Showing posts with label utamaduni. Show all posts
Showing posts with label utamaduni. Show all posts

Tuesday, December 17, 2019

Kofia ya CCM Nchini China

Naleta picha ya ujumbe wa CCM kwenye kikao na wenyeji wao mjini Shanghai, China, mwaka 2018. Hapo mezani upande wa kushoto kuna kofia ya CCM. Yawezekana walikwenda ziarani na magwanda yao na vikofia. Je, kuna sababu gani mimi kuandika ujumbe kuhusu kofia? Sina jambo la maana zaidi la kuongelea? Kwa nini nisiongelee madhumuni ya ziara na mafanikio yake?

Ninaandika ujumbe huu kama mtafiti, mwandishi, na mtoa ushauri juu ya masuala ya utamaduni na utandawazi. Nimekuwa nikifanya shughuli hizo hapa Marekani na Tanzania pia, ambako nimeendesha warsha mara kadhaa kuanzia mwaka 2008 katika miji ya Arusha, Tanga, na Dar es Salaam.

Ninajaribu kuwaelewesha watu kuwa tofauti za tamaduni zina athari kubwa, hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Tunapokutana na watu wa tamaduni tofauti na wetu, tuwe makini. Tunaweza tukaelewana vibaya, au tunaweza tusielewane. Ni muhimu tujielimishe kuhusu tofauti hizo kabla hayajatupata hayo.

Kofia ya CCM ni sehemu ya vazi rasmi la wana CCM. Ni utambulisho wao. Hata mimi ambaye sina chama ninawatambua kwa mavazi yao. Vyama vingine navyo vina mavazi yao. Kwa hapa nchini Tanzania, hakuna utata juu ya hayo mavazi. Lakini je, hali ni hiyo hiyo nje ya Tanzania kwenye tamaduni tofauti?

Nchini China, kofia ya kijani ni mkosi. Mwanaume kuvaa kofia ya kijani maana yake anatangaza kwamba mke wake ni mzinzi.

Kuhusu asili ya tafsiri hii ya waChina kuhusu kofia ya kijani, maelezo yanatofautiana. Baadhi ya maelezo ni kwamba zamani za kale, ndugu wa malaya walilazimishwa kuvaa kofia ya kijani wabebe aibu. Maelezo mengine ni kwamba zamani za kale, wahudumu katika madanguro walikuwa wanavaa kofia za kijani. Lakini kama nilivyogusia, maelezo yanahitilafiana. Ila jambo ambalo halina utata ni kwamba katika utamaduni wa China, kofia ya kijani ni mkosi kwani inatangaza habari ya uzinifu wa mke.

Sasa fikiria hiyo ziara ya ujumbe wa CCM China. Wafikirie wako sehemu mbali mbali kama wageni rasmi, wamevalia kofia za kijani. Bila shaka, wenyeji wao walifanya ukarimu na heshima kama ilivyo desturi. Lakini bila shaka, makada hao wa CCM watakuwa wameacha gumzo na taswira ambayo hawakutegemea.

Katika warsha ambazo nimeandaa Tanzania tangu mwaka 2008, waTanzania wachache sana wamekuwa wakihudhuria. Mbali ya warsha, nimekuwa nikielezea katika blogu zangu masuala ya athari za tofauti za tamaduni katika dunia ya utandawazi wa leo. Nimeandika hata kitabu, kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho kinapatikana Tanzania pia, kutoka katika maduka ya Kimahama (Arusha), Soma Book Cafe (Dar es salaam), na A Novel Idea (Arusha na Dar es Salaam).

Pamoja na kujaribu njia zote hizo, nimeona kuwa labda, kwa kuandika ujumbe huu kuhusu kofia ya CCM nchini China, waTanzania watanielewa vizuri na watachukua hatua stahiki katika masuala yote husikka, iwe ni mahusiano binafsi, biashara za kimataifa, utalii, diplomasia na kadhalika.

Thursday, October 11, 2018

Mchakato wa Kwenda Kuongelea Kitabu

Leo nimepata ujumbe kutoka kwa Dan, ambaye hivi majuzi alikipigia debe kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, katika duka la Barnes and Noble, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Anaendelea na juhudi yake. Ameandika:

Happy to spread the word about your book. Let me know if you are ever interested in doing a talk at our store. I can connect you with our manager.

Tafsiri yangu:

Ninafurahi kukitangaza kitabu chako. Nijulishe iwapo utapenda kuja kukiongelea katika duka letu. Nitaweza kukuunganisha na meneja wetu.

Kuwaalika waandishi kuongelea vitabu vyao ni utamaduni wa kawaida hapa Marekani. Ni fursa ya mwandishi kukutana na watu wanaotaka kujua mambo kama  historia ya mwandishi, changamoto za uandishi, falsafa na mawaidha yake kuhusu uandishi, na kadhalika. Vinakuwepo vitabu vya mwandishi, kwa watu kuvinunua na yeye kuvisaini. Wa-Marekani wanapenda kusainiwa vitabu, kama nilivyowahi kusema katika blogu hii.

Sunday, June 3, 2018

Vitendea Kazi vya Kampuni Yangu

Mwaka 2002, nilianzisha na kusajili kampuni ambayo niliita Africonexion, kama nilivyoandika katika blogu hii. Nilisajili kama kampuni binafsi, usajili ambao hapa Marekani hujulikana kama "sole proprietorship." Niliamua kuanzisha na kusajili kampuni hii ya kutoaelimu na ushauri wa masuala ya utamaduni kwa kuwa tayari nilikuwa na uzoefu wa shughuli hizo, nikihudumia vyuo, makanisa, mashirika, jumuia na watu binafsi.

Shughuli zangu hizi zimekuwa na mafanikio makubwa, kwa maana kwamba nimewasaidia watu kuelewa na kuepukana na mambo ambayo yanaweza kusababisha migogoro na kutoelewana. Wale ambao tayari walishakumbana na migogoro na kutoelewana nimewasaidia kufahamu kwa nini walijikuta katika migogoro na kutoelewana. Lakini mimi mwenyewe nimefanikiwa pia kujifunza mengi katika shughuli zote hizo.

Napenda kuelezea siri moja kubwa ya mafanikio haya. Siri hiyo ni kujielimisha kwa kutumia vitabu. Vitabu ndio vitendea kazi vyangu. Sichoki kununua na kusoma vitabu. Kulingana na shughuli za kampuni yangu, ninanunua na ninasoma vitabu kuhusu masuala kama utandawazi, utamaduni, na saikolojia. Jana, kwa mfano, bila kutegemea, nilikiona kitabu kiitwacho Riding the Waves of Culture, katika duka la Half Price Books, mjini Apple Valley. Nilipokiona tu, nilitambua kuwa kitakuwa kitendea kazi muhimu.

Mbali na kutumia vitabu vya wengine, ninatumia pia kitabu nilichoandika mwenyewe, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitabu hiki kilitokana na uzoefu nilioongelea hapa juu. Si mimi tu ambaye ninakichukulia kitabu hiki kama kitendea kazi muhimu. Mifano ni profesa na mwandishi maarufu Becky Fjelland Brooks, ambaye aliakiongelea kitabu katika blogu yake. Mzee Patrick Hemingway, ambaye aliwahi kuishi Tanzania miaka yapata ishirini na tano, aliwahi kuniambia kuwa kitabu hiki ni "a tool of survival" yaani kimbilio la usalama.

Hili suala la kuviona vitabu kama vitendea kazi ni muhimu. Hainiingii akilini mtu aanzishe biashara, kwa mfano, halafu asitafute na kusoma vitabu au maandishi mengine juu ya uendeshaji wa biashara. Atafanikishaje malengo yake kama hafahamu vitu kama saikolojia ya binadamu, ambao ndio wateja wake? Atafanikiwaje kama hafahamu namna ya kuwasiliana na watu? Kama wateja wake ni wa tamaduni tofauti na utamaduni wake, ni muhimu mno afahamu tofauti hizo.

Nilivutiwa na msimamo wa Mama Barbro Finskas Mushendwa, mmiliki wa kampuni ya utalii ya J.M Tours, yenye makao yake Arusha, Tanzania. Baada ya kusoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, aliamua kununua nakala kadhaa kwa ajili ya wafanyakazi wake, ambao walikuwa ni madreva wa watalii. Aliona haraka kuwa kitabu hiki kinafaa kama kitendea kazi na madreva wake walinithibitishia hivyo, kama nilivyoripoti katika blogu ya ki-Ingereza.

Mmiliki wa kampuni yoyote anajua ulazima wa vitendea kazi kama vile magari na kompyuta, sawa na mkulima navyojua ulazima wa jembe na shoka. Lakini sijui ni wamiliki wa makampuni na wafanya biashara wangapi wa Tanzania wenye mtazamo kama wa Mama Mushendwa, wa kutambua kuwa vitabu ni vitendea kazi. Ninaona wanaanzisha kampuni au biashara na kuziendesha kimazoea,  au kwa kutegemea kudra ya Mungu au hata waganga wa kienyeji. Daima ninaona matangazo ya waganga wa kienyeji wakinadi dawa za mafanikio kibiashara.

Ninapoongelea mada hii ya vitabu kama vitendea kazi, ninakumbuka juhudi aliyofanya Mwalimu Nyerere katika kutekeleza kile alichoita elimu yenye manufaa. Aliwahimiza watu kujisomea ili kuboresha shughuli walizokuwa wanafanya. Chini ya uongozi wake, vilichapishwa na kusambazwa vitabu kuhusu kilimo, uvuvi, useremala, na kadhalika. Ninakumbuka kwamba kijijini kwangu, vitabu hivyo vilihifadhiwa katika nyumba ya baba yangu.

Pamoja na mimi kutumia vitabu vya wengine kama vitendea kazi, ninashukuru kwamba nami ni mwandishi. Ninapangia kuendelea kuandika ili kuchangia ufanisi katika shughuli zangu na za wengine.

Wednesday, December 13, 2017

Mahojiano Yangu Katika "Wayne Eddy Affair"

Katika wiki chache zilizopita, nimehojiwa mara tatu katika kipindi kiitwacho "Wayne Eddy Affair" cha Kymn Radio hapa Northfield, Minnesota. Mwendeshaji wa kipindi, Wayne Eddy, ambaye anaonekana pichani hapa kushoto, tulikutana kwa bahati tu hapa Northfield, wiki chache zilizopita. Ni mzee mzoefu, ambaye emeendesha vipindi vya redio kwa zaidi ya miaka hamsini, na ni mchangamfu. Kutokana na mahojiano yetu, tumezoeana sana na tumekuwa marafiki.

Mahojiano hayo, ambayo yalikuwa ya papo kwa papo, yalihusu mambo mengi , hasa maisha yangu tangu kijijini kusini magharibi Tanzania, kusoma kwangu, historia na utamaduni wa Tanzania, kuja kwangu Marekani, na shughuli ninazofanya hapa. Katika sehemu ya tatu ya mahojiano haya, ninasikika nikisimulia hadithi ya ki-Matengo na na nyingine kutoka Burkina Faso. Karibu, uyasikilize mahojiano hayo mtandaoni hapa.

Thursday, December 7, 2017

Kitabu "Matengo Folktales" Chaendelea Kuwa Gumzo

Kama nilivyoeleza katika blogu hii, kitabu changu, Matengo Folktales, kilitajwa tarehe 23 November, 2017, katika programu ya televisheni iitwayo Jeopardy ambayo ni maarufu hapa Marekani. Kwa kuwa sikuwa na mazoea ya kuangalia program hii, wala nyingine yoyote, sikufahamu umaarufu wake. Kumbe sasa, baada ya kitabu changu kutajwa, nimeshuhudia na ninaendelea kushuhudia msisimko miongoni mwa wa-Marekani wa kina aina.

Mbali na watu ninaokutana nao mitaani, maprofesa wenzangu hapa chuoni St. Olaf nao wamekuwa wakinipongeza sana. Siku kadhaa nilizopita, kwenye mkutano mjini St. Paul, profesa moja wa chuo cha Macalester naye aliniambia kutajwa katika Jeopardy ni kwamba nimefikia kilele cha "popular culture" hapa Marekani.

Note hayo badi hayajaniingia sawa sawa kichwani, kwa sabbat, kama nilivyosema, sikuwa na mazoea wala ufahamu wa kipindi cha Jeopardy. Ninaanza kuelewa, ila sitaweza kuelewa kama wa-Marekani wenyewe wanavyoelewa, kwani ni suala la tofauti za tamaduni. Kama hukukulia katika utamaduni fulani, ni vigumu sana kuyafahamu mambo ya utamaduni ule sawa na wanavyofahamu wenye utamaduni ule. Ni hivyo kwa Wa-Afrika walioko hapa Marekani, na kwa wa-Marekani walioko Afrika.

Leo hapa chuoni tulikuwa na mkutano wa maprofesa, ambao tunafanya mara moja kila mwezi. Mkutano ulihusu masuala mbali mbali, na ulipokaribia kwisha, ilikuja zamu ya afire taaluma wa chuo kusema machache. Baadhi ya mambo aliyosema ni kutangaza mania ya watu waliochapisha vitabu katika siku za karibuni, na majina ya watu waliojipatia tuzo au heshima kwa namna nyingine. Kati ya watu has, alitaja tukio la kitabu changu kutajwa katika Jeopardy. Alianza kwa kuuliza, nani kati yetu anategemea itakuja siku atajwe katika Jeopardy?

Baada ya kusema hivyo, alionyesha kwenye skrini kubwa picha hii hapa kushoto kama iliyoonekana katika Jeopardy. Mkutano ulipoisha, watu waliendelea kuongea nami kwa furaha kuhusu maana ya tukio hili katika utamaduni wa Marekani. Kwangu hii ni elimu ya ziada, nikiwa kama mtafiti wa tamaduni, mada ambayo ninaitolea mihadhara katika taasisi na jumuia mbali mbali na nimeiandikia makala na pia kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Kwa kuwa ninafanya juhudi kujielimisha na kuelimisha wengine, nina kila sababu ya kujiwekea kumbukumbu ya mambo hayo, kama ninavyofanya hapa katika blogu yangu. Ni muhimu nijiwekee kumbukumbu hizi, ili angalau watoto wangu na vizazi vijavyo waweze kujua nilikuwa ninafanya nini wakati wa uhai wangu.

Tuesday, September 5, 2017

Wadau Wanauliza Wanilipe Kiasi Gani

Siku chache zilizopita nilileta taarifa katika blogu hii kuhusu mwaliko niliopata kutoka Red Wing, kwenda kuongelea utamaduni wa hadithi. Tarehe 31 Agosti, wameniletea ujumbe kuniulizia iwapo kiwango cha malipo yangu ni kiasi gani. Huu ni utaratibu wa kawaida hapa Marekani. Mtu akialikwa kuhutubia, analipwa. Viwango vya malipo hutofautiana kulingana na umaarufu wa mwalikwa.

Suala la malipo ni tata kwangu, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Kipaumbele changu ni kutoa huduma kwa jamii. Malipo ni matokeo. Ninatoa mihadhara kwa wenye uwezo wa kunilipa na kwa wasio na uwezo wa kunilipa. Sipendi kuchukua pesa maadam tu ni pesa. Lazima nijiridhishe kuhusu uhalali wa hizo pesa.

Kwa msingi huo, ninatafakari ulizo kutoka Red Wing kuhusu malipo. Mwaliko wa Red Wing unahusu hadithi za jadi za wahenga wetu. Si hadithi zangu, kwa sababu sikuzitunga mimi. Ni urithi wetu wa tangu zamani. Sina hati miliki. Suala la kupokea malipo ni tata. Wale walionisimulia hadithi zilizomo katika kitabu cha Matengo Folktales, kwa mfano, hawakuwa na utamaduni wa kulipwa, na sikuwalipa.

Hata hivyo, nitakwenda Red Wing si kusimulia hadithi tu, bali pia kuongelea utamaduni wa kusimulia hadithi. Nitatoa elimu kuhusu suala hilo, kuanzia chimbuko la usimuliaji wa hadithi hadi kuhusu mchango wa hadithi katika jamii. Itakuwa kama darasa la fasihi simulizi. Kwa upande huo, kulipwa hakuna dosari.

Jambo la ziada ni kwamba kutoka hapa mjini Northfield ninapoishi hadi Red Wing ni mwendo wa saa moja. Nitatumia muda kuandaa mambo ya kusema na nitaingia gharama za safari. Ninaona ni sahihi kupokea malipo.

Sunday, July 9, 2017

Wole Soyinka na Madikteta wa Afrika

Wole Soyinka ni mmoja wa waandishi bora kabisa kutoka Afrika. Ameandika tamthilia, riwaya, mashairi, insha, na wasifu wake. Pia ametafsiri riwaya ya ki-Yoruba ya D.O. Fagunwa. Tafsiri hiyo inaitwa Forest of a Thousand Daemons: A Hunter's Saga.

Pamoja na umahiri wake katika kubuni visa na katika kuimudu lugha ya ki-Ingereza, Soyinka anachota sana mbinu na vipengele vingine vya sanaa na masimulizi ya jadi, hasa ya wa-Yoruba, lakini pia ya mataifa mengine, akienda mbali hadi u-Griki ya kale. Umahiri wake kama mwandishi umetambuliwa kwa namna mbali mbali, ikiwemo tuzo ya Nobel katika fasihi, ambayo alitunukiwa mwaka 1986.

Katika kazi zake, anashughulikia masuala ya aina mbali mbali, kama vile siasa, itikadi, ukoloni, ukoloni mambo leo, utamaduni, na fasihi ya Afrika na kwingineko. Udikteta ni mada ambayo Soyinka ameishughulikia tangu zamani, sio tu katika maandishi na mahojiano, bali pia kama mwanaharakati. Tamthilia ya Kongi's Harvest ni mfano mzuri. Tamthilia hii tuliisoma nilipokuwa mwanafunzi katika idara ya "Literature," Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, 1973-76.

Wiki hii nimesoma A Play of Giants. Ni tamthilia ambayo inazama zaidi katika mada ya madikteta wa Afrika. Nilifahamu jambo hilo tangu zamani, kama nilivyoelezea siku chache zilizopita katika blogu hii. Soyinka anawaumbua madikteta hao. Anatumia kejeli kuelezea fikra na matendo yao, ulevi wa madaraka, uduni wa akili zao, na ukandamizaji wa haki za binadamu. Uduni wa akili zao unadhihirika kwa namna wanavyoongelea mambo yasiyo na maana, na kama wanaongelea mambo ya maana, hoja zao ni za ovyo kupindukia.

Madikteta hao wanaongelea jinsi wanavyoweza kudumu madarakani. Wanabadilishana mawazo na uzoefu wao. Wazo moja ni kutawala kwa mkono wa chuma na kuwafanya raia waishi kwa hofu. Hofu inaweza kujengwa mioyoni mwa raia kwa kutumia ushirikina na kuwafanya waamini kuwa mtawala anaona kila kinachoendelea nchini, Kwa njia hiyo, raia wanaogopa hata kuwazia kupinga utawala, kwani wanaamini kuwa mtawala atajua.

Udikteta ni mada ambayo imeanishwa katika kazi za fasihi tangu zamani sana. Tunaisoma katika The Epic of Gilgamesh, kwa mfano, na katika baadhi ya tamthilia za Shakespeare. Katika kusoma A Play of Giants, nimewazia sana riwaya ya Ngugi wa Thiong'o, Wizard of the Crow, ambamo dikteta anaumbuliwa pamoja na mfumo wa utawala wake kwa njia ya kejeli, sawa na anavyofanya Soyinka.

Ingawa kuna matumizi ya kejeli, A Play of Giants si tamthilia ya kufurahisha, bali inatibua akili na kunifanya nijiulize binadamu tunawezaje kuishi katika himaya ya udikteta. Kejeli ya mwandishi inanifanya mimi msomaji nicheke, lakini si kicheko cha furaha, bali dhihaka juu ya madikteta na aibu juu yetu wanadamu.

Monday, July 3, 2017

Ninapenda Muziki wa Reggae

Ukivaa kofia kama hii niliyovaa pichani hapa kushoto, halafu useme hupendi reggae, hakuna atakayekuelewa. Kofia, sawa na vazi lolote, inawasilisha ujumbe. Ni tamko. Kofia hii niliyovaa inawafanya watu wafikirie vitu kama Rastafari, reggae, Bob Marley, na Jamaica, ambako muziki wa reggae ulianzia.

Muziki wa reggae umeenea sana duniani, kuanzia visiwa vya Pacific, hadi Afrika Kusini; Senegal hadi Sweden. Reggae haichagui kabila, taifa, wala utamaduni. Niliwahi kwenda chuo kikuu cha Arizona, Tucson, nikaambiwa kuwa Wahindi Wekundu wanaipenda reggae. Siku moja, nilitembea katika mtaa mdogo mjini Tel Aviv, Israel, nikaona mbele yangu bango kubwa la picha ya Bob Marley.

Kwa hiyo, kutokana na kwamba siwezi kujumlisha habari za muziki wa reggae ulimwengu mzima, ninawazia zaidi Jamaica. Kutokana na kusoma vitabu juu ya Rastafari na reggae, ninavutiwa na jinsi muziki wa reggae ulivyounganika na itikadi ya Rastafari, ukawa ni sauti ya walalahoi dhidi ya unyonyaji, ukandamizaji, na dhulma za kijamii, kiuchumi, na kadhalika, ndani na nje ya Jamaica.

Sunday, April 2, 2017

Mhadhara Chuo Kikuu cha Minnesota Juu ya Kitereza

Juzi tarehe 31, Dr. Charlotte (Shoonie) Hartwig na mimi tulitoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Minnesota, juu ya mwandishi Aniceti Kitereza. Huyu ni mwandishi muhimu ambaye, hata hivyo, hafahamiki sana. Mama Shoonie amekuwa akiandika kitabu ambacho nami nimechangia, na mhadhara wetu ulihusu kitabu hiki ambacho tunategemea kukichapisha.

Kitereza alizaliwa mwaka 1896 katika kisiwa cha Ukerewe kilichomo katika Ziwa Victoria, upande wa Tanzania. Alisomea katika shule za wamisheni, na alipomaliza aliajiriwa kazi kadhaa. Alivyozidi kukua alipata dhamira ya kuhifadhi mila na desturi za zamani za wa-Kerewe, ili zisipotee. Kama sehemu ya juhudi hiyo aliandika riwaya katika lugha ya ki-Kerewe, ambao aliukamilisha mwanzoni mwa mwaka 1945. Andiko hili ni hazina ya mila na destruí za wa-Kerewe wa zamani, ila Kitereza aliandika kwa mtindo wa hadithi ya kubuni, ili wasomaji wasichoke kusoma.

Baada ya juhudi na mahangaiko ya miaka mingi ya kutafuta mchapishaji, na kufuatia ushauri wa marafiki zake wa-Marekani, Kitereza aliutafsiri mswada wake kwa ki-Swahili. Hata hivyo, aliendelea kungoja kwa miaka mingi hadi mwaka 1980 ambapo mswada ulichapishwa kama kitabu, Bwana Myombekere na Bibi Bugonoka na Ntulanalwo na Buliwhali.

Mama Shoonie ni mtu pekee aliyesalia mwenye taarifa za ndani za Kitereza, kwani yeye na mumewe, Dr. Gerald Hartwig, walimfahamu vizuri Kitereza baada ya kuonana naye kwa mara ya kwanza mwaka 1968 Ukerewe. Mbali ya kukutana naye mara kwa mara miaka ile ya mwanzo, waliendelea kuandikiana barua hadi miaka ya mwisho wa maisha yake. Kitereza alikuwa hodari wa kuandika barua; ananikumbusha waandishi kama Ernest Hemingway na Shaaban Robert.

Katika mhadhara wa juzi, Mama Shoonie alielezea maisha ya Kitereza na mambo aliyofanya kama mwandishi. Maelezo yake aliyaambatanisha na picha za Kitereza, mke wake, na familia nzima ya Hartwig. Watoto wa familia ya Hartwig walikuwa wadogo sana wakati huo. Mama Shoonie alielezea kuwa Kitereza alikuwa anajituma sana katika shughuli yake ya kuhifadhi mila na destruí za wahenga kwa kusukumwa na suali ambalo alilitunga mwenyewe, "Tunawajibika kuwafundisha nini watoto wetu?"

Ilipokuja zamu yangu, nilielezea kwa ufupi uandishi wa Kitereza kwa mujibu wa mtazamo wangu kama mwana fasihi. Nilisisitiza masuala kadhaa muhimu yanayojitokeza katika taaluma ya fasihi ya Afrika, hasa suala la uandishi katika lugha za ki-Afrika na suala la tafsiri. Niligusia jinsi riwaya ya Bwana Myombekere inavyoweza kutupa mtazamo mpya kuhusu historia ya riwaya ya ki-Afrika, na jinsi inavyoweza kuchambuliwa sambamba na kazi za waandishi kama Daniel O. Fagunwa na Amos Tutuola wa Nigeria, Gakaara wa Wanjau wa Kenya, na Shaaban Robert wa Tanzania. Huu utakuwa ni mtazamo wa fasihi linganishi.

Nimesoma tafsiri ya Kitereza ya riwaya yake. Ki-Swahili chake, ingawa kinatofautiana na ki-Swahili sanifu, kina ladha na mtiririko wa hadithi simulizi za lugha za ki-Bantu kama vile lugha yangu ya ki-Matengo. Kwa msingi huo, ninaipenda tafsiri ya Kitereza. Riwaya yake imetafsiriwa kwa ki-Faransa na ki-Jermani, lakini tafsiri hizo, kwa mujibu wa Profesa Gabriel Ruhumbika, zina walakini. Kauli ya Profesa Ruhumbika ina uzito sana, kwani lugha mama yake ni ki-Kerewe na pia yeye ni mashuhuri katika uwanja wa kutafsiri.

Profesa Ruhumbika mwenyewe ametafsiri kwa ki-Ingereza riwaya ya Kitereza kama ilivyoandikwa ki-Kikerewe, na tafsiri yake imechapishwa kama Mr. Myombekere and His Wife Bugonoka, Their Son Ntulanalwo and Daughter Buliwhali. Katika kuisoma tafsiri hii, nilivutiwa nayo, sawa na nilivyovutiwa na tafsiri ya ki-Swahili ya Kitereza mwenyewe. Ni tafsiri ambayo ninapendekeza isomwe na yeyote. Hivyo hivyo, ninakipendekeza kitabu cha Mama Shoonie kijacho. Ni kitabu chenye taarifa nyingi, zikiwemo barua na picha, ambazo ulimwengu haujaziona. 

Sunday, February 26, 2017

Mpiga Debe Wangu Kutoka Liberia

Nina jadi ya kuwatambulisha wasomaji na wapiga debe maarufu wa vitabu vyangu katika blogu hii. Ninafanya hivyo ili kuwashukuru, nikizingatia kuwa wanachangia mafanikio yangu kwa jinsi wanavyoupokea mchango wangu.

Leo ninapenda kumtambulisha Charles Chanda Dennis, raia wa Liberia ambaye anaishi hapa Marekani, jimbo la Minnesota. Huyu ni mtu maarufu, hasa katika jamii ya wa-Afrika na wa-Marekani Weusi. Ni mtangazaji na mwendeshaji wa kipindi kiitwacho African Roots Connection katika KMOJ Radio.

Sikumbuki ni lini nilifahamiana na Charles, lakini nadhani ni miaka karibu kumi iliyopita. Aliwahi kunialika kama mgeni katika kipindi chake tukahojiana juu ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Wiki chache zilizopita, alinialika tena, tukafanya mahojiano marefu na ya kina ambayo unaweza kuyasikiliza hapa:

https://www.dropbox.com/home?preview=Story+Telling.mp3

Miaka yapata mitano iliyopita, Charles alialikwa na wanafunzi hapa chuoni St. Olaf kutoa mhadhara juu ya historia ya mahusiano na harakati za watu wa asili ya Afrika. Nilihudhuria mhadhara ule. Charles alithibitisha kuwa ni msomi wa uhakika, mwenye uwezo mkubwa wa kuchambua mambo. Anafahamu vizuri njia waliyopitia watu weusi barani Afrika na nje ya Afrika, hasa Marekani.

Alivyonialika kwenye mahojiano safari hii, hatukuongelea angenihoji kuhusu nini hasa, bali nilihisi kuwa alitaka kufuatilia masuala ambayo ninashughulika nayo katika jamii, kama mwalimu na mtoa ushauri kuhusu tamaduni. Niliguswa na masuali yake, kama inavyosikika katika ukanda wa mahojiano niliyoweka hapa juu.

Niliguswa kwa namna ya pekee jinsi Charles alivyonitambulisha kwa wasikilizaji, akinipigia debe kwa bidii na kuwahamasisha watu wasome Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ninamshukuru kwa hilo, nikizingatia umaarufu wa kipindi chake cha African Roots Connection na KMOJ Radio kwa ujumla.

Saturday, February 18, 2017

Mahojiano Radio KMOJ: Charles Dennis na Joseph L. Mbele

Tarehe 4 Februari, 2017, nilikuwa mgeni katika programu ya African Roots Connection ya Radio KMOJ, Minnesota. Mwendesha kipindi Charles Dennis alifanya mahojiano nami juu ya masuala mbali mbali yanayohusu historia na utamaduni wa watu wenye asili ya Afrika. Unaweza kuyasikiliza mahojiano hayo hapa:
https://www.dropbox.com/home?preview=Story+Telling.mp3

(mpiga picha Zawadi Mbele)


Friday, February 17, 2017

Umuhimu wa Kuzifahamu Tamaduni za Wengine

Mada ya tofauti za tamaduni na athari zake duniani ninaishughulikia sana. Kwa mfano, nimeandika kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nimeongelea suala hilo pia katika kitabu changu kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Vile vile ninaliongelea mara kwa mara katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza.

Umuhimu wa kuzifahamu tofauti za tamaduni unaonekana wazi wazi wakati tunapokumbana na matatizo katika mahusiano yetu na watu wa tamaduni ambazo si zetu. Tusijidanganye kwamba jambo hilo ni la kinadharia tu na kwamba halituhusu. Miaka michache iliyopita, wafanya biashara wa Tanzania walikwenda Oman kushiriki maonesho ya biashara. Walipata shida kutokana na kutojua utamaduni wa watu wa Oman. Taarifa hiyo iliandikwa katika blogu ya Michuzi.

Suala hili haliwahusu wafanya bashara tu, bali wengine pia, kama vile wanafunzi wanaokwenda nchi za nje, wanadiplomasia, watu wanaokwenda mikutanoni, na kadhalika. Kwa kuzingatia hayo, na kwa kuwa nimekuwa nikifanya utafiti katika masuala hayo, nimekuwa nikipata mialiko ya kutoa ushauri kwa jumuia na taasisi mbali mbali hapa Marekani. Vyuo vya Marekani, kwa mfano, vinapopeleka wanafunzi nchi za nje, kama vile nchi za Afrika, vinazingatia suala la kuwaandaa wanafunzi kwa kuwaelimisha kuhusu utamaduni wa huko waendako. Mwaka hadi mwaka nimealikwa kutoa elimu hiyo.

Nimewahi pia kuendesha semina Tanzania, kwenye miji ya Arusha, Tanga, na Dar es Salaam. Vile vile, kwa kuombwa na ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, niliwahi kutoa mihadhara Zanzibar na Pemba, juu ya utamaduni wa Marekani, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Kwa jinsi ninayofahamu umuhimu wa suala hili, nimekuwa nikikumbushia mara kwa mara kila ninapoweza. Kwa mfano, uhusiano ulipoanza kuimarika baina ya Tanzania na u-Turuki, nilikumbushia suala hilo katika blogu hii. Ningependa kuona suala hili la athari za tofauti za tamaduni linapewa kipaumbele katika maisha yetu kwani kulipuuzia ni kujitakia matatizo yasiyo ya lazima. Hii ndio sababu iliyonifanya nianzishe kampuni ya kutoa elimu na ushauri iitwayo Africonexion: Cultural Consultants.

Monday, January 2, 2017

Mazungumzo na Wanafunzi wa Chuo cha Gustavus Adolphus

Leo mchana nilikuwa Mount Olivet Conference & Retreat Center katika maongezi na wanafunzi wa chuo cha Gustavus Adolphus wanaokwenda Tanzania kimasomo. Profesa Barbara Zust, alikuwa amenialika, kama nilivyoandika katika blogu hii.

Wanafunzi wengi wa programu hii wanasomea uuguzi, na lengo la kwenda Tanzania ni kujifunza namna masuala ya afya na matibabu yalivyo katika mazingira tofauti na ya Marekani, kwa maana ya utamaduni tofauti. Kwa lengo hilo, wanafunzi husoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Kwa hivyo, hiyo jana, kama ilivyokuwa miaka iliyopita, niliwakuta wanafunzi wamesoma kitabu hiki na wamejizatiti kwa masuali ambayo yalinithibitishia kuwa ni wanafunzi makini wenye duku duku ya kujua mambo. Tulikuwa na mazungumzo ya kina yaliyodumu kwa zaidi ya saa mbili. Mwanafunzi mmoja, msichana, aliniambia kuwa yeye na mama yake walisoma kitabu changu pamoja. Taarifa hii imanigusa. Ni kama vile mzazi ametafuta namna ya kushiriki yale ambayo binti yake atayapitia atakapokuwa ugenini Tanzania.

Hiyo leo, nilipoanza kuongea na wanafunzi hao, niliwapongeza kwa uamuzi wao wa kwenda katika programu hii, ambayo itawapanua mtazamo na fikra, na hivyo kuwaandaa kukabiliana na dunia ya utandawazi wa leo. Baada ya mazungumzo yetu, tuliagana tukiwa tumefurahi, kama inavyoonekana pichani. Anayeonekana kulia kwangu kule nyuma kabisa ni Profesa Zust. Mbele yangu ni Mchungaji Todd Mattson.

Kwa taarifa zaidi kuhusu safari ya hao wanafunzi, fuatilia blogu yao With One Voice Tanzania

Saturday, October 8, 2016

People Before Profit: Kitabu Kuhusu Utandawazi

Leo nimejipatia kitabu kiitwacho People Before Profit kilichoandikwa na Charles Derber. Nimeanza kukisoma leo hii hii.

Kwanza, niseme kuwa kitabu hiki kina utangulizi ulioandikwa na Noam Chomsky. Hilo pekee ni ishara ya thamani ya kitabu hiki, kwani Chomsky ni mchambuzi maarufu wa masuala ya ulimwengu kwa mtazamo wa kimaendeleo. Ninamheshimu sana, kama ninavyowaheshimu wachambuzi kama Seymour Hersh na Amy Goodman.

People Before Profit ni hazina ya elimu. Kinafafanua dhana ya utandawazi. Kwanza kinaelezea ukale wa utandawazi, na kwamba utandawazi una historia ndefu. Haukuanza zama zetu hizi, bali umekuwepo kwa miaka maelfu na maelfu, ukibadilika katika kila zama.

Pili kitabu kinaelezea uhusiano wa utandawazi na tekinolojia, kama vile mapinduzi ya miundombinu na viwanda. Tatu, kitabu kinaelezea mahusiano ya utandawazi na utamaduni, na hasa katika mazingira ya leo, kuna suala la mahusiano ya utandawazi na itikadi, kama vile demokrasia.

Kuna dhana kadhaa juu ya utandawazi ambazo tunapaswa kuzihoji, kwa mfando dhana ya kwamba utandawazi unaondoa tofauti miongoni mwa nchi na jamii mbali mbali, na kuifanya dunia iwe na sura moja. Dhana hii imekuwa ikijadiliwa sana.

Inahojiwa, kwa mfano na watu wanaosema kwamba pamoja na juhudi za utandawazi kuufunika ulimwengu, kuna pia nguvu za jamii na tamaduni mbali mbali zinazopambana ili kujilinda, kujihami, na kuendelea kuwepo kwa misingi tofauti na ile ya utandawazi. Nami, katika warsha zangu, kama zile nilizowahi kuendesha Arusha na Dar es Salaam, nilijaribu kuibua masuala haya.

Kifupi ni kwamba kitabu hiki kinaibua masuala muhimu ya kuelimisha kuhusu hiki kinachoitwa utandawazi. Ninakipendekeza kwa yeyote anayethamini elimu.

Tuesday, July 7, 2015

Ukiwa na Siri Iweke Kitabuni

Wengi wetu tumesikia kwamba ukiwa na siri iweke kitabuni; mw-Afrika hataiona. Kwetu wa-Tanzania, hali ni hiyo hiyo. Mwaka hadi mwaka, tumekuwa tukisikia jinsi utamaduni wa kusoma vitabu unavyokosekana Tanzania. Si jambo la kujivunia.

Nimekuwa nikiandika mara kwa mara hali ninayoiona hapa Marekani, katika matamasha ya vitabu, maduka ya vitabu, na maktaba. Wa-Marekani kama inavyoonekana katika picha nilizoweka hapa, wana tabia tofauti.

Picha ya katikati niliipiga katika tamasha la vitabu Minneapolis. Ya chini niliipiga katika tamasha la vitabu Mankato. Picha ya juu kabisa sikumbuki niliipata wapi. Zote zinaonyesha jinsi watu wanavyosaka vitabu na kuchungulia yaliyomo. Sijui kama kuna siri iliyofichwa kitabuni ambayo hawataigundua.

Ninaweza kuleta mfano moja mdogo kutokana na kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambamo nimeweka taarifa kuhusu wa-Marekani na wa-Afrika. Tangu kichapishwe, mwaka 2005, maelfu ya wa-Marekani wamekisoma. Wanazijua siri zilizomo.

Mama mmoja m-Tanzania aliyeanzisha na anaendesha taasisi fulani alikuja hapa Marekani kuonana na washirika wake. Kwenye jimbo la Colorado aliulizwa kama amesoma kitabu hiki. Alikiri kuwa hakuwa amekisoma. Baada ya kurudi Tanzania, aliwasiliana nami akanielezea tukio hili. Tulifanya mpango, nikampelekea nakala.

Hiyo si hali ya kujivunia. Wenzetu wa-Marekani wanazoeshwa kuvipenda vitabu tangu utotoni. Wanakulia katika utamaduni huo. Kutokana na kulelewa katika utamaduni huo, hata wazee wananunua na kusoma vitabu, kama vilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Friday, June 5, 2015

Ninaombwa Tafsiri ya Kitabu Changu

Mara kadhaa, wa-Marekani wameniuliza iwapo kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimetafsiriwa kwa ki-Swahili au wameniomba nikitafsiri. Hao ni watu ambao wameishi au wanaishi Afrika Mashariki, hasa kwa shughuli za kujitolea.

Tangu nilipoanza kupata maulizo au maombi hayo, nimekuwa na wazo la kukitafsiri kitabu hiki. Mwanzoni kabisa, kwa kuzingatia uwingi wa wa-Somali walioingia na wanaendelea kuingia hapa Minnesota, ambao nimekuwa nikiwasaidia katika kuufahamu utamaduni wa Marekani, niliwazia kumwomba mmoja wa marafiki zangu wa ki-Somali atafsiri kitabu hiki kwa ki-Somali. Ninao marafiki kadhaa wa ki-Somali ambao, sawa na wa-Afrika wengine, wamekisoma na wanakipenda kitabu hiki. Lakini bado sijalitekeleza wazo hilo.

Jana nimepata ujumbe wa aina hiyo kutoka kwa mama mmoja m-Marekani, ambaye simfahamu. Ninanukuu sehemu ya ujumbe wake, na nimeweka nukta nne mahali ambapo kuna maneno ambayo sijayanukuu:

....I hope one day that you will translate your wonderful book. It is such a wealth of knowledge for me, and I know my Tanzanian friends would feel the same. Of course most good people would never mean to hurt or offend a new acquaintance, but sometimes when we are lucky enough to make a friend from a different country, we can use a little guidance on how to be respectful of each others cultural differences. Your book has given me that gift, and so I thank you for that!....Last year I went to Africa for the wildlife, but I found it was the Tanzanian people who stole my heart. This year I will return and visit Eli's village and meet his family. I am so excited about my visit. That is why it is so important to me to do my best to not be the classic "UGLY AMERICAN". Thank you again for your response. I hope you will consider writing the Kiswahili version of your book in the future. I know there would be many people who would find it both helpful and fascinating, as I did....

Natafsiri ujumbe huu ifuatavyo:

....Natumaini siku moja utakitafsiri kitabu chako murua. Ni hazina kubwa ya maarifa kwangu, na ninajua kuwa marafiki zangu wa-Tanzania watakiri hivyo. Ni wazi kuwa watu wengi wenye roho nzuri hawanuii kumuumiza au kumkosea mtu pindi wanapofahamiana, lakini mara nyingine tunapobahatika kumpata rafiki kutoka nchi nyingine tunaweza kunufaika na mwongozo wa namna ya kuheshimiana kutokana na tofauti za tamaduni zetu. Kitabu chako kimekuwa tunu ya aina hiyo, na nakushuru kwa hilo....Mwaka jana nilikwenda Afrika kuwaona wanyama mbugani, lakini waliouteka moyo wangu ni wa-Tanzania. Mwaka huu nitaenda tena kijijini kwa Eli na kukutana na familia yake. Ninafurahi sana ninavyoingojea safari hiyo. Ndio maana ni muhimu sana kwangu kujitahidi kwa namna yoyote kutokuwa yule anayefahamika kama "M-MAREKANI WA OVYO." Narudia kukushukuru kwa jawabu lako. Ninatumaini utalichukulia maanani suala la kuandika toleo la ki-Swahili la kitabu chako siku zijazo. Ninajua kitabu hiki kitawasaidia na kuwasisimua wengi kama ilivyokuwa kwangu....

Kwa wale ambao hawafahamu, hii dhana ya "Ugly American" imejengeka sana katika mawazo ya wa-Marekani wanaoamini kuwa tabia ya wa-Marekani wanapokuwa nje za kigeni si nzuri. Dhana hiyo ilishamiri baada ya kuchapishwa kwa kitabu cha Eugene Burdick na William J. Lederer kiitwacho The Ugly American.

Sina la nyongeza la kusema kwa leo, bali kujiuliza: mimi ni nani niyapuuze maombi ya watu? Ninapaswa kuchukua hatua stahiki, nikizingatia ule usemi maarufu wa ki-Latini: "Vox Dei vox populi," yaani sauti ya umma ni sauti ya Mungu.

Tuesday, May 26, 2015

Mwaliko Chuo Kikuu cha Winona

Nimepata mwaliko kutoka Chuo Kikuu cha Winona, Minnesota, kwenda kutoa mhadhara tarehe 23 Juni. Huu utakuwa ni mchango wangu katika semina ya mafunzo kwa wanafunzi kutoka sehemu mbali mbali itakayofanyika Juni 17-27. Kama ilivyo kawaida yangu, nimeona niweke kumbukumbu hapa.

Mafunzo haya yatalenga kuwaandaa wanafunzi hao kwa masomo ya juu, waweze kuifahamu hali halisi ya maisha ya chuoni na taratibu za taaluma, waweze kujijengea hali ya kujitambua na uwezo wa uongozi.

Mratibu wa mafunzo, Alexander Hines, ambaye anafahamu kiasi shughuli zangu,  aliniambia tuangalie ni kipi kati ya vitabu vyangu viwili kitafaa zaidi kwa semina hii: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences au Matengo Folktales. Nilishauri kwamba hicho cha pili kingeendana vizuri zaidi na dhamira kuu ya semina.

Tumekubaliana. Tumekubaliana nikaelezee ni nini tunaweza kujifunza kutokana na tamaduni za jadi za Afrika katika masuala haya ya kujitambua, falsafa ya maisha, na uongozi katika dunia ya leo na kesho.

Kama ilivyo kawaida yangu, huwa napokea mialiko ya kutoa mchango wa mawazo kufuatana na mahitaji ya wale wanaonialika. Itabidi nitafakari na kuandaa mawazo yatakayotoa mchango unaohitajika katika semina. Wazo la kutumia kitabu cha Matengo Folktales kama msingi ni wazo muafaka, kwani masimulizi haya ya jadi yanathibitisha jinsi wahenga wetu walivyoyatafakari masuala muhimu ya maisha, mahusiano, na mengine yanatuhusu leo na yataendelea kuwa muhimu daima.
 

Monday, February 23, 2015

Mihadhara ya Mankato ni Kesho

Siku zinakwenda kasi. Naona kama ndoto, kwamba safari yangu ya kwenda Chuo cha South Central, mjini Mankato, kutoa mihadhara ni kesho asubuhi.

Ninangojea kwa hamu kutekeleza majukumu yaliyoko mbele yangu, ambayo ni kwanza kuongea na wanafunzi wanaojiandaa kwa safari ya Afrika Kusini kimasomo, na pili ni kutoa mhadhara kwa jumuia ya chuo ambao mada yake itakuwa "Writing About Americans."

Maongezi yote hayo yatahusu masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake ulimwenguni. Wanafunzi wanaokwenda Afrika Kusini wanajiandaa kuishi na kushughulika na wa-Afrika, katika utamaduni ambao ni tofauti na ule wa Marekani. Utaratibu huu wa maandalizi, ambao umeshakuwa jambo la kawaida hapa Marekani, ingekuwa bora ufuatwe na wengine, kama nilivyowahi kuwaasa wa-Tanzania wenzangu.

Katika maandalizi hayo, hao wanafunzi wanasoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kitabu ambacho, japo kidogo, kinawagusa watu, tangu nilipokichapisha, tarehe 5 Februari, 2005. Namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kukiandika kama nilivyoandika, hadi kimekuwa msingi wa mialiko ya kwenda kuongelea yaliyomo na yatokanayo.

Katika mhadhara wa "Writing About Americans," ninapangia kuelezea mchakato wa kuandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kuanzia chimbuko la wazo la kukiandika, mchakato wa kukiandika, mambo muhimu niliyojifunza katika kuandika huku, hadi jinsi kitabu kilivyopokelewa na jamii, hasa wa-Marekani, ambao ndio wanaoongoza katika usomaji wake.

Jambo moja kubwa nililojifunza katika kutafakari na kuandika ni kuheshimu tamaduni, pamoja na tofauti zake. Shaaban Robert angeishi miaka mingi zaidi ya ile aliyoishi, angetufundisha mengi kuhusu suala hilo.

Panapo majaliwa, nikikamilisha ziara ya kesho, nitaandika taarifa katika hii blogu yangu.

Sunday, February 15, 2015

Hadithi za Wa-Matengo Chuoni Montana

Leo nimepata ujumbe wa barua pepe kutoka kwa mwalimu mmoja wa Chuo Kikuu cha Montana.Ananiambia kuwa muhula huu anafundisha kozi ya Mythologies, na kati ya nyenzo anazotumia ni kitabu changu cha Matengo Folktales. Ananiulizia kama nitaweza kuongea na wanafunzi wake kwani itawafaidia sana kuweza kuongea na mtafiti aliyeandaa kitabu, akatoa maelezo kuhusu mambo kadha wa kadha, kama vile mchakato wa utafiti. Amependekeza kuwa ikiwezekana, tupange siku waweze kuongea nami kwa njia ya Skype.

Nimemjibu kuwa niko tayari kutoa mchango wangu, na kuwa ninafurahi kusikia kuwa anafundisha masimulizi ya wa-Matengo, sambamba na yale ya wa-Griki wa kale na wengine. Ingawa binti yangu Zawadi alishanionyesha namna ya kutumia Skype na akanisajili, sijawahi kutumia tekinolojia hii. Wengi wa rika langu au wale wanaotuzidi umri, tumezoea mambo ya zamani. Lakini dunia inavyobadilika, hasa tekinolojia, tunalazimika kukiri mazoea yana taabu.

Ujumbe niliopata leo umenifanya niwazie mambo kadhaa. Kwanza, ni kwamba nilifanya utafiti na kuandaa kitabu hiki kwa miaka yapata 23. Wakati nachapisha kitabu hiki, nilikuwa tayari ninafundisha huku Marekani, baada ya kufundisha Chuo Kukuu Cha Dar es Salaam. Nilikuwa na hamu kuwa kitabu kiwe mchango wangu kwa elimu Tanzania, kwa ufundishaji wa chuo kikuu, kwani hapakuwa na kitabu cha aina ile nchini, kilichofaa kufundishia somo hili la hadithi za mapokeo ("folktales"). Nilijua hayo, kwa vile mimi ndiye nilikuwa mhadhiri wa somo la fasihi simulizi, sambamba na somo la nadharia ya fasihi.

Kilichotokea ni kuwa kitabu hiki kinatumika au kimetumika katika vyuo vikuu vya Marekani. Vyuo ninavyovifahamu ni Wichita State University, University of California San Diego, St. Olaf College, Colorado College, na College of St. Benedict/St. John's University. Niliwahi kualikwa na hicho chuo cha St. Benedict/St. John's kutoa mhadhara katika darasa la "fairy tales," ambalo lilikuwa linasoma kitabu cha Matengo Folktales, kama nilivyoripoti katika blogu yangu, na nilitoa pia mhadhara kwa jumuia ya chuo kuhusu kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Hayo ni baadhi ya mawazo yaliyomo akilini mwangu, wakati huu ninapofikiria ujumbe niliopata leo. Ingawa kwa upande mmoja ninafurahi, sijawahi kuridhika na hali hii ya vitabu vyangu kuwa vinawafaidia wa-Marekani, lakini sio wa-Tanzania. Hata hivi, kosa si langu. Mimi natimiza wajibu wangu wa kufanya utafiti, kuandika, na kuchapisha maandishi. Baada ya hapo, mwenye macho haambiwi tazama.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...