Showing posts with label tekinolojia. Show all posts
Showing posts with label tekinolojia. Show all posts

Monday, November 13, 2017

Mwongozo wa Riwaya ya "Things Fall Apart"

Mimi mwalimu wa fasihi ya ki-Ingereza. Kati ya mambo ninayofanya ni kuandika miongozo ya fasihi. Nimeshaandika miongozo kadhaa, ikiwemo mwongozo wa Things Fall Apart, riwaya ya Chinua Achebe.

Nimeridhika kuwa mwongozo huu una mawazo muhimu ya kumwezesha mwalimu, mwanafunzi, na msomaji yeyote kuelewa mambo mapya juu ya Things Fall Apart na pia juu ya nadharia ya fasihi. Leo nimezipitia kurasa kadhaa, nikafurahia niliyoandika juu ya mhusika aitwaye Unoka.

Suali ni je, mwongozo huu unawafikia wanafunzi wa waalimu wa Tanzania? Ni wazi kuwa ningependa wafaidike nao, kama wanavyofaidika wanafunzi na wengine nje ya Tanzania, kama vile hapa Marekani. Ningekuwa na uwezo, ningepeleka nakala katika shule na vyuo vyote.

Kwa bahati nzuri, kitabu kinapatikana mtandaoni kama kitabu pepe. Ninafahamu kuwa kuna watu Tanzania ambao wanaweza kuagiza vitabu vya aina hiyo. Ninaamini kuwa kadiri siku zinavyokwenda na tekinolojia kuenea, wengi zaidi watakuwa na uwezo huo. Kwa hivi, nina matumaini makubwa kwa siku za usoni.

Njia nyingine ni kusafirisha vitabu. Mimi mwenyewe, kila ninapokwenda Tanzania, huchukua vitabu na kuvigawa kwenye maktaba na vyuo. Kuna wa-Tanzania wengi huku nje, ambao nao huenda Tanzania. Kama kungekuwa na nia ya kuchangia elimu, ingekuwa rahisi wao pia kuchukua vitabu. Vitu vingine wanachukua, kwa nini washindwe kuchukua vitabu?

Sunday, February 12, 2017

Nimemaliza Kusoma The Highly Paid Expert

Leo nimemaliza kusoma The Highly Paid Expert, kitabu kilichotungwa na Debbie Allen, ambacho nilikitaja katika blogu hii. Nimekifurahia kitabu hiki, kwa jinsi kilivyoelezea misingi na mbinu za kumwezesha mtu kuwa mtoa ushauri mwenye mafanikio kwake na kwa wateja.

Mambo anayoelezea mwandishi Debbie Allen yananihusu moja kwa moja katika ya kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants. Kwa hivi, kitabu hiki kimekuwa na mvuto wa pekee kwangu. Nimevutiwa na namna mwandishi anavyoelezea mbinu za mtu kujijenga katika uwanja wake hadi kufikia kileleni. Anaelezea mategemeo ya wateja na namna ya kushughulika nao. Anaelezea umuhimu wa kujifunza kutoka kwa wataalam wengine, matumizi ya tekinolojia katika kuwasiliana na wateja, kuendesha mikutano, na kujitangaza. Vile vile anasisitiza uaminifu na uwajibikaji.

Ameelezea vizuri namna wengi wetu tunavyoshindwa kujitangaza na tunavyoshindwa au kusita kutambua umaarufu na umuhimu wetu na thamani ya ujuzi wetu, jambo ambalo linatufanya tusitegemee malipo yanayoendana na ubingwa wetu. Tunaridhika na malipo hafifu, wakati tulistahili malipo makubwa.

Sura ya 24 ya The Highly Paid Expert inaelezea uandishi wa kitabu. Mwandishi anasema kuwa kitabu ni nyenzo muhimu ya mtaalam katika fani yake. Kitabu kinamjengea sifa na kuonekana. Kinamfanya mtaalam aaminike. Mwandishi anaeleza wazi kuwa kitabu hakileti utajiri, bali kinafungua milango ya fursa.

Hayo nimejionea mwenyewe. Kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimenifungulia fursa nyingi. Nimepata mialiko ya kwenda kutoa mihadhara au ushauri katika taasisi na jumuia mbali mbali, kama vile makanisa, vyuo, na makampuni.

Nimevutiwa na mambo anayoelezea mwandishi wa The Highly Paid Expert kuhusu uandishi na uuzaji wa kitabu. Yanafanana na yale ambayo nami nimekuwa nikieleza katika blogu hii. Kwa mfano, anasema kuwa jukumu kubwa la kutangaza na kuuza kitabu ni la mwandishi.

The Highly Paid Expert ni kati ya vitabu ambavyo nimevifurahia kwa dhati. Mawaidha yake mengi ni ya kukumbukwa daima. Mfano ni msisitizo wake juu ya kushirikiana na wengine. Mtu hufanikiwi kwa uwezo wako mwenyewe tu na kutojihusisha na wengine wenye utaalam, hata kama ni washindani wako.

Thursday, December 29, 2016

Vitabu Tulivyosoma Mwaka 2016

Zikiwa zimebaki siku mbili tu kabla ya kwisha mwaka 2016, nimeona wa-Tanzania kadhaa wakijitokeza katika mtandao wa Facebook na kutaja vitabu walivyosoma mwaka huu. Jambo hili limenifurahisha, nikizingatia kuwa nimekuwa nikihamasisha usomaji wa vitabu, kwa kutumia blogu yangu hii, blogu za wengine, na pia katika kitabu changu, CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Ninawapongeza watu hao kwa kuonyesha mfano mzuri. Ninawapongeza pia wasomaji waliojitokeza na kuchangia suala hili kwa namna mbali mbali, kama vile kuvijadili vitabu hivyo, kuulizia upatikanaji wake, au kupendekeza vitabu vingine. Kuhusu upatikanaji wa vitabu, watu wamepeana taarifa za maduka ya vitabu, na pia upatikanaji wa vitabu pepe mtandaoni. Ni jambo la kuvutia kwamba kuna wa-Tanzania wanaotambua matumizi ya manufaa ya tekinolojia ya mtandao.

Mazungumzo haya yameonyesha mambo kadhaa. Jambo moja ni kuwa wako wa-Tanzania wanaojibidisha kusoma vitabu. Jambo jingine ni kuwa wanasoma vitabu vya aina mbali mbali, kama vile vya siasa, ujasiriamali, fasihi, na maendeleo ya jamii au ya mtu binafsi. Vile vile wanasoma vitabu vya waandishi wa mataifa mbali mbali, vya ki-Swahili na vya ki-Ingereza. Jambo jingine ni kuwa wahusika wameonyesha moyo mkubwa wa kusaidiana, kama vile kwa kufahamishana vitabu bora na hata kuazimishana vitabu.

Ninawaenzi watu hao. Huenda wakawa chachu ya kustawisha utamaduni wa kusoma vitabu nchini Tanzania. Laiti watu wengi zaidi wangejumuika katika safari hii. Laiti kama watu maarufu nchini mwetu, kama vile wanasiasa na wasanii, wangejiunga na kuwa wahamasishaji wa usomaji wa vitabu. Kutokana na mvuto wa wasanii wetu, kwa mfano, wangeweza kuwa wahamasishaji wa watoto na vijana katika kupenda kusoma vitabu.

Kwa upande wangu, naona sihitaji kuorodhesha vitabu nilivyosoma mwaka 2016. Mara kwa mara, katika blogu hii au blogu ya ki-Ingereza, ninaandika taarifa za baadhi ya vitabu ninavyosoma. Vingine ni vile ninavyofundisha chuoni St. Olaf, na vingine ni vile ninavyojisomea mwenyewe. Ninapoandika  taarifa, ninajitahidi kuelezea upekee au ubora wa vitabu hivyo.

Wednesday, October 28, 2015

Maprofesa na Wajibu wa Kuandika

Profesa ni mtu aliyefikia kiwango cha juu cha ufanisi katika ufundishaji, utafiti, uandishi, na kutoa ushauri kwa jamii katika masuala mbali mbali yanayohusiana na utaalam wake. Siwezi kuongelea hapa vipengele vyote vya suala hili, kama vile vigezo vinavyotumika katika kupima ufanisi wa mhusika hadi kumfikisha kwenye hadhi ya uprofesa. Ninakumbushia tu suala la wajibu wa profesa wa kuandika.

Baadhi yetu wa-Tanzania tumeliwazia na kuliongelea suala hili kwa miaka mingi, kwa manufaa ya jamii, tukiliunganisha na masuala kama sera ya elimu, matatizo ya uchapishaji, na kukosekana kwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu.

Kilichonifanya nirejeshe mada hii leo ni kwamba nimejikumbusha tamko la Rais Kikwete, "Maprofesa Wananisikitisha," ambalo lilijadiliwa katika blogu yangu hii na blogu ya Profesa Matondo. Mambo yaliyosemwa katika majadiliano yale ni muhimu na yataendelea kuwa muhimu. Wajibu wa profesa wa kuandika, kama njia mojawapo ya kufundisha na kuchangia maendeleo ya taaluma ni jambo lililo wazi.

Hata hivi, kwa kuzingatia kuwa dunia inabadilika muda wote, kuna umuhimu wa kulitafakari suala hili kwa mtazamo unaozingatia mabadiliko haya. Fikra zilizokuwa sahihi miaka michache iliyopita, huenda zimepitwa na wakati. Wataalam katika nyanja mbali mbali, kama vile ujasiriamali, elimu, na biashara wanatufundisha kuwa mabadiliko yanatulazimisha kuwa wabunifu na wepesi wa kubadilisha fikra, mahusiano, mbinu na utendaji wetu. Ndio maana ni muhimu kusoma daima na kujielimisha kwa njia zingine.

Katika dunia ya utandawazi wa leo, ambamo tekinolojia mbali mbali zinastawi, zikiwemo tekinolojia za mawasiliano, tunawajibika kuwa na fikra mpya kuhusu usomaji, uchapishaji na uuzaji wa vitabu, na kadhalika. Shughuli nyingi sasa zinafanyika mtandaoni, ikiwemo ufundishaji, kama nilivyowahi kugusia katika blogu hii. Tunawajibika kufunguka akili na kuacha kujifungia katika hiki tunachokiita sera ya elimu ya Tanzania. Je, inawezekana kuandika kitabu chenye umuhimu kwa Tanzania lakini si kwa ulimwengu? Taaluma inaweza kufungiwa katika mipaka ya nchi? Kuna dhana katika ki-Ingereza tunayopaswa kuitafakari: "The local is global."

Naona ni jambo jema kuirejesha mada hii, tuendelee kuitafakari katika mazingira ya leo. Lakini, naona tusome kwanza mjadala uliofanyika katika blogu hii na blogu ya Profesa Matondo.

Thursday, February 26, 2015

Leo Nimefundisha Darasa Kwa Kutumia "Skype"

Asubuhi ya leo, nimefundisha darasa kwa kutumia "Skype." Ni darasa la Mwalimu Kristofer Olsen la somo la "Mythologies," katika Chuo Kikuu cha Montana, Marekani. Chuo hiki kiko mjini Bozeman, maili 995 kutoka hapa nilipo, Northfield, Minnesota. Niliandika kuhusu mpango wa kufundisha darasa hili katika blogu hii.

Katika mawasiliano ya barua pepe na Mwalimu Olsen, aliniuliza iwapo ningeweza kuongea na darasa lake la "Mythologies," ambalo lilikuwa linasoma kitabu changu cha Matengo Folktales. Aliniletea silabasi ya somo, inayoonyesha kuwa tarehe 24 na 26 wangejadili Matengo Folktales.

Jana jioni, binti yangu Zawadi alinielekeza tena namna ya kutumia "Skype," na alinisajili. Leo asubuhi, kipindi kilianza kama ilivypoangwa, saa nne na nusu za hapa Minnesota, ambayo ni saa tatu na nusu kule Montana. Nilikuwa mbele ya kompyuta, na wanafunzi na profesa wao walikuwa wananiona na kunisikia, nami nilikuwa nawaona na kuwasikia.

Tulifanya mengi. Niliombwa kusimulia hadithi mojawapo, ambayo ingechukua muda mfupi, nami nikasimulia hadithi ya "Hawk and Crow," iliyomo kitabuni. Niliwaambia wanafunzi kuwa kokote niendako kuongelea hadithi za jadi, huzisimulia papo kwa papo, badala ya kuzisoma. Katika kusimulia hadithi ya "Hawk and Crow," niliwaeleza machache kuhusu namna hadithi inavyosimuliwa, tofauti na inavyoonekana kimaandishi.

Masuali yao yalikuwa ya maana sana. Suali moja lilihusu jinsi nilivyorekodi hadithi na kuandaa kitabu cha Matengo Folktales. Suali jingine lilihusu mchakato wa kutafsiri. Jingine lilihusu vifo na mauaji katika hadithi hizo. Jingine lilihusu mhusika mjanja ("trickster") katika hadithi, kama vile Anansi na Sungura.

Niliwaeleza mambo kadhaa kuhusu mhusika huyu, katika tamaduni mbali mbali. Mhusika huyu hujitokeza kama mnyama (kama vile Anansi au Gizo, Kobe na Sungura), na katika tamaduni zingine hujitokeza katika umbo la binadamu, kama vile Nasreddin Hodja na Abu Nuwas. Niliongelea asili na maana ya mhusika huyu katika jamii, kwa kutumia nadharia za kisaikolojia za Carl Jung.

Niliguswa kwa namna ya pekee nilipoulizwa nifafanue dhana iliyomo katika blogu yangu kwamba ninaliona darasa kuwa ndio mahali pekee penye uhuru kamili wa kufikiri na kujieleza. Kumbe kuna watu wanaosoma blogu yangu kwa makini kiasi hiki.

Mawasiliano kama haya ya kutumia "Skype" ni maendeleo ya tekinolojia, ambayo yanatuwezesha kufanya mambo ambayo hatukuweza kuyafanya kabla. Jambo moja la kujifunza ni kuwa tunaweza kuendesha darasa bila kukutana katika chumba kimoja. Mimi kama mwalimu, ninaweza kuwafundisha wa-Tanzania ingawa niko nje ya Tanzania. Tuachane na mawazo kwamba sherti nirudi Tanzania ili kujenga nchi.

Wakati tekinolojia inasonga mbele na kutufungulia milango mipya, inashangza kuona jinsi wa-Tanzania kwa ujumla wanavyoendelea kuwa na mawazo yaliyopitwa na wakati. Kila ninapowasikia wakidai kuwa wataalam walioko nje warudi nyumbani wakajenge Taifa, nawazia suala hilo. Najiuliza ni lini wataamka usingizini na kutambua kuwa maendeleo ya tekinolojia ya mawasiliano yanazidi kuififisha mipaka ya kijiografia tuliyoizoea. Tunaingia kwenye dunia isiyo na mipaka, dunia ambamo mtu popote alipo anaweza akatoa mchango wake kwa walimwengu popote.

Thursday, May 6, 2010

Vitabu Pepe

Kadiri siku zinavyopita na mabadiliko ya aina aina kutokea, yakiwemo mabadiliko ya tekinolojia, lugha nayo inawajibika kukabiliana na mabadiliko haya.

Katika kuyamudu mabadiliko katika uwanja wa uandishi wa barua, kwa mfano, leo hii tuna kitu kiitwacho barua pepe. Zamani tulizoea barua ya karatasi na bahasha. Lakini leo tunaandika barua pepe, bila karatasi.

Kama ninavyoeleza hapa na katika kitabu cha Changamoto, ulimwengu wa vitabu nao unabadilika kufuatana na mabadiliko ya tekinolojia. Leo vitabu vinaandikwa na kusomwa bila karatasi, sawa na barua pepe. Sasa sijui vitabu hivi tutaviita vitabu pepe au vipi.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...