Showing posts with label utumwa. Show all posts
Showing posts with label utumwa. Show all posts

Wednesday, December 23, 2015

Ninajivunia Binti Huyu: Bukola Oriola

Nimefurahi kupata taarifa kuwa Rais Obama amemteua Bukola Oriola, kuwa mjumbe katika tume ya kumshauri kuhusu masuala ya usafirishwaji wa ghilba na utumikishwaji wa binadamu, kama ilivyotangazwa katika taarifa hii. Bukola ni binti kutoka Nigeria anayeishi hapa Minnesota, Marekani. Nimemfahamu tangu mwaka 2009, kwa kusoma taarifa zake katika magazeti ya wa-Afrika hapa Minnesota.

Niliguswa kwa namna ya pekee niliposoma kauli yake kuwa alikuwa ameandika mswada wa kitabu bali hakujua auchapishe vipi. Kwa kuwa nilikuwa na uzoefu wa kujichapishia vitabu, dhamiri yangu ilinisukuma niwasiliane naye ili nimsaidie. Nilielezea kisa hicho katika blogu hii.

Baada ya kitabu chake, Imprisoned: The Travails of a Trafficked Victim kuchapishwa, niliendelea kumhamasisha. Kwa mfano, nilimwalika kwenye tamasha la vitabu mjini Minneapolis tarehe 10 Oktoba, 2009, ambalo nilikuwa nashiriki. Nilitaka yeye kama mwandishi chipukizi aone na kujifunza kazi inayomngoja mwandishi baada ya kuchapisha kitabu. Alikuja, tukapiga picha inayoonekana hapa kushoto tukiwa kwenye meza yangu.

Kitabu kilimfungulia milango. Alikuwa anazunguka sehemu mbali mbali kutoa mihadhara kuhusu utumwa na mateso wanayopata wanawake wanaorubuniwa, kutoroshwa, kutekwa, na kisha kutumikishwa na kunyanyaswa. Alianzisha kipindi cha televisheni na pia taasisi aliyoiita The Enitan Story. Yote hayo ni kwa ajili ya kuwasaidia waathirika na kuielimisha jamii kuhusu tatizo hili ambalo limeota mizizi duniani.

Ninafurahi kwa mafanikio ya binti huyu. Naye, kwa kukumbuka nilivyomsaidia, aliandika ifuatavyo katika utangulizi wa kitabu chake:

     I would also like to thank those who worked with me to get this book published. My profound gratitude goes to Prof. Joseph Mbele of St. Olaf College, Northfield, Minnesota, who showed me how to get my book published, otherwise it would have been another Word Document on my computer. It would have not been able to give the message of hope to the hopeless. God bless you sir.

Kitendo cha Rais Obama kumteua Bukola kwenye tume hiyo ni heshima kubwa kwake. Hapa Minnesota na Marekani kwa ujumla watu wamezipokea taarifa hizi kwa furaha. Nchini kwake Nigeria taarifa hii imekuwa kishindo katika vyombo vya habari. Kwa upande wangu, naona fahari kuwa niliitikia wito wa dhamiri yangu nikamwelekeza namna ya kuchapisha kitabu ambacho kilichangia na bado kinachangia mafanikio yake. Mungu ni mkubwa.

Bukola mwenyewe anatambua kuwa kuna mkono wa Mungu katika mambo anayopitia na kuyashuhudia maishani. Anaamini kuwa ana wajibu mbele ya Mungu wa kuwasaidia wanyonge, na kuwa mtetezi wa wanaonyanyaswa na kudhulumiwa. Msikilize anavyojieleza:

Wednesday, December 7, 2011

Hifadhi za Historia Bagamoyo

Bagamoyo ni mji maarufu katika historia ya nchi yetu na dunia. Kwa mtu anayetaka kujifunza historia hiyo, napendekeza ziara Bagamoyo kuangalia hifadhi zilizopo. Mwaka huu, nilitembelea Bagamoyo, na wanafunzi kutoka Marekani, kama nilivyoelezea hapa. Mahali pamoja tulipotembelea ni Caravan Serai, hifadhi mojawapo ya historia. Hapa kushoto ninaonekana mbele ya mlango wa kuingilia Caravan Serai. Kuna sanamu ya mtumwa aliyebeba pembe ya ndovu.


Hapa kushoto tunaonekana katika eneo la Caravan Serai, tukiwa na mfanyakazi wa hifadhi hiyo, ambaye alikuwa anatuonyesha na kutuelezea yaliyomo.















Hapa anaonekana mtaalam wetu akitoa maelezo ya historia ya Caravan Serai.












Humo ndani kuna nyaraka, picha na vitu mbali mbali, kama vile vyombo vya nyumbani, na maelezo kuhusu vitu hivyo. Hapa kushoto, katika picha ya katikati, anaonekana Tippu Tip.










Hapa kushoto ni picha ya watumwa.













Hapa kushoto ni picha ya "bangili," kwa mujibu wa bandiko la maelezo, ambazo walikuwa wakivalishwa watumwa shingoni na kuunganishwa na watumwa wengine kwa mnyororo.










Hapa kushoto ni baadhi ya vitu vya nyumbani.













Vitu ni vingi katika hifadhi hii, na maandishi. Mtu ukiingia hapo, ukaangalia na kusoma yaliyomo, na kusikiliza maelezo, utajikuta umeelimika kutosha.

Hii Caravan Serai ni hifadhi mojawapo tu; kuna nyingine, kama vile ya Kanisa Katoliki, ambayo nimeisikia kwa miaka mingi, na niliiona kwa nje mwaka juzi. Napangia kuingia ndani yake na kuangalia siku za usoni.

Thursday, September 23, 2010

Nimeipata Nakala ya "Tendehogo."

Nilipokuwa Tanzania mwaka huu, nilikutana na rafiki yangu, mwandishi Edwin Semzaba, kama nilivyoandika hapa. Jambo moja tuliloongelea ni kutafsiri tamthilia yake ya Tendehogo. Basi, niliporejea hapa chuoni St. Olaf ninapofundisha, nilienda maktaba na kuagiza nakala ya tamthilia hii. Kwa vile nakala haiko hapa, waliniagizia kutoka Maktaba ya Congress iliyoko Washington DC.

Nimeshapata nakala hiyo, na sasa inabidi nianze mikakati ya kuitafsiri. Kazi ya kutafsiri kazi ya fasihi ni ngumu, yenye changamoto nyingi, hata kama mtu unazijua lugha husika vizuri sana. Hata kama lugha husika ni zako za kuzaliwa nazo au za tangu utotoni, kama kilivyo ki-Matengo na ki-Swahili kwa upande wangu.

Ninasema hivyo kutokana na uzoefu. Nimejishughulisha na kutafsiri tungo za ki-Swahili na hadithi za ki-Matengo kwenda ki-Kiingereza. Niliwahi hata kuandika makala kuhusu kutafsiri hadithi ya ki-Matengo. Soma hapa.

Miaka michache iliyopita nilianza kutafsiri Tendehogo, lakini nakumbuka nilitafsiri kurasa labda mbili au tatu. Sasa, pamoja na wasi wasi nilio nao kuhusu uwezo wangu, itabidi nijipige moyo konde na kuanza kuogelea.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...