Showing posts with label Camara Laye. Show all posts
Showing posts with label Camara Laye. Show all posts

Thursday, June 9, 2016

Kitabu Andika Kwa Ajili Yako

Mara kwa mara ninapata ujumbe kutoka kwa watu wanaohitaji ushauri kuhusu uandishi wa vitabu. Baadhi wanakuwa wameshaandika miswada na wanatafuta ushauri kuhusu kuchapisha vitabu.

Wengine, baada ya kupata ushauri wangu ambao kwa kawaida unahusu uchapishaji wa mtandaoni, wanaulizia utaratibu wa malipo. Yaani wanataka kujua watalipwaje kutokana na mauzo ya vitabu vyao.

Ninakaribisha maulizo kuhusu masuala haya ya uandishi, uchapishaji, na uuzaji wa vitabu, kama ninavyothibitisha katika blogu hii. Hapa ninapenda kusema neno la jumla kwa watu hao, hasa wanaowazia mauzo na malipo: kitabu andika kwa ajili yako.

Nimeona kuwa watu wana kiherehere cha kuchapisha vitabu na kuviuza, wajipatie fedha. Wanaamini kuwa wakishachapisha kitabu, kuna utitiri wa watu watakaonunua, na wao waandishi watajipatia fedha, na labda fedha nyingi.

Kwa ujumla, hii ni ndoto. Kwanza, ni waandishi wachache sana duniani wanaopata fedha kutokana na vitabu vyao za kutosha hata kumudu gharama za kawaida za maisha. Pili, tutafakari hali halisi ya mwamko wa jamii katika suala la kununua na kusoma vitabu. Je, tuna utamaduni wa kununua na kusoma vitabu? Wewe mwenyewe unanunua na kusoma vitabu? Kama sivyo, una sababu gani au una haki gani ya kudhani kuwa wengine watanunua kitabu chako?

Pamoja na yote hayo, ni kweli kuwa kama unaandika vitabu vinavyoitwa vya udaku, au vya mambo ya kusisimua hisia, kama vile mapenzi, kuna uwezekano kuwa vitanunuliwa. Lakini hivi ni vitabu vya msimu, au vitabu vya chap chap, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii. Havina thamani ya kuvifanya vidumu kama vinavyodumu vitabu vya akina William Shakespeare, Charles Dickens, Leo Tolstoy, au Shaaban Robert. Waandishi wa vitabu vya msimu wanaweza kujipatia fedha kiasi.

Kuna aina nyingine ya waandishi ambao nao wanaweza kujipatia fedha. Hao ni waandishi wanaofuata jadi mbaya ambayo imekuwepo Tanzania, ya watu kuandika vitabu na kuvisukumia mashuleni. Mashule yamekuwa kama majalala ya kupokea vitabu kiholela. Wahusika wanatafuta fedha na wanafunzi wanaathirika, kwa kuwa vitabu hivi havikidhi viwango vya hali ya juu kabisa vya taaluma na uandishi sahihi.

Tukiachilia mbali aina hizi za uandishi, tutafakari uandishi wa vitabu vya kuelimisha jamii, ambavyo havisukumwi na mahitaji ya shule. Tutafakari vitabu ambavyo mwandishi makini mwenye ujuzi fulani anaandika ili kuelezea yale anayoyajua kwa umahiri wote awezao. Ni aina ya uandishi unaotokana na msukumo wa ndani ya nafsi ya mwandishi, kiasi kwamba hawezi kutulia bila kuhitimisha kazi ya kujikomboa kutokana na msukumo huo.

Uandishi huo huwa ni kwa manufaa ya mwandishi mwenyewe. Ninaamini kuwa huo ndio uandishi wa dhati. Ndio uandishi wa kweli. Kitabu cha namna hiyo kikishachapishwa, haijalishi kama kinanunuliwa na kusomwa na yeyote. Mwandishi unakuwa umetua mzigo. Umejikomboa, na uko tayari kuanza shughuli nyingine, kama vile kuandika kitabu kingine.

Binafsi, nina ajenda yangu ya vitabu ninavyotaka kuandika. Siangalii kama vitasomwa au kama vitatumika mashuleni. Kuna vitabu vya fasihi ambavyo nimevisoma, ambavyo ninaviandikia tahakiki, kwa kupenda mimi mwenyewe, wala si kwa kusukumwa na mahitaji ya wengine.

Kwa mfano, kwa miaka mingi nilikuwa ninatafakari utungo wa Okot p'Bitek, uitwao Song of Lawino, na kuandika mawazo yangu, hadi hivi karibuni nikachapisha mwongozo, Notes on Okot p'Bitek's Song of Lawino. Vile vile, nilishawahi kuandika katika blogu hii kuwa ninataka kuandika mwongozo kuhusu kitabu cha Camara Laye kiitwacho The African Child. Ninaridhika kabisa na mtazamo wangu kwamba kitabu andika kwa ajili yako mwenyewe, na dhana hii nimeigusia kabla katika blogu hii.


Sunday, January 2, 2011

Mwongozo wa "Things Fall Apart"

Nimefundisha riwaya ya Things Fall Apart ya Chinua Achebe tangu yapata mwaka 1976, sehemu kama Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Burundi, na vyuo vya Colorado na St. Olaf.

Kutokana na uzoefu huu, na mengi niliyojifunza, na kwa lengo la kuweka kimaandishi mawazo yangu juu ya riwaya hii, niliandika mwongozo. Nimeshaongelea kidogo kuhusu mwongozo huu katika blogu hii, lakini napenda kueleza zaidi habari zake.



Aliyenisukuma kuandika mwongozo huu kwa wakati niliofanya hivyo ni rafiki yangu A.S. Muwanga, aliyekuwa katika Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Yeye na mimi tulikubaliana kuwa niandike pia mwongozo kuhusu kitabu cha The African Child, kilichoandikwa na Camara Laye. Muwanga alifanya mpango na kitabu kilichapishwa mwaka 1988 na Nyanza Publications Agency kama inavyoonekana katika picha hapo juu. Lengo mahsusi lilikuwa ni hasa kuwasaidia wanafunzi wa sekondari waliokuwa wanasoma riwaya hizo.

Miaka hiyo, 1976 hadi 1991, nilikuwa mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mwaka huo 1991, niliondoka pale mwaka 1991, nikaja kufundisha Chuo cha St. Olaf, katika idara ya kiIngereza.

Mwaka 1997, bodi ya South Dakota Humanities Council iliyokuwa ikiratibu mradi wa usomaji katika jimbo la South Dakota iliniomba kuandika mwongozo kuhusu Things Fall Apart. Katika utaratibu wao, walikuwa wanachagua kitabu ili kisomwe na vikundi mbali mbali katika jimbo zima.

Ili kuchangia zoezi hili, walikuwa wana utaratibu wa kutafuta mtu wa kuandika mwongozo kuhusu kitabu husika, na mwongozo huu ulikuwa unatumiwa sambamba na kitabu husika. Kila kikundi kilikuwa kinajadili kitabu kweye mji wao, au eneo lao, na kisha walikuwa wanajumuika na wenzao wa sehemu zingine katika mjadala kwa njia ya barua pepe.

Mwaka huo 1997 kitabu kimojawapo walichokuwa wamekichagua ni Things Fall Apart. Ndio maana nikaombwa kuandika mwongozo. Nilitumia fursa hii kurekebisha ule mwongozo niliouchapisha Dar es Salaam. Kwa vile ilikuwa imepita miaka mingi nami nilikuwa nimetafakari zaidi riwaya ya Things Fall Apart niliweza kuweka marekebisho na kuuboresha mwongozo ule.

Kitabu kingine kilichokuwa kinajadiliwa ni Crimes of Conscience cha Nadine Gordimer, na aliyeombwa kuandika mwongozo ni profesa Karen A. Kildahl. Kazi yake na yangu zilichapishwa katika kijitabu kimoja, kama inavyoonekana katika picha hapo juu. Yeye na mimi tulialikwa kwenda kuendesha warsha kuhusu hivi vitabu viwili, katika mji wa Brookings, warsha ambayo ilihudhuriwa na watu kutoka sehemu mbali mbali za jimbo la South Dakota.

Mpango huu wa kuhamasisha usomaji katika jimbo zima ulinivutia sana, nikaona kuwa kama tungeweza kufanya jambo kama hili Tanzania, kuwafanya watu wajadili kitabu kimoja baada ya kingine, katika mkoa mzima au nchi nzima, tungefika mbali sana. Hatimaye, wahusika katika bodi hii ya South Dakota Humanities Council waliuweka mwongozo wangu wa Things Fall Apart mtandaoni, ukatumiwa na watu kutoka sehemu mbali mbali duniani.

Nilianza kuwazia umuhimu wa kuufikisha huu mwongozo Tanzania, ukiwa umeboreshwa zaidi. Niliurekebisha, nikauchapisha Chuo Kikuu Dar es Salaam, mwaka 2003, kwa gharama ya dola 520 za Marekani.

Wakati huo nilikuwa nimeanzisha kijikampuni, na kukisajili hapa Minnesota, kwa jina la Africonexion. Shughuli zake ni masuala ya elimu, kama vile kutoa ushauri, warsha, uandishi na uchapishaji. Nilivyochapisha mwongozo huu Dar e Salaam, nilitumia jina la Africonexion kama kampuni husika.

Hata hivi, lazima niseme ukweli. Pamoja na juhudi hizi zote, sikuona mwamko wa kuridhisha miongoni mwa wa-Tanzania, wa kutumia fursa niliyowaletea. Lakini, naridhika kwamba sina lawama. Kama vijana wa shule wa Rukwa, Pemba, Morogoro na Kondoa hawana kitabu kama hiki, kosa ni la wananchi na serikali. Mimi kama mwalimu nawajibika kusema kuwa serikali inapotosha ukweli inaposema haina hela, wakati kila mtu anaona jinsi inavyofuja hela, kwa magari ya fahari, na kadhalika. Tabia hiyo na wananchi wanayo pia, kama nilivyoeleza hapa.

Harakati za mwongozo huu ziliendelea. Mwaka 2005 nilikuwa nimechapisha kitabu mtandaoni, kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Baada ya kuvutiwa na uchapishaji wa aina hii, niliamua kuchapisha mwongozo wangu wa Things Fall Apart kwa njia hiyo hiyo. Niliufanyia marekebisho na kuuboresha, na hatimaye niliuchapisha, kama inavyoonekena katika picha kushoto.

Mwongozo wangu huu unawafaidia wengi. Nilifurahi, kwa mfano, nilipoona umechaguliwa na Chuo Kikuu cha Cornell kwa ajili ya wanafunzi wa mwaka wa kwanza waliokuwa wanatakiwa kusoma Things Fall Apart.

Huo ni utaratibu wao, kwamba wanafunzi wote wa mwaka wa kwanza wasome kitabu fulani, na vitabu hubadilika mwaka hadi mwaka. Kwa jinsi Chuo Kikuu cha Cornell kilivyo maarufu duniani, na kwa kuwa kuna vijitabu vingi na machapisho mengine kuhusu riwaya hii, kuchaguliwa mwongozo wangu ni heshima ya pekee. Soma hapa. Niliumiza kichwa kwa miaka mingi kuufikisha mwongozo huu kwenye kiwango hiki na nilijua ubora wake, kwani hilo ni somo langu, lakini inapendeza pia kuwasikia wataalam wengine wanaonaje.

Ninaendelea na shughuli ya kuandika miongozo kwa vitabu vingine. Kwa mfano, ninataka kurekebisha mwongozo wangu wa The African Child, ili niuchapishe kama kijitabu. Vile vile, kwa miaka kadhaa nimejishughulisha na uandishi wa mwongozo wa utungo maarufu wa Song of Lawino, uliandikwa na Okot p'Bitek. Nikijaliwa uzima, nitaandika sana siku za usoni. Kwani kazi na wajibu wa mwalimu ni nini?

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...