Wednesday, July 15, 2015

Tamasha la Afrifest: Agosti 1

Tamasha la Afrifest linakaribia. Litafanyika Agosti 1 mjini Brooklyn Park, Minnesota. Tamasha hili, ambalo hufanyika kila mwaka wakati kama huu, ni fursa kwa watu wenye asili ya Afrika kuonyesha mchango wao kihistoria katika nyanja mbali mbali.

Kunakuwa na maonesho ya mchango wa watu wenye asili ya Afrika katika historia ya binadamu, kuanzia chimbuko lake Afrika hadi kuenea katika nchi za mbali, kama vile Mashariki ya Kati, Asia, Ulaya, Marekani ya Kaskazini, ya Kati, na ya Kusini.

Ni fursa ya kujikumbusha historia ya himaya za kale barani Afrika, utumwa, ukoloni, mapambano dhidi ya ukoloni, juhudi za kuwaunganisha watu wenye asili ya Afrika ulimwenguni ("Pan-Africanism"). Afrifest hukumbushia itikadi na harakati zingine zaidi ya "Pan Africanism," kama vile "Negritude" na "Rastafarianism." Tangu kuanzishwa kwa Afrifest, jukumu la kutoa elimu hii limekuwa juu yangu, na niliandaa kijitabu kiitwacho Africans in the World, ambacho hupatikana kwenye tamasha.

Afrifest ni fursa ya kuonyesha utamaduni wa watu wenye asili ya Afrika unavyojidhihirisha katika vyakula, mavazi, fasihi, muziki na kadhalika. Ni fursa ya watu wa nchi na mataifa mbali mbali kukutana na kufahamiana. Huwavutia watu wa kila namna, kama vile wale ambao wamesafiria Afrika au wanawazia kwenda, au wale wenye mahusiano na wa-Afrika wa huku ughaibuni yaani wanadiaspora. Huwavutia hata wale ambao hawana uhusiano na Afrika, kwa mfano wale ambao wanapenda tu kujua kuhusu Afrika.

Ninapenda kushiriki matamasha ya Afrifest kama mtafiti na mwalimu wa tamaduni na fasihi, zikiwemo fasihi za wa-Afrika na wengine wenye asili ya Afrika. Zaidi ya hayo, ninaelezea shughuli zangu kama mshauri katika programu za vyuo vya Marekani za kupeleka wanafunzi Afrika.

Katika Afrifest, sawa na matamasha mengine, nawakilisha vitabu vyangu na kukutana na wadau mbali mbali. Ni fursa ya kuongelea mambo ya uandishi, na hasa uzoefu wangu wa kuandika juu ya wa-Afrika na wa-Marekani.

Si rahisi kuelezea kila kitu kinachofanyika katika Afrifest. Mambo ambayo sijayagusia ni pamoja na maonesho ya taasisi zinazotoa huduma za kijamii. Kuna michezo ya watoto, na kwa mwaka huu, tumeanzisha program ya ziada: nitakuwa na wasaa wa kuwaelimisha na kuwaburudisha watoto na hata vijana na watu wazima kwa hadithi za jadi kama za wa-Matengo.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...