Showing posts with label Ernest Hemingway. Show all posts
Showing posts with label Ernest Hemingway. Show all posts

Saturday, October 28, 2017

Papa's Shadow: Filamu Kuhusu Ernest Hemingway

Kampuni ya Ramble Pictures, ambayo inatengeneza filamu, imemaliza kutengeneza filamu inayohusu safari za mwandishi Ernest Hemingway Afrika Mashariki miaka ya 1933-34 na 1953-54. Nilishaandika taarifa za awali kuhusu filamu hiyo katika blogu hii.

Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina ya Mzee Patrick Hemingway na mimi kuhusu safari hizo za Ernest Hemingway, falsafa yake juu ya maisha na sanaa. Patrick Hemingway ni moto pekee wa Ernest Hemingway aliye bado hai. Filamu inaelezea mambo juu ya mwandishi Ernest Hemingway ambayo yalikuwa hayafahamiki vizuri, hasa juu ya namna mwandishi huyu alivyoipenda Afrika.

Filamu hii inaitangaza Tanzania, kwa kuwa inaonyesha maeneo kadhaa ya nchi na watu wake, pamoja na safari ya kupanda Mlima Kilimanjaro. Chimbuko muhimu la filamu hii ni kozi niliyotunga na kufundisha iitwayo Hemingway in East Africa. Nilisafiri na wanafunzi 29 wa chuo cha St. Olaf, ninapofundisha, tukawa tunapita katika maeneo kadhaa ya Tanzania ambamo Ernest Hemingway alipita, huku tukisoma na kujadili maandishi yake kuhusu sehemu hizo.

Wakati filamu hiyo ilipokuwa inatengenezwa, niliweka taarifa mtandaoni, na nilipeleka taarifa sehemu kadhaa katika mfumo wa serikali ya Tanzania, kuelezea jinsi filamu hii itakavyoitangaza Tanzania. Nilifarijika kupata ujumbe kutoka Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, ukiafiki kuwa hii ni "fursa maridhawa ya kuitangaza Tanzania ulimwenguni" kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Filamu inapatikana katika tovuti ya Ramble Pictures.

Thursday, May 25, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nikitokea Minneapolis, nilipita Apple Valley, katika duka la vitabu la Half Price Books. Nilikuwa nimepania kununua kitabu juu ya Hemingway, Hemingway's Boat: Everything He Loved in Life, And Lost, kilichotungwa na Paul Hendrickson, ambacho nilikifahamu kwa miezi, na hivi karibuni nilikiona katika duka hilo, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

Kwa hivi, leo niliombea nikikute hiki kitabu, na kwa bahati nzuri nilikikuta. Baada ya kukichukua mahali kilipokuwepo, nilienda sehemu panapouzwa vitabu kwa bei ndogo zaidi. Bila kuhangaika sana, niliona kitabu kiitwacho F. Scott Fitzgerald, kilichotungwa na Arthur Mizener.  Nilifungua kurasa mbili tatu, nikakichukua.

Nilifahamu kwa muda mrefu kuwa Fitzgerald alizaliwa St. Paul, Minnesota, mji ninaoutembelea mara kwa mara. Nilishasoma riwaya yake maarufu, The Great Gatsby. Halafu, miaka hii ambapo nimekuwa nikisoma sana maandishi na habari za Ernest Hemingway, nimeelewa kuwa haiwezekani kumtenganisha Hemingway na Fitzgerald.

Hemingway alipokuwa kijana, akiishi Paris kama ripota wa gazeti la Toronto Star na pia kama mwandishi wa hadithi fupi na riwaya, alikuwa na mahusiano ya karibu na waandishi wengine waliokuwepo Paris, kama vile Gertrude Stein, Ezra Pound, na huyu F. Scott Fitzgerald. Fitzgerald alifanya bidii kumwezesha Hemingway kuanza kuandika riwaya, akafanya juhudi zilizomfanya Marx Perkins, mhariri maarufu wa kampuni ya Scribners Sons, akachapisha riwaya ya Hemingway, The Sun Also Rises. Hayo ndiyo mawazo yaliyonifanya nikanunua kitabu hiki.

Hapo hapo, nilivutiwa na kitabu kiitwacho The Works of John Donne, kilichoandaliwa na The Wordsworth Poetry Library. Sikuwa ninakifahamu kitabu hiki. Jina la mshairi John Donne nimelifahamu tangu zamani, labda nilipokuwa mwanafunzi katika shule ya sekondari. Nadhani nilishasoma mashairi yake mawili matatu, lakini sio zaidi.

Ila kwa kusoma maandishi ya wahakiki na wanataaluma, nilifahamu kuwa Donne anahesabiwa kama mshairi anayeandika mashairi magumu kuyaelewa. Habari hii ilichangia kunifanya nisiwe mwepesi wa kusoma mashairi yake. Nadhani si jambo zuri kwa mwandishi kuvumishiwa sifa kwamba tungo zake ni ngumu kueleweka. Inaweza kuwakatisha wasomaji hamu ya kujisomea maandishi ya mwandishi huyo.

Kwa Afrika, mashairi ya Christopher Okigbo yamepewa sifa hiyo. Pia mashairi ya Wole Soyinka. Lakini kwa umri nilio nao, na uzoefu wangu wa kusoma na kufundisha fasihi, naona ni vema kuwahimiza watu wajisomee wenyewe tungo zozote, kwani kwa kufanya hivyo, na kama wanafanya juhudi ya dhati, ni lazima wataambulia chochote. Nazingatia nadharia inayosema kwamba utungo wa fasihi una uwezo wa kuzalisha maana na tafsiri nyingi bila kikomo. Nadharia hii imefafanuliwa na wataalam kama Roland Barthes.

Thursday, March 16, 2017

Nimenunua "Two Thousand Seasons" (Ayi Kwei Armah)

Leo nilienda St. Paul, na wakati wa kurudi, nilipitia Apple Valley kuangalia vitabu katika duka la Half Price Books, kama ilivyo kawaida yangu. Hilo duka lina maelfu ya vitabu, na wateja wanapishana humo tangu asubuhi hadi jioni.

Kila ninapoingia katika duka la vitabu, ninajikuta nikianza kuangalia kama kuna vitabu vipya juu ya mwandishi Ernest Hemingway. Leo sikuona kitabu kipya juu ya Hemingway, nikaenda sehemu nyingine humo dukani, kwenye kona kabisa, ambapo sikosi kupitia.

Hapo, katikati ya msitu wa vitabu, niliona kitabu cha Ayi Kwei Armah, Two Thousand Seasons. Sikutegemea kukuta kitabu cha Armah. Nilikichukua hima, huku nikikumbuka enzi za ujana wangu Tanzania, kwani ni wakati ule ndipo nilianza kusikia habari za Ayi Kwei Armah.

Tangu nikiwa mwanafunzi sekondari, nilikuwa nafuatilia sana fasihi ya ki-Ingereza. Somo la fasihi ni somo nililolipenda na kuliweza sana. Nilipoingia Chuo kikuu cha Dar es Salaam, mwaka 1973, ndipo nilipofahamu kuwa Ayi Kwei Armah alikuwa anaishi Dar es Salaam. Alikuwa anafundisha chuo cha ualimu Chang'ombe, lakini tulishangaa kwa jinsi alivyokuwa hatumwoni kokote, hata chuo kikuu. Tulitegemea angejihusisha na chuo kikuu, lakini sidhani kama aliwahi hata kukanyaga pale.

Jambo hilo lilitushangaza, hasa kwa kuzingatia umaarufu wake kama mwandishi katika Afrika na ulimwenguni. Tulisoma riwaya yake, The Beautyful Ones Are Not Yet Born, na mimi binafsi nilisoma pia Fragments, Why are we So Blest?, na Two Thousand Seasons. Ayi Kwei Armah tulimfahamu pia kutokana na insha yake, "African Socialism: Utopian or Scientific?"

Nilijua tangu wakati ule kuwa wahakiki walikuwa wanalumbana kuhusu uandishi wa Armah. Baadhi walilalamika jinsi anavyoielezea Ghana katika The Beautyful Ones Are Not Yet Born. Anaelezea uozo wa kina namna. Wahakiki na wasomaji walishangaa kwa nini aliamua kuanika uozo huo machoni pa ulimwengu.

Two Thousand Seasons inahusu biashara ya utumwa iliyosababisha mamilioni ya wa-Afrika kupelekwa bara la Amerika kama watumwa. Armah kwa kushughulikia mada hii, alikuwa anaendeleza jadi ya waandishi wenzake wa Ghana, kama vile Ama Ata Aidoo katika tamthilia zake mbili: Dilemma of a Ghost na Anowa.

Saturday, March 4, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nilikwenda Minneapolis, na wakati wa kurudi nilipitia Apple Valley nikaingia katika duka la Half Price Books. Kama kawaida, nilitaka kuona vitabu mbali mbali, lakini nilikuwa hasa na dukuduku ya kuona kama kuna vitabu juu ya Ernest Hemingway.

Kwa hivyo, nilivyoingia tu dukani, nilienda moja kwa moja kwenye sehemu vinapowekwa vitabu vya Hemingway, yaani vilivyoandikwa naye au juu yake. Tofauti na siku zingine, leo nilikuta vitabu vichache, na vyote ni vile alivyoandika Hemingway mwenyewe. Nilikiona kitabu ambacho sikumbuki kama nimewahi kukiona kabla, The Fifth Column and Four Stories of the Spanish Civil War, nikakiangalia.

Niliona kuwa "The Fifth Column" ni tamthilia, ambayo sina katika maktaba yangu. Papo hapo nilihisi kuwa hadithi zilizomo katika kitabu ziko katika kitabu cha The Complete Short Stories of Ernest Hemingway, ambacho ninacho. Nimethibitisha hivyo baada ya kuja nyumbani.

Nilipotoka sehemu vinapowekwa vitabu vya Hemingway, nilienda sehemu ambapo sikosi kuangalia, kwani hapo vinawekwa vitabu ambavyo vinauzwa kwa bei ndogo sana. Kama kawaida, niliviangalia vitabu vingi, nikaamua kuchukua kitabu cha Gulliver's Travels cha Jonathan Swift.

Hii nakala ya Gulliver's Travels niliyonunua ni toleo la andiko halisi la Swift, si toleo lililorahisishwa. Jambo hilo lilinivutia. Jambo jingine ni kuwa kuna utangulizi ulioandikwa na Jacques Barzun, mwandishi ambaye maandishi yake nimeyafahamu tangu miaka ya themanini na kitu nilipokuwa ninasoma katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison. Katika nakala hii, kuna pia michoro aliyochora Warren Chappell.

Monday, January 30, 2017

Kitabu Nilichonunua Leo: "The Highly Paid Expert"

Leo nilikwenda Minneapolis na wakati wa kurudi, nilipita Mall of America, kuangalia vitabu katika duka la Barnes & Noble. Nilitaka hasa kuona kama kuna vitabu vipya juu ya mwandishi Ernest Hemingway.

Niliangalia scheme vinapowekwa vitabu vya fasihi, nikakuta kitabu kipya juu ya Ernest Hemingway, Everybody Behaves Badly: The Backstory to 'The Sun Also Rises.' kilichoandikwa na Lesley M.M. Blume. Kwa kuwa nimezama sana katika uandishi wa Hemingway, maisha na falsafa yake, na kwa kuwa nimeshasoma The Sun Also Rises, nilitamani kukinunua kitabu hiki, ambacho, kwa maelezo niliyoyaona, kinazungumzia yaliyo nyuma ya pazia.

Sikuwa na hela za kutosha, kwa hivyo nikaamua kuangalia vitabu vingine. Nilitumia muda zaidi katika sehemu ya "Business/Management." Huwa ninapenda sana kununua na kusoma vitabu vya taaluma hii, kwani vinanifundisha mengi kuhusu mambo ya ujasiriamali na biashara. Taaluma hii inanisaidia katika kuendesha shughuli za kampuni yangu ya Africonexion: Cultural Consultants.

Hatimaye, nilikiona kitabu kilichonivutia kwa namna ya pekee, The Highly Paid Expert, kilichoandikwa na Debbie Allen.  Kwa mujibu maelezo nyuma ya kitabu, huyu mwandishi ni mtaalam maarufu katika mambo ya biashara na ujasiriamali. Niliangalia ndani, nikaona mada anazoongelea ni za kuelimisha kabisa, kama vile matumizi ya tekinolojia za mawasiliano na mitandao.

Niliona anatoa ushauri wa kusisimua. Kwa mfano, anasema kuwa ni lazima mtu unayetaka mafanikio katika shughuli zako, uwasaidie wengine kufanikiwa. Unavyowasaidia wengine wafanikiwe, unajijengea mtandao wenye manufaa kwako pia. Ubinafsi na uchoyo wa maarifa haukuletei mafanikio. Kitabu hiki kinavutia kwa jinsi mwandishi anavyothibitisha mawazo yake, ambayo kijuu juu yanaonekana kama ya mtu anayeota ndoto.

Kwa bahati niliweza kuimudu gharama ya kitabu hiki, nikakinunua na kuondoka zangu, kwani nilikuwa sina hela iliyosalia. Sijutii kununua vitabu. Vitabu vinavyoelimisha ni mtaji, kwani hakuna mtaji muhimu zaidi ya elimu. Kwa wajasiriamali, wafanya biashara, watoa huduma, na kwa kila mtu, elimu ni tegemeo na nguzo muhimu. Ulazima wa kununua vitabu ni sawa na ilivyo lazima kwa mkulima kununua pembejeo.

Wednesday, January 11, 2017

Zawadi Kutoka Ramble Pictures Kwa Heshima Ya Hemingway

Wiki iliyopita nimepata zawadi ya picha kutoka Ramble Pictures, kampuni ya kutengeneza filamu. Kampuni hiyo ndiyo iliyotengeneza filamu ya Papa's Shadow, inayohusu maisha na safari za mwandishi maarufu Ernest Hemingway Afrika Mashariki, pamoja na maandishi yake kuhusu Afrika Mashariki. Sehemu kubwa ya filamu hiyo ni mazungumzo baina ya Mzee Patrick Hemingway na mimi, kuhusu masuala hayo.

Picha niliyopewa inaitangaza filamu ya Papa's Shadow. Inamwonesha Ernest Hemingway, Patrick Hemingway na mimi, Kuna pia Mlima Kilimanjaro na nchi tambarare chini ya mlima, na pia ndege ikiwa angani. Hiyo picha ya mlima na mazingira yake, pamoja na ndege, inakumshia hadithi maarufu ya Hemingway, "The Snows of Kilimanjaro."

Nimeguswa na picha hii. Ni heshima kubwa kuliko ninavyostahili kuwekwa sambamba na Ernest Hemingway na Patrick Hemingway. Ernest Hemingway alileta mapinduzi katika uandishi na alitunukiwa tuzo ya Nobel katika fasihi mwaka 1954. Patrick Hemingway ni mtu muhimu kwa watafiti wa Hemingway, akiwa ni mtoto pekee aliye bado hai wa Ernest Hemingway. Ametoa na anaendelea kutoa mchango mkubwa wa kuhariri maandishi ya Hemingway na kuyaandikia utangulizi.

Kwa upande mwingine ninafurahi kuoneshwa pamoja na Patrick Hemingway, ambaye ni mtu wa karibu kwangu. Ananifundisha mengi kuhusu Afrika Mashariki ya wakati alipoishi kule, kuhusu maisha na uandishi wa Hemingway, na kuhusu waandishi wengine, hasa wa wakati wa Hemingway.

Vile vile, Patrick Hemingway anakipenda sana kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Hata katika filamu ya Papa's Shadow, anakitaja, na kuna mahali anasoma kisehemu cha kitabu hiki kwa ki-Swahili na tafsiri yangu ya ki-Ingereza.

Filamu ya Papa's Shadow inaelezea upande wa Ernest Hemingway ambao haufahamiki vizuri, yaani jinsi alivyovutiwa na Afrika kwa maisha yake yote. Katika kufanya utafiti juu ya Hemingway na kusoma maandishi yake kwa miaka kadhaa, niligundua kuwa aliipenda Afrika tangu alipokuwa mtoto. Ndipo nikaamua kutunga kozi kuhusu mada hiyo.

Mwanafunzi mmoja katika kozi hiyo, Jimmy Gildea, alipata motisha ya kutengeneza filamu, na matokeo yake ni Papa's Shadow. Pamoja na kuelimisha juu ya uhusiano wa Hemingway na Afrika, filamu hii inaitangaza Tanzania. Nakala za filamu hii zinapatikana kwa kuwasiliana na Ramble Pictures kwa barua pepe: info@ramblepictures.com au kwa simu (952) 426-5809.

Tuesday, November 22, 2016

Ninaendelea Kusoma "Hamlet"

Miaka miwili iliyopita, niliandika katika blogu hii kuwa nina tabia ya kusoma vitabu kiholela. Wakati wowote nina vitabu kadhaa ninavyovisoma, bila mpangilio maalum, na pengine bila nia ya kufikia mwisho wa kitabu chochote.

Kusoma kwa namna hii hakuna ubaya wowote, bali kuna manufaa. Nilipokuwa mwanafunzi wa sekondari, katika seminari ya Likonde, mwalimu wetu, Padri Lambert OSB alituhimiza tuwe na mazoea ya kusoma sana vitabu, na pia mazoea ya kuvipitia vitabu kijuu juu, ambayo kwa ki-Ingereza huitwa "browsing."

Nikiachilia mbali vitabu ninavyofundisha, wakati huu nimezama zaidi katika kusoma Hamlet, kama nilivyoandika katika blogu hii. Ninasoma Hamlet pole pole, ili kuyanasa vizuri akilini yaliyomo, hasa maudhui kuhusu maisha, maadili, na tabia za binadamu. Kusoma pole pole kunaniwezesha kukifurahia ki-Ingereza cha Shakespeare, ingawa si rahisi kama ki-Ingereza tunachotumia leo.

Tofauti kati ya ki-Ingereza cha leo na kile cha Shakespeare ninaifananisha na tofauti kati ya ki-Swahili cha leo na kile cha mashairi ya zamani kama yale ya Muyaka au Utenzi wa Rasi lGhuli. Kwa msingi huo, kusoma utungo kama Hamlet ni chemsha bongo inayoboresha akili, sawa na mazoezi ya viungo yanavyoboresha afya ya mwili.

Mwandishi maarufu Ernest Hemingway alielezea vizuri thamani ya vitabu aliposema, "There is no friend as a loyal as a book," yaani hakuna rafiki wa kweli kama kitabu. Ujumbe uko wazi, nami sina la kuongeza. Kitabu bora ukishakinunua, ni rafiki wa kudumu.


  

Wednesday, October 26, 2016

Miaka 80 ya "The Snows of Kilimanjaro"

Kwa mara nyingine tena, ninaandika ujumbe kuhusu kutimia kwa miaka 80 tangu hadithi ya Ernest Hemingway, 'The Snows of Kilimanjaro" ilipochapishwa kwa mara ya kwanza. Niliandika ujumbe wa aina hiyo katika blogu hii. Leo nimesoma tena ujumbe wangu, nikajiridhisha kwamba niliyosema ndiyo ninayoamini hadi sasa.

Jambo moja kubwa kabisa ni kuwa wa-Tanzania tunajipotezea fursa za wazi za kutumia hazina kama hii hadithi ya Hemingway kuitangaza nchi yetu. Niliandika katika ujumbe wangu baadhi ya mambo ambayo tungeyafanya mwaka huu wa kumbukumbu. Lakini mwaka unaelekea ukingoni, na hakuna tulichofanya. Hii ni hasara ya kukosa utamaduni wa kusoma vitabu. Tunashindwa hata kutumia fursa zilizo wazi.

Nimeona niandike ujumbe huu leo kwa sababu wiki hii, hapa katika Chuo cha St. Olaf ninapofundisha, litatokea jambo la pekee linalohusiana na Ernest Hemingway. Keshokutwa, tarehe 28, pataonyeshwa kwa mara ya kwanza filamu ya "Papa's Shadow," ambayo niliwahi kuielezea katika blogu hii.

Hiyo ni filamu iliyotokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwaka 2013 iitwayo Hemingway in East Africa. Nilisafiri na wanafunzi 29 wa Chuo cha St. Olaf, tukazunguka maeneo kadhaa ya Tanzania kaskazini, ambamo alipita Ernest Hemingway mwaka 1933-34. Katika safari hiyo, tulikuwa tunasoma maandishi ya Hemingway kuhusu maeneo hayo na maeneo mengine ambayo alipitia mwaka 1953-54.

Maandishi hayo ni pamoja na Green Hills of Africa na Under Kilimanjaro, ambavyo ni vitabu, kadhalika hadithi fupi mbili: "The Short Happy Life of Francis Macomber" na "The Snows of Kilimanjaro." Pia aliandika makala katika magazeti na barua nyingi akielezea aliyoyaona na kufanya katika safari zake. Kwa ujumla wake, maandishi haya ya Ernest Hemingway yanaitangaza nchi yetu na Afrika Mashariki kwa ujumla kwa namna ambayo sisi wenyewe hatujaweza kujitangaza.

Hiyo filamu ya "Papa's Shadow" inawasilisha vizuri mambo muhimu ya uhusiano wa Ernest Hemingway na Afrika Mashariki. Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Tunajadili kwa kina na mapana fikra za Ernest Hemingway kuhusu Afrika, uandishi, na maisha kwa ujumla.

Kwa kuwa hiyo filamu inaonyesha sehemu mbali mbali za Tanzania na maelezo kuhusu mambo yanayoifanya Tanzania kivutio kwa watalii, kama vile Mlima Kilimanjaro, na kwa kuwa filamu hii imejengeka katika maandishi ya Ernest Hemingway, mwandishi maarufu sana ulimwenguni, ni wazi kuwa filamu hii itakuwa chachu ya kuitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Taarifa zaidi Kuhusu "Papa's Shadow," zinapatikana kwenye tovuti ya Ramble Pictures.

Saturday, June 25, 2016

Ninasoma "A Moveable Feast"

Nina tabia ya kusoma vitu vingi bila mpangilio, na niliwahi kutamka hivyo katika blogu hii. Kwa siku, naweza kusoma kurasa kadhaa za kitabu fulani, kurasa kadhaa za kitabu kingine, makala hii au ile, na kadhalika. Sina nidhamu, na sijui kama kuna umuhimu wa kuwa na nidhamu katika usomaji.

Siku kadhaa zilizopita, niliandika katika blogu hii kuhusu vitabu nilivyochukua katika safari yangu ya Boston. Nilisema kuwa kitabu kimojawapo kilikuwa A Moveable Feast cha Ernest Hemingway. Ni kweli, nilikuwa ninakisoma, sambamba na vitabu vingine, makala na kadhalika. Matokeo yake ni kuwa inachukua muda kumaliza kitabu.

A Moveable Feast ni kitabu kimojawapo maarufu sana cha Hemingway. Wako wahahiki wanaokiona kuwa kitabu bora kuliko vingine vya Hemingway, ingawa wengine wanataja vitabu tofauti, kama vile A Farewell to Arms, For Whom the Bell Tolls, na The Old Man and the Sea. Hemingway alikuwa mwandishi bora kiasi kwamba kila msomaji anaona chaguo lake.

Ninavyosoma A Moveable Feast, ninaguswa na umahiri wa Hemingway wa kuelezea mambo, kuanzia tabia za binadamu hadi mandhari za mahali mbali mbali. Picha ninayopata ya mji wa Paris na maisha ya watu katika mji huo miaka ya elfu moja mia tisa na ishirini na kitu haiwezi kusahaulika. Ni tofauti na picha ya Paris tuliyo nayo leo.

Hemingway haongelei maisha ya starehe na ulimbwende. Watu wanaishi maisha ya kawaida, na wengine, kama yeye mwenyewe na mke wake Hadley, wanaishi maisha ya shida. Mara kwa mara Hemingway anaongelea alivyokuwa na shida ya hela, ikambidi hata mara moja moja kuacha kula ili kuokoa hela.

Inasikitisha kusikia habari kama hizi, lakini pamoja na shida zake, Hemingway anasisitiza kwamba Paris ulikuwa mji bora kwa mwandishi kuishi. Anasema kuwa gharama za maisha hazikuwa kubwa. Alikuwa na fursa ya kuwa na waandishi maarufu waliomsaidia kukua katika uandishi, kama vile Gertrude Stein, Ezra Pound, na Scott Fitzgerald.

A Moveable Feast, kama vile Green Hills of Africa, ni kitabu chenye kuongelea sana uandishi na waandishi. Hemingway anatueleza alivyokuwa anasoma, akitegemea fursa zilizokuwepo, kama vile duka la vitabu la Shakespeare and Company lililomilikiwa na Sylvia Beach. Anatuambia alivyowasoma waandishi kama Turgenev, Tolstoy, D.H. Lawrence, na Anton Chekhov. Anatueleza alivyokuwa anajadiliana na wengine kuhusu waandishi hao.

Hayo, kama nilivyogusia, yananikumbusha Green Hills of Africa, ambamo kuna mengi kuhusu uandishi na waandishi. Katika Green Hills of Africa, tunamsikia Hemingway akiongelea uandishi hasa katika mazungumzo yake na mhusika aitwaye Koritchner. Vitabu kama A Moveable Feast vinatajirisha akili ya msomaji. Si vitabu vya msimu, bali ni urithi wa kudumu kwa wanadamu tangu zamani vilipoandikwa hadi miaka ya usoni.

Toleo la A Moveable Feast ninalosoma ni jipya ambalo limeandaliwa na Sean Hemingway. Toleo la mwanzo liliandaliwa na Mary Welsh Hemingway, mke wa nne wa Hemingway. Kutokana na taarifa mbali mbali, ninafahamu kuwa kuna tofauti fulani baina ya matoleo haya mawili, hasa kuhusu Pauline, mke wa pili wa Hemingway. Sean Hemingway amerejesha maandishi ya Hemingway juu ya Pauline ambayo Mary hakuyaweka katika toleo lake. Bahati nzuri ni kuwa miswada ya kitabu chochote cha Hemingway imehifadhiwa, kama nilivyojionea katika maktaba ya JF Kennedy.

Jambo moja linalonivutia katika maandishi ya Hemingway ni jinsi anavyorudia baadhi ya mambo kutoka andiko moja hadi jingine, iwe ni kitabu au hadithi, insha au barua. Kwa namna hiyo, tunapata mwanga fulani juu ya mambo yaliyokuwa muhimu mawazoni mwa Hemingway. Mfano moja ni namna Hemingway anavyoelezea athari mbaya za fedha katika uandishi. Mwandishi anaposukumwa au kuvutwa na fedha au mategemeo ya fedha anaporomoka kiuandishi. Dhana hiyo ya Hemingway inanikumbusha waliyosema Karl Marx na Friedrich Engels katika The Communist Manifesto, yakaongelewa pia na wengine waliofuata mwelekeo wa ki-Marxisti, kama vile Vladimir Ilyich Lenin.


Thursday, May 26, 2016

"The Snows of Kilimanjaro" Yatimiza Miaka 80

Mwaka huu 2016, The Snows of Kilimanjaro, hadithi maarufu ya Ernest Hemingway, inatimiza miaka 80 tangu ichapishwe kwa mara ya kwanza. Ilichapishwa katika jarida la Esquire, toleo la Agosti, 1936. Sidhani kama kuna hadithi fupi katika fasihi ya ki-Ingereza inayofahamika na ni maarufu kuzidi The Snows of Kilimanjaro.

Hemingway aliandika utangulizi mfupi wa hadithi yake, ambao unaamsha hisia zinazoendelezwa katika hadithi nzima, ikiwemo hisia ya masuali yasiyojibika:

"Kilimanjaro is a snow covered mountain 19,710 feet high, and it is said to be the biggest mountain in Africa. Its western summit is called the Masai "Ngáje Ngái," the House of God. Close to the western summit there is the dried and frozen carcass of a leopard. No one has explained what the leopard was seeking at that altitude." 

The Snows of Kilimanjaro inamhusu mtu aitwaye Harry, mzungu. Tunamwona akiwa mgonjwa kutokana na kidonda alichopata baada ya kuchomwa na mwiba porini. Kilichosababisha kidonda kufikia hali ya kutishia uhai wake ni kucheleweshwa kwa matibabu. Harry tunamwona amelala kwenye machela huku akihudumiwa na mkewe Helen, mzungu pia. Kuna pia watumishi wa-Afrika.

Mazingira inapotokea hadithi hii ni chini ya mlima Kilimanjaro. Lakini sehemu kubwa ya hadidhi ni kumbukumbu za Harry za mambo aliyofanya au kushuhudia sehemu mbali mbali za Ulaya, kama vile Paris, ikiwemo ushiriki wake katika vita. Juu ya yote, hadithi hii ni mtiririko wa fikra za Harry kuhusu uandishi. Tunamshuhudia akiwazia mengi ambayo alitaka aandike miaka iliyopita, au angependa kuwa ameandika, lakini hakuandika kwa sababu mbali mbali. Anajisikitikia kuwa sasa hataweza kuandika, kwani kifo kinamwelemea. Helen anafanya kila awezalo kumtuliza na kumpa matumaini kuwa atapona. Anamtunza na kujaribu kumzuia kujidhuru kwa ulevi. Anamweleza kuwa ndege itakuja kumwokoa.

Kwa kuwa huu ni mwaka wa kumbukumbu ya miaka 80 ya The Snows of Kilimanjaro, na kwa kuzingatia umaarufu wa Ernest Hemingway ulimwenguni, na umaarufu wa The Snows of Kilimanjaro, na kwa kuwa Mlima Kilimanjaro uko nchini mwetu, hii ilikuwa ni fursa ya kuitangaza nchi yetu. Niliwahi kuandika kidogo kuhusu jambo hili katika blogu hii. Ingekuwa wa-Tanzania tuna utamaduni wa kusoma na kuthamini vitabu, tungeichangamkia fursa ninayoelezea hapa.

Kuna mambo ambayo tungeweza kufanya. Wizara, taasisi na makampuni yanayohusika na utalii yangefurika matangazo na makala juu ya Hemingway na The Snows of Kilimanjaro. Wasomaji wa Hemingway, wanafasihi, na wengine tungekuwa tunafanya mijadala na makongamano. Vyombo vya habari, kama vile magazeti na televisheni, vingekuwa vinarusha matangazo na taarifa na mijadala hiyo. Huu ungekuwa mwaka wa kuitangaza nchi yetu na kuwavutia watalii nchini kwetu kwa namna ya pekee kabisa.

Kuna wenzetu ambao wanatumia jina na maandishi ya Hemingway kujitangaza na kuvutia watalii. Mifano ya wazi ni Cuba na mji wa Pamplona ulioko Hispania. Dunia ya leo ya ushindani mkubwa inahitaji ubunifu wa kwenda na wakati.  Dunia si ya kuichezea. Muyaka alitahadharisha hayo aliposema, "dunia mti mkavu, kiumbe siulemele" na tusijidanganye kuwa twaweza "kuudhibiti kwa ndole."

Sunday, May 22, 2016

Leo Nimemwandikia Mzee Patrick Hemingway

Leo nimemwandikia barua pepe Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliye hai wa mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Nilipiga naye picha inayoonekana hapa kushoto tarehe 27 Aprili, 2013, nyumbani pake mjini Craig, katika jimbo la Montana.

Nilifahamu habari zake kwa miaka mingi kabla ya kufahamiana naye na halafu tukakutana. Ni mzee mwenye maongezi ya kusisimua kuhusu baba yake Ernest Hemingway na waandishi wengine wa wakati wake. Pia ana kumbukumbu nyingi za Tanganyika, na kisha Tanzania, ambako aliishi kwa miaka yapata 25 kabla ya uhuru na baada ya uhuru, akiendesha kampuni ya utalii, na hatimaye akiwa mkufunzi katika Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori cha Mwika.

Tangu tulipoanza kufahamiana, ameguswa na ari yangu ya kutafiti maandishi, falsafa, na maisha ya Ernest Hemingway, na amevutiwa na msimamo wangu kuwa Ernest Hemingway ni mwandishi aliyetuenzi sana sisi watu wa Afrika Mashariki, na tunapaswa kujielimisha kuhusu mchango wake, na kisha kuutumia katika kujitangaza kama alivyotutangaza.

Hayo yamemfanya Mzee Patrick Hemingway awe tayari kunisaidia kwa dhati katika juhudi zangu za kujielimisha na kuuelimisha ulimwengu juu ya Ernest Hemingway. Miezi kadhaa iliyopita, nilivyomweleza kuwa napangia kutembelea hifadhi ya Ernest Hemingway katika John F. Kennedy Library, aliniambia kuwa nitakapokuwa tayari nimfahamishe ili anitambulishe kwa wahusika.

Nilipoongea naye tarehe 19 mwezi huu na kumtajia tarehe nilizopangia kwenda kwa shughuli hiyo, aliniagiza nimpelekee maelezo yangu kwa barua pepe, ili aweze kuandaa utambulisho huo. Aliniambia kuwa ninakwenda wakati mzuri, kwani kuna maonesho maalum juu ya Hemingway, ambayo yameanza siku chache zilizopita na yatadumu kwa miezi kadhaa.

Basi, leo nimemwandikia. Kilichobaki sasa ni kuandaa safari, nikajionee hiyo hifadhi kubwa kuliko zote duniani juu ya Ernest Hemingway. Hii itakuwa ni mara yangu ya kwanza kuitembelea hifadhi hiyo, lakini sitegemei kuwa itakuwa ni mara ya mwisho.

Wednesday, May 18, 2016

Muhula Unaisha; Umebaki Utafiti

Jana tumemaliza muhula wa masomo hapa chuoni St. Olaf. Nilikuwa ninafundisha "Folklore," Muslim Women Writers, na "First Year Writing." Kwa utaratibu wa chuo hiki, masomo matatu kwa muhula ndio kiwango cha juu kabisa. Hatufundishi zaidi ya masomo matatu. Kwa hivi, nilitegemea ningekuwa nimechoka, lakini sisikii uchovu. Alhamdulillah.

Kwa wiki nzima inayokuja, tutakuwa na mitihani. Baada ya hapo tutaanza likizo ndefu ya miezi mitatu na kidogo. Inaitwa likizo, lakini maprofesa tunaona ni wakati muafaka wa kufanya shughuli za kitaaluma kama utafiti na uandishi.

Nami nimeamua kwenda Boston kwa siku chache kufanya utafiti juu ya Ernest Hemingway katika maktaba ya John F. Kennedy. Humo kuna hifadhi kubwa kuliko zote duniani ya vitabu, miswada, picha na  kumbukumbu zingine zinazomhusu Hemingway. Ingawa nimefika Boston mara kadhaa, sijawahi kwenda katika maktaba hiyo maarufu.

Nina bahati kuwa ninafahamiana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway ambaye bado yuko hai. Yeye ndiye mmiliki wa haki zote za urithi wa Hemingway. Nilipomwambia kwa mara ya kwanza kwamba napangia kwenda kufanya utafiti katika maktaba ya John F. Kennedy,  aliniambia nimfahamishe ni lini ili anitambulishe kwa wahusika. Wiki chache zilizopita, katika maongezi yetu, nilimwambia tena kuwa napangia kwenda kwenye maktaba ile, alikumbushia kuwa nimweleze ni muda upi nitakwenda ili awafahamishe.

Ninashukuru sana kwa hilo, kwani katika kusoma taarifa za maktaba ile, nimefahamu kuwa kuna masherti yanayohusu kuitumia hifadhi ya Ernest Hemingway. Mtu hukurupuki tu ukafika pale na kufanya utafiti. Kuna baadhi ya kumbukumbu ambazo zimefungiwa. Mtafiti unahitaji kibali maalum kuweza kuzifanyia utafiti. Sherti nichukue hatua hima.

Saturday, May 14, 2016

Nimepita Tena Katika Duka la Half Price Books

Leo alasiri nilikwenda eneo la Minneapolis, mwendo wa maili 40, kwa shughuli binafsi. Ilikuwa siku nzuri, ya jua la wastani na hali ya hewa ya kupendeza. Wakati wa kurudi, nilipita mjini Apple Valley, nikaamua kupitia katika duka la Half Price Books. Nilitaka hasa kuangalia kama kuna chochote juu ya mwandishi Ernest Hemingway. Kufuatilia vitabu juu ya Hemingway imeshakuwa mazoea kwangu, wala siwezi kujizuia.

Ninajua kuwa sitakikuta kitabu kipya kilichoandikwa na Hemingway. Inafahamika kwamba miswada yote ya vitabu vya Ernest Hemingway imeshachapishwa. Kinachotokea ni kuwa yanachapishwa matoleo mapya ya vitabu vyake, kama vile matoleo yanayohaririwa na mjukuu wake, Sean Hemingway, ambavyo Mzee Patrick Hemingway, mtoto wa Ernest Hemingway, anaviandikia utangulizi.

Maandishi mapya kabisa ya Ernest Hemingway yanayochapishwa ni barua zake. Kuna mradi wa kukusanya barua zote za Ernest Hemingway tangu utotoni mwake. Wahariri wa mradi huu ni maprofesa Sandra Spanier na Robert W. Trogdon, ambao wamebobea katika utafiti juu ya Ernest Hemingway. Hadi sasa majuzuu matatu yamechapishwa, na kila juzuu ni mkusanyo wa barua za miaka michache. Inatarajiwa kuwa mradi huu ambao utachukua miaka mingi, utatoa majuzuu yatachapishwa 17.

Vitabu vingine vipya ambavyo vinaendelea kuchapishwa ni matokeo ya utafiti juu ya maisha na maandishi ya Ernest Hemingway. Tangu zamani, kumekuwa na watafiti wengi wanaojishughulisha na utafiti huu, na vitabu ambavyo wamechapisha na wanaendelea kuchapisha ni vingi. Si rahisi kwa mtu yeyote kufuatilia suala hili kikamilifu, lakini ninakuwa na duku duku ya kuona kuna vitabu gani vipya juu ya Hemingway katika duka la vitabu.

Nimefurahi leo kukikuta kitabu juu ya Hemingway ambacho sikuwa hata nimekisikia, The True Gen: An Intimate Portrait of Hemingway by Those Who Knew Him kilichoandikwa na Denis Brian. Katika kukipitia, niliona kuwa kitabu hiki ni taswira ya Hemingway inayotokana na kumbukumbu za watu waliomfahamu. Niliamua hapo hapo kukinunua. Baada ya kufika nyumbani, nimeanza kukisoma.  Kuna maelezo ya watu wengi, kuanzia wale waliokuwa watoto wakienda shule na mtoto Ernest Hemingway hadi waandishi, wake zake, na watu wengine.

Kama ilivyo kawaida, nilipokuwa hapo dukani Half Price Books niliwaona watu wengi humo wakizunguka zunguka kuangalia vitabu na kuvinunua. Wazazi wengi walikuwa na watoto wao. Kama kawaida, inavutia kuwaona watoto wa ki-Marekani wanavyolelewa katika utamaduni wa kupenda vitabu.

Sikukaa sana humo. Baada ya kununua kitabu changu, niliona niwahi nyumbani nikaanze kukisoma.


Sunday, March 20, 2016

Tukio Katika Nyumba ya Hemingway, Oak Park

Tarehe 27 Februari, nilizuru nyumba alimozaliwa mwandishi Ernest Hemingway, na pia jumba la kumbukumbu ya Hemingway, kama nilivyoandika katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza. Ilikuwa ni siku ya pekee, siku ambayo ndoto yangu ya miaka ilitimia.

Kati ya watu niliokutana nao katika nyumba ya Hemingway, ambao nao walikuwa wamekuja kuitembelea, ni binti aliyejitambulisha kuwa ni wa ukoo wa Hemingway. Alinipa kadi yake, iliyoonyesha kuwa jina lake ni Laura Hemingway.

Nilishangaa na kufurahi, nikaanza kuongelea namna ninavyomwenzi Hemingway. Niliongelea kozi yangu ya Hemingway, na jinsi ninavyowasiliana na mzee Patrick Hemingway. Binti huyu na wengine tuliokuwa tunasubiri kuanza ziara walivutiwa na taarifa hizo. Ninajitambua kuwa siwezi kuiachia fursa yoyote ya kuongelea habari za Hemingway.

Kwa bahati mbaya, niliporejea kutoka Chicago, niligundua kuwa nilikuwa nimepoteza anwani ya binti huyu. Leo amejitokeza katika facebook kuanzisha mawasiliano nami. Baada ya kuweka uhusiano huo, nimeweza kuipata picha tuliyopiga siku tulipokutana, ambayo inaonekana hapa juu.

Tuesday, October 13, 2015

Michango ya Papa's Shadow Imekamilika

Kwa mwezi mzima kumekuwa na kampeni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya filamu ya Papa's Shadow, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Leo, shughuli imekamilika, masaa sita kabla ya kipindi cha michango kwisha.

Mafanikio haya yamefungua njia kwa mambo makubwa siku zijazo. Papa's Shadow sasa itapatikana kwa wadau, pindi taratibu za malipo zitakapokamilika. Kwangu ni furaha kubwa, kama mchangiaji mkuu wa filamu hiyo, sambamba na Mzee Patrick Hemingway, wa maelezo na uchambuzi juu ya mwandishi Ernest Hemingway. Ninafurahi pia kwamba filamu hii itaitangaza Tanzania kwa namna ya pekee, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Umaarufu wa Ernest Hemingway ulimwenguni ni wa pekee. Pamoja na kuelezea uhalisi wa maisha ya binadamu, kama walivyofanya waandishi wengine maarufu, pamoja na kuzipa umaarufu kwa maandishi yake sehemu alizotembelea hapa duniani, Hemingway alianzisha jadi mpya kimtindo katika uandishi wa ki-Ingereza. Hilo limesemwa tena na tena na wataalam wa fasihi. Ninaamini kuwa Papa's Shadow itahamasisha ari mpya ya kusoma maandishi ya Hemingway.

Ninafurahi kuwa, katika Papa's Shadow, nimechangia kuleta mtazamo mpya juu ya Hemingway, na kuelekeza mawazo ya wasomaji na wapenzi wa Hemingway upande wa Afrika Mashariki, na hasa Tanzania. Wote waliochangia mradi huu kwa namna moja au nyingine, kwa hali na mali, wana sababu na haki ya kujipongeza.

Friday, October 9, 2015

Nimepata Toleo Jipya la "Green Hills of Africa"

Leo ni siku ya furaha kwangu. Nimepata nakala ya toleo jipya la Green Hills of Africa, kitabu cha Ernest Hemingway, kilichochapishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1935. Taarifa kwamba toleo hili lilikuwa linaandaliwa nilielezwa na Mzee Patrick Hemingway, kama nilivyoandika katika blogu hii. Kwa hivi, nilipogundua kwamba limechapishwa, niliagiza nakala hima.

Katika Green Hills of Africa, Hemingway anaelezea mizunguko yake katika nchi ya Tanganyika, mwaka 1933-34, akiwa na mke wake wa pili Pauline Pfeiffer. Anaelezea uzuri wa nchi, watu wa makabila, tamaduni, na dini mbali mbali, na wanyama katika mbuga alimowinda, kama vile Serengeti na eneo la Ziwa Manyara. Anaelezea miji alimopita, kama vile Mto wa Mbu, Babati, Kondoa, Handeni, na Tanga.

Toleo hili la Green Hills of Africa lina mambo ambayo hayakuwemo katika toleo la mwanzo, kama vile maandishi ya awali ambayo hayakutokea kitabuni, picha, na hata "diary" aliyoandika Pauline alipokuwa safarini na mumewe. Nilijua kuwa "diary" hii imehifadhiwa katika maktaba ya Chuo Kikuu cha Stanford, na nilikuwa nawazia kwenda kuisoma. Kuchapishwa kwake katika toleo hili ni jambo la kufurahisha sana.

Kutokana na jinsi Hemingway alivyoielezea nchi yetu, tukio la kuchapishwa kwa toleo hili la Green Hills of Africa mwaka huu ilipaswa tulipokee kwa shamra shamra. Pangekuwa na shughuli za uzinduzi wa toleo hili, makongamano, na tahakiki magazetini. Nakala zingejaa katika maduka ya vitabu, na wateja wangekuwa wanapigana vikumbo kuzinunua.

Sehemu zingine duniani wanatumia vilivyo bahati ya kutembelewa na Hemingway na kuandikwa katika maandishi yake. Ni kivutio kikubwa kwa watalii, kama ninavyosema katika blogu hii. Sisi tumeifanya nchi yetu kuwa kwenye miti ambako hakuna wajenzi.

Saturday, September 26, 2015

Nimehojiwa Kuhusu Hemingway na "Papa's Shadow"

Leo nimekuwa na mahojiano na mwandishi wa gazeti la Manitou Messenger linalochapishwa hapa chuoni St. Olaf. Ni gazeti la wanafunzi, ambalo limekuwa likichapishwa kila wiki kwa miaka 125. Mahojiano yetu yalikuwa juu ya filamu ya Papa's Shadow. Katika ujumbe wa kuomba mahojiano, mwandishi aliandika:

...we are doing a feature article this week on the documentary, Papa's Shadow and Ramble Pictures. We learned that you were instrumental in the inspiration for and production of this film, and we were hoping you could answer a few quick questions.

Katika mahojiano, tumeongelea nilivyoanza kuvutiwa sana na mwandishi Ernest Hemingway, nilipoombwa na Thomson Safaris kuongoza msafara mkubwa wa wanafunzi, wazazi na walimu, katika safari ya Tanzania mwaka 2002. Hatimaye, baada ya miaka mitano ya kusoma maandishi na habari za Hemingway, nilitunga kozi Hemingway in East Africa, kwa ajili ya Chuo cha Colorado.

Baadaye, niliona niunde kozi hiyo kwa ajili ya wanafunzi wa Chuo cha St. Olaf. Nilifanya hivyo mwaka 2012. Wakati wa kuandikisha wanafunzi, alinifuata kijana aitwaye Jimmy Gildea, akaniomba nimruhusu kujiunga na kozi, kwa kuwa alimpenda Hemingway na alitaka kurekodi filamu ya kozi. Nilimsajili katika darasa.

Kozi ilikwenda vizuri, kama nilivyoandika hapa. Baada ya kurejea tena Marekani, baadhi yetu tulifunga safari ya jimbo la Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Tuliongea naye sana.

Jimmy alikuwa amenirekodi ofisini mwangu nikizungumza juu ya Hemingway, akachanganya mazungumzo haya na yale tuliyofanya na Mzee Patrick Hemingway,na akaongezea mambo mengine aliyorekodi Tanzania. Kwa bahati nzuri, tulipomaliza kozi, familia ya Jimmy walikuja kumchukua wakaenda kupanda Mlima Kilimanjao. Papa's Shadow inaonyesha safari yao ya kupanda mlima. Ni rekodi nzuri sana. Ninaamini itawavutia watalii.

Kuna mambo mengine niliyomwambia huyu mwandishi wa Manitou Messenger. Hasa, nilisisitiza azma yangu ya kuendelea kufanya kila juhudi kuuelimisha ulimwengu juu ya namna Hemingway alivyoipenda Afrika na namna maisha yake na fikra zake zlivyofungamana na Afrika. Nilimwambia pia kuwa Jimmy ni mfano murua wa kuigwa na wahitimu wengine wa vyuo. Alifuata na anaendelea kufuata anachokipenda moyoni mwake, yaani kutengeneza filamu za kuelimisha. Yeye na vijana wenzake katika Ramble Pictures wanajituma kwa roho moja katika shughuli zao na hawatetereshwi na magumu au vipingamizi vyovyote.

Thursday, September 24, 2015

"Papa's Shadow" Yapongezwa na Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa

Tarehe 20 mwezi huu nilipeleka ujumbe Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa kuhusu filamu ya Papa's Shadow. Sikuandika ujumbe mrefu, bali niliwatumia kiunganishi hiki.

Bila kuchelewa, tarehe 22 nilipata ujumbe kutoka kwao, ukiwa umeandikwa na Ndugu Noel Kabanda. Uwakilishi unaafiki kuwa Papa's Shadow ni "fursa maridhawa ya kuitangaza Tanzania ulimwenguni" na unasisitiza kuwa "Serikali inatambua mchango wa sanaa katika kuitangaza Tanzania katika sekta mbali mbali ikiwemo utalii na utamaduni."

Kwanza, kwa kuzingatia uwingi wa majukumu yanayowakabili wawakilishi wetu katika balozi zetu, nimeona ni muhimu kusema nilivyoguswa na jinsi Uwakilishi ulivyoushughulikia ujumbe wangu.

Pili, ujumbe wa Uwakilishi unawatia moyo wahusika wa Ramble Pictures, ambao ndio watengeneaji wa Papa's Shadow. Timu nzima ya Ramble Pictures ni vijana wa ki-Marekani, na baadhi yao walikuja Tanzania mwaka 2013 kwenye kozi yangu ya Hemingway Katika Afrika Mashariki. Ni furaha kwangu, na jambo la kujivunia, kuwaeleza vijana hao kuwa Uwakilishi wa Kudumu waTanzania Umoja wa Mataifa umeipokea Papa's Shadow kwa namna hii.

Papa's Shadow si filamu ya maigizo. Ni filamu ya kuelimisha kuhusu mwandishi Ernest Hemingway. Sehemu kubwa ya filamu hiyo ni maongezi baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa mwandishi Hemingway. Tunaongelea maisha ya Hemingway, safari zake, uandishi wake, na fikra zake kuhusu masuala mbali mbali. Tunawafungua macho walimwengu kuhusu namna Hemingway alivyoipenda Afrika na alivyokuwa mtetezi wa Afrika.

Hemingway alisafiri na kuishi Afrika Mashariki mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54. Aliandika hadithi, insha, barua na maandishi mengine ambayo ni hazina kubwa. Wenzetu katika nchi zingine ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari za huko, wametumia fursa hiyo kujitangaza, na wanawavutia watalii wengi sana. Mifano ni miji kama Paris (Ufaransa), Havana (Cuba), Oak Park (Illinois, Marekani), Key West (Florida, Marekani), na Pamplona (Hispania). Hemingway anapendwa ulimwenguni kote ambako watu wana utamaduni wa kusoma vitabu. Sina shaka kuwa Papa's Shadow italeta msisimko wa aina hiyo kwa kuwaelekeza mashabiki wa Hemingway nchini kwetu.

Hamu ya kuona Tanzania inafunguka macho kuhusu fursa hii ilinihamasisha kufanya utafiti juu ya safari za Hemingway katika nchi yetu na maandishi aliyoandika. Kozi niliyotunga ilikuwa na lengo hili. Nilitaka pia kuwasaidia walimwengu kuelewa umuhimu wa Afrika katika maisha na uandishi wa Hemingway. Kwa msingi huo huo, nilishiriki kikamilifu katika kufanikisha filamu ya Papa's Shadow.

Nimeeleza hayo yote ili kuweka wazi umuhimu wa ujumbe wa Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa. Ni mfano wa mshikamano unaotakiwa baina yetu wanadiaspora, serikali, na wananchi wenzetu.

Wednesday, September 16, 2015

Filamu ya "Papa's Shadow:" Fursa ya Kuitangaza Tanzania

Nina furaha kuandika kuhusu filamu ambayo imeandaliwa iitwayo "Papa's Shadow," inayomhusu mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Katika filamu hiyo, ninaonekana nikiongea na Mzee Patrick Hemingway, ambaye ni mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye hai. Ana umri wa miaka 87. Tunaongelea maisha, safari, maandishi na fikra za Hemingway, hasa kuhusu Afrika.

Sehemu nyingi hapa duniani ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari zake, zimejipatia umaarufu. na zinafaidika hasa katika utalii. Mifano ni Cuba na mji wa Pamplona nchini Hispania. Watu wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla tuna bahati hiyo, kwani Hemingway alikuja na kuishi kwetu mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54, akaandika vitabu, hadithi, insha na barua kuhusu aliyoyaona.

Filamu ya "Papa's Shadow" ilitokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013 juu ya Hemingway. Kozi ile ilimhamasisha Jimmy Gildea, mmoja wa wanafunzi wangu, kutengeneza filamu hiyo. Alianzisha kampuni, Ramble Pictures, akaanza kutegeneza hiyo filamu ya kuelimisha. Anaendelea kutengeneza filamu zingine zenye kuelimisha.

"Papa's Shadow" inaitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Kuna kampeni ya kuchangisha fedha za kumalizia malipo ya usajili na taratibu zingine kabla ya filamu kuonyeshwa na kusambazwa. Naleta hapa ujumbe ambao umeandikwa na binti yangu Zawadi, mmoja wa watu wanaojitolea katika Ramble Pictures, unaoelezea kampeni hiyo.

Nitapenda ujumbe huu uwafikie wa-Tanzania popote duniani, hasa wanadiaspora, ofisi za ubalozi, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, na wadau wengine wote. Nilitumia miaka kadhaa kusoma maandishi ya Hemingway na kuandaa kozi ambayo ni chimbuko la filamu hii. Ninapangia kuendelea kufundisha kozi hiyo. Nawe m-Tanzania mwenzangu una fursa ya kutoa mchango wako. Tushirikiane. Tutafanikiwa. Sisi tuliokuwepo wakati Tanganyika ilipopata Uhuru tunakumbuka kauli mbiu ya Mwalimu Nyerere ya kuhimiza maendeleo ya Taifa jipya: "It can be done; play your part."

=====================================================

Hello!

My name is Zawadi Mbele, and I am contacting you today to let you know about an amazing project. Ramble Pictures, a Minneapolis-based, independent film company, recently launched a 30-day "Kickstarter" campaign in order to raise funds for the distribution of our completed documentary, Papa's Shadow.

Papa's Shadow is a personal film about Ernest Hemingway in East Africa. It explores his hunting expeditions and holds key dialogues on subjects such as race, language, and the cultures that distinguish us as citizens of the world. Featuring exclusive testimony by Ernest's only living son, Patrick Hemingway, as well as Tanzanian author and Hemingway scholar, Dr. Joseph Mbele, this documentary explores the integral role of two safaris in their shaping of an author and demise of a legend. 

Over the past four years, hard work and creative energy has been poured into making this feature-length documentary. The film has already been completed, however, we cannot show or distribute the film until we finish paying for copyright licensing. Again, please visit our Kickstarter webpage to learn more about how you can play an important role in bringing this documentary to distribution. Also, with Kickstarter, we are offering exclusive rewards with every donation, such as the new Hemingway Library Edition of "Greens Hills of Africa," signed by Patrick Hemingway. 

If there is someone else from your organization you would recommend contacting, we would be grateful to have our information passed along. If you can, please take the time to explore our webpage and let me know if you have any questions at all. You can email me directly or email Elizabeth Turner at elizabeth@ramblepictures.com.

Thank you for your time, and we look forward to hearing back from you!

Sincerely,

Zawadi Mbele
email: zawadi.mbele@gmail.com

Wednesday, September 9, 2015

Vijana Wameonana Na Mzee Patrick Hemingway

Leo nimepata ujumbe na picha kutoka kwa Jimmy Gildea, anayeonekana kushoto kabisa pichani hapa kushoto, kwamba walikuwa mjini Bozeman, Montana, wakingojea kuonana na Mzee Patrick Hemingway na mkewe Mama Carol.

Jimmy alikuwa ni mmoja wa wanafunzi wangu katika kozi ya Hemingway in East Africaambayo nilifundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013. Kutokana na kozi ile, na pia safari tuliyofunga kwenda Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, Jimmy ametengeneza filamu iitwayo Papa's Shadow, ambayo kwa kiasi kikubwa inatokana na kozi ile.

Katika filamu hii, ambayo si ya maigizo, Mzee Patrick Hemingway na mimi tunaongelea maisha na maandishi ya baba yake, Ernest Hemingway, na tunaongelea kwa undani zaidi maisha na mizunguko yake Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54, na pia falsafa yake kuhusu masuala ya maisha na uandishi. Katika kutengeneza filamu hiyo, Jimmy ameshirikiana na hao vijana wanaoonekana pichani, na wengine ambao hawamo pichani.

Nimetamani sana kama nami ningekuwa Bozeman leo kuonana na Mzee Patrick Hemingway na Mama Carol. Hata hivi, nafarijika kwamba ninampigia simu wakati wowote nikipenda. Kwa kuwa aliishi miaka yapata 25 Tanganyika (na hatimaye Tanzania), ameniambia kuwa anafurahi kuongea na mimi, kwa kuwa hana watu wa kuongea nao kuhusu Tanzania na Afrika.

Kwa upande wangu, najifunza mengi kutoka kwa Mzee Patrick Hemingway, juu ya Ernest Hemingway, waandishi wengine, historia ya Tanganyika, na mambo mengine mengine. Pia ninaguswa kwa jinsi anavyokipenda kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Hata katika filamu ya Papa's Shadow anakitaja na kukinukuu. Katika hiyo picha ya pili, tuliyopiga nyumbani mwake mjini Craig, Montana, anaonekana Mzee na Mama Carol Hemingway, na kitabu kiko mezani hapo mbele yake.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...