Friday, April 14, 2017

Neno Kuhusu Matokeo ya Kuchapisha Kitabu

Mimi kama mwandishi wa vitabu ninafurahi ninapopata wasaa wa kuelezea uzoefu wangu na kutoa ushauri kwa waandishi wengine au wale wanaowazia kuwa waandishi. Mara kwa mara ninaandika kuhusu mambo hayo kwa kujiamulia mwenyewe, lakini mara kwa mara ninaandika kuwajibu wanaoniulizia. Baadhi ya mawasiliano hayo huwa ni ya binafsi, na mengine hufanyika katika blogu hii.

Leo nimeona niseme neno kuhusu matokeo ya kuchapisha kitabu. Ninaandika kufuatia uzoefu wangu wa hapa Marekani. Kuchapisha kitabu ni aina ya ukombozi kwa mwandishi kutakana na jambo lilolokuwa linakusonga mawazoni. Ni kama kutua mzigo. Baada ya kumaliza kuandika, unajisikia mwenye faraja, tayari kuanza au kuendelea na majukumu mengine. Ni aina ya ukombozi.

Kuna waandishi chipukizi wanaoamini kuwa kuandika kitabu kutawaletea umaarufu au fedha. Wazo hili ni bora kuliweka kando. Fedha si jambo la kulipa kipaumbele; kwa kiasi kikubwa ni kubahatisha. Kwanza, kuna vitabu vingi mno vinavyochapishwa kila mwaka. Kwa hapa Marekani tu, vitabu zaidi ya milioni huchapishwa kila mwaka, kwa mujibu wa taarifa zilizopo. Sio rahisi mwandishi anayeanza safari ya uandishi ajipambanue na kuwa maarufu. Kwa wastani, nakala za kitabu zinazouzwa kwa mwaka ni 250, na ukomo wa mauzo kwa miaka yote ya kuwepo kitabu ni pungufu ya nakala 3,000.

Kwa hapa Marekani, kuna jadi kwamba waandishi, wakishachapisha kitabu, hufanya safari za kutangaza kitabu hicho. Safari hizi hupangwa na kuratibiwa na wadau wa vitabu kama vile wachapishaji wa vitabu, wauzaji wa vitabu, waendeshaji wa majarida yanayojihusisha na vitabu, na vikundi vya wasomaji katika miji na maeneo mbali mbali. Wote hao wanashiriki katika kufanikisha ziara ya mwandishi. Wanatangaza kwa namna yoyote ile ziara hiyo, magazetini, katika redio, katika televisheni, au mitandao ya kijamii.

Popote anapofika mwandishi, watu hujitokeza kumsikiliza akiongelea kitabu chake. Wanapata fursa ya kumwuliza masuali. Nakala za kitabu zinakuwepo, na watu wanapata fursa ya kununua na kusainiwa. Wenye maduka ya vitabu hupenda kuandaa mikusanyiko hiyo. Mbali na kwamba wanampa mwandishi fursa ya kukutana na wasomaji, na kutangaza kitabu chake, ni fursa kwa hayo maduka ya vitabu kujitangaza. Ni jadi iliyozoeleka kwamba nyakati hizo, kunakuwa na punguzo la bei ya kitabu kinachotangazwa, na hiki kinakuwa ni kivutio cha ziada kwa wateja.

Lakini jambo la msingi ni kuwa watu wa Marekani wanathamini sana fursa ya kukutana na mwandishi. Mimi mwenyewe, ingawa bado si mwandishi aliyetunukiwa tuzo maarufu kama Pulitzer, ninashuhudia jinsi watu wanavyovutiwa na fursa ya kukutana nami, iwe ni kwenye matamasha au kwenye mihadhara ninayotoa.

Hizi fursa za waandishi za kwenda kuongelea vitabu vyao ndio njia moja kuu ya waandishi kujijenga katika jamii. Mwandishi kuonekana na kusikilizwa moja kwa moja na wasomaji na wadau wengine wa vitabu ni njia ya kujijenga mioyoni mwao. Kukutana na mwandishi namna hiyo kunaleta picha na hisia ya pekee pale msomaji anaposoma kitabu cha mwandishi huyo. Bila shaka wote ambao tumewahi kukutana na waandishi tunajisikia hivyo tunaposoma maandishi yao.

Nimegusia hapo juu kuwa kuna watu wanaowazia kuwa kuchapisha kitabu kutawaletea umaarufu au fedha. Ni kweli, kutegemeana na kukubalika kwa kitabu katika jamii, mwandishi anaweza kupata umaarufu na fedha kiasi fulani. Lakini, kwa uzoefu wangu, ninapoalikwa kwenda kuongelea kitabu ndipo pana malipo makubwa, ukiachilia mbali kuwa vile vile nakala za vitabu zinauzwa hapo hapo. Vitabu ninavyoongelea hapa ni viwili: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales. Kipo kingine ambacho nimekuwa nikiandika kwa miaka kadhaa, kuhusu athari za tofauti za tamaduni, ambacho nina hakika kuwa kitawagusa watu kwa namna ya pekee.

Ningependa mambo hayo niliyoelezea yafanyike Tanzania. Ninatamani uje wakati ambapo, mwandishi akishachapisha kitabu muhimu, kiwe ni cha fasihi au maarifa, awe na fursa ya kuzunguka nchini kuongelea kitabu chake. Ninatamani uje wakati ambapo wananchi watakuwa na utamaduni wa kuvipenda vitabu na kupenda kukutana ana kwa ana na waandishi na kuongea nao.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...