Showing posts with label Things Fall Apart. Show all posts
Showing posts with label Things Fall Apart. Show all posts

Monday, November 13, 2017

Mwongozo wa Riwaya ya "Things Fall Apart"

Mimi mwalimu wa fasihi ya ki-Ingereza. Kati ya mambo ninayofanya ni kuandika miongozo ya fasihi. Nimeshaandika miongozo kadhaa, ikiwemo mwongozo wa Things Fall Apart, riwaya ya Chinua Achebe.

Nimeridhika kuwa mwongozo huu una mawazo muhimu ya kumwezesha mwalimu, mwanafunzi, na msomaji yeyote kuelewa mambo mapya juu ya Things Fall Apart na pia juu ya nadharia ya fasihi. Leo nimezipitia kurasa kadhaa, nikafurahia niliyoandika juu ya mhusika aitwaye Unoka.

Suali ni je, mwongozo huu unawafikia wanafunzi wa waalimu wa Tanzania? Ni wazi kuwa ningependa wafaidike nao, kama wanavyofaidika wanafunzi na wengine nje ya Tanzania, kama vile hapa Marekani. Ningekuwa na uwezo, ningepeleka nakala katika shule na vyuo vyote.

Kwa bahati nzuri, kitabu kinapatikana mtandaoni kama kitabu pepe. Ninafahamu kuwa kuna watu Tanzania ambao wanaweza kuagiza vitabu vya aina hiyo. Ninaamini kuwa kadiri siku zinavyokwenda na tekinolojia kuenea, wengi zaidi watakuwa na uwezo huo. Kwa hivi, nina matumaini makubwa kwa siku za usoni.

Njia nyingine ni kusafirisha vitabu. Mimi mwenyewe, kila ninapokwenda Tanzania, huchukua vitabu na kuvigawa kwenye maktaba na vyuo. Kuna wa-Tanzania wengi huku nje, ambao nao huenda Tanzania. Kama kungekuwa na nia ya kuchangia elimu, ingekuwa rahisi wao pia kuchukua vitabu. Vitu vingine wanachukua, kwa nini washindwe kuchukua vitabu?

Wednesday, March 22, 2017

Kitabu kwa Wasafiri Watokao Nebraska

Leo nimeona taarifa kutoka sinodi ya Nebraska ya Kanisa la Kiluteri la Marekani, kuhusu maandalizi ya safari za kwenda Tanzania. Safari hizo zimefanyika tangu miaka iliyopita. Kuna sehemu iitwayo "Preparatory Reading," na kama miaka iliyopita, katika sehemu hiyo kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimependekezwa kwa wasafiri hao:

For those persons wanting to more deeply explore cultural differences between Africans and Americans, the book Africans and Americans: Embracing Cultural Differences by Joseph Mbele is recommended. The book is available at www.africonxion.com.

Kwangu kama mwandishi, hii ni habari njema, ingawa si mpya. Viongozi wa programu kama hiyo ya Nebraska wana uzoefu wa miaka mingi wa kwenda Tanzania. Wana uzoefu wa utamaduni wa Tanzania. Kuendelea kwao kukipendekeza kitabu changu ni ushahidi kuwa wameona kinawafaa wa-Marekani wanaowapeleka Tanzania.

Watu kutoka Nebraska wanaosairi kwenda Tanzania nimewahi kuwataja katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Ninajisikia kama vile, kwa njia ya kitabu changu, nina uhusiano wa kudumu nao.

Nimeandika nilivyoandika, ingawa ninafahamu kuwa kwa mujibu wa utamaduni wa leo wa Tanzania, tunaogopa kuambiwa tunaringa. Ninaamini kuwa ni sahihi mtu kujivunia kazi yake na mafanikio yake, kama wafanyavyo wanamuziki wetu, ambao aghalabu tunawasikia wakitamba wanapoandaa albamu au wimbo wa kutupagawisha. Tunapowasikia wakisema hivyo, tunafurahi na kusubiri kwa hamu.

Lakini ni ajabu kuwa tunaona si sahihi kwa mwanataaluma kujivunia kazi yake. Lakini ninaona tujikumbushe kauli iliyomo katika "Azimio la Arusha" kuwa katika nchi yetu, kazi iwe ni kitu cha kujivunia; na uvivu, ulevi, na uzembe viwe ni vitu vya kuvionea aibu. "Azimio la Arusha" linazungumzia kila kazi yenye manufaa kwa mtu na jamii.

Kama kichekesho, ninakumbushia methali iliyomo katika riwaya ya Things Fall Apart ya Chinua Achebe: "The lizard that jumped from the high iroko tree to the ground said he would praise himself if no one else did," ambayo inamaanisha kuwa ukifanikisha jambo, usichelee kujisifu mwenyewe. Labda huo ndio utamaduni tunaouhitaji.

Saturday, November 5, 2016

Mteja wa Uingereza Kanunua Kitabu

Leo kwenye tovuti ninapochapisha vitabu vyangu nimeona kuwa mteja aliyeko Uingereza amenunua nakala ya Notes on Achebe's Things Fall Apart. Uzuri wa uchapishaji wa namna hii ninayotumia ni kuwa mwandishi unaweza kufuatilia taarifa kama hizi za mauzo, ukajua kitabu kimenunuliwa sehemu gani ya dunia, nakala ngapi, na malipo yako ni kiasi gani.

Kwa miaka yote tangu nilipoanza kuchapisha vitabu kwenye tovuti ya lulu.com maelfu ya wateja walionunua vitabu vyangu wamefanya hivyo kutokea hapa Marekani. Nilikuwa na hisia kuwa hii ni kwa kuwa utamaduni wa kununua vitu mtandaoni ulikuwa bado kujengeka sehemu zingine za dunia.

Ninahisi kuwa huyu mteja aliyenunua Notes on Achebe's Things Fall Apart ni mwalimu wa fasihi. Kama ni hivyo, ninafurahi kuwa atapata mawazo mapya juu ya Things Fall Apart. Ingawa kuna miongozo mingi ya Things Fall Apart, mwongozo wangu umepata umaarufu hata ukateuliwa kama mwongozo kwa wanafunzi katika chuo kikuu cha Cornell, ambacho kina jina kubwa katika masomo ya lugha na fasihi ya ki-Ingereza.

Vile vile, hivi karibuni, nilipohudhuria mkutano wa Africa Network, profesa Eric Michael Washington wa chuo cha Calvin aliniambia jinsi anavyotumia mawazo yaliyomo katika mwongozo huo, katika ufundishaji wake wa Things Fall Apart. Alisema anavutiwa zaidi na jinsi ninavyomwelezea mhusika aitwaye Unoka.

Mambo hayo yananipa hamasa ya kuendelea kuandika miongozo ya kazi za fasihi, azma ambayo niliwahi kuielezea katika blogu hii. Mimi kama mwalimu wa fasihi ninafarijika kuyaweka hadharani mawazo yangu kuhusu fasihi, ambayo yatadumu. 

Saturday, April 23, 2016

Ujumbe Mzuri Kutoka kwa Mwanafunzi

Leo nimepata ujumbe mzuri kutoka kwa m-Tanzania ambaye simfahamu. Amejitambulisha kwamba alipokuwa mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule ya sekondari ya Namtumbo, alisoma mwongozo wangu juu ya Things Fall Apart na Song of Lawino. Nimefurahi kusikia habari hii ya kusomwa maandishi yangu sehemu ya mbali kama Namtumbo ambayo iko njiani baina ya Songea na Tunduru.

Inawezekana kuwa huyu mtu alimaanisha kijitabu changu ambacho kilikuwa na mwongozo wa Things Fall Apart na The African Child, ambao niliuelezea katika blogu hii. Ni hivi karibuni tu nimechapisha mwongozo wa Song of Lawino. Si hoja, ili mradi watu wasome ninayoandika.

Mimi ni mwalimu, na dhana yangu ya ufundishaji ni pana. Inajumlisha ninavyofundisha darasani, ninavyoandika na kuchapisha vitabu na makala, ninavyoblogu, ninavyoshiriki matamasha ya vitabu na utamaduni, ninavyoongea na watu ana kwa ana, kama vile mitaani, ninavyoendesha warsha, ninavyoshiriki mijadala mitandaoni, na kadhalika.

Mwalimu si mtu wa kuficha mawazo na mitazamo yake. Hachelei kujieleza. Ni wajibu wake. Mwalimu wa Chuo kikuu ana wajibu wa pekee wa  kufanya utafiti na kuandika vitabu na makala ili kuchangia taaluma. Anawajibika kwa wanataaluma wenzake na pia kwa jamii. Huu wajibu mpana ndio unanifanya nijishughulishe na jamii katika nyanja kama magazeti, blogu, mitandao. Miongozo ninayoandika juu ya kazi za fasihi ni sehemu ya azma hii ya kuisogeza taaluma katika jamii.

Mwongozo wangu wa Things Fall Apart alioongelea huyu mtu inaonekana ni wa mwanzo mwanzo. Nilifanya juhudi kuuboresha. Uthibitisho wa ubora wake ni kwamba unapendekezwa kwa wanafunzi hapa Marekani wanaosoma Things Fall Apart, kama ilivyofanywa na Chuo Kikuu cha Cornell. Ninafurahi kwamba ninatoa mchango wangu kwa namna hiyo, kuanzia Marekani hadi Namtumbo.

Thursday, April 4, 2013

Mhadhara Katika Darasa la Wazee

Leo nilitoa mhadhara katika darasa la wazee, hapa Northfield. Somo wanalosomea ni "Folk and Fairy Tales."

 Hapa Northfield kuna masomo ambayo wazee husoma, yanayoendeshwa na taasisi iitwayo Cannon Valley Elder Collegium. Nimewahi kufundisha mara tatu darasa la wazee katika mfumo huo, na somo langu lilikuwa "The African Experience." Tulisoma na kujadili kitabu cha Things Fall Apart cha Chinua Achebe kama msingi wa kuongelea hali ya Afrika kabla na baada ya ukoloni, na hali ya leo ya ukoloni mamboleo.

 Nilivyoingia tu darasani leo, nilifurahi kuwaona wazee ambao walishasoma somo langu. Walikuwa yapata nusu ya darasa la leo.

 Nilichangia mawazo kuhusu somo hili la hadithi za fasihi simulizi, nikasimulia hadithi mbili za ki-Matengo ili kuthibitisha na kufafanua yale niliyosema kinadharia. Hadithi nilizosimulia ni "The Monster in the Rice Field" na "Nokamboka and the Baby Monster," ambazo zimo katika kitabu changu cha Matengo Folktales.

Tulikuwa na mazungumzo marefu, kuanzia saa saba na nusu mchana hadi saa tisa. Ilipendeza sana kuwaona wazee hao wakiimba nami wimbo wa ki-Matengo uliomo katika hadithi ya "The Monster in the Rice Field," wimbo unaorudiwa tena na tena. Ilivutia sana, na sote tulifurahi, tukazama katika kuichambua hadithi hii na ile ya "Nokamboka," ambazo zote zimejaa falsafa na masuali kuhusu maisha.

Tuesday, March 26, 2013

Ufundishaji Wangu wa Maandishi ya Achebe

Nimefundisha maandishi ya Chinua Achebe kuanzia miaka ya sabini na kitu. Kabla sijahitimu na shahada ya kwanza Chuo Kikuu Dar es Salaam, mwaka 1976, huenda nilifundisha Things Fall Apart katika shule za sekondari nilikopelekwa kufanya mazoezi ya kufundisha, yaani sekondari ya wasichana Iringa, 1974, na sekondari ya Kinondoni, 1975. Sina hakika.

Lakini baada ya kuhitimu shahada ya kwanza, mwaka 1976, nilipata fursa za kufundisha Things Fall Apart, nikianzia na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambapo nilikuwa mhadhiri. Mwaka 1980, chini ya mkataba wa ushirikiano baina ya Tanzania na Burundi, nilifundisha kwa wiki kadhaa katika Chuo Kikuu cha Burundi. Kitabu kimojawapo kilikuwa Things Fall Apart

Uzoefu huu ulinifanya niandike mwongozo wa Things Fall Apart, ili kuelezea mambo ambayo waandishi wengine hawajayaweka wazi.  Ilikuwa ni fursa kwangu kuwaelezea wanafunzi na walimwengu namna ninavyoichukulia riwaya hii ya Things Fall Apart. Kwa maelezo zaidi ya historia hii, soma hapa. Sihitaji kuficha ukweli kwamba mwongozo huu ni maarufu na wengi wanautumia.

Baada ya kuja kufundisha chuo cha St. Olaf, mwaka 1991, nimefundisha Things Fall Apart na maandishi mengine ya Achebe. Kuna muhula fulani nilitunga kozi nzima juu ya maandishi ya Achebe tu. Tulisoma riwaya zake kadhaa, na pia insha baadhi ya insha zake, zikiwemo "The Novelist at Teacher," "Colonialist Criticism," na "An Image of Africa." Tulisikiliza pia baadhi ya mahojiano yake. Ingekuwa muda unaruhusu, tungesoma pia mashairi yake.

Ni wazi kwamba Things Fall Apart ni moja ya riwaya ambazo nimezifundisha sana. Kila ninapoifundisha, nazua masuala mapya na tafakari mpya. Hiyo ni tabia ya fasihi. Hata misahafu ina tabia hiyo, ingawa wako watu wanaodai kuwa misahafu haibadiliki. Binafsi, kutokana na uzoefu wangu wa kusoma na kutafakari fasihi na maandishi mengine, siamini kwamba kuna andiko lolote, hata msahafu, ambalo haliguswi na mabadiliko, kuanzia na mabadiliko ya lugha na maana zake, ambayo hayakwepeki. Nimegusia suala hilo katika mwongozo wangu.

Monday, March 25, 2013

Achebe wa Enzi za Ujana Wetu

Sisi tuliosoma sekondari miaka ya sitini na kitu tunaikumbuka picha ya Chinua Achebe inayoonekena hapa kushoto. Ndio picha iliyokuwepo kwenye jalada, upande wa nyuma wa kitabu cha Things Fall Apart. Kwa bahati nzuri, ninayo nakala ya miaka ile ya Things Fall Apart. Niliipata miaka ya karibuni, nikaona niwe nayo, angalau kujikumbusha enzi za ujana wetu. Ninazo pia nakala za matoleo ya hivi karibuni, lakini ile ya zamani niliiona kama lulu.

Kuanzia mwaka 1966 hadi 1970 nilikuwa mwanafunzi wa sekondari, seminari ya Likonde. Wakati huo riwaya ya Things Fall Apart ilikuwa maarufu. Tulivijua pia vitabu vya watoto ambavyo Achebe alikuwa ameandika. Navikumbuka viwili: The Sacrificial Egg and Other Short Stories na Chike and the River. Shule yetu ilikuwa na maktaba kubwa na nzuri sana. Nidhamu ya kusoma ilikuwa kali, chini ya usimamizi wa mapadri waliokuwa waalimu wetu.

Miaka ile ile, Achebe alichapisha riwaya ya No Longer at Ease na Arrow of God na A Man of the People. Tulikuwa tunamsoma Achebe sambamba na Cyprian Ekwensi. Baadhi ya vitabu vya Ekwensi ambavyo tulivisoma ni Burning Grass, na People of the City na Jagua Nana. Hao wawili walikuwa kama mafahali wawili kutoka Nigeria katika uwanja wa uandishi.

Katika seminari ya Likonde, mwalimu wangu wa ki-Ingereza alikuwa Padri Lambert Doerr OSB, m-Jerumani, ambaye sasa ni askofu mstaafu pale Peramiho. Sidhani kama nimewahi kukutana na mtu anayesoma vitabu kama yeye. Alituwekea amri kwamba tusome angalau kitabu kimoja cha hadithi ya ki-Ingereza kwa wiki. Kitabu kimoja ilikuwa ni kiwango cha chini, lakini usikae wiki bila kumaliza angalau kitabu.

Padri Lambert alikuwa na mtindo wa kugawa daftari kwa kila mwanafunzi ambamo tulipaswa kuelezea kuhusu vitabu tulivyosoma, au ambavyo tulidai tumesoma. Wakati wowote alikuwa anaitisha daftari lako, ili akusikie ukimweleza habari ya kitabu chochote ulichokiorodhesha humo. Kumdanganya ilikuwa haiwezekani, wala huthubutu. Matokeo ya hayo ni kuwa kila mmoja wetu alisoma vitabu vingi sana, na ufahamu wetu wa ki-Ingereza ulikuwa mkubwa kabisa. Achebe, kwa uandishi wake wa kuvutia, alichangia kwa kiasi kikubwa kutufanya tupende kusoma.

Friday, March 22, 2013

Buriani, Chinua Achebe

Msiba mzito umetufika leo, wasomaji wa fasihi na walimwengu kwa ujumla. Chinua Achebe amefariki, akiwa na umri wa miaka 82.

Maarufu kama muasisi wa fasihi ya ki-Ingereza katika Afrika, Chinua Achebe ametoa mchango mkubwa katika uandishi, mchango ambao uliiweka Afrika mahala pazuri katika ramani ya fasihi ya dunia.

Tangu alipochapisha riwaya yake maarufu, Things Fall Apart, hadi kufariki kwake, Achebe ameandika riwaya, hadithi fupi, na insha kuhusu fasihi, uandishi, siasa na utamaduni. Amefanya mahojiano mengi, ambayo, kwa bahati nzuri yanapatikana mtandaoni au katika vitabu na majarida.

Achebe aliamini kwa dhati kuwa jukumu la msanii ni kuwa mwalimu wa jamii. Yeye mwenyewe amezingati wajibu huo tangu ujana wake, alipochapisha Things Fall Apart, hadi kurariki kwake. Amewafundisha waAfrika mengi kuhusu jamii yao, udhaifu na uwezo wao, na amewafundisha walimwengu kuwaona wa-Afrika kwa mtazamo tofauti na ule wa wakoloni. Amewafundisha walimwengu maana ya ubinadamu, ambayo inavuka mipaka ya kabila, taifa, dini, jinsia au nchi.

Sikupata fursa ya kukutana uso kwa uso na Chinua Achebe, bali nimesoma na kufundisha maandishi yake mara kwa mara. Nashukuru pia kuwa nilipata wazo la kuandika mwongozo wa Things Fall Apart. Kwa namna hiyo ya kusoma na kutafakari maandishi yake, najiona kama vile nami nimekutana na mwandishi huyu. Nimalizie tu kwa kusema kwamba kwa mchango wake mkubwa kwa walimwengu, Achebe atakumbukwa daima.

Sunday, January 2, 2011

Mwongozo wa "Things Fall Apart"

Nimefundisha riwaya ya Things Fall Apart ya Chinua Achebe tangu yapata mwaka 1976, sehemu kama Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Burundi, na vyuo vya Colorado na St. Olaf.

Kutokana na uzoefu huu, na mengi niliyojifunza, na kwa lengo la kuweka kimaandishi mawazo yangu juu ya riwaya hii, niliandika mwongozo. Nimeshaongelea kidogo kuhusu mwongozo huu katika blogu hii, lakini napenda kueleza zaidi habari zake.



Aliyenisukuma kuandika mwongozo huu kwa wakati niliofanya hivyo ni rafiki yangu A.S. Muwanga, aliyekuwa katika Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Yeye na mimi tulikubaliana kuwa niandike pia mwongozo kuhusu kitabu cha The African Child, kilichoandikwa na Camara Laye. Muwanga alifanya mpango na kitabu kilichapishwa mwaka 1988 na Nyanza Publications Agency kama inavyoonekana katika picha hapo juu. Lengo mahsusi lilikuwa ni hasa kuwasaidia wanafunzi wa sekondari waliokuwa wanasoma riwaya hizo.

Miaka hiyo, 1976 hadi 1991, nilikuwa mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mwaka huo 1991, niliondoka pale mwaka 1991, nikaja kufundisha Chuo cha St. Olaf, katika idara ya kiIngereza.

Mwaka 1997, bodi ya South Dakota Humanities Council iliyokuwa ikiratibu mradi wa usomaji katika jimbo la South Dakota iliniomba kuandika mwongozo kuhusu Things Fall Apart. Katika utaratibu wao, walikuwa wanachagua kitabu ili kisomwe na vikundi mbali mbali katika jimbo zima.

Ili kuchangia zoezi hili, walikuwa wana utaratibu wa kutafuta mtu wa kuandika mwongozo kuhusu kitabu husika, na mwongozo huu ulikuwa unatumiwa sambamba na kitabu husika. Kila kikundi kilikuwa kinajadili kitabu kweye mji wao, au eneo lao, na kisha walikuwa wanajumuika na wenzao wa sehemu zingine katika mjadala kwa njia ya barua pepe.

Mwaka huo 1997 kitabu kimojawapo walichokuwa wamekichagua ni Things Fall Apart. Ndio maana nikaombwa kuandika mwongozo. Nilitumia fursa hii kurekebisha ule mwongozo niliouchapisha Dar es Salaam. Kwa vile ilikuwa imepita miaka mingi nami nilikuwa nimetafakari zaidi riwaya ya Things Fall Apart niliweza kuweka marekebisho na kuuboresha mwongozo ule.

Kitabu kingine kilichokuwa kinajadiliwa ni Crimes of Conscience cha Nadine Gordimer, na aliyeombwa kuandika mwongozo ni profesa Karen A. Kildahl. Kazi yake na yangu zilichapishwa katika kijitabu kimoja, kama inavyoonekana katika picha hapo juu. Yeye na mimi tulialikwa kwenda kuendesha warsha kuhusu hivi vitabu viwili, katika mji wa Brookings, warsha ambayo ilihudhuriwa na watu kutoka sehemu mbali mbali za jimbo la South Dakota.

Mpango huu wa kuhamasisha usomaji katika jimbo zima ulinivutia sana, nikaona kuwa kama tungeweza kufanya jambo kama hili Tanzania, kuwafanya watu wajadili kitabu kimoja baada ya kingine, katika mkoa mzima au nchi nzima, tungefika mbali sana. Hatimaye, wahusika katika bodi hii ya South Dakota Humanities Council waliuweka mwongozo wangu wa Things Fall Apart mtandaoni, ukatumiwa na watu kutoka sehemu mbali mbali duniani.

Nilianza kuwazia umuhimu wa kuufikisha huu mwongozo Tanzania, ukiwa umeboreshwa zaidi. Niliurekebisha, nikauchapisha Chuo Kikuu Dar es Salaam, mwaka 2003, kwa gharama ya dola 520 za Marekani.

Wakati huo nilikuwa nimeanzisha kijikampuni, na kukisajili hapa Minnesota, kwa jina la Africonexion. Shughuli zake ni masuala ya elimu, kama vile kutoa ushauri, warsha, uandishi na uchapishaji. Nilivyochapisha mwongozo huu Dar e Salaam, nilitumia jina la Africonexion kama kampuni husika.

Hata hivi, lazima niseme ukweli. Pamoja na juhudi hizi zote, sikuona mwamko wa kuridhisha miongoni mwa wa-Tanzania, wa kutumia fursa niliyowaletea. Lakini, naridhika kwamba sina lawama. Kama vijana wa shule wa Rukwa, Pemba, Morogoro na Kondoa hawana kitabu kama hiki, kosa ni la wananchi na serikali. Mimi kama mwalimu nawajibika kusema kuwa serikali inapotosha ukweli inaposema haina hela, wakati kila mtu anaona jinsi inavyofuja hela, kwa magari ya fahari, na kadhalika. Tabia hiyo na wananchi wanayo pia, kama nilivyoeleza hapa.

Harakati za mwongozo huu ziliendelea. Mwaka 2005 nilikuwa nimechapisha kitabu mtandaoni, kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Baada ya kuvutiwa na uchapishaji wa aina hii, niliamua kuchapisha mwongozo wangu wa Things Fall Apart kwa njia hiyo hiyo. Niliufanyia marekebisho na kuuboresha, na hatimaye niliuchapisha, kama inavyoonekena katika picha kushoto.

Mwongozo wangu huu unawafaidia wengi. Nilifurahi, kwa mfano, nilipoona umechaguliwa na Chuo Kikuu cha Cornell kwa ajili ya wanafunzi wa mwaka wa kwanza waliokuwa wanatakiwa kusoma Things Fall Apart.

Huo ni utaratibu wao, kwamba wanafunzi wote wa mwaka wa kwanza wasome kitabu fulani, na vitabu hubadilika mwaka hadi mwaka. Kwa jinsi Chuo Kikuu cha Cornell kilivyo maarufu duniani, na kwa kuwa kuna vijitabu vingi na machapisho mengine kuhusu riwaya hii, kuchaguliwa mwongozo wangu ni heshima ya pekee. Soma hapa. Niliumiza kichwa kwa miaka mingi kuufikisha mwongozo huu kwenye kiwango hiki na nilijua ubora wake, kwani hilo ni somo langu, lakini inapendeza pia kuwasikia wataalam wengine wanaonaje.

Ninaendelea na shughuli ya kuandika miongozo kwa vitabu vingine. Kwa mfano, ninataka kurekebisha mwongozo wangu wa The African Child, ili niuchapishe kama kijitabu. Vile vile, kwa miaka kadhaa nimejishughulisha na uandishi wa mwongozo wa utungo maarufu wa Song of Lawino, uliandikwa na Okot p'Bitek. Nikijaliwa uzima, nitaandika sana siku za usoni. Kwani kazi na wajibu wa mwalimu ni nini?

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...