Showing posts with label mashairi. Show all posts
Showing posts with label mashairi. Show all posts

Thursday, March 8, 2018

Nimenunua Vitabu Vipya vya Mashairi

Katika siku chache zilizopita, nimenunua vitabu vipya viwili vya mashairi. Kimoja ni Collected Poems: 1974-2004  cha Rita Dove, ambacho nilikinunua mjini Moscow, Idaho. Kingine ni Diwani ya Tuzo ya Ushairi ya Ibrahim Hussein ambacho nilikinunua mtandaoni Amazon.

Nilipokuwa Moscow katika tamasha la Hemingway, niliingia katika duka la Book People of Moscow. Niliangalia, nikaona kitabu hiki Collected Poems, ambacho sikukifahamu kabla. Nilivutiwa kwa sababu nilifahamu habari za Rita Dove, kwamba ni mshairi maarufu sana, aliyepata tuzo kadhaa ikiwemo tuzo ya Pulitzer.

Zaidi ni kuwa niliwahi kusoma insha yake "Either I'm Nobody, or I'm a Nation," ambayo ni uchambuzi wa mashairi ya Derek Walcott. Nilikuwa ninafundisha tungo za Walcott, nikaitafuta makala hii na niliona ilivyojaa tafakari na ilivyoandikwa kwa ustadi. Makala hii ilinithibitishia kuwa Rita Dove ana akili sana. Hii ikawa sababu kubwa ya mimi kununua Collected Poems.

Diwani ya Tuzo ya Ushairi ya Ibrahim Hussein niliinunua baada ya kuiona imetajwa mtandaoni Amazon. Nilikuwa sifahamu kuwepo kwake, lakini kwa jinsi ninavyomwenzi Ebrahim Hussen ambaye nilimfahamu tulipokuwa wote katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, yeye akiwa mhadhiri wakati ninasoma, na hatimaye tukawa tunafundisha wote, niliona ninunue kitabu hiki. Mimi mwenyewe nimechapisha makala juu ya tungo za Ebrahim Hussein katika Encyclopedia of African Literature iliyohaririwa na profesa Simon Gikandi.

Nimeanza kuyasoma mashairi yaliyomo katika vitabu vyote viwili. Tayari nimeona kuwa Rita Dove anaandika kwa nidhamu ya hali ya juu, ya kutumia maneno yanayohitajika tu, na anatupeleka sehemu mbali mbali za dunia, tangu enzi za kale hadi leo, kama anavyofanya Derek Walcott katika tungo zake, iwe ni mashairi au tamthilia. Diwani ina washairi wengi chipukizi. Ni fursa yao kuonekana kwa wasomaji.

Monday, July 17, 2017

Nina Mashairi Yote ya John Donne

Nimegundua kuwa nina mashairi yote ya John Donne. Huyu ni mshairi mmoja maarufu sana katika ki-Ingereza, ambaye aliishi miaka ya 1572-1631, na niliwahi kumtaja katika blogu hii. Niliandika habari zake siku niliponunua kitabu kiitwacho The Works of John Donne.

Lakini wikiendi hii, katika kuangalia katika msitu wa vitabu vyangu ofisini, nimegundua kitabu kiitwacho The Complete English Poems of John Donne, kilichohaririwa na C.A. Patrides. Hiki kina mashairi yake yote.

Katika utangulizi wake, Patrides amesema mambo ambayo yamenifungua macho na kunifikirisha. Amesema, kwa mfano, "The text of Donne's poetry can vex an editor into nightmares." Anamaanisha kuwa maandishi ya Donne yanaweza kumchanganya akili mhariri akaishia katika majinamizi. Hii ni kwa sababu miswada ya mashairi ya Donne ni mingi na inahitilafiana.

Niliposoma utangulizi huu, nimewazia maandishi ya William Shakespeare, ambaye aliishi wakati ule ule wa John Donne. Maandishi ya Shakespeare, hasa tamthilia, nayo yanapatikana katika miswada inayohitilafiana, na kwa miaka yote wahariri wamekuwa wakijaribu kurekebisha na kuwasilisha kile ambacho wanaamini ni andiko sahihi la Shakespeare.

Tofauti hizi katika maandishi ya Donne na Shakespeare, haziko katika maneno na sentensi tu, bali pia katika alama kama vile nukta na mikato katika sentensi. Kwa hivyo, tunavyosoma andiko la Shakespeare, tunapaswa kuzingatia kuwa kuna vitu kadha wa kadha ambavyo vimeingizwa na wahariri wa karne moja hadi nyingine.

Hata hivi, kama nilivyosema katika ujumbe wangu wa mwanzo, nimeona nisome kwa makini mashairi ya Donne, hasa kwa kuzingatia kuwa nilikulia nikiwa nimesikia sana kwamba mashairi yake ni magumu. Nimepata mwamko mpya, wa kutaka kujipima akili kwa kuyakabili haya mashairi yanayosemekana ni magumu. Tena basi, nitapenda hata kujaribu kutafsiri baadhi ya mashairi haya kwa ki-Swahili, kama nilivyowahi kutamka katika blogu hii.

Thursday, May 25, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nikitokea Minneapolis, nilipita Apple Valley, katika duka la vitabu la Half Price Books. Nilikuwa nimepania kununua kitabu juu ya Hemingway, Hemingway's Boat: Everything He Loved in Life, And Lost, kilichotungwa na Paul Hendrickson, ambacho nilikifahamu kwa miezi, na hivi karibuni nilikiona katika duka hilo, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Kwa hivi, leo niliombea nikikute hiki kitabu, na kwa bahati nzuri nilikikuta. Baada ya kukichukua mahali kilipokuwepo, nilienda sehemu panapouzwa vitabu kwa bei ndogo zaidi. Bila kuhangaika sana, niliona kitabu kiitwacho F. Scott Fitzgerald, kilichotungwa na Arthur Mizener.  Nilifungua kurasa mbili tatu, nikakichukua.

Nilifahamu kwa muda mrefu kuwa Fitzgerald alizaliwa St. Paul, Minnesota, mji ninaoutembelea mara kwa mara. Nilishasoma riwaya yake maarufu, The Great Gatsby. Halafu, miaka hii ambapo nimekuwa nikisoma sana maandishi na habari za Ernest Hemingway, nimeelewa kuwa haiwezekani kumtenganisha Hemingway na Fitzgerald.

Hemingway alipokuwa kijana, akiishi Paris kama ripota wa gazeti la Toronto Star na pia kama mwandishi wa hadithi fupi na riwaya, alikuwa na mahusiano ya karibu na waandishi wengine waliokuwepo Paris, kama vile Gertrude Stein, Ezra Pound, na huyu F. Scott Fitzgerald. Fitzgerald alifanya bidii kumwezesha Hemingway kuanza kuandika riwaya, akafanya juhudi zilizomfanya Marx Perkins, mhariri maarufu wa kampuni ya Scribners Sons, akachapisha riwaya ya Hemingway, The Sun Also Rises. Hayo ndiyo mawazo yaliyonifanya nikanunua kitabu hiki.

Hapo hapo, nilivutiwa na kitabu kiitwacho The Works of John Donne, kilichoandaliwa na The Wordsworth Poetry Library. Sikuwa ninakifahamu kitabu hiki. Jina la mshairi John Donne nimelifahamu tangu zamani, labda nilipokuwa mwanafunzi katika shule ya sekondari. Nadhani nilishasoma mashairi yake mawili matatu, lakini sio zaidi.

Ila kwa kusoma maandishi ya wahakiki na wanataaluma, nilifahamu kuwa Donne anahesabiwa kama mshairi anayeandika mashairi magumu kuyaelewa. Habari hii ilichangia kunifanya nisiwe mwepesi wa kusoma mashairi yake. Nadhani si jambo zuri kwa mwandishi kuvumishiwa sifa kwamba tungo zake ni ngumu kueleweka. Inaweza kuwakatisha wasomaji hamu ya kujisomea maandishi ya mwandishi huyo.

Kwa Afrika, mashairi ya Christopher Okigbo yamepewa sifa hiyo. Pia mashairi ya Wole Soyinka. Lakini kwa umri nilio nao, na uzoefu wangu wa kusoma na kufundisha fasihi, naona ni vema kuwahimiza watu wajisomee wenyewe tungo zozote, kwani kwa kufanya hivyo, na kama wanafanya juhudi ya dhati, ni lazima wataambulia chochote. Nazingatia nadharia inayosema kwamba utungo wa fasihi una uwezo wa kuzalisha maana na tafsiri nyingi bila kikomo. Nadharia hii imefafanuliwa na wataalam kama Roland Barthes.

Saturday, March 11, 2017

Mashairi ya Robert Frost

Leo nina jambo la kusema, kuhusu mashairi ya Robert Frost, ambayo nimekuwa nikiyasoma sambamba na kazi zingine za fasihi au taaluma. Ni mazoea yangu kusoma kiholela, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Mashairi ya Frost ninayoongelea yamo katika kitabu kiitwacho Robert Frost: Selected Poems, ambacho binti yangu alininunulia. Wakati ule, nilijitahidi kuyasoma, lakini ninayafurahia zaidi wakati huu, labda ni kwa kuwa akili yangu imetulia kuliko wakati ule.

Leo, kwa mfano, nimesoma shairi liitwalo "The Black Cottage." Tunaelezwa kuhusu watu wawili wanavyoijongea nyumba ndogo iliyofichika nyuma ya miti na nyasi mbali na barabara. Wanaikaribia na kuchungulia ndani. Mmoja wao, ambaye ni mchungaji, anafahamu habari za nyumba hii ambayo sasa haina watu.

Anamweleza mwenzake kuwa bibi kizee aliyeishi humu alifariki, na watoto wake, wote wanaume, wanaishi mbali, ila hawataki kuiuza nyumba wala chochote kilichomo. Walipangia kuwa wanakuja mara moja kwa mwaka, lakini mwaka huu hawajaja. Baba yao alikufa katika vita ya wa-Marekani wenyewe kwa wenyewe ("Civil War"), eneo la Fredericksburg au Gettysburg.

Sehemu kubwa inayobaki ya shairi hili inaelezea fikra za marehemu bibi kizee kuhusu masuala mbali mbali yatokanayo na vita ile, kama vile malengo ya vita, na usawa wa binadamu. Mchungaji anaonesha kuwa fikra na mitazamo ya bibi kizee yule ilikuwa ya pekee na pia ya kutatanisha.

Hata mimi siwezi kusema nimeelewa vizuri mtazamo wa bibi kizee huyu, ingawa nimelisoma shairi hili na kulirudia. Itanibidi nilisome tena na tena. Vile vile, nimeona itakuwa jambo jema kufanya utafiti ili nione kama kuna tahakiki za shairi hili ambazo zimechapishwa. Daima, hii njia bora ya kujipanua upeo kuhusu utungo wa fasihi.

Kama kawaida, Frost anaandika kwa mtindo unaokufanya msomaji ujisikie kuwa anafanya nawe maongezi ya kina. Unawajibika kumsikiliza huku ukitafakari asemayo. Kusoma shairi hili, kama mashairi mengine ya Frost kunahitaji akili  tulivu.

Jambo moja linalonivutia katika kusoma mashairi haya ya Frost ni kuwa ninasoma alichoandika yeye mwenyewe, sio tafsiri. Ni bahati kuwa na uhusiano wa moja kwa moja na mwandishi namna hiyo. Ninakuwa na fursa kamili ya kuguswa na umahiri wa mwandishi katika kuelezea mambo, kuanzia hisia na fikra zake na za wahusika, hadi vitu na mazingira.

Saturday, February 25, 2017

Tafsiri Yangu ya "A Time to Talk" (Robert Frost)

Leo nimetafsiri shairi fupi la Robert Frost, "A Time to Talk." Hili ni shairi nililolisoma kwa mara ya kwanza miaka mitatu iliyopita, baada ya binti yangu Zawadi kuninunulia kitabu cha mashairi ya Frost, Robert Frost: Selected Poems. Kama nilivyoelezea katika blogu hii, nilikuwa nimelazwa hospitalini mjini Minneapolis, na binti yangu, kwa kujua ninavyopenda vitabu, alininunulia hiki kitabu kinisaidie kukabili hali niliyokuwemo.

Shairi hili la "A Time to Talk" lina mawaidha mazito kuhusu maisha. Linatukumbusha umuhimu wa uungwana na ukarimu katika mahusiano yetu binadamu. Tuache fikra ya kwamba hatuna muda wa kujumuika na wenzetu, kujuliana hali, na kadhalika. Robert Frost anavyoelezea mambo katika shairi hili ananikumbusha maisha ya vijijini, ambayo niliishi tangu utotoni. Kusalimiana ni wajibu, na watu hutumia muda kujuliana hali.

Bila shaka, Frost anaukosoa utamaduni wa ubinafsi, na utamaduni wa kila mtu na maisha yake. Anaikosoa hali ambayo wanafalsafa kama Karl Marx na wafuasi wake wameiongelea vizuri kwa kutumia dhana ya "alienation." Anavyoongelea kuhusu kuwa na muda wa kuongea na wenzetu, ninaona kuwa Frost anaikejeli jamii ambayo imejiaminisha kuwa muda ni hela ("time is money"). Ninavyosema hayo mambo yanayohusu utamaduni, kama yalivyoelezwa katika shairi hili, ninakumbuka nilivyoyaelezea katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Kwa kumalizia, napenda nirudie jambo ambalo ninalitamka daima. Kutafsiri kazi ya fasihi ni shughuli ngumu yenye mitego na vipingamizi vingi. Nilivyojaribu kulitafsiri shairi la Frost, simaanishi kuwa tafsiri yangu ndio kilele cha ufanisi. Msomaji makini anayezifahamu vizuri sana lugha za ki-Ingereza na ki-Swahili, na sio lugha tu, bali lugha ya kifasihi, bila shaka ataona vipengele ambayo vingeweza kuboreshwa. Kwa mfano, katika mstari wa pili, utatafsirije "a meaning walk," ili uziwasilishe kwa ki-Swahili dhana zilizomo katika huo usemi wa ki-Ingereza?
------------------------------------------------------------------------------------------------------------

A TIME TO TALK (Robert Frost, 1874-1963)

When a friend calls to me from the road
And slows his horse to a meaning walk,
I don't stand still and look around
On all the hills I haven't hoed,
And shout from where I am, What is it?
No, not as there is a time to talk.
I thrust my hoe in the mellow ground,
Blade-end up and five feet tall,
And plod: I go up to the stone wall
For a friendly visit.

MUDA WA MAONGEZI

Rafiki anaponiita kutoka barabarani
Huku akipunguza kwa makusudi mwendo wa farasi wake,
Sisimami tu na kuangalia huko na huko
Kubaini idadi ya vilima ambavyo bado sijalima
Na kisha kupaaza sauti pale nilipo, Vipi?
Hapana, hapana kwani kuna muda wa kuongea.
Nasimika jembe langu katika ardhi tepetepe,
Ubapa wa jembe ukiwa juu futi tano toka ardhini,
Na ninatembea taratibu: ninaelekea kwenye ukuta wa mawe
Kukutana na rafiki.

Saturday, February 11, 2017

Ninamwazia Mwandishi Alexander Pushkin

Kwa wiki yapata mbili, nimekuwa nikimwazia sana Alexander Pushkin, mwandishi maarufu wa u-Rusi. Nimefahamu tangu ujana wangu kuwa wa-Rusi wanamwenzi kama baba wa fasihi ya u-Rusi. Miaka ya baadaye, nilikuja kufahamu kuwa Pushkin alikuwa na asili ya Afrika, na kwamba hata katika baadhi ya maandishi yake aliongelea suala hilo.

Nilisoma makala za profesa moja wa Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, nikafahamu zaidi suala hilo. Katika kufuatilia zaidi, niliguswa na mengi, hasa maelezo juu ya kipaji cha Pushkin cha ajabu katika matumizi ya lugha ya ki-Rusi na ubunifu wake, na pia jinsi alivyokufa. Aliuawa katika ugomvi akiwa na umri wa miaka 37 tu.


Siku kadhaa zilizopita, nilitoa mhadhara katika darasa la Nu Skool, kuhusu umuhimu wa Afrika na wa-Afrika katika historia ya ulimwengu. Kati ya watu maarufu wenye asili ya Afrika ambao niliwataja kwa mchango wao ni Antar bin Shaddad wa Saudi Arabia na Pushkin. Antar bin Shaddad ni mshairi aliyeishi kabla ya Mtume Muhammad, na ambaye tungo zake zinakumbukwa kama hazina isiyo kifani katika lugha ya ki-Arabu. Pushkin ni hivyo hivyo; wa-Rusi wanakiri kuwa umahiri wake katika kuimudu lugha yao hauna mfano.

Kutokana na hayo nimekuwa na hamu ya kumsoma Pushkin, nikakumbuka kuwa nilishanunua kitabu chake maarufu, Eugene Onegin, ambayo ni hadithi iliyoandikwa kishairi. Ninajiandaa kuisoma.

Wednesday, December 14, 2016

Wosia wa Rabindranath Tagore Kuhusu Uhuru wa Kutoa Maoni

Rabindranath Tagore ni mmoja wa waandishi maarufu kabisa waliowahi kuishi. Alizaliwa mwaka 1861 Calcutta na kufariki 1941. Aliheshimika duniani kote wakati wa uhai wake na bado anaheshimika. Aliandika mashairi, tamthilia, insha, riwaya, hadithi fupi, na pia maelfu ya barua. Niliwahi kufundisha utungo wake maarufu Gitanjali, hapa chuoni St. Olaf.

Tagore alikuwa mwalimu aliyetukuka, kioo cha ubinadamu wa kweli ("humanism"), mwenye fikra pevu na nzito juu ya maisha na maadili. Watu maarufu kama W.B. Yeats, Mahatma Gandhi na Albert Einstein, walimmwenzi sana. Mwaka 1913 alipata tuzo ya Nobel katika fasihi. Nina vitabu vyake vitatu, kimojawapo kikiwa Rabindranath Tagore: An Anthology.

Kutoka katika kitabu hiki nimenukuu sehemu ya ujumbe wa tarehe 25 Septemba, 1930, kwa gazeti la Izvestia la Urusi. Ni ujumbe unaopaswa kutafakariwa na kuzingatiwa, tunaposhuhudia ukandamizaji wa uhuru wa watu kujieleza. Ili kuufikisha ujumbe kwa watu wasiojua ki-Ingereza, nimejaribu kuutafsiri.

     There must be disagreement where minds are allowed to be free. It would not only be an uninteresting but sterile world of mechanical regularity if all our opinions were forcibly made alike. If you have a mission which includes all humanity, you must, for the sake of that living humanity, acknowledge the existence of differences of opinion. Opinions are constantly changed and re-changed only through the free circulation of intellectual forces and moral persuasion. Violence begets violence and blind stupidity. Freedom of mind is needed for the reception of truth; terror hopelessly kills it. The brute cannot subdue the brute. It is only the man who can do it.

Tafsiri

     Lazima pawepo na kutokubaliana mahali ambapo akili zinaruhusiwa kuwa huru. Dunia itakuwa sio tu haipendezi bali tasa yenye kwenda kwa mwendo ule ule kama mashine, iwapo maoni yetu yote yatalazimishwa kufanana. Kama watu mna malengo yanayowahusu wanadamu kwa ujumla wao, sherti, kwa manufaa ya uhai wa jamii hiyo ya wanadamu, kutambua uwepo wa tofauti za maoni. Maoni hubadilishwa bila ukomo pale tu panapokuwa na mzunguko huru wa nguvu za akili na ushawishi wa mwenendo wa kimaadili. Mabavu huzaa mabavu na ujinga mithili ya upofu. Uhuru wa akili unahitajika ili ukweli upokelewe, na vitisho huua kabisa ukweli huo. Hayawani hawezi kumdhibiti hayawani. Ni binadamu tu ndiye anaweza.

Thursday, November 24, 2016

"A Far Cry From Africa," Shairi la Derek Walcott

Tangu nilipoanza kufundisha katika chuo cha St. Olaf, mwaka 1991, nimepata fursa ya kusoma na kufundisha fasihi iliyoandikwa kwa ki-Ingereza kutoka sehemu mbali mbali ulimwenguni, kwa kiwango kikubwa kuliko ilivyowezekana nilipokuwa ninafundisha katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mwandishi mmojawapo ambaye kazi zake nimezishughulikia sana ni Derek Walcott wa St. Lucia, pande za Caribbean, maarufu kwa utunzi wa mashairi na tamthilia, ambaye alipata tuzo ya Nobel mwaka 1992.

Nimesoma na kufundisha mashairi yake mengi na tamthilia zake kadhaa. Moja ya mashairi hayo ni "A Far Cry From Africa," ambalo lilichapishwa mwaka 1962. Linaelezea mahuzuniko juu ya vita ya Mau Mau nchini Kenya iliyodumu kuanzia mwaka 1952 hadi 1960. Masetla wazungu walipigana na wa-Afrika waliotaka kuchukua ardhi yao iliyoporwa. Kwa kuwa Derek Walcott ni chotara, damu ya kizungu na ki-Afrika, alihisi vita hiyo ikitokea ndani ya nafsi yake. Uhasama na ukatili wa pande hizo mbili aliuhisi mithili ya sumu katika mishipa ya damu yake. Alijihisi kama mateka aliyekosa namna ya kujinasua.

Walcott anaimudu lugha ya ki-Ingereza kwa namna inayonikumbusha umahiri wa Shakespeare. Nitafurahi iwapo nitapata ujasiri wa kujaribu kulitafsiri shairi kwa ki-Swahili.
-------------------------------------------------------------------------------

A Far Cry From Africa

Derek Walcott


A wind is ruffling the tawny pelt 
Of Africa, Kikuyu, quick as flies, 
Batten upon the bloodstreams of the veldt. 
Corpses are scattered through a paradise. 
Only the worm, colonel of carrion, cries: 
'Waste no compassion on these separate dead!' 
Statistics justify and scholars seize 
The salients of colonial policy. 
What is that to the white child hacked in bed? 
To savages, expendable as Jews?

Threshed out by beaters, the long rushes break 
In a white dust of ibises whose cries 
Have wheeled since civilizations dawn 
From the parched river or beast-teeming plain. 
The violence of beast on beast is read 
As natural law, but upright man 
Seeks his divinity by inflicting pain. 
Delirious as these worried beasts, his wars 
Dance to the tightened carcass of a drum, 
While he calls courage still that native dread 
Of the white peace contracted by the dead. 

Again brutish necessity wipes its hands 
Upon the napkin of a dirty cause, again 
A waste of our compassion, as with Spain, 
The gorilla wrestles with the superman. 
I who am poisoned with the blood of both, 
Where shall I turn, divided to the vein? 
I who have cursed 
The drunken officer of British rule, how choose 
Between this Africa and the English tongue I love? 
Betray them both, or give back what they give? 
How can I face such slaughter and be cool? 
How can I turn from Africa and live?

Friday, November 18, 2016

Mashairi Mazuri ya Ki-Ingereza

Tangu ujana wangu, nimebahatika kusoma na kuyafurahia mashairi mazuri ya ki-Ingereza. Ninakumbuka nilivyoingia kidato cha tano, Mkwawa High School, mwaka 1971, nikakutana na Mugyabuso Mulokozi na Kulikoyela Kahigi ambao nao walikuwa wanafunzi. Walikuwa na kitabu cha mashairi ya ki-Ingereza, tukawa tunayasoma na kuyafurahia. Mifano ni shairi la Thomas Hardy, "An Ancient to Ancients."

Mashairi ya Shakespeare yaitwayo "sonnets" yalituvutia. Mfano ni "Sonnet 18" ambayo mstari wake wa kwanza ni "Shall I compare thee to a summer's day?" Shairi la Samuel Taylor Coleridge, "The Rime of the Ancient Mariner," lilikuwa daima mawazoni mwetu. Shairi la W.B. Yeats, "The Second Coming," ni moja ya mashairi yaliyonigusa sana, kama nilivyoandika katika blogu hii. Shairi la Walter de la Mare, "The Listeners," limeng'ang'ania akili mwangu tangu enzi zile.

Mashairi mengine tulisoma darasani, kama vile yale ya Percy Bysshe Shelley na Alfred Lord Tennyson, ambao ni wa-Ingereza, na pia waandishi wa ki-Afrika kama vile Wole Soyinka, John Pepper Clark, Dennis Brutus, na Keorapetse Kgositsile. Hiyo ilikuwa ni miaka ya sabini na kitu.

Baada ya kuja masomoni katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, mwaka 1980, niliendelea kukutana na mashairi yenye mvuto mkubwa kwangu. Mifano ni shairi la William Wordsworth, "Lines Composed a Few Miles Above Tintern Abbey.'' Hilo tulilisoma kwa makini katika kozi ya "Poetry" iliyofundishwa na Profesa John Brenkman. Profesa Brenkman alitufundisha pia mashairi ya washairi wengine, kama vile Wallace Stevens.

Baada ya kuja kufundisha katika Chuo cha St. Olaf, mwaka 1991, nimepata fursa ya kusoma na kufundisha mashairi ya watunzi wengi zaidi, kuanzia wa Australia, kama vile Judith Wright na Oodgeroo Noonuccal hadi wa Marekani, kama vile Carl Sandburg na Lawrence Ferlinghetti, hadi wa Caribbean, kama vile Derek Walcott. Derek Walcott ni mshairi mojawapo ninayemwenzi sana, kwa uhodari wake wa kutumia lugha, kusisimua akili. na kuelezea hali halisi ya tabia na hisia za binadamu kwa upeo mpana wa historia na tamaduni mbali mbali.

Ninaendelea kusoma mashairi ya ki-Ingereza, ili kutajirisha akili yangu, na wakati mwingine ninayatafsiri kwa ki-Swahili. Kwa mfano nimetafsiri shairi la Stanley Kunitz, "The Layers," na shairi la Edmund Spencer, "Ye Tradefull Merchants." Ninajiona mwenye bahati kwa hizi fursa nilizo nazo za kufurahia kazi za watunzi maarufu. Jana, kwa mfano, nimesoma shairi la William Savage Landor, "To Wordsworth," nikaguswa sana.

Kuhitimisha ujumbe wangu, ninawazia ingekuwaje kama ningejua lugha nyingi zaidi, kama vile ki-Faransa, ki-Jerumani, ki-Hispania, na ki-Arabu, nikawa ninasoma tungo maarufu zilizomo katika lugha hizo.

Sunday, November 6, 2016

Buriani Mwandishi John Calvin Rezmerski

Leo hapa Minnesota zimeenea taarifa za kufariki kwa mwandishi John Calvin Rezmerski. Taarifa moja imechapishwa katika Minneapolis Star Tribune. Nilipata bahati ya kuonana naye miaka michache iliyopita mjini Mankato, Minnesota, kwenye tamasha la vitabu, Deep Valley Book Festival. Tuliongea, nikanunua kitabu chake cha mashairi kiitwacho What Do I Know?: New & Selected Poems, ambacho alikisaini hivi:

for Joseph Mbele--
Wonderful to talk with you at Deep Valley Book Festival,
John Calvin Rezmerski

Taarifa tulizopata leo zinaelezea mambo mema mengi ya bwana Rezmerski: alikuwa mwandishi makini wa mashairi, msimuliaji hadithi, mwalimu aliyependwa, mkarimu kwa watu. Kuhusu falsafa ya ushairi ya Rezmerski, Bill Holm, ambaye ni mwandishi maarufu hapa Minnesota, aliwahi kuandika: "John Rezmerski believes that poetry lives inside the daily speech of ordinary people, that the ear and the mouth are connected to the imagination and the heart."

Dhana hiyo ya ushairi inanikumbusha falsafa ya Shaaban Robert na pia William Wordsworth kuhusu ushairi. Inaendana hasa na falsafa ya Wordsworth, ambaye aliamini kuwa lugha ya watu wa kawaida ndio chimbuko la ushairi halisi na ndio inapaswa kutumiwa na washairi, tofauti na lugha ya urasimi, ambayo haikuendana na hisia halisi za binadamu bali ilikuwa lugha tasa.

Mara baada ya kusikia taarifa za kifo cha Rezmerski, nimetafuta nakala yangu ya What Do I Know?: New & Selected Poems, ili kusoma mashairi yaliyomo, kama njia ya kumkumbuka mwandishi huyu ambaye nilibahatika kumwona, ingawa ni mara moja tu. Shairi lake moja ni hili:

THE FUGITIVE

What if after all these years
in the same body,
I turn out to be somebody else?
What a new thing
to decide which pair of pants.
How sweet to have grapefruit
and like it for the first time.
I would burn old letters,
buy a new toothbrush,
learn to like the closeness
of cold on my clean skin.
I would pronounce every word
as though it were fine glass.
It is an old story
I tell the mirror
while I gape at my teeth
looking for someone else's cavities.

Nimelipenda shairi hili kwa jinsi linavyotumia mbinu mbali mbali za kuchezea akili ya msomaji, kuanzia kejeli hadi ubunifu wa mambo yasiyowezekana, hadi kuangalia mambo tuliyoyazoea kwa mtazamo wa kuyafanya yawe ya ajabu. Shairi limejaa mawazo na kauli tusizotegemea. Ili kulisoma na kulitafakari shairi hili kwa umakini, makala maarufu ya Cleanth Brooks, The Language of Paradox, inaweza kusaidia sana.

Wednesday, December 9, 2015

Mtunzi Haji Gora Haji

Leo nimeamua kuongelea kifupi utunzi wa Haji Gora Haji wa Zanzibar, mmoja wa waandishi maarufu wa ki-Swahili wa zama zetu hizi. Nafurahi kuwa niliwahi kuonana naye mjini Zanzibar na kuzungumza naye. Panapo majaliwa, nitaandika taarifa ya mazungumzo yetu, ambayo yalihusu maisha yake katika sanaa. Ni muhimu kuutangazia ulimwengu kazi murua inayofanywa na watu wetu wenye vipaji kama Haji Gora Haji.

Nina vitabu vyake vinne: Kimbunga (Dar es Salaam: Dar es Salaam University Press, 1994), Utenzi wa Visa vya Nabii Suleiman Bi Daudi (A.S.) (Zanzibar: Al-Khayria Press Ltd, 1999), Kamusi ya Kitumbatu (Zanzibar: Express Printing Services, 2006), na Siri ya Ging'ingi (Dar es Salaam: Taasisi ya Taaluma za Kiswahili Chuo Kikuu Dar es Salaam, 2009).

Kadiri siku zinavyopita, wasomaji na wahakiki wanajitokeza na kuongelea uandishi wa Haji Gora Haji. Mifano ya kutambuliwa huko ni taarifa ya Amanda Leigh Lichtenstein, ya Ridder Samson, na ya Pascal Bacuez. Nami nimetafsiri mashairi yake mawili nikayachapisha hapa, hapa, na hapa.

Haji Gora Haji, kama walivyo watunzi wengi, wa zamani hadi leo, wamejengeka katika jadi ya fasihi simulizi. Wanaitumia jadi hii katika utunzi wao, iwe ni mashairi kama walivyofanya W.B. Yeats na Derek Walcott, au riwaya, kama walivyofanya Charles Dickens na Chinua Achebe, au tamthilia, kama walivyofanya William Shakespeare, Wole Soyinka na Ebrahim Hussein, au hadithi fupi, kama walivyofanya Lu Hsun na Ama Ata Aidoo.

Ni hivyo hivyo kwa Haji Gora Haji, kama nilivyowahi kutamka. Utumiaji wa mbinu, miundo, na hata dhamira zitokanazo na fasihi simulizi kunachangia uwezo wa tungo kugusa fikra na hisia za hadhira kwa namna ya pekee kutokana na kwamba fasihi simulizi ni urithi wa wanadamu wote. Maudhui yatokanayo na fasihi simulizi ni ya thamani kwa wanadamu wote.

Kuthibitisha zaidi namna Haji Gora Haji alivyojengeka katika fasihi simulizi, sikiliza anavyosimulia hadithi ya Paa na Pweza.


Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...