Showing posts with label hadithi za wa-Matengo. Show all posts
Showing posts with label hadithi za wa-Matengo. Show all posts

Sunday, November 8, 2015

Nimealikwa Kusimulia Hadithi

Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mama mmoja m-Liberia aishiye hapa Minnesota. Amejitambulisha kwamba tulikutana katika tamasha la Afrifest, akauliza iwapo nitaweza kwenda kusimulia hadithi mjini Maple Grove tarehe 14 mwezi huu, katika sherehe ya kumbukumbu ya kuzaliwa mtoto.

Nilielezea katika blogu yangu ya ki-Ingereza nilivyosimulia hadithi katika tamasha la Afrifest, hapa na hapa. Nilisimulia hadithi mbili kutoka katika kitabu cha Matengo Folktales. Mama aliyeniletea mwaliko wa tarehe 14 amenikumbusha kwamba mtoto wake na wengine walioshuhudia hadithi zangu katika Afrifest walivutiwa na wanataka nikasimulie tena.

Hii itakuwa mara yangu ya kwanza kusimulia hadithi katika mkusanyiko wa wanafamilia na marafiki zao, katika sherehe ya kifamilia. Nimezoea kusimulia katika vyuo. Nitatumia sehemu ya muda nitakaokuwa nao kuelezea dhima ya hadithi katika jadi za wa-Afrika na wanadamu kwa ujumla, halafu nitasimulia hadithi, na kisha nitawahimiza wasikilizaji kusaidia kuichambua hadithi nitakayosimulia. Ninawazia kusimulia hadithi kutoka Afrika Magharibi, labda Liberia, Senegal, au Burkina Faso, zilizomo katika kitabu cha West African Folktales.

Hadithi za jadi ni hazina yenye mambo mengi, kama vile falsafa, mafundisho kuhusu saikolojia na tabia za wanadamu, kuhusu mema na mabaya. Ziko zinazosikitisha, zinazofurahisha na kuburudisha, na zinazochemsha bongo, kama zile ziitwazo kwa ki-Ingereza "dilemma tales." Zote ni muhimu katika maisha ya wanadamu, kama nilivyojaribu kuelezea katika kitabu cha Matengo Folktales.

Wednesday, July 15, 2015

Tamasha la Afrifest: Agosti 1

Tamasha la Afrifest linakaribia. Litafanyika Agosti 1 mjini Brooklyn Park, Minnesota. Tamasha hili, ambalo hufanyika kila mwaka wakati kama huu, ni fursa kwa watu wenye asili ya Afrika kuonyesha mchango wao kihistoria katika nyanja mbali mbali.

Kunakuwa na maonesho ya mchango wa watu wenye asili ya Afrika katika historia ya binadamu, kuanzia chimbuko lake Afrika hadi kuenea katika nchi za mbali, kama vile Mashariki ya Kati, Asia, Ulaya, Marekani ya Kaskazini, ya Kati, na ya Kusini.

Ni fursa ya kujikumbusha historia ya himaya za kale barani Afrika, utumwa, ukoloni, mapambano dhidi ya ukoloni, juhudi za kuwaunganisha watu wenye asili ya Afrika ulimwenguni ("Pan-Africanism"). Afrifest hukumbushia itikadi na harakati zingine zaidi ya "Pan Africanism," kama vile "Negritude" na "Rastafarianism." Tangu kuanzishwa kwa Afrifest, jukumu la kutoa elimu hii limekuwa juu yangu, na niliandaa kijitabu kiitwacho Africans in the World, ambacho hupatikana kwenye tamasha.

Afrifest ni fursa ya kuonyesha utamaduni wa watu wenye asili ya Afrika unavyojidhihirisha katika vyakula, mavazi, fasihi, muziki na kadhalika. Ni fursa ya watu wa nchi na mataifa mbali mbali kukutana na kufahamiana. Huwavutia watu wa kila namna, kama vile wale ambao wamesafiria Afrika au wanawazia kwenda, au wale wenye mahusiano na wa-Afrika wa huku ughaibuni yaani wanadiaspora. Huwavutia hata wale ambao hawana uhusiano na Afrika, kwa mfano wale ambao wanapenda tu kujua kuhusu Afrika.

Ninapenda kushiriki matamasha ya Afrifest kama mtafiti na mwalimu wa tamaduni na fasihi, zikiwemo fasihi za wa-Afrika na wengine wenye asili ya Afrika. Zaidi ya hayo, ninaelezea shughuli zangu kama mshauri katika programu za vyuo vya Marekani za kupeleka wanafunzi Afrika.

Katika Afrifest, sawa na matamasha mengine, nawakilisha vitabu vyangu na kukutana na wadau mbali mbali. Ni fursa ya kuongelea mambo ya uandishi, na hasa uzoefu wangu wa kuandika juu ya wa-Afrika na wa-Marekani.

Si rahisi kuelezea kila kitu kinachofanyika katika Afrifest. Mambo ambayo sijayagusia ni pamoja na maonesho ya taasisi zinazotoa huduma za kijamii. Kuna michezo ya watoto, na kwa mwaka huu, tumeanzisha program ya ziada: nitakuwa na wasaa wa kuwaelimisha na kuwaburudisha watoto na hata vijana na watu wazima kwa hadithi za jadi kama za wa-Matengo.

Monday, June 8, 2015

Nimerekebisha Kitabu Changu

Kwa zaidi ya wiki moja, nimekuwa nikikipitia kitabu changu cha Matengo Folktales kwa ajili ya kukiboresha. Rekebisho moja nililofanya ni kuongeza ukubwa wa herufi ili kitabu kisomeke kwa urahisi zaidi. Nilikuwa pia naangalia kama kuna kosa lolote katika uandishi wa maneno. Nimerekebisha dosari zilizoziona katika maneno yapata matano

Ingawa nimetumia masaa mengi katika shughuli hiyo, kwangu si kitu, nikifananisha na kazi niliyofanya kwa miaka yapata ishirini na tatu katika kukiandaa kitabu hiki, tangu kuzitafuta na kuzirekodi hadithi, kuziandika kwa kuzitafsiri kwa ki-Swahili, kuzitafsiri kwa ki-Ingereza, kuzichambua, kusoma nadharia mbali mbali ili kutajirisha uchambuzi, na kurekebisha tafsiri na uchambuzi tena na tena.

Bahati ni kwamba miaka ya sabini na kitu, nilianza pia kufundisha somo la fasihi simulizi ("Oral Literature") na nadharia ya fasihi (Theory of Literature") katika idara ya "Literature" ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Katika kufundisha nilijionea mwenyewe kuwa hapakuwa na kitabu nilichoona kinafaa kwa somo la fasihi simulizi kwa wanafunzi wa kiwango cha chuo kikuu. Kuna usemi kuwa kama kitabu unachosoma huridhiki nacho, andika hicho kitabu unachokitaka.

Hali hiyo ya kukosekana kitabu kilichofaa katika ufundishaji wangu ilinihamasisha kutafakari masuala niliyokuwa nakumbaba nayo katika kuandika kitabu changu. Nilipania kuwa kiwe kinafaa kwa kufundishia. Miaka ilipita, nami nikawa natafiti, natafakari, na kuandika kiasi nilivyoweza. Wakati huo huo, nilikuwa nahangaika kuziboresha tafsiri za hadithi katika muswada. Shughuli hii ilinifundisha mengi kuhusu tafsiri, kama nilivyogusia katika makala iliyochapishwa katika jarida la Metamorphoses.

Historia ya kitabu hiki ni ndefu, na labda nitaweza kuiandika kiasi fulani siku za usoni. Ninakumbuka, kwa mfano, kwamba nilipokuwa nasomea masomo ya juu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin, 1980-86, nilichukua somo la nadharia ya fasihi katika idara ya "Comparative Literature" lililofundishwa na Professor Keith Cohen. Kati ya nadharia tulizojifunza ni "Structuralism." Professor Cohen alitupa "homework" ya kuchambua hadithi yoyote kwa kutumia nadharia ya "Structuralism."

Nilitumia fursa hii kuichambua hadithi ya "The Tale of Two Women," ambayo imo katika Matengo Folktales. Mtu anayefahamu angalau kidogo nadharia ya "Structuralism" ataona athari zake, japo kidogo,  katika uchambuzi wangu.

Baada ya harakati za aina aina kwa miaka mingi, nilichapisha kitabu hiki mwaka 1999. Ndoto yangu ya kuandika kitabu cha kutumiwa katika ufundishaji wangu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam haikutimia nilivyotarajia. Niliondoka Tanzania mwaka 1991, nikaja kufundisha katika idara ya ki-Ingereza Chuoni St. Olaf, huku  nikiwa bado naufanyia kazi mswada wangu. Kwa hivi kitabu kilichapishwa huku Marekani, na wanaokisoma ni wa-Marekani, kuanzia katika jamii hadi vyuoni, kama nilivyoelezea hapa na  hapa.

Masimulizi ni mengi, na kama nilivyogusia, labda nitafute wasaa miaka ijayo niandike kumbukumbu zangu za historia ya kitabu hiki.

Saturday, March 9, 2013

Matokeo Zaidi ya Mhadhara wa Faribault

African Folk Tales

When Joseph Mbele visited our class last week, one of the things he talked about is how folk tales can be so very valuable in learning about a culture. He said that's a way to understand what's important and what a culture sees as valuable and moral.  It made me very happy that I had already planned to make (force?) each student in my Humanities of South Africa class to present a South African Folk Tale to the rest of the class.

Joseph Mbele has a book of folk tales himself, which I am purchasing as soon as I get my next paycheck: Matengo FolktalesThese folk tales are from Tanzania, and I can't wait to read this.

Since we're studying South Africa, however, I found this book:
 Each student will get one folktale to present to the class through any means they choose:
storytelling
a skit (collaboration is encouraged)
a video/film
a powerpoint with appropriate pictures while telling...maybe even reading in that case
anything else they can think of.
Some of the stories include the following (Aren't the pictures spectacular!!??)





Nelson Mandela's Favorite African Folktales was published by W.W.Norton&Company in 2002.
I can't list all the contributors or artists, but the book is worth checking out.Everything is copyrighted, so I only gave you a little sampling here.
I can't wait to see what my students do with these stories! 


Tuesday, November 30, 2010

Asante, Joseph Mbele

Jioni hii, katika kuzurura mtandaoni, mitaa ya Google, nimekumbana na makala kwenye blogu fulani, ambayo inanitaja. Soma hapa.

Sikuwa nimeiona makala hii ambayo inataja ziara niliyofanya College of St. Benedict/St. John's University mwaka jana. Nilialikwa kutoa mihadhara. Katika darasa la Profesa Lisa Ohm, niliongelea hadithi na utamaduni, kufuatia maelezo yaliyomo katika kitabu cha Matengo Folktales, ambacho walikuwa wanakitumia. Soma hapa.

Mhadhara wa pili niliutoa kwa wanafunzi na walimu waliokuwa wanajiandaa kwenda Tanzania na Afrika ya Kusini, lakini ulihudhuriwa na wengi wengine. Lengo lilikuwa kuwaarifu kuhusu tofauti za msingi baina ya tamaduni wa mw-Afrika na ule wa m-Marekani, kama nilivyoeleza katika kitabu cha Africans and Americans.

Nakumbuka jinsi ukumbi ulivyojaa watu kwenye mhadhara huu, na kwenye meza nyuma ya umati walikuwa wameweka nakala nyingi za vitabu hivi viwili, kama ilivyo desturi hapa Marekani, wanapowaita waandishi kuzungumzia vitabu na uandishi. Soma hapa.

Nimefurahi kuona kuwa mazungumzo yangu kwa hao wa-Marekani yameelezwa kama ilivyoelezwa na mwandishi huyu. Nimefurahi jinsi anavyokiri kuwa yale niliyowaambia ndiyo aliyoyakuta Afrika Kusini. Huwa nakutana na wa-Marekani wengi wanaosema hivyo hivyo, wanaporudi kutoka Afrika. Nami nafanya juhudi nijielimishe zaidi kuhusu tofauti za tamaduni hizi, ili niweze kuboresha mafunzo na mawaidha ninayotoa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...