Showing posts with label Jim Heynen. Show all posts
Showing posts with label Jim Heynen. Show all posts

Saturday, January 2, 2016

Kitabu Kinaposainiwa

Leo napenda kuirejesha mada ya kusainiwa vitabu, ambayo nimewahi kuileta katika blogu hii. Wanablogu wengine nao wameiongelea. Kwa mfano, Christian Bwaya amelielezea suala la kusaini vitabu kama jambo la ajabu, akatumia dhana ya muujiza. Nakubaliana na dhana hiyo, kutokana na uzoefu wangu kama mwandishi ambaye nimesaini vitabu vyangu mara nyingi, na pia mnunuaji wa vitabu ambaye nimesainiwa vitabu mara kwa mara. Hapa kushoto ninaonekana nikisaini kitabu changu mjini Faribault, Minnesota. Huyu ninayemsainia ni binti kutoka Sudan.


Ninafahamu muujiza huu unavyokuwa kwa pande zote mbili, mwenye kusaini kitabu chake na mwenye kusainiwa. Ninadiriki kusema kuwa kitendo cha kusainiwa kitabu kinafanana na ibada. Natumia neno ibada kwa maana ile ile ya dhana ya ki-Ingereza ya "ritual." Hapo kushoto anaonekana mwandishi Seena Oromia akinisainia kitabu chake mjini Minneapolis.

Ibada ni sehemu ya kila utamaduni, na kila ibada ina utaratibu wake, iwe ni misa kanisani, mazishi, au kitendo cha watu kula pamoja. Wahusika katika ibada wanapaswa kuzifahamu na kuzifuata taratibu hizo. Ibada ya kusainiwa kitabu ni tukio linalogusa nafsi na hisia ya anayesaini kitabu na yule anayesainiwa kitabu.

Ni tukio linaloambatana na heshima ya aina yake. Angalia tu picha nilizoweka hapa; utaona zinavyojieleza. Kuna usemi katika ki-Ingereza kwamba "A picture is worth a thousand words," yaani picha ina thamani sawa na maneno elfu. Hapa kushoto anaonekana mwandishi Jim Heynen akisaini kitabu chuoni St. Olaf.

Kwa ujumla wewe mwandishi huwajui watu wanaotaka kusainiwa vitabu. Inabidi uwaulize uandike jina gani. Wengine huwa wamenunua vitabu viwili au zaidi. Unawauliza usaini jina gani, kwa kila kitabu, nao wanakutajia jina lao au la mtu mwingine au watu wengine.  Hapa kushoto ninaonekana nikisaini vitabu vyangu katika mkutano Grantsburg, Wisconsin.

Kifalsafa, suala la kumsainia kitabu mtu ambaye humwoni ni jambo linalofikirisha. Mwandishi unajifanya unamjua unayemsainia, ingawa humjui. Naye, atakapokipata kitabu, atajiona kama vile kuna uhusiano baina yake na wewe mwandishi. Anafurahi kama vile mmeonana. Hii dhana ya kuonana imejengeka katika usomaji. Tunaposoma, tunakuwa na hisia ya kukutana na mwandishi, hata kama hayuko mbele yetu kimwili. Lakini tunaposhika kitabu ambacho tumesainiwa, ukaribu huo unakuwa mkubwa zaidi. Ni aina ya undugu.

Hapa kushoto naonekana nikisaini kitabu mjini Brooklyn Park, Minnesota. Ninayemsainia ni Adrian Mack, Mmarekani Mweusi.

Friday, March 4, 2011

Makala Yangu Imepita

Blogu yangu ni sehemu ninapoweka chochote nipendacho, hata mambo binafsi, kama kumbukumbu au hata kujifurahisha. Niliwahi kusema hivyo. Leo nina taarifa ambayo imeniletea furaha moyoni.

Niliandika siku chache zilizopita kwamba mhariri wa jarida la Monday Development alikuwa ameiomba makala yangu, "What is Development?" Baada ya kuikarabati kidogo, niliipeleka.

Ni siku chache tu zimepita, nami nimefurahi kupata ujumbe kutoka kwa msahihisha makala (copy editor) wa jarida hilo. Hakuona kitu cha kusahihisha. Badala yake ameandika: "Thank you for the thoughtful, honest and well-written article."

Kwa huku Marekani, uamuzi wa msahihisha makala ni wa mwisho kabla ya makala kuchapishwa. Taarifa kama hii inaniongezea ari ya kuendelea na jitihada ya kuandika vizuri. Ninajua kuwa ninaweza kuandika vizuri kwa ki-Ingereza. Kama andiko langu likawa si zuri, sababu itakuwa ni uvivu au kukosa muda, sio kutojua ki-Ingereza bora kinakuwaje.

Wakati moja, mwandishi Jim Heynen, ambaye tulikuwa tunafundisha wote katika idara ya ki-Ingereza hapa chuoni St. Olaf, aliiona insha yangu moja fupi, "If You Came Where I was Born," akaomba aitumie katika darasa lake la uandishi kama mfano wa uandishi bora. Aliitumia hivyo hadi alipostaafu. Kutokana na umaarufu wa huyu mwandishi, niliguswa sana na jambo hilo.

Kwa hali hiyo, sikushangaa kupata ujumbe wa msahihisha makala wa Monday Development kuhusu makala yangu. Ila nina furaha sana kutokana na ukweli kwamba mzunguko wa jarida hili ulivyo mpana, makala yangu hii italisambaza jina langu kuliko chochote kingine ambacho nimeandika hadi sasa. Ninahisi hivyo, na ninahisi makala hii fupi itanifungulia milango na fursa mbali mbali, nami sitasita kuweka taarifa hapa katika blogu yangu.

Lakini hayo hayaji kwa muujiza au kwa bahati nasibu. Ni matokeo ya kujituma na kujishughulisha kwa dhati. Pamoja na kuandika, nimejikita katika shughuli ya kufundisha uandishi bora wa ki-Ingereza. Kuangalia na kutathmini uandishi wa wanafunzi na kuona makosa wanayofanya katika kutumia ki-Ingereza na kuyasahihisha imekuwa ni namna ya kujinoa mimi mwenyewe.

Hitimisho langu ni kuwa kama mimi nimefikia hatua hiyo, kutokana na juhudi, kila mtu anaweza pia, katika uwanja wake, kwa kutumia juhudi. Hakuna sababu ya kukata tamaa. Hii ndio habari yangu ya leo, habari binafsi ambayo naamini itawapa moyo wengine, hata kama ni wachache. Inatosha.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...