Wednesday, May 8, 2013

Nimekutana na Mjukuu wa Mahatma Gandhi

Jioni hii tumepata bahati ya kuwa na Ela Gandhi, mjukuu wa Mahatma Gandhi. Alikuja kutoa mhadhara chuoni Carleton hapa mjini petu. Mada ya mhadhara wake ilikuwa, "The Challenges Facing Post-Apartheid South Africa."

Mama Ela Gandhi, ambaye alizaliwa Durban, ni mwanaharakati wa masuala ya amani na maendeleo. Aliongelea historia ya Mahatma Gandhi na mafundisho yake kuhusu namna ya kukabiliana na matatizo ya hujuma dhidi ya haki. Alisisitiza kuwa njia aliyofundisha Gandhi ya kutotumia mabavu na vita inatujengea mtandao wa urafiki na kuheshimiana, tofauti na vita, ambayo matunda yake ni kujenga mtandao wa maadui.

Alielezea umuhimu wa mafundisho ya watu kama Mahatma Gandhi, Albert Lutuli, Martin Luther King, na Nelson Mandela. Kisha alielezea changamoto zinazoikabili Afrika Kusini leo, kwani mategemeo ya wengi wakati wa kupambana na mfumo wa ukaburu hayajapatiwa ufumbuzi.

Nilikwenda kwenye mhadhara huu na baadhi ya wanafunzi wangu, ambao muhula huu tunasoma fasihi ya Afrika Kusini. Tumefurahi kumsikia Mama Ela Gandhi akiongelea masuala ambayo tumekuwa tukiyajadili darasani. Kwa mfano, katika kipindi cha leo, wakati tunasoma hadithi ya Nadine Gordimer iitwayo "A Chip of Glass Ruby" katika kuelezea dhamira mbali mbali zilizomo, nilikuwa nimewaelezea dhana ya  "Group Areas" inayotajwa katika hadithi hiyo. Kwa bahati nzuri, Mama Ela Gandhi katika mhadhara wake alifafanua dhana hiyo ya "Group Areas" vizuri kabisa.

Baada ya mhadhara wake, watu tulipata fursa ya kupiga naye picha. Nilipomwambia kuwa mimi ni m-Tanzania, alifurahi akakumbushia historia njema ya mahusiano baina ya nchi yake na Tanzania, akataja kazi nzuri iliyofanywa na Julius Nyerere. Nami niliongelea jinsi tulivyopata bahati Tanzania ya kujumuika na wakimbizi kutoka Afrika Kusini, baadhi wakiwa wahadhiri wetu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na wengine wakiwa viongozi wa vyama vya ukombozi ambao walifika kutoa hotuba. Kwa mfano, niliwataja Albie Sachs na Gora Ebrahim.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...