Showing posts with label wa-Matengo. Show all posts
Showing posts with label wa-Matengo. Show all posts

Wednesday, July 15, 2015

Tamasha la Afrifest: Agosti 1

Tamasha la Afrifest linakaribia. Litafanyika Agosti 1 mjini Brooklyn Park, Minnesota. Tamasha hili, ambalo hufanyika kila mwaka wakati kama huu, ni fursa kwa watu wenye asili ya Afrika kuonyesha mchango wao kihistoria katika nyanja mbali mbali.

Kunakuwa na maonesho ya mchango wa watu wenye asili ya Afrika katika historia ya binadamu, kuanzia chimbuko lake Afrika hadi kuenea katika nchi za mbali, kama vile Mashariki ya Kati, Asia, Ulaya, Marekani ya Kaskazini, ya Kati, na ya Kusini.

Ni fursa ya kujikumbusha historia ya himaya za kale barani Afrika, utumwa, ukoloni, mapambano dhidi ya ukoloni, juhudi za kuwaunganisha watu wenye asili ya Afrika ulimwenguni ("Pan-Africanism"). Afrifest hukumbushia itikadi na harakati zingine zaidi ya "Pan Africanism," kama vile "Negritude" na "Rastafarianism." Tangu kuanzishwa kwa Afrifest, jukumu la kutoa elimu hii limekuwa juu yangu, na niliandaa kijitabu kiitwacho Africans in the World, ambacho hupatikana kwenye tamasha.

Afrifest ni fursa ya kuonyesha utamaduni wa watu wenye asili ya Afrika unavyojidhihirisha katika vyakula, mavazi, fasihi, muziki na kadhalika. Ni fursa ya watu wa nchi na mataifa mbali mbali kukutana na kufahamiana. Huwavutia watu wa kila namna, kama vile wale ambao wamesafiria Afrika au wanawazia kwenda, au wale wenye mahusiano na wa-Afrika wa huku ughaibuni yaani wanadiaspora. Huwavutia hata wale ambao hawana uhusiano na Afrika, kwa mfano wale ambao wanapenda tu kujua kuhusu Afrika.

Ninapenda kushiriki matamasha ya Afrifest kama mtafiti na mwalimu wa tamaduni na fasihi, zikiwemo fasihi za wa-Afrika na wengine wenye asili ya Afrika. Zaidi ya hayo, ninaelezea shughuli zangu kama mshauri katika programu za vyuo vya Marekani za kupeleka wanafunzi Afrika.

Katika Afrifest, sawa na matamasha mengine, nawakilisha vitabu vyangu na kukutana na wadau mbali mbali. Ni fursa ya kuongelea mambo ya uandishi, na hasa uzoefu wangu wa kuandika juu ya wa-Afrika na wa-Marekani.

Si rahisi kuelezea kila kitu kinachofanyika katika Afrifest. Mambo ambayo sijayagusia ni pamoja na maonesho ya taasisi zinazotoa huduma za kijamii. Kuna michezo ya watoto, na kwa mwaka huu, tumeanzisha program ya ziada: nitakuwa na wasaa wa kuwaelimisha na kuwaburudisha watoto na hata vijana na watu wazima kwa hadithi za jadi kama za wa-Matengo.

Sunday, February 15, 2015

Hadithi za Wa-Matengo Chuoni Montana

Leo nimepata ujumbe wa barua pepe kutoka kwa mwalimu mmoja wa Chuo Kikuu cha Montana.Ananiambia kuwa muhula huu anafundisha kozi ya Mythologies, na kati ya nyenzo anazotumia ni kitabu changu cha Matengo Folktales. Ananiulizia kama nitaweza kuongea na wanafunzi wake kwani itawafaidia sana kuweza kuongea na mtafiti aliyeandaa kitabu, akatoa maelezo kuhusu mambo kadha wa kadha, kama vile mchakato wa utafiti. Amependekeza kuwa ikiwezekana, tupange siku waweze kuongea nami kwa njia ya Skype.

Nimemjibu kuwa niko tayari kutoa mchango wangu, na kuwa ninafurahi kusikia kuwa anafundisha masimulizi ya wa-Matengo, sambamba na yale ya wa-Griki wa kale na wengine. Ingawa binti yangu Zawadi alishanionyesha namna ya kutumia Skype na akanisajili, sijawahi kutumia tekinolojia hii. Wengi wa rika langu au wale wanaotuzidi umri, tumezoea mambo ya zamani. Lakini dunia inavyobadilika, hasa tekinolojia, tunalazimika kukiri mazoea yana taabu.

Ujumbe niliopata leo umenifanya niwazie mambo kadhaa. Kwanza, ni kwamba nilifanya utafiti na kuandaa kitabu hiki kwa miaka yapata 23. Wakati nachapisha kitabu hiki, nilikuwa tayari ninafundisha huku Marekani, baada ya kufundisha Chuo Kukuu Cha Dar es Salaam. Nilikuwa na hamu kuwa kitabu kiwe mchango wangu kwa elimu Tanzania, kwa ufundishaji wa chuo kikuu, kwani hapakuwa na kitabu cha aina ile nchini, kilichofaa kufundishia somo hili la hadithi za mapokeo ("folktales"). Nilijua hayo, kwa vile mimi ndiye nilikuwa mhadhiri wa somo la fasihi simulizi, sambamba na somo la nadharia ya fasihi.

Kilichotokea ni kuwa kitabu hiki kinatumika au kimetumika katika vyuo vikuu vya Marekani. Vyuo ninavyovifahamu ni Wichita State University, University of California San Diego, St. Olaf College, Colorado College, na College of St. Benedict/St. John's University. Niliwahi kualikwa na hicho chuo cha St. Benedict/St. John's kutoa mhadhara katika darasa la "fairy tales," ambalo lilikuwa linasoma kitabu cha Matengo Folktales, kama nilivyoripoti katika blogu yangu, na nilitoa pia mhadhara kwa jumuia ya chuo kuhusu kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Hayo ni baadhi ya mawazo yaliyomo akilini mwangu, wakati huu ninapofikiria ujumbe niliopata leo. Ingawa kwa upande mmoja ninafurahi, sijawahi kuridhika na hali hii ya vitabu vyangu kuwa vinawafaidia wa-Marekani, lakini sio wa-Tanzania. Hata hivi, kosa si langu. Mimi natimiza wajibu wangu wa kufanya utafiti, kuandika, na kuchapisha maandishi. Baada ya hapo, mwenye macho haambiwi tazama.

Thursday, April 4, 2013

Mhadhara Katika Darasa la Wazee

Leo nilitoa mhadhara katika darasa la wazee, hapa Northfield. Somo wanalosomea ni "Folk and Fairy Tales."

 Hapa Northfield kuna masomo ambayo wazee husoma, yanayoendeshwa na taasisi iitwayo Cannon Valley Elder Collegium. Nimewahi kufundisha mara tatu darasa la wazee katika mfumo huo, na somo langu lilikuwa "The African Experience." Tulisoma na kujadili kitabu cha Things Fall Apart cha Chinua Achebe kama msingi wa kuongelea hali ya Afrika kabla na baada ya ukoloni, na hali ya leo ya ukoloni mamboleo.

 Nilivyoingia tu darasani leo, nilifurahi kuwaona wazee ambao walishasoma somo langu. Walikuwa yapata nusu ya darasa la leo.

 Nilichangia mawazo kuhusu somo hili la hadithi za fasihi simulizi, nikasimulia hadithi mbili za ki-Matengo ili kuthibitisha na kufafanua yale niliyosema kinadharia. Hadithi nilizosimulia ni "The Monster in the Rice Field" na "Nokamboka and the Baby Monster," ambazo zimo katika kitabu changu cha Matengo Folktales.

Tulikuwa na mazungumzo marefu, kuanzia saa saba na nusu mchana hadi saa tisa. Ilipendeza sana kuwaona wazee hao wakiimba nami wimbo wa ki-Matengo uliomo katika hadithi ya "The Monster in the Rice Field," wimbo unaorudiwa tena na tena. Ilivutia sana, na sote tulifurahi, tukazama katika kuichambua hadithi hii na ile ya "Nokamboka," ambazo zote zimejaa falsafa na masuali kuhusu maisha.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...