Showing posts with label maktaba. Show all posts
Showing posts with label maktaba. Show all posts

Monday, January 6, 2020

Kitabu Kimeingia Kwenye Maktaba ya Peace Corps

Kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kimeingia kwenye maktaba ya Peace Corps iliyoko Washington DC. Mkurugenzi ameniandikia, na sehemu ya ujumbe ni hii:

We will add it to the Peace Corps library where our staff and visitors can enjoy it.

I look forward to reading more of it as I find the topic to be very relevant and important to our work. I have already begun reading it, and it has reminded me of my own experiences in Togo, West Africa. As I was reading, I was struck by the section on eye contact. I really love the verses you included from the poem by Sufi poet Ibn ‘Arabi about the veiled woman and eye contact, and I got a good chuckle at your stories of misunderstandings—as I, as well surely all of us, have had many such experiences and misunderstandings.

Kauli za mkurugenzi za kukumbuka aliyoona Afrika na kufananisha na yaliyomo kitabuni, zinafanana na kauli za waMarekani wengine waliosoma kitabu hiki baada ya kuishi Afrika. Afrika kwenyewe, kwa sasa, kitabu kinapatikana Tanzania na Kenya. Tanzania kinapatikana kutoka duka la Soma Book Cafe, lililoko Dar es Salaam, na pia duka liitwalo A Novel Idea, lililoko Dar es Salaam na Arusha. Kenya kinapatikana katika duka la Bookstop katika Yaya Center Mall, Nairobi.

Saturday, March 4, 2017

Vitabu Nilivyonunua Leo

Leo nilikwenda Minneapolis, na wakati wa kurudi nilipitia Apple Valley nikaingia katika duka la Half Price Books. Kama kawaida, nilitaka kuona vitabu mbali mbali, lakini nilikuwa hasa na dukuduku ya kuona kama kuna vitabu juu ya Ernest Hemingway.

Kwa hivyo, nilivyoingia tu dukani, nilienda moja kwa moja kwenye sehemu vinapowekwa vitabu vya Hemingway, yaani vilivyoandikwa naye au juu yake. Tofauti na siku zingine, leo nilikuta vitabu vichache, na vyote ni vile alivyoandika Hemingway mwenyewe. Nilikiona kitabu ambacho sikumbuki kama nimewahi kukiona kabla, The Fifth Column and Four Stories of the Spanish Civil War, nikakiangalia.

Niliona kuwa "The Fifth Column" ni tamthilia, ambayo sina katika maktaba yangu. Papo hapo nilihisi kuwa hadithi zilizomo katika kitabu ziko katika kitabu cha The Complete Short Stories of Ernest Hemingway, ambacho ninacho. Nimethibitisha hivyo baada ya kuja nyumbani.

Nilipotoka sehemu vinapowekwa vitabu vya Hemingway, nilienda sehemu ambapo sikosi kuangalia, kwani hapo vinawekwa vitabu ambavyo vinauzwa kwa bei ndogo sana. Kama kawaida, niliviangalia vitabu vingi, nikaamua kuchukua kitabu cha Gulliver's Travels cha Jonathan Swift.

Hii nakala ya Gulliver's Travels niliyonunua ni toleo la andiko halisi la Swift, si toleo lililorahisishwa. Jambo hilo lilinivutia. Jambo jingine ni kuwa kuna utangulizi ulioandikwa na Jacques Barzun, mwandishi ambaye maandishi yake nimeyafahamu tangu miaka ya themanini na kitu nilipokuwa ninasoma katika Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison. Katika nakala hii, kuna pia michoro aliyochora Warren Chappell.

Saturday, December 5, 2015

Kuwalea Watoto Kupenda Vitabu

Kati ya mambo yanayonivutia sana hapa Marekani ni namna wazazi wanavyowalea watoto katika utamaduni wa kupenda kusoma vitabu. Katika matamasha ya vitabu, maduka ya vitabu, na maktaba, ninawaona wazazi wakiwa na watoto. Nimewahi kuandika kuhusu suala hilo katika blogu hii. Lakini kwa kuwa hii ni mada ninayoitilia maanani sana, nimeamua kuiongelea tena.

Picha ya juu hapa kushoto ilipigwa mwaka 2008, niliposhiriki sherehe za kumbukumbu ya uhuru wa Nigeria hapa Minnesota. Nilikuwa na meza ya vitabu vyangu. Nakumbuka vizuri jinsi huyu mama m-Nigeria anayeonekana pichani alivyokuja mezani pangu na binti yake. Tulisalimiana, wakaangalia na kuvifurahia vitabu vyangu, kama inavyoonekana pichani.

Picha ya pili hapa kushoto nilipiga katika tamasha la vitabu la Deep Valley, mjini Mankato, Minnesota. Nilivutiwa na namna hao watoto walivyokuwa wanafuatana na mama yao kutoka meza hadi meza wakiangalia vitabu.

Picha ya tatu hapa kushoto nilipiga mwezi Agosti mwaka huu mjini Brooklyn Park, Minnesota, katika tamasha la Afrifest. Huyu bwana, m-Marekani Mweusi, alikuja na watoto wake kwenye meza yangu, kuangalia vitabu. Watoto hao ni wadogo sana, na sijui kama walikuwa wanajua kusoma, lakini, nilivutiwa na kitendo cha baba yao kuwaleta kuangalia vitabu.

Kwa wa-Marekani, umri wa mtoto si tatizo. Wanawasomea vitabu hata watoto wadogo sana, hasa kabla ya kulala. Watoto wanapenda kusomewa vitabu. Hapa naikumbuka video ya kusisimua inayomwonyesha mtoto mdogo akisomewa vitabu, halafu anavyoangua kilio kila anapoambiwa kuwa hadithi imeisha. Hebu iangalie.


Friday, October 9, 2015

Nimepata Toleo Jipya la "Green Hills of Africa"

Leo ni siku ya furaha kwangu. Nimepata nakala ya toleo jipya la Green Hills of Africa, kitabu cha Ernest Hemingway, kilichochapishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1935. Taarifa kwamba toleo hili lilikuwa linaandaliwa nilielezwa na Mzee Patrick Hemingway, kama nilivyoandika katika blogu hii. Kwa hivi, nilipogundua kwamba limechapishwa, niliagiza nakala hima.

Katika Green Hills of Africa, Hemingway anaelezea mizunguko yake katika nchi ya Tanganyika, mwaka 1933-34, akiwa na mke wake wa pili Pauline Pfeiffer. Anaelezea uzuri wa nchi, watu wa makabila, tamaduni, na dini mbali mbali, na wanyama katika mbuga alimowinda, kama vile Serengeti na eneo la Ziwa Manyara. Anaelezea miji alimopita, kama vile Mto wa Mbu, Babati, Kondoa, Handeni, na Tanga.

Toleo hili la Green Hills of Africa lina mambo ambayo hayakuwemo katika toleo la mwanzo, kama vile maandishi ya awali ambayo hayakutokea kitabuni, picha, na hata "diary" aliyoandika Pauline alipokuwa safarini na mumewe. Nilijua kuwa "diary" hii imehifadhiwa katika maktaba ya Chuo Kikuu cha Stanford, na nilikuwa nawazia kwenda kuisoma. Kuchapishwa kwake katika toleo hili ni jambo la kufurahisha sana.

Kutokana na jinsi Hemingway alivyoielezea nchi yetu, tukio la kuchapishwa kwa toleo hili la Green Hills of Africa mwaka huu ilipaswa tulipokee kwa shamra shamra. Pangekuwa na shughuli za uzinduzi wa toleo hili, makongamano, na tahakiki magazetini. Nakala zingejaa katika maduka ya vitabu, na wateja wangekuwa wanapigana vikumbo kuzinunua.

Sehemu zingine duniani wanatumia vilivyo bahati ya kutembelewa na Hemingway na kuandikwa katika maandishi yake. Ni kivutio kikubwa kwa watalii, kama ninavyosema katika blogu hii. Sisi tumeifanya nchi yetu kuwa kwenye miti ambako hakuna wajenzi.

Sunday, June 21, 2015

Niliyoyaona Maktabani Brookdale, Minnesota

Jana, kama nilivyoandika katika blogu hii, nilihudhuria mkutano Brooklyn Park, ambao tulifanyia katika maktaba ya Brookdale. Hapa kushoto ni picha ya upande wa Mbele wa maktaba hii, inavyoonekana kabla hujaingia ndani. Jana ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kufika hapa, na niliona jinsi jengo lilivyo tofauti na majengo ya maktaba zingine ambazo nimeingia hapa Minnesota.



Nilivyoingia ndani, nilijikuta sehemu hii inayoonekana kushoto, ingawa ni kubwa na pana zaidi ya hii inayoonekana pichani. Wakutubi wengi wapo katika eneo hilo, tayari kuwasiaida wateja, na sehemu ya maulizo ambayo ni kubwa pia, iko eneo hili. Unapokuwa sehemu hii, kwa mbele yako na pembeni kuna maeneo yenye vitabu, majarida, kompyuta nyingi na hifadhi mbali mbali za taarifa, kama vile CD, DVD na na kaseti.

Niliulizia kilipo chumba cha mkutano, nikapita katikati ya makabati ya vitabu vya kila aina hadi mwishoni kabisa.




Baada ya mkutano, nilirejea tena sehemu hii na kuchungulia katika makabati mbali mbali, hasa ya fasihi. Kuna utajiri mkubwa wa vitabu, vya masomo na taaluma mbali mbali, vya watoto na watu wazima, na vitu vingine vingi. Inapendeza kuona wenzetu wanavyowekeza katika vitu vya namna hii, kuelimisha jamii.

Hiyo jana ilikuwa ni Jumamosi, na ilikuwa ni alasiri. Jua lilikuwa linawaka vizuri, na walikuwepo watu wengi katika maktaba, watu wa kila rangi, na kila rika. Wwnginw walikuwa wanasoma vitabu, wengine wanaazima, wengine wanatumia kompyuta, na wengine walikuwa wanarudufu maandishi.

Nilivyoangalia hali hii, ya watu wengi kuwemo maktabani wakati wa alasiri, Jumamosi, niliwazia hali ya Tanzania. Nilijiuliza ni wapi katika Tanzania unaweza kuona hali hii, tena Jumamosi mchana. Ni wapi unaweza kuwaona watu wa rika mbali mbali wamejaa maktabani wanajisomea. Hata huyu dada Latonya  niliyekutana naye jana hapo nje ya maktaba alikuwa anakuja maktabani na akina dada wenzake.

Ningekuwa na uwezo, ningebadili mioyo ya wa-Tanzania, wawe kama hao wa-Marekani, wenye kupenda kusoma. Ningehamasisha ujenzi wa maktaba zaidi. Kwa mji kama Dar es Salaam, ningependa ziwepo maktaba Sinza, Kinondoni, Buguruni, Kigamboni, Kawe, Kimara, Ukonga na sehemu zingine. Ingekuwa ni Marekani, mji wa ukubwa wa Dar es Salaam ungekuwa na maktaba nyingi. Lakini, miaka hamsini na zaidi tangu tupate uhuru, maktaba ni hiyo hiyo moja. Si jambo la kujivunia.

Saturday, June 20, 2015

Msomaji Amenilalamikia

Leo alasiri nilikwenda Brooklyn Park, Minnesota, kuhudhuria mkutano wa bodi ya Afrifest Foundation ambayo mimi ni mwenyekiti wake. Tulifanyia mkutano wetu katika maktaba ya Brookdale.

Baada ya mkutano, nilipotoka nje kuelekea sehemu nilipopaki gari, alinikimbilia dada Latonya anayeonekana katika picha hapa kushoto, ambayo tulipiga miaka mitano iliyopita kwenye tamasha la Afrifest. Ni m-Marekani Mweusi kutoka Chicago, ila anaishi Minneapolis. Tulifahamiana miaka ile kwa kuwa naye alikuwa katika bodi ya Afrifest Foundation.

Hatukutegemea kama tungeonana leo, ghafla namna ile. Kwa hivi tulifurahi sana. Lakini hakupoteza muda, alianza kunihoji kwa nini siandiki sana katika blogu yangu ya ki-Ingereza kama zamani. Alisema, akimaanisha maandishi yangu ya kiSwahili, "Tunaona unaandika sana, na tunajua unaandika mambo ya maana, ila hatujui unachoandika. Inakuwa kama unatusahau marafiki zako wa-Marekani Weusi."

Kwa kweli, ingawa mazungumzo yalikuwa ya kirafiki, na hata kiutani, niliona kuwa alikuwa anaongea kwa dhati. Na sisi wa-Afrika ambao tunaishi Marekani tunafahamu kuwa wako wa-Marekani Weusi wengi ambao wanategemea sisi wa-Afrika tuwe na mshikamano nao, kama ndugu. Kwa hivi, sikuyachukulia malalamiko ya Latonya kama mzaha. Nilijikuta nikikiri kosa na kuahidi kuwa nitakuwa naandika kama zamani. Alivyowataja wa-Marekani Weusi hakuwa anatunga hadithi. Ninafahamu kuwa wanasoma maandishi yangu.

Latonya mwenyewe ni mmoja wa wafuatiliaji wa dhati wa maandishi yangu. Hapo pichani, anaonekana ameshika kitabu changu cha Africans and Americans:Embracing Cultural Differences, mara baada ya kukinunua. Maneno aliyoniambia leo yameniingia. Nilimwambia hivyo, nikaahidi kujirekebisha.

Monday, May 18, 2015

Kitabu cha Dr. John C. Sivalon, M.M.

Leo nimejipatia kitabu cha Dr. John C. Sivalon, M.M. Kanisa Katoliki na Siasa ya Tanzania Bara 1953 Hadi 1985. kilichochapishwa na shirika la Kanisa Katoliki la wa-Benediktini, Ndanda. Kutokana na kutopatikana madukani hapa Marekani, nimekipata kupitia maktaba ya hapa Chuoni St. Olaf, kwa utaratibu wa uazimishanaji wa vitabu baina ya maktaba. Nimejitengenezea nakala kwa matumizi yangu, kama inavyoruhusiwa kisheria.

Hiki ni kitabu kinachojulikana Tanzania kwa kuwa kinatajwatajwa sana na viongozi wa wa-Islam wanaosema kwamba wa-Islam wamekuwa wakihujumiwa na bado wanahujumiwa na serikali ya Tanzania kwa manufaa ya kanisa na wa-Kristu.

Kutokana na madai hayo, kwa miaka yote hii nimekuwa na hamu ya kujisomea kitabu hiki. Sikuwahi kusema lolote juu yake, kwa vile sikuwa nimekisoma. Baada ya kukipata, kama saa mbili tu zilizopita, nimekipitia chote, ila bado sijakisoma kwa makini.

Hata hivi, nimeona kuwa mwandishi ameandika kitabu hiki kwa busara bila ushabiki, nikakumbuka kitabu cha Hamza Njozi, Mauaji ya Mwembechai, ambacho nacho amekiandika kwa busara bila ushabiki. Nimeangalia mtandaoni nikaona kuwa Dr. Sivalon ameandika pia kitabu kingine, God's Mission and Postmodern Culture: The Gift of Uncertainty. Hiki itakuwa rahisi kukinunua hapa Marekani.

Napenda kusema kila mmoja wetu ajisomee mwenyewe kitabu hiki cha Dr. Sivalon cha Kanisa Katoliki na Siasa ya Tanzania Bara 1953 Hadi 1985, ayatafakari yaliyomo. Kwa kuzingatia kuwa bado sijakisoma kwa umakini, napenda kutoa fursa kwa yeyote ambaye amekisoma aweze kutuletea maoni yake. Nami, baada ya kukisoma ipasavyo, nitatoa maoni yangu.

Saturday, April 4, 2015

Nimerejea Salama Kutoka Leech Lake Tribal College

Nilirejea jana jioni kutoka Leech Lake Tribal College, kwenye mkutano kuhusu "Narratives of Identity." Nilikuwa mmoja wa wanajopo wanne waliotoa mada, na mada yangu ilikuwa "Being African in America."

Niliongelea uzoefu wangu katika miaka mingi ya kuishi na kufundisha hapa Marekani, nikielezea kazi kubwa isiyoisha ya kujitambulisha kama mu-Afrika, ambaye ni tofauti na mu-Amerika Mweusi. Nilielezea jinsi suala hilo linavyosabisha mikanganyiko na kutoelewana baina ya wa-Marekani Weusi na wa-Afrika tuishio Marekani.

Nilisema wazi kuwa namna wanavyojiita na kujitambulisha wa-Marekani Weusi ni tofauti na namna tunavyojiita na kujitambulisha sisi wa-Afrika. Nilimnukuu Chimamanda Ngozi Adichie wa Nigeria ambaye katika mahojiano na katika riwaya yake maarufu ya Americanah, ameelezea vizuri suala hilo.

Nilimnukuu pia mwandishi Jamaica Kincaid wa Antigua, pande za Caribbean, ambaye pamoja na kuwa ni mweusi pia, hakuwahi kujiita kama wanavyojiita  wa-Marekani Weusi. Hayo mawazo yake niliyasoma katika mahojiano yaliyochapishwa mwaka 1991 katika jarida la Mississippi Review.

Nilisisitiza umuhimu wa kuheshimu haki ya kila jamii kujiita au kujitambulisha kwa majina wanayoyataka au yanayowaridhisha wenyewe. Watu wengine sherti wafuate njia hiyo badala ya kuwapachika watu majina ya utambulisho kama walivyofanya wakoloni.

Nilienda mbali zaidi na kuelezea suala la haki ya kila jamii kujieleza wenyewe, sio kuzimishwa kama walivyotuzimisha wakoloni, na wao wakawa wanaandika juu yetu.

Siwezi kuelezea hapa yote niliyosema. Nawazia kuendelea kutafakari suala hilo na kujisomea zaidi, na kuwasoma upya watu kama Frantz Fanon, Aime Cesaire, na Ngugi wa Thiong'o, ili hatimaye niandike makala kamili.

Hiyo jana, wakati nilipokuwa najitambulisha mkutanoni, nilisema kuwa nimeleta vitabu vyangu viwili kama zawadi kwa maktaba ya chuo cha Leech Lake Tribal College. Vitabu hivyo ni Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales. Vitabu hivi vilipokelewa kwa furaha na shukrani tele.

Nina hakika kuwa mkutano ule umesisimua watu. Jana hiyo hiyo, katika ukurasa wa Facebook wa Leech Lake Tribal College iliandikwa taarifa hii:

We had some great speakers on campus today for the Narratives of Identity presentations. One of the many memorable remarks from today's visit was by Joseph Mbele, St Olaf College- “I am not a person of color. I am Tanzanian which is a concept of colonization. Only when I came to America was I referred to as black. Naming yourself, knowing yourself, is a right…Construction of identities are not fixed and it’s our right to identify ourselves.”

(Picha ya juu kabisa na ya katikati ni kutoka Leech Lake Tribal College)

Saturday, December 13, 2014

Zawadi ya Vitabu

Nimeona picha hii hapa kushoto katika Mjengwablog. Maggid Mjengwa (kulia) anaonekana akikabidhi vitabu kwa mzee wa kijiji cha Mahango, Madibira, kwa ajili ya maktaba ya kijiji.

Nimeguswa na taarifa hii, kwani vitabu ni sehemu muhimu ya maisha yangu. Hii sio tu kwa kuwa mimi ni mwandishi na mwalimu, bali pia kwa kuwa nathamini sana kitendo cha kupeleka vitabu popote vinapohitajika.

Kwa mtazamo wangu, kitabu cha maana kina thamani isiyopimika. Nikipata fursa ya kuchagua kati ya kitabu cha aina hiyo na kreti ya bia, nitachagua kitabu, kwa furaha kabisa.

Mimi mwenyewe hupeleka vitabu Tanzania. Nimeshapeleka kwenye maktaba mbali mbali, zikiwemo za Mbinga, vyuo vikuu vya Dar es Salaam, Makumira, na Tumaini,  na pia kwa watu binafsi. Kuna wakati niliwahamasisha wanadiaspora wanachama wa jumuia ya mtandaoni ya Tanzanet wakachangia dola 500 kuendeleza jukumu hilo. Mbali na hilo, kila ninapokwenda Tanzania, kwa kadiri ya uwezo wangu, nabeba vitabu kwa madhumuni hayo.

Siandiki makala hii kwa kuwa tu nimeona hii taarifa katika Mjengwablog. Wazo la vitabu kama zawadi nimekuwa nalo kwa muda mrefu. Niliwahi kuongelea jambo hili katika blogu hii. Mimi mwenyewe hufurahi nikipewa kitabu, kama nilivyoandika hapa, na hapa.

Kama ambavyo ninasema mara kwa mara katika blogu hii, ninapenda kununua vitabu. Sio kwamba nina pesa sana, bali ni kutokana na kuviona vitabu kuwa ni muhimu zaidi ya mambo mengi ambayo wengine wanayathamini zaidi. Kwa mfano, kama wewe ni mnywaji wa bia, ukiachana na bia, utagundua kuwa kumbe hela unazo. Ninasema hivyo kutokana na uzoefu wangu.

Nikirudi tena kwenye hii taarifa ya Mjengwablog, napenda kusema kuwa ni jambo jema sana kuanzisha na kuboresha maktaba vijijini. Ingetakiwa katika nchi yetu tuwe na mwamko wa namna hiyo. Kuna wageni ambao wanajitahidi kupeleka huduma ya vitabu vijijini. Mifano ni shirika la TETEA na Friends of African Village Libraries. Ingetakiwa sisi wenye nchi yetu tuwe mstari wa mbele katika kutimiza majukumu hayo, badala ya kuwaachia au kuwaangalia tu wageni wakifanya hivyo.

Kwa miaka mingi kidogo, nimewazia kuanzisha maktaba kijijini kwangu, lakini bado sijafanya hivyo. Kitu kimoja kinachonisukuma ni kuona jinsi wanakijiji wanavyotumia muda wao mwingi kwenye kilabu cha pombe. Papo hapo, kuna shule kadhaa jirani na kijiji, zikiwemo shule za sekondari, ambazo zingefaidika na kuwepo kwa maktaba kijijini. Wazo hili sio lazima alitekeleze mtu mmoja. Ni wajibu kwetu wote tunaotambua umuhimu wa vitabu.

Monday, March 11, 2013

Maktaba ya Karatu

Wadau wa blogu yangu hii watakuwa wanajua jinsi ninavyoleta taarifa za maktaba mbali mbali, hasa zile ninazopata fursa ya kuzitembelea. Mfano ni taarifa hii hapa.

Mwaka huu, tarehe 7 Januari, nilipata fursa ya kuiona maktaba ya Karatu. Nilikuwa njiani kuelekea kwenye uwanja wa mnada, lakini papo hapo nilitaka kuiona maktaba. Kuna kibao nilikiona wakati natembea, kikielekeza iliko maktaba.

Nilipofika hapo nilipiga tu hii picha, nikaendelea na safari yangu ya mnadani. Maktaba iko juu kwenye sehemu ya mwinuko ambao nadhani ndio juu kabisa pale Karatu. Sikuingia ndani. Nikifika tena Karatu, nitaweka kipaumbele kuingia humo na kuona ilivyo. 


Monday, December 17, 2012

Hongera JWTZ Kwa Kufungua Maktaba


Nimevutiwa sana na taarifa juzi kuwa Rais Kikwete, Amiri Jeshi wa Tanzania, amefungua maktaba ya kisasa kwenye chuo cha mafunzo cha Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) Monduli. Ni habari njema kabisa.

Mimi ni mdau mkubwa wa maktaba na katika blogu hii ninaziongelea mara kwa mara. Mifano ni maktaba za TangaDar es SalaamSongeaLushotoMoshiIringa, na Southdale.

Kwa miaka mingi sijawahi kusikia rais au kiongozi mwingine wa kitaifa Tanzania akifungua maktaba, ukiachilia mbali tarehe 9 Desemba, 1967, ambapo Mwalimu Nyerere alifungua Maktaba Kuu ya Taifa, Dar es Salaam.

Pita katika maktaba yoyote Tanzania, utaona kuwa maktaba ni kitu ambacho wa-Tanzania hawakithamini sana, isipokuwa labda wanafunzi. Na hao wanafunzi wanaonekana maktabani endapo wamebanwa sana na mwalimu au wanakabiliwa na mitihani.

Wakaazi wa Tanga, kwa mfano, wamekuwa na bahati ya kuwa na maktaba tangu mwaka 1958, kabla ya Uhuru. Ingebidi wawe juu kabisa kitaifa kwenye suala la elimu. Lakini wapi, ukiingia katika maktaba ile, hutawaona. Je, unadhani kuwa ukimwuliza mkaazi wa Arusha au Songea akuonyeshe maktaba iko wapi, ataweza kukuambia? Jaribu uone.

Tanzania tumezoea kusikia kuhusu ufunguzi wa baa, sio maktaba. Kama unafungua baa maarufu, unaweza kabisa kumleta waziri akawa mgeni rasmi. Kutokana na utamaduni huo, kitendo cha JWTZ cha kufungua maktaba ya kisasa ni cha pekee. Ni kitendo kinacholeta matumaini kuwa labda tutashtuka na kuelewa umuhimu wa maktaba. Natoa pongezi kwa JWTZ.

Tuesday, January 10, 2012

Nimeenda Maktaba ya Southdale, Edina.

Leo nilienda mjini Edina, kwenye maktaba ya Southdale. Nilikwenda kukutana na mama mmoja m-Marekani Mweusi, ambaye ninamsaidia kuchapisha kitabu chake kwa kutumia tekinolojia ya uchapishaji mtandaoni, kama ninavyochapisha vitabu vyangu.

Niliposogea kwenye jengo hilo, niliona magari mengi yamepaki. Ni kama inavyokuwa kwenye sherehe nchini Tanzania.

Niliona watu wakiingia na kutoka, wakiwemo wazee. Hii ni kawaida hapa Marekani. Hapo mlangoni, nilipishana na wazee wawili wakitoka, mwanamme na mwanamke, wazee sana, na huyu mwanamme alikuwa anatembelea mkongojo. Pamoja na uzee wote huu, wanaona umuhimu wa kwenda maktaba. Humo ndani, kama kawaida, kulikuwa na watu wengi wakisoma, kuazima au kurudisha vitabu, na wengine kwenye kompyuta na kwenye sehemu za kusikilizia vitabu, maana siku hizi vitabu vinapatikana vikiwa vimerekodiwa katika kanda.

Ukiangalia maelezo ya maktaba hii Southdale, utaona kuwa wanavyoitumia maktaba hii inaendana vizuri na yale aliyoyawazia na kuyatamka Mwalimu Nyerere wakati anafungua maktaba ya Taifa Dar es Salaam, kama nilivyoandika hapa.

Thursday, November 10, 2011

Maktaba Kuu ya Taifa, Dar es Salaam

Sijui ni wangapi kati ya mamilioni ya watu wanaoishi Dar es Salaam ambao wameingia katika Maktaba Kuu ya Taifa, au wana mazoea ya kuingia humo. Hapa siongelei wanafunzi, kwani hao wanaingia humo. Naongelea watu wasio wanafunzi.

Yawezekana wako ambao wana vijiwe vyao hapa nje ya maktaba, ambavyo wanahudhuria kila siku au kila wiki, lakini hawajawahi kukanyaga ndani ya maktaba hii.

Lakini, Mwalimu Nyerere alipofungua maktaba hii, tarehe 9 Desemba, 1967, alitoa ushauri wa maana, na baadhi ya maneno yake ni haya:

I am also forced to say that we shall probably not be able to go ahead as quickly as we would like, because even when a library service is run with the utmost economy, it still costs quite a lot of money. For a public library should not just be a place where books can be borrowed. It must also be a center for much wider adult education work of all kinds – ranging from the promotion of the desire for literacy by story telling and discussion, to the erudite lectures of visiting professors in our country. The libraries also have an important role to play in overcoming one of their own limitations; for a good librarian backed by a good library, can encourage people to write books as well as read them. Our traditional stories and histories can be written in Swahili so that the whole nation can read them; personal experiences, which are of wider interest, can be written as a story or a book; knowledge gained through practical development work can be written down so that it is shared. (…) (W)e can make our libraries into real cultural and community centers. It is up to us to provide them, to help them develop, and to use them to the full.

(Source: The Mwalimu Nyerere Foundation)

Hebu nijaribu kuyatafsiri kwa ki-Swahili:

Vile vile nalazimika kusema kuwa huenda hatutafanikiwa kusonga mbele kwa kasi ambayo tungependa, kwa sababu hata pale maktaba inapoendeshwa kwa umakini kabisa kimatumizi, bado inagharimu hela nyingi sana. Kwani maktaba ya umma isiwe tu mahali pa kuazimia vitabu. Sherti pawe pia mahali pa kutekelezea suala zima la elimu ya watu wazima kwa mapana yake--kuanzia kuhimiza kusoma na kuandika kupitia usimuliaji wa hadithi na uchambuzi wake, hadi mihadhara ya kisomi ya wahadhiri na maprofesa nchini mwetu. Maktaba pia zina wajibu muhimu wa kuchangia katika kurekebisha mapungufu yanayozikabili; kwani mkutubi bora awapo na maktaba bora, anaweza kuwahimiza watu kuandika vitabu sambamba na kuvisoma. Hadithi zetu za jadi na historia zinaweza kuandikwa kwa ki-Swahili ili Taifa zima liweze kuzisoma; taarifa za uzoefu wa watu binafsi, ambazo ni muhimu kwa jamii, zinaweza kuandikwa kama simulizi au kitabu; ujuzi upatikanao katika shughuli za maendeleo unaweza kuandikwa ili na wengine waupate. (...) (Tu)naweza kuzifanya maktaba zetu sehemu halisi za kuendeshea shughuli za kitamaduni na kijamii. Ni juu yetu kuzifanya ziwepo, kuchangia ustawi wake, na kuzitumia kikamilifu kabisa.

Saturday, November 5, 2011

Maktaba ya Mkoa, Tanga

Maktaba ya mkoa, mjini Tanga, ilifunguliwa mwaka 1958. Wa-Ingereza, ambao walikuwa wanatawala Tanganyika, ndio waliojenga maktaba hii. Ni jengo zuri sana, kama inavyoonekana hapa kushoto.








Nimetembelea maktaba hii mara kadhaa. Ni mazoea yangu kutembelea maktaba, kama nilivyoeleza hapa na hapa. Tangu nilipofika hapo maktaba ya Tanga mara ya kwanza, miaka kadhaa iliyopita, nilipata fursa ya kufahamiana na mkurugenzi, ambaye anaonekana nami katika picha hapa kushoto. Nimepata fursa ya kuingia ndani na kuangalia vitabu na machapisho mengine, nikachangia nakala za vitabu vyangu.



Maktaba hii ilikuwa nzuri sana tangu ilipofunguliwa. Lakini leo, hali si nzuri, kama ilivyoelezwa hapa. Maktaba inahitaji ukarabati, vitabu vipya, majarida na kadhalika. Kwa nchi tajiri kama Tanzania, ambayo ina rasilimali kuliko nchi nyingi, haieleweki kwa nini isiwezekane kukarabati maktaba kama hii. Jawabu linaeleweka: ni ujinga, ufisadi na ukosefu wa uongozi kitaifa.





Uongozi wa maktaba unajitahidi sana kufanya kazi vizuri, ingawa mazingira ni magumu. Wanajitahidi kukidha mahitaji kufuatana na mabadiliko ya wakati. Kwa mfano, mara ya mwisho nilipoingia katika maktaba hii, nilionyeshwa sehemu ambayo imewekwa maalum kwa mahitaji ya wanafunzi wa chuo kikuu huria. Wanastahili pongezi.

Wednesday, October 12, 2011

Maktaba ya Mkoa, Ruvuma

Nilipiga picha hii ya maktaba ya Mkoa, Ruvuma, tarehe 30 Julai mwaka huu. Niliwahi kuingia katika maktaba hii, ambayo iko mjini Songea, miaka kadhaa iliyopita, lakini safari hii sikupata muda. Nilizunguka maeneo mengine, kama vile Makumbusho ya Maji Maji, ambayo habari zake nategemea kuziandika baadaye.

Napenda kuandika habari za maktaba za Tanzania. Nimeshaandika kuhusu maktaba ya Lushoto, Kilimanjaro, na Iringa. Nitaendelea kufanya hivyo.

Monday, May 23, 2011

Maktaba ya Mkoa, Kilimanjaro

Tarehe 3 Agosti, mwaka jana, nilikuwa mjini Moshi nikiwa na hamu ya kuufahamu zaidi mji huo. Lengo langu moja lilikuwa kuiona maktaba ya mkoa, kwani nilikuwa sijawahi kufika hapo.

Haikuwa vigumu kufika mahali hapo. Niliingia ndani nikaona kuwa ni maktaba yenye hali nzuri kwa ujumla, kwa upande wa vitabu na majarida, nikifananisha na maktaba kadhaa nilizoziona sehemu zingine za nchi.


Kwa kawaida, ninapoingia katika maktaba za Tanzania, nimezoea kuwaona zaidi wanafunzi. Katika maktaba ya Moshi, niliwaona watu wazima kadhaa wakisoma. Sijui kama hii ndio kawaida katika maktaba hii, lakini niliguswa na jambo hilo.

Kila maktaba duniani, hata kama ni bora namna gani, inahitaji vitabu na majarida mapya muda wote, pamoja na tekinolojia na vifaa vya kisasa vya kupatia maandishi na taarifa. Na ndiyo changamoto kwa maktaba za Tanzania. Nimeona niweke hii taarifa fupi na picha kwenye blogu yangu, ili wengine wapate angalau fununu kuhusu hii maktaba ya Moshi.

Wednesday, April 27, 2011

Maktaba ya Lushoto

Kila ninapokuwa Tanzania, najitahidi kutembelea taasisi za elimu kama vile shule na maktaba. Mwaka jana, wakati nipo mjini Lushoto, nilipata dukuduku ya kujua kama kuna maktaba hapo, na iko wapi. Nimeshaona maktaba za hata miji midogo kama Mbinga na Mbulu.

Niliulizia mitaani, na watoto wa shule ya msingi wakanionyesha maktaba ilipo. Hiyo ilikuwa ni tarehe 5 Agosti. Niliingia ndani nikaona vitabu vya aina aina, vya taaluma mbali mbali, kuanzia fasihi, hadi masuala ya jamii na maendeleo. Niliona hata vitabu viwili vitatu vya Karl Marx, Kwame Nkrumah, na Issa Shivji.

Ingawa maktaba hii haina vitabu maelfu na maelfu, nilipata hisia kuwa mtu anayeishi katika mji huu akiamua anaweza kujielimisha kiasi cha kueleweka kwa kusoma vitabu vilivyomo katika maktaba hii.

Niliongea na mama mhudumu wa maktaba. Alinieleza mazingira magumu ya maktaba hii, nami nilijionea mwenyewe. Niliona jinsi yanavyohitajika makabati bora, kwa mfano. Nilimwambia kuwa nami kama mwalimu naguswa na moyo wa kujitolea wa watu wa aina yake, kwani sote tuko katika kusukuma gurudumu la elimu kwa jamii. Alifurahi kusikia hivyo.

Jambo la msingi ni kuwa nawasifu walioanzisha maktaba hii, na wale wanaoiendesha. Changamoto iliyopo ni kwa jamii yetu kuboresha taasisi kama hii maktaba. Pesa tunazo. Tatizo ni vipaumbele. Tukiangalia bajeti ya ulabu, kwa mfano, kwa wiki, mwezi au mwaka, ni wazi kuwa tungeweza kuwa na maktaba nzuri katika kila mji.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...