Thursday, July 30, 2015

Nimepata Vitabu vya Warsha: Jamii na Taaluma

Leo nimepata vitabu vya warsha itakayofanyika hapa chuoni St. Olaf tarehe 17-20, mwezi Agosti, kuhusu jamii na taaluma. Warsha itawahusisha maprofesa wachache, kuongelea masuala kama nafasi ya mwanataaluma katika jamii, itikadi katika taaluma, na uhuru wa taaluma.

Washiriki wa warsha tunapata vitabu vya bure, ambavyo tutavijadili katika warsha. Tutaanza na viwili. Kimoja ni Not for Profit: Why Democracy Needs the Humanities, kilichotungwa na Martha C. Nussbaum. Cha pili ni Versions of Academic Freedom, kilichoandikwa na Stanley Fish. Kwetu tuliomo katika masomo ya nadharia ya fasihi, maandishi ya Stanley Fish katika uwanja huo ni maarufu sana.

Baada ya vitabu hivyo, tutajadili Compromising Scholarship: Religious and Political Bias in American Higher Education, kitabu cha George Yancey, na Professors and Their Politics, ambacho kimehaririwa na Neil Gross na Solon Simmon. Hiki cha pili ni mkusanyo wa insha za wataalam mbali mbali.

Warsha itakuwa nzito, sawa na masomo ya kiwango cha juu kabisa. Tutakuwa tunasoma kurasa nyingi kila siku kwa maandalizi ya mjadala wa masaa mawili kila siku. Ni fursa ya kujinoa katika fikra na mitazamo juu ya masuala muhimu ya taaluma, ufundishaji, na nafasi na mchango wetu katika jamii. Ni fursa pia ya sisi wenyewe kubadilishana mawazo na kufahamiana. Cha zaidi ni kuwa ninapenda vitabu vya kufikirisha na kuelimisha, na kuvipata vya bure si jambo dogo.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...