Showing posts with label ki-Swahili. Show all posts
Showing posts with label ki-Swahili. Show all posts

Thursday, March 29, 2018

Kitabu Kinaendelea Kupigiwa Debe Nebraska

Mfanya biashara au mtoa huduma hufarijika anapoona wateja wakija tena kufuata kile walichokipata kabla. Imekuwa hivyo kwangu kama mwandishi. Mimi si mfanyabiashara, bali ni mwalimu. Uandishi ni sehemu ya ualimu. Ninafarijika na kufurahi ninapoona watu wakifaidika na maandishi yangu.

Ninaandika ujumbe huu kuelezea ujumbe juu ya kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kutoka Nebraska, jimbo mojawapo la Marekani. Waumini wa kanisa la ki-Luteri la Marekani, ELCA, wa sinodi ya Nebraska wana programu ya kuzuru Tanzania iitwayo vision trip, kujifunza masuala ya utamaduni na maisha ya wa-Tanzania na kubadilishana uzoefu, ili kujenga mahusiano na maelewano.

Mwaka hadi mwaka, waratibu wa programu wamekipendekeza kitabu changu hicho. Leo nimeona chapisho la mwongozo kwa ajili safari ya mwaka 2018. Humo, kama ilivyokuwa miaka iliyopita, kitabu changu kimeendelea kupendekezwa kwa wasafiri:

For those persons wanting to more deeply explore cultural differences between Africans and Americans, the book Africans and Americans by Joseph Mbele is recommended. This book is available at: www.africonexion.com

Tafsiri kwa ki-Swahili:

Kwa wale wanaotaka kufuatilia zaidi tofauti za tamaduni baina ya wa-Afrika na wa-Marekani, kitabu "Africans and Americans" cha Joseph Mbele kinapendekezwa. Kitabu hiki kinapatikana www.africonexion.com


Ninafurahi na kushukuru kwamba watu wanaona umuhimu wa kitabu hiki. Kingekuwa hakina manufaa, wangeacha kukipendekeza tangu zamani. Niliwahi kukutana na baadhi ya hao wasafiri wa Nebraska katika safari ya kwenda Tanzania wakiwa na kitabu changu, kama nilivyoandika katika blogu ya ki-Ingereza. Ninafurahi kuwa kitabu changu kinasaidia lengo la kujenga maelewano baina ya wa-Tanzania na wa-Marekani.

Saturday, May 27, 2017

"Witchcraft by a Picture" (John Donne)

Juzi, nilinunua kitabu cha mashairi kiitwacho The Works of John Donne, kama nilivyosema katika blogu hii. John Donne aliishi Uingereza, hasa London, miaka ya 1572-1631.

Katika kuyasoma mashairi yake, nimeona kuwa yanahitaji utulivu wa pekee, na tafakari, kwani matumizi yake ya lugha yanaonyesha uangalifu mkubwa. Ki-Ingereza chake ni cha miaka ile, ambayo ni miaka ya William Shakespeare, si cha leo. Hapa naleta shairi mojawapo, "Witchcraft by a Picture." Labda siku moja nitapata ujasiri wa kujaribu kulitafsiri kwa ki-Swahili.



         Witchcraft by a Picture

I fixe mine eye on thine, and there
     Pitty my picture burning in thine eye,
My picture drown'd in a transparent teare,
     When I looke lower I espie;
          Hadst thou the wicked skill
By pictures made and mard, to kill,
How many wayes mightst thou performe thy will?

But now I have drunke thy sweet salt teares,
     And though thou poure more I'll depart;
My picture vanish'd, vanish feares,
     That I can be endamag'd by that art;
          Though thou retaine of mee
One picture more, yet that will bee,
Being in thine owne heart, from all malice free.

Wednesday, April 12, 2017

Blogu Yangu Imepanda Chati Ghafla

Tangu wiki mbili zilizopita, blogu yangu hii imepanda chati ghafla. Ninaongelea kigezo cha "pageviews," ambazo ninaziangalia kila nitakapo. Kwa miaka na miaka, "pageviews" za blogu hii kwa siku zilikuwa kama 130, sio zaidi sana na sio pungufu sana.

Lakini, kuanzia wiki mbili hivi zilizopita, "pageviews" zimeongezeka ghafla kwa kiwango kikubwa, na sasa ni yapata 900 au zaidi kila siku. Sielewi ni nini kimesababisha ongezeko hilo. Mkondo wa mada zangu haujabadilika. Kwa kiasi kikubwa ninashughulika na masuala ya elimu na utamaduni.

Nimeona kuwa ongezeko hilo la "pageviews," limetokea hapa Marekani. Kwa nchi zingine, kama vile Tanzania na Kenya, hali haijabadilika. Ni ajabu kiasi kwamba blogu ya ki-Swahili inasomwa zaidi Marekani kuliko Afrika Mashariki.

Mtu unaweza kujiuliza ni watu gani wanaosoma hii blogu ya ki-Swahili kwa wingi namna hii hapa Marekani. Ukweli ni kuwa kuna watu wengi hapa, hasa kutoka Kenya na Tanzania, wanaokifahamu ki-Swahili. Wako pia watu kutoka Burundi, Uganda, Rwanda, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Vile vile, kuna wa-Marekani ambao wameishi Afrika Mashariki na wanakifahamu ki-Swahili. Pia kuna wa-Marekani wengi ambao wamejifunza au wanajifunza ki-Swahili katika vyuo vikuu mbali mbali hapa hapa Marekani. Ninahisi kuwa hao nao ni kati ya wasomaji wa blogu hii.

Ninavyowazia suala hili la ukuaji wa idadi ya "pageviews" katika blogu, ninawazia jinsi watu wanavyotumia blogu kwa matangazo, hasa ya biashara. Katika ulimwengu wa leo ambamo tekinolojia za mawasiliano zinaendelea kusambaa na kuimarika, wafanya biashara na wajasiriamali wanatumia fursa za mitandao kama vile blogu kutangaza shughuli zao.

Kwa upande wangu, sijajiingiza katika matumizi haya ya blogu, ukiachilia mbali matangazo ya vitabu vyangu na mihadhara ninayotoa au matamasha ninayoshiriki. Lakini, endapo nitabadili msimamo, bila shaka nitakaribisha matangazo ya waandishi, wachapishaji, na wauzaji wa vitabu, kwa sababu blogu yangu inajitambulisha kwa masuala ya aina hiyo.

Saturday, February 25, 2017

Tafsiri Yangu ya "A Time to Talk" (Robert Frost)

Leo nimetafsiri shairi fupi la Robert Frost, "A Time to Talk." Hili ni shairi nililolisoma kwa mara ya kwanza miaka mitatu iliyopita, baada ya binti yangu Zawadi kuninunulia kitabu cha mashairi ya Frost, Robert Frost: Selected Poems. Kama nilivyoelezea katika blogu hii, nilikuwa nimelazwa hospitalini mjini Minneapolis, na binti yangu, kwa kujua ninavyopenda vitabu, alininunulia hiki kitabu kinisaidie kukabili hali niliyokuwemo.

Shairi hili la "A Time to Talk" lina mawaidha mazito kuhusu maisha. Linatukumbusha umuhimu wa uungwana na ukarimu katika mahusiano yetu binadamu. Tuache fikra ya kwamba hatuna muda wa kujumuika na wenzetu, kujuliana hali, na kadhalika. Robert Frost anavyoelezea mambo katika shairi hili ananikumbusha maisha ya vijijini, ambayo niliishi tangu utotoni. Kusalimiana ni wajibu, na watu hutumia muda kujuliana hali.

Bila shaka, Frost anaukosoa utamaduni wa ubinafsi, na utamaduni wa kila mtu na maisha yake. Anaikosoa hali ambayo wanafalsafa kama Karl Marx na wafuasi wake wameiongelea vizuri kwa kutumia dhana ya "alienation." Anavyoongelea kuhusu kuwa na muda wa kuongea na wenzetu, ninaona kuwa Frost anaikejeli jamii ambayo imejiaminisha kuwa muda ni hela ("time is money"). Ninavyosema hayo mambo yanayohusu utamaduni, kama yalivyoelezwa katika shairi hili, ninakumbuka nilivyoyaelezea katika kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Kwa kumalizia, napenda nirudie jambo ambalo ninalitamka daima. Kutafsiri kazi ya fasihi ni shughuli ngumu yenye mitego na vipingamizi vingi. Nilivyojaribu kulitafsiri shairi la Frost, simaanishi kuwa tafsiri yangu ndio kilele cha ufanisi. Msomaji makini anayezifahamu vizuri sana lugha za ki-Ingereza na ki-Swahili, na sio lugha tu, bali lugha ya kifasihi, bila shaka ataona vipengele ambayo vingeweza kuboreshwa. Kwa mfano, katika mstari wa pili, utatafsirije "a meaning walk," ili uziwasilishe kwa ki-Swahili dhana zilizomo katika huo usemi wa ki-Ingereza?
------------------------------------------------------------------------------------------------------------

A TIME TO TALK (Robert Frost, 1874-1963)

When a friend calls to me from the road
And slows his horse to a meaning walk,
I don't stand still and look around
On all the hills I haven't hoed,
And shout from where I am, What is it?
No, not as there is a time to talk.
I thrust my hoe in the mellow ground,
Blade-end up and five feet tall,
And plod: I go up to the stone wall
For a friendly visit.

MUDA WA MAONGEZI

Rafiki anaponiita kutoka barabarani
Huku akipunguza kwa makusudi mwendo wa farasi wake,
Sisimami tu na kuangalia huko na huko
Kubaini idadi ya vilima ambavyo bado sijalima
Na kisha kupaaza sauti pale nilipo, Vipi?
Hapana, hapana kwani kuna muda wa kuongea.
Nasimika jembe langu katika ardhi tepetepe,
Ubapa wa jembe ukiwa juu futi tano toka ardhini,
Na ninatembea taratibu: ninaelekea kwenye ukuta wa mawe
Kukutana na rafiki.

Friday, February 19, 2016

"Tenzi Tatu za Kale:" Makala Inayosomwa Kuliko Zote

Mara kwa mara, ninaangalia takwimu zinazohusu blogu yangu hii: idadi ya watembeleaji, makala wanazozitembelea, na nchi walimo. Kuanzia wiki kadhaa zilizopita, makala inayotembelewa kuliko zote ni "Tenzi Tatu za Kale." Idadi ya watembeleaji iliongezeka ghafla pale Ndugu Michuzi alipoiweka makala hii katika blogu yake.

Ninajiuliza kwa nini makala hii inawavutia wasomaji namna hii. Je, hii ni ishara ya kupendwa kwa somo la fasihi ya ki-Swahili? Siamini kama ni hivyo, kwani ninaandika makala nyingi kuhusu fasihi, ambazo zinagusia tungo mbali mbali. Ingekuwa uwingi wa wasomaji unaonekana kwenye makala hizo pia, ningeamini kuwa kuna msisimko wa kupenda fasihi.

Ninapata hisia kwamba labda uhusiano na mahitaji ya shuleni au vyuoni. Ninahisi kuwa labda wanaosoma makala ya "Tenzi Tatu za Kale" ni wanafunzi ambao wanatakiwa kusoma Utenzi wa Al Inkishafi, au Utenzi wa Mwana Kupona, au Utenzi wa Fumo Liyongo: moja, mbili, au zote tatu.

Kama ni hivyo, si jambo la kuridhisha wala kufurahisha. Uwanja wa fasihi ya ki-Swahili ni mpana, na mwenye mapenzi na fasihi hii ninamtegemea awe anasoma tungo nyingi. Hata wanafunzi wa fasihi wanatakiwa kusoma tungo mbali mbali, si zile zilizomo katika mitaala tu.

Ningependa sana kuona mijadala ya fasihi ya ki-Swahili katika blogu hii. Ndio maana ninaweka taarifa mbali mbali kuhusu tungo za ki-Swahili. Tuienzi fasihi hii kwa kuisoma bila mipaka, kuichambua, na kuitangaza.
 

Wednesday, December 9, 2015

Mtunzi Haji Gora Haji

Leo nimeamua kuongelea kifupi utunzi wa Haji Gora Haji wa Zanzibar, mmoja wa waandishi maarufu wa ki-Swahili wa zama zetu hizi. Nafurahi kuwa niliwahi kuonana naye mjini Zanzibar na kuzungumza naye. Panapo majaliwa, nitaandika taarifa ya mazungumzo yetu, ambayo yalihusu maisha yake katika sanaa. Ni muhimu kuutangazia ulimwengu kazi murua inayofanywa na watu wetu wenye vipaji kama Haji Gora Haji.

Nina vitabu vyake vinne: Kimbunga (Dar es Salaam: Dar es Salaam University Press, 1994), Utenzi wa Visa vya Nabii Suleiman Bi Daudi (A.S.) (Zanzibar: Al-Khayria Press Ltd, 1999), Kamusi ya Kitumbatu (Zanzibar: Express Printing Services, 2006), na Siri ya Ging'ingi (Dar es Salaam: Taasisi ya Taaluma za Kiswahili Chuo Kikuu Dar es Salaam, 2009).

Kadiri siku zinavyopita, wasomaji na wahakiki wanajitokeza na kuongelea uandishi wa Haji Gora Haji. Mifano ya kutambuliwa huko ni taarifa ya Amanda Leigh Lichtenstein, ya Ridder Samson, na ya Pascal Bacuez. Nami nimetafsiri mashairi yake mawili nikayachapisha hapa, hapa, na hapa.

Haji Gora Haji, kama walivyo watunzi wengi, wa zamani hadi leo, wamejengeka katika jadi ya fasihi simulizi. Wanaitumia jadi hii katika utunzi wao, iwe ni mashairi kama walivyofanya W.B. Yeats na Derek Walcott, au riwaya, kama walivyofanya Charles Dickens na Chinua Achebe, au tamthilia, kama walivyofanya William Shakespeare, Wole Soyinka na Ebrahim Hussein, au hadithi fupi, kama walivyofanya Lu Hsun na Ama Ata Aidoo.

Ni hivyo hivyo kwa Haji Gora Haji, kama nilivyowahi kutamka. Utumiaji wa mbinu, miundo, na hata dhamira zitokanazo na fasihi simulizi kunachangia uwezo wa tungo kugusa fikra na hisia za hadhira kwa namna ya pekee kutokana na kwamba fasihi simulizi ni urithi wa wanadamu wote. Maudhui yatokanayo na fasihi simulizi ni ya thamani kwa wanadamu wote.

Kuthibitisha zaidi namna Haji Gora Haji alivyojengeka katika fasihi simulizi, sikiliza anavyosimulia hadithi ya Paa na Pweza.


Thursday, November 26, 2015

Utendi wa Mikidadi na Mayasa

Wiki hii, bila kutegemea, nimevutiwa na wazo la kusoma Utendi wa Mikidadi na Mayasa. Ninazo tendi kadhaa, kuanzia za zamani kama vile Mwana Kupona, Fumo Liongo, na Ras il Ghuli, hadi za enzi zetu hizi. Ninapenda kuzisoma na kuzitafakari, sambamba na tungo za aina hiyo za mataifa mengine, kama vile Gilgamesh, Iliad na Odyssey, Sundiata, na Kalevala.

Nimeusikia Utendi wa Mikidadi na Mayasa tangu zamani. Sijui lini nilinunua nakala yangu ya utendi huu, lakini sikupata wasaa wa kuusoma. Kwa kuupitia haraka haraka, nimeona kuwa una mambo yanayofanana na yale yaliyomo katika tendi zingine maarufu za ki-Swahili kama Ras il Ghuli. Kwa mfano, dhamira ya mapigano kama njia ya kuthibitisha ushujaa imejengeka katika Utendi wa Mikidadi na Mayasa, kama ilivyo katika Utendi wa Ras il Ghuli.

Mayasa ni shujaa mwanamke anayenikumbusha shujaa mwanamke aitwaye Dalgha katika Utendi wa Ras il Ghuli. Wote wawili ni wapiganaji hodari na hatari sana, ambao yeyote anayetaka kuwaoa sherti kwanza apigane nao na kuwashinda. Hata ungekuwa mwanamme hodari na jasiri kiasi gani, kupambana nao ni kama kujitakia aibu au kifo.

Baada ya kuonja mvuto wa  Utendi wa Mikidadi na Mayasa, ninajizatiti kuusoma kikamilifu. Nikiweka nidhamu nikamaliza kuusoma, nitafurahi kuandika juu yake katika blogu hii, angalau kifupi, kama nilivyoandika juu ya Tenzi Tatu za Kale.

Monday, November 23, 2015

Kutafsiri Fasihi

Dhana ya tafsiri si rahisi kama inavyoaminika na jamii. Wataalam wanaijadili, kwa misimamo tofauti. Kuna vitabu na makala nyingi juu ya nadharia za tafsiri na shughuli ya kutafsiri. Kati ya vitabu vyangu, kuna ninachopenda kukipitia, kiitwacho Theories of Translation, ambacho ni mkusanyo wa insha za watu kama Johann Wolfgang von Goethe, Friedrich Nietzsche, Walter Benjamin, Roman Jakobson, Michael Riffaterre na Jacques Derrida.

Insha hizi zinafikirisha. Jose Ortega y Gasset, kwa mfano, anasema kuwa kutafsiri ni jambo lisilowezekana. Ni kama ndoto. Ni kujidanganya. Walter Benjamin anauliza masuali mengi magumu. Derrida, katika insha yake juu ya Mnara wa Babel, iliyotafsiriwa na Joseph F. Graham, anaandika:

          The "tower of Babel" does not merely figure the irreducible multiplicity of tongues; it exhibits an incompletion, the impossibility of finishing, of totalizing, of saturating, of completing something on the order of edification, architectural construction, system and architectonics. What the multiplicity of idioms limits is not only a "true" translation, a transparent and adequate inter-expression, it is also a structural order, a coherence of construct. There is often (let us translate) something like an internal limit to formalization, an incompleteness of constructure. It would be easy and up to a certain point justified to see there the translation of a system in deconstruction.
          One should never pass over in silence the question of the tongue in which the question of the tongue is raised and into which a discourse on translation is translated.

Kutokana na uzoefu wangu wa kutafsiri hadithi za jadi za ki-Matengo, nami nimeanza kuelezea suala la kutafsiri hadithi. Ninatafsiri pia mashairi ya ki-Ingereza kwa ki-Swahili na mashairi ya ki-Swahili kwa ki-Ingereza. Ninawazia kujijengea msingi wa kuandika zaidi kuhusu kazi ya kutafsiri, na ndoto yangu hatimaye ni kutafsiri Utenzi wa Ras il Ghuli. Ninaamini kwamba kuutafsiri utenzi huu utakuwa ni mtihani mkubwa kuliko yote ambayo nimejaribu kufanya, na kitakuwa ni kipimo thabiti cha uwezo wangu. Ninahamasika na namna mabingwa kama Richmond Lattimore na Robert Fagles walivyotafsiri tenzi za The Iliad na The Odyssey.

Saturday, June 20, 2015

Msomaji Amenilalamikia

Leo alasiri nilikwenda Brooklyn Park, Minnesota, kuhudhuria mkutano wa bodi ya Afrifest Foundation ambayo mimi ni mwenyekiti wake. Tulifanyia mkutano wetu katika maktaba ya Brookdale.

Baada ya mkutano, nilipotoka nje kuelekea sehemu nilipopaki gari, alinikimbilia dada Latonya anayeonekana katika picha hapa kushoto, ambayo tulipiga miaka mitano iliyopita kwenye tamasha la Afrifest. Ni m-Marekani Mweusi kutoka Chicago, ila anaishi Minneapolis. Tulifahamiana miaka ile kwa kuwa naye alikuwa katika bodi ya Afrifest Foundation.

Hatukutegemea kama tungeonana leo, ghafla namna ile. Kwa hivi tulifurahi sana. Lakini hakupoteza muda, alianza kunihoji kwa nini siandiki sana katika blogu yangu ya ki-Ingereza kama zamani. Alisema, akimaanisha maandishi yangu ya kiSwahili, "Tunaona unaandika sana, na tunajua unaandika mambo ya maana, ila hatujui unachoandika. Inakuwa kama unatusahau marafiki zako wa-Marekani Weusi."

Kwa kweli, ingawa mazungumzo yalikuwa ya kirafiki, na hata kiutani, niliona kuwa alikuwa anaongea kwa dhati. Na sisi wa-Afrika ambao tunaishi Marekani tunafahamu kuwa wako wa-Marekani Weusi wengi ambao wanategemea sisi wa-Afrika tuwe na mshikamano nao, kama ndugu. Kwa hivi, sikuyachukulia malalamiko ya Latonya kama mzaha. Nilijikuta nikikiri kosa na kuahidi kuwa nitakuwa naandika kama zamani. Alivyowataja wa-Marekani Weusi hakuwa anatunga hadithi. Ninafahamu kuwa wanasoma maandishi yangu.

Latonya mwenyewe ni mmoja wa wafuatiliaji wa dhati wa maandishi yangu. Hapo pichani, anaonekana ameshika kitabu changu cha Africans and Americans:Embracing Cultural Differences, mara baada ya kukinunua. Maneno aliyoniambia leo yameniingia. Nilimwambia hivyo, nikaahidi kujirekebisha.

Friday, June 5, 2015

Ninaombwa Tafsiri ya Kitabu Changu

Mara kadhaa, wa-Marekani wameniuliza iwapo kitabu changu Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kimetafsiriwa kwa ki-Swahili au wameniomba nikitafsiri. Hao ni watu ambao wameishi au wanaishi Afrika Mashariki, hasa kwa shughuli za kujitolea.

Tangu nilipoanza kupata maulizo au maombi hayo, nimekuwa na wazo la kukitafsiri kitabu hiki. Mwanzoni kabisa, kwa kuzingatia uwingi wa wa-Somali walioingia na wanaendelea kuingia hapa Minnesota, ambao nimekuwa nikiwasaidia katika kuufahamu utamaduni wa Marekani, niliwazia kumwomba mmoja wa marafiki zangu wa ki-Somali atafsiri kitabu hiki kwa ki-Somali. Ninao marafiki kadhaa wa ki-Somali ambao, sawa na wa-Afrika wengine, wamekisoma na wanakipenda kitabu hiki. Lakini bado sijalitekeleza wazo hilo.

Jana nimepata ujumbe wa aina hiyo kutoka kwa mama mmoja m-Marekani, ambaye simfahamu. Ninanukuu sehemu ya ujumbe wake, na nimeweka nukta nne mahali ambapo kuna maneno ambayo sijayanukuu:

....I hope one day that you will translate your wonderful book. It is such a wealth of knowledge for me, and I know my Tanzanian friends would feel the same. Of course most good people would never mean to hurt or offend a new acquaintance, but sometimes when we are lucky enough to make a friend from a different country, we can use a little guidance on how to be respectful of each others cultural differences. Your book has given me that gift, and so I thank you for that!....Last year I went to Africa for the wildlife, but I found it was the Tanzanian people who stole my heart. This year I will return and visit Eli's village and meet his family. I am so excited about my visit. That is why it is so important to me to do my best to not be the classic "UGLY AMERICAN". Thank you again for your response. I hope you will consider writing the Kiswahili version of your book in the future. I know there would be many people who would find it both helpful and fascinating, as I did....

Natafsiri ujumbe huu ifuatavyo:

....Natumaini siku moja utakitafsiri kitabu chako murua. Ni hazina kubwa ya maarifa kwangu, na ninajua kuwa marafiki zangu wa-Tanzania watakiri hivyo. Ni wazi kuwa watu wengi wenye roho nzuri hawanuii kumuumiza au kumkosea mtu pindi wanapofahamiana, lakini mara nyingine tunapobahatika kumpata rafiki kutoka nchi nyingine tunaweza kunufaika na mwongozo wa namna ya kuheshimiana kutokana na tofauti za tamaduni zetu. Kitabu chako kimekuwa tunu ya aina hiyo, na nakushuru kwa hilo....Mwaka jana nilikwenda Afrika kuwaona wanyama mbugani, lakini waliouteka moyo wangu ni wa-Tanzania. Mwaka huu nitaenda tena kijijini kwa Eli na kukutana na familia yake. Ninafurahi sana ninavyoingojea safari hiyo. Ndio maana ni muhimu sana kwangu kujitahidi kwa namna yoyote kutokuwa yule anayefahamika kama "M-MAREKANI WA OVYO." Narudia kukushukuru kwa jawabu lako. Ninatumaini utalichukulia maanani suala la kuandika toleo la ki-Swahili la kitabu chako siku zijazo. Ninajua kitabu hiki kitawasaidia na kuwasisimua wengi kama ilivyokuwa kwangu....

Kwa wale ambao hawafahamu, hii dhana ya "Ugly American" imejengeka sana katika mawazo ya wa-Marekani wanaoamini kuwa tabia ya wa-Marekani wanapokuwa nje za kigeni si nzuri. Dhana hiyo ilishamiri baada ya kuchapishwa kwa kitabu cha Eugene Burdick na William J. Lederer kiitwacho The Ugly American.

Sina la nyongeza la kusema kwa leo, bali kujiuliza: mimi ni nani niyapuuze maombi ya watu? Ninapaswa kuchukua hatua stahiki, nikizingatia ule usemi maarufu wa ki-Latini: "Vox Dei vox populi," yaani sauti ya umma ni sauti ya Mungu.

Tuesday, May 12, 2015

Vitabu vya Shaaban Robert

Jina la Shaaban Robert ni maarufu miongoni mwa wa-Tanzania na wengine wa nchi zingine wanaokijua ki-Swahili. Lakini, tujiulize ni wa-Tanzania wepi ambao wamesoma angalau vitabu vichache vya Shaaban Robert. Ni wangapi wamesoma au wanasoma mashairi yake, tenzi zake, insha zake, barua zake, na riwaya zake?

Ni wangapi wamesoma vitabu vyake vingine, kama vile Wasifu wa Siti Binti Saad, Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini, na tafsiri yake ya mashairi ya Omar Khayyam? Kama hatuna majibu ya kuridhisha, tuache kujigamba, kujidanganya na kudanganyana kuwa tunamwenzi mwandishi wetu huyu maarufu.

Ingawa kulikuwa na kipindi cha uhaba, leo vitabu vya Shaaban Robert vinapatikana kirahisi Tanzania, baada ya kampuni ya uchapishaji ya Mkuki na Nyota kuanza kuvichapisha upya. Mwaka hadi mwaka, ninapokwenda Tanzania, nimekuwa nikijinunulia vitabu hivyo, kama hivi vinavyoonekana pichani, sambamba na vitabu vya waandishi wengine maarufu katika lugha ya ki-Swahili.

Imekuwa ni faraja kwangu kuvisoma, baada ya kuzinduka kutoka katika mazoea ya kusoma zaidi maandishi ya ki-Ingereza. Ninajiona kama vile nimeanza kujikomboa kimawazo. Lugha yako ni utambulisho wako, na kuifahamu na kuitumia vizuri ni ishara ya kuiheshimu lugha hiyo. Ni ishara ya kujiheshimu.

Pamoja na kununua na kusoma vitabu alivyoandika Shaaban Robert, ninajitahidi kupanua akili yangu kwa namna nyngine pia. Ninayo maandishi yanayochambua maandishi ya Shaaban Robert. Mfano ni vitabu vinavyoonekana hapa pichani, kimoja cha A.G. Gibbe, na kingine cha Clement Ndulute. Maandishi mengine yamo katika majarida na vitabu vingine ambavyo baadhi ninavyo pia.

Ninajitahidi, kwa uwezo wangu, kushiriki katika kuandika kuhusu kazi za Shaaban Robert. Nimechapisha insha juu ya Shaaban Robert katika Encyclopaedia of African Literature iliyohaririwa na Simon Gikandi. Katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, kuna pia insha yangu iitwayo "Shaaban Robert: Mwalimu wa Jamii." Kadiri nitakavyokuwa naendelea kusoma maandishi yake, nategemea kuandika zaidi. Nina nafasi nzuri ya kufanya hivyo kwa kuwa ni mwalimu wa fasihi za kimataifa na nadharia ya fasihi.

Tuesday, February 17, 2015

Tatizo si Lugha ya Kufundishia, ni Uzembe

Jana, katika blogu hii, mdau mmoja aliniomba niandike makala kuhusu lugha ya kufundishia nchini Tanzania. Aliandika hivi:

Prof Mbele. Pole na kazi za kila siku.
Ningependa kujua nini maoni yako kuhusu kutumia kiswahili kama lugha kuu ya kufundishia mpaka chuo kikuu. Je unalionaje hili, unaona kutakuwa na athari zozote kutokana na elimu?. Je ni kweli tutakuwa tumejitenga na dunia?.

Ningeomba kama ungepata nafasi basi ukaliandika hili kama post katika blog na wala si comment. Nakutakia siku njema


Kwa kweli mada hii ya lugha ya kufundishia Tanzania imejadiliwa sana, katika vitabu, majarida, magazeti, mitandao, mikutano, na kadhalika. Siamini kama ninaweza kusema lolote ambalo halijasemwa. Hata hivi, nina mtazamo wangu, kama watu wengine.

Ninaamini kwa dhati kuwa tatizo si lugha ya kufundishia bali uzembe. Ingekuwa watu wanatambua umuhimu wa elimu, kwa maana halisi ya elimu, hawangekuwa wanatoa visingizio au lawama kama wanavyofanya. Hawangekuwa wanatumia muda wao katika kulalamika. Wangeelekeza nguvu zao na akili zao katika kutatua matatizo yoyote na kusonga mbele.

Kwamba mwanafunzi anafanya vizuri akifundishwa kwa lugha yake, ni hoja inayovutia, lakini sina hakika kama ninaikubali sana. Ingekuwa ninaikubali sana au kabisa, ningesema basi tuwafundishe watoto wetu kwa ki-Nyakyusa, ki-Sukuma, ki-Yao, na kadhalika. Kwa wengi, ki-Swahili ni lugha yao ya pili. Sisi hatukufundishwa kwa lugha mama, bali tulifundishwa kwa lugha ngeni ya ki-Swahili na baadaye ki-Ingereza, na hatukutetereka. Kwa nini mambo yawe kinyume leo, kama si uzembe?

Kama lugha ya ki-Ingereza ni tatizo, jawabu ni kufanya bidii kujifunza lugha hiyo. Kusema kwamba tuache kufundishia kwa ki-Ingereza eti kwa vile ufahamu wa ki-Ingereza ni mdogo ni kuhalalisha uzembe. Kinachotakiwa ni kufanya bidii kujifunza lugha hiyo kama tulivyokuwa tunafanya sisi.

Uzembe umetufikisha hapa tulipo. Kwa nini majirani zetu wa Malawi, Kenya, na Uganda hawatoi visingizio kama wanavyotoa wa-Tanzania? Ki-Ingereza sio lugha ya wenzetu hao, bali ki-Chewa, ki-Yao, ki-Ganda, ki-Acholi, ki-Kamba, Kikuyu, na kadhalika, kama ilivyo kwetu ki-Pare, ki-Luguru, ki-Makonde na kadhalika.

Kwa nini hao majirani zetu wawe wanatumia ki-Ingereza hadi chuo kikuu bila malalamiko kama wanayotoa wa-Tanzania? Enzi zetu, tulikuwa tunasomeshwa kwa ki-Ingereza sekondari (au kabla?)na kuendelea. Tulisoma chuo kikuu na hao wenzetu kutoka nchi za jirani, kwa ki-Ingereza bila matatizo. Leo ki-Ingereza kimekuwa shida. Ni nini kimetokea, kama si uzembe?

Ingawa nina mengine ya kusema, ninaamini kuwa blogu ni mahali pa makala fupi fupi, tofauti na kitabu. Kwa leo naona niishie hapa. Nitaendelea kuandika, ili kuongelea vipengele vya ujumbe wa mdau ambavyo sijavigusia hapa.

Thursday, November 27, 2014

Kitabu Changu cha Ki-Swahili

Kitu kimoja ninachojivunia kama mwandishi ni juhudi niliyofanya kwa miaka mingi katika kuandika kwa ki-Swahili. Aliyenihamasisha na kunisukumia katika uandishi wa ki-Swahili ni rafiki yangu Mugyabuso Mulokozi, ambaye sasa ni profesa mstaafu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Tangu tulipokuwa tunasoma wote "Mkwawa High School," aliona jinsi nilivyokuwa nimezama katika ki-Ingereza bila kujibidisha upande wa ki-Swahili.

Hatimaye, hasa tulipokuwa chuo kikuu, ambapo yeye nami tulikuwa tunafundisha, nilijitosa katika ulimwengu wa ki-Swahili. Kwanza nilisoma maandishi ya ki-Swahili, kisha nikaanza kufanya utafiti na kuandika makala magazetini. Kati ya maandishi niliyochapisha ni mapitio ya tamthilia ya Kijiji Chetu, iliyotungwa na Ngalimecha Ngahyoma.

Baadaye, nilianza utafiti kuhusu tungo za zamani za ki-Swahili, kama vile Utenzi wa Fumo Liongo, Al-Inkishafi na Utenzi wa Ras il Ghuli. Utafiti huu niliuendeleza nilipokuwa nasomea shahada ya uzamifu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, huku Marekani, miaka ya 1980-86.

Hatimaye, kwa kuombwa na Ndugu Maggid Mjengwa, mmiliki na mwendeshaji wa Mjengwablog, niliandika makala katika gazeti aliloanzisha, Kwanza Jamii. Baadaye, makala hizi nilizikusanya na kuzichapisha kama kitabu kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Nilipochapisha kitabu hiki, niliandika taarifa katika blogu yangu ya ki-Ingereza.

Kuandika kwa ki-Swahili ni namna ya kuienzi lugha hii. Lugha ni utambulisho wa utaifa na ni kielelezo cha jinsi mtu unavyoheshimu utaifa wako na unavyojitambua na kujiheshimu wewe mwenyewe, kama alivyobainisha Frantz Fanon hasa katika vitabu vyake viwili: The Wretched of the Earth na Black Skin, White Masks.

Ninajivunia kitabu hiki kwa vile kimenipa fursa ya kupima uwezo wangu wa kuandika ki-Swahili sanifu. Ingawa bado naandika zaidi kwa ki-Ingereza, sijarudi nyuma katika uandishi wa ki-Swahili. Mbali na hili suala la kujitambua na kujitambulisha kwa kuienzi lugha yetu kwa vitendo, kitabu hiki kilitokana pia na msukumo wa watu waliokuwa wananiuliza kwa nini naandika kwa ki-Ingereza tu. Watu hao waliniambia kuwa ingekuwa bora niandike pia kwa ki-Swahili, ili wa-Tanzania walio wengi waweze kuyaelewa mawazo yangu. Nami niliona hii ni hoja nzuri.

Hata hivi, kitabu hiki hakijapata wasomaji wengi. Labda hii ni kwa sababu nilikichapisha huku Marekani, mtandaoni. Kama hili ndilo tatizo, napenda kusema kuwa kitabu hiki, sawa na vitabu vyangu vingine, kinapatikana kutoka kwangu, kwa anwani hii: africonexion@gmail.com au simu namba (507) 403 9756.

Lakini pia kuna suala la kukosekana kwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu miongoni mwa wa-Tanzania, jambo ambalo limekuwa likisemwa na wahusika mbali mbali katika sekta ya vitabu. Tungekuwa na utamaduni huu, tungeona tahakiki na mijadala kuhusu vitabu, sio tu miongoni mwa wanafunzi na wasomi, bali katika jamii, kupitia vyombo vya habari, magazeti, na mitandao ya mawasiliano.

Monday, March 25, 2013

Toleo Jipya la "Kioo cha Lugha"

Siku chache ziilizopita, nilipata nakala ya jarida la Kioo cha Lugha, kutoka Taasisi ya Taaluma za Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mimi ni mwanakamati katika kamati ya uhariri wa jarida hilo. Ni furaha kubwa kwangu kushirikiana na wanataaluma wenzangu katika mambo ninayoyapenda. Masuala ya la lugha, fasihi, utamaduni, na falsafa yana nafasi ya pekee katika maisha yangu.















Toleo hili la Kioo cha Lugha lina makala nyingi, kama inavyoonesha katika picha hii hapa kushoto. Wanaodhani kuwa ki-Swahili kina mapungufu katika kuelezea taaluma mbali mbali, watafakari upya suala hilo, hasa kwa kusoma machapisho kama yale yatokayo katika Taasisi ya Taaluma za Kiswahili, ambayo ni ya taaluma mbali mbali. Niliwahi kugusia suala hilo katika ujumbe huu hapa.

Wednesday, January 19, 2011

Andika ki-Swahili; ki-Ingereza Hatuelewi

Kuna tabia katika jamii ya wa-Tanzania ya kulalamika pale mtu anapoandika ki-Ingereza. Malalamiko haya yanaonekana mara kwa mara katika blogu ya Michuzi, kwa mfano, ambayo inasomwa sana na wa-Tanzania, pale inapotokea makala iliyoandikwa kwa ki-Ingereza.

Walalamikaaji wanakumbushia kuwa wa-Tanzania wengi hawajui ki-Ingereza, na kwa hivi wanataka mwandishi awafikirie hao kwa kuandika kwa ki-Swahili, lugha wanayoifahamu. Ujumbe unaojitokeza katika malalamiko hayo ni kwamba ni jambo la uzalendo kwa mwandishi kuwafikiria hao wa-Tanzania walio wengi, ili nao wapate kufaidika na yale yanayoandikwa.

Sijawahi kuona malalamiko hayo yakipingwa. Inaonekana kuwa hoja inayotolewa katika malalamiko hayo inakubalika miongoni mwa wa-Tanzania.

Katika kulitafakari suala hili, naona kuna haja ya kuwakosoa hao walalamikaji. Ingawa ni kweli kuwa mtu akiandika kwa ki-Swahili anawafikia wananchi wasiojua ki-Ingereza, kuna pia tatizo la uvivu katika jamii yetu.

Malalamiko hayo ni sehemu ya tatizo hili la uvivu ambalo naliongelea tena na tena katika blogu hii na zingine, na pia katika maandishi mengine. Wa-Tanzania wanapenda kutafuta visingizio na kuwalaumu wengine. Kwa nini wa-Tanzania waridhike na hali yao, ya kujua ki-Swahili tu, badala ya kujifunza lugha zingine?

Kama wa-Tanzania wanataka kudekezwa, ni bora wajue kuwa dunia hii ya ushindani haidekezi mtu. Wasipojituma katika masuala ya elimu, ikiwemo elimu ya lugha mbali mbali, sio tu watabaki nyuma, bali wataumia. Mawasiliano ya kimataifa yatakuwa mtihani mkubwa ambao watashindwa. Mikataba ya nje watashindwa kuielewa.

Wakati huu tunanyoosheana vidole kutokana na mikataba tunayohisi waTanzania wenzetu wanaisaini kifisadi. Lakini, kwa jinsi tunavyoendekeza uvivu ninaoongelea, tutaendelea kusaini mikataba mibovu kwa kutojua lugha. Nchi itaendelea kuumia.

Hata kama watu hawana vitabu, kuna maktaba katika miji mbali mbali. Mtu yeyote anaweza kujipangia utaratibu wa kwenda kusoma vitabu vilivyomo, akajiongezea angalau ufahamu wa ki-Ingereza. Lakini wa-Tanzania wako radhi kukaa kwenye kijiwe nje ya maktaba, siku hadi siku, wiki hadi wiki, mwezi hadi mwezi, mwaka hadi mwaka, bila kuingia humo maktabani. Hili ni tatizo kubwa katika nchi yetu.

Thursday, September 23, 2010

Nimeipata Nakala ya "Tendehogo."

Nilipokuwa Tanzania mwaka huu, nilikutana na rafiki yangu, mwandishi Edwin Semzaba, kama nilivyoandika hapa. Jambo moja tuliloongelea ni kutafsiri tamthilia yake ya Tendehogo. Basi, niliporejea hapa chuoni St. Olaf ninapofundisha, nilienda maktaba na kuagiza nakala ya tamthilia hii. Kwa vile nakala haiko hapa, waliniagizia kutoka Maktaba ya Congress iliyoko Washington DC.

Nimeshapata nakala hiyo, na sasa inabidi nianze mikakati ya kuitafsiri. Kazi ya kutafsiri kazi ya fasihi ni ngumu, yenye changamoto nyingi, hata kama mtu unazijua lugha husika vizuri sana. Hata kama lugha husika ni zako za kuzaliwa nazo au za tangu utotoni, kama kilivyo ki-Matengo na ki-Swahili kwa upande wangu.

Ninasema hivyo kutokana na uzoefu. Nimejishughulisha na kutafsiri tungo za ki-Swahili na hadithi za ki-Matengo kwenda ki-Kiingereza. Niliwahi hata kuandika makala kuhusu kutafsiri hadithi ya ki-Matengo. Soma hapa.

Miaka michache iliyopita nilianza kutafsiri Tendehogo, lakini nakumbuka nilitafsiri kurasa labda mbili au tatu. Sasa, pamoja na wasi wasi nilio nao kuhusu uwezo wangu, itabidi nijipige moyo konde na kuanza kuogelea.

Saturday, August 14, 2010

Nimefika Lutheran Junior Seminary, Morogoro

Juzi nilienda Lutheran Junior Seminary, Morogoro, kuangalia kitengo cha ufundishaji wa ki-Swahili na Utamaduni.

Kwa miaka mingi nilifahamu habari za kitengo hiki, kupitia mtandao wao, ila sikuwahi kuwatembelea. Nilifurahi kuonana na walimu na kutembezwa katika mazingira ya shule.


Kwa vile ninashughulika na program za kuleta wanafunzi wa Marekani hapa Tanzania na kwingineko Afrika, niliona ni muhimu nipate ufahamu mzuri wa kitengo hiki cha Morogoro, endapo tutahitaji kuwaleta wanafunzi wetu.

Nilitambulishwa kwa mwalimu ambaye alikuwa darasani akiwafundisha wageni somo la utamaduni. Kumbe anakifahamu kitabu changu cha Africans and Americans na anakitumia. Nilifurahi kuona kuwa niliyoandika yanawanufaisha wengi, hadi huku Morogoro.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...