Showing posts with label wasomaji. Show all posts
Showing posts with label wasomaji. Show all posts

Sunday, April 15, 2018

Mialiko kwa Mwandishi wa Kitabu

Kutokana na mawasiliano kutoka kwa waandishi chipukizi Tanzania ninafahamu kuwa hao ni miongoni mwa wasomaji wa blogu yangu hii ambamo ninaandika mara kwa mara kuhusu vitabu. Mbali na kuviongelea vitabu, nimekuwa nikiandika kuhusu uandishi, uchapishaji, na uuzaji wa vitabu kutokana na uzoefu wangu.

Leo ninapenda kuongelea kipengele cha mialiko kwa mwandishi wa kitabu, jadi ninayoiona hapa Marekani, mwandishi kualikwa kuzungumza sehemu mbali mbali baada ya kuchapisha kitabu. Mada hii nimeigusia kwa kiasi fulani katika blogu hii Hata hivyo, nimeona niongezee neno.

Kama wewe ni mfuatiliaji wa blogu yangu hii, utakuwa unafahamu kuwa ninapata mialiko mara kwa mara kuongelea mada zinazohusiana na vitabu vyangu: Matengo Folktales na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Suali ni je, kwa nini watu wanialike badala ya wao kusoma tu nilichoandika? Wananialika nikawasomee?

Jibu ni hapana. Kinachowafanya wanialike ni kutambua kwao, baada ya kusoma kitabu, kwamba wana mambo yatokanayo na yale yaliyomo kitabuni ambayo wangetaka kuyafahamu zaidi. Kitabu changu si kwamba kinajitosheleza, bali kina madokezo muhimu. Ni chachu ya dukuduku kwa wasomaji. Hata kama hakijitoshelezi, wanavutiwa na mwelekeo wa fikra. Hiyo ni sababu muhimu ya kunialika nikazungumze nao.

Wengine wakishasoma kitabu, wanakuwa na imani kwamba ninaweza kuwasaidia mawazo juu ya mipango wanayotaka kutekeleza au mambo yanayowakabili. Kwa mfano, viongozi wa kampuni au taasisi wanaona kwamba ninaweza kuwasaidia katika kuzielewa na kuzitatua changamoto zitokanazo na kuwa na timu ya watu wa tamaduni mbali mbali. Mfano ni nilivyoalikwa RBC Wealth Management.

Kuhusu kitabu cha Matengo Folktales, watu wanataka kufahamu zaidi juu ya utamaduni wa kusimulia hadithi ulivyo Afrika na pia wanataka kusikiliza hadithi zinavyosimuliwa. Ndivyo ilivyokuwa nilipoalikwa chuo kikuu cha St. Benedict/St. John's na pia maktaba ya Redwing.

Kwa upande wa Tanzania, jadi hii ya kuwaalika waandishi kuzungumzia uandishi na vitabu ingekuwa na manufaa kama ilivyo Marekani. Waandishi wangekuwa wanaielimisha jamii uzoefu wao katika vipengele mbali mbali, kama vile jinsi walivyopata wazo la kuandika au walivyoanza kuandika, mchakato wa uandishi, ugumu au urahisi wake, vipingamizi, uchapishaji, uhusiano na wachapishaji, wasomaji, wahakiki, na wauzaji wa vitabu. Waandishi wangetumia fursa hizi kutoa ushauri kwa waandishi chipukizi.

Katika mkutano na mwandishi, vitabu vya mwandishi vinaweza kuwepo, ili wahudhuriaji wanunue. Huu ni utaratibu unaofanyika sana hapa Marekani. Ni njia nzuri ya vitabu kuifikia jamii. Vile vile, kwa uzoefu wangu hapa Marekani, uwepo wa mwandishi na jinsi anavyojieleza, kunawavutia watu kununua kitabu. Kitu kingine kinachovutia ni kusainiwa kitabu na mwandishi, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii, katika kubadilishana mawazo na mwanablogu Christian Bwaya.

Tuesday, July 18, 2017

Mhadhiri wa Algeria Amekifurahia Kitabu

Mimi kama mwandishi, ninaguswa na maoni ya wasomaji. Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mhadhiri wa chuo kikuu kimoja cha Algeria, Samir, ambaye tumewasiliana kwa miaka michache, na nilimpelekea nakala ya kijitabu changu, Notes on Achebe's Things Fall Apart.

Nanukuu sehemu ya ujumbe wake:

I hope this finds you safe. I am so pleased to let you know that your book on Achebe's TFA is very helpful!! It really helped me. It is a pleasure also to inform you that I am citing you in my phd thesis on Gender in Ngugi's fiction. Your name will also be cited in my Acknowledgements and Dedications. Thank you so much....We love you much.

Kwa wale wasiojua ki-Ingereza, napenda kuelezea anachosema mhadhiri huyu kwa ujumla. Anasema kuwa anategemea ujumbe wake utanifikia nikiwa salama. Amefurahi sana kunifahamisha kuwa kitabu changu kuhusu riwaya ya Achebe ya Things Fall Apart ni mchango mkubwa sana na kimemsaidia sana. Anafurahi kunifahamisha vile vile kuwa ananukuu kitabu changu katika tasnifu yake ya uzamifu kuhusu jinsia katika riwaya za Ngugi wa Thiong'o. Jina langu litatajwa katika orodha ya watu waliochangia tasnifu hii. Anahitimisha kwa kusema, "Asante sana....Tunakupenda sana."

Ujumbe wowote kutoka kwa wasomaji makini una manufaa kwangu kama mwandishi. Ninayachukulia maanani maoni yao, hasa nikijua kuwa wametumia hela zao kununua kitabu changu. Kuna wengine ambao ninakuwa nimewapa nakala ya bure. Hao wanaponiandikia maoni yao juu ya kitabu ninaona kama wamelipa fadhila. Maoni yao ni muhimu kwangu kuliko hela.

Kitabu hiki na vingine vinapatikana hapa

Friday, July 7, 2017

Wadau Wangu Wapya

Nina furaha kama mwandishi kuwa nimejipatia wadau wapya, na ninawatambulisha hapa kama ilivyo kawaida yangu. Hao ni Brian Faloon na mkewe Kristin, wenyeji wa Rochester, Minnesota. Brian ni rais wa Rochester International Association (RIA). Kristin na mimi ni wanabodi katika bodi ya RIA, ambamo nilijiunga mwaka jana kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Baada ya mimi kujiunga na bodi, nilipata fursa ya kutoa mhadhara katika chuo kikuu cha Minnesota Rochester, mada ikiwa "Folklore as Expression of Ethics," kama nilivyoeleza katika blogu ya ki-Ingeeza. Brian alihudhuria.

Brian aliuongelea mhadhara ule katika mkutano uliofuata wa bodi ya RIA. Baada ya muda, nilipata mwaliko wa kutoa mhadhara chuo kikuu cha Winona, mwaliko ambao niliuelezea katika blogu hii. Kristin aliniuliza iwapo itawezekana yeye kuhudhuria. Niliwasiliana na waandaaji, kuwauliza iwapo ninaweza kumwalika mgeni kuhudhuria, nikajibiwa kuwa ni ruksa. Nilimweleza Kristin hivyo.

Nilisafiri tarehe 27 Juni hadi Winona, mwendo wa saa mbili. Nilivyoingia ukumbini, niliwakuta Kristi na Brian wameketi, pamoja na wasikilizaji wengine yapata 50. Nilitambulishwa na wenyeji wangu, nikatoa mhadhara kama nilivyoelezea katika blogu ya ki-Ingereza. Nilivyomaliza mhadhara na muda wa masuali na majibu, Kristin na Brian walinisogelea tukaongea. Walifurahia mhadhara. Nilivyowashukuru kwa kusafiri mwendo mrefu na kuhudhuria, walinijibu kuwa wao ni mashabiki wangu. Walichosema ni ukweli, kwani walianza kuwa wadau tangu waliposoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Tarehe 4 Julai, nilipata ujumbe kutoka kwa Kristin. Kati ya mambo aliyoandika ni haya:

We greatly enjoyed hearing your presentation and thought it was very good! Thank you for letting us attend! I believe it would be an excellent presentation to do in our community and schools here in Rochester as we have the same tensions between the two groups....I would like to coordinate something when we have time. We can discuss it at the next meeting if you're interested.

Ninajivunia hao wadau wangu wapya. Moyo wangu wa kutumia ujuzi wangu kwa manufaa ya walimwengu unaniletea fursa kama hii anayoongelea Kristin. Ninazipokea fursa hizi kwa moyo mkunjufu. Ninaamini ni mipango ya Mungu, wala sijali suala la kulipwa au kutolipwa fedha, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Mungu ana mipango yake, na anasawazisha mambo.

Friday, April 14, 2017

Neno Kuhusu Matokeo ya Kuchapisha Kitabu

Mimi kama mwandishi wa vitabu ninafurahi ninapopata wasaa wa kuelezea uzoefu wangu na kutoa ushauri kwa waandishi wengine au wale wanaowazia kuwa waandishi. Mara kwa mara ninaandika kuhusu mambo hayo kwa kujiamulia mwenyewe, lakini mara kwa mara ninaandika kuwajibu wanaoniulizia. Baadhi ya mawasiliano hayo huwa ni ya binafsi, na mengine hufanyika katika blogu hii.

Leo nimeona niseme neno kuhusu matokeo ya kuchapisha kitabu. Ninaandika kufuatia uzoefu wangu wa hapa Marekani. Kuchapisha kitabu ni aina ya ukombozi kwa mwandishi kutakana na jambo lilolokuwa linakusonga mawazoni. Ni kama kutua mzigo. Baada ya kumaliza kuandika, unajisikia mwenye faraja, tayari kuanza au kuendelea na majukumu mengine. Ni aina ya ukombozi.

Kuna waandishi chipukizi wanaoamini kuwa kuandika kitabu kutawaletea umaarufu au fedha. Wazo hili ni bora kuliweka kando. Fedha si jambo la kulipa kipaumbele; kwa kiasi kikubwa ni kubahatisha. Kwanza, kuna vitabu vingi mno vinavyochapishwa kila mwaka. Kwa hapa Marekani tu, vitabu zaidi ya milioni huchapishwa kila mwaka, kwa mujibu wa taarifa zilizopo. Sio rahisi mwandishi anayeanza safari ya uandishi ajipambanue na kuwa maarufu. Kwa wastani, nakala za kitabu zinazouzwa kwa mwaka ni 250, na ukomo wa mauzo kwa miaka yote ya kuwepo kitabu ni pungufu ya nakala 3,000.

Kwa hapa Marekani, kuna jadi kwamba waandishi, wakishachapisha kitabu, hufanya safari za kutangaza kitabu hicho. Safari hizi hupangwa na kuratibiwa na wadau wa vitabu kama vile wachapishaji wa vitabu, wauzaji wa vitabu, waendeshaji wa majarida yanayojihusisha na vitabu, na vikundi vya wasomaji katika miji na maeneo mbali mbali. Wote hao wanashiriki katika kufanikisha ziara ya mwandishi. Wanatangaza kwa namna yoyote ile ziara hiyo, magazetini, katika redio, katika televisheni, au mitandao ya kijamii.

Popote anapofika mwandishi, watu hujitokeza kumsikiliza akiongelea kitabu chake. Wanapata fursa ya kumwuliza masuali. Nakala za kitabu zinakuwepo, na watu wanapata fursa ya kununua na kusainiwa. Wenye maduka ya vitabu hupenda kuandaa mikusanyiko hiyo. Mbali na kwamba wanampa mwandishi fursa ya kukutana na wasomaji, na kutangaza kitabu chake, ni fursa kwa hayo maduka ya vitabu kujitangaza. Ni jadi iliyozoeleka kwamba nyakati hizo, kunakuwa na punguzo la bei ya kitabu kinachotangazwa, na hiki kinakuwa ni kivutio cha ziada kwa wateja.

Lakini jambo la msingi ni kuwa watu wa Marekani wanathamini sana fursa ya kukutana na mwandishi. Mimi mwenyewe, ingawa bado si mwandishi aliyetunukiwa tuzo maarufu kama Pulitzer, ninashuhudia jinsi watu wanavyovutiwa na fursa ya kukutana nami, iwe ni kwenye matamasha au kwenye mihadhara ninayotoa.

Hizi fursa za waandishi za kwenda kuongelea vitabu vyao ndio njia moja kuu ya waandishi kujijenga katika jamii. Mwandishi kuonekana na kusikilizwa moja kwa moja na wasomaji na wadau wengine wa vitabu ni njia ya kujijenga mioyoni mwao. Kukutana na mwandishi namna hiyo kunaleta picha na hisia ya pekee pale msomaji anaposoma kitabu cha mwandishi huyo. Bila shaka wote ambao tumewahi kukutana na waandishi tunajisikia hivyo tunaposoma maandishi yao.

Nimegusia hapo juu kuwa kuna watu wanaowazia kuwa kuchapisha kitabu kutawaletea umaarufu au fedha. Ni kweli, kutegemeana na kukubalika kwa kitabu katika jamii, mwandishi anaweza kupata umaarufu na fedha kiasi fulani. Lakini, kwa uzoefu wangu, ninapoalikwa kwenda kuongelea kitabu ndipo pana malipo makubwa, ukiachilia mbali kuwa vile vile nakala za vitabu zinauzwa hapo hapo. Vitabu ninavyoongelea hapa ni viwili: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales. Kipo kingine ambacho nimekuwa nikiandika kwa miaka kadhaa, kuhusu athari za tofauti za tamaduni, ambacho nina hakika kuwa kitawagusa watu kwa namna ya pekee.

Ningependa mambo hayo niliyoelezea yafanyike Tanzania. Ninatamani uje wakati ambapo, mwandishi akishachapisha kitabu muhimu, kiwe ni cha fasihi au maarifa, awe na fursa ya kuzunguka nchini kuongelea kitabu chake. Ninatamani uje wakati ambapo wananchi watakuwa na utamaduni wa kuvipenda vitabu na kupenda kukutana ana kwa ana na waandishi na kuongea nao.

Wednesday, April 12, 2017

Blogu Yangu Imepanda Chati Ghafla

Tangu wiki mbili zilizopita, blogu yangu hii imepanda chati ghafla. Ninaongelea kigezo cha "pageviews," ambazo ninaziangalia kila nitakapo. Kwa miaka na miaka, "pageviews" za blogu hii kwa siku zilikuwa kama 130, sio zaidi sana na sio pungufu sana.

Lakini, kuanzia wiki mbili hivi zilizopita, "pageviews" zimeongezeka ghafla kwa kiwango kikubwa, na sasa ni yapata 900 au zaidi kila siku. Sielewi ni nini kimesababisha ongezeko hilo. Mkondo wa mada zangu haujabadilika. Kwa kiasi kikubwa ninashughulika na masuala ya elimu na utamaduni.

Nimeona kuwa ongezeko hilo la "pageviews," limetokea hapa Marekani. Kwa nchi zingine, kama vile Tanzania na Kenya, hali haijabadilika. Ni ajabu kiasi kwamba blogu ya ki-Swahili inasomwa zaidi Marekani kuliko Afrika Mashariki.

Mtu unaweza kujiuliza ni watu gani wanaosoma hii blogu ya ki-Swahili kwa wingi namna hii hapa Marekani. Ukweli ni kuwa kuna watu wengi hapa, hasa kutoka Kenya na Tanzania, wanaokifahamu ki-Swahili. Wako pia watu kutoka Burundi, Uganda, Rwanda, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Vile vile, kuna wa-Marekani ambao wameishi Afrika Mashariki na wanakifahamu ki-Swahili. Pia kuna wa-Marekani wengi ambao wamejifunza au wanajifunza ki-Swahili katika vyuo vikuu mbali mbali hapa hapa Marekani. Ninahisi kuwa hao nao ni kati ya wasomaji wa blogu hii.

Ninavyowazia suala hili la ukuaji wa idadi ya "pageviews" katika blogu, ninawazia jinsi watu wanavyotumia blogu kwa matangazo, hasa ya biashara. Katika ulimwengu wa leo ambamo tekinolojia za mawasiliano zinaendelea kusambaa na kuimarika, wafanya biashara na wajasiriamali wanatumia fursa za mitandao kama vile blogu kutangaza shughuli zao.

Kwa upande wangu, sijajiingiza katika matumizi haya ya blogu, ukiachilia mbali matangazo ya vitabu vyangu na mihadhara ninayotoa au matamasha ninayoshiriki. Lakini, endapo nitabadili msimamo, bila shaka nitakaribisha matangazo ya waandishi, wachapishaji, na wauzaji wa vitabu, kwa sababu blogu yangu inajitambulisha kwa masuala ya aina hiyo.

Thursday, September 8, 2016

Wasomaji Wangu Wa Nebraska Waendao Tanzania

Nina jadi ya kuwaongelea wasomaji wangu katika blogu hii, kama njia ya kuwaenzi. Ni jambo jema kwa mwandishi kufanya hivyo. Leo ninapenda kuwakumbuka wasomaji wangu wa sinodi ya Nebraska ya Kanisa la Kiluteri la Marekani, ambao tangu zamani wamekuwa na programu ya kupeleka watu Tanzania kuendeleza uhusiano baina yao na wa-Luteri wa Tanzania.

Hao wasafiri, sawa na wenzao wa sinodi zingine za Marekani, wamekuwa wakitumia kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika kujiandaa kwa safari, ili kuzielewa tofauti za tamaduni za Marekani na Afrika. Ni elimu muhimu katika ulimwengu wa utandawazi wa leo, ambayo nje ya ufundishaji wa darasani, ninashughulika nayo.


Wakati huu ninapoandika, waumini wa Nebraska wanajiandaa kwa safari ya Tanzania, ambayo itafanyika mwezi Februari mwaka 2017. Wameitangaza safari hii mtandaoni, na mratibu mojawapo wa safari, Martin Malley, ameniandikia ujumbe leo akisema, "We still recommend your book." Katika ukurasa wa 16 wa chapisho la maelezo na maandalizi ya safari, kitabu hicho kimetajwa.

Ninapowakumbuka wasomaji wangu wa Nebraska, ninakumbuka nilivyokutana katika uwanja wa ndege wa Amsterdam na kikundi cha watu wa Nebraska waliokuwa wanakwenda Tanzania, tukasafiri pamoja. Mimi sikuwajua, ila wao walinitambua, kama nilivyoelezea katika blogu yangu ya ki-Ingereza.


Saturday, January 2, 2016

Kitabu Kinaposainiwa

Leo napenda kuirejesha mada ya kusainiwa vitabu, ambayo nimewahi kuileta katika blogu hii. Wanablogu wengine nao wameiongelea. Kwa mfano, Christian Bwaya amelielezea suala la kusaini vitabu kama jambo la ajabu, akatumia dhana ya muujiza. Nakubaliana na dhana hiyo, kutokana na uzoefu wangu kama mwandishi ambaye nimesaini vitabu vyangu mara nyingi, na pia mnunuaji wa vitabu ambaye nimesainiwa vitabu mara kwa mara. Hapa kushoto ninaonekana nikisaini kitabu changu mjini Faribault, Minnesota. Huyu ninayemsainia ni binti kutoka Sudan.


Ninafahamu muujiza huu unavyokuwa kwa pande zote mbili, mwenye kusaini kitabu chake na mwenye kusainiwa. Ninadiriki kusema kuwa kitendo cha kusainiwa kitabu kinafanana na ibada. Natumia neno ibada kwa maana ile ile ya dhana ya ki-Ingereza ya "ritual." Hapo kushoto anaonekana mwandishi Seena Oromia akinisainia kitabu chake mjini Minneapolis.

Ibada ni sehemu ya kila utamaduni, na kila ibada ina utaratibu wake, iwe ni misa kanisani, mazishi, au kitendo cha watu kula pamoja. Wahusika katika ibada wanapaswa kuzifahamu na kuzifuata taratibu hizo. Ibada ya kusainiwa kitabu ni tukio linalogusa nafsi na hisia ya anayesaini kitabu na yule anayesainiwa kitabu.

Ni tukio linaloambatana na heshima ya aina yake. Angalia tu picha nilizoweka hapa; utaona zinavyojieleza. Kuna usemi katika ki-Ingereza kwamba "A picture is worth a thousand words," yaani picha ina thamani sawa na maneno elfu. Hapa kushoto anaonekana mwandishi Jim Heynen akisaini kitabu chuoni St. Olaf.

Kwa ujumla wewe mwandishi huwajui watu wanaotaka kusainiwa vitabu. Inabidi uwaulize uandike jina gani. Wengine huwa wamenunua vitabu viwili au zaidi. Unawauliza usaini jina gani, kwa kila kitabu, nao wanakutajia jina lao au la mtu mwingine au watu wengine.  Hapa kushoto ninaonekana nikisaini vitabu vyangu katika mkutano Grantsburg, Wisconsin.

Kifalsafa, suala la kumsainia kitabu mtu ambaye humwoni ni jambo linalofikirisha. Mwandishi unajifanya unamjua unayemsainia, ingawa humjui. Naye, atakapokipata kitabu, atajiona kama vile kuna uhusiano baina yake na wewe mwandishi. Anafurahi kama vile mmeonana. Hii dhana ya kuonana imejengeka katika usomaji. Tunaposoma, tunakuwa na hisia ya kukutana na mwandishi, hata kama hayuko mbele yetu kimwili. Lakini tunaposhika kitabu ambacho tumesainiwa, ukaribu huo unakuwa mkubwa zaidi. Ni aina ya undugu.

Hapa kushoto naonekana nikisaini kitabu mjini Brooklyn Park, Minnesota. Ninayemsainia ni Adrian Mack, Mmarekani Mweusi.

Thursday, December 3, 2015

Kuhusu Kublogu

Nimekuwa mwanablogu tangu mwaka 2008. Ninaendesha blogu hii ya Hapa Kwetu na nyingine ya ki-Ingereza. Kublogu kuna mambo mengi. Kublogu kunanipa fursa ya kujieleza kwa uhuru. Hili ni jambo la msingi, kama alivyoelezea mwanablogu Christian Bwaya.

Lakini kublogu kuna matokeo yenye manufaa. Kumeniwezesha kuwafikia watu mbali mbali ambao wanatembelea blogu zangu. Siwezi kujua wanapata ujumbe gani katika maandishi yangu. Kama taaluma inayotufundisha, hili ni suala tata.

Ujumbe wa andiko ni zao la kazi anayofanya msomaji juu ya andiko. Na kwa kuwa wasomaji wana akili zinazotofautiana, na wana nidhamu na uzoefu tofauti wa kusoma, kila mmoja anaibuka na ujumbe tofauti, kwa kiwango kidogo au kikubwa.

Niliwahi kuelezea kwa nini ninablogu, lakini sidhani kama nilikuwa na majibu ya uhakika. Baadaye, katika kutafakari suala hili, nilifikia hatua ya kutamka kwamba ninablogu kwa ajili yangu mwenyewe. Labda huu ndio ukweli wa mambo.

Imani iliyojengeka katika jamii ni kuwa mwandishi anawaandikia wasomaji. Tumezoea kuona waandishi wakiulizwa wanamwandikia nani, nao wanaelezea walengwa wao. Jadi hii na imani hii imekosolewa kwa uhodari na Roland Barthes katika makala yake, "The Death of the Author."

Makala hii ya Barthes naona inaipa uzito hoja yangu kuwa ninapoblogu ninajiandikia mwenyewe. Sijui ni nani atasoma au anasoma ninachoandika. Kusema kwamba ninawaandikia wasomaji ni kama kuota ndoto. Ni kujiridhisha kwa jambo ambalo halina uhakika bali ni bahati nasibu. Nikisema ninajiandikia mwenyewe ninasema jambo la uhakika.

Monday, October 26, 2015

Shukrani kwa Wa-Tanzania Wadau wa Kitabu Changu

Blogu yangu ni mahali ninapojiandikia mambo yoyote kwa namna nipendayo. Siwajibiki kwa mtu yeyote, wala sina mgeni rasmi. Leo nimewazia mafanikio ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nimejikumbusha kuwa mtu hufanikiwi kwa juhudi zako pekee, hata ungekuwa hodari namna gani. Kuna watu unaopaswa kuwashukuru.

Nami napenda kufanya hivyo, kama ilivyo jadi yangu. Nimewahi kuwaongelea na kuwashukuru wanablogu wa-Tanzania, na nimewahi kuwaongelea na kuwashukuru wa-Kenya. Ninapenda kuendelea kuwakumbuka wa-Tanzania.


Mwanzoni kabisa, nilipokuwa nimeandika mswada wa awali kabisa wa kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, rafiki yangu Profesa Joe Lugalla, wa Chuo Kikuu cha New Hampshire, alipata kuusoma, akapendezwa nao.

Yeye, kwa jinsi alivyoupokea mswada ule, alikuwa kati ya watu wa mwanzo kabisa kunitia hamasa ya kuuboresha. Tangu wakati ule hadi leo amekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha watu wakisome kitabu hiki. Kwangu hili ni jambo la kushukuru sana, nikizingatia kuwa Profesa Lugalla sio tu ni m-Tanzania mwenzangu anayefahamu ninachosema kitabuni, bali pia yeye ni mtaalam wa kimataifa wa soshiolojia na anthropolojia.


Mtu mwingine aliyenihamasisha tangu miaka ya mwanzo ya kuwepo kwa kitabu changu ni Mhashamu Askofu Owdenburg Mdegella wa dayasisi ya Iringa ya Kanisa la ki-Luteri Tanzania. Nakumbuka tulivyokutana katika eneo la shule ya Peace House, Arusha, na hapo hapo akaanza kuongelea kitabu changu, akisema kuwa ni muhimu wazungu wakisome ili watufahamu sisi wa-Afrika. Siwezi kusahau kauli yake hiyo na namna alivyoongea kwa msisimko. Nilimwelewa vizuri kwa nini aliongea hivyo, kwani yeye anahusika moja kwa moja na mipango ya ushirikiano baina ya wa-Marekani na wa-Tanzania, hasa wa Iringa.


Dada Subi, mwanablogu maarufu miongoni mwa wa-Tanzania, ni mtu mwingine ambaye namkumbuka kwa namna ya pekee, kwa yote aliyofanya katika kunihamasisha na kukipigia debe kitabu changu. Nakumbuka aliwahi kuwasiliana nami juu ya kitabu hiki, lakini cha zaidi ni kuwa alikipigia debe katika blogu yake.

Dada Subi alinisaidia sana katika shughuli zangu za kublogu. Ingawa hatujawahi kuonana, ninamfahamu ni mkarimu sana.




Napenda nichukue fursa hii kumtaja na kumshukuru Bwana Muhiddin Issa Michuzi, mwanablogu maarufu wetu wa-Tanzania. Ingawa tumewahi kukutana mara moja tu, Michuzi amekuwa mstari wa mbele kutangaza shughuli zangu katika blogu yake, ikiwemo kitabu changu. Kutokana na hayo tumekuwa kama watu tuliozoeana. Kwangu hilo ni jambo la kushukuru.

Sitachoka kuwashukuru wachangiaji wa mafanikio yangu. Kama nilivyosema, hakuna mtu anayefanikiwa kwa uwezo wake peke yake. Ule usemi wa ki-Ingereza, "No man is an island," yaani hakuna mtu ambaye ni kisiwa, una ukweli usiopingika.

Kwa wanaotaka, walioko Tanzania, Kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences kinapatikana Burunge Visitor Centre, simu 0754 297 504.

Monday, October 12, 2015

Kama Mwandishi, Ninawaenzi wa-Kenya

Mimi kama mwandishi, ninawaenzi wa-Kenya. Naandika kutokana na uzoefu wangu. Tena na tena, mwaka hadi mwaka, nimeshuhudia wa-Kenya wakifuatilia vitabu vyangu. Wamekuwa bega kwa bega nami kama wasomaji wangu.

Tangu nilipochapisha kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, wa-Kenya walikichangamkia. Ndugu Tom Gitaa, mmiliki wa gazeti la Mshale aliandaa mkutano kuniwezesha kukitambulisha kitabu hicho, kama ilivyoelezwa katika taarifa hii.

Kati ya watu waliohudhuria alikuwepo Julia Opoti, m-Kenya mwingine, ambaye alishajipambanua kama mpiga debe wa kitabu hiki. Siku hiyo alimleta rafiki yake m-Kenya, Dorothy Rombo, naye akapata kunifahamu na kukifahamu kitabu changu.

Julia hakuishia hapo. Siku moja ulifanyika mkutano mkubwa wa wa-Kenya hapa Minnesota, ambao uliwakutanisha wana-diaspora wa Kenya na viongozi mbali mbali waliofika kutoka Kenya ili kuongelea fursa zilizopo nchini kwao katika uwekezaji na maendeleo kwa ujumla, na namna wana-diaspora wanavyoweza kushirikiana na wenzao walioko nyumbani.

Nilihudhuria mkutano ule sambamba na wengine waliokuwa wanaonesha bidhaa na huduma zao. Nilikuwa na meza ya vitabu vyangu. Julia alimleta ofisa wa ubalozi wa Kenya, Washington DC kwenye meza yangu, akatutambulisha. Alimwelezea kuhusu kitabu changu cha Africans Americans: Embracing Cultural Differences, naye akanunua nakala. Baada ya siku kadhaa aliniandikia ujumbe kama nilivyoandika katika blogu hii. Maneno ya afisa huyu yalinigusa, na baadhi ni haya:

Kuhusu kitabu chako, hivi sasa nafikiri kimesomwa na watu kadri ya watano hapa ubalozi wetu na kimependwa sana. Ni matumaini yangu kuwa ukipata wasaa mzuri utaandika vitabu zaidi katika fani hii ili upate kunufaisha watu juu ya swali hili muhimu la tafauti ya mila na utamaduni

Siku nyingine nilikuwa natoa mhadhara katika Chuo cha Principia. Aliyeanzisha mchakato wa kunialika ni m-Kenya ambaye alikuwa amesoma taarifa zangu mtandaoni. Mama mmoja m-Kenya aliyehudhuria aliamua kuniunganisha na jamii ya wa-Kenya wa Kansas City, ambako alikuwa anaishi, ili niweze kwenda kutoa mhadhara. Mipango ilikamilika nikaenda, kama nilivyoelezea hapa.

Mara kwa mara, nimeona jinsi wa-Kenya wanavyojitokeza katika matamasha ya vitabu ninayoshiriki. Katika Afrifest, kwa mfano, hawakosekani. Nimewahi kuelezea jambo hilo, miaka michache iliyopita na mwaka jana.

Nimeona niandike taarifa hii kwa kuwa naguswa na tabia za majirani zetu hao wa-Kenya. Walinifanyia ukarimu mkubwa nilipokuwa nafanya utafiti nchini mwao baina ya mwaka 1989 na 1991, hata kunialika kutoa mihadhara kuhusu utafiti wangu. Naendelea kuguswa na moyo wao huku ughaibuni. Nimejithibitishia kuwa wanaheshimu taaluma, nami nawaheshimu kwa hilo. Nategemea kuandika zaidi kuhusu suala hilo hapa katika blogu yangu.

Saturday, June 20, 2015

Msomaji Amenilalamikia

Leo alasiri nilikwenda Brooklyn Park, Minnesota, kuhudhuria mkutano wa bodi ya Afrifest Foundation ambayo mimi ni mwenyekiti wake. Tulifanyia mkutano wetu katika maktaba ya Brookdale.

Baada ya mkutano, nilipotoka nje kuelekea sehemu nilipopaki gari, alinikimbilia dada Latonya anayeonekana katika picha hapa kushoto, ambayo tulipiga miaka mitano iliyopita kwenye tamasha la Afrifest. Ni m-Marekani Mweusi kutoka Chicago, ila anaishi Minneapolis. Tulifahamiana miaka ile kwa kuwa naye alikuwa katika bodi ya Afrifest Foundation.

Hatukutegemea kama tungeonana leo, ghafla namna ile. Kwa hivi tulifurahi sana. Lakini hakupoteza muda, alianza kunihoji kwa nini siandiki sana katika blogu yangu ya ki-Ingereza kama zamani. Alisema, akimaanisha maandishi yangu ya kiSwahili, "Tunaona unaandika sana, na tunajua unaandika mambo ya maana, ila hatujui unachoandika. Inakuwa kama unatusahau marafiki zako wa-Marekani Weusi."

Kwa kweli, ingawa mazungumzo yalikuwa ya kirafiki, na hata kiutani, niliona kuwa alikuwa anaongea kwa dhati. Na sisi wa-Afrika ambao tunaishi Marekani tunafahamu kuwa wako wa-Marekani Weusi wengi ambao wanategemea sisi wa-Afrika tuwe na mshikamano nao, kama ndugu. Kwa hivi, sikuyachukulia malalamiko ya Latonya kama mzaha. Nilijikuta nikikiri kosa na kuahidi kuwa nitakuwa naandika kama zamani. Alivyowataja wa-Marekani Weusi hakuwa anatunga hadithi. Ninafahamu kuwa wanasoma maandishi yangu.

Latonya mwenyewe ni mmoja wa wafuatiliaji wa dhati wa maandishi yangu. Hapo pichani, anaonekana ameshika kitabu changu cha Africans and Americans:Embracing Cultural Differences, mara baada ya kukinunua. Maneno aliyoniambia leo yameniingia. Nilimwambia hivyo, nikaahidi kujirekebisha.

Wednesday, March 11, 2015

Video ya Kumbukumbu ya Miaka Kumi ya Kitabu

Jana, binti yangu Zawadi na mimi tulirecodi video ya kumbukumbu ya miaka kumi tangu nilipochapisha kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Hatukuwazia tungefanya shughuli hiyo jana. Tulijishitukiza bila maandalizi. Tulitayarisha kompyuta nami nikaanza kuongea. Zawadi alifanya shughuli yote ya kiufundi hadi kuiweka video katika
mtandao wa You Tube.

Katika kumbukumbu hii ya miaka kumi ya kitabu changu, napenda kuwashukuru wasomaji wangu, familia, na marafiki na wengine wote walionihamasisha kwa namna moja au nyingine.

Kwa mwezi huu wote, yeyote anayetaka kitabu hiki, popote duniani, ataweza kukipata kutoka kwangu kwa bei nafuu ya dola 12. Awasiliane nami kwa barua pepe, africonexion@gmail.com au simu (507) 403 9756. Mwisho wa fursa hii ni tarehe 31.

Wednesday, January 28, 2015

Katika Blogu, Sijui Ninamwandikia Nani Zaidi Yangu Mwenyewe

Je, mwandishi wa blogu anamwandikia nani? Kwa mtazamo wangu, hili ni suali gumu. Naliona gumu kulitafakari, achilia mbali kulijibu.

Baada ya kuona ugumu wa suali hili, nimeamua kukiri kuwa ninajiandikia mwenyewe. Ndio maana makala ninazoandika aghalabu zinanihusu mimi mwenyewe, shughuli zangu, matatizo na mafanikio yangu, mategemeo yangu na kumbukumbu zangu.

Sipendi sana kuwaongelea watu wengine, wala sipendi sana kuongelea mambo kinadharia, bila kujihusisha mwenyewe. Naweza kusema kuwa ndivyo nilivyoandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Sijajificha nyuma ya pazia la nadharia au taaluma. Nimejiweka wazi kwa namna nilivyoweza.

Mwandishi Ernest Hemingway aliongelea suala hili vizuri alipofafanua dhana ya ukweli katika uandishi. Nilivyomwelewa, anasema kuwa ukweli katika uandishi ni kwa mwandishi kuifungua na kuiweka bayana nafsi yake.

Ningependa sana niweze kuandika namna hii aliyoongelea Hemingway. Ni ndoto inayovutia, sawa na nyota inayong'aa mbali, ambayo mtu unaifuata kwa hamu ingawa haifikiki. Lakini, naona huku ndiko kujiandikia mwenyewe.

Kusema kuwa kuna hadhira ninayoiandikia katika blogu yangu ni kama kuota ndoto. Ni kujidanganya. Nasema hivi sio tu kutokana na tafakari yangu mwenyewe, bali ninakumbuka makala ya kufikirisha ya Walter J. Ong, "The Writer's Audience is Always a Fiction."

(Picha hapo juu nilijipiga mwenyewe jana, kwa ajili ya matangazo ya mihadhara yangu Mankato)

Tuesday, June 7, 2011

Mwaliko Nyumbani kwa Wateja Wangu

Jana jioni nilikuwa nyumbani kwa familia inayoonekana katika hii picha. Ni familia ya Shannon Gibney, mwandishi chipukizi ambaye tayari ni maarufu.

Miaka michache iliyopita, Shannon Gibney alisoma kitabu changu cha Africans and Americans, akaandika mapitio katika Minnesota Spokesman Recorder, kama nilivyosema hapa.

Siku chache zilizopita alinialika nyumbani kwake kwa chakula cha jioni, tukapanga hiyo tarehe ya jana. Aliniambia kuwa mume wake, ambaye anatoka Liberia, na bado ni mgeni hapa Marekani, amekuwa akisoma kitabu changu.

Nilifurahi kukutana na familia hii. Kwa zaidi ya saa mbili nilizokuwa nao, maongezi yetu yalihusu masuala niliyoongelea katika kitabu, yaani tofauti za tamaduni za wa-Marekani na wa-Afrika. Wote wawili wanakifahamu vizuri sana kitabu hiki, na walikuwa wananikumbusha mengi, ingawa mimi ndiye mwandishi.

Huyu bwana aliezea mshangao wake kwa jinsi maelezo ya kitabu hiki yanavyofanana na hali ya Liberia, ingawa mimi mwandishi sijafika kule. Niliguswa na furaha yake kwamba niliyoandika yamemwelewesha mambo ya wa-Marekani ambayo yalikuwa yanamtatiza. Nami nashukuru kwa hilo.

Familia hii ilinikarimu vizuri sana, nami nimebaki nashangaa kwa jinsi uandishi wa kitabu unavyoweza kukujengea urafiki na watu kiasi hicho.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...