Wednesday, September 6, 2017

Muhula wa Masomo Unaanza

Wiki hii hapa chuoni St. Olaf, tunaanza muhula mpya wa masomo. Nitafundisha madarasa matatu. Mawili ni ya "First Year Writing," na moja ni "Post-colonial Literature." Katika "First Year Writing," tunafundisha uandishi bora wa ki-Ingereza.

Kozi ninayotaka kuongelea hapa  ni "Post-colonial Literature." Niliajiriwa hapa chuoni St. Olaf kuanzisha kozi hiyo, na nilianza kufundisha mwaka 1991. Ni kozi inayohusu fasihi kutoka nchi zilizokuwa katika himaya ya u-Ingereza wakati wa ukoloni ila zilikuja kuwa huru.

Ninapofundisha kozi hii, huwa ninaamua waandishi wepi kutoka nchi zipi nifundishe. Kwa muhula huu, niliamua kufundisha fasihi kutoka Afrika Kusini. Nilichagua waandishi wawili: Alex la Guma na Nadine Gordimer. Wote ni waandishi wa hadithi fupi na riwaya.

Nadhani tangu nilipokuwa mwanafunzi Mkwawa High School, nilisoma hadithi za Alex la Guma katika kitabu cha hadithi fupi kiitwacho Quartet. Baadaye, nilipokuwa mwanafunzi katika idara ya Literature, chuo kikuu cha Dar es Salaam, Alex la Guma alikuja kutoka London akatufundisha kwa siku kadhaa. Alialikwa na mkuu wa idara, mwalimu Grant Kamenju wa Kenya.

Nilifahamu kuwa Alex la Guma alikuja kuwa mwakilishi Uingereza wa chama cha ukombozi cha African National Congress cha Afrika Kusini, (ANC), kisha akawa mwakilishi wa ANC nchini Cuba. Alipofariki, nchini Cuba, nilikuwa ninasoma katika Chuo Kikuu cha Wisconsin Madison.

Nadine Gordimer ni mzungu aliyejihusisha na ANC. Alikuwa mpinzani wa utawala wa makaburu. Baada ya kuja Marekani kufundisha, nimebahatika kumwona Nadine Gordimer kwenye mkutano fulani wa kitaaluma. Sikumbuki ulikuwa ni mwaka gani. Nimefundisha hadithi zake fupi zilizokusanywa katika kitabu Six Feet of the Country, na riwaya zake, The Conservationist, The Pickup, na July's People.

Kufundisha juu ya waandishi hao wawili ni fursa ya kutafakari historia na siasa, hasa ukaburu na harakati za ukombozi katika Afrika Kusini. Yote hayo yamefungamana na fasihi, hasa katika karne ya ishirini, ambayo ndiyo kozi yangu itashughulikia. Tutafakari mitazamo ya waandishi hao wawili kuhusu siasa, mahusiano ya jamii, utamaduni, na itikadi katika Afrika Kusini. Tutaangalia athari za fasihi ya ulimwengu katika maandishi ya waandishi hao wawili na tutatambua mchango wa waandishi hao katika fasihi ya Afrika na ulimwengu.

1 comment:

Anonymous said...

What a totally energizing course to teach implementing politics, sociology and literature. Your students are so blessed to have you for a revealing teacher of the interaction of what the authors perceive and then share in their books. merri

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...