Showing posts with label Chinua Achebe. Show all posts
Showing posts with label Chinua Achebe. Show all posts

Monday, November 13, 2017

Mwongozo wa Riwaya ya "Things Fall Apart"

Mimi mwalimu wa fasihi ya ki-Ingereza. Kati ya mambo ninayofanya ni kuandika miongozo ya fasihi. Nimeshaandika miongozo kadhaa, ikiwemo mwongozo wa Things Fall Apart, riwaya ya Chinua Achebe.

Nimeridhika kuwa mwongozo huu una mawazo muhimu ya kumwezesha mwalimu, mwanafunzi, na msomaji yeyote kuelewa mambo mapya juu ya Things Fall Apart na pia juu ya nadharia ya fasihi. Leo nimezipitia kurasa kadhaa, nikafurahia niliyoandika juu ya mhusika aitwaye Unoka.

Suali ni je, mwongozo huu unawafikia wanafunzi wa waalimu wa Tanzania? Ni wazi kuwa ningependa wafaidike nao, kama wanavyofaidika wanafunzi na wengine nje ya Tanzania, kama vile hapa Marekani. Ningekuwa na uwezo, ningepeleka nakala katika shule na vyuo vyote.

Kwa bahati nzuri, kitabu kinapatikana mtandaoni kama kitabu pepe. Ninafahamu kuwa kuna watu Tanzania ambao wanaweza kuagiza vitabu vya aina hiyo. Ninaamini kuwa kadiri siku zinavyokwenda na tekinolojia kuenea, wengi zaidi watakuwa na uwezo huo. Kwa hivi, nina matumaini makubwa kwa siku za usoni.

Njia nyingine ni kusafirisha vitabu. Mimi mwenyewe, kila ninapokwenda Tanzania, huchukua vitabu na kuvigawa kwenye maktaba na vyuo. Kuna wa-Tanzania wengi huku nje, ambao nao huenda Tanzania. Kama kungekuwa na nia ya kuchangia elimu, ingekuwa rahisi wao pia kuchukua vitabu. Vitu vingine wanachukua, kwa nini washindwe kuchukua vitabu?

Tuesday, July 18, 2017

Mhadhiri wa Algeria Amekifurahia Kitabu

Mimi kama mwandishi, ninaguswa na maoni ya wasomaji. Leo nimepata ujumbe kutoka kwa mhadhiri wa chuo kikuu kimoja cha Algeria, Samir, ambaye tumewasiliana kwa miaka michache, na nilimpelekea nakala ya kijitabu changu, Notes on Achebe's Things Fall Apart.

Nanukuu sehemu ya ujumbe wake:

I hope this finds you safe. I am so pleased to let you know that your book on Achebe's TFA is very helpful!! It really helped me. It is a pleasure also to inform you that I am citing you in my phd thesis on Gender in Ngugi's fiction. Your name will also be cited in my Acknowledgements and Dedications. Thank you so much....We love you much.

Kwa wale wasiojua ki-Ingereza, napenda kuelezea anachosema mhadhiri huyu kwa ujumla. Anasema kuwa anategemea ujumbe wake utanifikia nikiwa salama. Amefurahi sana kunifahamisha kuwa kitabu changu kuhusu riwaya ya Achebe ya Things Fall Apart ni mchango mkubwa sana na kimemsaidia sana. Anafurahi kunifahamisha vile vile kuwa ananukuu kitabu changu katika tasnifu yake ya uzamifu kuhusu jinsia katika riwaya za Ngugi wa Thiong'o. Jina langu litatajwa katika orodha ya watu waliochangia tasnifu hii. Anahitimisha kwa kusema, "Asante sana....Tunakupenda sana."

Ujumbe wowote kutoka kwa wasomaji makini una manufaa kwangu kama mwandishi. Ninayachukulia maanani maoni yao, hasa nikijua kuwa wametumia hela zao kununua kitabu changu. Kuna wengine ambao ninakuwa nimewapa nakala ya bure. Hao wanaponiandikia maoni yao juu ya kitabu ninaona kama wamelipa fadhila. Maoni yao ni muhimu kwangu kuliko hela.

Kitabu hiki na vingine vinapatikana hapa

Wednesday, March 22, 2017

Kitabu kwa Wasafiri Watokao Nebraska

Leo nimeona taarifa kutoka sinodi ya Nebraska ya Kanisa la Kiluteri la Marekani, kuhusu maandalizi ya safari za kwenda Tanzania. Safari hizo zimefanyika tangu miaka iliyopita. Kuna sehemu iitwayo "Preparatory Reading," na kama miaka iliyopita, katika sehemu hiyo kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimependekezwa kwa wasafiri hao:

For those persons wanting to more deeply explore cultural differences between Africans and Americans, the book Africans and Americans: Embracing Cultural Differences by Joseph Mbele is recommended. The book is available at www.africonxion.com.

Kwangu kama mwandishi, hii ni habari njema, ingawa si mpya. Viongozi wa programu kama hiyo ya Nebraska wana uzoefu wa miaka mingi wa kwenda Tanzania. Wana uzoefu wa utamaduni wa Tanzania. Kuendelea kwao kukipendekeza kitabu changu ni ushahidi kuwa wameona kinawafaa wa-Marekani wanaowapeleka Tanzania.

Watu kutoka Nebraska wanaosairi kwenda Tanzania nimewahi kuwataja katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Ninajisikia kama vile, kwa njia ya kitabu changu, nina uhusiano wa kudumu nao.

Nimeandika nilivyoandika, ingawa ninafahamu kuwa kwa mujibu wa utamaduni wa leo wa Tanzania, tunaogopa kuambiwa tunaringa. Ninaamini kuwa ni sahihi mtu kujivunia kazi yake na mafanikio yake, kama wafanyavyo wanamuziki wetu, ambao aghalabu tunawasikia wakitamba wanapoandaa albamu au wimbo wa kutupagawisha. Tunapowasikia wakisema hivyo, tunafurahi na kusubiri kwa hamu.

Lakini ni ajabu kuwa tunaona si sahihi kwa mwanataaluma kujivunia kazi yake. Lakini ninaona tujikumbushe kauli iliyomo katika "Azimio la Arusha" kuwa katika nchi yetu, kazi iwe ni kitu cha kujivunia; na uvivu, ulevi, na uzembe viwe ni vitu vya kuvionea aibu. "Azimio la Arusha" linazungumzia kila kazi yenye manufaa kwa mtu na jamii.

Kama kichekesho, ninakumbushia methali iliyomo katika riwaya ya Things Fall Apart ya Chinua Achebe: "The lizard that jumped from the high iroko tree to the ground said he would praise himself if no one else did," ambayo inamaanisha kuwa ukifanikisha jambo, usichelee kujisifu mwenyewe. Labda huo ndio utamaduni tunaouhitaji.

Monday, June 8, 2015

Mhadhiri wa Algeria Amefurahi Kupata Kitabu

Jana, niliporejea kutoka kanisani, nilikuta ujumbe katika ukurasa wangu wa Facebook kutoka kwa Samir Zine Arab, mhadhiri wa "African Literature and Listening Skills" katika chuo kikuu cha Hassiba Ben Bouali Chlef, Algeria. Alikuwa anashukuru kupata nakala ya kijitabu changu, Notes on Achebe's Things Fall Apart ambayo nilimtumia siku kadhaa zilizopita.

Ujumbe wake, ulioambatana na picha inayoonyesha kitabu pamoja na bahasha niliyotumia, kama inavyoonekana hapa kushoto, ameusambaza kwa marafiki zake wa Facebook ambao mimi ni mmoja wao. Amenigusa kwa namna alivyoandika:

Dear friends, brothers and sisters! Today I'm the happiest man on earth! This morning I received a lovely book from a great professor Joseph Mbele! Thank you so much dear!!

Pamoja na ujumbe huu, Mwalimu Samir ameniandikia pia ujumbe binafsi ambao nao umenigusa sana. Kwake na kwangu imekuwa ni furaha. Ninavutiwa na watu wa aina ya huyu mwalimu, ambao wana duku duku ya kutafuta elimu. Aliposikia tu kuhusu kijitabu changu, alikitaka.

Ninafurahi kuwa wanafunzi Algeria watapata fursa ya kuyafamu na kuyatafakari mawazo niliyoandika katika kijitabu hiki, ambacho Mwalimu Samir alikitamani tangu nilipokitaja katika Facebook, tarehe 11 Mei. Taarifa zaidi za kijitabu hiki niliandika katika blogu hii. Tangu nilipoandika taarifa hiyo, kuna kitu cha ziada ambacho nimefanya. Nimechapisha kijitabu hiki kama kitabu pepe, yaani "ebook."

Thursday, July 4, 2013

Tumemaliza Kusoma "Half of a Yellow Sun"

Kwa wiki hizi sita, katika kipindi hiki cha "summer," nimekuwa nikifundisha kozi juu ya fasihi ya Afrika. Jana tumemaliza kusoma Half of a Yellow Sun, riwaya ya Chimamanda Ngozi Adichie wa Nigeria.  Huyu ni mwandishi chipukizi, lakini tayari ameshajipatia umaarufu sana na nyota yake inazidi kung'ara.

Amechapisha vitabu kadhaa akianzia na Purple Hibiscus na The Thing Around Your Neck. Ninavyo vitabu hivyo, na nimeshawahi kufundisha Purple Hibiscus.  Hivi karibuni, amechapisha Americanah, kitabu ambacho kinaongelewa sana miongoni mwa wasomaji, walimu, na wahakiki.

Kilipochapishwa kitabu cha Half of a Yellow Sun, nilisoma taarifa zake. Taarifa hizi zilielezea kuwa kitabu hiki kinahusu vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini Nigeria, ambapo sehemu ya kusini mashariki ilijitenga na kutangaza kuwa imekuwa taifa huru la Biafra.

Mwaka 2008 Chimamanda Ngozi Adichie alikuwa mmoja wa waandishi walioalikwa kuhudhuria tamasha la vitabu Minneapolis. Alikuja kuzindua kitabu cha Half of a Yellow Sun. Nilihudhuria, nikasikiliza hotuba yake, kisha nikajumuika na umati wa watu waliokuwa wananunua nakala na kusainiwa na mwandishi. Nilipata pia fursa ya kupiga naye picha inayoonekana hapa kushoto.

Pamoja na kuwa nilinunua nakala ya Half of a Yellow Sun siku hiyo, sikupata fursa ya kukisoma. Lakini miaka yote hii nilikuwa na nia ya kufanya hivyo, na nimefanya hivyo katika kufundisha somo la fasihi ya Afrika.

Wote tumependezwa sana na Half of a Yellow Sun. Chimamanda Ngozi Adichie ana kipaji kikubwa sana cha kubuni na kusimulia hadithi. Yeyote anayesoma maandishi yake na anakijua ki-Ingereza vizuri, atakiri kuwa mwandishi huyu anaimudu vizuri sana lugha hiyo. Ni kweli kuwa kwa ujumla Half of a Yellow Sun inahusu vita ya Biafra, 1966-1970, lakini kwanza inaongelea maisha ya kila siku ya watu, hasa katika mazingira ya Chuo Kikuu cha Nsukka. Chimamanda alizaliwa na kukulia hapo, na katika maandishi yake hupenda kuongelea maisha ya wasomi na familia zao chuoni pale.

Hata katika mazingira ya vita, Half of a Yellow Sun inatuonyesha watu wakijitahidi kuendelea na shughuli zao za kawaida, kama vile kuelimisha watoto, hata kama ni chini ya mti. Tunawaona watu wakitafuta riziki za maisha. Na tunawaona watoto wakicheza michezo, pamoja na dhiki kubwa ya magonjwa na njaa. Pamoja na ukatili mkubwa uliojitokeza katika vita ya Biafra, Chimamanda Ngozi Adichie amejiepusha na kishawishi cha kuangalia suala zima kama suala la aina mbili tu ya watu, yaani wabaya na wema. Anaonyesha jinsi binadamu tulivyo na uwezo wa kuwa wabaya, sawa na wale ambao tunawaona ndio wabaya.

Half of a Yellow Sun imefuata vizuri mtiririko wa matukio yaliyotangulia vita na matukio ya vita yenyewe. Kwangu mimi kama m-Tanzania, nimeguswa na jinsi Chimamanda Ngozi Adichie alivyoelezea mchango wa Tanzania katika kuiunga mkono Biafra. Ameelezea furaha ya watu wa Biafra na heshima waliyokuwa nayo kwa Tanzania na Mwalimu Nyerere. Wakati nasoma kitabu hiki na suala hili la Tanzania, nilikumbuka kitabu kipya cha Chinua Achebe kiitwacho There Was a Country. Humo Achebe ameelezea vizuri sana jinsi msimamo wa Tanzania ulivyoshangiliwa na watu wa Biafra. Jina la Tanzania lilikuwa linatajwa kila mahali. Miziki ya Tanzania ilipigwa kila mahali. Katika Half of a Yellow Sun, kuna baa ambayo ilibadilishwa jina ikaitwa Tanzania Bar.

Kwa wasiofahamu napenda kusema kuwa sehemu iliyoitwa Biafra ni sehemu wanayoishi zaidi watu wa kabila la Igbo. Kutokana na siasa za Nigeria, ambamo ukabila una nafasi kubwa sana, dhuluma dhidi ya waIgbo, ikiwemo wengi kuuawa, hasa sehemu za kaskazini mwa Nigeria, ndio kitu kilichosababisha wakakimbilia kwao na kujitangaza kuwa ni taifa huru la Biafra. Chinua Achebe, ambaye alifariki hivi karibuni, na Chimamanda Ngozi Adichie ni wa kabila hilo.

Kwa kumalizia, bora niseme tu kwamba kuliko kusimuliwa, ni bora mtu ujipatie nakala ujisomee. Nasema hivyo nikijua fika kwamba ushauri huu hauna maana kwa jamii ya wa-Tanzania, kwani utamaduni wa kununua vitabu na kuvisoma haupo. Kuna uwezekano mkubwa kwamba ushauri wangu utazingatiwa na watu wa nchi zingine kama vile Kenya, ambayo ni makini kwa masuala ya aina hiyo.

Friday, March 22, 2013

Buriani, Chinua Achebe

Msiba mzito umetufika leo, wasomaji wa fasihi na walimwengu kwa ujumla. Chinua Achebe amefariki, akiwa na umri wa miaka 82.

Maarufu kama muasisi wa fasihi ya ki-Ingereza katika Afrika, Chinua Achebe ametoa mchango mkubwa katika uandishi, mchango ambao uliiweka Afrika mahala pazuri katika ramani ya fasihi ya dunia.

Tangu alipochapisha riwaya yake maarufu, Things Fall Apart, hadi kufariki kwake, Achebe ameandika riwaya, hadithi fupi, na insha kuhusu fasihi, uandishi, siasa na utamaduni. Amefanya mahojiano mengi, ambayo, kwa bahati nzuri yanapatikana mtandaoni au katika vitabu na majarida.

Achebe aliamini kwa dhati kuwa jukumu la msanii ni kuwa mwalimu wa jamii. Yeye mwenyewe amezingati wajibu huo tangu ujana wake, alipochapisha Things Fall Apart, hadi kurariki kwake. Amewafundisha waAfrika mengi kuhusu jamii yao, udhaifu na uwezo wao, na amewafundisha walimwengu kuwaona wa-Afrika kwa mtazamo tofauti na ule wa wakoloni. Amewafundisha walimwengu maana ya ubinadamu, ambayo inavuka mipaka ya kabila, taifa, dini, jinsia au nchi.

Sikupata fursa ya kukutana uso kwa uso na Chinua Achebe, bali nimesoma na kufundisha maandishi yake mara kwa mara. Nashukuru pia kuwa nilipata wazo la kuandika mwongozo wa Things Fall Apart. Kwa namna hiyo ya kusoma na kutafakari maandishi yake, najiona kama vile nami nimekutana na mwandishi huyu. Nimalizie tu kwa kusema kwamba kwa mchango wake mkubwa kwa walimwengu, Achebe atakumbukwa daima.

Sunday, January 2, 2011

Mwongozo wa "Things Fall Apart"

Nimefundisha riwaya ya Things Fall Apart ya Chinua Achebe tangu yapata mwaka 1976, sehemu kama Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Burundi, na vyuo vya Colorado na St. Olaf.

Kutokana na uzoefu huu, na mengi niliyojifunza, na kwa lengo la kuweka kimaandishi mawazo yangu juu ya riwaya hii, niliandika mwongozo. Nimeshaongelea kidogo kuhusu mwongozo huu katika blogu hii, lakini napenda kueleza zaidi habari zake.



Aliyenisukuma kuandika mwongozo huu kwa wakati niliofanya hivyo ni rafiki yangu A.S. Muwanga, aliyekuwa katika Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Yeye na mimi tulikubaliana kuwa niandike pia mwongozo kuhusu kitabu cha The African Child, kilichoandikwa na Camara Laye. Muwanga alifanya mpango na kitabu kilichapishwa mwaka 1988 na Nyanza Publications Agency kama inavyoonekana katika picha hapo juu. Lengo mahsusi lilikuwa ni hasa kuwasaidia wanafunzi wa sekondari waliokuwa wanasoma riwaya hizo.

Miaka hiyo, 1976 hadi 1991, nilikuwa mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mwaka huo 1991, niliondoka pale mwaka 1991, nikaja kufundisha Chuo cha St. Olaf, katika idara ya kiIngereza.

Mwaka 1997, bodi ya South Dakota Humanities Council iliyokuwa ikiratibu mradi wa usomaji katika jimbo la South Dakota iliniomba kuandika mwongozo kuhusu Things Fall Apart. Katika utaratibu wao, walikuwa wanachagua kitabu ili kisomwe na vikundi mbali mbali katika jimbo zima.

Ili kuchangia zoezi hili, walikuwa wana utaratibu wa kutafuta mtu wa kuandika mwongozo kuhusu kitabu husika, na mwongozo huu ulikuwa unatumiwa sambamba na kitabu husika. Kila kikundi kilikuwa kinajadili kitabu kweye mji wao, au eneo lao, na kisha walikuwa wanajumuika na wenzao wa sehemu zingine katika mjadala kwa njia ya barua pepe.

Mwaka huo 1997 kitabu kimojawapo walichokuwa wamekichagua ni Things Fall Apart. Ndio maana nikaombwa kuandika mwongozo. Nilitumia fursa hii kurekebisha ule mwongozo niliouchapisha Dar es Salaam. Kwa vile ilikuwa imepita miaka mingi nami nilikuwa nimetafakari zaidi riwaya ya Things Fall Apart niliweza kuweka marekebisho na kuuboresha mwongozo ule.

Kitabu kingine kilichokuwa kinajadiliwa ni Crimes of Conscience cha Nadine Gordimer, na aliyeombwa kuandika mwongozo ni profesa Karen A. Kildahl. Kazi yake na yangu zilichapishwa katika kijitabu kimoja, kama inavyoonekana katika picha hapo juu. Yeye na mimi tulialikwa kwenda kuendesha warsha kuhusu hivi vitabu viwili, katika mji wa Brookings, warsha ambayo ilihudhuriwa na watu kutoka sehemu mbali mbali za jimbo la South Dakota.

Mpango huu wa kuhamasisha usomaji katika jimbo zima ulinivutia sana, nikaona kuwa kama tungeweza kufanya jambo kama hili Tanzania, kuwafanya watu wajadili kitabu kimoja baada ya kingine, katika mkoa mzima au nchi nzima, tungefika mbali sana. Hatimaye, wahusika katika bodi hii ya South Dakota Humanities Council waliuweka mwongozo wangu wa Things Fall Apart mtandaoni, ukatumiwa na watu kutoka sehemu mbali mbali duniani.

Nilianza kuwazia umuhimu wa kuufikisha huu mwongozo Tanzania, ukiwa umeboreshwa zaidi. Niliurekebisha, nikauchapisha Chuo Kikuu Dar es Salaam, mwaka 2003, kwa gharama ya dola 520 za Marekani.

Wakati huo nilikuwa nimeanzisha kijikampuni, na kukisajili hapa Minnesota, kwa jina la Africonexion. Shughuli zake ni masuala ya elimu, kama vile kutoa ushauri, warsha, uandishi na uchapishaji. Nilivyochapisha mwongozo huu Dar e Salaam, nilitumia jina la Africonexion kama kampuni husika.

Hata hivi, lazima niseme ukweli. Pamoja na juhudi hizi zote, sikuona mwamko wa kuridhisha miongoni mwa wa-Tanzania, wa kutumia fursa niliyowaletea. Lakini, naridhika kwamba sina lawama. Kama vijana wa shule wa Rukwa, Pemba, Morogoro na Kondoa hawana kitabu kama hiki, kosa ni la wananchi na serikali. Mimi kama mwalimu nawajibika kusema kuwa serikali inapotosha ukweli inaposema haina hela, wakati kila mtu anaona jinsi inavyofuja hela, kwa magari ya fahari, na kadhalika. Tabia hiyo na wananchi wanayo pia, kama nilivyoeleza hapa.

Harakati za mwongozo huu ziliendelea. Mwaka 2005 nilikuwa nimechapisha kitabu mtandaoni, kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Baada ya kuvutiwa na uchapishaji wa aina hii, niliamua kuchapisha mwongozo wangu wa Things Fall Apart kwa njia hiyo hiyo. Niliufanyia marekebisho na kuuboresha, na hatimaye niliuchapisha, kama inavyoonekena katika picha kushoto.

Mwongozo wangu huu unawafaidia wengi. Nilifurahi, kwa mfano, nilipoona umechaguliwa na Chuo Kikuu cha Cornell kwa ajili ya wanafunzi wa mwaka wa kwanza waliokuwa wanatakiwa kusoma Things Fall Apart.

Huo ni utaratibu wao, kwamba wanafunzi wote wa mwaka wa kwanza wasome kitabu fulani, na vitabu hubadilika mwaka hadi mwaka. Kwa jinsi Chuo Kikuu cha Cornell kilivyo maarufu duniani, na kwa kuwa kuna vijitabu vingi na machapisho mengine kuhusu riwaya hii, kuchaguliwa mwongozo wangu ni heshima ya pekee. Soma hapa. Niliumiza kichwa kwa miaka mingi kuufikisha mwongozo huu kwenye kiwango hiki na nilijua ubora wake, kwani hilo ni somo langu, lakini inapendeza pia kuwasikia wataalam wengine wanaonaje.

Ninaendelea na shughuli ya kuandika miongozo kwa vitabu vingine. Kwa mfano, ninataka kurekebisha mwongozo wangu wa The African Child, ili niuchapishe kama kijitabu. Vile vile, kwa miaka kadhaa nimejishughulisha na uandishi wa mwongozo wa utungo maarufu wa Song of Lawino, uliandikwa na Okot p'Bitek. Nikijaliwa uzima, nitaandika sana siku za usoni. Kwani kazi na wajibu wa mwalimu ni nini?

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...