Showing posts with label ufundishaji. Show all posts
Showing posts with label ufundishaji. Show all posts

Sunday, November 5, 2017

Hadithi Zetu za Jadi

Hadithi zetu za jadi ni hazina kubwa ya utamaduni wetu. Kila kabila lilikuwa na hadithi nyingi, pamoja na aina nyingine za fasihi simulizi, kama vile nyimbo, na methali. Hadithi zina tafakari juu ya maisha na tabia za binadamu ingawa mara nyingi wahusika wana taswira za wanyama, ndege au viumbe vingine. Zinaelezea masuala ya familia, malezi ya watoto, wajibu wa wazazi na watoto. Zinatoa tahadhari kuhusu tabia mbaya na maelekezo juu tabia njema. Zinafundisha huruma, maelewano, ushiriano na kusaidiana.

Hadith zinaelezea mahangaiko, mategemeo, mafanikio, ubora na udhaifu wa binadamu, Kuna hadithi za kusisimua hisia na fikra, zenye kuibua masuali kuhusu maana ya maisha, kama walivyoibua wanafalsafa wa mkondo uitwao "existentialism," kama nilivyogusia katika kitabu cha Matengo Folktales.

Kitabu hiki ni mkusanyo wa hadithi kumi za ki-Matengo, ambazo nilizitafsiri kwa ki-Ingereza. Niliandika uchambuzi wa kila hadithi na nikaandika pia insha ya jumla kuhusu hadithi, ili kuwapa wasomaji kianzio cha kuzichambua.

Nilipokuwa ninaandaa kitabu hiki, nilikuwa mhadhiri katika Chuo kikuu cha Dar es Salaam. Somo mojawapo nililokuwa ninafundisha ni "Oral Literature" (fasihi simulizi). Hapakuwa na kitabu cha kufaa kufundishia somo hilo kwa wanafunzi wa chuo kikuu. Hapakuwa na kitabu cha kufundishia hadithi za jadi, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Kwa hivyo, lengo langu lilikuwa ni kuziba pengo, kwa kuandika kitabu ambacho nilitaka kiwepo. Hii ni falsafa ambayo imekaa kichwani mwangu: kama hakuna kitabu ambacho ungetaka kiwepo, andika hicho kitabu. Au kama kitabu unachosoma hakikuridhishi, andika hicho ambacho kitakuridhisha.

Ingawa kitabu changu si kikamilifu, angalau kinakidhi mahitaji yangu ya kufundisha somo la hadith i za jadi kwa wanafunzi wa chuo kikuu. Ni faraja kwangu kuwa si mimi peke yangu mwenye wazo hilo. Kuna wengine ambao wanakitumia kama ilivyokuwa katika chuo kikuu cha Montana na chuo cha St. Benedict/St. John's.

Friday, December 2, 2016

Ndugu wa Uganda Anataka Kitabu

Kama ilivyo kawaida katika blogu hii, ninapenda kujiwekea kumbukumbu mbali mbali. Jana niliwatembelea akina mama wawili wa-Kenya waishio Brooklyn Park, Minnesota, ambao walitaka tukutane ili niweze kuwapa ushauri kuhusu fursa za kujiendeleza kielimu ya juu na katika ajira. Wakati tulipokuwa katika maongezi, waliwasiliana na bwana mmoja wa kutoka Uganda, wakamwita kuja kuungana nasi.

Tulizungumza kuhusu masuala mbali mbali, yakiwemo masuali waliyoniuliza juu ya ufundishaji na uandishi wangu. Mmoja wa hao akina mama nilikuwa nimemwahidi kumpa nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Huyu jamaa wa Uganda aliniulizia namna ya kukipata kitabu kile, nikamweleza kuwa anaweza kukipata mtandaoni Amazon.com au lulu.com/spotlight/mbele, au kutoka kwangu. Nikamshauri kwamba kwa upnde wa gharama, ni rahisi zaidi kukinunua Amazon.com. Lakini yeye alisisitiza kuwa nimpelekee, akanipa na anwani yake.
,
M-Ganda huyu amenikumbusha wa-Ganda wengine niliokutana nao hapa Minnesota, wakajiptia kitabu changu. Mmoja ni Steven Kaggwa ambaye alikuwa anamiliki mgahawa wa Tam Tam. Baada ya kukisoma kitabu hiki, aliniambia kuwa aliwaelezea wafanya kazi wake. Mmoja wao, Sally, hakuishia tu kujinunulia nakala, bali alinunua nakala nyingine ambayo aliniambia alikuwa anampelekea mkuu wake wa kazi, ambaye ni m-Marekani. Niliguswa na taarifa ya huyu mama, kama nilivyoguswa miaka michache baadaye, wakati mama mmoja kutoka Togo alivyonunua nakala za kitabu hiki kwa ajili ya wakuu wa kazini kwake, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

M-Ganda mwingine ninayemkumbuka nilikutana naye katika tamasha la vitabu ambalo nilikuwa ninashiriki. Alikuwa amefika kikazi hapa Minnesota, lakini alikuja kwenye tamasha hilo, na ndipo tulipofahamiana. Bila kusita alinunua kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differenes, akaenda zake. Yeye na hao wengine wameniacha nikitafakari jinsi hao wenzetu walivyo. Ninaona kuwa sio tu wameenda shule, bali wameelimika, kwani uthibitisho wa kuelimika ni kuwa na hamu ya kutafuta elimu hata baada ya kumaliza shule.

Thursday, September 15, 2016

Ujumbe kwa Ndugu na Marafiki

Napenda kuwajulisha ndugu na marafiki kuwa leo tumemaliza wiki ya kwanza ya muhula mpya wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Nimeanza vizuri, kama nilivyogusia katika blogu hii, kwa ari kubwa. Wanafunzi wanaonekana wenye ari ya kujifunza. Sitawaangusha.

Tarehe 17 mwezi uliopita ilikuwa ni kumbukumbu ya kuzaliwa kwangu. Nilitimiza miaka 65 ya maisha yangu. Ninavyoingia mwaka wa 66, ninamshukuru Mungu kwa kuniweka hai na mwenye uwezo wa kutekeleza majukumu yangu kama nilivyozoea.

Uhai na afya ni baraka kutoka kwa Mungu. Nitaendelea kutumia fursa hii, ambayo ni dhamana, kwa kufanya kazi zangu za kufundisha kwa juhudi yote na uadilifu, kusoma kwa bidii, na kuandika ili kuuneemesha ulimwengu kwa elimu.

Nawaombeni ndugu na marafiki mniombee ili nizingatie mwelekeo huo, nami nawaombea baraka na mafanikio.

Wednesday, October 28, 2015

Maprofesa na Wajibu wa Kuandika

Profesa ni mtu aliyefikia kiwango cha juu cha ufanisi katika ufundishaji, utafiti, uandishi, na kutoa ushauri kwa jamii katika masuala mbali mbali yanayohusiana na utaalam wake. Siwezi kuongelea hapa vipengele vyote vya suala hili, kama vile vigezo vinavyotumika katika kupima ufanisi wa mhusika hadi kumfikisha kwenye hadhi ya uprofesa. Ninakumbushia tu suala la wajibu wa profesa wa kuandika.

Baadhi yetu wa-Tanzania tumeliwazia na kuliongelea suala hili kwa miaka mingi, kwa manufaa ya jamii, tukiliunganisha na masuala kama sera ya elimu, matatizo ya uchapishaji, na kukosekana kwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu.

Kilichonifanya nirejeshe mada hii leo ni kwamba nimejikumbusha tamko la Rais Kikwete, "Maprofesa Wananisikitisha," ambalo lilijadiliwa katika blogu yangu hii na blogu ya Profesa Matondo. Mambo yaliyosemwa katika majadiliano yale ni muhimu na yataendelea kuwa muhimu. Wajibu wa profesa wa kuandika, kama njia mojawapo ya kufundisha na kuchangia maendeleo ya taaluma ni jambo lililo wazi.

Hata hivi, kwa kuzingatia kuwa dunia inabadilika muda wote, kuna umuhimu wa kulitafakari suala hili kwa mtazamo unaozingatia mabadiliko haya. Fikra zilizokuwa sahihi miaka michache iliyopita, huenda zimepitwa na wakati. Wataalam katika nyanja mbali mbali, kama vile ujasiriamali, elimu, na biashara wanatufundisha kuwa mabadiliko yanatulazimisha kuwa wabunifu na wepesi wa kubadilisha fikra, mahusiano, mbinu na utendaji wetu. Ndio maana ni muhimu kusoma daima na kujielimisha kwa njia zingine.

Katika dunia ya utandawazi wa leo, ambamo tekinolojia mbali mbali zinastawi, zikiwemo tekinolojia za mawasiliano, tunawajibika kuwa na fikra mpya kuhusu usomaji, uchapishaji na uuzaji wa vitabu, na kadhalika. Shughuli nyingi sasa zinafanyika mtandaoni, ikiwemo ufundishaji, kama nilivyowahi kugusia katika blogu hii. Tunawajibika kufunguka akili na kuacha kujifungia katika hiki tunachokiita sera ya elimu ya Tanzania. Je, inawezekana kuandika kitabu chenye umuhimu kwa Tanzania lakini si kwa ulimwengu? Taaluma inaweza kufungiwa katika mipaka ya nchi? Kuna dhana katika ki-Ingereza tunayopaswa kuitafakari: "The local is global."

Naona ni jambo jema kuirejesha mada hii, tuendelee kuitafakari katika mazingira ya leo. Lakini, naona tusome kwanza mjadala uliofanyika katika blogu hii na blogu ya Profesa Matondo.

Thursday, February 26, 2015

Leo Nimefundisha Darasa Kwa Kutumia "Skype"

Asubuhi ya leo, nimefundisha darasa kwa kutumia "Skype." Ni darasa la Mwalimu Kristofer Olsen la somo la "Mythologies," katika Chuo Kikuu cha Montana, Marekani. Chuo hiki kiko mjini Bozeman, maili 995 kutoka hapa nilipo, Northfield, Minnesota. Niliandika kuhusu mpango wa kufundisha darasa hili katika blogu hii.

Katika mawasiliano ya barua pepe na Mwalimu Olsen, aliniuliza iwapo ningeweza kuongea na darasa lake la "Mythologies," ambalo lilikuwa linasoma kitabu changu cha Matengo Folktales. Aliniletea silabasi ya somo, inayoonyesha kuwa tarehe 24 na 26 wangejadili Matengo Folktales.

Jana jioni, binti yangu Zawadi alinielekeza tena namna ya kutumia "Skype," na alinisajili. Leo asubuhi, kipindi kilianza kama ilivypoangwa, saa nne na nusu za hapa Minnesota, ambayo ni saa tatu na nusu kule Montana. Nilikuwa mbele ya kompyuta, na wanafunzi na profesa wao walikuwa wananiona na kunisikia, nami nilikuwa nawaona na kuwasikia.

Tulifanya mengi. Niliombwa kusimulia hadithi mojawapo, ambayo ingechukua muda mfupi, nami nikasimulia hadithi ya "Hawk and Crow," iliyomo kitabuni. Niliwaambia wanafunzi kuwa kokote niendako kuongelea hadithi za jadi, huzisimulia papo kwa papo, badala ya kuzisoma. Katika kusimulia hadithi ya "Hawk and Crow," niliwaeleza machache kuhusu namna hadithi inavyosimuliwa, tofauti na inavyoonekana kimaandishi.

Masuali yao yalikuwa ya maana sana. Suali moja lilihusu jinsi nilivyorekodi hadithi na kuandaa kitabu cha Matengo Folktales. Suali jingine lilihusu mchakato wa kutafsiri. Jingine lilihusu vifo na mauaji katika hadithi hizo. Jingine lilihusu mhusika mjanja ("trickster") katika hadithi, kama vile Anansi na Sungura.

Niliwaeleza mambo kadhaa kuhusu mhusika huyu, katika tamaduni mbali mbali. Mhusika huyu hujitokeza kama mnyama (kama vile Anansi au Gizo, Kobe na Sungura), na katika tamaduni zingine hujitokeza katika umbo la binadamu, kama vile Nasreddin Hodja na Abu Nuwas. Niliongelea asili na maana ya mhusika huyu katika jamii, kwa kutumia nadharia za kisaikolojia za Carl Jung.

Niliguswa kwa namna ya pekee nilipoulizwa nifafanue dhana iliyomo katika blogu yangu kwamba ninaliona darasa kuwa ndio mahali pekee penye uhuru kamili wa kufikiri na kujieleza. Kumbe kuna watu wanaosoma blogu yangu kwa makini kiasi hiki.

Mawasiliano kama haya ya kutumia "Skype" ni maendeleo ya tekinolojia, ambayo yanatuwezesha kufanya mambo ambayo hatukuweza kuyafanya kabla. Jambo moja la kujifunza ni kuwa tunaweza kuendesha darasa bila kukutana katika chumba kimoja. Mimi kama mwalimu, ninaweza kuwafundisha wa-Tanzania ingawa niko nje ya Tanzania. Tuachane na mawazo kwamba sherti nirudi Tanzania ili kujenga nchi.

Wakati tekinolojia inasonga mbele na kutufungulia milango mipya, inashangza kuona jinsi wa-Tanzania kwa ujumla wanavyoendelea kuwa na mawazo yaliyopitwa na wakati. Kila ninapowasikia wakidai kuwa wataalam walioko nje warudi nyumbani wakajenge Taifa, nawazia suala hilo. Najiuliza ni lini wataamka usingizini na kutambua kuwa maendeleo ya tekinolojia ya mawasiliano yanazidi kuififisha mipaka ya kijiografia tuliyoizoea. Tunaingia kwenye dunia isiyo na mipaka, dunia ambamo mtu popote alipo anaweza akatoa mchango wake kwa walimwengu popote.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...