Showing posts with label Matengo Folktales. Show all posts
Showing posts with label Matengo Folktales. Show all posts

Wednesday, October 10, 2018

Naambiwa Niongeze Bei ya Kitabu

Katika matamasha ya vitabu ninayoshiriki, ninakutana na mambo mengi, zikiwemo tabia na mitazamo ya wateja. Moja ambalo linanigusa zaidi ni pale mteja anaposhauri niongeze bei ya kitabu changu. Hiyo imetokea mara kadhaa, kuhusiana na vitabu vyangu viwili: Africans and Americans: Embracing Cultual Differences na Matengo Folktales.

Vitabu hivi ninaviuza kwenye matamasha kwa dola 14 kila kimoja. Kwa kujua kwamba watu wengine wanatoa  noti ya dola 20 au noti mbili za dola kumi kumi, ninajitahidi kuwa na chenji. Ajabu ni kwamba watu wengine hawasubiri chenji, na wengine wanakataa. Wanachotaka ni kitabu waende zao. Ninakumbuka watu waliowahi kutoa noti ya dola 20 bila kutaka chenji. Mmoja wa hao, nilipojiandaa kumpa chenji, alisema hiyo chenji ni shukrani yake kwangu kwa kuandika kitabu.

Tarehe 4 mwezi huu nilikutana na jambo jingine kabisa. Mama moja, Jackie, ambaye nimemfahamu miezi michache iliyopita na akasoma hivi vitabu vyangu viwili, alinialika kwenye mhadhara wa rafiki yake Maria kuhusu vitabu na maisha yake. Alikuwa ameniambi nije na nakala za vitabu vyangu, ili aweze kuvipeleka katika tamasha la vitabu. Baada ya mhadhara, wakati tulipokuwa tunajumuika kwa viburudisho na maongezi, Jackie akanulizia bei ya vitabu vyangu, nami nikamwambia kuwa ni dola 14. Alisema nipandishe iwe 15, kwa ulinganisho na kitabu cha dola 10 na pia kwa urahisi wa chenji.

Alinitambulisha kwa rafiki yake, akamwambia kuhusu hivi vitabu vyangu. Alivyokuwa akielezea hayo, akaniambia nivitoe kwenye begi, nikampa. Huyu rafiki alichagua Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, akapanda ngazi kwenda kuchukua hela akaja akanipa na kitabu akachukua. Dakika chache baadaye, mama huyu alinitambulisha kwa mama mwingine, na akamwambia kuhusu vitabu. Naye akanunua Matengo Folktales.

Kwa hivyo nimejikuta nikiafiki wazo la kuongeza bei ya vitabu vyangu. Hata hivyo, bei hiyo ni ndogo kulingana na bei za mahali pengine za vitabu hivyo. Ninaamini kuwa taarifa hii ina ujumbe kuhusu watu wanaothamini vitabu kuliko fedha. Kama nilivyowahi kusema tena na tena, blogu hii ni sehemu ambapo ninajiwekea mambo yangu binafsi, kama vile kumbukumbu, hisia, na mitazamo. Ikitokea haja, siku zijazo, ya kuandika kitabu kuhusu maisha na kazi zangu, blogu hii itakuwa chanzo muhimu cha taarifa.

Sunday, December 10, 2017

Maonesho ya St. Dominic Boutique, Northfield, Minnesota

Jana, November 9, shule ya St. Dominic ya hapa Northfield, ilikuwa na wageni wengi. Palifanyika maonesho ya vitu mbali mbali vya matumizi na mapambo ya nyumbani na mavazi na urembo, machapisho, kazi za sanaa. Tamasha hilo lililoitwa St. Dominique Boutique lilijumuisha watengenezaji na wauzaji wa vitu hivyo yapata 60, na watu wengi kutoka maeneo mbali mbali walifika kuangalia na kununua. Mimi nilikuwepo, nikapata fursa ya kuongea na watu juu ya maandishi, mihadhara na utoaji ushauri kuhusu masuala ya tamaduni.




Nilipofika maoneshoni na kuelekezwa kwenye sehemu niliyopangiwa, huyu mzee anayeonekana hapa kushoto alisogea hima na kunisaidia kuandaa meza yangu. Alijitambulisha kuwa alihudhuria mhadhara niliotoa katika kanisa mjini Faribault. Hapo nilikumbuka kuwa niliwahi kutoa mihadhara miwili katika kanisa liitwalo First English Lutheran Church kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni. Waumini walipata fursa ya kununua nakala za kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Mzee huyu, ambaye alininieleza kuwa ni padri mstaafu, alikuwa na meza yake pembeni yangu. Kwa hiyo, tuliweza kuongea muda wote wa maonesho.






Kuanzia saa tatu asubuhi hadi saa nane, watu walikuwa wanafika na kuangalia vitu na kununua, na kuongea na sisi tuliokuja kuonesha bidhaa na vitu vyetu vingine.







































Huyu dada hapa kushoto alifika kwenye meza yangu na dada yake mkubwa. Tuliongea kirefu kuhusu shughuli zangu na kuhusu vitabu vyangu. Hatimaye huyu dada alinunua hivi viwili alivyoshika, tukapiga picha. Kama kawaida, nimejionea mwaka hadi mwaka jinsi wa-Marekani wanavyopenda vitabu. Wakishauliza bei na kutajiwa, wanatoa hela hapo hapo na kununua.












Huyu bwana hapa kushoto sikumwelewa mwanzo alipofika mezani pangu, akaangalia na kuondoka bila kusema kitu, pamoja na kwamba nilimsalimia. Baada ya dakika chache alisogea tena na kuangalia, na hakusema kitu. Kisha akakaa kwenye kiti kilichokuwa pembeni yangu, bila kunisalimia. Akachukua kijidaftari mfukoni mwake, akaanza kuandika sentensi mbili tatu, akanipa. Alikuwa ananiuliza iwapo nimesikia habari za m-Marekani Andrew Foster aliyeanzisha shule Ghana kwa ajili ya wasiosikia. Nilivyosoma na kumwangalia alivyokuwa ananiangalia, nilianza kuhisi kuwa ni mlemavu. Hasikii.

Tuliendelea kuzungumza kwa maandishi, hadi mwisho, na tulipoagana, nilimwandikia ujumbe wa mwisho kumwuliza kama angependa tupige picha, tukapiga. Nitaandika kuhusu tukio hili siku nyingine, katika blogu hii.


Kama nilivyoandika katika blogu hii, kitabu changu cha Matengo Folktales kilitajwa tarehe 23 Novemba katika "Jeopardy," programu  maarufu ya televisheni hapa Marekani. Baada ya kutajwa hivyo na kuleta msisimko hapa Marekani, niliamua kuitumia hiyo kama fursa.

Nilitengeneza bango lenye tamko lililokuwepo kwenye kipindi cha Jeopardy."  Ilikuwa ni burudani kuwaonyesha wa-Marekani hili bango na kitabu, huku nikifanya utani kuhusu kitabu changu kuonekana "Jeopardy."



Ninaipongeza shule ya St. Dominic kwa kuandaa maonesho hayo. Ingawa ilikuwa ni mara yao ya kwanza kufanya hivyo, shughuli ilifanikiwa sana. Watu wa aina mbali mbali walifika. Ingawa shule ni ya madhehebu ya Katoliki, hapo kwenye meza yangu pekee niliweza kuongea na watu wa imani mbali mbali. Kwa kadiri nilivyoona, itakuwa vizuri iwapo maonesho haya yatakuwa endelevu kwa siku zijazo. 

Thursday, December 7, 2017

Kitabu "Matengo Folktales" Chaendelea Kuwa Gumzo

Kama nilivyoeleza katika blogu hii, kitabu changu, Matengo Folktales, kilitajwa tarehe 23 November, 2017, katika programu ya televisheni iitwayo Jeopardy ambayo ni maarufu hapa Marekani. Kwa kuwa sikuwa na mazoea ya kuangalia program hii, wala nyingine yoyote, sikufahamu umaarufu wake. Kumbe sasa, baada ya kitabu changu kutajwa, nimeshuhudia na ninaendelea kushuhudia msisimko miongoni mwa wa-Marekani wa kina aina.

Mbali na watu ninaokutana nao mitaani, maprofesa wenzangu hapa chuoni St. Olaf nao wamekuwa wakinipongeza sana. Siku kadhaa nilizopita, kwenye mkutano mjini St. Paul, profesa moja wa chuo cha Macalester naye aliniambia kutajwa katika Jeopardy ni kwamba nimefikia kilele cha "popular culture" hapa Marekani.

Note hayo badi hayajaniingia sawa sawa kichwani, kwa sabbat, kama nilivyosema, sikuwa na mazoea wala ufahamu wa kipindi cha Jeopardy. Ninaanza kuelewa, ila sitaweza kuelewa kama wa-Marekani wenyewe wanavyoelewa, kwani ni suala la tofauti za tamaduni. Kama hukukulia katika utamaduni fulani, ni vigumu sana kuyafahamu mambo ya utamaduni ule sawa na wanavyofahamu wenye utamaduni ule. Ni hivyo kwa Wa-Afrika walioko hapa Marekani, na kwa wa-Marekani walioko Afrika.

Leo hapa chuoni tulikuwa na mkutano wa maprofesa, ambao tunafanya mara moja kila mwezi. Mkutano ulihusu masuala mbali mbali, na ulipokaribia kwisha, ilikuja zamu ya afire taaluma wa chuo kusema machache. Baadhi ya mambo aliyosema ni kutangaza mania ya watu waliochapisha vitabu katika siku za karibuni, na majina ya watu waliojipatia tuzo au heshima kwa namna nyingine. Kati ya watu has, alitaja tukio la kitabu changu kutajwa katika Jeopardy. Alianza kwa kuuliza, nani kati yetu anategemea itakuja siku atajwe katika Jeopardy?

Baada ya kusema hivyo, alionyesha kwenye skrini kubwa picha hii hapa kushoto kama iliyoonekana katika Jeopardy. Mkutano ulipoisha, watu waliendelea kuongea nami kwa furaha kuhusu maana ya tukio hili katika utamaduni wa Marekani. Kwangu hii ni elimu ya ziada, nikiwa kama mtafiti wa tamaduni, mada ambayo ninaitolea mihadhara katika taasisi na jumuia mbali mbali na nimeiandikia makala na pia kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Kwa kuwa ninafanya juhudi kujielimisha na kuelimisha wengine, nina kila sababu ya kujiwekea kumbukumbu ya mambo hayo, kama ninavyofanya hapa katika blogu yangu. Ni muhimu nijiwekee kumbukumbu hizi, ili angalau watoto wangu na vizazi vijavyo waweze kujua nilikuwa ninafanya nini wakati wa uhai wangu.

Monday, November 27, 2017

Kitabu "Matengo Folktales" Chatajwa Katika "Jeopardy."

Tarehe 23 Novemba, 2017, nitaikumbuka daima. Kwanza, ilikuwa ni sikukuu ya "Thanksgiving" ambayo ni maarufu hapa Marekani.

Jambo la pili liliofanya targhe 23 iwe muhimu kwangu ni kuwa jioni ya siku hiyo, katika kipindi maarufu cha televisheni kiitwacho "Jeopardy," kitabu changu kiitwacho Matengo Folktales kilitajwa. "Jeopardy" ni mchezo kama chemsha bongo. Watu hushindana kujibu masuali ambayo mwendesha kipindi huwauliza, na wanapotoa jibu sahihi hupata fedha. Suali lililoulizwa lilikuwa kuhusu mhusika katika hadithi.
Nilikifahamu kipindi hiki kijuujuu. Lakini baada ya kitabu kutajwa, nimeona wa-Marekani wanaonifahamu wanavyosisimka na kunipongeza. Hata hapa chuoni St. Olaf habari imezagaa hadi kwa wakuu wa chuo. Mkuu wa idara yangu ya ki-Ingereza ameandika ujumbe kwetu waalimu na wanafunzi: Congratulations to Joseph Mbele for an honor that few of us will ever achieve--being mentioned in a clue on Jeopardy! See the image below, referencing Joseph's "Matengo Folktales" book....

Sasa zimepita siku tatu na bado watu wanaendelea kusimulia tukio hili. Ninaendelea kupata taarifa kutoka sehemu mbali mbali za Marekani. Hata hivi, sielewi ni nani aliyepeleka taarifa za kitabu changu kwenye kituo cha "Jeopardy." Unaweza kusikiliza katika video ya YouTube hapa chini. Ukisogeza video ukifikishe kwenye dakika 15:29 ndipo utasikia jina langu na jina la kitabu.

Tuesday, September 5, 2017

Wadau Wanauliza Wanilipe Kiasi Gani

Siku chache zilizopita nilileta taarifa katika blogu hii kuhusu mwaliko niliopata kutoka Red Wing, kwenda kuongelea utamaduni wa hadithi. Tarehe 31 Agosti, wameniletea ujumbe kuniulizia iwapo kiwango cha malipo yangu ni kiasi gani. Huu ni utaratibu wa kawaida hapa Marekani. Mtu akialikwa kuhutubia, analipwa. Viwango vya malipo hutofautiana kulingana na umaarufu wa mwalikwa.

Suala la malipo ni tata kwangu, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Kipaumbele changu ni kutoa huduma kwa jamii. Malipo ni matokeo. Ninatoa mihadhara kwa wenye uwezo wa kunilipa na kwa wasio na uwezo wa kunilipa. Sipendi kuchukua pesa maadam tu ni pesa. Lazima nijiridhishe kuhusu uhalali wa hizo pesa.

Kwa msingi huo, ninatafakari ulizo kutoka Red Wing kuhusu malipo. Mwaliko wa Red Wing unahusu hadithi za jadi za wahenga wetu. Si hadithi zangu, kwa sababu sikuzitunga mimi. Ni urithi wetu wa tangu zamani. Sina hati miliki. Suala la kupokea malipo ni tata. Wale walionisimulia hadithi zilizomo katika kitabu cha Matengo Folktales, kwa mfano, hawakuwa na utamaduni wa kulipwa, na sikuwalipa.

Hata hivyo, nitakwenda Red Wing si kusimulia hadithi tu, bali pia kuongelea utamaduni wa kusimulia hadithi. Nitatoa elimu kuhusu suala hilo, kuanzia chimbuko la usimuliaji wa hadithi hadi kuhusu mchango wa hadithi katika jamii. Itakuwa kama darasa la fasihi simulizi. Kwa upande huo, kulipwa hakuna dosari.

Jambo la ziada ni kwamba kutoka hapa mjini Northfield ninapoishi hadi Red Wing ni mwendo wa saa moja. Nitatumia muda kuandaa mambo ya kusema na nitaingia gharama za safari. Ninaona ni sahihi kupokea malipo.

Friday, April 14, 2017

Neno Kuhusu Matokeo ya Kuchapisha Kitabu

Mimi kama mwandishi wa vitabu ninafurahi ninapopata wasaa wa kuelezea uzoefu wangu na kutoa ushauri kwa waandishi wengine au wale wanaowazia kuwa waandishi. Mara kwa mara ninaandika kuhusu mambo hayo kwa kujiamulia mwenyewe, lakini mara kwa mara ninaandika kuwajibu wanaoniulizia. Baadhi ya mawasiliano hayo huwa ni ya binafsi, na mengine hufanyika katika blogu hii.

Leo nimeona niseme neno kuhusu matokeo ya kuchapisha kitabu. Ninaandika kufuatia uzoefu wangu wa hapa Marekani. Kuchapisha kitabu ni aina ya ukombozi kwa mwandishi kutakana na jambo lilolokuwa linakusonga mawazoni. Ni kama kutua mzigo. Baada ya kumaliza kuandika, unajisikia mwenye faraja, tayari kuanza au kuendelea na majukumu mengine. Ni aina ya ukombozi.

Kuna waandishi chipukizi wanaoamini kuwa kuandika kitabu kutawaletea umaarufu au fedha. Wazo hili ni bora kuliweka kando. Fedha si jambo la kulipa kipaumbele; kwa kiasi kikubwa ni kubahatisha. Kwanza, kuna vitabu vingi mno vinavyochapishwa kila mwaka. Kwa hapa Marekani tu, vitabu zaidi ya milioni huchapishwa kila mwaka, kwa mujibu wa taarifa zilizopo. Sio rahisi mwandishi anayeanza safari ya uandishi ajipambanue na kuwa maarufu. Kwa wastani, nakala za kitabu zinazouzwa kwa mwaka ni 250, na ukomo wa mauzo kwa miaka yote ya kuwepo kitabu ni pungufu ya nakala 3,000.

Kwa hapa Marekani, kuna jadi kwamba waandishi, wakishachapisha kitabu, hufanya safari za kutangaza kitabu hicho. Safari hizi hupangwa na kuratibiwa na wadau wa vitabu kama vile wachapishaji wa vitabu, wauzaji wa vitabu, waendeshaji wa majarida yanayojihusisha na vitabu, na vikundi vya wasomaji katika miji na maeneo mbali mbali. Wote hao wanashiriki katika kufanikisha ziara ya mwandishi. Wanatangaza kwa namna yoyote ile ziara hiyo, magazetini, katika redio, katika televisheni, au mitandao ya kijamii.

Popote anapofika mwandishi, watu hujitokeza kumsikiliza akiongelea kitabu chake. Wanapata fursa ya kumwuliza masuali. Nakala za kitabu zinakuwepo, na watu wanapata fursa ya kununua na kusainiwa. Wenye maduka ya vitabu hupenda kuandaa mikusanyiko hiyo. Mbali na kwamba wanampa mwandishi fursa ya kukutana na wasomaji, na kutangaza kitabu chake, ni fursa kwa hayo maduka ya vitabu kujitangaza. Ni jadi iliyozoeleka kwamba nyakati hizo, kunakuwa na punguzo la bei ya kitabu kinachotangazwa, na hiki kinakuwa ni kivutio cha ziada kwa wateja.

Lakini jambo la msingi ni kuwa watu wa Marekani wanathamini sana fursa ya kukutana na mwandishi. Mimi mwenyewe, ingawa bado si mwandishi aliyetunukiwa tuzo maarufu kama Pulitzer, ninashuhudia jinsi watu wanavyovutiwa na fursa ya kukutana nami, iwe ni kwenye matamasha au kwenye mihadhara ninayotoa.

Hizi fursa za waandishi za kwenda kuongelea vitabu vyao ndio njia moja kuu ya waandishi kujijenga katika jamii. Mwandishi kuonekana na kusikilizwa moja kwa moja na wasomaji na wadau wengine wa vitabu ni njia ya kujijenga mioyoni mwao. Kukutana na mwandishi namna hiyo kunaleta picha na hisia ya pekee pale msomaji anaposoma kitabu cha mwandishi huyo. Bila shaka wote ambao tumewahi kukutana na waandishi tunajisikia hivyo tunaposoma maandishi yao.

Nimegusia hapo juu kuwa kuna watu wanaowazia kuwa kuchapisha kitabu kutawaletea umaarufu au fedha. Ni kweli, kutegemeana na kukubalika kwa kitabu katika jamii, mwandishi anaweza kupata umaarufu na fedha kiasi fulani. Lakini, kwa uzoefu wangu, ninapoalikwa kwenda kuongelea kitabu ndipo pana malipo makubwa, ukiachilia mbali kuwa vile vile nakala za vitabu zinauzwa hapo hapo. Vitabu ninavyoongelea hapa ni viwili: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales. Kipo kingine ambacho nimekuwa nikiandika kwa miaka kadhaa, kuhusu athari za tofauti za tamaduni, ambacho nina hakika kuwa kitawagusa watu kwa namna ya pekee.

Ningependa mambo hayo niliyoelezea yafanyike Tanzania. Ninatamani uje wakati ambapo, mwandishi akishachapisha kitabu muhimu, kiwe ni cha fasihi au maarifa, awe na fursa ya kuzunguka nchini kuongelea kitabu chake. Ninatamani uje wakati ambapo wananchi watakuwa na utamaduni wa kuvipenda vitabu na kupenda kukutana ana kwa ana na waandishi na kuongea nao.

Saturday, April 8, 2017

Mwaliko Chuo Kikuu cha Winona

Tangu mwaka uanze, nimetoa mihadhara au kufanyiwa mahojiano nje ya chuo ninapofundisha, mara nyingi kuliko kawaida. Nilitegemea kuwa kuanzia mwezi huu wa Aprili, hali ingebadilika. Lakini dalili hazionyeshi mabadiliko.

Tarehe 6, nilipata mwaliko kutoka kwa Alex Hines, mkuu wa idara ya Inclusion and Diversity katika Chuo Kikuu cha Winona, wa kwenda kutoa mhadhara:

We would like to extend an invitation for you to attend HOPE Academic & Leadership Academy during the week of June 26th through June 29th and conduct a two hour presentation from 7-9 p.m. on Embracing African and African American Culture.

Hii itakuwa ni mara ya tatu mimi kwenda kutoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Winona. Mara ya kwanza, niliongelea masuala ya utamaduni kama nilivyoyaeleza katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Mara ya pili, niliongelea mahusiano ya binadamu na uongozi, kwa kutumia kitabu cha Matengo Folktales, kama nilivyoandika katika blogu hii

Mwaliko huu wa sasa, kama ilivyoelezwa katika barua niliyonukuu hapa juu, msingi wake ni kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Alex Hines, tangu tulipofahamiana, miaka mingi iliyopita, amekuwa ni mmoja wa wale wanaonitegemea katika programu zao. Ninafurahi kwa imani ya wadau juu yangu, nami ninahamasika kufanya makubwa zaidi kwa ajili yao.

Blogu hii ni mahali ninapohifadhi kumbukumbu zangu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii. Labda kuna siku nitapata wazo la kuandika kitabu kuhusu shughuli zangu. Ikitokea hivyo, kumbukumbu hizi zitanifaa.

Tuesday, November 24, 2015

Kitabu Changu Bado Kiko Maoneshoni

Nimepita tena katika duka la vitabu la hapa chuoni St. Olaf, kama ilivyo kawaida yangu, kuangalia vitabu vipya, na pia kuangalia vitabu ambavyo maprofesa wa masomo mbali mbali wanapangia kufundisha.

Katika kuzunguka humo dukani, nilipita tena sehemu ambapo vinawekwa vitabu vilivyoandikwa na maprofesa wa chuo hiki. Kabla sijafika kwenye sehemu hiyo, macho yangu yalivutiwa na kitabu change cha Matengo Folktales, ambacho kilikuwa bado kiko sehemu maalum vinakowekwa vitabu ambavyo uongozi wa duka huamua kuvipa fursa ya kuonekana vizuri zaidi kwa kipindi fulani, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii.

Kuna mambo yanayonigusa kila niingiapo katika duka hili la vitabu na maduka mengine ya vitabu popote hapa Marekani. Kubwa zaidi ni jinsi wahudumu wanavyokuwa ni watu makini katika masuala ya vitabu. Wanajua habari za vitabu, na wanaweza kukuelimisha kwa namna mbali mbali. Hawako katika kazi hii kwa kubahatisha au kwa kubabaisha. Wanajua wanachokifanya. Unaweza kuingia katika duka la vitabu hapa Marekani bila mpango wa kununua kitabu, lakini ukianza kuongea na wahudumu, unaweza kujikuta umeelimishwa kuhusu vitabu fulani ukaishia kununua.

Katika haya maduka ya vyuo, nimeona wana huu utaratibu wa kuwa na sehemu ya kuweka vitabu vilivyoandikwa na maprofesa wa vyuo hivyo, na pengine pia vitabu vya watu waliohitimu zamani, ambao huitwa "alumni" (wanaume) au "alumnae" (wanawake). Ni namna mojawapo ambayo taasisi hizo huwatambua na kuwaenzi waalimu na wahitimu. Nami najisikia vizuri kama profesa wa chuo hiki cha St. Olaf kuwa kazi zangu zinatambuliwa, vikiwemo vitabu.

Kwa upande wa biashara, naona kuwa haya maduka ya vitabu ya vyuo vya Marekani yanaonyesha ubunifu wa kibiashara kwa kuweka vitabu vyetu namna hiyo. Mbali  ya wanafunzi, tuna wageni wengi wanaopita hapa chuoni kila siku, wakiwemo wazazi wa wanafunzi, wahitimu wa zamani, na wale wanaokuja kuangalia ubora wa chuo ili wawalete vijana wao kusoma hapa. Duka la vitabu ni sehemu moja muhimu wanamoingia. Humo wanakuwa na fursa ya kununua vitabu vyetu hasa inapokuwa kwamba wamesikia habari zetu. Kwa mfano, duka la St. Olaf limeshauza nakala mia kadhaa za vitabu vyangu.

Hayo ni baadhi ya mambo niliyojifunza katika suala hili ambayo nimeona niyaweke katika blogu yangu, kwa lugha rahisi kabisa. Labda yanaweza kuwa na manufaa kwa vyuo nchini mwangu.

Sunday, November 8, 2015

Nimealikwa Kusimulia Hadithi

Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mama mmoja m-Liberia aishiye hapa Minnesota. Amejitambulisha kwamba tulikutana katika tamasha la Afrifest, akauliza iwapo nitaweza kwenda kusimulia hadithi mjini Maple Grove tarehe 14 mwezi huu, katika sherehe ya kumbukumbu ya kuzaliwa mtoto.

Nilielezea katika blogu yangu ya ki-Ingereza nilivyosimulia hadithi katika tamasha la Afrifest, hapa na hapa. Nilisimulia hadithi mbili kutoka katika kitabu cha Matengo Folktales. Mama aliyeniletea mwaliko wa tarehe 14 amenikumbusha kwamba mtoto wake na wengine walioshuhudia hadithi zangu katika Afrifest walivutiwa na wanataka nikasimulie tena.

Hii itakuwa mara yangu ya kwanza kusimulia hadithi katika mkusanyiko wa wanafamilia na marafiki zao, katika sherehe ya kifamilia. Nimezoea kusimulia katika vyuo. Nitatumia sehemu ya muda nitakaokuwa nao kuelezea dhima ya hadithi katika jadi za wa-Afrika na wanadamu kwa ujumla, halafu nitasimulia hadithi, na kisha nitawahimiza wasikilizaji kusaidia kuichambua hadithi nitakayosimulia. Ninawazia kusimulia hadithi kutoka Afrika Magharibi, labda Liberia, Senegal, au Burkina Faso, zilizomo katika kitabu cha West African Folktales.

Hadithi za jadi ni hazina yenye mambo mengi, kama vile falsafa, mafundisho kuhusu saikolojia na tabia za wanadamu, kuhusu mema na mabaya. Ziko zinazosikitisha, zinazofurahisha na kuburudisha, na zinazochemsha bongo, kama zile ziitwazo kwa ki-Ingereza "dilemma tales." Zote ni muhimu katika maisha ya wanadamu, kama nilivyojaribu kuelezea katika kitabu cha Matengo Folktales.

Tuesday, August 25, 2015

Nimekikuta Kitabu Changu Kinameremeta Dukani

Mchana huu nimemaliza kusahihisha mtihani wa kumalizia muhula wa somo langu la "African Literature." Nimekwenda chuoni kuwarudishia wanafunzi daftari zao, nikiwa na furaha ya kuwa na wiki mbili tatu za "uhuru," kabla ya kuanza muhula mwingine.

Baada ya kurudisha daftari, niliingia katika duka la vitabu. Nilizunguka kidogo tu humo ndani nikaona kitabu changu cha Matengo Folktales kimewekwa mahali pa wazi, pamoja na vitabu vingine vichache. Kinaonekana pichani chenye rangi ya manjano na ramani ya Afrika.

Huu ni utaratibu wa duka letu la vitabu. Kila wakati wanachagua vitabu vichache na kuviweka sehemu hizo za wazi ili viweze kuonekana kirahisi kwa wateja. Kufuatana na utaratibu uliopo, kitabu kitakuwa hapo kwa siku kadhaa, na hata wiki kadhaa, kabla ya kurudishwa sehemu yake.

Katika duka hili la chuoni St. Olaf vinapatkana vitabu vyangu vyote. Mbali ya wanafunzi, waalimu, na wafanyakazi wengine wa chuo, wageni wanaokitembelea chuo hupenda kuingia katika hili duka la vitabu, ambalo huuza pia bidhaa mbali mbali, kama ilivyo kawaida katika maduka ya vitabu ya vyuo vya Marekani.

Kila ninapoviona vitabu vyangu katika duka hili, mawazo hunijia, hasa kuhusu namna vitabu hivi vinavyowafaidia wa-Marekani. Vinawafaidia kielimu, kwa kuwa vinatumika katika masomo. Vinawafaidia kibiashara, kwa kuviuza, na vinachangia ajira hata kama ni kiasi kidogo sana, kwa wachapishaji, wasafirishaji, na wahudumu wa duka kama hili la Chuo cha St. Olaf. Nawazia mambo ya aina hii.

Friday, June 12, 2015

Siku ya Mhadhara Chuo Kikuu Winona Inakaribia

Siku hazikawii. Zimebaki siku kumi na moja tu kufikia siku ya mhadhara wangu Chuo Kikuu cha Winona, utakaotokana na utafiti wangu juu ya falsafa zilizomo katika masimulizi ya jadi kama inavyodhihirika katika kitabu changu cha Matengo Folktales. Niliandika taarifa ya awali ya mhadhara huu katika blogu hii.

Leo nimeamka nikiwa nauwazia mhadhara huu kwa dhati. Nimejikuta nikijikumbusha mambo muhimu. Ninataka kwenda kutoa mhadhara madhubuti, wa kusisimua na kuelimisha. Hili huwa ni lengo langu kila ninapokubali mwaliko kama huu wa kwenda kutoa mhadhara popote.

Ninatambua wajibu wangu wa kuitendea haki taaluma. Ni wajibu wangu kama mtafiti na mwalimu kuitendea haki taaluma. Ni wajibu wangu kuwa mfano wa kuigwa na vijana wanaotafuta elimu, kama hao vijana watakaonisikiliza Chuoni Winona.

Ninatambua wajibu wangu wa kuwathibitishia wanaonialika kwamba hawakukosea kwa kunialika. Ninataka wasikilizaji wangu wakiri kuwa uamuzi wa kunialika ulikuwa sahihi. Sitaki wanaonialika na wanaonisikiliza niwaache wakisema kuwa afadhali wangemwalika mtu mwingine. Sitaki. Nataka wote wakiri kuwa mimi ndiye niliyefaa kutoa mhadhara ule. Wakiri kuwa mimi ndiye niliyefaa kujibu au kujadili masuali yao.

Ninatambua wajibu wangu mbele ya Mungu. Uhai wangu siku hadi siku, akili timamu, na vipaji alivyonipa Mungu ni dhamana kwa faida ya wanadamu. Ninapovitumia vipaji hivi ipasavyo, ninatimiza wajibu wangu kwa Mungu. Ninamtukuza Mungu. Ni furaha kwangu kutambua kwamba kutumia vipaji kwa namna hii ni kumtukuza Mungu, sawa na kusali.

Hayo ndiyo mawazo ambayo yamekuwa yakizunguka akilini mwangu tangu asubuhi. Ni aina ya mawazo yanayonisukuma nyakati kama hizi, ninapojiandaa kutekeleza mialiko. Ninapokubali mwaliko, ninafanya hivyo kwa dhati. Nikiona sitaweza kwa vigezo nilivyofafanua hapa juu, huwa nakiri tangu mwanzo ili wahusika wamtafute mtu mwingine, hata kama kwa kufanya hivyo ninajikosesha malipo yanayoendana na mwaliko.

Monday, June 8, 2015

Nimerekebisha Kitabu Changu

Kwa zaidi ya wiki moja, nimekuwa nikikipitia kitabu changu cha Matengo Folktales kwa ajili ya kukiboresha. Rekebisho moja nililofanya ni kuongeza ukubwa wa herufi ili kitabu kisomeke kwa urahisi zaidi. Nilikuwa pia naangalia kama kuna kosa lolote katika uandishi wa maneno. Nimerekebisha dosari zilizoziona katika maneno yapata matano

Ingawa nimetumia masaa mengi katika shughuli hiyo, kwangu si kitu, nikifananisha na kazi niliyofanya kwa miaka yapata ishirini na tatu katika kukiandaa kitabu hiki, tangu kuzitafuta na kuzirekodi hadithi, kuziandika kwa kuzitafsiri kwa ki-Swahili, kuzitafsiri kwa ki-Ingereza, kuzichambua, kusoma nadharia mbali mbali ili kutajirisha uchambuzi, na kurekebisha tafsiri na uchambuzi tena na tena.

Bahati ni kwamba miaka ya sabini na kitu, nilianza pia kufundisha somo la fasihi simulizi ("Oral Literature") na nadharia ya fasihi (Theory of Literature") katika idara ya "Literature" ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Katika kufundisha nilijionea mwenyewe kuwa hapakuwa na kitabu nilichoona kinafaa kwa somo la fasihi simulizi kwa wanafunzi wa kiwango cha chuo kikuu. Kuna usemi kuwa kama kitabu unachosoma huridhiki nacho, andika hicho kitabu unachokitaka.

Hali hiyo ya kukosekana kitabu kilichofaa katika ufundishaji wangu ilinihamasisha kutafakari masuala niliyokuwa nakumbaba nayo katika kuandika kitabu changu. Nilipania kuwa kiwe kinafaa kwa kufundishia. Miaka ilipita, nami nikawa natafiti, natafakari, na kuandika kiasi nilivyoweza. Wakati huo huo, nilikuwa nahangaika kuziboresha tafsiri za hadithi katika muswada. Shughuli hii ilinifundisha mengi kuhusu tafsiri, kama nilivyogusia katika makala iliyochapishwa katika jarida la Metamorphoses.

Historia ya kitabu hiki ni ndefu, na labda nitaweza kuiandika kiasi fulani siku za usoni. Ninakumbuka, kwa mfano, kwamba nilipokuwa nasomea masomo ya juu katika Chuo Kikuu cha Wisconsin, 1980-86, nilichukua somo la nadharia ya fasihi katika idara ya "Comparative Literature" lililofundishwa na Professor Keith Cohen. Kati ya nadharia tulizojifunza ni "Structuralism." Professor Cohen alitupa "homework" ya kuchambua hadithi yoyote kwa kutumia nadharia ya "Structuralism."

Nilitumia fursa hii kuichambua hadithi ya "The Tale of Two Women," ambayo imo katika Matengo Folktales. Mtu anayefahamu angalau kidogo nadharia ya "Structuralism" ataona athari zake, japo kidogo,  katika uchambuzi wangu.

Baada ya harakati za aina aina kwa miaka mingi, nilichapisha kitabu hiki mwaka 1999. Ndoto yangu ya kuandika kitabu cha kutumiwa katika ufundishaji wangu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam haikutimia nilivyotarajia. Niliondoka Tanzania mwaka 1991, nikaja kufundisha katika idara ya ki-Ingereza Chuoni St. Olaf, huku  nikiwa bado naufanyia kazi mswada wangu. Kwa hivi kitabu kilichapishwa huku Marekani, na wanaokisoma ni wa-Marekani, kuanzia katika jamii hadi vyuoni, kama nilivyoelezea hapa na  hapa.

Masimulizi ni mengi, na kama nilivyogusia, labda nitafute wasaa miaka ijayo niandike kumbukumbu zangu za historia ya kitabu hiki.

Tuesday, May 26, 2015

Mwaliko Chuo Kikuu cha Winona

Nimepata mwaliko kutoka Chuo Kikuu cha Winona, Minnesota, kwenda kutoa mhadhara tarehe 23 Juni. Huu utakuwa ni mchango wangu katika semina ya mafunzo kwa wanafunzi kutoka sehemu mbali mbali itakayofanyika Juni 17-27. Kama ilivyo kawaida yangu, nimeona niweke kumbukumbu hapa.

Mafunzo haya yatalenga kuwaandaa wanafunzi hao kwa masomo ya juu, waweze kuifahamu hali halisi ya maisha ya chuoni na taratibu za taaluma, waweze kujijengea hali ya kujitambua na uwezo wa uongozi.

Mratibu wa mafunzo, Alexander Hines, ambaye anafahamu kiasi shughuli zangu,  aliniambia tuangalie ni kipi kati ya vitabu vyangu viwili kitafaa zaidi kwa semina hii: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences au Matengo Folktales. Nilishauri kwamba hicho cha pili kingeendana vizuri zaidi na dhamira kuu ya semina.

Tumekubaliana. Tumekubaliana nikaelezee ni nini tunaweza kujifunza kutokana na tamaduni za jadi za Afrika katika masuala haya ya kujitambua, falsafa ya maisha, na uongozi katika dunia ya leo na kesho.

Kama ilivyo kawaida yangu, huwa napokea mialiko ya kutoa mchango wa mawazo kufuatana na mahitaji ya wale wanaonialika. Itabidi nitafakari na kuandaa mawazo yatakayotoa mchango unaohitajika katika semina. Wazo la kutumia kitabu cha Matengo Folktales kama msingi ni wazo muafaka, kwani masimulizi haya ya jadi yanathibitisha jinsi wahenga wetu walivyoyatafakari masuala muhimu ya maisha, mahusiano, na mengine yanatuhusu leo na yataendelea kuwa muhimu daima.
 

Saturday, April 4, 2015

Nimerejea Salama Kutoka Leech Lake Tribal College

Nilirejea jana jioni kutoka Leech Lake Tribal College, kwenye mkutano kuhusu "Narratives of Identity." Nilikuwa mmoja wa wanajopo wanne waliotoa mada, na mada yangu ilikuwa "Being African in America."

Niliongelea uzoefu wangu katika miaka mingi ya kuishi na kufundisha hapa Marekani, nikielezea kazi kubwa isiyoisha ya kujitambulisha kama mu-Afrika, ambaye ni tofauti na mu-Amerika Mweusi. Nilielezea jinsi suala hilo linavyosabisha mikanganyiko na kutoelewana baina ya wa-Marekani Weusi na wa-Afrika tuishio Marekani.

Nilisema wazi kuwa namna wanavyojiita na kujitambulisha wa-Marekani Weusi ni tofauti na namna tunavyojiita na kujitambulisha sisi wa-Afrika. Nilimnukuu Chimamanda Ngozi Adichie wa Nigeria ambaye katika mahojiano na katika riwaya yake maarufu ya Americanah, ameelezea vizuri suala hilo.

Nilimnukuu pia mwandishi Jamaica Kincaid wa Antigua, pande za Caribbean, ambaye pamoja na kuwa ni mweusi pia, hakuwahi kujiita kama wanavyojiita  wa-Marekani Weusi. Hayo mawazo yake niliyasoma katika mahojiano yaliyochapishwa mwaka 1991 katika jarida la Mississippi Review.

Nilisisitiza umuhimu wa kuheshimu haki ya kila jamii kujiita au kujitambulisha kwa majina wanayoyataka au yanayowaridhisha wenyewe. Watu wengine sherti wafuate njia hiyo badala ya kuwapachika watu majina ya utambulisho kama walivyofanya wakoloni.

Nilienda mbali zaidi na kuelezea suala la haki ya kila jamii kujieleza wenyewe, sio kuzimishwa kama walivyotuzimisha wakoloni, na wao wakawa wanaandika juu yetu.

Siwezi kuelezea hapa yote niliyosema. Nawazia kuendelea kutafakari suala hilo na kujisomea zaidi, na kuwasoma upya watu kama Frantz Fanon, Aime Cesaire, na Ngugi wa Thiong'o, ili hatimaye niandike makala kamili.

Hiyo jana, wakati nilipokuwa najitambulisha mkutanoni, nilisema kuwa nimeleta vitabu vyangu viwili kama zawadi kwa maktaba ya chuo cha Leech Lake Tribal College. Vitabu hivyo ni Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales. Vitabu hivi vilipokelewa kwa furaha na shukrani tele.

Nina hakika kuwa mkutano ule umesisimua watu. Jana hiyo hiyo, katika ukurasa wa Facebook wa Leech Lake Tribal College iliandikwa taarifa hii:

We had some great speakers on campus today for the Narratives of Identity presentations. One of the many memorable remarks from today's visit was by Joseph Mbele, St Olaf College- “I am not a person of color. I am Tanzanian which is a concept of colonization. Only when I came to America was I referred to as black. Naming yourself, knowing yourself, is a right…Construction of identities are not fixed and it’s our right to identify ourselves.”

(Picha ya juu kabisa na ya katikati ni kutoka Leech Lake Tribal College)

Saturday, March 21, 2015

Leo Nimehojiwa na "African Global Roots"

Nimerejea mchana huu kutoka Minneapolis, kwenye mahojiano na African Global Roots (AGR). Wiki mbili hivi zilizopita, Ndugu Petros Haile, mkurugenzi wa AGR alikuwa ameniomba tufanye mahojiano hayo.

Ndugu Haile nami tumefahamiana kwa miaka kadhaa. Nimewahi kushiriki katika program zake kwa kupeleka vitabu vyangu. Vile vile, alivyovyofahamu kuwa nimepeleka wanafunzi Tanzania kwenye kozi ya Hemingway, aliniomba niandike makala, ambayo aliichapisha.

Kwa mahojiano ya leo, Ndugu Haile alitaka tuongelee kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho alishakisoma miaka iliyopita. Alitamani, kwa kutumia mawasiliano ya AGR kusambaza ujumbe katika jamii ya wa-Afrika hapa Marekani na ulimwenguni na kwa watu wengine, kuhusu umuhimu wa kuyaelewa masuala ninayoongelea katika kitabu changu.

Kwa kuwa nilijua kuwa Ndugu Haile alitaka kunihoji kuhusu dhughuli zangu za kuelimisha umma, nilichukua pia nakala ya kitabu changu cha Matengo Folktales, ambacho ni ushahidi wa namna ninavyojitahidi kujifunza kutokana na masimulizi ya jadi ya mababu na mabibi zetu wa Afrika, na namna ninavyotumia hazina hii kuuelimisha ulimwengu kuhusu mchango wa wahenga wetu katika dunia.

Mahojiano yalikuwa mazuri. Ndugu Haile alitunga masuali muhimu kutokana na yaliyomo katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na pia aliniuliza masuali kuhusu utafiti wangu ulioniwezesha kuandika kitabu cha Matengo Folktales.

 Mahojiano haya tumefanyia katika kituo cha Afric Tempo, kinachomilikiwa na Ndugu Malick wa Senegal. Leo ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kufika mahali hapo, ambapo pana mgahawa, stoo, na studio ya kurekodia programu za televisheni.

Sitaandika zaidi kwa leo. Nangojea hadi mahojiano yatakapopatikana mtandaoni, ndipo niwaeleze walimwengu. Inafurahisha sana kuweza kukutana na kushirikiana na watu kama Malick na Petros, wenye kupenda kujitolea kwa hali na mali ili kujenga maelewano katika jamii. Jambo moja tuliloongelea leo na kukubaliana ni kuwa tunaamini kuwa Mungu ametuweka duniani kwa madhumuni kama hayo.


Thursday, February 26, 2015

Leo Nimefundisha Darasa Kwa Kutumia "Skype"

Asubuhi ya leo, nimefundisha darasa kwa kutumia "Skype." Ni darasa la Mwalimu Kristofer Olsen la somo la "Mythologies," katika Chuo Kikuu cha Montana, Marekani. Chuo hiki kiko mjini Bozeman, maili 995 kutoka hapa nilipo, Northfield, Minnesota. Niliandika kuhusu mpango wa kufundisha darasa hili katika blogu hii.

Katika mawasiliano ya barua pepe na Mwalimu Olsen, aliniuliza iwapo ningeweza kuongea na darasa lake la "Mythologies," ambalo lilikuwa linasoma kitabu changu cha Matengo Folktales. Aliniletea silabasi ya somo, inayoonyesha kuwa tarehe 24 na 26 wangejadili Matengo Folktales.

Jana jioni, binti yangu Zawadi alinielekeza tena namna ya kutumia "Skype," na alinisajili. Leo asubuhi, kipindi kilianza kama ilivypoangwa, saa nne na nusu za hapa Minnesota, ambayo ni saa tatu na nusu kule Montana. Nilikuwa mbele ya kompyuta, na wanafunzi na profesa wao walikuwa wananiona na kunisikia, nami nilikuwa nawaona na kuwasikia.

Tulifanya mengi. Niliombwa kusimulia hadithi mojawapo, ambayo ingechukua muda mfupi, nami nikasimulia hadithi ya "Hawk and Crow," iliyomo kitabuni. Niliwaambia wanafunzi kuwa kokote niendako kuongelea hadithi za jadi, huzisimulia papo kwa papo, badala ya kuzisoma. Katika kusimulia hadithi ya "Hawk and Crow," niliwaeleza machache kuhusu namna hadithi inavyosimuliwa, tofauti na inavyoonekana kimaandishi.

Masuali yao yalikuwa ya maana sana. Suali moja lilihusu jinsi nilivyorekodi hadithi na kuandaa kitabu cha Matengo Folktales. Suali jingine lilihusu mchakato wa kutafsiri. Jingine lilihusu vifo na mauaji katika hadithi hizo. Jingine lilihusu mhusika mjanja ("trickster") katika hadithi, kama vile Anansi na Sungura.

Niliwaeleza mambo kadhaa kuhusu mhusika huyu, katika tamaduni mbali mbali. Mhusika huyu hujitokeza kama mnyama (kama vile Anansi au Gizo, Kobe na Sungura), na katika tamaduni zingine hujitokeza katika umbo la binadamu, kama vile Nasreddin Hodja na Abu Nuwas. Niliongelea asili na maana ya mhusika huyu katika jamii, kwa kutumia nadharia za kisaikolojia za Carl Jung.

Niliguswa kwa namna ya pekee nilipoulizwa nifafanue dhana iliyomo katika blogu yangu kwamba ninaliona darasa kuwa ndio mahali pekee penye uhuru kamili wa kufikiri na kujieleza. Kumbe kuna watu wanaosoma blogu yangu kwa makini kiasi hiki.

Mawasiliano kama haya ya kutumia "Skype" ni maendeleo ya tekinolojia, ambayo yanatuwezesha kufanya mambo ambayo hatukuweza kuyafanya kabla. Jambo moja la kujifunza ni kuwa tunaweza kuendesha darasa bila kukutana katika chumba kimoja. Mimi kama mwalimu, ninaweza kuwafundisha wa-Tanzania ingawa niko nje ya Tanzania. Tuachane na mawazo kwamba sherti nirudi Tanzania ili kujenga nchi.

Wakati tekinolojia inasonga mbele na kutufungulia milango mipya, inashangza kuona jinsi wa-Tanzania kwa ujumla wanavyoendelea kuwa na mawazo yaliyopitwa na wakati. Kila ninapowasikia wakidai kuwa wataalam walioko nje warudi nyumbani wakajenge Taifa, nawazia suala hilo. Najiuliza ni lini wataamka usingizini na kutambua kuwa maendeleo ya tekinolojia ya mawasiliano yanazidi kuififisha mipaka ya kijiografia tuliyoizoea. Tunaingia kwenye dunia isiyo na mipaka, dunia ambamo mtu popote alipo anaweza akatoa mchango wake kwa walimwengu popote.

Sunday, February 15, 2015

Hadithi za Wa-Matengo Chuoni Montana

Leo nimepata ujumbe wa barua pepe kutoka kwa mwalimu mmoja wa Chuo Kikuu cha Montana.Ananiambia kuwa muhula huu anafundisha kozi ya Mythologies, na kati ya nyenzo anazotumia ni kitabu changu cha Matengo Folktales. Ananiulizia kama nitaweza kuongea na wanafunzi wake kwani itawafaidia sana kuweza kuongea na mtafiti aliyeandaa kitabu, akatoa maelezo kuhusu mambo kadha wa kadha, kama vile mchakato wa utafiti. Amependekeza kuwa ikiwezekana, tupange siku waweze kuongea nami kwa njia ya Skype.

Nimemjibu kuwa niko tayari kutoa mchango wangu, na kuwa ninafurahi kusikia kuwa anafundisha masimulizi ya wa-Matengo, sambamba na yale ya wa-Griki wa kale na wengine. Ingawa binti yangu Zawadi alishanionyesha namna ya kutumia Skype na akanisajili, sijawahi kutumia tekinolojia hii. Wengi wa rika langu au wale wanaotuzidi umri, tumezoea mambo ya zamani. Lakini dunia inavyobadilika, hasa tekinolojia, tunalazimika kukiri mazoea yana taabu.

Ujumbe niliopata leo umenifanya niwazie mambo kadhaa. Kwanza, ni kwamba nilifanya utafiti na kuandaa kitabu hiki kwa miaka yapata 23. Wakati nachapisha kitabu hiki, nilikuwa tayari ninafundisha huku Marekani, baada ya kufundisha Chuo Kukuu Cha Dar es Salaam. Nilikuwa na hamu kuwa kitabu kiwe mchango wangu kwa elimu Tanzania, kwa ufundishaji wa chuo kikuu, kwani hapakuwa na kitabu cha aina ile nchini, kilichofaa kufundishia somo hili la hadithi za mapokeo ("folktales"). Nilijua hayo, kwa vile mimi ndiye nilikuwa mhadhiri wa somo la fasihi simulizi, sambamba na somo la nadharia ya fasihi.

Kilichotokea ni kuwa kitabu hiki kinatumika au kimetumika katika vyuo vikuu vya Marekani. Vyuo ninavyovifahamu ni Wichita State University, University of California San Diego, St. Olaf College, Colorado College, na College of St. Benedict/St. John's University. Niliwahi kualikwa na hicho chuo cha St. Benedict/St. John's kutoa mhadhara katika darasa la "fairy tales," ambalo lilikuwa linasoma kitabu cha Matengo Folktales, kama nilivyoripoti katika blogu yangu, na nilitoa pia mhadhara kwa jumuia ya chuo kuhusu kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Hayo ni baadhi ya mawazo yaliyomo akilini mwangu, wakati huu ninapofikiria ujumbe niliopata leo. Ingawa kwa upande mmoja ninafurahi, sijawahi kuridhika na hali hii ya vitabu vyangu kuwa vinawafaidia wa-Marekani, lakini sio wa-Tanzania. Hata hivi, kosa si langu. Mimi natimiza wajibu wangu wa kufanya utafiti, kuandika, na kuchapisha maandishi. Baada ya hapo, mwenye macho haambiwi tazama.

Wednesday, December 3, 2014

Wazo la Kutafsiri Kitabu

Kwa wiki kadhaa, nimekuwa nikiwazia kutafsiri kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Siku chache zilizopita, niliandika kuhusu kitabu hiki katika blogu hii.

Nawazia kuzirekebisha insha zilizomo, na kuchapisha kitabu cha ki-Ingereza. Kufanya hivyo kutakipa kitabu hadhira kubwa zaidi kuliko ile ya wajuao ki-Swahili. Nina hakika, kwa mfano, kuwa wa-Marekani watakitafuta na kukisoma. Kwa ujumla wasomaji wa vitabu vyangu ni wa-Marekani.

Ninaposhiriki matamasha hapa Marekani, watu kadha wa kadha huja kwenye meza yangu na kuangalia vitabu, kuvinunua, au tu kuongea nami. Wako wanaoniuliza kama nimechapisha kitabu kingine, kwani vile vilivyopo mezani, vya ki-Ingereza, wanavyo au wamevisoma. Kauli hizi hata binti zangu, ambao hushirikiana nami, wamezisikia tena na tena.

Kwa miaka kadhaa, sijachapisha kitabu kipya. Sababu kubwa ni kuwa kuandika kitabu huchukua muda. Yaweza kuwa miezi au miaka. Kwa mfano, ilichukua miaka 23 hivi kuandaa kitabu cha Matengo Folktales. Vile vile, muda mwingi natumia katika kufanya utafiti na kuandika makala. Kutafsiri kitabu cha CHANGAMOTO, ni njia moja ya wazi ya kupatikana hicho kitabu kingine.

Kutafsiri CHANGAMOTO sio jambo la haraka. Kuna kitabu kingine katika lugha ya ki-Ingereza ambacho nataka kumaliza kukiandika kabla ya kuanza kutafsiri CHANGAMOTO. Hata hivi, siwezi kusema kuwa ni lazima ningoje. Muda wote ninakuwa na kazi kadhaa ninazoandika, na huwa sio rahisi kujua ni ipi itamalizika kabla ya ipi. Wanadamu tumejaliwa uwezo wa kufanya shughuli nyingi kwa pamoja, "multitasking" kwa ki-Ingereza. Ninachoombea ni uzima na akili timamu.

Monday, August 4, 2014

Furaha ya Kusainiwa Kitabu

Wapenzi wa vitabu wakishajipatia nakala ya kitabu cha mwandishi fulani, huguswa pale mwandishi anaposaini kitabu hicho. Aghalabu mwandishi huandika ujumbe mfupi kwa mteja huyu na kasha kuweka sahihi. Ni jambo linalowagusa sana wasomaji. Mimi mwenyewe, kama mwandishi, nimeshasaini vitabu vyangu vingi. Ninazo baadhi ya picha za matukio haya kutoka miaka iliyopita.

Msomaji makini na mwanablogu Christian Bwaya hivi karibuni ameelezea vizuri katika blogu yake, hisia zake baada ya kujipatia kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differencesambacho nilikuwa nimekisaini:

Namshukuru kwa dhati mwandishi wa kitabu hiki, Prof. Mbele kwa kunitumia kitabu hiki bila malipo, tena kwa gharama zake. Si jambo linalowatokea wengi. Ni furaha iliyoje hatimaye nimekipokea leo asubuhi. Naanza kukisoma kitabu hiki kwa mara nyingine, safari hii kikiwa na saini ya mwandishi. Ni upendeleo na muujiza wa pekee kunitokea katika siku za hivi karibuni. Ni lazima nimshukuru kwa dhati. Asante sana Profesa.

Utamaduni wa kusaini na kusainiwa vitabu nimeuzoea. Hata juzi tarehe 2 Agosti, niliposhiriki tamasha la Afrifest kule Brooklyn Park, Minnesota, nikiwa na vitabu vyangu, wadau kadhaa walionunua vitabu vyangu waliomba kusainiwa.

Hapa kushoto anaonekana mdau akiniangalia wakati nasaini nakala ya Matengo Folktales, ambayo alikuwa amenunua hapo.
Baada ya kusainiwa nakala yake, aliona furaha ya ziada kupiga picha nami huku akiwa ameshika kitabu hicho. Hiyo nayo ni kawaida hapa Marekani; wadau wakishanunua kitabu na kusainiwa, wanapenda kupiga picha na mwandishi, ikiwezekana.

Mdau huyu, aitwaye Adrian, m-Marekani Mweusi, alinifahamu tangu miaka kadhaa iliyopita. Alikuwa anasoma katika chuo fulani mjini Minneapolis. Kulikuwa na mkutano wa kitaaluma, nami nilikuwa mmoja wa wanajopo, nikitoa mada. Adrian alivutiwa sana. Halafu, alinisikiliza tena mwaka jana, nilipokuwa naongea katika jopo la watu wawili, nikiwa na Profesa Mahmud el-Khati, m-Marekani Mweusi, tukiongelea mbele ya umati, mahusiano baina ya wa-Afrika na wa-Marekani Weusi.

Adrian ni msomi kijana makini. Tayari naona nyota yake imeanza kung'ara katika medani ya uongozi katika jamii. Nina imani atafika mbali katika jamii ya wa-Marekani weusi na Marekani kwa ujumla.
Hapa kushoto ni picha nyingine, kutoka hiyo hiyo juzi katika tamasha la Afrifest, nikiwa na mdau kutoka Liberia, ambaye alikuwa amenunua kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, nami nikiwa nimekisaini. Inaonekana aliguswa sana, na hakuweza kujizuia kuniwekea mkono wake begani pangu.

Suala hili la kusaini au kusainiwa vitabu linastahili  kutafakariwa. Naamini lina vipengele kadhaa muhimu, kama vile kiutamaduni, kisoshiolojia, kisaikolojia, na kifalsafa. hata katika maduka ya vitabu hapa Marekani, aghalabu utaona vimepangwa vitabu vya mwandishi vikiwa na ujumbe "Signed copy." Jambo hili linaisukuma akili yangu kutaka kulielewa zaidi. Ningependa kujifunza zaidi kuhusu suala hili, kwa kusoma maandishi mbali mbali na kufanya tafakari mwenyewe.

Monday, July 28, 2014

Vitabu Nitakavyoonesha Katika Tamasha la Afrifest, Agosti 2

Kila mwaka wakati wa tamasha Afrifest, ninakuwa na meza ambapo naonesha vitabu vyangu na machapisho mengine. Meza ya vitabu huwavuta watu waje hapo. Kwa kawaida, mbali ya kutaka kunifahamu na kufahamu shughuli zangu, watu wanaofika hapo huwa na hamu ya kujua vitabu vinahusu nini. Wengi huvishika wao wenyewe na kuangalia ndani.

Kwa mawazo yangu, hiyo si fursa ya kuvipigia debe vitabu hivyo. Ninachofanya ni kujibu masuali niulizwayo. Kama suali linahusu kitabu au vitabu moja kwa moja, naelezea pia chimbuko la kitabu na uhusiano wake na shughuli zangu.

Ninaposema shughuli zangu, ninamaanisha ufundishaji wa fasihi na lugha ya ki-Ingereza, utafiti katika masimulizi ya jadi, uandishi, utoaji wa ushauri kuhusu tofauti za tamaduni kwa wa-Marekani waendao Afrika. Pia naongelea kuhusu kuwaandaa wanafunzi na kuwapeleka katika safari za masomo Afrika.

Kwa namna moja au nyingine, masuala ya aina hiyo yanajitokeza katika vitabu vyangu. Ni kawaida kwamba mtu anayekuja kwenye meza yangu anakuwa na hamu zaidi ya mada fulani, na hiyo inamfanya aulizie zaidi kuhusu kitabu fulani, na huamua kukinunua.

Tarehe 2 Agosti, katika tamasha la Afrifest litakalofanyika North View Junior High School, Brooklyn Park, hapa Minnesota, nitapeleka vitabu vifuatavyo.

Kimoja ni Matengo Folktales, ambacho ni mkusanyo wa hadithi kumi za jadi za wa-Matengo, nilizorekodi miaka ya katikati ya sabini na kitu, nikazitafsiri kwa ki-Ingereza na kuziandikia uchambuzi.

Kitabu hiki nimekiandika kwa namna ya kuweza kusomwa na yeyote, na pia katika masomo ya kiwango chochote, hadi chuo kikuu.













Kitabu kingine ni Notes on Achebe's "Things Fall Apart". Maelezo ya historia ya kitabu hiki niliyaandika katika blogu hii.

















Kitabu kingine  ni Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Wasomaji wa blogu hii watakuwa wamekisikia, na wengine wamekisoma.

Kitabu hiki nilikiandika katika mazingira maalum. Nikiwa mmoja wa washauri katika pogram za Associated Colleges of the Midwest za kupeleka wanafunzi Afrika, nilikuwa nikiongelea sana, kwenye mikutano yetu masuala ya athari za tofauti za tamaduni, kwani wanafunzi wanaporudi kutoka Afrika, wanakuwa na masuali mengi kuhusu mambo waliyoyaona kule. Mengine yalikuwa ya kustaajabisha na mengine ya kukera, na mengine ya kukanganya akili. Kazi yangu ilikuwa kufafanua, kwa sababu nawafahamu kutosha wa-Marekani na wa-Afrika. Basi washauri wenzangu katika program hizi walinishawishi niandike mwongozo, uweze kutumiwa nao na wanafunzi wao wanapokwenda Afrika.








Kingine ni CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Ni mkusanyo wa insha kuhusu masuala ya siasa, uchumi, elimu, na utamaduni, kwa kuzingatia hasa hali ya Tanzania.

Lengo lilikuwa kuwajibu wale waliokuwa wananiuliza kwa nini siandiki kwa ki-Swahili, ili wa- Tanzania walio wengi waweze kusoma. Pamoja na kukubaliana na mtazamo wao, sherti niseme pia kuwa wa-Tanzania waache kujiziuka; wajifunze ki-Ingereza na ikiwezekana, lugha zingine pia. Kiswahili kina manufaa, lakini hakitawafikisha mbali katika dunia ya utandawazi wa leo. Shaaban Robert, ambaye wa-Tanzania hupenda sana kuunukuu usemi wake kuwa titi la mama li tamu, akimaanisha lugha yake ya ki-Swahili, hakuwa mvivu kama walivyo wa-Tanzania wa leo. Pamoja na kuwa hakuwa na fursa kama tulizo nazo leo, alijitahidi akajifunza ki-Ingereza na hata kukitumia. Aliziheshimu lugha na tamaduni za kigeni.

Kitabu kingine ni Africans in the World. Hiki ni kijitabu kidogo sana. Kinahusu historia ya wa-Afrika na wengine wenye asili ya Afrika, pamoja na siasa, utamaduni, na mengine kama hayo. Kilitokana na Afrifest ya kwanza mwaka 2007. Niliandaa magango kumi, kila bango likiwa linaelezea kipengele fulani. Hatimaye, yaliyomo kwenye mabango niliyachapisha kwa umbo la hiki kijitabu. Hakuna tofauti yoyote kati ya yale mabango na hiki kijitabu, isipokuwa ukubwa tu. Ufundishaji wangu wa somo la "Africa and the Americas," chuoni St. Olaf, ulinirahizishia kazi ya kuandika kazi hii.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...