Showing posts with label Uganda. Show all posts
Showing posts with label Uganda. Show all posts

Friday, December 2, 2016

Ndugu wa Uganda Anataka Kitabu

Kama ilivyo kawaida katika blogu hii, ninapenda kujiwekea kumbukumbu mbali mbali. Jana niliwatembelea akina mama wawili wa-Kenya waishio Brooklyn Park, Minnesota, ambao walitaka tukutane ili niweze kuwapa ushauri kuhusu fursa za kujiendeleza kielimu ya juu na katika ajira. Wakati tulipokuwa katika maongezi, waliwasiliana na bwana mmoja wa kutoka Uganda, wakamwita kuja kuungana nasi.

Tulizungumza kuhusu masuala mbali mbali, yakiwemo masuali waliyoniuliza juu ya ufundishaji na uandishi wangu. Mmoja wa hao akina mama nilikuwa nimemwahidi kumpa nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Huyu jamaa wa Uganda aliniulizia namna ya kukipata kitabu kile, nikamweleza kuwa anaweza kukipata mtandaoni Amazon.com au lulu.com/spotlight/mbele, au kutoka kwangu. Nikamshauri kwamba kwa upnde wa gharama, ni rahisi zaidi kukinunua Amazon.com. Lakini yeye alisisitiza kuwa nimpelekee, akanipa na anwani yake.
,
M-Ganda huyu amenikumbusha wa-Ganda wengine niliokutana nao hapa Minnesota, wakajiptia kitabu changu. Mmoja ni Steven Kaggwa ambaye alikuwa anamiliki mgahawa wa Tam Tam. Baada ya kukisoma kitabu hiki, aliniambia kuwa aliwaelezea wafanya kazi wake. Mmoja wao, Sally, hakuishia tu kujinunulia nakala, bali alinunua nakala nyingine ambayo aliniambia alikuwa anampelekea mkuu wake wa kazi, ambaye ni m-Marekani. Niliguswa na taarifa ya huyu mama, kama nilivyoguswa miaka michache baadaye, wakati mama mmoja kutoka Togo alivyonunua nakala za kitabu hiki kwa ajili ya wakuu wa kazini kwake, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

M-Ganda mwingine ninayemkumbuka nilikutana naye katika tamasha la vitabu ambalo nilikuwa ninashiriki. Alikuwa amefika kikazi hapa Minnesota, lakini alikuja kwenye tamasha hilo, na ndipo tulipofahamiana. Bila kusita alinunua kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differenes, akaenda zake. Yeye na hao wengine wameniacha nikitafakari jinsi hao wenzetu walivyo. Ninaona kuwa sio tu wameenda shule, bali wameelimika, kwani uthibitisho wa kuelimika ni kuwa na hamu ya kutafuta elimu hata baada ya kumaliza shule.

Wednesday, April 6, 2016

"Song of Lawino" Yatimiza Miaka 50

Mwaka huu, Song of Lawino, utungo maarufu wa Okot p'Bitek wa Uganda, unatimiza miaka hamsini tangu uchapishwe. Utungo huu, ambao unafahamika kama wimbo, ulichapishwa na East African Publishing House mwaka 1966 ukapata umaarufu tangu mwanzo.

Ulisomwa mashuleni na katika jamii kote Afrika Mashariki na sehemu zingine. Ulileta msisimko na upeo mpya katika dhana ya ushairi katika ki-Ingereza, na ulichochea washairi wengine kutunga kwa mtindo aliotumia Okot p'Bitek, ambao ulijaa athari za ushairi wa jadi wa ki-Afrika.

Siku chache zilizopita, niliandika katika blogu hii kuwa nimechapisha mwongozo wa Song of Lawino. Kitu ambacho sikusema ni kuwa nilikuwa na sababu ya kuchapisha mwongozo huu wakati huu, na sababu yenyewe ni hayo maadhimisho ya miaka 50.

Nilisoma taarifa, zaidi ya mwaka mmoja uliopita, kwamba idara ya "Literature" ya Chuo Kikuu cha Makerere ilikuwa inaandaa maadhimisho ya kumbukumbu hii, ambayo yangehusisha mihadhara na shughuli zingine. Ingekuwa niko Afrika Mashariki, ningeshiriki. Kwangu ingekuwa fursa sio tu ya kushiriki maadhimisho, bali pia kujikumbusha ziara ambazo niliwahi kufanya katika Chuo Kikuu cha Makerere.

Mara ya kwanza, mwaka 1978, nilienda kuhudhuria mkutano wa waalimu wa "Literature" kutoka vyuo vikuu vya Afrika Mashariki, na mara ya pili, mwaka 1990, nilikwenda kama mtahini wa nje katika idara ya "Literature and Mass Communications."

Kwa vile nilijua kuwa nisingeweza kuhudhuria maadhimisho, niliamua kuendelea kurekebisha mswada wa mwongozo wa Song of Lawino ambao nilikuwa nimeanza kuuandika miaka yapata ishirini iliyopita. Nilijiwekea lengo la kuchapisha mwongozo huu wakati huu wa maadhimisho ya miaka 50. Nafurahi kuwa nimefanikisha azma yangu.

Kwa mujibu wa taarifa nilizozisoma, maadhimisho yalifana. Ingawa shughuli rasmi zilifanyika katika Chuo Kikuu cha Makerere, taarifa za maadhimisho haya zilizagaa katika vyombo vya habari nchini Uganda. Mifano ni taarifa hii hapa na hii hapa.

Shughuli moja iliyonivutia katika maadhimisho haya ni kuzinduliwa kwa tafsiri ya Luganda ya Song of Lawino. Wanafasihi tunafahamu kuwa utungo huu una historia ndefu ya kutafsiriwa. Nimegusia suala hilo katika mwongozo wangu. Hadi leo, kuna tafsiri katika lugha zaidi ya thelathini. Kwa njia hii, umaarufu wake unaendelea kuenea ulimwenguni.


Thursday, July 11, 2013

Tumeanza Kusoma "Abyssinian Chronicles"

Baada ya kumaliza kitabu cha Half of a Yellow Sun, darasa langu la fasihi ya Afrika tumekuwa tukisoma Abyssinian Chronicles, riwaya ya Moses Isegawa.

Moses Isegawa ni kijana aliyezaliwa na kukulia Uganda. Lakini mwaka 1990 aliondoka Uganda akaenda kuishi Netherlands, akiwa amechukua uraia wa nchi ile.

Nilikuwa nimesikia habari za kitabu chake hiki kwa miaka kadhaa. Nilinunua nakala, ila sikupata fursa ya kukisoma, ingawa nilikipitia juu juu. Hata hivyo katika kukipitia hivyo, niliona wazi kabisa kuwa ni kitabu murua, kilichoelezea kwa ufasaha na mvuto mkubwa maisha ya leo ya watu wa Uganda, kuanzia kijijini hadi mjini.

Nilipokuwa naandaa kozi yangu hii, miezi michache iliyopita, niliamua kitabu hiki kiwemo katika orodha yangu. Tumesoma karibu kurasa 100 tu,  wakati kitabu kina kurasa 480. Kiasi tulichosoma kimetupa fursa ya kuongelea dhamira mbali mbali zinazojitokeza, kama vile mila na desturi za arusi, masuala ya wahusika, na sanaa.

Kwa upande wangu, nimekuwa nikiwaambia wanafunzi kuwa maelezo ya maisha ya vijijini yamenikumbusha maisha yangu mwenyewe, maana nilizaliwa na kukulia nilikulia kijijini.

Moses Isegawa alikiandika kitabu hiki kwa lugha ya kidachi (Dutch), na jina lake lilikuwa Abessijnse kronieken, ambacho kilichapishwa Amsterdam mwaka 1998. Nakala 100,000 ziliuzwa hima, ingawa idadi ya watu wa nchi ile ni yapata milioni 16 tu.

Mwandishi alikiweka kitabu chake hiki katika lugha ya ki-Ingereza. Kwa kawaida, tunasema alikitafsiri. Lakini kwa mujibu wa falsafa za leo, dhana ya tafsiri ni dhana tata, na kile tunachokiita tafsiri sio tafsiri kwa kweli, bali utungo mpya. Huo ndio mtazamo wangu kuhusu Abyssinian Chronicles.

Muhula wetu umeisha leo, na mategemeo yangu ni kuwa wanafunzi na mimi mwenyewe tutaendelea kukisoma kitabu hiki hadi ukurasa wa mwisho. Sioni kama kuna tatizo kufikia mwisho wa muhula bila kumaliza kusoma kitabu. Dhana ya kumaliza kusoma kitabu nayo ni dhana tata na naweza kusema ni dhana muflisi. Kwa kutafakari kwa undani maana ya kusoma ni nini, na nini kinafanyika tunaposema tunasoma kitabu, nimejionea kuwa huwezi kumaliza kusoma kitabu chochote, hata kama umefika ukurasa wa mwisho na sentensi ya mwisho. Hilo ni suala jingine la falsafa, ambalo nalifafanua wakati wa kufundisha fasihi.

Abyssinian Chronicles ni kitabu kinachoelezea mambo ya miaka ya karibuni, ya sabini na kitu hadi themanini na kitu. Kinavutia sana. Ni ushahidi mwingine wa jinsi wenzetu wa nchi jirani, na wa nchi zingine za Afrika, walivyo katika anga za juu sana katika uandishi kwa lugha hizi za kigeni.

Friday, December 17, 2010

Nimenunua Kitabu Kipya cha Chimamanda Ngozi Adichie

Leo nimenunua, The Thing Around Your Neck, kitabu kipya cha Chimamanda Ngozi Adichie. Huyu dada ni mwandishi wa ki-Nigeria, mwenye kipaji sana cha kuandika riwaya na hadithi fupi. Pia ana mawazo ya kusisimua na kufikirisha kuhusu simulizi. Umaarufu wake unakua kwa kasi. Amepata tuzo mbali mbali, ikiwemo ya Taasisi ya MacArthur

Riwaya yake ya kwanza, Purple Hibiscus, niliifundisha hapa chuoni St. Olaf. Inavutia sana kwa dhamira, maudhui, na matumizi ya lugha. Inaongelea maisha ya familia ya profesa wa chuo kikuu cha Nsukka, Nigeria, kwa namna ya kukufanya msomaji ujisikie uko sehemu hiyo. Matukio na migogoro baina ya wahusika imeelezwa kwa uhalisi wa kuvutia.

Mwaka 2006 nilipata bahati ya kumwona Chimamanda Ngozi Adichie, alipofika mjini Minneapolis kwenye tamasha la vitabu. Alikuja kuzindua kitabu chake cha pili, Half of a Yellow Sun. Nilinunua nakala, ambayo aliisaini, na tulipata muda wa kuzungumza kiasi, hata akaniambia kuhusu anavyoendesha blogu. Tulipiga picha inayoonekana hapa chini.
Bado sijapata muda wa kusoma Half of a Yellow Sun, ila ninayo hapa ofisini muda wote, na auala la kuisoma limo kwenye orodha yangu ya mambo muhimu ya kufanya.

The Thing Around Your Neck ni mkusanyo wa hadithi fupi. Nimeanza kusoma hadithi ya kwanza, ambayo inakumbusha Purple Hibiscus, kwa vile wahusika ni familia ya profesa katika chuo kikuu cha Nsukka. Lakini kwa kuangalia haraka haraka, nimeona kuwa kitabu hiki kina hadithi zinazohusu Nigeria na pia Marekani. Kwa maneno mengine, wahusika wa ki-Nigeria wako Nigeria na pia Marekani.

Hii imenikumbusha kitabu kingine cha hadithi kiitwacho Tropical Fish: Tales from Entebbe. Mwandishi ni Doreen Baingana wa Uganda, dada ambaye naye ana kipaji sana. Baadhi ya hadithi zilizomo katika kitabu hiki zinahusu matokeo yanayotokea Uganda na zingine zinahusu maisha ya wa-Ganda wakiwa Marekani.

Mpangilio huu wa hadithi za Adichie na Baingana unaendana na ukweli kwamba waandishi wote wawili wana uzoefu wa kuishi nchini kwao na pia Marekani. Ni katika kizazi kipya cha waandishi ambao wanailetea sifa sana Afrika.

Nina hamu ya kusoma The Thing Around Your Neck. Nina mategemeo ya kuandika makala katika blogu hii.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...