa ya kujiongezea uzoefu wa kuandika kwa ki-Swahili, na pia kuwasiliana na wa-Tanzania wengi, wakiwemo wale wasiojua ki-Ingereza. Ninafahamu pia kuwa wako wasomaji wa blogu hii ambao si wa-Tanzania. Kuna hata wa-Marekani ambao wameniambia kuwa wanaisoma. Wanajikumbusha mambo ya Tanzania na pia lugha ya ki-Swahili.

Katika blogu yangu ya ki-Ingereza siandiki sana masuala ya Tanzania. Kadiri siku zinavyozidi kwenda, napata hisia kuwa ninaandika kwa ajili ya walimwengu kwa ujumla. Naona jinsi ninavyozingatia masuala ya taaluma, hasa fasihi. Naamini natoa mchango kwa wale wapendao fasihi au wenye duku duku ya kuifahamu. Hapo nawafikiria sana wa-Tanzania.

Katika kuongelea kazi za fasihi, siandiki makala ndefu, bali nagusia vipengele muhimu, na pia natoa dokezo ambazo ni changamoto kwa yeyote, aweze kuzifanyia utafiti na tafakari. Naamini kuwa kwa namna hii, yeyote atajiongezea ufahamu wa fasihi.

Labda nijieleze zaidi kwa wa-Tanzania wenzangu: siandiki kwa ajili ya wale ambao lengo lao kuu ni kupasi mtihani. Naandika kwa ajili ya wale wenye kupenda fasihi au wenye duku duku ya kujifunza fasihi. Pia kama nilivyosema kabla, naandika kwa ki-Ingereza ili kutoa mfano wa uandishi bora wa ki-Ingereza, jambo ambalo linahitajika katika jamii yangu ya wa-Tanzania.

Ingawa kuendesha hizi blogu mbili si kazi rahisi, nitajitahidi kuzimudu kwa kadiri ya uwezo wangu. Kazi ya kuendesha blogu hizi inaniwekea aina ya nidhamu katika maisha yangu. Kuandika katika blogu hizi mara kwa mara imeshakuwa kama deni na wajibu, lakini naona manufaa yake kwangu, kwa jinsi ninavyotumia muda wangu na akili yangu kwenye shughuli ya maana.

Wednesday, November 24, 2010

Kitendo cha CHADEMA Kususia Hotuba ya JK

Kitendo cha wabunge wa CHADEMA kususia hotuba ya JK Bungeni kimeibua mjadala mkubwa miongoni mwa wa-Tanzania. Wakati mjadala huu ukiendelea, nami nina la kusema.

CHADEMA imesema kuwa, mapema kabisa, ilipeleka malalamiko kwenye tume ya uchaguzi (NEC) kuhusu mchakato wa utangazaji wa matokeo ya urais, na kuomba utangazaji ule usimamishwe ili kuchunguza dosari ambazo CHADEMA ilikuwa na taarifa nazo.

Kwa msingi huu, ningependa kusikia taarifa ya NEC, niweze kufahamu kama kweli ililetewa malalamiko hayo. Kama iliyapata, napenda kujua iliyashughulikia vipi. CHADEMA inasema kuwa NEC haikuyajibu wala kuyashughulikia malalamiko yale.

Kama hii ni kweli, basi naitupia NEC lawama nzito. CHADEMA imesema kwamba kutokana na kuupuziwa malalamiko yao na NEC, na kutokana na kwamba sheria inasema kuwa tangazo la NEC la mshindi wa urais haliwezi kupingwa mahakamani au penginepo, walilazimika kutafuta hatua zingine za kuelezea malalamiko yao. CHADEMA wanasema kuwa kususia hotuba ya JK ni njia waliyoamua kuchukua kwa msingi huo.

Kama hali ndio hiyo inayoelezwa na CHADEMA, na kama NEC haitatoa maelezo ya kuthibitisha vingine, msimamo wangu ni kuwa CHADEMA walikuwa na haki ya kususia hotuba ya JK kama walivyofanya. Kama raia ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa, bali ni mpenda haki, uwazi, na ukweli, nawaunga mkono CHADEMA kwa suala hilo.

Nchi lazima iwe na kiongozi muda wote. Kwa msingi huu, JK ni rais, na CHADEMA hawajakataa hilo, ingawa kuna watu ambao, kwa sababu wanazozijua wao, wanaizushia CHADEMA uwongo kuwa haimtambui rais na serikali yake. Najiuliza kama watu hao wana akili timamu au kama wanaitakia mema nchi yetu.

Monday, November 22, 2010

Kitabu Kilivyopokelewa Ubalozi wa Kenya

Mwaka 2007 mwanzoni, jumuia ya wa-Kenya wanaoishi Minnesota waliandaa mkutano kuhusu uwekezaji nchini kwao. Walihudhuria wa-Kenya wengi sana, wakiwemo maofisa wa serikali na taasisi mbali mbali waliofika kutoka Nairobi. Nilishiriki, nikiwa na meza ambapo niliweka vitabu vyangu na machapisho mengine.

Nilikutana na wa-Kenya wengi, baadhi ambao tulifahamiana kabla na wengine kwa mara ya kwanza. Mmoja wa hao tuliofahamiana kabla alikuwa Julia Opoti, ambaye ni mwanahabari anayeendelea kujipatia umaarufu, na ni shabiki wa siku nyingi wa maandishi yangu. Alikuja kwenye meza yangu akiwa na bwana mmoja, akatutambulisha.

Yule bwana alikuwa afisa katika ubalozi wa Kenya, Washington DC. Julia alikuwa amemwambia kuhusu kitabu cha Africans and Americans naye akakinunua. Tarehe 17 Aprili, yule afisa aliniandikia ujumbe huu:

Kuhusu kitabu chako, hivi sasa nafikiri kimesomwa na watu kadri ya watano hapa ubalozi wetu na kimependwa sana. Ni matumaini yangu kuwa ukipata wasaa mzuri utaandika vitabu zaidi katika fani hii ili upate kunufaisha watu juu ya swali hili muhimu la tafauti ya mila na utamaduni.


Ujumbe huu, ingawa ulinifurahisha, haukunishangaza, kwa sababu ninafahamu jinsi wa-Kenya wanavyothamini vitabu na elimu kwa ujumla. Nimefahamu jambo hilo tangu nilipoanza kutembelea Kenya, mwaka 1989, na katika kuwaona huku ughaibuni. Nimeshasema hivyo hata katika kitabu changu cha CHANGAMOTO. Jambo la pili ni kuwa nilivutiwa na wito kuwa niendelee kuandika, wito ambao nimeupata kutoka kwa wasomaji wengine pia. Naendelea kuandika.

Friday, November 19, 2010

Wabunge wa CCM Wanakera

Wabunge wa CCM wanakera. Tukianzia na wabunge hao walioapishwa safari hii, sitasahau kuwa hao ndio waheshimiwa waliotoroka midahalo wakati wa kampeni. Wote walitoroka midahalo, kitendo ambacho kimenikera. Mimi kama mwalimu, ninayetambua umuhimu wa midahalo, ninawashutumu hao waheshimiwa. Soma hapa.

Kila nitakapokuwa naona sura za hao waheshimiwa wa CCM, nitakuwa nakumbuka kitendo chao hiki cha kutoroka midahalo. Nitakuwa naangalia kama watajirekebisha au kama kitendo kile ni ishara ya tabia na mwenendo watakaofuata kwa miaka mitano ijayo.

Tukirudi nyuma, kwenye awamu iliyopita, wabunge wa CCM walikera. Ni nani atakayesahau yaliyotokea wakati Dr. Slaa alipoanza kutamka kuwa kuna ufisadi katika nchi yetu? Wabunge wote wa CCM walimpinga vikali na kumtupia shutuma nzito kwamba alikuwa mzushi.

Dr. Slaa hakuyumba, bali aliendelea kutoa madai yake. Hatimaye, ilianza kuthibitika kuwa aliyokuwa anayasema ni kweli, kwamba tuna mafisadi. Baada ya wananchi kuanza kuona ukweli huo, ukawa haupingiki tena, tuliwaona baadhi ya wabunge wa CCM wakijitokeza na kuanza kujinadi kuwa nao ni wapiganaji dhidi ya ufisadi. Sijui kama walikuwa wanaongea kwa dhati au kwa lengo jingine.

Tukirudi nyuma zaidi, tunakumbuka suala la machafuko yaliyotokea Visiwani mwaka 2001. Machafuko yale, yaliyotokana na CCM, chama tawala, kushindwa kutumia haki na busara, yaliiletea Tanzania aibu kubwa duniani. Kwa uthibitisho, soma hapa.

Lakini, pamoja na maovu yote yaliyofanyika Visiwani, pamoja na fedheha yote iliyoiangukia Tanzania, wabunge wa CCM hawakukubali kuwa serikali ya CCM ilikuwa na makosa, wala hawakukubali kuwa Tanzania ilikuwa inafedheheka. Wao waliitetea serikali ya CCM. Maadam palikuwa na suala lililohusu chama cha upinzani, yaani CUF, wabunge wa CCM waliamua kuikingia kifua serikali ya CCM, badala ya kusimamia haki za binadamu na heshima ya Tanzania.

Je, kuna kero kubwa zaidi ya hii ya kutojali maslahi ya Taifa na badala yake kuangalia maslahi ya kikundi fulani?

Thursday, November 18, 2010

Kwa Nini Wabunge wa CHADEMA Wamesusia Hotuba ya JK

Leo, Novemba 18, katika ukurasa wake katika mtandao wa Facebook, Dr. Slaa ameelezea kwa nini wabunge wa CHADEMA wamesusia hotuba ya JK Bungeni. Mimi ni raia ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa. Nina ugomvi wangu na CCM, kama ninavyoeleza mara kwa mara katika blogu hii na blogu zingine, katika makala mbali mbali, na hata katika kitabu cha CHANGAMOTO. Papo hapo, ninaheshimu midahalo, na nimeshaishutumu CCM kwa kukimbia midahalo wakati wa kampeni zilizopita. Naweka hapa kauli hii ya Dr. Slaa kwa vile ninawaheshimu watu wanaojitokeza na kujieleza kwa hoja:
------------------------------------------------------------------------

Wabunge wetu wamechukua uamuzi mgumu sana, uamuzi ambao unataka ujasiri na uthubutu wa vitendo. Ni lazima tuelewe kuwa mgogoro uliopo siyo na Kikwete kama Kikwete, la hasha bali na mfumo uliomuingiza madarakani safari hii, mfumo ambao tunautuhumu kuwa haukuwa huru na wa haki. Uamuzi huu haukuwa wa chuki binafsi au kisirani dhidi ya Kikwete kama Kikwete, bali dhidi ya mfumo ulioundwa na kulelewa na CCM na ambao umetuonesha kuwa hauwezi na haupaswi kulelewa kwa muda mwingine wowote ujao.


Kuanzia wakati wa kutangaza matokeo tulitoa malalamiko yetu kwa Tume ya Uchaguzi ili waweze kuyafanyia kazi ili mshindi apatikane katika mazingira ya haki na uwazi. Tume haikusikiliza na ikaendelea na mfumo wake mbovu wa kutangaza matokeo bila kujali malalamiko yetu. Tukazungumza hadharani juu ya kutopatana kwa matokeo ya uchaguzi yanayotangazwa na tume na yale yaliyoko majimboni na kuomba tume wasitishe ili waangalie ushahidi tulio nao, tume haikusikiliza na matokeo yake wakamtangaza Kikwete kuwa Rais licha ya kwamba matokeo majimboni yalikuwa yanaashiria vinginevyo.


Ni muhimu kutambua kuwa ni rahisi kukubali matokeo ya Ubunge kwa sababu yanarasimishwa majimboni na yanaweza kupingwa mahakamani. Katika urais kimsingi ukiangalia Katiba utaona kuwa haijalishi nani kashinda kwenye kura, bali nani katangazwa mshindi. Tunachotuhumu sisi ni kuwa matokeo ya Uchaguzi yangetangazwa kama ilivyoahidiwa na Tume mwezi Machi yangeonesha wazi mshindi ni tofauti na yule aliyetangazwa. Lakini wao tume wakijua kuwa mara wakishatangaza hakuna mahakama inayoweza kuhoji wakafanya hila na haraka ya kutangaza matokeo ya Urais kwa kumtangaza Kikwete kuwa ni Rais.


Kama toka siku ya kwanza tulitoa malalamiko na zikapita siku tano bila kujibiwa wala kusikilizwa na baadaye tunatakiwa tukubali tu kwa vile "keshatangazwa" katika dhamira safi tunaweza vipi kufanya hivyo? Ugomvi wetu wa kisiasa (na siyo chuki wala uhasama binafsi) hauko zaidi na Kikwete bali natume iliyomtangaza. Na kwa vile yeye mwenyewe haoni matatizo katika tume au mfumo wetu wa uchaguzi tunaona kuwa aidha alitoa baraka zake au alikubali kunufaishwa na mfumo huo mbovu.


Hivyo, wabunge wetu kutoka nje ni kutuma ishara mbili: Kwanza, tunapinga mfumo wa kichakachuaji wa tume ya Uchaguzi uliomtangaza Kikwete kuwa Rais, na pili kwa vile Tume imeshindwa kutuonesha uwazi wa ushindi wa Kikwete tunashindwa kukubali kama ni mshindi halali. Ni mpaka pale uchunguzi huru wa kura utakapoonesha kuwa Kikwete kashinda kihalali ndipo tutakuwa tayari kumtambua ukiondoa uwezekano mwingine wa kuelewana.


Tukumbuke kuwa, kama uchaguzi huu ungeendeshwa katika hali ya uwazi, haki na ufanisi tusingefika hapa. CHADEMA siyo wa kulaumiwa katika hili wala wabunge wetu wasibebeshwe mzigo kwa hili; watu waliotufikisha hapa ni Serikali ya CCM na vyombo vyake ikiwemo Tume ya Uchaguzi. Wangeonesha weledi na kutokupendelea kwa wazi tusingefikia mahali pa kutulazimisha kuchukua hatua hizi ambazo kwa kila kipimo ni za wastani sana ukilinganisha na hatua ambazo tungeweza kuzichukua.


Nawasihi tuwaunge mkono wabunge wetu na uongozi wetu kwa kuwatia moyo kwani uamuzi waliouchukua ni uamuzi wa kijasiri lakini ulioweka historia katika Tanzania kuwa hatuwezi tena kusukumwa na kuburuzwa kwa kutumia nguvu ya taasisi au cheo cha mtu. Tuwatie shime na tusimame nao katika wakati huu wa kihistoria.


Pamoja tunaweza, mpaka kieleweke!

Tuesday, November 16, 2010

Mzee Kataraia Amekipenda Kitabu Hiki

Blogu yangu hii ni kama kisebule changu binafsi. Naamua nini cha kukiweka hapa, na sidhani kama ninasukumwa na ukweli kwamba watu wanasoma ninayoandika. Yeyote anayepita hapa na kuchungulia, ni hiari yake. Niliwahi kujieleza hivyo katika makala hii hapa.

Basi, leo napenda kuelezea nilivyokutana na Mzee Kataraia juzi, tarehe 14, mjini Minneapolis. Hatukuwa tumefahamiana. Lakini mara tulipotambulishwa, alianza kunielezea jinsi alivyokipenda kitabu changu cha Africans and Americans.

Niliguswa, nikamsikiliza kwa unyenyekevu. Ingawa napenda kuandika makala na vitabu, na watu wengi wananielezea wanavyopendezwa na kufaidika na maandishi yangu, napata taabu kustahimili sifa. Ila huwa namshukuru Mungu kwa kunipa vipaji, niendelee kutekeleza wajibu wa kuwanufaisha viumbe wake. Hii ndio tafsiri yangu. Sifa zote na shukrani namrudishia Muumba.

Nikiwa namsikiliza, Mzee Kataraia aliendelea kunieleza jinsi alivyosafiri sehemu zingine hapa Marekani, akawaonyesha wa-Tanzania kadhaa kitabu hiki, nao wakakisoma. Aliniambia kuwa wiki hizi alizokuwa hapa Marekani, ameshafanya safari kadhaa kwa ndege. Wakati wa kungojea ndege, ameona watu wakisoma kwenye kompyuta zao, na ndege ikiwa hewani amewaona watu wakisoma vitabu. Hapo nami nikamwunga mkono, kuwa nami nimeona sana tabia hizo hapa Marekani.

Maongezi yetu yalikuwa mafupi sana, labda dakika tano tu, kwa sababu tulikuwa katika shughuli nyingine za kusalimiana na kuongea na watu. Lakini kwa dakika zile chache nilipata picha kuwa Mzee Kataraia ni m-Tanzania wa pekee.

Kwanza, kama ninavyoandika katika blogu hii mara kwa mara, si rahisi kumkuta m-Tanzania anayevutiwa na vitabu, labda vitabu vya udaku. Halafu niliguswa na moyo wa Mzee Kataraia wa kuwakumbuka wengine. Alivyoona amekuta kitu cha manufaa, ameenda kuwaonyesha wengine, wanufaike. Nimeguswa.

Sitamsahau Mzee huyu. Nitajiona nina bahati iwapo nitakutana naye tena. Nimegundua huyu ni Mzee aliyeelimika. Kwa mtazamo wangu, kama nilivyosema katika mahojiano Radio Mbao, ishara muhimu ya kuelimika ni kuwa daima na kiu ya kutafuta elimu.

Monday, November 15, 2010

Tumesoma Masimulizi ya "Popol Vuh"

Leo katika darasa langu mojawapo tumemaliza kuongelea masimulizi ya kale ya Popol Vuh. Ni masimulizi ya zamani sana ya taifa la wa-Maya wa Amerika ya Kati. Wa-Maya wa zamani waliishi maeneo ambayo leo yanahusisha nchi za Mexico, Guatemala, Belize na Honduras. Walikuwa maarufu kwa mafanikio waliyofikia katika nyanja mbali mbali, kama vile ujenzi wa miji, ugunduzi wa hati ya kuandikia lugha yao, utafiti wa sayari, na utengenezaji wa kalenda.

Nilisikia juu ya Popol Vuh kwa mara ya kwanza mnamo mwaka 1982 kutoka kwa Profesa Harold Scheub, nilipokuwa nasomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu Cha Wisconsin-Madison. Hata hivi hatukusoma kitabu hiki. Sasa nimefurahi kuwa katika darasa langu tumefanikiwa kukisoma na kukijadili, ingawa mambo yake mengi si rahisi kueleweka kwetu watu wa leo, wa tamaduni tofauti kabisa na ule utamaduni wa wa-Maya wa zamani.

Popol Vuh ni masimulizi kuhusu mambo mengi yahusuyo jinsi dunia ilivyoumbwa, na matukio mbali mbali yaliyofuatia, yakiwahusisha miungu na mashujaa wa aina aina. Ni masimulizi yenye uzito, kwani yanabeba mambo ya imani, maadili, utabiri na falsafa. Baadhi ya masimulizi ya Popol Vuh yanatukumbusha masimulizi ya vitabu vya dini kama Biblia au Quran, na pia masimulizi mengine kama Gilgamesh, au hata masimulizi maarufu ya wa-Kerewe, alivyoyaandika Mzee Kitereza katika kitabu chake cha Bwana Myombekere na Bibi Bugonoka na Ntulanalwo na Buliwhali.

Kusoma vitabu vya aina hii ni jambo jema sana, kwani linatupa mwanga kuhusu hali halisi ya yale waliyopitia na kuwazia wanadamu sehemu mbali mbali za dunia.

Friday, November 12, 2010

Huduma ya Vitabu Gesti

Tarehe 29 Oktoba nilikuwa Chicago, kuhudhuria mkutano wa washauri wa programu ya masomo iitwayo ACM Botswana. Vyuo vingi hapa Marekani vinaendesha programu za kupeleka wanafunzi nchi mbali mbali, nami ni mshauri katika programu kadhaa.

Nilifikia katika hoteli ya Best Western River North. Nimeshalala hapo mara kadhaa, ninapohudhuria mikutano ya ACM Botswana na ACM Tanzania. Safari hii niliona hoteli hii imeanzisha huduma ya vitabu.



Nilivyoingia chumbani, niliona tangazo kwenye meza ndogo ya taa, pembeni mwa kitanda.









Nilipoliangalia karibu zaidi, niliona kuwa ni tangazo la huduma ya vitabu.


























Nilifuatilia. Nikateremka chini, kuelekea sehemu ya mapokezi. Wakati nashuka kwenye lifti, baada ya kufika chini kabisa, nikaona kuwa ukutani pana tangazo kuhusu huduma ya vyakula katika hoteli hii, na pia hii huduma ya vitabu, pamoja na uwepo wa hoteli hii katika mtandao wa Facebook, pia kuwa hoteli ina blogu yake. Hoteli imeanzisha huduma ya vitabu katika kuchangia maendeleo ya jamii.









Halafu karibu na sehemu ya mapokezi ndipo wameweka kabati la hivi vitabu. Nililisogelea nikaona kuna vitabu vya aina aina.








Na utaratibu ni kuwa mgeni anakaribishwa kuvisoma, na hata kuvichukua, na pia kuchangia vitabu.


Jambo hili lilinifurahisha. Nikaanza kuwazia gesti zetu za Tanzania. Kitu cha kwanza nilichokumbuka ni jinsi taa ndani ya gesti za Tanzania zilivyo. Mara nyingi taa katika chumba iko juu sana na mwanga wake ni hafifu. Huwezi kusomea. Mazingira ya kusoma, kwa ujumla hayako. Gesti nyingi ziko pamoja na baa, ambapo muziki na kelele ni mtindo mmoja, na varangati za hapa na pale.

Cha kushangaza pia ni kuwa katika gesti nyingi Tanzania, kuna nakala ya Biblia. Sijui utaratibu huu wa kuweka Biblia ulianzaje. Pia najiuliza kama kuna m-Tanzania yeyote anayesoma Biblia gesti. Sifa na heshima za gesti tunazijua. Hazifanani na sifa na heshima ya Biblia. Nashangaa kwa nini sisi wa-Kristu tunaruhusu kitabu cha dini yetu kuwekwa katika mazingira ya namna hii.

Tuesday, November 9, 2010

Mdahalo wa Dr. Slaa, ITV, Utumike Mashuleni

Mimi ni mwalimu, mwenye uzoefu wa kufundisha tangu mwaka 1976, nilipoanza kufundisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na hatimaye kutoa mihadhara katika vyuo vikuu sehemu mbali mbali duniani.

Kutokana na wadhifa wangu, napenda kusema kuwa ingekuwa bora iwapo mdahalo wa Dr. Slaa ITV ungesambazwa mashuleni, kwani una mambo muhimu ya kuwafundisha vijana wetu. Jambo la kwanza ni kuwa mdahalo ule unatoa changamoto kuhusu masuala ya nchi yetu, ni kichocheo cha fikra.

Jambo la pili ni kuwa vijana wetu wakiona jinsi Dr. Slaa anavyoyakabili masuali, kwa ufasaha, ufahamu, na kujiamini, wataona mfano wa kuiga na kigezo cha kujipima. Wataelewa kuwa wana wajibu wa kujielimisha sana.

Wengi tunafahamu jinsi kiwango cha elimu kilivyoporomoka nchini, kiasi kwamba hata kwenye mahojiano ya kutafuta ajira, wa-Tanzania wanapata taabu. Kwa mfano, taarifa zimezagaa kuwa wa-Tanzania wanaogopa kushindana na wa-Kenya.

Sisi miaka tulipokuwa tunasoma hatukuwa tunawaogopa wa-Kenya, wala wa-Ganda, wala wengine wowote. Tulisoma nao pale Chuo Kikuu Dar es Salaam, bila kuwaogopa kwa lolote. Kwa hali hii, ni muhimu vijana wetu wapewe kila aina ya msaada na changamoto ya kuwajengea mwamko mpya. Mdahalo wa Dr. Slaa una mchango kwa upande huo.

Vile vile, mdahalo huu wa Dr. Slaa unatoa mfano mzuri wa uwajibikaji katika kuitumia lugha ya ki-Swahili. Haipendezi kuona wale tunaowaita viongozi, kama vile wabunge, mawaziri, na wakurugenzi, wakishindwa kukitumia ki-Swahili ipasavyo, na badala yake wanachanganya lugha. Hii ni dalili ya kutoelimika vizuri, na kutoiheshimu lugha yetu ya ki-Swahili.

Nafahamu kuwa wa-Tanzania wengine wakisoma ujumbe kama huu wangu, watarukia mambo ya ushabiki wa vyama vya siasa. Mimi ni raia ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa. Kwa wadhifa wangu kama mwalimu, naangalia maslahi ya vijana wetu kielimu.

Wanaopenda kudhania kuwa mtu akitoa maoni kama yangu basi anahusika na chama fulani cha siasa nawaomba waelewe kuwa msimamo wangu kama mtu asiye mwanachama wa chama cha siasa ni kuwa mifumo ya siasa tunayoifuata Tanzania ni ya kikoloni mambo leo. Haijalishi kama ni chama kimoja au vyama vingi. Haitajenga demokrasia. Nimeelezea hayo katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Wednesday, November 3, 2010

Mwalimu Nyerere Aliiogopa CCM

Ingawa alikuwa mwanzilishi wa CCM, kwa nia njema ya kuendeleza mapinduzi katika nchi yetu, miaka ilivyozidi kwenda Mwalimu Nyerere alishuhudia jinsi CCM ilivyobadilika na kuwa mzigo kwake na pia tishio kwa usalama wa Taifa.

Mwaka 1993 Mwalimu alichapisha kitabu kiitwacho Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania (Harare: Zimbabwe Publishing House, 1993). Pamoja na mambo mengine katika kitabu hiki, Mwalimu alisema kuwa kuna kansa katika uongozi wa CCM. Nanukuu baadhi ya maneno yake:

Chama cha Mapinduzi, kwa sababu ya uzito wa historia yake, hadhi ya jina lake, mfumo wa wavu wake, mazoea ya watu, na ubovu wa Vyama vya Upinzani, kinaweza kuchaguliwa na Watanzania, pamoja na kansa ya uongozi wake. Au watu wanaweza wakachoka, wakasema, "potelea mbali:" wakachagua Chama cho chote, ilimradi tu watokane na kansa ya uongozi wa CCM. Hainifurahishi kuyasema haya, lakini uhai wa Nchi yetu unataka yasemwe
. (Ukurasa 61)

Mwalimu hakuishia hapo, bali aliongezea namna hii:

Nilisema awali kwamba kansa ya uongozi ndani ya Chama cha Mapinduzi isingekuwa ni jambo la kutisha sana kama tungekuwa tumeanza kuona Chama kizuri cha upinzani kinachoweza kuiongoza Nchi yetu badala ya CCM. Ubovu wa uongozi ndani ya CCM ndio uliofanya nikapendekeza tuanzishe mfumo wa Vyama Vingi. Nilitumaini kuwa tunaweza kupata Chama kingine kizuri ambacho kingeweza kuiongoza Nchi yetu badala ya CCM; au ambacho kingekilazimisha Chama cha Mapinduzi kusafisha uongozi wake, kwa kuhofia kuwa bila kufanya hivyo kitashindwa katika uchaguzi ujao. Lakini bado sijakiona Chama makini cha upinzani; na wala dalili zo zote za kuondoa kansa ya uongozi ndani ya CCM. Bila upinzani mzuri wa nje, na bila demokrasia halisi ndani ya Chama cha Mapinduzi, Chama hiki kitazidi kudidimia chini ya uzito wa uongozi mbovu. Kwa hali yetu ya kisiasa ilivyo nchini hili si jambo la kutarajia bila hofu na wasi wasi
! (Ukurasa 66)

Ni wa-Tanzania wangapi wenye utamaduni wa kusoma vitabu? Ni wangapi wanaosoma vitabu vya Mwalimu Nyerere? Ni wazi kuwa umbumbumbu miongoni mwa wa-Tanzania ni neema kwa CCM.

Sunday, October 31, 2010

Polisi Wajifunze Nidhamu, Wazingatie Haki

Mara kadhaa, hasa wakati wa kampeni za kisiasa na uchaguzi, tumeshuhudia vitendo vya polisi na vyombo vingine vya dola ambavyo vimechangia kuleta hofu miongoni mwa wananchi na pia kuvuruga amani.

Katika uchaguzi wa mwaka huu, vitendo hivi vimejitokeza tena, kama inavyoonekana katika video hii



Kwanza namsifu na kumshukuru huyu dada anayeongea katika video hii kwa kutuelezea hayo anayoelezea, kwa uwazi na kwa dhati. Nafikiri ametoa somo la maana sana, na nategemea wahusika watajirekebisha. Kama wahenga walivyosema, kosa si kufanya kosa, bali kurudia kosa.

Kwa upande mwingine, ni lazima niseme kuwa, kwa ujumla, kazi ya polisi si rahisi. Katika mazingira kama haya ya kampeni za siasa na uchaguzi, hali inaweza kuwa ngumu pia, kwa sababu ya ushindani mkubwa na pengine uhasama unaoweza kuwepo katika jamii. Kwa hivi, naamini kuwa polisi wanaweza kufanya maamuzi au vitendo kwa lengo la kulinda amani, kumbe ikawa vitendo vyao vikachangia kuharibika kwa amani.

Hata hivi, naamini kuwa polisi wakipata mafunzo zaidi wataweza kukwepa makosa ambayo si ya lazima. Kwa mfano, mwaka 2001, polisi walikiuka maadili ya kazi yao kule Visiwani, kwa kufanya umachinga kwa CCM. Matokeo yake ni kuwa Taifa letu lilipata aibu kimataifa, kutokana na CCM kuitumia polisi kwa manufaa yake, na polisi kujidhalilisha kwa kukubali kutumiwa namna hii. Kwa taarifa, soma hapa. Kosa la aina hii halina utetezi, kwani tunategemea polisi wawe wanaongozwa na sheria tu, na wawe wanalinda haki za raia wote.

Saturday, October 30, 2010

Mahojiano: JK na Wanahabari

Jana tangu asubuhi hadi leo mchana nilikuwa Chicago, katika mkutano. JK alifanya mahojiano yake na wanahabari jana hiyo hiyo. Leo nimeona yamewekwa katika blogu maarufu ya wavuti. Nami nimeyaweka hapa kwangu, nikitanguliza shukrani kwa Da Subi.




Thursday, October 28, 2010

Mgombea wa CCM Kufanya Mahojiano

Zikiwa zimebaki siku tatu tu hadi uchaguzi ufanyike nchini Tanzania, tumepata habari kuwa mgombea urais kwa tiketi ya CCM atafanya mahojiano na vyombo vya habari. Hii ni tofauti na msimamo wa CCM katika kipindi chote cha kampeni, ambapo wagombea wake walikuwa hawashiriki midahalo.

Wengi wetu tunafahamu kuwa midahalo, mahojiano, na kadhalika, ni mambo muhimu katika jamii inayothamini elimu. Sasa kwa nini CCM haikutambua hilo kabla? Tena CCM ni chama chenye wanachama milioni kadhaa, wakiwemo "wasomi" wengi.

Ni lazima niulize: hao ni wasomi kweli au ni wababaishaji? Ni aibu kuwa hawakuweza kuchangamka kabla na kutambua umuhimu wa midahalo, hadi saa hii ya mwisho, na baada ya Dr. Slaa kuonyesha mfano.

Mimi kama mwalimu, na pia raia ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa, nawajibika kuwashutumu CCM kwa kutoonyesha mfano bora, pale walipotamba kuwa mgombea wao hahitaji kushiriki midahalo. Na pamoja na hayo, wagombea wao wote wakawa hawashiriki midahalo. Sijui kama ilikuwa ni fikra zao au ndio nidhamu ya chama. Kama ndio nidhamu ya chama, ni heri nibaki bila chama, kuliko kuwa katika himaya ya udikteta.

Narudia kuushutumu uamuzi wa kutoshiriki midahalo. Na hao wagombea wote nawashutumu kwa kutii amri isiyo na busara kama hiyo. Je, sasa, kwa vile JK ameamua kufanya mahojiano, nao watakimbilia kwenye vyombo vya habari kufanya mahojiano? Akili gani hiyo? Mimi kama mwalimu, lazima niulize: tunawafundisha nini watoto wetu, ambao ni taifa la kesho?

Baada ya kusema hayo, mimi kama raia mwema, ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa, nina masuali kwa mgombea wa CCM. Kwa vile hakuna muda wa kuuliza yote, nitauliza matatu tu.

La kwanza ni kwa nini wale ambao Dr. Slaa amewataja katika orodha yake ya mafisadi hawajampeleka mahakamani hadi leo?

La pili ni je, kwa nini CCM inadai kuwa amani Tanzania inatokana na uongozi wa CCM, wakati CCM inashiriki kikamilifu katika kuhujumu amani, hasa nyakati za kampeni na uchaguzi? Mifano ni mingi, kuanzia Visiwani hadi Bara, na hata ripoti za kimataifa zinathibitisha hilo. Kwa mfano, soma hapa na pia angalia video hizi hapa.

Ukweli ni kitu muhimu sana. Je, CCM haitambui kuwa wanaotunza amani Tanzania kikweli kweli ni sisi mamilioni ya raia ambao si wanachama wa chama chochote cha siasa? Hatuna rekodi yoyote ya kuvuruga amani kama wenzetu wenye vyama wanavyofanya. Kwa nini CCM inafunika ukweli huo?

Suali la tatu ni je, CCM ina maelezo gani kuhusu shutuma alizotoa Mwalimu Nyerere dhidi ya CCM katika kitabu chake cha Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania? Kuzifahamu kwa ufupi shutuma hizi, soma hapa.

Tuesday, October 26, 2010

Mbumbumbu Waache Kugombea Uongozi

Kitu kimoja kinachonikera ni jinsi wakati wa kugombea uongozi, mbumbumbu wengi wanavyojitokeza kuwania uongozi. Halafu, kwa jinsi wapiga kura wengine walivyo mbumbumbu, wanawapigia kura hao mbumbumbu wenzao na kuwawezesha kushinda.

Baada ya hapo, kunakuwa na matatizo mengi. Tatizo moja kubwa ni jinsi hao mbumbumbu wanaoitwa viongozi wanavyojifanya miungu. Hawakubali kukosolewa.

Kwa mfano, gazeti likiwakosoa, wanalitishia au wanazuia lisichapishwe. Kama kuna kitabu kimewakosoa, wanakipiga marufuku. Msimamo wangu ni kuwa watu wasiojiamini au wasioheshimu uhuru wa watu kutoa fikra, wasigombee uongozi.

Nchi inahitaji viongozi wa kweli, ambao wanatambua kuwa wao si miungu, na ambao hawatetereki kwa kukosolewa. Kibaya zaidi ni kuwa hao mbumbumbu wanadhani kuwa wao ndio nchi. Wakikosolewa, wanasema ni hatari kwa usalama wa taifa. Ni usalama wa taifa au ni usalama wa mbumbumbu? Ni taifa gani ambalo linatetereka kwa sababu ya mbumbumbu kukosolewa?

Haya ninayosema nayasema kwa dhati. Mimi mwenyewe ninakosolewa na hata kutukanwa. Kwa mfano, soma hapa, na hapa.

Sioni sababu ya kuwazuia watu wanaofanya hivyo, hata kama ningekuwa kiongozi. Ni muhimu watu wawe huru kutoa mawazo yao. Ingawa tunasema kuwa tutumie lugha ya kuheshimiana, na mimi nakubali hivyo, lakini hatimaye nasema kuwa hata anayetukana anakuwa amepata fursa ya kujieleza. Ni bora iwe hivyo kuliko kuwafunga watu mdomo, kwani madhara ya kuwanyima watu fursa ya kujieleza yanaweza kuwa mazito. Nimefafanua zaidi msimamo wangu huo katika kitabu cha CHANGAMOTO.

Napenda kurudia, mbumbumbu waache kugombea uongozi. Nafasi hizi zinahitaji viongozi, si watu ambao hawajiamini.

Sunday, October 24, 2010

Video za Mdahalo wa Dr Slaa, ITV

Zimepatikana video za mdahalo wa Dr. Slaa katika ITV. Ni wazi kuwa Dr. Slaa ni mtu anayejua anachoongea, anayeijua nchi, anayewaheshimu wananchi, na anaipenda sana nchi yetu. Anafahamu vizuri nini anachotaka kifanyike ili kuinusuru na kuiendeleza nchi yetu. Ni muhimu kuwa na mtu wa aina hii, hata kama mnapishana mawazo. Nyerere alikuwa mtu wa aina hii hata kama baadhi walipishana naye mawazo.

Mimi kama msomi nimevutiwa sana na jinsi Dr. Slaa anavyoongea kwa kujiamini. Kwa hilo nalo amenikumbusha ya Mwalimu Nyerere, ambaye wakati mwingine alikuwa anatumbukia pale Chuo Kikuu Dar es Salaam ili kujibizana na wasomi masuali ya papo kwa papo. Nami nilikuwepo, kwanza kama mwanafunzi, na kisha kama mhadhiri. Mtu wa namna hii ananivutia sana.

Saturday, October 23, 2010

Mdahalo, ITV, Dr. Slaa

Mgombea urais kwa tiketi ya CHADEMA, Dr. Slaa, amefanya mdahalo ITV, kama ilivyotangazwa kwa siku kadhaa. Mimi kama mwalimu naiheshimu sana midahalo, kwani ni njia madhubuti ya kuelimishana, na katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi, ni njia madhubuti ya kuwaelewa wagombea. Namsifu Dr. Slaa kwa kujitokeza mbele ya umma namna hii, na nawashutumu wale wote ambao wamekataa kushiriki midahalo. Sikiliza mdahalo huu wa ITV na Dr. Slaa hapa:



Check this out on Chirbit

Mdahalo huu unaweza kuufuatilia pia na kupata taarifa nyingi zaidi hapa.

Friday, October 22, 2010

Mazungumzo Mjini Faribault Kuhusu Tamaduni, Oktoba 21

Jana jioni, kama nilikuwa mjini Faribault, kuongelea kitabu changu cha Africans and Americans, kama nilivyoandika juzi katika blogu hii. Matangazo yalikuwa yamewekwa sehemu mbali mbali, kama vile gazeti la Faribault Daily New na ukumbi wa Facebook. Wahudhuriaji walikuja kutoka Faribault na miji ya karibu. Wengine, ambao tumefahamiana Facebook, walikuja kutoka Minneapolis.


Nilianza kwa kuelezea kifupi, nilivyokuja Marekani mara ya kwanza, kusomea shahada ya uzamifu katika chuo kikuu cha Wisconsin-Madison, 1980-86, ndipo nikapata uzoefu wa kuishi katika utamaduni tofauti na wangu, na nikaanza kupata ufahamu wa yale niliyokuja baadaye kuyaandika katika kitabu cha Africans and Americans na kadhalika. Niliongelea jinsi tunavyojengeka katika utamaduni wetu na kuona utamaduni wetu ndio sahihi na wenye mantiki bora.

Kumbe, tukienda kwenye utamaduni wa wengine, tunaona mambo tofauti, na hii inaweza kuwa chanzo cha matatizo katika mahusiano yetu na watu wa utamaduni ule. Nilitaja mifano mingi kutokana na maisha yangu, uzoefu wangu wa kuangalia na kuchunguza matatizo duniani. Nilitoa mifano ya matatizo yanayotokea baina ya wa-Marekani na wa-Afrika, kwani ufahamu wangu uko zaidi upande huo.

Nilisisitiza, kama ninavyofanya daima, umuhimu wa kujielimisha, ili tujitambue na kuwafahamu wengine. Jukumu hili halikwepeki, na hakuna pa kukimbilia, kwani dunia inazidi kuwa kijiji. Watu wanatapakaa duniani kutoka tamaduni mbali mbali. Si miji ya Marekani tu ambao inakumbana na suala la kuingiliwa na watu kutoka sehemu zingine za dunia, bali hata Afrika ni hivyo hivyo. Miji kama Dar es Salaam, kwa mfano, inaendelea kuwa na watu kutoka mbali, kama vile China, na hivi kuwa changamoto katika suala la kumudu tofauti za tamaduni. Bila juhudi ya kujielimisha na kuelimishana tunajitakia matatizo.
Baada ya mazungumzo yangu na kipindi cha masuali na majibu, watu walipata fursa ya kuviangalia au kuvinunua vitabu vyangu, kama ilivyopangwa kwenye ratiba.






Huyu mama mwenye shati jeupe alikuwa mfanyakazi katika chuo cha St. Olaf, ambapo nafundisha. Nilimkuta hapo ila alistaafu miaka kadhaa iliyopita. Ni mwenyeji wa Faribault na ni mmoja wa mashabiki wangu wakubwa.





Shughuli nzima ilikuwa ya mafanikio mazuri. Kila mtu alifurahi, na waandaaji waliwahimiza waliokuwepo kuandaa mazungumzo ya aina hii sehemu zao za kazi.

Mmoja wa waliohudhuria ni Bwana Milo Larson, mwenyekiti wa Faribault Diversity Coalition. Leo ameandika kwenye ukumbi wa Facebook kuhusu mazungumzo yangu:

Great Forum by Joseph Mbele last night at the Library, always learn something new about the different cultures whenever I hear him. Everybody should see him just once, would be a more harmonious place
.

Monday, October 18, 2010

Nataongelea Kitabu Changu Faribault, Minnesota, Oktoba 21

Tarehe 21 Oktoba nitakwenda Faribault, Minnesota, kuongelea kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nimealikwa na uongozi wa Maktaba ya Faribault kwa kushirikiana na mji wa Faribault.

Nimeshatembelea Faribault mara kadhaa, kutoa mihadhara na kushiriki shughuli zinazohusu elimu kwa jamii na hata kusuluhisha migogoro inayotokana na tofauti ya tamaduni, kama inavyoelezwa hapa na hapa.

Kwa hapa Marekani, ni jambo la kawaida kuwaita waandishi kuongelea vitabu vyao. Huwa ni fursa ya kukutana ana kwa ana na mwandishi, kuuliza masuali, na kununua vitabu.

Kitu kimoja kinachowavutia sana wa-Marekani ni kununua kitabu wakati huo na kumpa mwandishi aandike jina lake na pia ujumbe kwenye nakala ya kitabu hicho.

Wengine wananunua vitabu kadhaa, halafu wanapokuja kuwekewa sahihi, inabidi wakuambie uandike jina la nani, kwani wanawanunulia pia marafiki, watoto, au ndugu wengine. Ni mila ambayo iko ndani kabisa ya mioyo ya wa-Marekani. Wanaona furaha, kama inavyoonekana kwenye picha hii hapa, ambayo ilipigwa karibu na Grantsburg, Wisconsin, nikiwa naweka hizo sahihi vitabuni.

Kuhusu shughuli ya hiyo tarehe 21 Oktoba mjini Faribault, Mama Delane James, mkurugenzi wa maktaba ya Faribault, ameandika mwaliko huu katika ukumbi wa Facebook:


Dear Friends:

I hope you will be able to join us in the Great Hall at 6:30 p.m. as St. Olaf Professor Mbele speaks about his book, Africans and American: Embracing Cultural Differences.

Professor Mbele visited with our library staff last spring and we all agree... he is incredible! We are thrilled to be hosting this event and hope you can make it!

--Delane


Saturday, October 16, 2010

Maonesho ya Vitabu Minneapolis, Oktoba 16

Nimerejea jioni hii kutoka Minneapolis, kushiriki maonesho ya vitabu ambayo huandaliwa na jarida la Rain Taxi na kufanyika mara moja kwa mwaka.





Kama kawaida, nilipeleka vitabu vyangu. Nilikuwa nimelipia meza ndogo. Lakini hii ilitosha kwa vitabu tu, bila maandishi mengine. Kwa vile idadi ya vitabu vyangu si ile ile ya mwaka jana au mwaka juzi, siku zijazo itanilazimu kulipia meza kubwa ili niweze kuweka maandishi mengine pia.








Leo ninaleta hapa picha mbali mbali nilizopiga, kama mfano wa namna wa-Marekani wanavyojali suala la vitabu.








Kama nilivyosema siku zilizopita, wa-Marekani wanafurika kwenye maonesho ya vitabu. Wanafika tangu asubuhi, milango ya ukumbi inapofunguliwa. Na siku nzima watu wanakuwa wengi katika ukumbi, wakienda na kuja.







Wanafika watu wa kila rika: watoto, vijana, watu wazima, na waze, wanawake kwa wanaume.







Pamoja na hali ya uchumi wa Marekani kuwa mbaya miaka hii, watu wanavichambua vitabu na kuvinunua.







Wana dukuduku na hamu ya kusoma. Ukisikiliza maongezi yao, utawasikia wakiongelea sifa walizosikia kwa wenzao kuhusu kitabu hiki au kile. Au utawasikia wale waliosoma kitabu fulani wakiwaeleza wenzao na kuwahamasisha wanunue.



Mimi kama m-Tanzania ninashinda kwenye shughuli hizi nikiwa na masikitiko makubwa, kwani hali kama hii haiko Tanzania. Ninajua, kwa sababu ninashiriki maonesho ya vitabu kule, kama ninavyoripoti mara kwa mara katika blogu hii.






Ni wazi kuwa wa-Tanzania tumeshajichimbia kaburi katika dunia hii inayoendeshwa na elimu, ujuzi na maarifa. Tusijidanganye.







Kwa mtazamo wangu, dalili ya kuelimika ni kuwa na duku duku na hamu ya kudumu ya kujitafutia elimu. Shule inapaswa iwe ni chanzo tu na kichocheo cha duku duku na hamu hii ya kujitafutia elimu.






Kupata digirii, kwa mfano, si mwisho wa elimu, bali hatua moja au chachu katika safari ya kutafuta elimu. Hayo niliyaelezea pia katika mahojiano katika Kombolela Show.


Kama ninavyosema mara kwa mara, napenda sana kushirikia maonesho ya aina hii, kwani ni fursa ya kukutana na watu walio katika fani za uandishi, uchapishaji, uhariri na uuzaji wa vitabu. Kila mmoja wao ana jambo la kunichangamsha akili au kunipanua mawazo.




Kukutana na watu wanaotaka kununua vitabu ni jambo jingine linalonigusa. Wakati mwingi natumia kujibu maulizo ya watu wanaotaka kujua maandishi yangu yanahusu nini.



Watu wengi wanapoona kuwa natoka Afrika, wanapenda kuelezea vipengele vya maisha yao. Kama walishafika Tanzania au sehemu yoyote ya Afrika, wanaelezea. Kwa maana hiyo, kushiriki tamasha la vitabu ni kweli fursa ya kuonana na kufahamiana na watu wa aina mbali mbali.

Wednesday, October 6, 2010

Vitabu Vyangu Kwa Bei Nafuu

Lulu.com, ambako nachapisha vitabu vyangu, kumetokea tangazo linalotoa fursa kwa mwandishi kupunguza bei ya vitabu vyake akipenda.

Kwa heshima ya wasomaji wangu, nimeamua kutumia fursa hiyo. Nimepunguza bei ya vitabu vyangu vyote kwa mwezi huu Oktoba.

Vitabu hivi vimetajwa hapo kulia na pia hapa. Bofya sehemu ya kununulia, ili kuona punguzo hilo.

Wale ambao hawanunui vitu mtandaoni na wanavihitaji vitabu hivi wanaweza kuwasiliana nami kwa barua pepe: info@africonexion.com.

Siku ya mwisho ya punguzo hili ni Oktoba 31.

Chukua Chako Mapema

Pale CCM ilipoanzishwa, baadhi ya wa-Tanzania walianzisha minong'ono wakitafsiri CCM kama "Chukua Chako Mapema."

Nilitaja jambo hilo katika makala fupi, "Jokes Play Social Role," ambayo ilichapishwa katika gazeti la Daily News (Tanzania) (Juni 16, 1987) ukurasa 4.

Ni miaka mingi imepita, na ushahidi wa nini hasa maana ya CCM umeendelea kujitokeza. Tumsikilize katibu mkuu wa CCM:

Monday, October 4, 2010

Mahojiano Yangu "Kombolela Show"

Tarehe 2 Oktoba, nilihojiwa katika "Kombolela Show." Hiki ni kipindi cha redio kinachoendeshwa na Jaduong Metty, ambaye pia ni mmiliki wa blog ya Metty's Reflections. Kusikiliza mahojiano, bofya hapa au hapa

Friday, October 1, 2010

Mwalimu Nyerere Aliongelea Uozo Katika CCM

Mwalimu Nyerere aliongelea uozo katika CCM. Kwa mfano, wakati alipokuwa anajiandaa kung'atuka uenyekiti wa CCM, alizunguka nchi nzima akikagua uhai wa CCM. Wakati wa ziara hiyo, inaonekana Mwalimu alitatizwa na yale aliyoyaona. Aliwahi kusema kuwa kuna watu ndani ya CCM ambao hata mtihani juu ya Azimio la Arusha hawawezi kupasi.

Mwaka 1993 Mwalimu alichapisha kitabu kiitwacho Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania (Harare: Zimbabwe Publishing House, 1993). Pamoja na mambo mengine katika kitabu hiki, Mwalimu alisema kuwa kuna kansa katika uongozi wa CCM. Nanukuu baadhi ya maneno yake:

Chama cha Mapinduzi, kwa sababu ya uzito wa historia yake, hadhi ya jina lake, mfumo wa wavu wake, mazoea ya watu, na ubovu wa Vyama vya Upinzani, kinaweza kuchaguliwa na Watanzania, pamoja na kansa ya uongozi wake. Au watu wanaweza wakachoka, wakasema, "potelea mbali:" wakachagua Chama cho chote, ilimradi tu watokane na kansa ya uongozi wa CCM. Hainifurahishi kuyasema haya, lakini uhai wa Nchi yetu unataka yasemwe
. (Ukurasa 61)

Mwalimu hakuishia hapo, bali aliongezea namna hii:

Nilisema awali kwamba kansa ya uongozi ndani ya Chama cha Mapinduzi isingekuwa ni jambo la kutisha sana kama tungekuwa tumeanza kuona Chama kizuri cha upinzani kinachoweza kuiongoza Nchi yetu badala ya CCM. Ubovu wa uongozi ndani ya CCM ndio uliofanya nikapendekeza tuanzishe mfumo wa Vyama Vingi. Nilitumaini kuwa tunaweza kupata Chama kingine kizuri ambacho kingeweza kuiongoza Nchi yetu badala ya CCM; au ambacho kingekilazimisha Chama cha Mapinduzi kusafisha uongozi wake, kwa kuhofia kuwa bila kufanya hivyo kitashindwa katika uchaguzi ujao. Lakini bado sijakiona Chama makini cha upinzani; na wala dalili zo zote za kuondoa kansa ya uongozi ndani ya CCM. Bila upinzani mzuri wa nje, na bila demokrasia halisi ndani ya Chama cha Mapinduzi, Chama hiki kitazidi kudidimia chini ya uzito wa uongozi mbovu. Kwa hali yetu ya kisiasa ilivyo nchini hili si jambo la kutarajia bila hofu na wasi wasi! (Ukurasa 66)

Mwalimu Nyerere aliongelea hayo miaka yapata ishirini iliyopita. Leo hali ikoje? Kwa mtazamo wangu, uozo aliosemea Mwalimu umeongezeka. Hayo yamekuwa mawazo yangu tangu zamani. Kwa mfano, soma hapa.

Wednesday, September 29, 2010

Programu za Kupeleka Wanafunzi Tanzania

Leo hapa chuoni St. Olaf tulikuwa na shughuli ya kuzitangaza programu za masomo ambamo chuo kinapeleka wanafunzi wake.

Tunafanya hivyo mara moja kwa mwaka. Walimu washauri wa programu tunakuwepo na taarifa mbali mbali za programu tunazohusika nazo, na wanafunzi wanakuja kupata taarifa hizo, na pia kujiandikisha iwapo wana nia ya kujiunga na programu hizo.

Vyuo vingi hapa Marekani vina programu za aina hiyo, na vyuo kadhaa vinapeleka wanafunzi Tanzania. Hii inatokana na kufahamu faida wanayopata wanafunzi kwa kwenda kuishi na kujifunza katika nchi zingine. Inapanua akili na upeo. Kuishi miongoni mwa watu wa utamaduni tofauti kunampa kijana fursa ya kukomaa kwa namna mbali mbali na kuwa tayari kwa maisha ya zama zetu za utandawazi wa leo. Programu hizi zinachangia maelewano mema duniani.

Pamoja kazi yangu ya kufundisha katika idara ya ki-Ingereza hapa St. Olaf, ninashughulika katika program zinazopeleka wanafunzi nchi za ki-Afrika, ikiwemo Tanzania. Nimefanya shughuli hii kwa miaka yote niliyofundisha hapa ughaibuni, katika programu kama LCCT, ACM Tanzania, na ACM Botswana. Leo nilijipanga kwenye meza kama inavyoonekana katika picha, nikingojea wanafunzi, nimwage sera.

Hii ni fursa ya kuitangaza nchi. Kama nilivyowahi kusema kwenye blogu hii, picha ni vielelezo murua kabisa. Ni lazima niseme kuwa shughuli hii ya kuitangaza Tanzania ilikuwa inanipendeza sana miaka ya mwanzo, wakati Tanzania ilipokuwa kweli nchi ya kupigiwa mfano, ambayo nilikuwa najivunia. Tanzania ile, ya Mwalimu Nyerere, inatoweka. Nchi inazidi kuwa ya matabaka ya wenye mali wanaostarehe, na maskini wanaoteseka. Badala ya jamii yenye amani na utulivu, tunaendelea kuona kushamiri kwa ukatili kama ule unaofanywa dhidi ya albino na wale wanaoitwa vibaka. Program hizi za kuleta wanafunzi Tanzania zinaiingizia nchi hela nyingi, lakini naogopa kuwa hela hizi zinachotwa na mafisadi. Siku hizi, ninapowaambia wanafunzi hao kwenda Tanzania, ninasema nikiwa na wasi wasi. Lakini naendelea kufanya shughuli hii, kwani ni muhimu, sio tu kwa hao wanafunzi, bali kwa nchi yetu na yao, na dunia kwa ujumla, kama nilivyoandika hapa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...