Showing posts with label uandishi bora. Show all posts
Showing posts with label uandishi bora. Show all posts

Thursday, May 19, 2016

Nimenunua "Good Prose," Kitabu Kuhusu Uandishi

Siku chache zilizopita, katika duka la vitabu la hapa chuoni St. Olaf, nilikiona kitabu kiitwacho Good Prose: The Art of Nonfiction. Jina hilo lilinivutia, nikapata duku duku ya kukiangalia. Nilivyoona kuwa mwandishi mojawapo, Tracy Kidder alikuwa amepata tuzo ya Pulitzer, nilivutiwa kabisa. Hii ni tuzo ya uandishi yenye hadhi kuliko zote zinazotolewa hapa Marekani.

Nilivyochungulia kurasa zake, niliona kina mawaidha mazuri kuhusu uandishi bora. Si uandishi wa kazi za fasihi, bali uandishi kama wa insha. Huu ndio uandishi wangu, na ndio uandishi ninaofundisha. Nilivutiwa pia nilipoona waandishi maarufu wamenukuliwa katika kitabu hiki, kama vile Norman Mailer,  Ernest Hemingway, Vladimir Nabokov, na William Strunk, Jr.

Kwa bahati mbaya sikuwa na hela, nikaondoka bila kukinunua, kwa shingo upande. Leo nilikwenda tena dukani, nikakuta kitabu bado kipo. Nilikinunua hapo hapo.

Pamoja na kwamba nina uzoefu wa miaka mingi wa kufundisha uandishi bora wa ki-Ingereza, na pamoja kwamba ninawafundisha watu ambao ki-Ingereza ni lugha mama yao, siridhiki na ufahamu wangu. Ninajifananisha na waandishi wa ki-ingereza ambao ni maarufu duniani, na hiki ndicho kigezo sahihi, kwani katika kujipima huko, ninatambua kuwa sijawafikia. Kwa hivyo, ninatambua umuhimu wa kujielimisha muda wote. Ni ujinga kuridhika na elimu uliyo nayo.

Mtu ukitaka kujipima katika fani yako, jifananishe na wale walifanikiwa kwa kiwango cha juu kabisa. Kwa mwandishi, naona ni wajibu kujipima dhidi ya waandishi waliotwaa tuzo maarufu kama Nobel, Booker, na Pulitzer. Hapo mtu utatambua kuwa bado una njia ndefu ya kusafiri.

Good Prose: The Art of Nonfiction ni kitabu nitakachokisoma kwa makini. Kimeelezwa kwenye jalada kama "Stories and advice from a lifetime of writing and editing," na kwamba ni "an inspiring book about writing--about the creation of good prose." Bila shaka kitabu hiki kitanihamasisha kutafakari zaidi suala la uandishi bora, suala ambalo nimekuwa nikilizungumzia katika blogu hii.


Thursday, June 2, 2011

Mfano wa Uandishi Bora wa ki-Ingereza

Kusoma kuna faida nyingi. Kusoma vitabu vilivyoandikwa kwa lugha iliyotukuka ni neema. Nina bahati kuwa nafundisha somo la fasihi, na muda wote nawaongoza wanafunzi katika kutafakari na kujadili maandishi bora kabisa kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Wiki chache zilizopita, tulisoma riwaya iitwayo Reef, iliyoandikwa na Romesh Gunesekera wa Sri Lanka na kusifiwa sana na wahakiki. Ingawa riwaya nzima imeandikwa kwa ki-Ingereza kilichopevuka na kinavutia sana, napenda kunukuu kipande kimoja ambacho kilinigusa kwa namna ya pekee. Mwandishi anaelezea safari ya gari katika kisiwa cha Sri Lanka. Ninaposoma uandishi kama huu, uliosheheni maneno na tamathali murua, hadi kuleta picha kamili na ya kugusa ya kile kinachoelezwa, huwa najiuliza kama kweli sisi wa-Tanzania tutaweza kufikia kiwango hiki. Ni changamoto kubwa na ni kipimo cha kujipima uwezo wetu:

We drove for hours; whistling over a ribbon of tarmac measuring the perpetual embrace of the shore and the sea, bounded by a fretwork of undulating coconut trees, pure unadorned forms framing the seascape into a kaleidoscope of bluish jewels. Above us a tracery of green and yellow leaves arrowed to a vanishing-point we could never reach. At times the road curved as though it were the edge of a wave itself rushing in and then retreating into the ocean. We skittered over these moving surfaces at a speed I had never experienced before. Through the back window I watched the road pour out from under us and settle into a silvery picture of serene timelessness. We overtook the occasional bus belching smoke or a lorry lisping with billowing hay; we blasted through bustling towns and torpid villages. We passed churches and temples, crosses and statues, grey shacks and lattice-work mansions.... (uk. 69)

Pamoja na mengine yote tuliyojadili darasani kwangu, niliwaelekeza wanafunzi kwenye kifungu hiki, kama mfano wa uandishi bora wa ki-Ingereza. Wanafunzi hao ni wa-Marekani, ambao lugha yao ni ki-Ingereza. Inakuwa ni changamoto ya aina yake kwao.

Friday, March 4, 2011

Makala Yangu Imepita

Blogu yangu ni sehemu ninapoweka chochote nipendacho, hata mambo binafsi, kama kumbukumbu au hata kujifurahisha. Niliwahi kusema hivyo. Leo nina taarifa ambayo imeniletea furaha moyoni.

Niliandika siku chache zilizopita kwamba mhariri wa jarida la Monday Development alikuwa ameiomba makala yangu, "What is Development?" Baada ya kuikarabati kidogo, niliipeleka.

Ni siku chache tu zimepita, nami nimefurahi kupata ujumbe kutoka kwa msahihisha makala (copy editor) wa jarida hilo. Hakuona kitu cha kusahihisha. Badala yake ameandika: "Thank you for the thoughtful, honest and well-written article."

Kwa huku Marekani, uamuzi wa msahihisha makala ni wa mwisho kabla ya makala kuchapishwa. Taarifa kama hii inaniongezea ari ya kuendelea na jitihada ya kuandika vizuri. Ninajua kuwa ninaweza kuandika vizuri kwa ki-Ingereza. Kama andiko langu likawa si zuri, sababu itakuwa ni uvivu au kukosa muda, sio kutojua ki-Ingereza bora kinakuwaje.

Wakati moja, mwandishi Jim Heynen, ambaye tulikuwa tunafundisha wote katika idara ya ki-Ingereza hapa chuoni St. Olaf, aliiona insha yangu moja fupi, "If You Came Where I was Born," akaomba aitumie katika darasa lake la uandishi kama mfano wa uandishi bora. Aliitumia hivyo hadi alipostaafu. Kutokana na umaarufu wa huyu mwandishi, niliguswa sana na jambo hilo.

Kwa hali hiyo, sikushangaa kupata ujumbe wa msahihisha makala wa Monday Development kuhusu makala yangu. Ila nina furaha sana kutokana na ukweli kwamba mzunguko wa jarida hili ulivyo mpana, makala yangu hii italisambaza jina langu kuliko chochote kingine ambacho nimeandika hadi sasa. Ninahisi hivyo, na ninahisi makala hii fupi itanifungulia milango na fursa mbali mbali, nami sitasita kuweka taarifa hapa katika blogu yangu.

Lakini hayo hayaji kwa muujiza au kwa bahati nasibu. Ni matokeo ya kujituma na kujishughulisha kwa dhati. Pamoja na kuandika, nimejikita katika shughuli ya kufundisha uandishi bora wa ki-Ingereza. Kuangalia na kutathmini uandishi wa wanafunzi na kuona makosa wanayofanya katika kutumia ki-Ingereza na kuyasahihisha imekuwa ni namna ya kujinoa mimi mwenyewe.

Hitimisho langu ni kuwa kama mimi nimefikia hatua hiyo, kutokana na juhudi, kila mtu anaweza pia, katika uwanja wake, kwa kutumia juhudi. Hakuna sababu ya kukata tamaa. Hii ndio habari yangu ya leo, habari binafsi ambayo naamini itawapa moyo wengine, hata kama ni wachache. Inatosha.

Friday, December 10, 2010

Laiti Ningekuwa Kama Hemingway

Laiti ningekuwa kama Hemingway, mwandishi maarufu sana duniani. Ningeandika kuhusu nchi yangu na watu wake kwa umakini, ubunifu, na ukweli wa kumgusa kila msomaji. Ningeandika kuhusu maziwa, mito, milima na mabonde. Ningeandika kuhusu fukwe, nyanda na visiwa. Ningeandika kuhusu miji na vijiji, mitaa na vitongoji.

Nimetamka hayo, na nimeanza kufanya mazoezi. Lakini bado njia ni ndefu mbele yangu.

Laiti ningekuwa kama Hemingway, aliyeangalia mazingira, matukio, na tabia za wanadamu kwa macho na akili yote, aliyejawa nidhamu ya kutumia lugha, akiangalia kila neno, tena na tena, akibadili na kusahihisha tena na tena, akitafuta namna ya kuandika sentensi sahihi yenye ukweli mtupu.

Laiti ningekuwa kama Hemingway, aliyetufundisha kuwa kazi ya mwandishi ni kujitoa mhanga ili nafsi yake yote ibakie katika kitabu tu, asibakishe hata chembe nje ya kitabu. Kila kitabu kiwe ni mauti ya mwandishi, vinginevyo kitabu hiki ni mzaha na udanganyifu. Je, nitayaweza hayo?

Hemingway aliandika kuhusu nchi mbali mbali alizozitembelea, ikiwemo nchi yangu. Nimekutana na watu wa nchi mbali mbali wanaomshukuru Hemingway kwa hilo. Tutalipaje fadhila, isipokuwa kwa kujijengea nidhamu ya kuyaangalia mazingira na maisha, nidhamu ya kuiheshimu lugha na sentensi, tuweze nasi kuandika mambo ya thamani? Tutalipaje fadhila kama hatuna ushujaa wa kuwa wakweli kama Hemingway?

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...