Showing posts with label kumbukumbu. Show all posts
Showing posts with label kumbukumbu. Show all posts

Wednesday, October 10, 2018

Naambiwa Niongeze Bei ya Kitabu

Katika matamasha ya vitabu ninayoshiriki, ninakutana na mambo mengi, zikiwemo tabia na mitazamo ya wateja. Moja ambalo linanigusa zaidi ni pale mteja anaposhauri niongeze bei ya kitabu changu. Hiyo imetokea mara kadhaa, kuhusiana na vitabu vyangu viwili: Africans and Americans: Embracing Cultual Differences na Matengo Folktales.

Vitabu hivi ninaviuza kwenye matamasha kwa dola 14 kila kimoja. Kwa kujua kwamba watu wengine wanatoa  noti ya dola 20 au noti mbili za dola kumi kumi, ninajitahidi kuwa na chenji. Ajabu ni kwamba watu wengine hawasubiri chenji, na wengine wanakataa. Wanachotaka ni kitabu waende zao. Ninakumbuka watu waliowahi kutoa noti ya dola 20 bila kutaka chenji. Mmoja wa hao, nilipojiandaa kumpa chenji, alisema hiyo chenji ni shukrani yake kwangu kwa kuandika kitabu.

Tarehe 4 mwezi huu nilikutana na jambo jingine kabisa. Mama moja, Jackie, ambaye nimemfahamu miezi michache iliyopita na akasoma hivi vitabu vyangu viwili, alinialika kwenye mhadhara wa rafiki yake Maria kuhusu vitabu na maisha yake. Alikuwa ameniambi nije na nakala za vitabu vyangu, ili aweze kuvipeleka katika tamasha la vitabu. Baada ya mhadhara, wakati tulipokuwa tunajumuika kwa viburudisho na maongezi, Jackie akanulizia bei ya vitabu vyangu, nami nikamwambia kuwa ni dola 14. Alisema nipandishe iwe 15, kwa ulinganisho na kitabu cha dola 10 na pia kwa urahisi wa chenji.

Alinitambulisha kwa rafiki yake, akamwambia kuhusu hivi vitabu vyangu. Alivyokuwa akielezea hayo, akaniambia nivitoe kwenye begi, nikampa. Huyu rafiki alichagua Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, akapanda ngazi kwenda kuchukua hela akaja akanipa na kitabu akachukua. Dakika chache baadaye, mama huyu alinitambulisha kwa mama mwingine, na akamwambia kuhusu vitabu. Naye akanunua Matengo Folktales.

Kwa hivyo nimejikuta nikiafiki wazo la kuongeza bei ya vitabu vyangu. Hata hivyo, bei hiyo ni ndogo kulingana na bei za mahali pengine za vitabu hivyo. Ninaamini kuwa taarifa hii ina ujumbe kuhusu watu wanaothamini vitabu kuliko fedha. Kama nilivyowahi kusema tena na tena, blogu hii ni sehemu ambapo ninajiwekea mambo yangu binafsi, kama vile kumbukumbu, hisia, na mitazamo. Ikitokea haja, siku zijazo, ya kuandika kitabu kuhusu maisha na kazi zangu, blogu hii itakuwa chanzo muhimu cha taarifa.

Saturday, April 8, 2017

Mwaliko Chuo Kikuu cha Winona

Tangu mwaka uanze, nimetoa mihadhara au kufanyiwa mahojiano nje ya chuo ninapofundisha, mara nyingi kuliko kawaida. Nilitegemea kuwa kuanzia mwezi huu wa Aprili, hali ingebadilika. Lakini dalili hazionyeshi mabadiliko.

Tarehe 6, nilipata mwaliko kutoka kwa Alex Hines, mkuu wa idara ya Inclusion and Diversity katika Chuo Kikuu cha Winona, wa kwenda kutoa mhadhara:

We would like to extend an invitation for you to attend HOPE Academic & Leadership Academy during the week of June 26th through June 29th and conduct a two hour presentation from 7-9 p.m. on Embracing African and African American Culture.

Hii itakuwa ni mara ya tatu mimi kwenda kutoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Winona. Mara ya kwanza, niliongelea masuala ya utamaduni kama nilivyoyaeleza katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Mara ya pili, niliongelea mahusiano ya binadamu na uongozi, kwa kutumia kitabu cha Matengo Folktales, kama nilivyoandika katika blogu hii

Mwaliko huu wa sasa, kama ilivyoelezwa katika barua niliyonukuu hapa juu, msingi wake ni kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Alex Hines, tangu tulipofahamiana, miaka mingi iliyopita, amekuwa ni mmoja wa wale wanaonitegemea katika programu zao. Ninafurahi kwa imani ya wadau juu yangu, nami ninahamasika kufanya makubwa zaidi kwa ajili yao.

Blogu hii ni mahali ninapohifadhi kumbukumbu zangu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii. Labda kuna siku nitapata wazo la kuandika kitabu kuhusu shughuli zangu. Ikitokea hivyo, kumbukumbu hizi zitanifaa.

Wednesday, May 18, 2016

Muhula Unaisha; Umebaki Utafiti

Jana tumemaliza muhula wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Nilikuwa ninafundisha "Folklore," Muslim Women Writers, na "First Year Writing." Kwa utaratibu wa chuo hiki, masomo matatu kwa muhula ndio kiwango cha juu kabisa. Hatufundishi zaidi ya masomo matatu. Kwa hivi, nilitegemea ningekuwa nimechoka, lakini sisikii uchovu. Alhamdulillah.

Kwa wiki nzima inayokuja, tutakuwa na mitihani. Baada ya hapo tutaanza likizo ndefu ya miezi mitatu na kidogo. Inaitwa likizo, lakini maprofesa tunaona ni wakati muafaka wa kufanya shughuli za kitaaluma kama utafiti na uandishi.

Nami nimeamua kwenda Boston kwa siku chache kufanya utafiti juu ya Ernest Hemingway katika maktaba ya John F. Kennedy. Humo kuna hifadhi kubwa kuliko zote duniani ya vitabu, miswada, picha na  kumbukumbu zingine zinazomhusu Hemingway. Ingawa nimefika Boston mara kadhaa, sijawahi kwenda katika maktaba hiyo maarufu.

Nina bahati kuwa ninafahamiana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway ambaye bado yuko hai. Yeye ndiye mmiliki wa haki zote za urithi wa Hemingway. Nilipomwambia kwa mara ya kwanza kwamba napangia kwenda kufanya utafiti katika maktaba ya John F. Kennedy,  aliniambia nimfahamishe ni lini ili anitambulishe kwa wahusika. Wiki chache zilizopita, katika maongezi yetu, nilimwambia tena kuwa napangia kwenda kwenye maktaba ile, alikumbushia kuwa nimweleze ni muda upi nitakwenda ili awafahamishe.

Ninashukuru sana kwa hilo, kwani katika kusoma taarifa za maktaba ile, nimefahamu kuwa kuna masherti yanayohusu kuitumia hifadhi ya Ernest Hemingway. Mtu hukurupuki tu ukafika pale na kufanya utafiti. Kuna baadhi ya kumbukumbu ambazo zimefungiwa. Mtafiti unahitaji kibali maalum kuweza kuzifanyia utafiti. Sherti nichukue hatua hima.

Monday, November 2, 2015

Hifadhi ya Majengo ya Kihistoria

Miezi kadhaa iliyopita, niliposikia kuwa jengo la CCM mtaa wa Lumumba, Dar es Salaam, limebomolewa ili kujengwa jengo la kisasa, nilifadhaika. Niliwazia utamaduni ninaouona hapa Marekani wa kuhifadhi majengo ya kihistoria. Nimeona katika miji wanahifadhi maeneo wanayoyaita "historic districts." Mfano ni picha zinazoonekana hapa, ambazo nilipiga mjini Faribault. Ninaona maeneo haya katika miji mingine pia.

Maeneo ya kihistoria, yenye majengo ya zamani, ni kumbukumbu ya historia ambayo inastahili kuhifadhiwa kwa ajili ya vizazi vijavyo. Vile vile, ni kivutio kwa watalii. Kwa mtazamo huo, nililiwazia jengo la awali la CCM Lumumba. Lilikuwa na umuhimu wa pekee katika historia za harakati za kupigania Uhuru. Ni jengo ambamo TANU ilizaliwa. Ni urithi wetu sote wa-Tanzania.

Sijui ni nani walioamua kulibomoa na kwa nini. Sijui kwa nini hawakutafuta sehemu nyingine ya kujenga hilo jengo la kisasa. Ninafahamu kuwa majengo yanaweza kuzeeka mno yakawa si salama kwa watu kuingia. Papo hapo, ninafahamu kuna aina za ukarabati ("restoration") zinazowezekana na jengo likabaki salama. Sidai kwamba nina sababu zaidi ya hizo nilizotoa, na labda mtu ataweza kusema kuwa sababu zangu ni zile ambazo kwa ki-Ingereza huitwa "sentimental."

Thursday, July 2, 2015

Leo ni Kumbukumbu ya Kifo cha Hemingway

Leo ni siku ya kumbukumbu ya kifo cha mwandishi Ernest Hemingway. Alikufa tarehe 2 Julai, mwaka 1961, nyumbani mwake Ketchum, Idaho. Alikufa katika nyumba nayoonekana pichani ambayo ilipigwa na Jimmy Gildea wakati wa safari zake za kuandaa filamu ya Papa's Shadow.

Maelezo ya namna Hemingway alivyokufa yanapingana kidogo. Kila mtu anakiri kuwa alikufa kwa risasi ya bunduki. Karibu kila mtu anasema kuwa Hemingway alijiua kwa kujipiga risasi, akiwa peke yake ghorofa ya juu.

Lakini mke wake, Mary Welsh Hemingway, ambaye wakati wa tukio alikuwa katika nyumba hiyo kwa chini, alitoa tamko kuwa ilikuwa ni ajali:

Mr. Hemingway accidentally killed himself while cleaning a gun this morning at 7:30 A.M. No time has been set for the funeral services, which will be private.

Kila ninapowazia kifo cha Hemingway, nakumbuka jinsi alivyokuwa na mikosi ya ajali katika maisha yake. Ninavyowazia kuwa alijiua, nakumbuka misiba kadhaa ya watu kujiua katika ukoo wa Hemingway. Ninawazia pia kuwa mimi nimeishi miaka mingi kumzidi Hemingway, ambaye alizaliwa mwaka 1899 akafa mwaka 1962.

Ninajiuliza nimefanya nini katika miaka yangu yote hii, nikijifananisha na Hemingway, ambaye alikuwa mwandishi maarufu aliyeongoza njia kwa aina yake ya uandishi, akapata tuzo ya Nobel mwaka 1954.

Hemingway aliongelea kifo, tena na tena, katika maandishi yake. Kauli yake moja inayojulikana zaidi ni hii:

Every man's life ends the same way. It is only the details of how he lived and how he died that distinguish one man from another.


Monday, June 1, 2015

Blogu Zangu Zimenisaidia

Hapa Chuoni St. Olaf kuna utaratibu unaomtaka kila mwalimu kuandika ripoti ya shughuli alizofanya katika mwaka wa shule unaoisha. Hizo ni shughuli za kitaaluma, yaani vitabu ulivyochapishwa, makala ulizochapisha, ushiriki wako katika mikutano ya kitaaluma, kazi ulizofanya katika uongozi wa vyama vya kitaaluma, kozi ulizotunga na kufundisha, uhariri katika majarida ya kitaaluma. Vile vile unaorodhesha huduma ulizotoa katika jamii nje ya chuo, kama vile ushauri ("consultancy"), na mihadhara katika mikutano ya vikundi na jumuia.

Nimekuwa na jadi ya kuandika mambo ya aina hiyo katika blogu hii ya hapakwetu na blogu ya ki-Ingereza. Katika kuandika ripoti yangu ya mwaka unaoisha, blogu zangu zimekuwa hazina ya kumbukumbu na taarifa nilizohitaji. Huu ni uthibitisho wa manufaa ya shughuli ninayofanya ya kublogu. Ninakumbuka kuwa niliwahi kuelezea namna blogu ilivyonisaidia darasani.

Watu wengine wanaandika kumbukumbu zao katika "diary." Lakini mimi kwa vile sina mazoea ya kufanya hivyo, nitaendelea kublogu kama ninavyofanya. Lengo ni kuhifadhi kumbukumbu. Tena, kwa kuwa nimezoea kuelezea shughuli zangu kwa upana, tangu chimbuko hadi matokeo, taarifa zangu zitaweza kutumika hata kwa kuandika kitabu. Ndoto ya kuandika kitabu cha aina hiyo nimekuwa nayo kitambo. Panapo majaliwa, nitaitekeleza.

Wednesday, March 11, 2015

Video ya Kumbukumbu ya Miaka Kumi ya Kitabu

Jana, binti yangu Zawadi na mimi tulirecodi video ya kumbukumbu ya miaka kumi tangu nilipochapisha kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Hatukuwazia tungefanya shughuli hiyo jana. Tulijishitukiza bila maandalizi. Tulitayarisha kompyuta nami nikaanza kuongea. Zawadi alifanya shughuli yote ya kiufundi hadi kuiweka video katika
mtandao wa You Tube.

Katika kumbukumbu hii ya miaka kumi ya kitabu changu, napenda kuwashukuru wasomaji wangu, familia, na marafiki na wengine wote walionihamasisha kwa namna moja au nyingine.

Kwa mwezi huu wote, yeyote anayetaka kitabu hiki, popote duniani, ataweza kukipata kutoka kwangu kwa bei nafuu ya dola 12. Awasiliane nami kwa barua pepe, africonexion@gmail.com au simu (507) 403 9756. Mwisho wa fursa hii ni tarehe 31.

Wednesday, December 7, 2011

Hifadhi za Historia Bagamoyo

Bagamoyo ni mji maarufu katika historia ya nchi yetu na dunia. Kwa mtu anayetaka kujifunza historia hiyo, napendekeza ziara Bagamoyo kuangalia hifadhi zilizopo. Mwaka huu, nilitembelea Bagamoyo, na wanafunzi kutoka Marekani, kama nilivyoelezea hapa. Mahali pamoja tulipotembelea ni Caravan Serai, hifadhi mojawapo ya historia. Hapa kushoto ninaonekana mbele ya mlango wa kuingilia Caravan Serai. Kuna sanamu ya mtumwa aliyebeba pembe ya ndovu.


Hapa kushoto tunaonekana katika eneo la Caravan Serai, tukiwa na mfanyakazi wa hifadhi hiyo, ambaye alikuwa anatuonyesha na kutuelezea yaliyomo.















Hapa anaonekana mtaalam wetu akitoa maelezo ya historia ya Caravan Serai.












Humo ndani kuna nyaraka, picha na vitu mbali mbali, kama vile vyombo vya nyumbani, na maelezo kuhusu vitu hivyo. Hapa kushoto, katika picha ya katikati, anaonekana Tippu Tip.










Hapa kushoto ni picha ya watumwa.













Hapa kushoto ni picha ya "bangili," kwa mujibu wa bandiko la maelezo, ambazo walikuwa wakivalishwa watumwa shingoni na kuunganishwa na watumwa wengine kwa mnyororo.










Hapa kushoto ni baadhi ya vitu vya nyumbani.













Vitu ni vingi katika hifadhi hii, na maandishi. Mtu ukiingia hapo, ukaangalia na kusoma yaliyomo, na kusikiliza maelezo, utajikuta umeelimika kutosha.

Hii Caravan Serai ni hifadhi mojawapo tu; kuna nyingine, kama vile ya Kanisa Katoliki, ambayo nimeisikia kwa miaka mingi, na niliiona kwa nje mwaka juzi. Napangia kuingia ndani yake na kuangalia siku za usoni.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...