Showing posts with label hadithi za mapokeo. Show all posts
Showing posts with label hadithi za mapokeo. Show all posts

Sunday, February 15, 2015

Hadithi za Wa-Matengo Chuoni Montana

Leo nimepata ujumbe wa barua pepe kutoka kwa mwalimu mmoja wa Chuo Kikuu cha Montana.Ananiambia kuwa muhula huu anafundisha kozi ya Mythologies, na kati ya nyenzo anazotumia ni kitabu changu cha Matengo Folktales. Ananiulizia kama nitaweza kuongea na wanafunzi wake kwani itawafaidia sana kuweza kuongea na mtafiti aliyeandaa kitabu, akatoa maelezo kuhusu mambo kadha wa kadha, kama vile mchakato wa utafiti. Amependekeza kuwa ikiwezekana, tupange siku waweze kuongea nami kwa njia ya Skype.

Nimemjibu kuwa niko tayari kutoa mchango wangu, na kuwa ninafurahi kusikia kuwa anafundisha masimulizi ya wa-Matengo, sambamba na yale ya wa-Griki wa kale na wengine. Ingawa binti yangu Zawadi alishanionyesha namna ya kutumia Skype na akanisajili, sijawahi kutumia tekinolojia hii. Wengi wa rika langu au wale wanaotuzidi umri, tumezoea mambo ya zamani. Lakini dunia inavyobadilika, hasa tekinolojia, tunalazimika kukiri mazoea yana taabu.

Ujumbe niliopata leo umenifanya niwazie mambo kadhaa. Kwanza, ni kwamba nilifanya utafiti na kuandaa kitabu hiki kwa miaka yapata 23. Wakati nachapisha kitabu hiki, nilikuwa tayari ninafundisha huku Marekani, baada ya kufundisha Chuo Kukuu Cha Dar es Salaam. Nilikuwa na hamu kuwa kitabu kiwe mchango wangu kwa elimu Tanzania, kwa ufundishaji wa chuo kikuu, kwani hapakuwa na kitabu cha aina ile nchini, kilichofaa kufundishia somo hili la hadithi za mapokeo ("folktales"). Nilijua hayo, kwa vile mimi ndiye nilikuwa mhadhiri wa somo la fasihi simulizi, sambamba na somo la nadharia ya fasihi.

Kilichotokea ni kuwa kitabu hiki kinatumika au kimetumika katika vyuo vikuu vya Marekani. Vyuo ninavyovifahamu ni Wichita State University, University of California San Diego, St. Olaf College, Colorado College, na College of St. Benedict/St. John's University. Niliwahi kualikwa na hicho chuo cha St. Benedict/St. John's kutoa mhadhara katika darasa la "fairy tales," ambalo lilikuwa linasoma kitabu cha Matengo Folktales, kama nilivyoripoti katika blogu yangu, na nilitoa pia mhadhara kwa jumuia ya chuo kuhusu kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Hayo ni baadhi ya mawazo yaliyomo akilini mwangu, wakati huu ninapofikiria ujumbe niliopata leo. Ingawa kwa upande mmoja ninafurahi, sijawahi kuridhika na hali hii ya vitabu vyangu kuwa vinawafaidia wa-Marekani, lakini sio wa-Tanzania. Hata hivi, kosa si langu. Mimi natimiza wajibu wangu wa kufanya utafiti, kuandika, na kuchapisha maandishi. Baada ya hapo, mwenye macho haambiwi tazama.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...