Showing posts with label Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison. Show all posts
Showing posts with label Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison. Show all posts

Thursday, October 19, 2017

"Men Made Out of Words" ( Wallace Stevens)

Wallace Stevens ni mmoja wa washairi maarufu wa Marekani. Mara ya kwanza kupata fursa ya kuyasoma mashairi yake ni nilipokuwa ninasomea shahada ya uzamifu katika huo kikuu cha Wisconsin-Madison,1980-86. Nilichukua kozi kadhaa katika idara ya ki-Ingereza, mojawapo ikiwa "Poetry." Alitufundisha profesa John Brenkman.

Profesa Brenkman alikuwa na mtindo wa kufundisha ambao ulilifanya somo la "Poetry" livutie. Kwa uzoefu wangu wa kabla ya hapo, katika kusoma Tanzania, ushairi wa ki-Ingereza ndilo lilikuwa somo gumu kuliko mengine. Nilidokeza jambo hilo katika kijitabu changu cha Notes on Okot p Bitek's Song of Lawino.

Tangu nilipofundishwa na Profesa Brenkman, jina la Wallace Stevens limekuwa linanivutia, na daima niko tayari kusoma mashairi yake. Huu ni ushahidi wa jambo ambalo linafahamika vizuri, yaani namna mwalimu bora anavyoweza kumwathiri mwanafunzi. Jana nimeangalia kitabu changu cha mashairi, The Voice That is Great Within Us, na shairi moja lililonivutia ni "Men Made Out of Words," la Wallace Stevens. Ni shairi ambalo limeandikwa kwa uchache wa maneno na tamathali za usemi, na falsafa yake inachangamsha bongo.

MEN MADE OUT OF WORDS (Wallace Stevens)

What should we be without the sexual myth,
The human revery or poem of death?

Castratos of moon-mash--Life consists
Of propositions about life. The human

Revery is a solitude in which
We compose these propositions, torn by dreams,

By the terrible incantations of defeats
And by the fear that defeats and dreams are one.

The whole race is a poet that writes down
The eccentric propositions of its fate.


Wednesday, September 6, 2017

Muhula wa Masomo Unaanza

Wiki hii hapa chuoni St. Olaf, tunaanza muhula mpya wa masomo. Nitafundisha madarasa matatu. Mawili ni ya "First Year Writing," na moja ni "Post-colonial Literature." Katika "First Year Writing," tunafundisha uandishi bora wa ki-Ingereza.

Kozi ninayotaka kuongelea hapa  ni "Post-colonial Literature." Niliajiriwa hapa chuoni St. Olaf kuanzisha kozi hiyo, na nilianza kufundisha mwaka 1991. Ni kozi inayohusu fasihi kutoka nchi zilizokuwa katika himaya ya u-Ingereza wakati wa ukoloni ila zilikuja kuwa huru.

Ninapofundisha kozi hii, huwa ninaamua waandishi wepi kutoka nchi zipi nifundishe. Kwa muhula huu, niliamua kufundisha fasihi kutoka Afrika Kusini. Nilichagua waandishi wawili: Alex la Guma na Nadine Gordimer. Wote ni waandishi wa hadithi fupi na riwaya.

Nadhani tangu nilipokuwa mwanafunzi Mkwawa High School, nilisoma hadithi za Alex la Guma katika kitabu cha hadithi fupi kiitwacho Quartet. Baadaye, nilipokuwa mwanafunzi katika idara ya Literature, chuo kikuu cha Dar es Salaam, Alex la Guma alikuja kutoka London akatufundisha kwa siku kadhaa. Alialikwa na mkuu wa idara, mwalimu Grant Kamenju wa Kenya.

Nilifahamu kuwa Alex la Guma alikuja kuwa mwakilishi Uingereza wa chama cha ukombozi cha African National Congress cha Afrika Kusini, (ANC), kisha akawa mwakilishi wa ANC nchini Cuba. Alipofariki, nchini Cuba, nilikuwa ninasoma katika Chuo Kikuu cha Wisconsin Madison.

Nadine Gordimer ni mzungu aliyejihusisha na ANC. Alikuwa mpinzani wa utawala wa makaburu. Baada ya kuja Marekani kufundisha, nimebahatika kumwona Nadine Gordimer kwenye mkutano fulani wa kitaaluma. Sikumbuki ulikuwa ni mwaka gani. Nimefundisha hadithi zake fupi zilizokusanywa katika kitabu Six Feet of the Country, na riwaya zake, The Conservationist, The Pickup, na July's People.

Kufundisha juu ya waandishi hao wawili ni fursa ya kutafakari historia na siasa, hasa ukaburu na harakati za ukombozi katika Afrika Kusini. Yote hayo yamefungamana na fasihi, hasa katika karne ya ishirini, ambayo ndiyo kozi yangu itashughulikia. Tutafakari mitazamo ya waandishi hao wawili kuhusu siasa, mahusiano ya jamii, utamaduni, na itikadi katika Afrika Kusini. Tutaangalia athari za fasihi ya ulimwengu katika maandishi ya waandishi hao wawili na tutatambua mchango wa waandishi hao katika fasihi ya Afrika na ulimwengu.

Saturday, February 11, 2017

Ninamwazia Mwandishi Alexander Pushkin

Kwa wiki yapata mbili, nimekuwa nikimwazia sana Alexander Pushkin, mwandishi maarufu wa u-Rusi. Nimefahamu tangu ujana wangu kuwa wa-Rusi wanamwenzi kama baba wa fasihi ya u-Rusi. Miaka ya baadaye, nilikuja kufahamu kuwa Pushkin alikuwa na asili ya Afrika, na kwamba hata katika baadhi ya maandishi yake aliongelea suala hilo.

Nilisoma makala za profesa moja wa Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, nikafahamu zaidi suala hilo. Katika kufuatilia zaidi, niliguswa na mengi, hasa maelezo juu ya kipaji cha Pushkin cha ajabu katika matumizi ya lugha ya ki-Rusi na ubunifu wake, na pia jinsi alivyokufa. Aliuawa katika ugomvi akiwa na umri wa miaka 37 tu.


Siku kadhaa zilizopita, nilitoa mhadhara katika darasa la Nu Skool, kuhusu umuhimu wa Afrika na wa-Afrika katika historia ya ulimwengu. Kati ya watu maarufu wenye asili ya Afrika ambao niliwataja kwa mchango wao ni Antar bin Shaddad wa Saudi Arabia na Pushkin. Antar bin Shaddad ni mshairi aliyeishi kabla ya Mtume Muhammad, na ambaye tungo zake zinakumbukwa kama hazina isiyo kifani katika lugha ya ki-Arabu. Pushkin ni hivyo hivyo; wa-Rusi wanakiri kuwa umahiri wake katika kuimudu lugha yao hauna mfano.

Kutokana na hayo nimekuwa na hamu ya kumsoma Pushkin, nikakumbuka kuwa nilishanunua kitabu chake maarufu, Eugene Onegin, ambayo ni hadithi iliyoandikwa kishairi. Ninajiandaa kuisoma.

Saturday, February 21, 2015

Lugha na Mwamko wa Elimu Tanzania

Katika kuendelea kutekeleza ombi nililopata kutoka kwa mdau wa blogu hii, juu ya sera ya lugha ya kufundishia nchini Tanzania, napenda kuongelea suala la lugha na mwamko wa elimu. Huu ni mwendelezo wa ujumbe nilioandika katika makala yangu, "Tatizo si Lugha ya Kufundishia, ni Uzembe." ambayo niliichapisha katika blogu hii.

Kwanza, nasisitiza mtazamo wangu kuwa tatizo si lugha ya kufundishia, bali uzembe.

Mimi kama mwelimishaji, nimeshuhudia tatizo hili lilivyo katika jamii ya wa-Tanzania. Nitaanza kwa kutoa mfano. Mwaka 1980, nilipokuwa mhadhiri katika idara ya "Literature" ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, nilifika kusomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, Marekani.

Niliondoka Tanzania wakati jamii ikiwa bado inazingatia mafundisho ya Mwalimu Nyerere kuhusu elimu. Kwa miaka sita niliyokuwa masomoni, nilifanya bidii katika masomo na pia nilinunua vitabu vingi sana, nikijua kuwa ndio nyenzo itakayonifanya nifundishe kwa kiwango cha juu kabisa pindi nitakaporejea tena Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Nilipohitimu masomo, nilirejea nchini nikiwa na shehena yangu ya vitabu. Badala ya kuniulizia kuhusu masomo niliyosomea au elimu niliyoipata, watu waliniuliza kama nimeleta "pick-up." Walinishangaa kwa kuleta vitabu badala ya gari. Haikutegemewa kuwa mtu ukae "majuu" miaka yote ile halafu usirudi na gari.

Hapo nilitambua wazi kabisa kuwa mwamko wa elimu, ambao alikuwa ameuchochea Mwalimu Nyerere, ulikuwa umedidimia. Niliendelea kufundisha katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam huku nikishuhudia mwamko wa elimu ukiendelea kudidimia nchini.

Jadi ya kuthamini mali na vitu badala ya elimu iliendelea kushamiri. Wasomi wakipata fursa ya kwenda nje, inayojulikana kama "sabbatical," walitegemea na walitegemewa kutumia fursa hiyo kujitafutia vitu, hasa magari. Mwenye kuleta gari au magari alionekana ndiye msomi bora. Ni tofauti kabisa na hapa Marekani, ambapo profesa unathaminiwa kwa ujuzi wako, hata kama unatembelea baiskeli au unapekua kwa miguu. Binafsi, kwa kuwa kipaumbele changu elimu na taaluma nimeridhika kufundisha hapa Marekani, tangu nilipoanza, mwaka 1991.

Tanzania, ilikuwa ni jambo la kawaida kwa walimu kushughulikia shughuli zao za kujipatia pesa hata kama walipaswa wawe darasani wakifundisha. Jambo hili limekuwa likitajwa na wanafunzi wetu wa ki-Marekani tunaowapeleka kusoma Tanzania, kwani katika vyuo vyao hapa Marekani, profesa hawezi kukosa kuingia darasani bila sababu ya maana kama vile kuumwa. Na akikosa kipindi, hufanya mpango wa kukifidia.

Katika jamii ya wa-Tanzania, nilishuhudia kushamiri utamaduni wa kutafuta vyeti kwa njia yoyote, badala ya kutafuta elimu. Nilishuhudia jinsi watu walivyokuwa tayari kutafuta hata vyeti feki. Hata baadhi ya wale wanaoitwa viongozi wamejipatia hivyo vyeti feki, kutoka  vyuo ambavyo havina hadhi itambulikanayo katika ulimwengu wa taaluma.

Kama ambavyo nimekuwa nikilalamika tena na tena katika blogu hii, utamaduni wa kununua na kusoma vitabu umekosekana katika jamii ya wa-Tanzania. Wazazi, ambao wangetegemewa kuwa wanunuaji wa kuaminika wa vitabu na wawe wanawasomea vitabu watoto wao, kama wafanyavyo wa-Marekani, hawafanyi hivyo.

Hao tunaowaita viongozi Tanzania, na wa-Tanzania wengine wengi, hutembelea nchi za nje. Sijui ni wangapi wanatumia fursa hii kununua vitabu na kurudi navyo Tanzania. Katika miji wanayopita na katika viwanja vya ndege, kuna maduka ya vitabu. Sijui ni wangapi wanapita katika maduka hayo na kununua vitabu. Nimewahi kusafiri mara kwa mara na wa-Tanzania, na nimeona kuwa zawadi wanazonunua ni vitu kama vipodozi, marashi, na mizinga ya vinywaji vikali. Wa-Tanzania hupenda zawadi za aina hiyo. Vitabu je? Jibu mwenyewe.

Sijui ni nyumba zipi katika Tanzania ambazo zina maktaba. Sijui ni nyumba ngapi ambazo zina vitabu angalau 50 au 100, kwa ajili ya watoto na wazazi. Kutegemea kuwa utamwona m-Tanzania amekaa sebuleni, bustanini, ufukweni, ndani ya basi au ndege, anasoma kitabu, ni kama kutegemea kumwona jogoo amevaa suruali.

Niliwahi kuhudhuria tamasha la vitabu Dar es Salaam, mwaka 2004. Watoto walikuwepo, na waalimu, lakini watu wazima walikuwa wachache sana. Hata hao wanaoitwa viongozi, wa ngazi yoyote, hawakuwepo. Watoto walifanya maonesho mbali mbali na waliimba nyimbo. Katika wimbo mmojawapo, waliwasihi wazazi wawe wananunua vitabu na kusoma pamoja na watoto wao majumbani. Wazazi wenyewe hawakuwepo kwenye tamasha. Lakini jioni, nilipokuwa naelekea nyumbani, niliwaona hao watu wazima wamekusanyika kwenye mabaa.

Katika hali hii, tatizo linalohitaji kushughulikiwa ni mwamko wa elimu. Bila mwamko wa elimu, hata lugha ya kufundishia ikibadilishwa mara ngapi, hata tukisema tutumie lugha zetu za ki-Nyaturu, ki-Nyasa, ki-Zaramo, na kadhalika, tusitegemee kuwa tutaleta mapinduzi yatakiwayo. Kinachohitajika ni mwamko wa elimu. Huu ndio msingi, ambao tumeuharibu.

Thursday, January 8, 2015

""Till I End My Song:" Tungo za Mwisho za Washairi Maarufu

Kila siku ninapokuwa chuoni St. Olaf, ambapo nafundisha, sikosi kupita katika duka la vitabu. Mbali ya vitabu vilivyomo dukani, wanaweka pia vitabu vingi kwenye meza na makabati nje ya duka. Hapo nje unaweza kuvipata vitabu kwa bei nafuu kuliko kuviagiza wewe mwenyewe sehemu nyingine.

Basi, siku moja, katika kuangalia angalia vitabu hapo nje, nilikiona kitabu ambacho rangi za jaladaa lake zilinivutia. Nilivutiwa zaidi nilipoona kimehaririwa na Harold Bloom, na kinauzwa kwa  dola 4.98, ambalo ni punguzo kubwa, kwani bei yake ya halisi ni dola 24.99. Hapo hapo niliamua kukinunua, ingawa nilikuwa na hela kidogo tu, kwani ilikuwa ni mara tu baada ya Krismasi, huku tungiingojea siku kuu ya Mwaka Mpya.

Harold Bloom ni bingwa mojawapo duniani katika masomo ya ki-Ingereza na fasihi yake, sio tu kwa upande wa uchambuzi wa maandishi bali pia upande wa nadharia ya fasihi. Ameandika au kuhariri vitabu vingi. Nilipokuwa nasomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu Cha Wisconsin-Madison, 1980-86, tulisoma baadhi ya maandishi ya Harold Bloom, sambamba na maandishi ya watalaam wengine, kama vile M.H. Abrams, Jacques Derrida, Edward Said, Wayne Booth, Michael Raffartere, Terry Eagleton, na Fredrick Jameson. Ninavyo baadhi ya vitabu vya wataalam hao, na nimehudhuria mihadhara ya Edward Said, Wayne Booth, na M.H. Abrams.

Nilivyoona hiki kitabu kipya, Till I End My Song, chenye jina la Harold Bloom, sikuweza kujizuia kukinunua. Nilivyoona kitabu kimeelezwa kama "A Gathering of Last Poems" nilipata shauku ya kukiangalia zaidi, hata kabla ya kukinunua. Nilihisi kuwa ni mkusanyiko wa mashairi ya waandishi maarufu, ambayo yalikuwa ni mashairi yao ya mwisho au ya mwisho mwisho kabla hawajafariki. Hapo dukuduku na shauku vikanielemea. Nilivutiwa, kwani sikuwahi kusikia kuhusu kitabu kilichojaribu kufanya hivyo katika lugha yoyote.

Dukuduku yangu ilikuwa kubwa: je, tungo za mwisho kabisa za washairi maarufu kama Shakespeare, Christopher Marlowe, Milton, Geradd Manley Hopkins, Wallace Stevens, na Robert Lowell, zilikuwaje? Walisema nini? Walituachia usia gani? Nilikuwa nimesoma mashairi mengi ya watunzi hao, lakini sikuwahi kuwazia dhana hii ya mkusanyiko wa mashairi yao ya "lala salama," kama wasemavyo wa-Swahili.

Harold Bloom anafafanua, katika sentensi za mwanzo kabisa za utangulizi wake, maana ya "last poems," dhana iliyomwongoza katika kuandaa kitabu hiki. Nanukuu:

There are three kinds of "last poems" in this anthology. Some literally are the final poems these women and men composed. Others were intended to mark the end, though the poet survived a while longer and continued to work. A third group consists of poems that seem to me an imaginative conclusion to a poetic career. With all three kinds I have made an aesthetic judgement: everything in this volume is here because of its artistic excellence.

Kwa jinsi kitabu hiki kilivyokusanya tungo za washairi mashuhuri sana, wa tangu zamani hadi leo, ni hazina kubwa kwa yeyote anayependa kuuelewa urithi wa uandishi katika lugha ya ki-Ingereza.

Wednesday, March 30, 2011

Maskani Yangu Madison, 1980-86

Wikiendi hii iliyopita, nilipokuwa Madison kwenye mkutano wa Peace Corps, nilitembelea sehemu kadhaa nilizozifahamu tangu wakati nasoma Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, 1980-86. Nilivutiwa kwa namna ya pekee na wazo la kutembelea maskani yangu miaka ile.

Niliingia Madison nikitokea Tanzania mwezi Agosti mwaka 1980. Sikumbuki tarehe. Lakini nilifikia mahali palipoitwa Union South, katika eneo la Chuo. Hapo nilikaa siku chache, nikingojea fedha kutoka Ofisi ya Fulbright, ambao ndio walinilipia gharama zote za masomo.

Baada ya siku chache za kukaa Union South, nilihamia Saxony Apartments, sehemu inayoonekana hapa kushoto. Jengo nilimoishi liko nyuma ya hili linaloonekana.

Saxony Apartments ilikuwa maarufu, kwa vile walikuwepo wa-Afrika wengi. Tulijisikia nyumbani.

Nadhani nilikaa hapo Saxony Apartments kwa mwaka moja na zaidi, nikahamia Mtaa wa West Wilson, namba 420, jengo linaloonekana hapa kushoto. Ni karibu na Ziwa Monona. Wa-Tanzania tulikuwa na mshikamano sana, tukitembeleana na kushirikiana katika raha na shida. Nakumbuka mikusanyiko tuliyofanyia hapa kwangu.

Miaka yangu ya mwisho mjini Madison, niliishi mahala paitwapo Eagle Heights, eneo lenye nyumba nyingi sana za wanafunzi wenye familia. Nilikuwa naishi katika nyumba hii, orofa ya juu. Ukianzia kushoto, ni dirisha la tatu na la nne.

Wikiendi hii nilipokuwa nazungukia maeneo hayo nilijiwa na kumbukumbu nyingi za miaka ile. Niliwakumbuka wa-Tanzania na wa-Afrika wengine tuliosoma wote, na mengine mengi. Yawezekana baadhi yao wataziona picha hizi na kukumbuka mambo ya miaka ile.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...