Showing posts with label misahafu. Show all posts
Showing posts with label misahafu. Show all posts

Thursday, May 5, 2016

Nimepata Qur'an Mpya

Nimekuwa na kawaida ya kuandika katika blogu hii taarifa za vitabu ninavyonunua, au vitabu ninavyosoma, ingawa siandiki juu ya vyote. Kwa siku nyingi sijafanya hivyo, lakini leo nimeamua kuandika kuhusu Qur'an mpya niliyoipata hivi karibuni, ambayo ni tafsiri ya ki-Ingereza ya Maulana Wahiduddin Khan na Farida Khanam ambaye ni binti yake.

Ninayo nakala nyingine ya Qur'an tangu mwaka 1982, ambayo ni tafsiri ya Abdullah Yusuf Ali. Hii ni kubwa kwa kuwa ina maelezo mengi. Hii mpya niliipata tarehe 28 Aprili, mwaka huu, kutoka kwa Dr. Nadia Mohamed, mzaliwa wa Misri.


Anaonekana amesimama kulia pichani. Nimefahamiana naye zaidi ya mwaka, tangu tuliposafiri kwenda kwenye semina chuoni Leech Lake, ambapo tulipiga hii picha, pamoja na profesa mwingine wa chuo kile.

Dr. Nadia Mohamed ni profesa mwenye shahada ya uzamili katika sheria za ki-Islam na shahada ya uzamifu katika elimu. Nilikuwa nimemwalika kuja kutoa mhadhara katika darasa langu la Muslim Women Writers, na baada ya kipindi ndipo alinipa Qur'an hiyo.

Tafsiri ni mtihani mkubwa, nami nimesema hivyo tena na tena katika blogu hii. Kwa kuwa hii Qur'an niliyopata karibuni ni tafsiri tofauti na ile ya Abdullah Yusuf Ali, ninategemea kufananisha hizi tafsiri mbili kutanisaidia kupata mwanga zaidi kuhusu yasemwayo katika Qur'an.

Ninasoma Qur'an sawa na ninavyosoma misahafu ya dini zingine kwa lengo la kujielimisha. Ninaamini kuwa ni muhimu kwa wanadamu kufahamiana ili tuweze kujenga maelewano miongoni mwetu. Kuzifahamu dini za wengine, tamaduni zao, na lugha zao ni njia ya kulifikia lengo hilo.

Ninapenda kusisitiza hilo, kwani nimeshakumbana na watu wanaodhani au kutegemea kwamba kwa kuwa ninasoma Qur'an, hatimaye nitasilimu. Sioni mantiki ya dhana hiyo. Je, ninaposoma msahafu wa dini ya Hindu, inamaanisha nitaacha u-Kristu niwe m-Hindu? Ninaposoma maandishi ya watu wanaozikana dini, kama vile akina Karl Marx, inamaanisha kuwa hatimaye nitaikana dini? Nimesoma fikra za Karl Marx na wapinzani wengine wa dini kwa zaidi ya miaka 40, na bado mimi ni m-Katoliki.

Monday, February 1, 2016

Dini sio Misahafu Pekee

Leo ninapenda kuendelea kuongelea dini, kujenga hoja kwamba dini si misahafu pekee. Ninaongelea mada hii kwa kuwa ninaamini umuhimu wa mijadala ya dini, na kwa kuzingatia tabia ambayo imejengeka Tanzania ya baadhi ya wa-Islam na wa-Kristu kulumbana kuhusu dini zao. Wanaonekana viwanjani wakihubiri dhidi ya dini ya wapinzani wao. Wananukuu misahafu katika kujenga hoja kwamba dini yao ni bora zaidi au ndio dini ya kweli.

Binafsi, naona kuwa malumbano haya ni upuuzi mtupu. Dini haiko katika misahafu tu. Ni mfungamano wa nadharia na vitendo. Dini ni mfungamano wa mafundisho ya misahafu na maisha ya kila muumini. Bila mfungamano huo, dhana ya dini inapwaya.

Kuna maana gani kwa muumini wa dini kuringia msahafu wa dini yake iwapo maisha yake hayaendani na mafundisho yaliyomo katika msahafu? Badala ya kulumbana kuhusu misahafu, tuangalie maisha ya waumini. Je, tabia za mu-Islam ni bora kuliko za m-Kristu? M-Kristu ni bora kuliko mu-Islam? Jamii ya wa-Islam ni bora kuliko jamii ya wa-Kristu? Wa-Kristu ni bora kuliko wa-Islam? Tofauti za imani zina uzito gani? Je, wa-Kristu, ambao wanaamini kuwa Yesu ni mwana wa Mungu, ni watu waovu kuliko wa-Islam, ambao hawaamini kuwa Yesu ni mwana wa Mungu bali ni nabii?

Kama waumini wa dini fulani ni wema, waungwana, wakarimu, wastahimilivu, wenye huruma, wa amani kuliko wengine, ninaamini kuwa waumini hao watawavutia hata watu wasio na dini. Dini si misahafu tu; ni mfungamano wa nadharia na vitendo.

Monday, January 4, 2016

Nawazia Dini na Uandishi wa Wanawake wa ki-Islam

Muhula ujao, kuanzia mwezi Februari hadi Mei, nitafundisha kozi mpya hapa chuoni St. Olaf ambayo nimeiita "Muslim Women Writers." Ni kozi ya fasihi kwa ki-Ingereza, ambamo tutasoma maandishi ya wanawake wa-Islam kutoka Bangladesh, India, Iran, Misri, Sudan, Senegal, na Marekani. Taarifa fupi ya kozi hiyo nimeandika hapa.

Wakati huu ninapongojea kufundisha kozi hii katika mazingira ya leo ambamo maelewano miongoni mwa waumini wa dini na madhehebu mbali mbali yanatatanisha, ninajikuta nikiwazia mara kwa mara masuala ya dini. Katika siku zijazo, labda kwa miezi kadhaa, ninategemea kuandika tena na tena katika blogu hii kuhusu dini na kozi yangu.

Nimeshaandika mara kadhaa kuhusu dini. Nimeandika kuhusu umuhimu wa mijadala ya dini, umuhimu wa kuziheshimu dini zote, na nilivyozuru nyumba za ibada za dini nyingine. Sioni mantiki kwa dini yoyote kuwafundisha waumini wake kwamba Muumba anawapenda wao zaidi kuliko watu wa dini nyingine. Msimamo wangu ni kwamba Mungu (Allah) hana ubaguzi.

Ninafurahi na kujivunia kwamba kanisa langu Katoliki linasimama katika msingi huo, kama ilivyodhihirishwa katika ziara na ujumbe wa Papa John Paul wa Pili nchini Nigeria, ziara ya Papa Francis katika msikiti Uturuki, na katika sala ya Papa Francis ya kuuombea ulimwengu. Na zaidi ni kuwa Kanisa Katoliki lina baraza la kujenga maelewano miongoni mwa dini mbali mbali liitwalo Pontifical Council for Inter-religious Dialogue.

Katika kujiandaa kwa kozi yangu, nimekuwa nikiwazia kuwa ingekuwa vizuri kama ningesoma Quran yote. Ninayo Quran takriban tangu mwaka 1982. Nimekuwa nikisoma visehemu hapa na pale, lakini si yote kikamilifu. Ingawa ninafahamu misingi ya u-Islam kiasi cha kuridhisha, wazo la kuisoma Quran linanivutia.

Kuna mambo mengine ambayo nimekuwa nikifanya, kama vile utafiti ili kufahamu misimamo na mitazamo ya wanawake wa-Islam kuhusu u-Islam na nafasi yao katika dini hiyo. Nimeanza pia kuwatafuta wanawake wasomi wa ki-Islam na kujitambulisha kwao, ili waweze kuniongezea elimu kwa manufaa yangu na ya wanafunzi wangu. Ninafurahi kwa mafanikio ya kutia moyo ambayo nimeanza kuyaona.

Nimeandika ujumbe huu kwa kuzingatia kuwa wengi wanaosoma blogu yangu ni waumini wa dini. Wana wajibu wa kuchangia mawazo, hasa wakiona nimepotosha jambo lolote. Kwa muumini yeyote, hili si  suala la hiari, bali ni wajibu.

Saturday, April 18, 2015

Misahafu na Balaa Linaloitwa Dini

Si kila kinachoitwa dini ni dini. Katika historia, kumekuwepo na uovu mwingi ambao umefanyika kwa jina la dini. Hadi leo, uovu wa aina hiyo unaendelea kufanyika. Siku nyingine, panapo majaliwa, nitaleta na kuongelea mifano, kwa uwazi na haki.

Misahafu imetumika na inaendelea kutumika kuhalalisha uovu. Kwa kiasi fulani hii ni kwa sababu mtu anaweza kuzipata nukuu kutoka katika msahafu ambazo zinapingana au zina utata. Lakini vile vile ni suala la tafsiri. Wataalam wa lugha wanatueleza kuwa matumizi ya lugha yanatoa mwanya wa tafsiri mbali mbali.  

Kwa msingi huo, watu waovu wanaweza kutafsiri nukuu za msahafu kwa namna ya kuhalalisha uovu. Katika tamthilia ya Shakespeare, The Merchant of Venice, Antonio anasema, "The devil can cite Scripture for his own purpose." Shetani anaweza kunukuu msahafu kwa faida yake mwenyewe. Historia imethibitisha ukweli huo tena na tena.
 

Tatizo jingine ni imani miongoni mwa waumini wa dini kwamba kila kilichomo katika misahafu sherti kikubaliwe na kufuatwa kilivyo, bila mabadiliko. Imani hii ni chanzo cha matatizo makubwa.

Mtu ukiusoma msahafu wowote bila upendeleo wala ushabiki, utaona kuwa msahafu ulitokea katika mazingira maalum ya kihistoria, kijamii, na kitamaduni. Kuna mambo katika misahafu ambayo yalikusudiwa kwa jamii za zamani, na hayatuhusu sisi watu wa leo.

Kwa msingi huu, ni muhimu tujijengee utamaduni wa kuichambua misahafu ili tuone ni yepi yanatufaa na yepi yaliwafaa watu wa zamani lakini hayatufai sisi watu wa leo.


Mungu ametujalia akili. Tuzitumie. Mungu ametuweka katika dunia tofauti na ile ya watu wa zamani. Tuna ufahamu  na akili tofauti na watu wa zamani, katika masuala kama haki za binadamu.

Utandawazi wa leo na tekinolojia imetupa ufahamu tofauti wa ulimwengu na watu wake, ufahamu wa mahusiano tunayoyahitaji katika dunia ya leo ambayo siku hadi siku inageuka kuwa kijiji.

Je, katika mazingira hayo, ni sahihi kuishikilia misahafu neno kwa neno, kikasuku, badala ya kupambanua yale yanayotuhusu na yale yaliyowahusu watu wa zamani? Je, ukasuku huu, unaosababisha au kuhalalisha balaa juu ya balaa, na maovu ya kila aina, ndio dini?

Kwa kumalizia ujumbe wangu, napenda kusisitiza mtazamo wangu kuwa mijadala ya dini ni muhimu, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii.

 

Tuesday, March 26, 2013

Ufundishaji Wangu wa Maandishi ya Achebe

Nimefundisha maandishi ya Chinua Achebe kuanzia miaka ya sabini na kitu. Kabla sijahitimu na shahada ya kwanza Chuo Kikuu Dar es Salaam, mwaka 1976, huenda nilifundisha Things Fall Apart katika shule za sekondari nilikopelekwa kufanya mazoezi ya kufundisha, yaani sekondari ya wasichana Iringa, 1974, na sekondari ya Kinondoni, 1975. Sina hakika.

Lakini baada ya kuhitimu shahada ya kwanza, mwaka 1976, nilipata fursa za kufundisha Things Fall Apart, nikianzia na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambapo nilikuwa mhadhiri. Mwaka 1980, chini ya mkataba wa ushirikiano baina ya Tanzania na Burundi, nilifundisha kwa wiki kadhaa katika Chuo Kikuu cha Burundi. Kitabu kimojawapo kilikuwa Things Fall Apart

Uzoefu huu ulinifanya niandike mwongozo wa Things Fall Apart, ili kuelezea mambo ambayo waandishi wengine hawajayaweka wazi.  Ilikuwa ni fursa kwangu kuwaelezea wanafunzi na walimwengu namna ninavyoichukulia riwaya hii ya Things Fall Apart. Kwa maelezo zaidi ya historia hii, soma hapa. Sihitaji kuficha ukweli kwamba mwongozo huu ni maarufu na wengi wanautumia.

Baada ya kuja kufundisha chuo cha St. Olaf, mwaka 1991, nimefundisha Things Fall Apart na maandishi mengine ya Achebe. Kuna muhula fulani nilitunga kozi nzima juu ya maandishi ya Achebe tu. Tulisoma riwaya zake kadhaa, na pia insha baadhi ya insha zake, zikiwemo "The Novelist at Teacher," "Colonialist Criticism," na "An Image of Africa." Tulisikiliza pia baadhi ya mahojiano yake. Ingekuwa muda unaruhusu, tungesoma pia mashairi yake.

Ni wazi kwamba Things Fall Apart ni moja ya riwaya ambazo nimezifundisha sana. Kila ninapoifundisha, nazua masuala mapya na tafakari mpya. Hiyo ni tabia ya fasihi. Hata misahafu ina tabia hiyo, ingawa wako watu wanaodai kuwa misahafu haibadiliki. Binafsi, kutokana na uzoefu wangu wa kusoma na kutafakari fasihi na maandishi mengine, siamini kwamba kuna andiko lolote, hata msahafu, ambalo haliguswi na mabadiliko, kuanzia na mabadiliko ya lugha na maana zake, ambayo hayakwepeki. Nimegusia suala hilo katika mwongozo wangu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...