Showing posts with label wakimbizi. Show all posts
Showing posts with label wakimbizi. Show all posts

Thursday, November 14, 2019

Kijana Msomali Amekipenda Kitabu Hiki

Jana, nilikuwa posta hapa chuoni nikipata huduma. Ghafla nikasikia kwa nyuma ninaitwa, "Professor Mbele!" Nilipinduka nikamwona kijana mmoja, mwanafunzi wetu mSomali ananisogea. Aliniambia amesoma kitabu changu, akimaanisha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Nilifurahi, ila sikujua nimwambie nini, ila aliongezea kuwa alitamani kipatikane kama "audio book" ili mama yake aweze kusikiliza. Niliguswa sana, kwa sababu ninaelewa hali ya waSomali hapa Minnesota na Marekani kwa ujumla.

Wako wengi sana, wakimbizi au wahamiaji kutoka nchini kwao. Jimbo hili la Minnesota lina idadi kubwa ya waSomali kuliko sehemu nyingine duniani ukiachilia mbali Somalia yenyewe.

Ninafahamu pia kuwa waSomali hawakuwa na jadi ya maandishi. Utamaduni wao ni wa masilimuzi. Walipata mwafaka wa namna ya kuandika lugha yao mwaka 1972. Watu wazima wengi hawajui kuandika na kusoma, na wazee ndio kabisa.

Wote hao wako hapa Marekani, ambapo utamaduni ni wa maandishi. Ninafahamu changamoto zinazowakabili, kwani nina uzoefu katika masuala yao, ikiwemo fasihi simulizi na elimu. Kijana huyu alivyoniambia kuhusu mama yake, niliguswa sana. Nimeshampelekea ujumbe rafiki yangu mSomali kumwelezea suala hilo. Huyu tulishaongelea kutafsiri kitabu changu kwa kiSomali. Nimemwambia kuwa kutokana na kauli ya huyu kijana ya kutaka mama yake asome kitabu hiki, inabidi tukamilishe tafsiri halafu irekodiwe kama "audio book." Itachukua muda, lakini hii si hoja.

Sunday, August 27, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nilienda Mall of America. Nilipitia Apple Valley katika duka la half Price Books. Kama kawaida, niliangalia kwanza sehemu vinapowekwa vitabu vya Ernest Hemingway. Hapo nilinunua The Dangerous Summer, kitabu ambacho nilikifahamu kwa miaka. Nilijua kwamba kinahusu utamaduni wa Hispania wa "bull fighting." Nilijua pia kuwa hiki ni moja ya vitabu vya Hemingway ambamo alielezea utamaduni huu kwa umakini na ufahamu wa hali ya juu.

Kitu kimoja kilichonifanya ninunue kitabu hiki leo ni utangulizi mrefu ulioandikwa na James A. Mitchener, mwandishi ambaye nimemfahamu kwa jina kwa miaka kadhaa na nimeshaona baadhi ya vitabu vyake, ila sijawahi kuvisoma. Nilivyoanza kusoma utangulizi wake katika The Dangerous Summer, nilivutiwa sana na uandishi wake. Vile vile, nilitaka kujua anaeleza nini kuhusu kitabu hiki. Utangulizi wake umenipa hamu ya kusoma vitabu vyake.

Baada ya hapo, nilielekea vinapowekwa vitabu vya bei ndogo zaidi. Niliangalia kijuu juu vitabu vilivyojazana hapo, na ghafla nikaona kitabu kiitwacho Bamboo Among the Oaks, kilichohaririwa na Mai Neng Moua. Nilifurahi kukiona, kwani mwandishi alikuwa mwanafunzi hapa chuoni St. Olaf miaka ya tisini na kitu. Nilikuwa nimesikia habari za kitabu hiki, kwamba ni mkusanyo wa maandishi ya watu wa taifa la Hmong waliohamia Marekani.

Taifa la Hmong asili yake ni kusini mwa China na nchi za Cambodia, Laos, Thailand, na Vietnam. Wakati wa vita baina ya Marekani na Vietnam, jamii ya Hmong ilishirikiana na shirika la kijasusi la CIA la Marekani. Kwa mujibu wa mhariri wa Bamboo Among the Oaks, walifanya hivyo "to defend their own territory and way of life and to rescue American pilots downed along the Ho Chi Minh Trail."

Kwetu sisi wa-Tanzania, kutokana na mwelekeo wetu wa kishoshalisti, tulishikamana na nchi zilizokuwa na mwelekeo huo. Tuliunga mkono Vietnam ya Kaskazini chini ya kiongozi wao Ho Chi Minh. Hatukupendeza na hao waliosaidiana na Marekani, nchi ambayo tuliiona ya kibeberu. Kwa mtazamo huo, suala la jamii ya Hmong ni tata kwetu.

Marekani iliposhindwa, washindi, yaani Pathet Lao, walianza kulipiza kisasi dhidi ya jamii ya Hmong. Hii ndio sababu ya wao kukimbilia nchi zingine, kuanzia Thailand, na kisha nchi za mbali, kama vile Argentina, Australia, Canada, Ufaransa, Ujerumani, na Marekani. Katika jimbo la Minnesota, ambapo ninaishi, watu wa jamii ya Hmong ni wengi. Vijana wao wengi tunawafundisha chuoni St. Olaf.

Nimesikia mambo kadhaa kuhusu jamii hiyo nchini Marekani, hasa kuhusiana na tofauti baina ya utamaduni wao na ule wa Marekani. Kuna changamoto inayotokana na nia ya wazee kudumisha utamaduni wa jadi mwelekeo wa vijana wa kupendelea utamaduni wa Marekani.

Kwa mategemeo kwamba kitabu hiki, ambacho ni mkusanyo wa mashairi, hadithi, tamthilia, na insha, kitanipa mwanga zaidi kuhusu jamii hii, niliamua bila kusita kukinunua. Nilivutiwa na wazo kuwa kitanipa upeo wenye uhusiano na yale niliyoandika katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Wednesday, May 8, 2013

Nimekutana na Mjukuu wa Mahatma Gandhi

Jioni hii tumepata bahati ya kuwa na Ela Gandhi, mjukuu wa Mahatma Gandhi. Alikuja kutoa mhadhara chuoni Carleton hapa mjini petu. Mada ya mhadhara wake ilikuwa, "The Challenges Facing Post-Apartheid South Africa."

Mama Ela Gandhi, ambaye alizaliwa Durban, ni mwanaharakati wa masuala ya amani na maendeleo. Aliongelea historia ya Mahatma Gandhi na mafundisho yake kuhusu namna ya kukabiliana na matatizo ya hujuma dhidi ya haki. Alisisitiza kuwa njia aliyofundisha Gandhi ya kutotumia mabavu na vita inatujengea mtandao wa urafiki na kuheshimiana, tofauti na vita, ambayo matunda yake ni kujenga mtandao wa maadui.

Alielezea umuhimu wa mafundisho ya watu kama Mahatma Gandhi, Albert Lutuli, Martin Luther King, na Nelson Mandela. Kisha alielezea changamoto zinazoikabili Afrika Kusini leo, kwani mategemeo ya wengi wakati wa kupambana na mfumo wa ukaburu hayajapatiwa ufumbuzi.

Nilikwenda kwenye mhadhara huu na baadhi ya wanafunzi wangu, ambao muhula huu tunasoma fasihi ya Afrika Kusini. Tumefurahi kumsikia Mama Ela Gandhi akiongelea masuala ambayo tumekuwa tukiyajadili darasani. Kwa mfano, katika kipindi cha leo, wakati tunasoma hadithi ya Nadine Gordimer iitwayo "A Chip of Glass Ruby" katika kuelezea dhamira mbali mbali zilizomo, nilikuwa nimewaelezea dhana ya  "Group Areas" inayotajwa katika hadithi hiyo. Kwa bahati nzuri, Mama Ela Gandhi katika mhadhara wake alifafanua dhana hiyo ya "Group Areas" vizuri kabisa.

Baada ya mhadhara wake, watu tulipata fursa ya kupiga naye picha. Nilipomwambia kuwa mimi ni m-Tanzania, alifurahi akakumbushia historia njema ya mahusiano baina ya nchi yake na Tanzania, akataja kazi nzuri iliyofanywa na Julius Nyerere. Nami niliongelea jinsi tulivyopata bahati Tanzania ya kujumuika na wakimbizi kutoka Afrika Kusini, baadhi wakiwa wahadhiri wetu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na wengine wakiwa viongozi wa vyama vya ukombozi ambao walifika kutoa hotuba. Kwa mfano, niliwataja Albie Sachs na Gora Ebrahim.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...