Showing posts with label muziki. Show all posts
Showing posts with label muziki. Show all posts

Monday, July 3, 2017

Ninapenda Muziki wa Reggae

Ukivaa kofia kama hii niliyovaa pichani hapa kushoto, halafu useme hupendi reggae, hakuna atakayekuelewa. Kofia, sawa na vazi lolote, inawasilisha ujumbe. Ni tamko. Kofia hii niliyovaa inawafanya watu wafikirie vitu kama Rastafari, reggae, Bob Marley, na Jamaica, ambako muziki wa reggae ulianzia.

Muziki wa reggae umeenea sana duniani, kuanzia visiwa vya Pacific, hadi Afrika Kusini; Senegal hadi Sweden. Reggae haichagui kabila, taifa, wala utamaduni. Niliwahi kwenda chuo kikuu cha Arizona, Tucson, nikaambiwa kuwa Wahindi Wekundu wanaipenda reggae. Siku moja, nilitembea katika mtaa mdogo mjini Tel Aviv, Israel, nikaona mbele yangu bango kubwa la picha ya Bob Marley.

Kwa hiyo, kutokana na kwamba siwezi kujumlisha habari za muziki wa reggae ulimwengu mzima, ninawazia zaidi Jamaica. Kutokana na kusoma vitabu juu ya Rastafari na reggae, ninavutiwa na jinsi muziki wa reggae ulivyounganika na itikadi ya Rastafari, ukawa ni sauti ya walalahoi dhidi ya unyonyaji, ukandamizaji, na dhulma za kijamii, kiuchumi, na kadhalika, ndani na nje ya Jamaica.

Sunday, August 9, 2015

Shaaban Robert na Mbaraka Mwinshehe Waliongelea Umuhimu wa Shule

Nikiachilia mbali jinsi wazazi wangu walivyohimiza elimu, nikiachilia mbali jinsi Mwalimu Nyerere alivyohimiza elimu, naukumbuka kwa namna ya pekee mchango wa mwandishi Shaaban Robert na mwanamuziki Mbaraka Mwinshehe katika kuhimiza elimu.

Ninakumbuka jinsi baba yangu, nilipokuwa shule ya msingi, alivyokuwa ananitia msukosuko iwapo nilishindwa kupata 100% katika zoezi lolote au mtihani wowote. Ninakumbuka pia jinsi Mwalimu Nyerere alivyokuwa anahimiza elimu, kwa watu wote, kuanzia watoto hadi wazee, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Shaaban Robert ni mtu anayenifanya nimkumbuke baba yangu. Nilijionea hayo niliposoma kitabu kiitwacho Barua za Shaaban Robert, ambacho habari zake niliziandika katika blogu hii. Humo tunaona jinsi Shaaban Robert alivyokuwa anamhamasisha mdogo wake Yusuf Ulenge afanye bidii katika elimu, akimtimizia mahitaji yote ya shule. Kwa wazazi na walezi, Shaaban Robert ni mfano wa kuigwa.

Mbaraka Mwinshehe, mwanamuziki ambaye wakati wa ujana wangu alitingisha Afrika Mashariki, ya Kati, na Kusini kwa nyimbo na muziki wake, aliimba wimbo maarufu wa kuwaasa vijana wazingatie elimu. Wimbo huo, "Enyi Vijana Sikilizeni," unaweza kuusikiliza hapa:

https://archive.org/details/EnyiVijanaSikilizeni

Wednesday, July 15, 2015

Tamasha la Afrifest: Agosti 1

Tamasha la Afrifest linakaribia. Litafanyika Agosti 1 mjini Brooklyn Park, Minnesota. Tamasha hili, ambalo hufanyika kila mwaka wakati kama huu, ni fursa kwa watu wenye asili ya Afrika kuonyesha mchango wao kihistoria katika nyanja mbali mbali.

Kunakuwa na maonesho ya mchango wa watu wenye asili ya Afrika katika historia ya binadamu, kuanzia chimbuko lake Afrika hadi kuenea katika nchi za mbali, kama vile Mashariki ya Kati, Asia, Ulaya, Marekani ya Kaskazini, ya Kati, na ya Kusini.

Ni fursa ya kujikumbusha historia ya himaya za kale barani Afrika, utumwa, ukoloni, mapambano dhidi ya ukoloni, juhudi za kuwaunganisha watu wenye asili ya Afrika ulimwenguni ("Pan-Africanism"). Afrifest hukumbushia itikadi na harakati zingine zaidi ya "Pan Africanism," kama vile "Negritude" na "Rastafarianism." Tangu kuanzishwa kwa Afrifest, jukumu la kutoa elimu hii limekuwa juu yangu, na niliandaa kijitabu kiitwacho Africans in the World, ambacho hupatikana kwenye tamasha.

Afrifest ni fursa ya kuonyesha utamaduni wa watu wenye asili ya Afrika unavyojidhihirisha katika vyakula, mavazi, fasihi, muziki na kadhalika. Ni fursa ya watu wa nchi na mataifa mbali mbali kukutana na kufahamiana. Huwavutia watu wa kila namna, kama vile wale ambao wamesafiria Afrika au wanawazia kwenda, au wale wenye mahusiano na wa-Afrika wa huku ughaibuni yaani wanadiaspora. Huwavutia hata wale ambao hawana uhusiano na Afrika, kwa mfano wale ambao wanapenda tu kujua kuhusu Afrika.

Ninapenda kushiriki matamasha ya Afrifest kama mtafiti na mwalimu wa tamaduni na fasihi, zikiwemo fasihi za wa-Afrika na wengine wenye asili ya Afrika. Zaidi ya hayo, ninaelezea shughuli zangu kama mshauri katika programu za vyuo vya Marekani za kupeleka wanafunzi Afrika.

Katika Afrifest, sawa na matamasha mengine, nawakilisha vitabu vyangu na kukutana na wadau mbali mbali. Ni fursa ya kuongelea mambo ya uandishi, na hasa uzoefu wangu wa kuandika juu ya wa-Afrika na wa-Marekani.

Si rahisi kuelezea kila kitu kinachofanyika katika Afrifest. Mambo ambayo sijayagusia ni pamoja na maonesho ya taasisi zinazotoa huduma za kijamii. Kuna michezo ya watoto, na kwa mwaka huu, tumeanzisha program ya ziada: nitakuwa na wasaa wa kuwaelimisha na kuwaburudisha watoto na hata vijana na watu wazima kwa hadithi za jadi kama za wa-Matengo.

Tuesday, May 10, 2011

Kitabu Kuhusu Mwanamuziki Salif Keita

Mchana huu nilikuwa kwenye chuo jirani cha Carleton kuhudhuria uzinduzi wa kitabu kuhusu Salif Keita, kilichoandikwa na Profesa Cherif Keita.

Profesa Keita ambaye anafundisha Carleton anatoka kijiji kimoja na Salif Keita, na walikua wakicheza pamoja utotoni. Ni marafiki hadi leo, na Profesa Keita alishamleta Salif Keita kwenye mji wetu huu wa Northfield kutumbuiza.

Profesa Keita ni mtafiti aliyezama sana katika masuala ya utamaduni, fasihi na falsafa ya jadi ya watu wa Mali. Ndiye hasa mtu anayeweza kutueleza kwa undani kuhusu maisha, sanaa na falsafa ya mwanamuziki Salif Keita.

Salif Keita ni miongoni mwa wanamuziki wa ki-Afrika ambao ni maarufu kabisa. Salif Keita ni albino, na maisha yake tangu alipozaliwa yamekuwa na misukosuko ya kusikitisha. Profesa Keita katika maelezo yake leo alidokezea hayo.

Salif pia ni mwanaharakati katika kutetea haki na maslahi ya albino. Ameanzisha na anaendesha taasisi inayoshughulikia suala hilo. Kiasi fulani cha mauzo ya kitabu hiki kitasaidia taasisi hiyo.

Nimenunua kitabu hiki leo na ninangojea kwa hamu kukisoma. Kama ilivyo kawaida ya blogu hii, Insh'Allah nitaandika habari zake baada ya kukisoma.

Wednesday, March 2, 2011

Orijino Komedi Wamtangaza Yesu



Kibao hiki cha Orijino Komedi kiliniacha hoi kabisa tangu nilipokiona mara ya kwanza. Mimi ni m-Katoliki. Kila ninapokiangalia kibao hiki, naishiwa nguvu, kwa jinsi Orijino Komedi wanavyoimba na kukatika. Ni balaa babu kubwa. Papo hapo wanawasilisha ujumbe kwa namna isiyosahaulika. Najikuta nikisema Mungu asifiwe kwa vipaji alivyowajalia Orijino Komedi.

Nashukuru kwamba miaka zaidi ya kumi iliyopita niliamua kuanza kumtafakari Yesu mimi mwenyewe. Ninaamini kwa dhati kuwa, kwa jinsi alivyokuwa karibu na watu na pia mpenda michapo, Yesu angeafiki jinsi Orijino Komedi wanavyotangaza neno lake kwa huo mtindo wao wa kuyaruka majoka.

Nawashukuru sana Orijino Komedi kwa kuleta neno la Yesu kwa namna hii ya kuvutia na kugusa moyo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...