Showing posts with label Afrika Kusini. Show all posts
Showing posts with label Afrika Kusini. Show all posts

Wednesday, September 6, 2017

Muhula wa Masomo Unaanza

Wiki hii hapa chuoni St. Olaf, tunaanza muhula mpya wa masomo. Nitafundisha madarasa matatu. Mawili ni ya "First Year Writing," na moja ni "Post-colonial Literature." Katika "First Year Writing," tunafundisha uandishi bora wa ki-Ingereza.

Kozi ninayotaka kuongelea hapa  ni "Post-colonial Literature." Niliajiriwa hapa chuoni St. Olaf kuanzisha kozi hiyo, na nilianza kufundisha mwaka 1991. Ni kozi inayohusu fasihi kutoka nchi zilizokuwa katika himaya ya u-Ingereza wakati wa ukoloni ila zilikuja kuwa huru.

Ninapofundisha kozi hii, huwa ninaamua waandishi wepi kutoka nchi zipi nifundishe. Kwa muhula huu, niliamua kufundisha fasihi kutoka Afrika Kusini. Nilichagua waandishi wawili: Alex la Guma na Nadine Gordimer. Wote ni waandishi wa hadithi fupi na riwaya.

Nadhani tangu nilipokuwa mwanafunzi Mkwawa High School, nilisoma hadithi za Alex la Guma katika kitabu cha hadithi fupi kiitwacho Quartet. Baadaye, nilipokuwa mwanafunzi katika idara ya Literature, chuo kikuu cha Dar es Salaam, Alex la Guma alikuja kutoka London akatufundisha kwa siku kadhaa. Alialikwa na mkuu wa idara, mwalimu Grant Kamenju wa Kenya.

Nilifahamu kuwa Alex la Guma alikuja kuwa mwakilishi Uingereza wa chama cha ukombozi cha African National Congress cha Afrika Kusini, (ANC), kisha akawa mwakilishi wa ANC nchini Cuba. Alipofariki, nchini Cuba, nilikuwa ninasoma katika Chuo Kikuu cha Wisconsin Madison.

Nadine Gordimer ni mzungu aliyejihusisha na ANC. Alikuwa mpinzani wa utawala wa makaburu. Baada ya kuja Marekani kufundisha, nimebahatika kumwona Nadine Gordimer kwenye mkutano fulani wa kitaaluma. Sikumbuki ulikuwa ni mwaka gani. Nimefundisha hadithi zake fupi zilizokusanywa katika kitabu Six Feet of the Country, na riwaya zake, The Conservationist, The Pickup, na July's People.

Kufundisha juu ya waandishi hao wawili ni fursa ya kutafakari historia na siasa, hasa ukaburu na harakati za ukombozi katika Afrika Kusini. Yote hayo yamefungamana na fasihi, hasa katika karne ya ishirini, ambayo ndiyo kozi yangu itashughulikia. Tutafakari mitazamo ya waandishi hao wawili kuhusu siasa, mahusiano ya jamii, utamaduni, na itikadi katika Afrika Kusini. Tutaangalia athari za fasihi ya ulimwengu katika maandishi ya waandishi hao wawili na tutatambua mchango wa waandishi hao katika fasihi ya Afrika na ulimwengu.

Wednesday, July 27, 2016

Tumejadili "Valley Song," Tamthilia ya Athol Fugard

Leo katika darasa langu la African Literature, tumejadili Valley Song, tamthilia ya Athol Fugard, mwanatamthilia maarufu wa Afrika na ulimwenguni. Alizaliwa Afrika Kusini mwaka 1932. Ametunga tamthilia nyingi ambazo kwa ujumla wake ni kama rekodi ya yale ambayo Afrika Kusini imepitia kisiasa, kijamii, na kitamaduni. Kitabu chake cha Notebooks: 1960-1977 ni hazina ya kumbukumbu zake za kukua kwake kama msanii, falsafa yake ya sanaa, na tathmini yake ya wasanii mbali mbali kama vile Samuel Beckett, Bertolt Brecht, na Albert Camus.

Nimefundisha tamthilia kadhaa za Fugard, na ninaguswa zaidi na zaidi na kazi zake. Miaka ya karibuni, kwa mfano, nimejikuta ninafundisha Sorrows and Rejoicings tena na tena. Baadaye niliamua kufundisha tamthilia ambayo sikuwahi kuifundisha, nikachagua Valley Song.

Valley Song inahusu familia ya Buks, mkulima chotara nchini Afrika Kusini . Anaonekana tangu mwanzo akiwa ameshika mbegu za maboga. Ni mkulima anayefurahia kuona mbegu zinavyoota shambani, kustawi na kuzaa mazao. Lakini, anakabiliana na matatizo kadhaa. Kwa mfano, binti yake alitorokea mjini, ambako alifariki katika mazingira ya kutatanisha, akiwa ameacha mtoto mchanga aitwaye Veronika.

Ana wasi wasi kwamba atapoteza shamba na nyumba yake kutokana na kishawishi cha wazungu wenye fedha wanaofika fika kuangalia shamba na nyumba hiyo.  Juu ya yote, Veronika, ambaye sasa ni msichana mkubwa, anasema tena na tena kuwa anataka kwenda mjini akawe mwimbaji maarufu. Hapendi kuendelea kuishi shamba ambapo anaona hakuna fursa kama mjini.

Ndoto hii ya Veronika inamsumbua Buks, kwani anawazia jinsi binti yake alivyotorekea mjini na kufariki huko.  Hata hivyo, baada ya kumsikiliza sana Veronika, anamwacha aende. Dhamira ya jinsi mbegu za maboga zinavyoota na kustawi na kuzaa maboga makubwa makubwa inahusishwa na ndoto ya Veronika ya kukuza kipaji chake cha uimbaji na kisha kuwa na mafanikio makubwa.

Valley Song inaishia kwa matumaini ya namna hiyo, ambalo ni jambo jema lenye kugusa mioyo yetu. Tamthilia hii, ingawa fupi, ni uthibitisho mwingine wa kipaji cha Fugard kama msanii mwenye ufahamu wa kina wa uhalisia wa maisha, majaribu yake na uwezo wa binadamu wa kupambana nayo.

Sunday, June 28, 2015

Tamasha la Vitabu Mankato Limefana

Leo, nikiwa na binti yangu Zawadi, tulikwenda Mankato kushiriki tamasha la vitabu, Deep Valley Book Festival. Niliandika habari za tamasha hilo katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Nilipeleka vitabu vyangu vinavyoonekana mtandaoni, pamoja kijitabu kiitwacho Africans in the World. Vile vile tulipeleka "t-shirt" kama hizo tulizovaa pichani, zenye nembo ya kampuni yangu ndogo Africonexion: Cultural Consultants. Tunajifunza mengi katika kukutana na watu wanaofika kwenye meza yetu. Hatujui nini kitamvutia mtu fulani na kwa nini. Lakini watu hujieleza. Tunasikia habari nyingi, nyingine za kushangaza, zinazomfanya mtu anunue hiki au kile.

Inatufurahisha kuwaangalia watu wakipita kwenye meza mbali mbali kuangalia vitabu, kuongea na waandishi, wachapishaji na wengine wanaokutana nao katika tamasha. Nasi tunapata fursa ya kukutana na watu mbali mbali. Leo, kwa mfano, wamefika watu kwenye meza yetu ambao wametuambia wamefika Afrika: Botswana, Tanzania, na Namibia. Tunahisi walivutiwa na "t-shirt" tulizovaa, zenye ya ramani ya Afrika. Kila mmoja ametusimulia habari za safari yake. Tulijua kuwa tutakutana na baadhi ya watu tuliokutana nao wakati nilipotoa mihadhara katika Chuo cha South Central, katika maandalizi ya safari ya Afrika Kusini. Kama tulivyotarajia, walikuwepo watu kadhaa.



Hapa kushoto anaonekana kiongozi wa safari ya Afrika Kusini, mwalimu Becky Fjelland Davis, ambaye ni mwandishi. Alishiriki tamasha. Mwingine ni Paul Dobratz ambaye alihudhuria shughuli zote nilizofanya wakati wa ziara yangu Chuoni South Central. Naye alikuwemo katika safari ya Afrika Kusini. Binti yangu nami tulifurahi sana kusikia habari za safari.




Kama ilivyo kawaida hapa Marekani, watu wa rika mbali mbali huhudhuria matamasha haya ya vitabu. Wanayathamini sana, na mahudhurio huwa makubwa.

Daima ninaguswa ninapowaona wazazi wakiwa na watoto wao. Ninaguswa na jinsi wanavyowalea watoto wao katika utamaduni wa kupenda kusoma vitabu.






Imekuwa siku ya furaha sana kwa binti yangu na mimi. Tumefurahi kukutana na kuongea na watu wa aina aina, tuliowafahamu na ambao hatukuwafahamu. Tumerudi na kumbukumbu nyingi.

Sunday, March 1, 2015

Imekuwa Wiki ya Mafanikio

Wiki hii inayoisha imekuwa ya mafanikio makubwa kwangu. Napenda kwanza nifafanue kuwa dhana yangu ya mafanikio ni tofauti na ya wale wanaowazia fedha. Mimi ni mwelimishaji, darasani na katika jamii. Ni mtoa ushauri katika masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake, hasa katika dunia ya tandawazi wa leo. Ushauri huo natoa kwa njia mbali mbali, hasa maandishi na mazungumzo na watu binafsi au vikundi. Dhana yangu ya mafanikio imejengeka katika shughuli hizo.

Kwanza, nilijiandaa kwa ziara ya chuo cha South Central, mjini Mankato, ambako nilifanya mazungumzo na darasa la wanafunzi wanaojiandaa kwenda Afrika Kusini kimasomo, na halafu nikatoa mhadhara kwa wanajumuia hapo chuoni, ambao mada yake ilikuwa "Writing About Americans."

Maandalizi ya mazungumzo hayo yote yalikhusu kukusanya fikra zilizokuwa akilini mwangu na kuziweka pamoja ili kukidhi mahitaji ya mazungumzo yale. Ilikuwa rahisi kujitayarisha kwa maongezi na wanafunzi waendao Afrika Kusini. Nmaongezi ya aina hiyo na wa-Marekani wengi katika maandalizi ya kwenda Afrika.

Katika kuandaa mhadhara wa "Writing About Americans," nilijikuta ninatafakari namna ya kuwasilisha mada yangu. Hatimaye, niliamua kuzingatia uzoefu wangu wa kuandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Niliamua nielezee chimbuko la wazo na azma ya kuandika kitabu hicho, mchakato wa kuandika, na mambo niliyojifunza katika kuandika huko. Baada ya kuamua hivyo, nilikaa chini nikatmia dakika chache tu kuandika dondoo ambazo ningetumia katika mhadhara.

Nilipoziangalia dondoo hizo, nilijua kwa hakika kwamba nitatoa mhadhara mzuri. Na ndivyo ilivyokuwa, kama alivyoeleza Mwalimu Becky Fjelland Davis katika blogu yake. Baada ya ziara yangu, niliandika katika blogu yangu kwamba nilitegemea kuwa tathmini ya ziara yangu ingeendelea miongoni mwa wale waliohidhuria.

Ukweli wa dhana yangu umeendelea kujitokeza, na hapa napenda kuleta ujumbe ulioandikwa na mtu aliyehudhuria mhadhara wangu:

Dr. Mbele,

I attended the talk you gave at South Central and found it to be very interesting and insightful. You showed how valuable writing is in itself, by giving us a mirror of ourselves as authors.

Thank you for your willingness to share you observations of Africans and Americans as well as your own self-assessments.

I thoroughly enjoyed your talk and only wish that I could have remained loner to hear the questions from the audience.

Thank you for sharing your life and writing experiences with us at South Central College
.

Baada ya ziara ya Mankato, nilijikuta nikiongea kwa njia ya Skype na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Montana, ambao walikuwa wanasoma kitabu changu cha Matengo Folktales. Niliandika kuhusu mazungumzo hayo katika blogu hii. Mazungumzo yale yalikwenda vizuri sana. Wanafunzi na mwalimu wao walifurahi, na mimi pia.

Wameendelea kuelezea furaha yao. Mwanafunzi mmoja ameniandikia hivi:

Hello Dr. Mbele!

I was a student from Professor Olsen's Skype class earlier today, my name is Sara Saxton. I'm I just wanted to say thank you so much for your time and expressing your mind to our class! I really enjoyed hearing about your definition of a classroom. I agree with the aspect of having a classroom be a "safe place" for learning. I feel as though I have experienced many things outside of the classroom, but there is nothing that compares to being able to ask questions you've always wanted to ask in a classroom. Anyway, I just wanted to let you know I really enjoyed hearing about your tales and watching you preform them. It was great!

Thank you again
!!

Mwanafunzi mwingine kaniandikia hivi:

Shikamoo Dr. Mbele,

I hope I have used the greeting properly. I wanted to say thank you taking the time to speak with, and preform for our class today over Skype. Growing up in Montana there are not many oppertunities to experience the vastness of culture the world has to offer and your time and knowledge was greatly appreciated. I hope to have the chance to speak with you again someday.

Asante sana
!

Kama ninavyosema mara kwa mara, blogu yangu hii ni mahali ambapo nahifadhi mambo yangu, kama vile mawazo, hisia na kumbukumbu. Nafurahi nimeandika hayo niliyoandika, muhtasari wa mafanikio niliyoyapa wiki hii inayoisha. Ni mafanikio yanayougusa moyo wangu na yenye maana kwangu kuliko fedha.

Monday, February 23, 2015

Mihadhara ya Mankato ni Kesho

Siku zinakwenda kasi. Naona kama ndoto, kwamba safari yangu ya kwenda Chuo cha South Central, mjini Mankato, kutoa mihadhara ni kesho asubuhi.

Ninangojea kwa hamu kutekeleza majukumu yaliyoko mbele yangu, ambayo ni kwanza kuongea na wanafunzi wanaojiandaa kwa safari ya Afrika Kusini kimasomo, na pili ni kutoa mhadhara kwa jumuia ya chuo ambao mada yake itakuwa "Writing About Americans."

Maongezi yote hayo yatahusu masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake ulimwenguni. Wanafunzi wanaokwenda Afrika Kusini wanajiandaa kuishi na kushughulika na wa-Afrika, katika utamaduni ambao ni tofauti na ule wa Marekani. Utaratibu huu wa maandalizi, ambao umeshakuwa jambo la kawaida hapa Marekani, ingekuwa bora ufuatwe na wengine, kama nilivyowahi kuwaasa wa-Tanzania wenzangu.

Katika maandalizi hayo, hao wanafunzi wanasoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kitabu ambacho, japo kidogo, kinawagusa watu, tangu nilipokichapisha, tarehe 5 Februari, 2005. Namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kukiandika kama nilivyoandika, hadi kimekuwa msingi wa mialiko ya kwenda kuongelea yaliyomo na yatokanayo.

Katika mhadhara wa "Writing About Americans," ninapangia kuelezea mchakato wa kuandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kuanzia chimbuko la wazo la kukiandika, mchakato wa kukiandika, mambo muhimu niliyojifunza katika kuandika huku, hadi jinsi kitabu kilivyopokelewa na jamii, hasa wa-Marekani, ambao ndio wanaoongoza katika usomaji wake.

Jambo moja kubwa nililojifunza katika kutafakari na kuandika ni kuheshimu tamaduni, pamoja na tofauti zake. Shaaban Robert angeishi miaka mingi zaidi ya ile aliyoishi, angetufundisha mengi kuhusu suala hilo.

Panapo majaliwa, nikikamilisha ziara ya kesho, nitaandika taarifa katika hii blogu yangu.

Sunday, January 25, 2015

Mipango ya Ziara Yangu Mankato Inaendelea

Kama nilivyoandika katika blogu hii, nitakwenda kuongea na wanafunzi wa chuo cha South Central mjini Mankato. Mipango ya ziara hii, ambayo itafanyika tarehe 24 Februari, inaendelea vizuri.

Mwenyeji wangu, mwalimu Rebecca Fjelland Davis, amenieleza kuwa shughuli ya kwanza nitakayofanya siku hiyo ni kuongea na wanafunzi katika darasa lake, kuanzia saa nne hadi saa tano na dakika hamsini asubuhi. Hao ni wanafunzi wanaojiandaa kwa safari ya kimasomo Afrika Kusini. Kama sehemu ya maandalizi hayo, wanasoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na maongezi yangu nao yatahusu yale niliyoandika kitabuni.

Baada ya darasa hilo, kuanzia yapata saa sita, nitatoa mhadhara kwa wanachuo na wana jamii. Mwalimu Fjelland Davis ameniarifu kuwa duka la vitabu la hapo chuoni litakuwa limeandaa nakala za kitabu changu, kwa ajili ya kuuza. Kama ilivyo desturi hapa Marekani, nategemea kuwa baada ya mazungumzo nitasaini nakala za vitabu.

Hii sio mara yangu ya kwanza kufanya shughuli mjini Mankato. Nimewahi kwenda kutoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Mankato kwa wanachuo waliokuwa wanajiandaa kwenda Afrika Kusini. Nilialikwa na Profesa Scott Fee, ambaye ni muasisi na mratibu wa mpango wa ushirikiano baina ya chuo kikuu cha Mankato na chuo kiitwacho Eden Campus cha Afrika Kusini. Nakumbuka ukumbi ulivyojaa watu siku hiyo, nami kwa kutekeleza ombi la Profesa Fee, niliwasilisha nakala yapata 40 za Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nimewahi pia kushiriki maonesho ya Deep Valley Book Festival, na mengine yaliyofanyika katika uwanja wa maonesho ya magari, ambao jina lake nimesahau. Ningekuwa na blogu miaka ile, ningekuwa nimeandika taarifa. Siku nyingine nilialikwa Mankato na taasisi inayoshughulika na huduma kwa jamii, nikaongea na wahamiaji na wakimbizi kutoka nchi mbali mbali, kama vile Somalia, Ethiopia, na Sudani. Mazungumzo hayo yaliripotiwa katika gazeti la Mankato Free Press.

Nikirudi kwenye mwaliko wa tarehe 24 Februari, napenda kusema kuwa Mwalimu Fjelland Davis na Profesa Scott Fee wanashirikiana katika mpango wa kupeleka wanafunzi Afrika Kusini. Wote wawili walihusika katika mhadhara niliotoa kwa wanafunzi wao ambao taarifa yake iliandikwa hapa na hapa.

Wednesday, December 17, 2014

Mwaliko Mwingine

Leo nimepata mwaliko mwingine wa kwenda kuzungumza na wanachuo wa chuo cha South Central ambao wanajiandaa kwa safari ya masomo Afrika Kusini. Mwaliko umetoka kwa mwalimu wao, Becky Djelland Davis. Hii ni mara pili yeye kunialika. Mara ya kwanza ilikuwa ni mwaka jana, naye baadaye aliandika kuhusu mazungumzo yale katika blogu yake.

Nami nimeguswa kwa namna alivyoniandikia leo:

I will be taking students to South Africa again in May. This coming semester, we will again be reading your book Africans and Americans. I hope that perhaps you can talk with my students again? They loved you last time!

Huu ni mwaliko wa tatu kwa siku za hivi karibuni, na yote inangojea utekelezaji katika miezi michache ijayo. Wa kwanza niliuelezea hapa, na wa pili hapa. Mialiko hii ninayopata sio jambo jepesi au la mteremko. Inahitaji tafakari katika kujiandaa ili nitoe mawazo na mitazamo ya kiwango kinachokidhi mahitaji ya hao wanaonialika, na bora zaidi ni kufanya vizuri kuliko wanavyotegemea.

Hiyo inawezekana kutokana na juhudi ya kutafiti na kutafakari mambo kwa kina na upeo mpana zaidi ya yale yaliyomo katika kitabu changu, ambacho ndicho kinachochea hii mialiko. Sijioni kama ni mtaalam, bali mtafutaji wa elimu.

Kwa kuhitimisha, sherti nikiri kuwa ninafurahi kuona kuwa watu walionialika kabla wanaendelea kufanya hivyo, nami siwezi kuwaangusha. Hii ndio habari moja muhimu ya leo, ambayo nimeona niiwekee kumbukumbu katika blogu yangu hii.

Sunday, November 16, 2014

Mwandishi Unapoitwa Kuongelea Kitabu Chako

Siku hizi, mara kwa mara, nawazia jukumu linaloningoja, la kwenda mjini Zumbrota, Minnesota, kutoa mhadhara. Mada ni "Incorporating Immigrants into our Culture and Worship," kama nilivyoeleza katika blogu hii. Mwaliko wa kutoa mhadhara huu umetokana na kitabu nilichoandika, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Sikualikwa nikaongelee kitabu hiki, lakini kwa hali yoyote, baadhi ya yaliyomo kitabuni yatajitokeza katika mhadhara na katika kipindi cha majibu na masuali. Napenda kusema machache kuhusu jukumu la kutoa mhadhara kuhusu kitabu ulichoandika.

Mara nyingi, hutokea kwamba watu utakaozungumza nao wanakuwa wameshakisoma kitabu. Ni lazima utafakari kabla kwamba utaongelea nini, na jambo hilo hutegemea aina ya kitabu.

Kama ni riwaya, watu hutegemea utawaeleza mambo kama vile nini kilikuwa chanzo cha wewe kuandika, yaani nini kilichokufanya uandike, njia uliyopitia katika kuandika, maandishi au waandishi waliokuathiri, matatizo uliyokumbana nayo, na mambo uliyojifunza.

Lakini, watu hutegemea pia, au labda zaidi, kuwa utasoma angalau kurasa kadhaa za riwaya yako, ili wasikie sauti yako na sauti ya wahusika katika hadithi yako kwa mujibu wako wewe kama mtunzi.

Hapa kushoto tunamwona mwandishi Nuruddin Farah wa Somalia, alipokuwa anaongelea riwaya yake mpya ya Crossbones, chuoni Carleton. Anaonekana akisoma kurasa kadhaa.

Wasikilizaji huvutiwa kumsikia mwandishi namna hiyo, kwani usomaji wake ni aina ya tafsiri sio tu ya kile alichoandika, bali kilichokuwa mawazoni mwake wakati anaandika. Watu huamini kuwa usomaji wa mwandishi una ukweli na uhalisi ambao msomaji mwingine hawezi kuufikia.


Hiyo ndiyo halisi inavyokuwa, iwapo kitabu ni riwaya au mashairi. Sauti na usomaji wa mwandishi vina mvuto huo niliouelezea, ingawaje kwa kifupi.

Lakini kuna pia vitabu vya aina tofauti, kama hiki changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Unapokuwa umealikwa kuongelea kitabu cha aina hiyo, ni lazima utafakari vizuri suala zima.

Iwapo watu hao wameshakisoma, nadhani jukumu lako sio kuwasomea kurasa za kitabu, bali ni kuongelea mambo yatokanayo na yale uliyoandika. Jukumu lako ni kufafanua baadhi ya yale uliyoandika, ambayo unaamini yanakidhi mahitaji ya watu watu wale, kufuatana na mwaliko wao.

Pengine, inawezekana uzungumze bila kufungua kitabu, ingawa unacho mbele yako. Kwa mfano, kwenye hii mada ya mhadhara wangu wa Zumbrota, siamini kama nitahitaji kuwasomea kurasa zozote kutoka kitabuni. Badala yake, ikibidi, nitajumlisha mafundisho yatokanayo, yenye kukidhi mategemeo ya mada.

Aina hii ya mhadhara nimeshatoa mara nyingi. Kwa mfano, hapa kushoto ninaonekana nikiongea na wanachuo waliokuwa wanajiandaa kwenda Afrika Kusini kwenye ziara ya kimasomo. Walishasoma kitabu changu, na profesa wao aliniita kuja kuongelea masuala ya aina niliyozungumzia kitabuni, kama sehemu ya maandilizi ya safari ya wanafunzi wale. Kwa vile wanafunzi walikuwa wameshasoma kitabu, mhadhara huu ulitawaliwa zaidi na masuali na majibu. Profesa wao aliandika kuhusu mhadhara wangu katika blogu yake.

Kwa ujumla, fursa hizi hunifurahisha, sio tu kwa sababu nakutana na wasomaji na wadau wengine ana kwa ana, bali pia napata wasaa wa kujipima ni kiasi gani naifahamu mada husika na vipengele vyake.

Wednesday, May 8, 2013

Nimekutana na Mjukuu wa Mahatma Gandhi

Jioni hii tumepata bahati ya kuwa na Ela Gandhi, mjukuu wa Mahatma Gandhi. Alikuja kutoa mhadhara chuoni Carleton hapa mjini petu. Mada ya mhadhara wake ilikuwa, "The Challenges Facing Post-Apartheid South Africa."

Mama Ela Gandhi, ambaye alizaliwa Durban, ni mwanaharakati wa masuala ya amani na maendeleo. Aliongelea historia ya Mahatma Gandhi na mafundisho yake kuhusu namna ya kukabiliana na matatizo ya hujuma dhidi ya haki. Alisisitiza kuwa njia aliyofundisha Gandhi ya kutotumia mabavu na vita inatujengea mtandao wa urafiki na kuheshimiana, tofauti na vita, ambayo matunda yake ni kujenga mtandao wa maadui.

Alielezea umuhimu wa mafundisho ya watu kama Mahatma Gandhi, Albert Lutuli, Martin Luther King, na Nelson Mandela. Kisha alielezea changamoto zinazoikabili Afrika Kusini leo, kwani mategemeo ya wengi wakati wa kupambana na mfumo wa ukaburu hayajapatiwa ufumbuzi.

Nilikwenda kwenye mhadhara huu na baadhi ya wanafunzi wangu, ambao muhula huu tunasoma fasihi ya Afrika Kusini. Tumefurahi kumsikia Mama Ela Gandhi akiongelea masuala ambayo tumekuwa tukiyajadili darasani. Kwa mfano, katika kipindi cha leo, wakati tunasoma hadithi ya Nadine Gordimer iitwayo "A Chip of Glass Ruby" katika kuelezea dhamira mbali mbali zilizomo, nilikuwa nimewaelezea dhana ya  "Group Areas" inayotajwa katika hadithi hiyo. Kwa bahati nzuri, Mama Ela Gandhi katika mhadhara wake alifafanua dhana hiyo ya "Group Areas" vizuri kabisa.

Baada ya mhadhara wake, watu tulipata fursa ya kupiga naye picha. Nilipomwambia kuwa mimi ni m-Tanzania, alifurahi akakumbushia historia njema ya mahusiano baina ya nchi yake na Tanzania, akataja kazi nzuri iliyofanywa na Julius Nyerere. Nami niliongelea jinsi tulivyopata bahati Tanzania ya kujumuika na wakimbizi kutoka Afrika Kusini, baadhi wakiwa wahadhiri wetu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na wengine wakiwa viongozi wa vyama vya ukombozi ambao walifika kutoa hotuba. Kwa mfano, niliwataja Albie Sachs na Gora Ebrahim.

Tuesday, November 13, 2012

Kitabu cha Mazungumzo ya Nelson Mandela

Leo nimenunua kitabu cha Nelson Mandela, Conversations with Myself. Ingawa sijui nitakisoma lini, kutokana na utitiri wa vitabu vyangu, nimekinunua kutokana na umaarufu wa Mandela na kutokana na ukweli kwamba kumbukumbu zake na mawaidha yake ni hazina kubwa.

Idadi ya vitabu vinavyosimulia na kuchambua mchango wa Mandela vinaendelea kuchapishwa. Yeye mwenyewe pia amejitahidi kuandika. Kwa mfano, tulipokuwa vijana, tulikifahamu kitabu chake kiitwacho  Long Walk to Freedom. Haikuwa rahisi mtu usikijue kitabu hiki, kwani kilichapishwa katika mfululizo maarufu wa vitabu vya shirika la Heinemann, ambalo tulilifahamu sana kutokana na vitabu vyake ambavyo tulikuwa tunavisoma.

Miaka ya karibuni, Mandela amejikakamua akaandaa kitabu cha hadithi, Nelson Mandela's Favorite African Folktales. Ni mkusanyiko wa hadithi za asili za ki-Afrika.

Kwa kuangalia juu juu, nimeona kuwa hiki kitabu cha Conversations with Myself ni mkusanyiko wa barua mbali mbali za Mandela na maandishi mengine ambayo yanatufunulia picha ya Mandela sio tu kama mwanasiasa na mpigania ukombozi maarufu bali kama binadamu. Ni kitabu kikubwa, kurasa 454. Nitakuwa nakisoma kidogo kidogo. Isipokuwa ni kimoja kati ya vitabu vya pekee kabisa katika maktaba yangu.


Tuesday, November 30, 2010

Asante, Joseph Mbele

Jioni hii, katika kuzurura mtandaoni, mitaa ya Google, nimekumbana na makala kwenye blogu fulani, ambayo inanitaja. Soma hapa.

Sikuwa nimeiona makala hii ambayo inataja ziara niliyofanya College of St. Benedict/St. John's University mwaka jana. Nilialikwa kutoa mihadhara. Katika darasa la Profesa Lisa Ohm, niliongelea hadithi na utamaduni, kufuatia maelezo yaliyomo katika kitabu cha Matengo Folktales, ambacho walikuwa wanakitumia. Soma hapa.

Mhadhara wa pili niliutoa kwa wanafunzi na walimu waliokuwa wanajiandaa kwenda Tanzania na Afrika ya Kusini, lakini ulihudhuriwa na wengi wengine. Lengo lilikuwa kuwaarifu kuhusu tofauti za msingi baina ya tamaduni wa mw-Afrika na ule wa m-Marekani, kama nilivyoeleza katika kitabu cha Africans and Americans.

Nakumbuka jinsi ukumbi ulivyojaa watu kwenye mhadhara huu, na kwenye meza nyuma ya umati walikuwa wameweka nakala nyingi za vitabu hivi viwili, kama ilivyo desturi hapa Marekani, wanapowaita waandishi kuzungumzia vitabu na uandishi. Soma hapa.

Nimefurahi kuona kuwa mazungumzo yangu kwa hao wa-Marekani yameelezwa kama ilivyoelezwa na mwandishi huyu. Nimefurahi jinsi anavyokiri kuwa yale niliyowaambia ndiyo aliyoyakuta Afrika Kusini. Huwa nakutana na wa-Marekani wengi wanaosema hivyo hivyo, wanaporudi kutoka Afrika. Nami nafanya juhudi nijielimishe zaidi kuhusu tofauti za tamaduni hizi, ili niweze kuboresha mafunzo na mawaidha ninayotoa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...