Showing posts with label wajibu. Show all posts
Showing posts with label wajibu. Show all posts

Sunday, December 17, 2017

Tumetoka Darasani

Picha hii ilipigwa tarehe 29 Novemba. Niko na wanafunzi wangu, tukiwa tumetoka darasani. katika somo la "First Year Writing." Hili ni somo la uandishi bora wa ki-Ingereza. Ninalipenda somo hili kama ninavyoyapenda masomo yangu mengine. Darasa letu lina wanafunzi 19.

Baada ya kumaliza kipindi tulitawanyika, lakini dakika chache baadaye nilikutana na hao wawili katika jengo la Buntrock Commons karibu na maktaba, tukapiga picha. Huyu wa katikati anatoka Norway, na huyu mwenzake ni wa hapa Marekani.

Nina bahati na ninafurahi kuwa mwalimu, kushughulika na wanafunzi na vitabu muda wote. Ni kazi ambayo niliitamani tangu nilipokuwa kijana mdogo. Nilipofundishwa ualimu katika chuo kikuu cha Dar es Salaam, ambapo nilisomea Literature, English, na Education, nilifundishwa kuwa mwalimu anashika nafasi ya wazazi, in loco parentis, kwa ki-Latini. Ninawaona wanafunzi kama watoto wangu.

Ninachukulia jukumu langu la kuwaelimisha na kuwalea wanafunzi kwa dhati. Tangu nilipoanza kufundisha, chuo kikuu cha Dar es Salaam, mwaka 1973, nimezingatia wajibu na maadili ya ualimu, ambayo ni kujielimisha kwa bidii, kufundisha kwa uwezo wangu wote, na kuwatendea haki wnafunzi wote bila upendeleo.

Ninafurahi kufundisha hapa chuoni St. Olaf. Walimu wanachapa kazi na uongozi wa chuo unawaheshimu. Wanafunzi wanajua wajibu wao. Wana heshima, na ni wasikivu, wenye dukuduku ya kuhoji na kujua mambo. Ninawapenda. Pamoja na kuwafundisha kwa moyo wote, ninapenda kuwatania. Popote tunapokutana, tunafurahi kama inavyoonekana pichani.

Sunday, January 22, 2017

Maandamano Makubwa Dhidi ya Rais Trump

Jana hapa Marekani yamefanyika maandamano makubwa dhidi ya rais Donald Trump, ambaye aliapishwa juzi. Maandamano haya yaliyoandaliwa na kukusudiwa kwa wanawake, yanasemekana kuwa makubwa kuliko yote yaliyowahi kufanyika katika historia ya Marekani kwa siku moja. Maandamano haya yamefana sana, kwa mahudhurio na hotuba mbali mbali, na yametoa ujumbe wa wazi kuwa serikali ya Rais Trump isitegemee kuwa itatekeleza ajenda yake bila vipingamizi.

Marekani ni nchi inayoheshimu uhuru wa watu kujieleza. Katiba inalinda uhuru huo. Ndio maana maandamano ya kumpinga Rais Trump yalifanyika nchi nzima bila kipingamizi. Polisi walikuwepo kwa ajili ya kulinda amani, si kuzuia maandamano, wala kuwakamata wahutubiaji waliokuwa wanamrarua Rais Trump. Polisi wana wajibu wa kuhakikisha kuwa waandamanaji wanayo mazingira muafaka na fursa kamili ya kutekeleza haki yao ya kuandamana na kuelezea mawazo yao.

Ninajua kuna wengine walioshiriki maandamano ya jana ambao si wa-Marekani. Kuna wakimbizi na wahamiaji kutoka nchi mbali mbali ambao walishiriki. Hapa Marekani, huhitaji kuwa raia ili kushiriki maandamano. Mimi sikushiriki, kwa sababu zangu binafsi.

Kwa kuwa mimi si raia wa Marekani, na sijawahi kuwazia kuwa raia, sioni kama nina haki au sababu ya kujihusisha na siasa za ndani za Marekani. Sipigi kura wakati wa uchaguzi wa viongozi. Kwa nini nijihusishe na maamuzi ya hao viongozi? Kama maamuzi yataiathiri nchi yangu, hapo nitaona nina wajibu wa kuisemea nchi yangu. Ninatambua wajibu wangu wa kuitetea nchi yangu popote nilipo.

Ingekuwa maandamano yanahusu masuala ya Tanzania ningeshiriki, kwa sababu Tanzania ni nchi yangu. Serikali ya Tanzania ikifanya mambo yasiyokubalika, halafu wa-Tanzania au marafiki wa Tanzania wakaandaa maandamano ya kupinga au kulaani, ni haki yangu kushiriki. Kule Uingereza, mwaka 2015, wa-Tanzania waliandamana kupinga mwenendo wa uchaguzi Zanzibar. Maandamano kama yale ni haki yangu kushiriki.

Huu utamaduni wa Marekani na nchi kama Uingereza unaendana na tangazo la kimataifa la haki za binadamu. Baada ya maandamano haya ya kihistoria ya jana dhidi yake, Rais Trump ametuma ujumbe: "Peaceful protests are a hallmark of our democracy. Even if I don't always agree, I recognize the rights of people to express their views." Tafsiri kwa ki-Swahili ni, "Maandamano ya upinzani ya amani ni kielelezo thabiti cha demokrasia yetu. Hata kama mara nyingine sikubaliani na wahusika, ninatambua haki ya watu kuelezea mawazo yao."

Friday, June 12, 2015

Siku ya Mhadhara Chuo Kikuu Winona Inakaribia

Siku hazikawii. Zimebaki siku kumi na moja tu kufikia siku ya mhadhara wangu Chuo Kikuu cha Winona, utakaotokana na utafiti wangu juu ya falsafa zilizomo katika masimulizi ya jadi kama inavyodhihirika katika kitabu changu cha Matengo Folktales. Niliandika taarifa ya awali ya mhadhara huu katika blogu hii.

Leo nimeamka nikiwa nauwazia mhadhara huu kwa dhati. Nimejikuta nikijikumbusha mambo muhimu. Ninataka kwenda kutoa mhadhara madhubuti, wa kusisimua na kuelimisha. Hili huwa ni lengo langu kila ninapokubali mwaliko kama huu wa kwenda kutoa mhadhara popote.

Ninatambua wajibu wangu wa kuitendea haki taaluma. Ni wajibu wangu kama mtafiti na mwalimu kuitendea haki taaluma. Ni wajibu wangu kuwa mfano wa kuigwa na vijana wanaotafuta elimu, kama hao vijana watakaonisikiliza Chuoni Winona.

Ninatambua wajibu wangu wa kuwathibitishia wanaonialika kwamba hawakukosea kwa kunialika. Ninataka wasikilizaji wangu wakiri kuwa uamuzi wa kunialika ulikuwa sahihi. Sitaki wanaonialika na wanaonisikiliza niwaache wakisema kuwa afadhali wangemwalika mtu mwingine. Sitaki. Nataka wote wakiri kuwa mimi ndiye niliyefaa kutoa mhadhara ule. Wakiri kuwa mimi ndiye niliyefaa kujibu au kujadili masuali yao.

Ninatambua wajibu wangu mbele ya Mungu. Uhai wangu siku hadi siku, akili timamu, na vipaji alivyonipa Mungu ni dhamana kwa faida ya wanadamu. Ninapovitumia vipaji hivi ipasavyo, ninatimiza wajibu wangu kwa Mungu. Ninamtukuza Mungu. Ni furaha kwangu kutambua kwamba kutumia vipaji kwa namna hii ni kumtukuza Mungu, sawa na kusali.

Hayo ndiyo mawazo ambayo yamekuwa yakizunguka akilini mwangu tangu asubuhi. Ni aina ya mawazo yanayonisukuma nyakati kama hizi, ninapojiandaa kutekeleza mialiko. Ninapokubali mwaliko, ninafanya hivyo kwa dhati. Nikiona sitaweza kwa vigezo nilivyofafanua hapa juu, huwa nakiri tangu mwanzo ili wahusika wamtafute mtu mwingine, hata kama kwa kufanya hivyo ninajikosesha malipo yanayoendana na mwaliko.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...