Showing posts with label Montana. Show all posts
Showing posts with label Montana. Show all posts

Sunday, May 22, 2016

Leo Nimemwandikia Mzee Patrick Hemingway

Leo nimemwandikia barua pepe Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliye hai wa mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Nilipiga naye picha inayoonekana hapa kushoto tarehe 27 Aprili, 2013, nyumbani pake mjini Craig, katika jimbo la Montana.

Nilifahamu habari zake kwa miaka mingi kabla ya kufahamiana naye na halafu tukakutana. Ni mzee mwenye maongezi ya kusisimua kuhusu baba yake Ernest Hemingway na waandishi wengine wa wakati wake. Pia ana kumbukumbu nyingi za Tanganyika, na kisha Tanzania, ambako aliishi kwa miaka yapata 25 kabla ya uhuru na baada ya uhuru, akiendesha kampuni ya utalii, na hatimaye akiwa mkufunzi katika Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori cha Mwika.

Tangu tulipoanza kufahamiana, ameguswa na ari yangu ya kutafiti maandishi, falsafa, na maisha ya Ernest Hemingway, na amevutiwa na msimamo wangu kuwa Ernest Hemingway ni mwandishi aliyetuenzi sana sisi watu wa Afrika Mashariki, na tunapaswa kujielimisha kuhusu mchango wake, na kisha kuutumia katika kujitangaza kama alivyotutangaza.

Hayo yamemfanya Mzee Patrick Hemingway awe tayari kunisaidia kwa dhati katika juhudi zangu za kujielimisha na kuuelimisha ulimwengu juu ya Ernest Hemingway. Miezi kadhaa iliyopita, nilivyomweleza kuwa napangia kutembelea hifadhi ya Ernest Hemingway katika John F. Kennedy Library, aliniambia kuwa nitakapokuwa tayari nimfahamishe ili anitambulishe kwa wahusika.

Nilipoongea naye tarehe 19 mwezi huu na kumtajia tarehe nilizopangia kwenda kwa shughuli hiyo, aliniagiza nimpelekee maelezo yangu kwa barua pepe, ili aweze kuandaa utambulisho huo. Aliniambia kuwa ninakwenda wakati mzuri, kwani kuna maonesho maalum juu ya Hemingway, ambayo yameanza siku chache zilizopita na yatadumu kwa miezi kadhaa.

Basi, leo nimemwandikia. Kilichobaki sasa ni kuandaa safari, nikajionee hiyo hifadhi kubwa kuliko zote duniani juu ya Ernest Hemingway. Hii itakuwa ni mara yangu ya kwanza kuitembelea hifadhi hiyo, lakini sitegemei kuwa itakuwa ni mara ya mwisho.

Monday, December 7, 2015

Nimesaini Vitabu Kwa Ajili ya Filamu ya "Papa's Shadow"

Wakati wa kampeni ya Ramble Pictures ya kuchangisha fedha kulipia gharama za filamu ya Papa's Shadow, nilichangia fedha kiasi na pia nakala za kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Walikuwa wameweka viwango mbali mbali vya michango ambavyo viliendana na vizawadi na vivutio kwa wachangiaji. Waliochangia dola 200 au zaidi waliahidiwa nakala ya kitabu changu kama zawadi.

Leo, Jimmy Gildea, mwanzilishi wa Ramble Pictures na mtengenezaji wa Papa's Shadow, ambaye alikuwa mwanafunzi katika kozi yangu ya Hemingway, alinifuata hapa chuoni St. Olaf, nikasaini nakala tano za kitabu changu, na kumkabidhi.

Tulipata fursa ya kuongelea habari za Ernest Hemingway, ziara yetu ya Montana, msisimko na mafanikio ya kampeni ya kuchangisha fedha, na kadhalika. Vile vile, Jimmy alinirekodi nikiwa nasoma kitabu cha Green Hills of Africa na pia nikiwa natembea katika sehemu iliyoonyesha vizuri mandhari ya chuo. Jimmy aliniuliza iwapo nina picha za ujana na utoto wangu. Anakusanya hayo ili kuyatafutia nafasi katika filamu ya Papa's Shadow, ingawa tayari ni nzuri sana, kwa jinsi nilivyoiona.

Papa's Shadow inategemewa kupatikana wiki chache kuanzia sasa, labda mwezi Februari. Si filamu ya kuigiza bali ni mazungumzo juu ya maisha, uandishi, na falsafa, ya Ernest Hemingway, hasa inavyohusiana na safari zake Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54. Sehemu kubwa ya filamu hii ni mazungumzo baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye bado hai. Ni filamu inayoelimisha, si burudani.

Wednesday, September 9, 2015

Vijana Wameonana Na Mzee Patrick Hemingway

Leo nimepata ujumbe na picha kutoka kwa Jimmy Gildea, anayeonekana kushoto kabisa pichani hapa kushoto, kwamba walikuwa mjini Bozeman, Montana, wakingojea kuonana na Mzee Patrick Hemingway na mkewe Mama Carol.

Jimmy alikuwa ni mmoja wa wanafunzi wangu katika kozi ya Hemingway in East Africaambayo nilifundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013. Kutokana na kozi ile, na pia safari tuliyofunga kwenda Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, Jimmy ametengeneza filamu iitwayo Papa's Shadow, ambayo kwa kiasi kikubwa inatokana na kozi ile.

Katika filamu hii, ambayo si ya maigizo, Mzee Patrick Hemingway na mimi tunaongelea maisha na maandishi ya baba yake, Ernest Hemingway, na tunaongelea kwa undani zaidi maisha na mizunguko yake Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54, na pia falsafa yake kuhusu masuala ya maisha na uandishi. Katika kutengeneza filamu hiyo, Jimmy ameshirikiana na hao vijana wanaoonekana pichani, na wengine ambao hawamo pichani.

Nimetamani sana kama nami ningekuwa Bozeman leo kuonana na Mzee Patrick Hemingway na Mama Carol. Hata hivi, nafarijika kwamba ninampigia simu wakati wowote nikipenda. Kwa kuwa aliishi miaka yapata 25 Tanganyika (na hatimaye Tanzania), ameniambia kuwa anafurahi kuongea na mimi, kwa kuwa hana watu wa kuongea nao kuhusu Tanzania na Afrika.

Kwa upande wangu, najifunza mengi kutoka kwa Mzee Patrick Hemingway, juu ya Ernest Hemingway, waandishi wengine, historia ya Tanganyika, na mambo mengine mengine. Pia ninaguswa kwa jinsi anavyokipenda kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Hata katika filamu ya Papa's Shadow anakitaja na kukinukuu. Katika hiyo picha ya pili, tuliyopiga nyumbani mwake mjini Craig, Montana, anaonekana Mzee na Mama Carol Hemingway, na kitabu kiko mezani hapo mbele yake.

Friday, May 23, 2014

Tunawazia Kwenda Tena Montana Kuonana na Mzee Patrick Hemingway

Mwishoni mwa mwezi Aprili, mwaka jana nilienda Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway. Huyu ni mzee wa miaka 86 sasa, na ndiye mtoto pekee aliyebaki wa mwandishi maarufu, Ernest Hemingway. Niliandika kifupi kuhusu safari hii katika blogu hii.

Tulisafiri watu watano. Wanafunzi wangu ambao wanaonekana kushoto kabisa pichani, baba ya huyu mwanafunzi aliyevaa kaptura, na rubani wa ndege ya huyu baba mzazi. Mzazi wa mwanafunzi na rubani wake hawamo pichani. Mzee anayeonekana pichani ndiye Mzee Patrick Hemingway. Hapa tuko nje ya nyumba yake iliyoko katika mji mdogo wa Craig. Maskani yake hasa hasa, kwa miaka mingi, ni katika mji wa Bozeman, Montana.

Wanafunzi hao wawili ni kati ya wanafunzi 29 wa chuo cha St. Olaf, ambao nilienda nao Tanzania mwezi Januari, 2013, kuwasomesha kuhusu maandishi na safari za Hemingway katika Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54.

Wakati tukiwa Tanzania, wanafunzi hao walinisikia nikiongelea habari za Mzee Patrick Hemingway, kwamba ni mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway, na kwamba nina mawasiliano naye kwa simu, na kwamba ninapangia kwenda Montana kuonana naye.

Huyu mwanafunzi aliyevaa kaptura alisema bila kusita kuwa baba yake angewezeza kutupeleka Montana kwa ndege yake. Hatimaye, siku tuliyopanga, alikuja na ndege yake hapa Minnesota, akitokea nyumbani kwake Ohio. Tulipokutana, nilikuja kufahamu kuwa baba huyu sio tu shabiki wa maandishi ya Hemingway, lakini pia ni msomaji hodari wa vitabu, vya fasihi ya ki-Ingereza, ingawa shughuli zake kimaisha ni biashara.

Kama nilivyogusia kabla, Mzee Patrick Hemingway aliwahi kuishi Tanzania kwa miaka yapata 25 akifanya shughuli kadhaa, ikiwemo ya utalii na kufundisha chuo cha Mweka. Alitukaribisha vizuri sana, tukaongea naye kwa masaa mengi. Huyu mwanafunzi mwingine ni mpiga picha na video, na alirekodi mazungumzo hayo, ambayo ni hazina kubwa. Yana mengi kuhusu maisha, maandishi na mitazamo ya Hemingway, na pia habari nyingi kuhusu waandishi wengine wa nyakati za Hemingway, hasa wale waliokuwa na mawasiliano au uhusiano na Hemingway.

Tuliwazia kwenda tena Montana huu mwezi Mei, kama mwaka jana, lakini kutokana na mimi kuumwa tangu mwanzo wa mwaka, hatujaweza kufanya hiyo safari. Tuna matumaini ya kwenda baada ya miezi michache kuanzia sasa, nitakapokuwa nimepona kabisa, Mungu akipenda.

Kuna mengi bado ya kuongea na Mzee Patrick Hemingway. Jambo moja muhimu ni maisha yake Tanzania. Hilo ni suala ambalo napenda kulifuatilia sana, hasa nikizingatia kuwa mwaka 1954, Hemingway mwenyewe alikwenda hadi Iringa kumtembelea mwanao Patrick akakaa yapat5a wiki tatu. Hiyo ni habari ambayo nataka kuifuatilia kwa undani. Hatujui, huenda Hemingway aliandika hiki au kile kuhusu Iringa, kwani hakuwa mtu aliyekaa mahali asiandike mambo ya mahali hapo. Suala hili linahitaji kufanyiwa utafiti wa kina katika hifadhi ya maandishi ya Hemingway yaliyoiko Cuba na pia maktaba ya John F. Kennedy kule Boston. Mungu akinijalia uzima, nategeme4a kwenda huko miaka ya usoni.

Friday, May 3, 2013

Chakula cha Jioni na Mzee Patrick Hemingway

Kwa siku mbili tatu hivi, nimeandika kuhusu ziara yangu Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliye bado hai wa mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Kwa mfano, soma hapa.

Nilienda na wanafunzi wawili, ambao walikuwa miongoni mwa wanafunzi niliowapeleka Tanzania mwezi Januari mwaka huu, kwa kozi niliyoiita "Hemingway in East Africa." Katika  msafara wetu, alikuwepo pia baba mzazi wa mwanafunzi mmojawapo, ambaye alitupa usafiri wa ndege yake, na rubani wake.

Katika picha hapa kushoto, tunaonekana wote, na mwenyeji wetu, Mzee Patrick Hemingway na mkewe Carol, wakati wa chakula cha jioni. Kutoka kulia kwenda kushoto hapo mezani ni mwanafunzi Jimmy, Mzee Patrick Hemingway, Bwana Cooper (mwenye ndege), rubani, mwanafunzi Clay, Mama Carol, na mimi.

Tulienda kupata chakula cha jioni siku tuliyowasili Montana, yaani tarehe 27. Ilikuwa ni baada ya masaa kadhaa ya kuongea na Mzee Patrick Hemingway, akajibu masuali yangu kuhusu baba yake Ernest Hemingway na maandishi yake yahusuyo Afrika. Hiyo ndiyo ilikuwa sababu ya mimi kuandaa safari hii ya kwenda kumwona.

Mazungumzo yetu yalikuwa marefu, na ilifikia wakati niliona nihitimishe, ili kutomchosha sana Mzee wetu. Lakini Mzee Hemingway ni mwongeaji sana. Pamoja na uzee wake, ana kumbukumbu nzuri sana ya mambo na anapenda kusimulia michapo ya miaka ile ya zamani, ikiwemo ile inayomhususu Ernest Hemingway.

Ziara yetu ilikuwa ya mafanikio makubwa sana. Sote tunakubaliana hivyo, akiwemo Mzee Patrick Hemingway mwenyewe, kama alivyonieleza leo kwenye simu. Leo nimepata barua kutoka kwa mzee mwenye ndege, na kati ya mambo aliyoandika ni "It was a truly remarkable, memorable, and thought provoking weekend."

Tuesday, April 30, 2013

Safari ya Montana Kumwona Mzee Patrick Hemingway

Juzi nilileta ujumbe kuwa nimepata fursa ya kuonana na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliye bado hai wa mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Kwangu kama mtafiti na mwalimu, tukio hili ni la kukumbukwa daima. Hapa napenda tu kuongelea mipango ya safari ilivyokuwa.

Nilipokuwa Tanzania mwezi Januari na wanafunzi nikiwafundisha kozi kuhusu Ernest Hemingway, niliwaambia wanafunzi kuwa mtoto pekee aliyebaki wa Ernest Hemingway nina mawasiliano naye kwa simu, na kwamba ni mzee wa miaka 85. Niliwaambia pia kuwa ninapangia kwenda kuonana naye. Mwanafunzi mmoja ambaye amekuwa akirekodi kozi yangu na habari zinazohusika alisema atapenda tutanguzane kwenye hiyo safari. Mwanafunzi mwingine alisema kuwa ana hakika kuwa baba yake atatupeleka kwa ndege yake.

Baada ya kurejea Marekani, tuliendelea na mipango yetu. Niliwasiliana kwa karibu na Mzee Hemingway na huyu kijana wa mwenye ndege aliwasiliana na baba yake, tukakubaliana tufanye safari tarehe 27 wikiendi iliyopita.

Mzee mwenye ndege alikuja kutoka kwao Ohio na rubani wake, nasi tukajumuika nao katika uwanja mdogo wa Lakeville, inavyoonekana pichani kushoto. Kulia kabisa ni mzee mwenye ndege. Kijana wake ni huyu aliyevaa kaptula. Kijana huyu na huyu mwenzake mrefu kabisa ndio wale walifika Tanzania kwenye kozi yangu.

Mzee huyu ni msomi na msomaji wa vitabu. Ni msomaji makini wa mwandishi Hemingway. Wakati nilipokuwa nafundisha kozi yangu kule Tanzania, alitafuta silabasi kutoka chuoni kwangu akafuatilia kozi nzima.

Mzee Hemingway alikuwa ametushauri tukatue uwanja wa Great Falls, Montana. Safari ilichukua yapata masaa matatu, baada ya kutua kwenye mji wa Bismarck, Dakota ya Kaskazini, kwa ajili ya kupata mafuta ya ndege. Hali ya hewa ilikuwa nzuri njia nzima.

Baada ya kufika Great Falls, tulichukua gari tukaenda kwenye mji mdogo wa Craig, ambako Mzee Hemingway alisema angekuwepo.
Tulipata msisimko mkubwa tulipomwona anatungoja nje ya nyumba yake. Nilimwomba hapo hapo tupige picha, kabla hatujaingia ndani kwa mazungumzo, ambayo nitaelezea baadaye. Nimeandika ujumbe huu kwa lengo la kujitunzia kumbukumbu. Mengine ya msingi, yale tuliyojifunza kutoka kwa Mzee Hemingway, yatakuja siku za usoni.

Sunday, April 28, 2013

Hatimaye, Nimeonana na Mzee Patrick Hemingway

Nimerejea jioni kutoka Montana, ambako nilikwenda jana, kuonana na Mzee Patrick Hemingway, mtu maarufu sana. Ni yeye pekee ndiye bado hai kati ya watoto wa mwandishi maarufu Ernest Hemingway.

Mwandishi Hemingway, ambaye alizaliwa mwaka 1899 jirani na Chicago na kufariki 1961, ni maarufu duniani kote. Kwa miaka yapata kumi, nimevutiwa na jinsi alivyoandika kuhusu Afrika, kutokana na kutembelea na kuishi Afrika Mashariki, mwaka 1933-34, na mwaka 1953-54. Ninasoma na kufundisha maandishi ya Hemingway, kama nilivyoandika hapa, na hapa.

Kwa muda mrefu nilitaka niwasiliane na Mzee Patrick Hemingway, ambaye ni mtoto pekee wa Hemingway aliyebaki. Nilifahamu kuwa aliishi Tanzania miaka yapata 25. Moja ya shughuli alizofanya ni kufundisha katika chuo cha Mweka. Nilisoma sana maandishi yake na kusikiliza mazungumzo yake ambayo yako mtandaoni.

Nilijua kuwa huyu ni hazina kubwa kwa yeyote anayefuatilia maandishi na maisha ya Ernest Hemingway. Siku moja, miaka yapata miwili iliyopita, nilijipa moyo nikampigia simu. Nilifurahi jinsi alivyonifanyia ukarimu, tukaongea sana. Kuanzia hapo, nimeongea naye mara kwa mara.

Hatimaye, jana nilisafiri hadi Montana, ambako tumepata fursa ya kuongea kwa masaa mengi, jana na leo. Nimefurahi kwa namna ambayo siwezi hata kuelezea. Nategemea kuandika taarifa mbali mbali za ziara hii siku zijazo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...