Showing posts with label mwandishi. Show all posts
Showing posts with label mwandishi. Show all posts

Tuesday, July 18, 2017

Mhadhiri wa Algeria Amekifurahia Kitabu

Mimi kama mwandishi, ninaguswa na maoni ya wasomaji. Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mhadhiri wa chuo kikuu kimoja cha Algeria, Samir, ambaye tumewasiliana kwa miaka michache, na nilimpelekea nakala ya kijitabu changu, Notes on Achebe's Things Fall Apart.

Nanukuu sehemu ya ujumbe wake:

I hope this finds you safe. I am so pleased to let you know that your book on Achebe's TFA is very helpful!! It really helped me. It is a pleasure also to inform you that I am citing you in my phd thesis on Gender in Ngugi's fiction. Your name will also be cited in my Acknowledgements and Dedications. Thank you so much....We love you much.

Kwa wale wasiojua ki-Ingereza, napenda kuelezea anachosema mhadhiri huyu kwa ujumla. Anasema kuwa anategemea ujumbe wake utanifikia nikiwa salama. Amefurahi sana kunifahamisha kuwa kitabu changu kuhusu riwaya ya Achebe ya Things Fall Apart ni mchango mkubwa sana na kimemsaidia sana. Anafurahi kunifahamisha vile vile kuwa ananukuu kitabu changu katika tasnifu yake ya uzamifu kuhusu jinsia katika riwaya za Ngugi wa Thiong'o. Jina langu litatajwa katika orodha ya watu waliochangia tasnifu hii. Anahitimisha kwa kusema, "Asante sana....Tunakupenda sana."

Ujumbe wowote kutoka kwa wasomaji makini una manufaa kwangu kama mwandishi. Ninayachukulia maanani maoni yao, hasa nikijua kuwa wametumia hela zao kununua kitabu changu. Kuna wengine ambao ninakuwa nimewapa nakala ya bure. Hao wanaponiandikia maoni yao juu ya kitabu ninaona kama wamelipa fadhila. Maoni yao ni muhimu kwangu kuliko hela.

Kitabu hiki na vingine vinapatikana hapa

Friday, May 5, 2017

Mwanahabari Amy Goodman Amehutubia Hapa Kwetu

Leo, mwanahabari na mwanaharakati maarufu Amy Goodman amehutubia chuoni Carleton hapa Northfield. Mada yake ilihusu "threats to freedom of the press and the importance of independent media," yaani mambo yanayotishia uhuru wa vyombo vya habari na umuhimu wa media zisizo chini ya mamlaka yoyote. Ninaamini tafsiri yangu inaweza kuboreshwa.

Amy Goodman ni maarufu kama mwendesha kipindi kiitwacho Democracy Now!, ambacho kinachambua masuala kwa mtazamo tofauti na ule wa watawala wakandamizi na propaganda zao za kurubuni watu na kuhalalisha hali iliyopo. Mtazamo wa Amy Goodman ni wa kichochezi kwa maslahi ya walalahoi, wavuja jasho, na wale wanaoonewa na kudhulumiwa. Ni mwana harakati ambaye hasiti kujitosa sehemu ambapo watu wanadhulumiwa ili kuwaunga mkono na kuwezesha sauti zao kusikika ulimwenguni.

Katika mhadhara wake wa leo, ameongelea zaidi hali ya Marekani, akiainisha madhaifu ya vyombo vya habari na media kwa ujumla. Alianza hotuba yake kwa kauli ya kusisimua na kufikirisha ya Thomas Jefferson, "were it left to me to decide whether we should have a government without newspapers or newspapers without a government, I should not hesitate a moment to prefer the latter," yaani "ingekuwa ni mamlaka yangu kuamua kama tuwe na serikali bila magazeti au magazeti bila serikali, nisingesita hata dakika moja kuchagua hilo la pili."

Baada ya hotuba yake, Amy alisaini nakala za kitabu chake, Democracy Now: Twenty Years of Covering the Movements Changing America. Wakati ananisainia, aliniuliza ninatoka wapi. Nilipomtajia Tanzania, alitabasamu, akasema "Julius Nyerere." Niliguswa, ingawa sikushangaa, kuwa Amy ni mmoja wa watu wa ughaibuni wanaomwenzi Mwalimu Nyerere. 

Saturday, January 2, 2016

Kitabu Kinaposainiwa

Leo napenda kuirejesha mada ya kusainiwa vitabu, ambayo nimewahi kuileta katika blogu hii. Wanablogu wengine nao wameiongelea. Kwa mfano, Christian Bwaya amelielezea suala la kusaini vitabu kama jambo la ajabu, akatumia dhana ya muujiza. Nakubaliana na dhana hiyo, kutokana na uzoefu wangu kama mwandishi ambaye nimesaini vitabu vyangu mara nyingi, na pia mnunuaji wa vitabu ambaye nimesainiwa vitabu mara kwa mara. Hapa kushoto ninaonekana nikisaini kitabu changu mjini Faribault, Minnesota. Huyu ninayemsainia ni binti kutoka Sudan.


Ninafahamu muujiza huu unavyokuwa kwa pande zote mbili, mwenye kusaini kitabu chake na mwenye kusainiwa. Ninadiriki kusema kuwa kitendo cha kusainiwa kitabu kinafanana na ibada. Natumia neno ibada kwa maana ile ile ya dhana ya ki-Ingereza ya "ritual." Hapo kushoto anaonekana mwandishi Seena Oromia akinisainia kitabu chake mjini Minneapolis.

Ibada ni sehemu ya kila utamaduni, na kila ibada ina utaratibu wake, iwe ni misa kanisani, mazishi, au kitendo cha watu kula pamoja. Wahusika katika ibada wanapaswa kuzifahamu na kuzifuata taratibu hizo. Ibada ya kusainiwa kitabu ni tukio linalogusa nafsi na hisia ya anayesaini kitabu na yule anayesainiwa kitabu.

Ni tukio linaloambatana na heshima ya aina yake. Angalia tu picha nilizoweka hapa; utaona zinavyojieleza. Kuna usemi katika ki-Ingereza kwamba "A picture is worth a thousand words," yaani picha ina thamani sawa na maneno elfu. Hapa kushoto anaonekana mwandishi Jim Heynen akisaini kitabu chuoni St. Olaf.

Kwa ujumla wewe mwandishi huwajui watu wanaotaka kusainiwa vitabu. Inabidi uwaulize uandike jina gani. Wengine huwa wamenunua vitabu viwili au zaidi. Unawauliza usaini jina gani, kwa kila kitabu, nao wanakutajia jina lao au la mtu mwingine au watu wengine.  Hapa kushoto ninaonekana nikisaini vitabu vyangu katika mkutano Grantsburg, Wisconsin.

Kifalsafa, suala la kumsainia kitabu mtu ambaye humwoni ni jambo linalofikirisha. Mwandishi unajifanya unamjua unayemsainia, ingawa humjui. Naye, atakapokipata kitabu, atajiona kama vile kuna uhusiano baina yake na wewe mwandishi. Anafurahi kama vile mmeonana. Hii dhana ya kuonana imejengeka katika usomaji. Tunaposoma, tunakuwa na hisia ya kukutana na mwandishi, hata kama hayuko mbele yetu kimwili. Lakini tunaposhika kitabu ambacho tumesainiwa, ukaribu huo unakuwa mkubwa zaidi. Ni aina ya undugu.

Hapa kushoto naonekana nikisaini kitabu mjini Brooklyn Park, Minnesota. Ninayemsainia ni Adrian Mack, Mmarekani Mweusi.

Tuesday, October 13, 2015

Michango ya Papa's Shadow Imekamilika

Kwa mwezi mzima kumekuwa na kampeni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya filamu ya Papa's Shadow, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Leo, shughuli imekamilika, masaa sita kabla ya kipindi cha michango kwisha.

Mafanikio haya yamefungua njia kwa mambo makubwa siku zijazo. Papa's Shadow sasa itapatikana kwa wadau, pindi taratibu za malipo zitakapokamilika. Kwangu ni furaha kubwa, kama mchangiaji mkuu wa filamu hiyo, sambamba na Mzee Patrick Hemingway, wa maelezo na uchambuzi juu ya mwandishi Ernest Hemingway. Ninafurahi pia kwamba filamu hii itaitangaza Tanzania kwa namna ya pekee, kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Umaarufu wa Ernest Hemingway ulimwenguni ni wa pekee. Pamoja na kuelezea uhalisi wa maisha ya binadamu, kama walivyofanya waandishi wengine maarufu, pamoja na kuzipa umaarufu kwa maandishi yake sehemu alizotembelea hapa duniani, Hemingway alianzisha jadi mpya kimtindo katika uandishi wa ki-Ingereza. Hilo limesemwa tena na tena na wataalam wa fasihi. Ninaamini kuwa Papa's Shadow itahamasisha ari mpya ya kusoma maandishi ya Hemingway.

Ninafurahi kuwa, katika Papa's Shadow, nimechangia kuleta mtazamo mpya juu ya Hemingway, na kuelekeza mawazo ya wasomaji na wapenzi wa Hemingway upande wa Afrika Mashariki, na hasa Tanzania. Wote waliochangia mradi huu kwa namna moja au nyingine, kwa hali na mali, wana sababu na haki ya kujipongeza.

Wednesday, September 9, 2015

Vijana Wameonana Na Mzee Patrick Hemingway

Leo nimepata ujumbe na picha kutoka kwa Jimmy Gildea, anayeonekana kushoto kabisa pichani hapa kushoto, kwamba walikuwa mjini Bozeman, Montana, wakingojea kuonana na Mzee Patrick Hemingway na mkewe Mama Carol.

Jimmy alikuwa ni mmoja wa wanafunzi wangu katika kozi ya Hemingway in East Africaambayo nilifundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013. Kutokana na kozi ile, na pia safari tuliyofunga kwenda Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, Jimmy ametengeneza filamu iitwayo Papa's Shadow, ambayo kwa kiasi kikubwa inatokana na kozi ile.

Katika filamu hii, ambayo si ya maigizo, Mzee Patrick Hemingway na mimi tunaongelea maisha na maandishi ya baba yake, Ernest Hemingway, na tunaongelea kwa undani zaidi maisha na mizunguko yake Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54, na pia falsafa yake kuhusu masuala ya maisha na uandishi. Katika kutengeneza filamu hiyo, Jimmy ameshirikiana na hao vijana wanaoonekana pichani, na wengine ambao hawamo pichani.

Nimetamani sana kama nami ningekuwa Bozeman leo kuonana na Mzee Patrick Hemingway na Mama Carol. Hata hivi, nafarijika kwamba ninampigia simu wakati wowote nikipenda. Kwa kuwa aliishi miaka yapata 25 Tanganyika (na hatimaye Tanzania), ameniambia kuwa anafurahi kuongea na mimi, kwa kuwa hana watu wa kuongea nao kuhusu Tanzania na Afrika.

Kwa upande wangu, najifunza mengi kutoka kwa Mzee Patrick Hemingway, juu ya Ernest Hemingway, waandishi wengine, historia ya Tanganyika, na mambo mengine mengine. Pia ninaguswa kwa jinsi anavyokipenda kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Hata katika filamu ya Papa's Shadow anakitaja na kukinukuu. Katika hiyo picha ya pili, tuliyopiga nyumbani mwake mjini Craig, Montana, anaonekana Mzee na Mama Carol Hemingway, na kitabu kiko mezani hapo mbele yake.

Tuesday, July 28, 2015

Kitabu Umechapisha, Kazi ni Kukiuza

Pamoja na kuandika vitabu, ninajitahidi kujielimisha kuhusu masuala yanayohusiana na uchapishaji, utangazaji, na uuzaji wa vitabu. Kwa bahati nzuri, kuna vitabu vingi na vingine vinaendelea kuchapishwa, na pia makala nyingi kuhusu masuala hayo.

Napenda kuongelea suala la kukiuza kitabu. Niliwahi kuongelea suala hili katika blogu hii. Nimeliongelea pia katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Ni suali linalonigusa na kunifikirisha daima, nami napenda kuwashirikisha waandishi wengine katika kulitafakari.

Usemi kwamba chema chajiuza, kibaya chajitembeza unaweza kuwa na mantiki nzuri kuhusiana na vitabu. Wateja wakiridhishwa au kufurahishwa na kitabu, hawakosi kuwaambia wengine. Aina hii ya utangazaji, ambayo kwa ki-Ingereza huitwa "word of mouth," ni muhimu sana.

Mimi mwenyewe nimeshuhudia hivyo kutokana na kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Tangu nilipokichapisha kitabu hiki, mwaka 2005, wasomaji wamekuwa wakiwaambia wengine. Kwa lugha ya mitaani, wanakipigia debe.

Waandishi wengi hawajui kuwa baada ya kuchapisha kitabu, wana jukumu la kukitangaza na kukiuza. Wengi wanamtegemea mchapishaji afanye kazi hiyo. Hakuna shaka kwamba mchapishaji hujitahidi kukitangaza kitabu. Anawajibika kufanya hivyo, kwani anatafuta fedha za kugharamia uchapishaji, kuwalipa wafanyakazi wake, na kujipatia faida.

Lakini, waandishi tunapaswa kuona mbali zaidi. Kwanza, tusijiziuke. Mchapishaji hawezi kufanya kila kitu, hata kama angependa. Gharama za kukitangaza kitabu ni kipingamizi kwa mchapishaji, hasa yule ambaye si tajiri.

Pili, dunia inabadilika muda wote, nasi tunawajibika kujifunza mambo mapya muda wote. Leo hii kuna tekinolojia zinazomwezesha mwandishi kujichapishia kitabu chake. Katika mazingira haya, mwandishi anawajibika kubeba jukumu la kutangaza na kuuza kitabu. Si busara kutegemea "word of mouth" pekee.

Haikuwa rahisi kwangu kuanza kuvitangaza vitabu vyangu. Kutokana na malezi, mila na desturi, nilijiuliza italeta picha gani katika jamii iwapo ningekuwa natangaza na kuuza vitabu vyangu. Nilielezea wasi wasi huo katika blogu hii, na jinsi nilivyojikomboa.

Leo sioni tatizo kutangaza vitabu vyangu. Nimejifunza na ninaendelea kujifunza umuhimu na mbinu za kufanya hivyo, kwa kusoma vitabu na makala mbali mbali. Ndio maana mara kwa mara naandika katika blogu hii kuhusu matamasha ya vitabu ninayoshiriki. Kusoma kumenileta katika upeo huu mpya. Elimu ni mkombozi.

Saturday, June 13, 2015

Nimepata Kitabu "Infidel" cha Ayaan Hirsi Ali

Leo nimepata kitabu Infidel cha Ayaan Hirsi Ali ambacho nilikinunua mtandaoni tarehe 3 Juni. Ayaan alizaliwa Somalia, akakulia Somalia, Saudi Arabia, Ethiopia na Kenya. Kisha alihamia u-Holanzi, ambako aliwahi hata kuwa mbunge.

Katika kukua kwake alianza kuhoji malezi ya ki-Islam aliyoyapata, na hatimaye alijitoa katika dini hii na kuwa mtu asiye na dini. Hayo amekuwa akisimulia katika vitabu na mihadhara yake. Kitabu chake cha kwanza, ambacho sina, ni The Caged Virgin: An Emancipation Proclamation for Women and Islam, ambacho Salman Rushdie amekielezea hivi:

This is an immensely important book--passionate, challenging, and necessary. It should be read as widely as possible, because it tells the truth--the unvarnished, uncomfortable truth.

Mtazamo wa Ayaan Hirsi Ali umemletea matatizo makubwa tangu mwanzo. Anatafutwa kuuawa. Alikuwa chini ya ulinzi u-Holanzi na hatimaye alihamia Marekani. Bado anaandika, anatoa mihadhara na anafanya mahojiano.

Baada ya kusikia habari zake kwa miaka kadhaa, niliamua kutafuta ukweli mimi mwenyewe. Nilinunua kitabu chake kiitwacho Nomad, nikakisoma, kama nilivyoandika katika blogu hii. Nilifahamu kuwa kitabu chake kingine kinachofahamika sana ni Infidel. Sikuwa na haraka nacho, kwani ninanunua na kusoma vitabu vingine muda wote.  Lakini, hatimaye, nimeamua kukinunua nikisome. Sijui anasema nini katika kitabu hiki, na duku duku inanisukuma nisome.

Wednesday, January 28, 2015

Katika Blogu, Sijui Ninamwandikia Nani Zaidi Yangu Mwenyewe

Je, mwandishi wa blogu anamwandikia nani? Kwa mtazamo wangu, hili ni suali gumu. Naliona gumu kulitafakari, achilia mbali kulijibu.

Baada ya kuona ugumu wa suali hili, nimeamua kukiri kuwa ninajiandikia mwenyewe. Ndio maana makala ninazoandika aghalabu zinanihusu mimi mwenyewe, shughuli zangu, matatizo na mafanikio yangu, mategemeo yangu na kumbukumbu zangu.

Sipendi sana kuwaongelea watu wengine, wala sipendi sana kuongelea mambo kinadharia, bila kujihusisha mwenyewe. Naweza kusema kuwa ndivyo nilivyoandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Sijajificha nyuma ya pazia la nadharia au taaluma. Nimejiweka wazi kwa namna nilivyoweza.

Mwandishi Ernest Hemingway aliongelea suala hili vizuri alipofafanua dhana ya ukweli katika uandishi. Nilivyomwelewa, anasema kuwa ukweli katika uandishi ni kwa mwandishi kuifungua na kuiweka bayana nafsi yake.

Ningependa sana niweze kuandika namna hii aliyoongelea Hemingway. Ni ndoto inayovutia, sawa na nyota inayong'aa mbali, ambayo mtu unaifuata kwa hamu ingawa haifikiki. Lakini, naona huku ndiko kujiandikia mwenyewe.

Kusema kuwa kuna hadhira ninayoiandikia katika blogu yangu ni kama kuota ndoto. Ni kujidanganya. Nasema hivi sio tu kutokana na tafakari yangu mwenyewe, bali ninakumbuka makala ya kufikirisha ya Walter J. Ong, "The Writer's Audience is Always a Fiction."

(Picha hapo juu nilijipiga mwenyewe jana, kwa ajili ya matangazo ya mihadhara yangu Mankato)

Friday, March 22, 2013

Buriani, Chinua Achebe

Msiba mzito umetufika leo, wasomaji wa fasihi na walimwengu kwa ujumla. Chinua Achebe amefariki, akiwa na umri wa miaka 82.

Maarufu kama muasisi wa fasihi ya ki-Ingereza katika Afrika, Chinua Achebe ametoa mchango mkubwa katika uandishi, mchango ambao uliiweka Afrika mahala pazuri katika ramani ya fasihi ya dunia.

Tangu alipochapisha riwaya yake maarufu, Things Fall Apart, hadi kufariki kwake, Achebe ameandika riwaya, hadithi fupi, na insha kuhusu fasihi, uandishi, siasa na utamaduni. Amefanya mahojiano mengi, ambayo, kwa bahati nzuri yanapatikana mtandaoni au katika vitabu na majarida.

Achebe aliamini kwa dhati kuwa jukumu la msanii ni kuwa mwalimu wa jamii. Yeye mwenyewe amezingati wajibu huo tangu ujana wake, alipochapisha Things Fall Apart, hadi kurariki kwake. Amewafundisha waAfrika mengi kuhusu jamii yao, udhaifu na uwezo wao, na amewafundisha walimwengu kuwaona wa-Afrika kwa mtazamo tofauti na ule wa wakoloni. Amewafundisha walimwengu maana ya ubinadamu, ambayo inavuka mipaka ya kabila, taifa, dini, jinsia au nchi.

Sikupata fursa ya kukutana uso kwa uso na Chinua Achebe, bali nimesoma na kufundisha maandishi yake mara kwa mara. Nashukuru pia kuwa nilipata wazo la kuandika mwongozo wa Things Fall Apart. Kwa namna hiyo ya kusoma na kutafakari maandishi yake, najiona kama vile nami nimekutana na mwandishi huyu. Nimalizie tu kwa kusema kwamba kwa mchango wake mkubwa kwa walimwengu, Achebe atakumbukwa daima.

Friday, November 11, 2011

Nitakutana na Mteja Maarufu

Mara kwa mara napata fursa ya kukutana na wateja. Hao ni watu waliosoma vitabu vyangu au wanapangia kufanya hivyo au wamehudhuria mihadhara yangu. Wengine, ambao hatupati fursa ya kukutana uso kwa uso, wanawasiliana nami kwa barua pepe. Kwangu ni jambo la kushukuru, kwamba Mungu kanijalia uwezo na fursa hizo.

Siku chache zilizopita, nilipata ujumbe kutoka kwa mama mmoja akisema kuwa alipata taarifa zangu kutoka kwa mama mwingine wa Shepherd of the Valley Lutheran Church. Nilivyoangalia mtandaoni, nimegundua kuwa huyu aliyeniandikia ni mtu maarufu.

Wakati anaulizia kama tungeweza kukutana, alisema kuwa amenunua kitabu changu cha Africans and Americans na atakisoma hima. Anapangia kuandika kitabu kingine, na anapenda kusikia mawaidha yangu kuhusu masuala ya utamaduni katika malezi ya watoto.

Huyu namhesabu kama mteja maarufu, kwa vile anafahamika sana kutokana na shughuli zake za kuandika na kuelimisha umma. Nangojea siku tuliyopanga kukutana, wiki ijayo, nikizingatia kuwa mteja ni mfalme.

Nimalizie tu kwa kusema kuwa niliwahi kwenda Shepherd of the Valley kuongelea suala la tofauti za tamadununi. Kanisa hili lina ushirikiano na waumini wa Tungamalenga, Iringa. Nilifanya hiyo shughuli, na sikutegemea kuwa ingezua hayo niliyoeleza hapa juu. Ndivyo mambo yanavyokwenda hapa duniani. Unaweza kufanya jambo, usijue litazua nini, litaishia wapi au vipi.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...