Showing posts with label The Snows of Kilimanjaro. Show all posts
Showing posts with label The Snows of Kilimanjaro. Show all posts

Wednesday, January 11, 2017

Zawadi Kutoka Ramble Pictures Kwa Heshima Ya Hemingway

Wiki iliyopita nimepata zawadi ya picha kutoka Ramble Pictures, kampuni ya kutengeneza filamu. Kampuni hiyo ndiyo iliyotengeneza filamu ya Papa's Shadow, inayohusu maisha na safari za mwandishi maarufu Ernest Hemingway Afrika Mashariki, pamoja na maandishi yake kuhusu Afrika Mashariki. Sehemu kubwa ya filamu hiyo ni mazungumzo baina ya Mzee Patrick Hemingway na mimi, kuhusu masuala hayo.

Picha niliyopewa inaitangaza filamu ya Papa's Shadow. Inamwonesha Ernest Hemingway, Patrick Hemingway na mimi, Kuna pia Mlima Kilimanjaro na nchi tambarare chini ya mlima, na pia ndege ikiwa angani. Hiyo picha ya mlima na mazingira yake, pamoja na ndege, inakumshia hadithi maarufu ya Hemingway, "The Snows of Kilimanjaro."

Nimeguswa na picha hii. Ni heshima kubwa kuliko ninavyostahili kuwekwa sambamba na Ernest Hemingway na Patrick Hemingway. Ernest Hemingway alileta mapinduzi katika uandishi na alitunukiwa tuzo ya Nobel katika fasihi mwaka 1954. Patrick Hemingway ni mtu muhimu kwa watafiti wa Hemingway, akiwa ni mtoto pekee aliye bado hai wa Ernest Hemingway. Ametoa na anaendelea kutoa mchango mkubwa wa kuhariri maandishi ya Hemingway na kuyaandikia utangulizi.

Kwa upande mwingine ninafurahi kuoneshwa pamoja na Patrick Hemingway, ambaye ni mtu wa karibu kwangu. Ananifundisha mengi kuhusu Afrika Mashariki ya wakati alipoishi kule, kuhusu maisha na uandishi wa Hemingway, na kuhusu waandishi wengine, hasa wa wakati wa Hemingway.

Vile vile, Patrick Hemingway anakipenda sana kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Hata katika filamu ya Papa's Shadow, anakitaja, na kuna mahali anasoma kisehemu cha kitabu hiki kwa ki-Swahili na tafsiri yangu ya ki-Ingereza.

Filamu ya Papa's Shadow inaelezea upande wa Ernest Hemingway ambao haufahamiki vizuri, yaani jinsi alivyovutiwa na Afrika kwa maisha yake yote. Katika kufanya utafiti juu ya Hemingway na kusoma maandishi yake kwa miaka kadhaa, niligundua kuwa aliipenda Afrika tangu alipokuwa mtoto. Ndipo nikaamua kutunga kozi kuhusu mada hiyo.

Mwanafunzi mmoja katika kozi hiyo, Jimmy Gildea, alipata motisha ya kutengeneza filamu, na matokeo yake ni Papa's Shadow. Pamoja na kuelimisha juu ya uhusiano wa Hemingway na Afrika, filamu hii inaitangaza Tanzania. Nakala za filamu hii zinapatikana kwa kuwasiliana na Ramble Pictures kwa barua pepe: info@ramblepictures.com au kwa simu (952) 426-5809.

Wednesday, October 26, 2016

Miaka 80 ya "The Snows of Kilimanjaro"

Kwa mara nyingine tena, ninaandika ujumbe kuhusu kutimia kwa miaka 80 tangu hadithi ya Ernest Hemingway, 'The Snows of Kilimanjaro" ilipochapishwa kwa mara ya kwanza. Niliandika ujumbe wa aina hiyo katika blogu hii. Leo nimesoma tena ujumbe wangu, nikajiridhisha kwamba niliyosema ndiyo ninayoamini hadi sasa.

Jambo moja kubwa kabisa ni kuwa wa-Tanzania tunajipotezea fursa za wazi za kutumia hazina kama hii hadithi ya Hemingway kuitangaza nchi yetu. Niliandika katika ujumbe wangu baadhi ya mambo ambayo tungeyafanya mwaka huu wa kumbukumbu. Lakini mwaka unaelekea ukingoni, na hakuna tulichofanya. Hii ni hasara ya kukosa utamaduni wa kusoma vitabu. Tunashindwa hata kutumia fursa zilizo wazi.

Nimeona niandike ujumbe huu leo kwa sababu wiki hii, hapa katika Chuo cha St. Olaf ninapofundisha, litatokea jambo la pekee linalohusiana na Ernest Hemingway. Keshokutwa, tarehe 28, pataonyeshwa kwa mara ya kwanza filamu ya "Papa's Shadow," ambayo niliwahi kuielezea katika blogu hii.

Hiyo ni filamu iliyotokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwaka 2013 iitwayo Hemingway in East Africa. Nilisafiri na wanafunzi 29 wa Chuo cha St. Olaf, tukazunguka maeneo kadhaa ya Tanzania kaskazini, ambamo alipita Ernest Hemingway mwaka 1933-34. Katika safari hiyo, tulikuwa tunasoma maandishi ya Hemingway kuhusu maeneo hayo na maeneo mengine ambayo alipitia mwaka 1953-54.

Maandishi hayo ni pamoja na Green Hills of Africa na Under Kilimanjaro, ambavyo ni vitabu, kadhalika hadithi fupi mbili: "The Short Happy Life of Francis Macomber" na "The Snows of Kilimanjaro." Pia aliandika makala katika magazeti na barua nyingi akielezea aliyoyaona na kufanya katika safari zake. Kwa ujumla wake, maandishi haya ya Ernest Hemingway yanaitangaza nchi yetu na Afrika Mashariki kwa ujumla kwa namna ambayo sisi wenyewe hatujaweza kujitangaza.

Hiyo filamu ya "Papa's Shadow" inawasilisha vizuri mambo muhimu ya uhusiano wa Ernest Hemingway na Afrika Mashariki. Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway. Tunajadili kwa kina na mapana fikra za Ernest Hemingway kuhusu Afrika, uandishi, na maisha kwa ujumla.

Kwa kuwa hiyo filamu inaonyesha sehemu mbali mbali za Tanzania na maelezo kuhusu mambo yanayoifanya Tanzania kivutio kwa watalii, kama vile Mlima Kilimanjaro, na kwa kuwa filamu hii imejengeka katika maandishi ya Ernest Hemingway, mwandishi maarufu sana ulimwenguni, ni wazi kuwa filamu hii itakuwa chachu ya kuitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Taarifa zaidi Kuhusu "Papa's Shadow," zinapatikana kwenye tovuti ya Ramble Pictures.

Thursday, May 26, 2016

"The Snows of Kilimanjaro" Yatimiza Miaka 80

Mwaka huu 2016, The Snows of Kilimanjaro, hadithi maarufu ya Ernest Hemingway, inatimiza miaka 80 tangu ichapishwe kwa mara ya kwanza. Ilichapishwa katika jarida la Esquire, toleo la Agosti, 1936. Sidhani kama kuna hadithi fupi katika fasihi ya ki-Ingereza inayofahamika na ni maarufu kuzidi The Snows of Kilimanjaro.

Hemingway aliandika utangulizi mfupi wa hadithi yake, ambao unaamsha hisia zinazoendelezwa katika hadithi nzima, ikiwemo hisia ya masuali yasiyojibika:

"Kilimanjaro is a snow covered mountain 19,710 feet high, and it is said to be the biggest mountain in Africa. Its western summit is called the Masai "Ngáje Ngái," the House of God. Close to the western summit there is the dried and frozen carcass of a leopard. No one has explained what the leopard was seeking at that altitude." 

The Snows of Kilimanjaro inamhusu mtu aitwaye Harry, mzungu. Tunamwona akiwa mgonjwa kutokana na kidonda alichopata baada ya kuchomwa na mwiba porini. Kilichosababisha kidonda kufikia hali ya kutishia uhai wake ni kucheleweshwa kwa matibabu. Harry tunamwona amelala kwenye machela huku akihudumiwa na mkewe Helen, mzungu pia. Kuna pia watumishi wa-Afrika.

Mazingira inapotokea hadithi hii ni chini ya mlima Kilimanjaro. Lakini sehemu kubwa ya hadidhi ni kumbukumbu za Harry za mambo aliyofanya au kushuhudia sehemu mbali mbali za Ulaya, kama vile Paris, ikiwemo ushiriki wake katika vita. Juu ya yote, hadithi hii ni mtiririko wa fikra za Harry kuhusu uandishi. Tunamshuhudia akiwazia mengi ambayo alitaka aandike miaka iliyopita, au angependa kuwa ameandika, lakini hakuandika kwa sababu mbali mbali. Anajisikitikia kuwa sasa hataweza kuandika, kwani kifo kinamwelemea. Helen anafanya kila awezalo kumtuliza na kumpa matumaini kuwa atapona. Anamtunza na kujaribu kumzuia kujidhuru kwa ulevi. Anamweleza kuwa ndege itakuja kumwokoa.

Kwa kuwa huu ni mwaka wa kumbukumbu ya miaka 80 ya The Snows of Kilimanjaro, na kwa kuzingatia umaarufu wa Ernest Hemingway ulimwenguni, na umaarufu wa The Snows of Kilimanjaro, na kwa kuwa Mlima Kilimanjaro uko nchini mwetu, hii ilikuwa ni fursa ya kuitangaza nchi yetu. Niliwahi kuandika kidogo kuhusu jambo hili katika blogu hii. Ingekuwa wa-Tanzania tuna utamaduni wa kusoma na kuthamini vitabu, tungeichangamkia fursa ninayoelezea hapa.

Kuna mambo ambayo tungeweza kufanya. Wizara, taasisi na makampuni yanayohusika na utalii yangefurika matangazo na makala juu ya Hemingway na The Snows of Kilimanjaro. Wasomaji wa Hemingway, wanafasihi, na wengine tungekuwa tunafanya mijadala na makongamano. Vyombo vya habari, kama vile magazeti na televisheni, vingekuwa vinarusha matangazo na taarifa na mijadala hiyo. Huu ungekuwa mwaka wa kuitangaza nchi yetu na kuwavutia watalii nchini kwetu kwa namna ya pekee kabisa.

Kuna wenzetu ambao wanatumia jina na maandishi ya Hemingway kujitangaza na kuvutia watalii. Mifano ya wazi ni Cuba na mji wa Pamplona ulioko Hispania. Dunia ya leo ya ushindani mkubwa inahitaji ubunifu wa kwenda na wakati.  Dunia si ya kuichezea. Muyaka alitahadharisha hayo aliposema, "dunia mti mkavu, kiumbe siulemele" na tusijidanganye kuwa twaweza "kuudhibiti kwa ndole."

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...