Showing posts with label imani. Show all posts
Showing posts with label imani. Show all posts

Tuesday, December 17, 2019

Kofia ya CCM Nchini China

Naleta picha ya ujumbe wa CCM kwenye kikao na wenyeji wao mjini Shanghai, China, mwaka 2018. Hapo mezani upande wa kushoto kuna kofia ya CCM. Yawezekana walikwenda ziarani na magwanda yao na vikofia. Je, kuna sababu gani mimi kuandika ujumbe kuhusu kofia? Sina jambo la maana zaidi la kuongelea? Kwa nini nisiongelee madhumuni ya ziara na mafanikio yake?

Ninaandika ujumbe huu kama mtafiti, mwandishi, na mtoa ushauri juu ya masuala ya utamaduni na utandawazi. Nimekuwa nikifanya shughuli hizo hapa Marekani na Tanzania pia, ambako nimeendesha warsha mara kadhaa kuanzia mwaka 2008 katika miji ya Arusha, Tanga, na Dar es Salaam.

Ninajaribu kuwaelewesha watu kuwa tofauti za tamaduni zina athari kubwa, hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Tunapokutana na watu wa tamaduni tofauti na wetu, tuwe makini. Tunaweza tukaelewana vibaya, au tunaweza tusielewane. Ni muhimu tujielimishe kuhusu tofauti hizo kabla hayajatupata hayo.

Kofia ya CCM ni sehemu ya vazi rasmi la wana CCM. Ni utambulisho wao. Hata mimi ambaye sina chama ninawatambua kwa mavazi yao. Vyama vingine navyo vina mavazi yao. Kwa hapa nchini Tanzania, hakuna utata juu ya hayo mavazi. Lakini je, hali ni hiyo hiyo nje ya Tanzania kwenye tamaduni tofauti?

Nchini China, kofia ya kijani ni mkosi. Mwanaume kuvaa kofia ya kijani maana yake anatangaza kwamba mke wake ni mzinzi.

Kuhusu asili ya tafsiri hii ya waChina kuhusu kofia ya kijani, maelezo yanatofautiana. Baadhi ya maelezo ni kwamba zamani za kale, ndugu wa malaya walilazimishwa kuvaa kofia ya kijani wabebe aibu. Maelezo mengine ni kwamba zamani za kale, wahudumu katika madanguro walikuwa wanavaa kofia za kijani. Lakini kama nilivyogusia, maelezo yanahitilafiana. Ila jambo ambalo halina utata ni kwamba katika utamaduni wa China, kofia ya kijani ni mkosi kwani inatangaza habari ya uzinifu wa mke.

Sasa fikiria hiyo ziara ya ujumbe wa CCM China. Wafikirie wako sehemu mbali mbali kama wageni rasmi, wamevalia kofia za kijani. Bila shaka, wenyeji wao walifanya ukarimu na heshima kama ilivyo desturi. Lakini bila shaka, makada hao wa CCM watakuwa wameacha gumzo na taswira ambayo hawakutegemea.

Katika warsha ambazo nimeandaa Tanzania tangu mwaka 2008, waTanzania wachache sana wamekuwa wakihudhuria. Mbali ya warsha, nimekuwa nikielezea katika blogu zangu masuala ya athari za tofauti za tamaduni katika dunia ya utandawazi wa leo. Nimeandika hata kitabu, kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho kinapatikana Tanzania pia, kutoka katika maduka ya Kimahama (Arusha), Soma Book Cafe (Dar es salaam), na A Novel Idea (Arusha na Dar es Salaam).

Pamoja na kujaribu njia zote hizo, nimeona kuwa labda, kwa kuandika ujumbe huu kuhusu kofia ya CCM nchini China, waTanzania watanielewa vizuri na watachukua hatua stahiki katika masuala yote husikka, iwe ni mahusiano binafsi, biashara za kimataifa, utalii, diplomasia na kadhalika.

Sunday, June 4, 2017

Vitabu Vinavyopinga Dini

Ingawa mimi ni muumini wa dini, m-Katoliki, ninapenda kuzifahamu dini zingine. Sijiwekei mipaka. Sina tatizo na watu wa dini tofauti na yangu, wala watu wasio na dini. Ninajifunza kutoka kwao. Mtu unajifunza mengi kutoka kwa watu wenye mawazo tofauti na yako.

Ninasoma vitabu vya dini zingine, kama nilivyowahi kueleza katika blogu hii. Vile vile ninasoma vitabu vinavyohoji au kupinga dini. Fikra za wapinga dini zinafikirisha. Mfano ni kauli ya Karl Marx: "Religion is the sigh of the oppressed creature, the heart of a heartless world, and the soul of soulless conditions. It is the opium of the people."

Ninaipenda kauli hiyo ya Marx kwa kuwa inafikirisha na kusisimua akili. Kuna ubaya gani kwa mtu kuiponda dini namna hii? Kuna sababu gani ya mimi muumini kumchukia mtu wa aina hiyo? Kama vile mimi ninavyotetea haki na uhuru wa kuwa na mawazo yangu, naye ana haki na uhuru wa kuwa na mawazo tofauti na yangu. Ana uhuru wa kujieleza na kusambaza mawazo yake.

Ninavyo vitabu vinavyohoji u-Kristu. Mifano ni Jesus: Prophet of Islam, kilichotungwa na Muhammad Ata Ur-Rahim na Ahmad Thomson; The Gnostic Gospels, kilichotungwa na Elaine Pagels; na The Essential Gnostic Gospels, Including the Gospel of Thomas & The Gospel of Mary, kilichotungwa na Alan Jacobs. Nina vitabu vinavyouhoji u-Islam, vya waandishi kama Ayaan Hirsi Ali na Nawaal el Saadawi. Kuna vingine ambavyo bado sina, ila nitavinunua, kama vile vya Wafa Sultan na Ibn Warraq.

Kama mtu umejengeka katika dini yako na unatambua umuhimu na maana yake, kuna sababu gani ya kuvichukia vitabu vinavyoihoji dini? Jazba au masononeko ya nini, kama si ishara ya udhaifu na ubabaishaji wako mwenyewe? Binafsi, niko imara, na wahenga walisema, kelele za chura hazimzuii ng'ombe kunywa maji.

Fikra zinazohoji dini ninaziona kuwa zenye manufaa. Mimi kama muumini ninazichukulia hizo kama fursa ya kuimarisha imani, sawa na misukosuko inavyomkomaza mtu. Wakristu tunafundishwa uvumilivu, na hii ni njia ya kujipima tuna imani kiasi gani. Kama kawaida, nakaribisha maoni.

Monday, January 4, 2016

Nawazia Dini na Uandishi wa Wanawake wa ki-Islam

Muhula ujao, kuanzia mwezi Februari hadi Mei, nitafundisha kozi mpya hapa chuoni St. Olaf ambayo nimeiita "Muslim Women Writers." Ni kozi ya fasihi kwa ki-Ingereza, ambamo tutasoma maandishi ya wanawake wa-Islam kutoka Bangladesh, India, Iran, Misri, Sudan, Senegal, na Marekani. Taarifa fupi ya kozi hiyo nimeandika hapa.

Wakati huu ninapongojea kufundisha kozi hii katika mazingira ya leo ambamo maelewano miongoni mwa waumini wa dini na madhehebu mbali mbali yanatatanisha, ninajikuta nikiwazia mara kwa mara masuala ya dini. Katika siku zijazo, labda kwa miezi kadhaa, ninategemea kuandika tena na tena katika blogu hii kuhusu dini na kozi yangu.

Nimeshaandika mara kadhaa kuhusu dini. Nimeandika kuhusu umuhimu wa mijadala ya dini, umuhimu wa kuziheshimu dini zote, na nilivyozuru nyumba za ibada za dini nyingine. Sioni mantiki kwa dini yoyote kuwafundisha waumini wake kwamba Muumba anawapenda wao zaidi kuliko watu wa dini nyingine. Msimamo wangu ni kwamba Mungu (Allah) hana ubaguzi.

Ninafurahi na kujivunia kwamba kanisa langu Katoliki linasimama katika msingi huo, kama ilivyodhihirishwa katika ziara na ujumbe wa Papa John Paul wa Pili nchini Nigeria, ziara ya Papa Francis katika msikiti Uturuki, na katika sala ya Papa Francis ya kuuombea ulimwengu. Na zaidi ni kuwa Kanisa Katoliki lina baraza la kujenga maelewano miongoni mwa dini mbali mbali liitwalo Pontifical Council for Inter-religious Dialogue.

Katika kujiandaa kwa kozi yangu, nimekuwa nikiwazia kuwa ingekuwa vizuri kama ningesoma Quran yote. Ninayo Quran takriban tangu mwaka 1982. Nimekuwa nikisoma visehemu hapa na pale, lakini si yote kikamilifu. Ingawa ninafahamu misingi ya u-Islam kiasi cha kuridhisha, wazo la kuisoma Quran linanivutia.

Kuna mambo mengine ambayo nimekuwa nikifanya, kama vile utafiti ili kufahamu misimamo na mitazamo ya wanawake wa-Islam kuhusu u-Islam na nafasi yao katika dini hiyo. Nimeanza pia kuwatafuta wanawake wasomi wa ki-Islam na kujitambulisha kwao, ili waweze kuniongezea elimu kwa manufaa yangu na ya wanafunzi wangu. Ninafurahi kwa mafanikio ya kutia moyo ambayo nimeanza kuyaona.

Nimeandika ujumbe huu kwa kuzingatia kuwa wengi wanaosoma blogu yangu ni waumini wa dini. Wana wajibu wa kuchangia mawazo, hasa wakiona nimepotosha jambo lolote. Kwa muumini yeyote, hili si  suala la hiari, bali ni wajibu.

Sunday, June 7, 2015

Nimetoka Kanisani Kusali

Ni Jumapili, saa sita na kidogo mchana. Nimetoka kanisani kusali. Mimi ni m-Kristu wa kawaida, m-Katoliki. Namwabudu Mungu na ninaamini kuwa yeye ndiye anayeongoza maisha yangu. Katika raha na matatizo, ninamtegemea yeye. Ninamshukuru kwa kunipa uhai siku hadi siku.

Namshukuru Mungu kwa kunipa akili na utashi nitafakari mambo na kujiamulia. Ninamshukuru kwa jinsi anavyotuneemesha, kwa kuwaumba wanadamu wa kila aina, wenye dini mbali mbali, tamaduni na lugha mbali mbali. Dunia inapendeza kwa tofauti hizo, sawa na maua yanavyopendeza, kwa uwingi wa tofauti za rangi.

Namshukuru Mungu kwa yote aliyoyaweka duniani: nchi kavu, bahari, milima, mabonde, mito, miti, majani na maua. Ametuwekea wanyama wa kila aina, ndege na wadudu, jua, mwezi na nyota, mvua na upepo, vitu vinavyoonekana na visivyoonekana.

Vyote ni mazao ya uumbaji wa Mungu. Ninaomba niwe na moyo wa kuwapenda wanadamu wote na vyote alivyoumba Mungu. Ninaomba niwe mtu mwema, mwenye kutambua na kuzingatia kila siku kuwa Mungu amenipa uhai, akili, na vipaji, si kwa ajili yangu, bali kwa manufaa ya walimwengu bila kujali tofauti zao, za taifa, kabila, dini, jinsia, umri, utamaduni, lugha, na kadhalika.

Kuwa kanisani, kujumuika na waumini wenzangu, ni fursa ya kujikumbusha imani ya dini yangu, kuwaombea walimwengu wote, wabarikiwe. Sasa, baada ya kutoka kanisani, ninajisikia mwenye faraja, moyo mkunjufu, na ari ya kuendelea na majukumu yangu.

Tuesday, December 11, 2012

Mungu ni Mmoja: Anaitwa Allah, Brahman, Chiuta, Ruwa na Kadhalika

Uzuri wa kuwa na blogu yako ni kuwa hutawaliwi na mtu katika kuamua nini cha kuandika. Uamuzi wote ni wako. Nimesema kabla kuwa katika blogu yangu hii, masuala ambayo yanasemwa kuwa ni nyeti, kama dini, ni ruksa kujadiliwa. Tena sio tu ruksa, bali muhimu kujadiliwa.

Leo napenda kutoa hoja kuwa Mungu ni mmoja: anaitwa Allah, Brahman, Chiuta, Ruwa, na kadhalika, kutokana na kuwepo kwa lugha nyingi hapa duniani. Huyu ndiye aliye juu ya yote, mwenye uwezo wote, kama inavyosemwa katika ki-Arabu, "Allahu akbar." Ni dhana ya msingi katika dini zetu.

Kama wewe ni mu-Islam, halafu unasema kuwa Allah ni tofauti na Mungu wanayemwabudu wa-Kristu, au Mungu wanayemwabudu wa-Hindu, jichunguze upya, kwani utakuwa unasema kuna miungu zaidi ya mmoja. Utakuwa unaongelea kuwepo kwa mungu mwingine zaidi ya Allah. U-Islam hautambui kuwepo kwa Mungu mwingine zaidi ya Allah.

Kama wewe ni m-Kristu, halafu unasema kuwa Mungu unayemwabudu ni tofauti na Allah, basi inabidi ujichunguze, kwa misingi hiyo hiyo. U-Kristu hautambui kuwepo kwa mungu zaidi ya huyu ambaye sisi wa-Kristu tunayemwabudu, ambaye kwa ki-Arabu huitwa Allah. Usishangazwe na jina Allah. Wa-Kristu ambao ni wa-Arabu nao hutumia jina Allah, wakimaanisha Mungu, kama nilivyowahi kusema katika blogu hii.

Huyu Mungu mmoja anatajwa kwa majina mbali mbali kufuatana na lugha. Wa-Tumbuka wa Malawi na Zambia humwita Chiuta. Wa-Hindu humwita Brahman. Wa-Kamba na wa-Kikuyu humwita Ngai. Wachagga humwita Ruwa.

Hoja yangu ni kuwa majina yote hayo yanamtaja Mungu huyu huyu. Muumini anayeamini kuwa kuna Mungu mmoja tu, sherti akubali na azingatie hilo. Ni ushahidi kuwa Mungu alijitambulisha kwa wanadamu duniani kote tangu mwanzo kabisa.

Nimeona nitoe mawazo yangu, kwa uhuru kabisa, kwani ni haki yangu. Kama kuna anayetaka kuyajadili au kuyapinga, namkaribisha kwa mikono miwili kufanya hivyo.

Tuesday, October 16, 2012

Wa-Kristu Tunamwabudu Allah!

Najua kuwa kichwa cha habari hii kitawashtua wengi. Huenda watu watasema nimechanganyikiwa au nimekufuru.  Huenda wako watakaouliza, "Iweje wa-Kristu wawe wanamwabudu Allah?"

Kwa siku kadhaa, nimekuwa nikijuliza suali: Je, wa-Arabu ambao ni wa-Kristu wanatumia jina gani kumtaja Mungu? Ninafahamu kuwa kuna mamilioni ya wa-Arabu ambao ni wa-Kristu, huko Mashariki ya Kati na sehemu zingine za dunia. Sasa je, Mungu wanamwitaje kwa ki-Arabu?

Nimefanya uchunguzi kidogo nikagundua kuwa jina wanalotumia, ni hilo hilo wanalotumia wa-Islam, yaani Allah. Hili ndilo neno lililopo katika ki-Arabu. Katika Biblia ya ki-Arabu, ambayo huitwa "al-Kitab al- Muqadis" yaani Kitabu Kitakatifu, Mungu anaitwa Allah muda wote.

Nilivyogundua hivyo nimetambua jinsi wengi wetu tulivyopotea, kwani tunaamini kuwa Allah ni tofauti na Mungu. Tunalumbana hadi tunatokwa jasho, na povu mdomoni, kwa umbumbumbu wa kutojua lugha. Taarifa iliyonifungua macho ni hii hapa.


Thursday, February 23, 2012

Dini Inayoenea kwa Kasi Kuliko Zote Tanzania

Mara kwa mara ninawasikia watu wakiongelea suala la dini inayoenea kwa kasi kuliko zote Tanzania, Afrika au duniani kwa ujumla. Kila mtu ana mtazamo wake. Wengine wanatoa pia takwimu, ambazo sijui kama ni za kweli au ndoto. Ni mchezo wa kuringiana nani zaidi kwa kutumia takwimu, wakati dini ni suala la mtu binafsi. Wala hutaingia ahera kwa msingi kuwa dini yako hapa duniani ilikuwa na wafuasi wengi kuliko dini nyingine.

Kwa mtazamo wangu, dini inayoenea kwa kasi kuliko zote Tanzania ni ufisadi na ushirikina. Ufisadi na ushirikina huo unaendelea kushamiri kiasi kwamba unajitokeza hata kwenye nyumba za ibada za dini mbali mbali. Hebu tutafakari hilo.

Wednesday, November 30, 2011

Makafiri

Ingawa watu wengi wanaamini kuwa masuala ya dini ni hatari kujadiliwa, blogu yangu haina kipingamizi kwenye kujadili masuala hayo, kama ilivyo kwa masuala mengine. Kama kuna tatizo, tatizo haliko kwenye mada, bali tatizo ni wahusika, kama nilivyoandika hapa.

Leo napenda kuongelea suala ambalo limenikera kwa muda mrefu. Ni suala la watu kuwaita wengine makafiri. Nimeshasoma taarifa kutoka sehemu mbali mbali za Tanzania ambazo zimenifanya niandike ujumbe huu.

Leo katika mtandao wa Facebook, nimeona taarifa kutoka Mbeya ambamo mtu analalamika kuwa kuna makafiri sana kule. Miezi kadhaa iliyopita, nilisoma taarifa kutoka Zanzibar, kwamba watu wa kijiji fulani walikuwa hawataki makafiri kwenye eneo lao. Ukipita mtandaoni, utaona kuwa jadi hii ya kuwaita wengine makafiri inajitokeza mara kwa mara miongoni mwa watu wa Visiwani.

Sijui hao wanaowaita wengine makafiri walipata wapi uwezo wa kufahamu undani wa watu wengine kiasi hicho. Nilidhani kuwa sote tunaosema tunamwamini Mungu tunafahamu kuwa mwenye uwezo wa kumhukumu binadamu, uwezo wa kujua yupi ni kafiri na yupi si kafiri, ni Mungu tu.

Hatujui ya Mungu, na bora tuwe wanyenyekevu. Hao wanaowaita wenzao makafiri huenda Mungu anawajua kuwa ndio makafiri wenyewe. Binafsi siwezi kumtambua kafiri, kwa sababu sina njia ya kuona yaliyomo moyoni au akilini mwa yeyote. Sithubutu kumwita yeyote kafiri, kwani nitaona kuwa kufanya hivyo ni kufuru, yaani kujifanya mimi ni Mungu.

Sunday, May 8, 2011

Kikombe cha Mwenyekiti Maggid

Kama sote tunavyojua, wa-Tanzania tuko kwenye awamu ya vikombe. Waganga wamejitokeza nchini mwetu, wakiwa na vikombe vya kuponyesha magonjwa mbali mbali. Wateja wengi wanatoa ushuhuda kuhusu uponyaji wao.

Nami napenda kutoa ushuhuda kuhusu kikombe cha Mwenyekiti Maggid Mjengwa.

Nianze kwa kusema kuwa Mwenyekiti Maggid ni mwalimu, mwandishi na mwanablogu. Hajawa mganga wa kienyeji. Isipokuwa, kikombe ameninywesha. Tega sikio nikuhadithie.

Mwaka 2009 mwanzoni, Mwenyekiti Maggid alianzisha gazeti la Kwanza Jamii, akaniomba niwe mchangiaji. Nilikubali. Sikutambua kuwa nilijipalia mkaa, maana nilijikuta nahangaika kuandika hizo makala na kuzituma kwa muda uliotakiwa.

Ilikuwa ni kazi ya kuumiza kichwa. Kwanza kabisa, wakati mwingine nilikuwa sijui niandike kuhusu nini. Huku siku na saa za kuwasilisha makala zinaendelea kusogea, nami bila kujua mada ya kuandikia, nilibaki nimekodoa macho na jasho linanitoka. Mara kwa mara Mwenyekiti Maggid alikuwa ananiletea ujumbe usiku kwenye saa sita za hapa Marekani ya kati, iwapo nilichelewa.

Tatizo jingine nililopambana nalo ni kuandika kwa ki-Swahili. Nilizoea kuandika kwa ki-Ingereza, lakini kuandika ki-Swahili sanifu ulikuwa ni mtihani wa kuumiza kichwa.

Sisi wa-Katoliki, katika falsafa ya dini yetu, tunatumia dhana ya kikombe kuelezea magumu ya maisha au mateso ambayo Mungu anatuletea tuyakabili. Ni kama tunavyotumia dhana ya msalaba. Mungu ana malengo yake anapotutwisha msalaba maishani.

Napenda niendelee kufafanua falsafa za kidini zinazohusiana na mada yangu. Babu wa Loliondo ametueleza tena na tena kuwa kikombe si kikombe tu bali ni suala la imani, na uwezo wa kutibu ni wa Mungu, si binadamu.

Mungu anaweza kumtumia binadamu yoyote kuleta ujumbe au uponyaji duniani. Kwa imani yangu, ndivyo ilivyokuwa kuhusiana na hiki kikombe cha Mwenyekiti Maggid. Naamini kilipangwa na Mungu. Matokeo ya magumu niliyopitia, ambayo nayaita kikombe cha Mwenyekiti Maggid, yamekuwa mazuri. Makala nilizoandika zilisomwa na bado zinasomwa na watu wengi.

Makala mojawapo, baada ya mimi kuitafsiri kwa ki-Ingereza, ikachapishwa huku Marekani, ilimvutia Chad Brobst, mhariri wa jarida la Monday Developments. Aliiomba, nami nikairekebisha kidogo, akaichapisha. Kila toleo la Monday Developments huteua makala moja kama makala ya mfano. Kwa mwezi Aprili, iliteuliwa makala yangu. Watu wengi sana duniani wataiona.

Vile vile, makala nilizoandika katika Kwanza Jamii nilizikusanya nikazichapisha kama kitabu, CHANGAMOTO, ambacho watu waliokisoma wamekipenda. Ninajivunia kitabu hiki kwa vile ni kitabu changu cha kwanza kwa ki-Swahili.

Nimeshawahi kuandika kuwa wito wa Mwenyekiti Maggid kunitaka niandike makala za ki-Swahili ulisaidia kuniondolea kasumba tuliyo nayo wasomi wengi, ya kutoweza au kutotaka kutumia ki-Swahli ipasavyo. Nilifanya bidii kujiongezea ufahamu wa ki-Swahili. Nilisoma vitabu vya mabingwa kama Shaaban Robert na kujijengea nidhamu ya matumizi ya lugha.

Sisiti kukiri kuwa kikombe alichoninywesha Mwenyekiti Maggid kimechangia kunitibu ugonjwa sugu unaowaathiri wasomi wengi, mbali ya kuwaneemesha walimwengu kama nilivyoelezea.

Wednesday, April 6, 2011

Mijadala ya Dini ni Muhimu

Watu wengi katika jamii yetu wanasema kuwa tusiendekeze mijadala ya dini. Wanasema kuwa ni tishio kwa amani na maelewano. Ninapenda kutafakari suala hilo.

Binafsi, naamini kuwa watu wenye akili timamu wanaweza kujadili mada yoyote bila matatizo. Watu wa aina hiyo wanajua kuwa katika mjadala wanachopaswa kufanya ni kutoa hoja, kusikiliza hoja, na kupinga hoja kwa hoja.

Watu wenye akili timamu wanafahamu kuwa, katika mjadala, kila mtu ana uhuru wa kuelezea fikra zake na mtazamo wake, na ana haki ya kusikilizwa. Na kila mtu ana wajibu wa kusikiliza hoja na mtazamo wa wengine.

Suala la mijadala, kwa watu wenye akili timamu, ni suala lililojengeka katika haki, uhuru, na wajibu, kama nilivyoelezea hapo juu. Wajibu huo ni pamoja na wajibu wa kuheshimiana katika hiyo mijadala. Kwa maana hiyo, mada yoyote inaweza kujadiliwa na watu wenye akili timamu, iwe ni siasa, uchumi, au dini.

Kuna pia wajibu wa kujielimisha. Mbali ya kwenda shule, au kusoma vitabu, mijadala ni njia mojawapo muhimu ya kuelimishana. Siamini kama dini zetu zinatutegemea tuwe waumini mbumbumbu. Naamini kuwa Muumba mwenyewe anatutegemea tuwe waumini tunaojibidisha kuzifahamu dini zetu. Kwa hivi, kusoma kuhusu dini na kushiriki mijadala kuhusu dini ni wajibu.

Sasa tatizo liko wapi, inapokuja kwenye dini, hadi watu waseme kuwa tusiendekeze mijadala ya dini? Tatizo si mada, bali vichwa vya wahusika. Labda ni wajinga au walevi. Hili ndilo tatizo. Wajinga au walevi wakipewa mada yoyote, uwezekano wa kushikana mashati ni mkubwa. Hata kama mada ni kuhusu umuhimu wa kujenga hospitali au kupeleka watoto shule, wajinga au walevi wanaweza kushikana mashati.

Suali ni je, kwa nini mada yoyote iwe ni hatari kujadiliwa? Na tukisema leo tusijadili dini, huenda kesho tutasema tusijadili siasa, na keshokutwa tusijadili elimu, na kadhalika. Kwa nini mada yoyote iwe ni hatari kujadiliwa? Inamaanisha kuwa wa-Tanzania ni wajinga au walevi?

Kama ni walevi, tupunguze ulabu. Kama ni wajinga, kinachopaswa kufanya ni juhudi za kufuta ujinga, ili tufikie mahali wa-Tanzania wawe na akili timamu kama nilivyoelezea hapo juu. Tunahitaji maandalizi ili mada kama dini ziweze kujadiliwa sawa na mada zingine, kuchangia elimu na maelewano.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...