Showing posts with label fasihi ya Afrika. Show all posts
Showing posts with label fasihi ya Afrika. Show all posts

Wednesday, July 12, 2017

Mazungumzo Global Minnesota Kuhusu Fasihi





Leo nilikwenda Minneapolis, kwa mwaliko wa taasisi iitwayo Global Minnesota, kutoa mhadhara juu ya fasihi simulizi na andishi wa Afrika, kuanzia chimbuko lake barani Afrika hadi Marekani, ambako hii fasihi simulizi ililetwa na watu waliosafirishwa kutoka Afrika kama watumwa. Watoa mada tulikuwa wawili, mwingine ni Profesa Mzenga Wanyama anayefundisha katika chuo cha Augsburg.


Pichani hapa kushoto, tunaonekana kama ifuatavyo. Kutoka kushoto ni Tazo kutoka Zambia, ambaye alihitimu chuo cha St. Olaf  mwaka jana, na amajiriwa kwa mwaka huu moja na Global Minnesota. Wa pili ni Carol, rais wa Global Minnesota. Wa tatu ni Profesa Wanyama. Wa nne ni mimi, na wa tano ni Tim, mkurugenzi wa programu wa Global Minnesota, ambaye alikuwa mtu wa kwanza kuniuliza kama ningekuwa tayari kutoa mhadhara Global Minnesota, wakati tulipokutana katika tamasha la Togo miezi michache iliyopita.


















Hapa kushoto ninaonekana nikiongea. Sina kawaida ya kusoma hotuba, hata kama nimeandika vizuri. Ninashindwa kuangalia karatasi badala ya kuangalia watu. Hata darasani, sisomi nilichoandaa kimaandishi. Katika kujiandaa kwa ajili ya kutoa mihadhara, ninaandika sana hoja na maelezo yangu. Lakini wakati wa kutoa mhadhara, ninatumia kumbukumbu tu ya yale niliyoandika.

Kwa hivyo, katika mhadhara wa leo, nimeongelea chimbuko la binadamu ambalo liliendana na uwezo kutembea wima kwa miguu tu, kutumia lugha, na  kutumia na kutengeneza zana za kazi. Hayo yote kwa pamoja yalisababisha kuumbika kwa kiumbe aitwaye binadamu kimwili, kiakili, na kadhalika. Huu ndio msingi wa kukua kwa lugha na fasihi, ambayo ilihitaji ubunifu, kumbukumbu, na uwezo wa kutambua na kuunda sanaa,  ikiwemo fasihi, ambayo ni sanaa inayotumia lugha.

Maendeleo ya tekinolojia, ambayo ilianzia na kutengeneza zana za mawe au miti, yalifikia hatua ya binadamu kuvumbua maandishi. Hapo ndipo ikawezekana kuandika yale yaliyokuwa katika fasihi simulizi, na ushahidi tunauona katika Misri ya miaka yapata elfu nne au tano iliyopita. Hadithi zilizoandikwa wakati ule ni kama "The Tale of Two Brothers," "The Story of Sinuhe," na "The Tale of the Ship-wrecked Sailor."

Lakini pia, uandishi ulimwezesha binadamu kutunga fasihi kimaandishi. Waandishi, hasa wa mwanzo, walikuwa wamelelewa katika fasihi simulizi, kiasi kwamba kazi zao andishi zilibeba athari za wazi za fasihi simulizi. Mifano kutoka Afrika ni The Golden Ass (Apuleus), Chaka (Thomas Mofolo), The Palm Wine Drinkard (Amos Tutuola), Things Fall Apart (Chinua Achebe), The Dilemma of a Ghost (Ama Ata Aidoo). Waandishi weusi wa bara la Marekani kama vile Zora Neal Hurston, Toni Morrison, na Edwidge Dandicat.




Baada ya mimi kuongea, alifuata Profesa Mzenga Wanyama, kama inavyoonekana pichani hapa kushoto. Yeye aliongelea zaidi waandishi weusi wa Marekani, akianzia na Phyllis Wheatley. Aliongelea elimu na itikadi aliyofundishwa msichana na hata alipoandika mashairi yake, akawa anaelezea pia waandishi wa ki-Afrika kama vile Achebe na Ngugi wa Thiong'o, na Chimamanda Ngozi Adichie. Kati ya masuala aliyosisitiza ni utumwa wa fikra na umuhimu wa kujikomboa. Baada ya hotuba zetu, palikuwa na muda mfupi wa masuali na majibu.









Baada ya kikao kwisha, hawakosekani wahudhuriaji wenye kupenda kuongea zaidi na mtoa mada. Hapa kushoto niko na profesa mstaafu wa College of St. Benedict, Minnesota. Ni mzaliwa wa India. Nilimwambia kuwa nilishawahi kualikwa kwenye chuo kile kutoa mihadhara.













Hapa kushoto anaonekana Carol, rais wa Global Minnesota, na binti yangu Assumpta, ambaye aliwahi kufanya kazi na Carol, wakati taasisi ilipokuwa inaitwa International Institute of Minnesota.















Hapa kushoto niko na mama moja kutoka Brazil, ambaye ni mfanyakazi katika Minnesota Department of Human Services. Sikumbuki kama nimewahi kuongea na mama yeyote wa Brazil mwenye asili ya Afrika. Kwa hiyo, hiyo ilikuwa ni kumbukumbu ya pekee.
















Hapa kushoto niko na vijana wawili waliohitimu masomo chuo cha St. Olaf ambapo ninafundisha. Huyu wa kushoto kabisa ni raia wa Swaziland, na huyu wa kulia ni Tazo wa Zambia anayeonekana katika picha ya kwanza hapo juu.













Hapo kushoto niko na binti zangu, Assumpta na Zawadi. Ninafurahi wanapokuja kunisikiliza katika mihadhara. Wataweza kuelezea habari zangu kwa yeyote atakayependa kuelewa zaidi shughuli zangu katika jamii.

Nimalizie kwa kusema kuwa wakati tulipokuwa tunaagana, viongozi wa Global Minnesota walielezea nia yao ya kuniita tena kwenye program nyingine. Tim aliongezea kuwa kama  angekuwa amekumbuka, vitabu vyangu vingekuwepo kwa ajili ya watu waliohudhuria mkutano wa leo. Nami nilikuwa sijawazia jambo hilo. Siku zijazo litaweza kufanyika.

Monday, July 10, 2017

Nitawasilisha Mada Global Minnesota

Nimealikwa na taasisi iitwayo Global Minnesota kutoa mada tarehe 12 Julai juu ya mwendelezo wa fasihi ya ki-Afrika kuanzia chimbuko lake kama fasihi simulizi hadi fasihi andishi ya leo. Mael"ezo zaidi yako mtandaoni

--------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------
Global Conversations: African Folktales to Contemporary Authors

JULY 12 @ 6:00 PM CDT / Free

From ancient oral traditions to contemporary literature, African stories reflect wisdom, cultural identities, and social values developed over countless generations. Join us, St. Olaf College Associate Professor Joseph Mbele, and Augsburg College Associate Professor Mzenga Wanyama for an exploration of how these stories find expression today, both in Africa and in the African diaspora.

Speakers
Joseph Mbele, Associate Professor of English at St. Olaf College, is a folklorist and author. His writings, including Matengo Folktales, illuminate the underlying values that shape cultures. Dr. Mbele has done fieldwork in Kenya, Tanzania, and the U.S., and has given lectures and presented conference papers in Canada, Finland, India, Israel, Kenya, Tanzania, Uganda, and the U.S. After earning a Ph.D. from the University of Wisconsin and before coming to St. Olaf in 1990 to teach post-colonial and third-world literature, he taught in the Literature Department at the University of Dar es Salaam, Tanzania. Over the years, he has taught courses such as Swahili Literature, Theory of Literature, African Literature, Sociology of Literature, Postcolonial and Third World Literature, The Epic, and African-American Literature.

Mzenga Aggrey Wanyama, Associate Professor of English at Augsburg College, was born and raised in Kenya where he received his bachelor’s of education and master’s degrees from the University of Nairobi and then taught English language and literature in Kenyan High schools and at Kenyatta University. In the United States, he had a two-year stint in the graduate program at Howard University in Washington, D.C. before attending the University of Minnesota where he earned a Ph.D. in English. Mzenga also worked as an Assistant Professor of English at St. Cloud State University where he taught courses in literature and writing. His areas of focus are Postcolonial theory and literature and African American literary history.

Presented in partnership with the Friends of the Minneapolis Central Library.

Global Conversations: African Folktales to Contemporary Authors
Wednesday, July 12, 2017
6:00 PM

Monday, December 12, 2016

Leo Nimemaliza Kufundisha Muhula wa Kwanza

Leo nimemaliza kufundisha muhula wa kwanza. Nilikuwa ninafundisha kozi tatu: "First Year Writing," "African Literature," na "Muslim Women Writers." Nilihitimisha ufundishaji wa "First Year Writin"g wiki iliyopita, ili kuwapa wanafunzi muda wa kuandika insha kuu ya mwisho. Katika kozi hii, ninafundisha uandishi bora wa ki-Ingereza, na uangalifu unaotakiwa katika vipengele vyote , kuanzia neno, hadi sentensi, hadi insha.

Katika African Literature tumemalizia muhula tukisoma riwaya ya Mia Couto, The Tuner of Silences. Mia Couto ni mwandishi wa Msumbiji, ambaye ni maarufu sana. Amepata sifa na tuzo kem kem, ikiwemo tuzo ya Neustadt. The Tuner of Silences ni riwaya inayosisimua akili kwa jinsi ilivyosheheni ubunifu wa kisanaa na kifikra.

Kuna mengi ya kutafakari katika riwaya hii, hasa yatokanayo na dini, fasihi linganishi, historia, falsafa kama vile "existentialism," na mikondo ya falsafa ya sanaa kama vile "surrealism."  Vile vile, taaluma ya saikolojia, kama vile mkondo wa "psychoanalysis," inasaidia kutafakari dhamira zilizomo. Kuisoma na kuufaidi utajiri wa riwaya kama The Tuner of Silences kunahitaji upeo mpana wa mawazo ambao unatokana na kusoma kwingi, sio tu fasihi bali taaluma mbali mbali.

Katika kuiongelea The Tuner of Silences darasani, nimesisitiza jambo hilo, Nimefundisha wanafunzi umuhimu wa kuzingatia nadharia za usomaji kama zilivyoelezwa na Cleanth Brooks katika insha yake, "The Language of Paradox," na pia zilivyoelezwa na Roland Barthes katika kitabu chake kiitwacho S/Z: An Essay.

Katika kozi ya "Muslim Women Writers," tumemalizia muhula tukisoma riwaya ya Monica Ali, Brick Lane. Ni riwaya ndefu, inayoelezea maisha ya watu wa Bangladesh ambao wanaishi Uingereza. Ni jamii ya ki-Islam, na tunaiona inavyojitahidi kustahimili na kustawi katika mazingira ya ugenini.

Hii ni jamii kama jamii zingine, yenye watu wenye maadili mema na ari ya kuwa mfano kwa wengine, na pia wako ambao tabia zao zina walakini. Wanapenda kufuatilia habari za wenzao, na ni wapiga majungu. Tofauti baina ya utamaduni wao na ule wa wa-Ingereza zinajitokeza, na pia tofauti baina ya vijana na watu wazima au wazee. Vijana wanaonekana kuiga mambo ya vijana wa kizungu, yakiwemo ambayo si mazuri.

Kufundisha kazi ya fasihi kutoka Bangladesh imekuwa ni fursa ya kuelezea historia ya fasihi ya nchi hiyo, ukiwemo mchango mkubwa wa Rabindranath Tagore, mwandishi wa mashairi, tamthilia, riwaya, na insha, ambaye aliitwaa tuzo ya Nobel mwaka 1913. Kwa bahati nzuri, Tagore ametajwa katika Brick Lane, kwa jinsi alivyo hazina kwa watu wa Bangladesh. Lakini jambo la kuzingatia ni kuwa Tagore ni mwamba katika fasihi ya ulimwengu, aliyeheshimiwa na miamba wenzake kama vile W.B. Yeats wa Ireland, aliyekuwa na urafiki na mawasiliano na Tagore.

Leo, katika kuhitimisha kozi yetu ya "Muslim Women Writers," nimewaomba wanafunzi ushauri juu ya kuitumia tena riwaya hii siku za usoni, nitakapofundisha kozi hii. Wameniambia kuwa ni riwaya muhimu sana, ingawa inachukua muda sana kuisoma. Wameshauri kwamba nitakapofundisha tena kozi hii, Brick Lane iwe mwanzoni, wakati wanafunzi wakiwa bado hawajachoka na masomo. Riwaya zingine, ambazo ni fupi fupi, zije baadaye. Nimewashukuru kwa ushauri huo wa wanafunzi ambao wamepitia kozi yangu, nikizingatia kuwa adhabu ya kaburi aijuaye maiti.

Monday, October 31, 2016

Black African Voices: Tungo za Afrika

Pamoja na kwamba fasihi ya Afrika, kama ilivyo ulimwenguni kote, inastawi kwa kasi kadiri miaka inavyopita, na waandishi wapya hujijokeza na kujipambanua, ni lazima pia kukumbuka na kusoma uandishi wa zamani. Kwa yeyote anayependa fasihi, awe ni mwanafunzi, mwalimu au msomaji wa kawaida, usomaji wa aina hii ni jambo lisilohitaji mjadala. Fasihi inahitaji usomaji usio na kikomo, sio tu kwa kuwa ina historia ndefu, bali pia kwa kuwa inastawi ulimwenguni kote na daima inaendelea kuchanua kama maua.

Mimi, mwalimu wa fasihi, ninazingatia umuhimu wa kufundisha kazi za tangu zamani hadi leo. Fasihi ya kila taifa au sehemu yoyote ya dunia ina historia, na fasihi inayoandikwa leo ni mwendelezo wa mkondo ulioanza zamani.

Katika siku hizi chache, nimekuwa ninasoma Black African Voices, kitabu kilichohaririwa na James E. Miller na wenzake. Sikumbuki ni lini nilikinunua kitabu hiki, lakini mara kwa mara katika kuangalia vitabu vyangu, nilikuwa ninakichungulia kitabu hiki, nikawa ninakumbuka kwa furaha enzi za ujana wangu, kuanzia miaka ya sitini na kitu, nilipokuwa ninasoma badhi ya tungo zilizomo. Kuna hadithi kadhaa na nyimbo za fasihi simulizi, mashairi, hadithi fupi na maandishi mengine ya waandishi mbali mbali.

Baadhi ya waandishi ambao tungo zao zimo katika kitabu hiki ni Ezekiel Mphahlele, Raphael Armatoe, Peter Abrahams, Birago Diop, David Diop, Cyprian Ekwensi, Richard Rive, Wole Soyinka, John Pepper Clark, James D. Rubadiri, na Grace Ogot. Ni furaha isiyoelezeka kuzisoma tena hadithi zilizonisisimua tangu miaka ile ya sitini na kitu, nilipokuwa mwanafunzi katika seminari ya Likonde, 1967-70 na Mkwawa High School, 1971-72.

Baadhi ya hadithi hizo ni "No Room at Solitaire," ya Richard Rive; "The Dignity of Begging," ya Bloke Modisane, "The Rain Came," ya Grace Ogot. Baadhi ya mashairi yaliyonisisimua miaka ile ni "Stanley Meets Mutesa" (James D. Rubadiri), "Africa" na "Listen Comrades" (David Diop), na "Prayer to Masks" (Leopold Sedar Senghor). Kuna pia tamthilia ya Edufa ya Efua Sutherland.

Katika Black African Voices kuna pia tungo za waandishi ambao sikuwafahamu miaka ile ya ujana wangu, kama vile J, Benibengor Blay (Ghana), Tshakatumba (Congo), Rui Nogar (Mozambique). Siwezi kuwataja waandishi wote ambao kazi zao zimo katika kitabu hiki, bali ninapenda tu kusisitiza kuwa ninaguswa sana na uandishi huu wa kuanzia miaka ya kabla ya kuzaliwa kwangu hadi ujana wangu. Wahariri walifanya kazi nzuri kuzikusanya tungo hizi katika kitabu kimoja.

Tuesday, August 25, 2015

Nimekikuta Kitabu Changu Kinameremeta Dukani

Mchana huu nimemaliza kusahihisha mtihani wa kumalizia muhula wa somo langu la "African Literature." Nimekwenda chuoni kuwarudishia wanafunzi daftari zao, nikiwa na furaha ya kuwa na wiki mbili tatu za "uhuru," kabla ya kuanza muhula mwingine.

Baada ya kurudisha daftari, niliingia katika duka la vitabu. Nilizunguka kidogo tu humo ndani nikaona kitabu changu cha Matengo Folktales kimewekwa mahali pa wazi, pamoja na vitabu vingine vichache. Kinaonekana pichani chenye rangi ya manjano na ramani ya Afrika.

Huu ni utaratibu wa duka letu la vitabu. Kila wakati wanachagua vitabu vichache na kuviweka sehemu hizo za wazi ili viweze kuonekana kirahisi kwa wateja. Kufuatana na utaratibu uliopo, kitabu kitakuwa hapo kwa siku kadhaa, na hata wiki kadhaa, kabla ya kurudishwa sehemu yake.

Katika duka hili la chuoni St. Olaf vinapatkana vitabu vyangu vyote. Mbali ya wanafunzi, waalimu, na wafanyakazi wengine wa chuo, wageni wanaokitembelea chuo hupenda kuingia katika hili duka la vitabu, ambalo huuza pia bidhaa mbali mbali, kama ilivyo kawaida katika maduka ya vitabu ya vyuo vya Marekani.

Kila ninapoviona vitabu vyangu katika duka hili, mawazo hunijia, hasa kuhusu namna vitabu hivi vinavyowafaidia wa-Marekani. Vinawafaidia kielimu, kwa kuwa vinatumika katika masomo. Vinawafaidia kibiashara, kwa kuviuza, na vinachangia ajira hata kama ni kiasi kidogo sana, kwa wachapishaji, wasafirishaji, na wahudumu wa duka kama hili la Chuo cha St. Olaf. Nawazia mambo ya aina hii.

Monday, June 8, 2015

Mhadhiri wa Algeria Amefurahi Kupata Kitabu

Jana, niliporejea kutoka kanisani, nilikuta ujumbe katika ukurasa wangu wa Facebook kutoka kwa Samir Zine Arab, mhadhiri wa "African Literature and Listening Skills" katika chuo kikuu cha Hassiba Ben Bouali Chlef, Algeria. Alikuwa anashukuru kupata nakala ya kijitabu changu, Notes on Achebe's Things Fall Apart ambayo nilimtumia siku kadhaa zilizopita.

Ujumbe wake, ulioambatana na picha inayoonyesha kitabu pamoja na bahasha niliyotumia, kama inavyoonekana hapa kushoto, ameusambaza kwa marafiki zake wa Facebook ambao mimi ni mmoja wao. Amenigusa kwa namna alivyoandika:

Dear friends, brothers and sisters! Today I'm the happiest man on earth! This morning I received a lovely book from a great professor Joseph Mbele! Thank you so much dear!!

Pamoja na ujumbe huu, Mwalimu Samir ameniandikia pia ujumbe binafsi ambao nao umenigusa sana. Kwake na kwangu imekuwa ni furaha. Ninavutiwa na watu wa aina ya huyu mwalimu, ambao wana duku duku ya kutafuta elimu. Aliposikia tu kuhusu kijitabu changu, alikitaka.

Ninafurahi kuwa wanafunzi Algeria watapata fursa ya kuyafamu na kuyatafakari mawazo niliyoandika katika kijitabu hiki, ambacho Mwalimu Samir alikitamani tangu nilipokitaja katika Facebook, tarehe 11 Mei. Taarifa zaidi za kijitabu hiki niliandika katika blogu hii. Tangu nilipoandika taarifa hiyo, kuna kitu cha ziada ambacho nimefanya. Nimechapisha kijitabu hiki kama kitabu pepe, yaani "ebook."

Thursday, July 4, 2013

Tumemaliza Kusoma "Half of a Yellow Sun"

Kwa wiki hizi sita, katika kipindi hiki cha "summer," nimekuwa nikifundisha kozi juu ya fasihi ya Afrika. Jana tumemaliza kusoma Half of a Yellow Sun, riwaya ya Chimamanda Ngozi Adichie wa Nigeria.  Huyu ni mwandishi chipukizi, lakini tayari ameshajipatia umaarufu sana na nyota yake inazidi kung'ara.

Amechapisha vitabu kadhaa akianzia na Purple Hibiscus na The Thing Around Your Neck. Ninavyo vitabu hivyo, na nimeshawahi kufundisha Purple Hibiscus.  Hivi karibuni, amechapisha Americanah, kitabu ambacho kinaongelewa sana miongoni mwa wasomaji, walimu, na wahakiki.

Kilipochapishwa kitabu cha Half of a Yellow Sun, nilisoma taarifa zake. Taarifa hizi zilielezea kuwa kitabu hiki kinahusu vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini Nigeria, ambapo sehemu ya kusini mashariki ilijitenga na kutangaza kuwa imekuwa taifa huru la Biafra.

Mwaka 2008 Chimamanda Ngozi Adichie alikuwa mmoja wa waandishi walioalikwa kuhudhuria tamasha la vitabu Minneapolis. Alikuja kuzindua kitabu cha Half of a Yellow Sun. Nilihudhuria, nikasikiliza hotuba yake, kisha nikajumuika na umati wa watu waliokuwa wananunua nakala na kusainiwa na mwandishi. Nilipata pia fursa ya kupiga naye picha inayoonekana hapa kushoto.

Pamoja na kuwa nilinunua nakala ya Half of a Yellow Sun siku hiyo, sikupata fursa ya kukisoma. Lakini miaka yote hii nilikuwa na nia ya kufanya hivyo, na nimefanya hivyo katika kufundisha somo la fasihi ya Afrika.

Wote tumependezwa sana na Half of a Yellow Sun. Chimamanda Ngozi Adichie ana kipaji kikubwa sana cha kubuni na kusimulia hadithi. Yeyote anayesoma maandishi yake na anakijua ki-Ingereza vizuri, atakiri kuwa mwandishi huyu anaimudu vizuri sana lugha hiyo. Ni kweli kuwa kwa ujumla Half of a Yellow Sun inahusu vita ya Biafra, 1966-1970, lakini kwanza inaongelea maisha ya kila siku ya watu, hasa katika mazingira ya Chuo Kikuu cha Nsukka. Chimamanda alizaliwa na kukulia hapo, na katika maandishi yake hupenda kuongelea maisha ya wasomi na familia zao chuoni pale.

Hata katika mazingira ya vita, Half of a Yellow Sun inatuonyesha watu wakijitahidi kuendelea na shughuli zao za kawaida, kama vile kuelimisha watoto, hata kama ni chini ya mti. Tunawaona watu wakitafuta riziki za maisha. Na tunawaona watoto wakicheza michezo, pamoja na dhiki kubwa ya magonjwa na njaa. Pamoja na ukatili mkubwa uliojitokeza katika vita ya Biafra, Chimamanda Ngozi Adichie amejiepusha na kishawishi cha kuangalia suala zima kama suala la aina mbili tu ya watu, yaani wabaya na wema. Anaonyesha jinsi binadamu tulivyo na uwezo wa kuwa wabaya, sawa na wale ambao tunawaona ndio wabaya.

Half of a Yellow Sun imefuata vizuri mtiririko wa matukio yaliyotangulia vita na matukio ya vita yenyewe. Kwangu mimi kama m-Tanzania, nimeguswa na jinsi Chimamanda Ngozi Adichie alivyoelezea mchango wa Tanzania katika kuiunga mkono Biafra. Ameelezea furaha ya watu wa Biafra na heshima waliyokuwa nayo kwa Tanzania na Mwalimu Nyerere. Wakati nasoma kitabu hiki na suala hili la Tanzania, nilikumbuka kitabu kipya cha Chinua Achebe kiitwacho There Was a Country. Humo Achebe ameelezea vizuri sana jinsi msimamo wa Tanzania ulivyoshangiliwa na watu wa Biafra. Jina la Tanzania lilikuwa linatajwa kila mahali. Miziki ya Tanzania ilipigwa kila mahali. Katika Half of a Yellow Sun, kuna baa ambayo ilibadilishwa jina ikaitwa Tanzania Bar.

Kwa wasiofahamu napenda kusema kuwa sehemu iliyoitwa Biafra ni sehemu wanayoishi zaidi watu wa kabila la Igbo. Kutokana na siasa za Nigeria, ambamo ukabila una nafasi kubwa sana, dhuluma dhidi ya waIgbo, ikiwemo wengi kuuawa, hasa sehemu za kaskazini mwa Nigeria, ndio kitu kilichosababisha wakakimbilia kwao na kujitangaza kuwa ni taifa huru la Biafra. Chinua Achebe, ambaye alifariki hivi karibuni, na Chimamanda Ngozi Adichie ni wa kabila hilo.

Kwa kumalizia, bora niseme tu kwamba kuliko kusimuliwa, ni bora mtu ujipatie nakala ujisomee. Nasema hivyo nikijua fika kwamba ushauri huu hauna maana kwa jamii ya wa-Tanzania, kwani utamaduni wa kununua vitabu na kuvisoma haupo. Kuna uwezekano mkubwa kwamba ushauri wangu utazingatiwa na watu wa nchi zingine kama vile Kenya, ambayo ni makini kwa masuala ya aina hiyo.

Friday, March 22, 2013

Buriani, Chinua Achebe

Msiba mzito umetufika leo, wasomaji wa fasihi na walimwengu kwa ujumla. Chinua Achebe amefariki, akiwa na umri wa miaka 82.

Maarufu kama muasisi wa fasihi ya ki-Ingereza katika Afrika, Chinua Achebe ametoa mchango mkubwa katika uandishi, mchango ambao uliiweka Afrika mahala pazuri katika ramani ya fasihi ya dunia.

Tangu alipochapisha riwaya yake maarufu, Things Fall Apart, hadi kufariki kwake, Achebe ameandika riwaya, hadithi fupi, na insha kuhusu fasihi, uandishi, siasa na utamaduni. Amefanya mahojiano mengi, ambayo, kwa bahati nzuri yanapatikana mtandaoni au katika vitabu na majarida.

Achebe aliamini kwa dhati kuwa jukumu la msanii ni kuwa mwalimu wa jamii. Yeye mwenyewe amezingati wajibu huo tangu ujana wake, alipochapisha Things Fall Apart, hadi kurariki kwake. Amewafundisha waAfrika mengi kuhusu jamii yao, udhaifu na uwezo wao, na amewafundisha walimwengu kuwaona wa-Afrika kwa mtazamo tofauti na ule wa wakoloni. Amewafundisha walimwengu maana ya ubinadamu, ambayo inavuka mipaka ya kabila, taifa, dini, jinsia au nchi.

Sikupata fursa ya kukutana uso kwa uso na Chinua Achebe, bali nimesoma na kufundisha maandishi yake mara kwa mara. Nashukuru pia kuwa nilipata wazo la kuandika mwongozo wa Things Fall Apart. Kwa namna hiyo ya kusoma na kutafakari maandishi yake, najiona kama vile nami nimekutana na mwandishi huyu. Nimalizie tu kwa kusema kwamba kwa mchango wake mkubwa kwa walimwengu, Achebe atakumbukwa daima.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...