Showing posts with label Utalii. Show all posts
Showing posts with label Utalii. Show all posts

Saturday, November 30, 2019

Wadau wa Utalii wa Kielimu Tumekutana

Tarehe 2 Novemba nilikutana na mama Georgina, ambaye anatoka Ghana na ni mmiliki wa kampuni iitwayo African Travel Seminars. Anapeleka wasafiri kwenda nchi za Afrika, kuanzia kaskazini, hadi kusini, mashariki hadi magharibi, na Tanzania imo. Mbali ya kuwaonesha vivutio vya utalii, anawaelimisha kuhusu maisha na tamaduni za waAfrika.

Niliifahamu kuhusu kampuni yake kuanzia miaka ya tisini na kitu, nikaona jinsi shughuli zake zinavyofanana na zangu, ambazo zimeelezwa katika tovuti ya Africonexion. Hivi karibuni nilianza kuwasiliana na huyu mama, na tukapanga kukutana.

Kabla hatujakutana, mama huyu alisoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ameamua awe anawapa wageni anaowapelea Afrika. Yeye nami tunafahamu kuwa hii itawawezesha wageni kuelewa mwenendo na tabia za waAfrika na pia kujielewa namna wao wenyewe wanavyoeleweka kwa mtazamo wa waAfrika.

Tumejithibitishia kuwa malengo yetu yanafanana. Tunapenda kuendeleza elimu kuhusu Afrika kwa waMarekani na tunapenda kujenga maelewano baina ya waMarekani na waAfrika. Yeye nami tuna uzoefu wa kuongelea masala haya hapa Marekani, kwa wanafunzi na walimu, watu wanaoenda Afrika kwa shughuli za kujitolea, watalii, nakadhalika.

Sunday, June 3, 2018

Vitendea Kazi vya Kampuni Yangu

Mwaka 2002, nilianzisha na kusajili kampuni ambayo niliita Africonexion, kama nilivyoandika katika blogu hii. Nilisajili kama kampuni binafsi, usajili ambao hapa Marekani hujulikana kama "sole proprietorship." Niliamua kuanzisha na kusajili kampuni hii ya kutoaelimu na ushauri wa masuala ya utamaduni kwa kuwa tayari nilikuwa na uzoefu wa shughuli hizo, nikihudumia vyuo, makanisa, mashirika, jumuia na watu binafsi.

Shughuli zangu hizi zimekuwa na mafanikio makubwa, kwa maana kwamba nimewasaidia watu kuelewa na kuepukana na mambo ambayo yanaweza kusababisha migogoro na kutoelewana. Wale ambao tayari walishakumbana na migogoro na kutoelewana nimewasaidia kufahamu kwa nini walijikuta katika migogoro na kutoelewana. Lakini mimi mwenyewe nimefanikiwa pia kujifunza mengi katika shughuli zote hizo.

Napenda kuelezea siri moja kubwa ya mafanikio haya. Siri hiyo ni kujielimisha kwa kutumia vitabu. Vitabu ndio vitendea kazi vyangu. Sichoki kununua na kusoma vitabu. Kulingana na shughuli za kampuni yangu, ninanunua na ninasoma vitabu kuhusu masuala kama utandawazi, utamaduni, na saikolojia. Jana, kwa mfano, bila kutegemea, nilikiona kitabu kiitwacho Riding the Waves of Culture, katika duka la Half Price Books, mjini Apple Valley. Nilipokiona tu, nilitambua kuwa kitakuwa kitendea kazi muhimu.

Mbali na kutumia vitabu vya wengine, ninatumia pia kitabu nilichoandika mwenyewe, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitabu hiki kilitokana na uzoefu nilioongelea hapa juu. Si mimi tu ambaye ninakichukulia kitabu hiki kama kitendea kazi muhimu. Mifano ni profesa na mwandishi maarufu Becky Fjelland Brooks, ambaye aliakiongelea kitabu katika blogu yake. Mzee Patrick Hemingway, ambaye aliwahi kuishi Tanzania miaka yapata ishirini na tano, aliwahi kuniambia kuwa kitabu hiki ni "a tool of survival" yaani kimbilio la usalama.

Hili suala la kuviona vitabu kama vitendea kazi ni muhimu. Hainiingii akilini mtu aanzishe biashara, kwa mfano, halafu asitafute na kusoma vitabu au maandishi mengine juu ya uendeshaji wa biashara. Atafanikishaje malengo yake kama hafahamu vitu kama saikolojia ya binadamu, ambao ndio wateja wake? Atafanikiwaje kama hafahamu namna ya kuwasiliana na watu? Kama wateja wake ni wa tamaduni tofauti na utamaduni wake, ni muhimu mno afahamu tofauti hizo.

Nilivutiwa na msimamo wa Mama Barbro Finskas Mushendwa, mmiliki wa kampuni ya utalii ya J.M Tours, yenye makao yake Arusha, Tanzania. Baada ya kusoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, aliamua kununua nakala kadhaa kwa ajili ya wafanyakazi wake, ambao walikuwa ni madreva wa watalii. Aliona haraka kuwa kitabu hiki kinafaa kama kitendea kazi na madreva wake walinithibitishia hivyo, kama nilivyoripoti katika blogu ya ki-Ingereza.

Mmiliki wa kampuni yoyote anajua ulazima wa vitendea kazi kama vile magari na kompyuta, sawa na mkulima navyojua ulazima wa jembe na shoka. Lakini sijui ni wamiliki wa makampuni na wafanya biashara wangapi wa Tanzania wenye mtazamo kama wa Mama Mushendwa, wa kutambua kuwa vitabu ni vitendea kazi. Ninaona wanaanzisha kampuni au biashara na kuziendesha kimazoea,  au kwa kutegemea kudra ya Mungu au hata waganga wa kienyeji. Daima ninaona matangazo ya waganga wa kienyeji wakinadi dawa za mafanikio kibiashara.

Ninapoongelea mada hii ya vitabu kama vitendea kazi, ninakumbuka juhudi aliyofanya Mwalimu Nyerere katika kutekeleza kile alichoita elimu yenye manufaa. Aliwahimiza watu kujisomea ili kuboresha shughuli walizokuwa wanafanya. Chini ya uongozi wake, vilichapishwa na kusambazwa vitabu kuhusu kilimo, uvuvi, useremala, na kadhalika. Ninakumbuka kwamba kijijini kwangu, vitabu hivyo vilihifadhiwa katika nyumba ya baba yangu.

Pamoja na mimi kutumia vitabu vya wengine kama vitendea kazi, ninashukuru kwamba nami ni mwandishi. Ninapangia kuendelea kuandika ili kuchangia ufanisi katika shughuli zangu na za wengine.

Friday, October 9, 2015

Nimepata Toleo Jipya la "Green Hills of Africa"

Leo ni siku ya furaha kwangu. Nimepata nakala ya toleo jipya la Green Hills of Africa, kitabu cha Ernest Hemingway, kilichochapishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1935. Taarifa kwamba toleo hili lilikuwa linaandaliwa nilielezwa na Mzee Patrick Hemingway, kama nilivyoandika katika blogu hii. Kwa hivi, nilipogundua kwamba limechapishwa, niliagiza nakala hima.

Katika Green Hills of Africa, Hemingway anaelezea mizunguko yake katika nchi ya Tanganyika, mwaka 1933-34, akiwa na mke wake wa pili Pauline Pfeiffer. Anaelezea uzuri wa nchi, watu wa makabila, tamaduni, na dini mbali mbali, na wanyama katika mbuga alimowinda, kama vile Serengeti na eneo la Ziwa Manyara. Anaelezea miji alimopita, kama vile Mto wa Mbu, Babati, Kondoa, Handeni, na Tanga.

Toleo hili la Green Hills of Africa lina mambo ambayo hayakuwemo katika toleo la mwanzo, kama vile maandishi ya awali ambayo hayakutokea kitabuni, picha, na hata "diary" aliyoandika Pauline alipokuwa safarini na mumewe. Nilijua kuwa "diary" hii imehifadhiwa katika maktaba ya Chuo Kikuu cha Stanford, na nilikuwa nawazia kwenda kuisoma. Kuchapishwa kwake katika toleo hili ni jambo la kufurahisha sana.

Kutokana na jinsi Hemingway alivyoielezea nchi yetu, tukio la kuchapishwa kwa toleo hili la Green Hills of Africa mwaka huu ilipaswa tulipokee kwa shamra shamra. Pangekuwa na shughuli za uzinduzi wa toleo hili, makongamano, na tahakiki magazetini. Nakala zingejaa katika maduka ya vitabu, na wateja wangekuwa wanapigana vikumbo kuzinunua.

Sehemu zingine duniani wanatumia vilivyo bahati ya kutembelewa na Hemingway na kuandikwa katika maandishi yake. Ni kivutio kikubwa kwa watalii, kama ninavyosema katika blogu hii. Sisi tumeifanya nchi yetu kuwa kwenye miti ambako hakuna wajenzi.

Thursday, September 24, 2015

"Papa's Shadow" Yapongezwa na Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa

Tarehe 20 mwezi huu nilipeleka ujumbe Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa kuhusu filamu ya Papa's Shadow. Sikuandika ujumbe mrefu, bali niliwatumia kiunganishi hiki.

Bila kuchelewa, tarehe 22 nilipata ujumbe kutoka kwao, ukiwa umeandikwa na Ndugu Noel Kabanda. Uwakilishi unaafiki kuwa Papa's Shadow ni "fursa maridhawa ya kuitangaza Tanzania ulimwenguni" na unasisitiza kuwa "Serikali inatambua mchango wa sanaa katika kuitangaza Tanzania katika sekta mbali mbali ikiwemo utalii na utamaduni."

Kwanza, kwa kuzingatia uwingi wa majukumu yanayowakabili wawakilishi wetu katika balozi zetu, nimeona ni muhimu kusema nilivyoguswa na jinsi Uwakilishi ulivyoushughulikia ujumbe wangu.

Pili, ujumbe wa Uwakilishi unawatia moyo wahusika wa Ramble Pictures, ambao ndio watengeneaji wa Papa's Shadow. Timu nzima ya Ramble Pictures ni vijana wa ki-Marekani, na baadhi yao walikuja Tanzania mwaka 2013 kwenye kozi yangu ya Hemingway Katika Afrika Mashariki. Ni furaha kwangu, na jambo la kujivunia, kuwaeleza vijana hao kuwa Uwakilishi wa Kudumu waTanzania Umoja wa Mataifa umeipokea Papa's Shadow kwa namna hii.

Papa's Shadow si filamu ya maigizo. Ni filamu ya kuelimisha kuhusu mwandishi Ernest Hemingway. Sehemu kubwa ya filamu hiyo ni maongezi baina yangu na Mzee Patrick Hemingway, mtoto pekee aliyebaki wa mwandishi Hemingway. Tunaongelea maisha ya Hemingway, safari zake, uandishi wake, na fikra zake kuhusu masuala mbali mbali. Tunawafungua macho walimwengu kuhusu namna Hemingway alivyoipenda Afrika na alivyokuwa mtetezi wa Afrika.

Hemingway alisafiri na kuishi Afrika Mashariki mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54. Aliandika hadithi, insha, barua na maandishi mengine ambayo ni hazina kubwa. Wenzetu katika nchi zingine ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari za huko, wametumia fursa hiyo kujitangaza, na wanawavutia watalii wengi sana. Mifano ni miji kama Paris (Ufaransa), Havana (Cuba), Oak Park (Illinois, Marekani), Key West (Florida, Marekani), na Pamplona (Hispania). Hemingway anapendwa ulimwenguni kote ambako watu wana utamaduni wa kusoma vitabu. Sina shaka kuwa Papa's Shadow italeta msisimko wa aina hiyo kwa kuwaelekeza mashabiki wa Hemingway nchini kwetu.

Hamu ya kuona Tanzania inafunguka macho kuhusu fursa hii ilinihamasisha kufanya utafiti juu ya safari za Hemingway katika nchi yetu na maandishi aliyoandika. Kozi niliyotunga ilikuwa na lengo hili. Nilitaka pia kuwasaidia walimwengu kuelewa umuhimu wa Afrika katika maisha na uandishi wa Hemingway. Kwa msingi huo huo, nilishiriki kikamilifu katika kufanikisha filamu ya Papa's Shadow.

Nimeeleza hayo yote ili kuweka wazi umuhimu wa ujumbe wa Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa. Ni mfano wa mshikamano unaotakiwa baina yetu wanadiaspora, serikali, na wananchi wenzetu.

Wednesday, September 16, 2015

Filamu ya "Papa's Shadow:" Fursa ya Kuitangaza Tanzania

Nina furaha kuandika kuhusu filamu ambayo imeandaliwa iitwayo "Papa's Shadow," inayomhusu mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Katika filamu hiyo, ninaonekana nikiongea na Mzee Patrick Hemingway, ambaye ni mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye hai. Ana umri wa miaka 87. Tunaongelea maisha, safari, maandishi na fikra za Hemingway, hasa kuhusu Afrika.

Sehemu nyingi hapa duniani ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari zake, zimejipatia umaarufu. na zinafaidika hasa katika utalii. Mifano ni Cuba na mji wa Pamplona nchini Hispania. Watu wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla tuna bahati hiyo, kwani Hemingway alikuja na kuishi kwetu mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54, akaandika vitabu, hadithi, insha na barua kuhusu aliyoyaona.

Filamu ya "Papa's Shadow" ilitokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013 juu ya Hemingway. Kozi ile ilimhamasisha Jimmy Gildea, mmoja wa wanafunzi wangu, kutengeneza filamu hiyo. Alianzisha kampuni, Ramble Pictures, akaanza kutegeneza hiyo filamu ya kuelimisha. Anaendelea kutengeneza filamu zingine zenye kuelimisha.

"Papa's Shadow" inaitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Kuna kampeni ya kuchangisha fedha za kumalizia malipo ya usajili na taratibu zingine kabla ya filamu kuonyeshwa na kusambazwa. Naleta hapa ujumbe ambao umeandikwa na binti yangu Zawadi, mmoja wa watu wanaojitolea katika Ramble Pictures, unaoelezea kampeni hiyo.

Nitapenda ujumbe huu uwafikie wa-Tanzania popote duniani, hasa wanadiaspora, ofisi za ubalozi, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, na wadau wengine wote. Nilitumia miaka kadhaa kusoma maandishi ya Hemingway na kuandaa kozi ambayo ni chimbuko la filamu hii. Ninapangia kuendelea kufundisha kozi hiyo. Nawe m-Tanzania mwenzangu una fursa ya kutoa mchango wako. Tushirikiane. Tutafanikiwa. Sisi tuliokuwepo wakati Tanganyika ilipopata Uhuru tunakumbuka kauli mbiu ya Mwalimu Nyerere ya kuhimiza maendeleo ya Taifa jipya: "It can be done; play your part."

=====================================================

Hello!

My name is Zawadi Mbele, and I am contacting you today to let you know about an amazing project. Ramble Pictures, a Minneapolis-based, independent film company, recently launched a 30-day "Kickstarter" campaign in order to raise funds for the distribution of our completed documentary, Papa's Shadow.

Papa's Shadow is a personal film about Ernest Hemingway in East Africa. It explores his hunting expeditions and holds key dialogues on subjects such as race, language, and the cultures that distinguish us as citizens of the world. Featuring exclusive testimony by Ernest's only living son, Patrick Hemingway, as well as Tanzanian author and Hemingway scholar, Dr. Joseph Mbele, this documentary explores the integral role of two safaris in their shaping of an author and demise of a legend. 

Over the past four years, hard work and creative energy has been poured into making this feature-length documentary. The film has already been completed, however, we cannot show or distribute the film until we finish paying for copyright licensing. Again, please visit our Kickstarter webpage to learn more about how you can play an important role in bringing this documentary to distribution. Also, with Kickstarter, we are offering exclusive rewards with every donation, such as the new Hemingway Library Edition of "Greens Hills of Africa," signed by Patrick Hemingway. 

If there is someone else from your organization you would recommend contacting, we would be grateful to have our information passed along. If you can, please take the time to explore our webpage and let me know if you have any questions at all. You can email me directly or email Elizabeth Turner at elizabeth@ramblepictures.com.

Thank you for your time, and we look forward to hearing back from you!

Sincerely,

Zawadi Mbele
email: zawadi.mbele@gmail.com

Sunday, February 8, 2015

Mwenyeji Wetu Longido, Tanzania

Picha hii ilipigwa Januari, 2013, nilipokuwa Longido, Tanzania. Niko na Ndugu Ally Ahamadou, mkurugenzi wa programu ya utalii wa utamaduni hapa Longido. Yeye ndiye alikuwa mwenyeji wa misafara yangu katika kozi kuhusu safari na maandishi ya Ernest Hemingway.

Programu ya utalii wa utamaduni Longido ni moja kati ya programu maarufu za aina hii nchini Tanzania. Taarifa kuhusu program hii zinapakana kirahisi mtandaoni.

Binafsi nimeshuhudia jambo hili kwa jinsi makala niliyochapisha katika blogu yangu ya ki-Ingereza kuhusu utalii wa utamaduni Longido inavyotembelewa na wasomaji wengi. Hali hii imenithibitishia kuwa blogu inaweza kuwa nyenzo yenye uwezo mkubwa wa kutangaza utalii.

Ingawa Ndugu Ally Ahmadou si mzaliwa wa Longido, bali Tanga, niliona anakubalika sana na watu wa Longido. Hata kwa kuongea naye muda mfupi tu, unapata picha kuwa huyu ni mpenzi Longido na shughuli za utalii wa utamaduni. Programu hii ya utalii wa utamaduni Longido niliona inapendwa na watu wa Longido, kwa kuwa faida zake katika jamii yao wanaziona.

Ndugu Ally Ahmadou nilimwona kuwa mtu mwepesi wa kuangalia fursa mpya katika shughuli ya utalii. Mfano ni jinsi tulivyoongelea suala la vitabu katika utalii, suala ambalo nimeliongelea katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii na nililigusia pia katika blogu hii. Ndugu Ally alipofahamu kuwa nimechapisha vitabu vinavyoweza kuchangia katika sekta hiyo, alichukua nakala za kutosha za Matengo Folktales na Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kwa ajili ya watalii ambao wangependa kuvinunua.

Thursday, May 29, 2014

Duka Dogo Langoni pa Hifadhi ya Tarangire

Mwezi Januari, mwaka 2013, nilikuwa nazunguka maeneo ya kaskazini mwa Tanzania na wanafunzi 29 wa chuo cha St. Olaf. Tulikuwa katika kozi kuhusu safari za mwandishi Ernest Hemingway, tukisoma maandishi aliyoandika kuhusu sehemu hizo. Kati ya sehemu tulizotembelea ni hifadhi za Ngorongoro, Serengeti, Manyara, na Tarangire.

Kwenye sehemu ya kuingilia Tarangire, niliona duka dogo ambalo lilinivutia. Niliamua kupiga picha.



 


Kwa wale ambao wamefika Tarangire, hapa mahali ni karibu kabisa na Tarangire Safari Lodge. Ingawa nilishafika Tarangire mara mbili tatu miaka iliyotangulia, sikumbuki kama nililiona duka hili. Nilivutiwa na rangi mbali mbali za vitu vilivyokuwa vinauzwa humo. Nilijisikia kama vile naangalia kazi ya sanaa.

















Kwa wale ambao hawajafika, nimeona ni jambo jema kuwapa fununu kidogo kuhusu vitu ambavyo vinanivutia nchini mwetu.










Friday, August 5, 2011

Mitaani Mbamba Bay

Agosti tarehe 2 nilisafiri kutoka kijijini kwangu Lituru nikapitia Mbinga, na kufika Mbamba Bay, mwambao wa Ziwa Nyasa kwa matembezi.

Mbamba Bay, ingawa mji mdogo sana, unavutia kwa utulivu wake na mazingira, ukiwa ufukweni mwa Ziwa linalomeremeta kwa maji yake maangavu, kama nilivyowahi kuandika hapa.

Nilikuwa na bahati kwamba tarehe 3 Agosti ilikuwa siku ya jua na hali ya hewa ya kuvutia sana. Nami nilitumia fursa hii vilivyo. Niliteremkia ufukweni kufurahia upepo mwanana na mandhari murua ya Ziwa.


Kukaa nje ya nchi yako kunakupa mtazamo tofauti wa masuala ya nchi yako. Kwa mfano, hapa Tanzania, watoto wetu wana uhuru sana wa kucheza na kuzunguka mitaani, tofauti na Marekani, ambako watoto huangaliwa sana muda wote na wazazi au walezi wao, kwani si salama kuwaacha watoto bila uangalizi. Wa-Marekani wanaokuja huku kwetu wanashangaa wanapowaona watoto wakijizungukia wenyewe mitaani, raha mstarehe. Nimeongelea tofauti hizo katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Joto la Mbambay ni kishawishi kikubwa cha kutafuta sehemu ya kujipatia kinywaji baridi. Nami nilisogea baa hii iitwayo Bush House, nikatuliza kiu.



Hali ya Mbamba Bay ni ya utulivu usio kifani. Ni mahali pazuri kwa mapumziko. Kadiri siku zinavyopita, nina imani kuwa Mbamba Bay patakuwa kivutio kikubwa kwa watalii wa nje na ndani ya nchi. Nami niliamua kufika Mbamba Bay ili kupiga picha nichangie katika kuitangaza sehemu hii ya Tanzania.










Tuesday, June 28, 2011

Naenda kwa wa-Nyakyusa

Hivi karibuni, nitakuwa Tanzania na wanafunzi katika programu ya masomo inayoendeshwa na vyuo kadhaa vya Marekani kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Kabla ya kuwafikisha Chuo Kikuu Dar es Salaam ambapo watasoma kwa muhula mmoja, nitakuwa nao maeneo ya nyanda za juu, hasa Iringa. Lakini, katika kupanga safari hii, nimeamua kuwafikisha hadi Mbeya na Ziwa Nyasa, wakaone na kujifunza. Iringa naifahamu vizuri, ila Mbeya nilipita tu mara moja, miaka ya mwisho ya sabini na kitu.

Wakati nangojea kwenda Mbeya, nawazia utamaduni wa wa-Nyakyusa. Mimi kama mtafiti, nimesoma kiasi kuhusu masimulizi yao ya jadi. Ninakumbuka maandishi ya watafiti kama Monica Wilson. Nina kitabu kiitwacho The Oral Literature of the Banyakyusa, kilichoandikwa na Christon S. Mwakasaka. Nadhani nilikinunua Dar es Salaam, nikawa nakisoma mara moja moja.

Lakini wakati huu ninapongojea safari ya Mbeya, kitabu hiki kinanivutia kwa namna ya pekee. Kina hadithi za jadi, lakini vile vile nyimbo na tungo zingine zinazoelezea mambo ya hivi karibuni ya historia na siasa u-Nyakyusa na Tanzania kwa ujumla.

Natafuta maandishi mengine ya kuongezea ufahamu wangu. Kwa hilo naweza kusema nimeathiriwa na wa-Marekani. Wao, kabla ya kusafiri, wana hiyo tabia ya kusoma habari za sehemu waendako. Ni jadi nzuri. Kusafiri kunatupanua akili, lakini kusoma habari za tuendako kunautajirisha zaidi ufahamu wetu.

Saturday, April 10, 2010

Mpambano na Lonely Planet

Siku kadhaa zilizopita niliandika kuhusu msomaji wa kitabu changu cha Africans and Americans ambaye alisema kinafaa kuliko kile cha Lonely Planet. Bofya hapa. Nilitamka kiutani kuwa Lonely Planet wakae chonjo, maana wamepata mshindani.

Lakini baadaye, nililazimika kuandika tena kuhusu Lonely Planet, baada ya wao kuandika taarifa iliyoudhalilisha mji wetu wa Arusha. Bofya hapa. Hapo uzalendo ulinisukuma kusema kuwa hao sasa wanatuchokoza, na lazima tujizatiti kujibu mapigo.

Dada Subi, ambaye ni mfuatiliaji makini wa maandishi ya wanablogu wa Bongo na pia mshauri wetu tunayempenda na kumheshimu sana, kanibonyeza leo asubuhi kuwa kuna jambo limetokea Lonely Planet, yaani mteja anayepangia kwenda Tanzania anaulizia kitabu au vitabu vya kusoma, ambavyo si vya aina ya Lonely Planet.

Basi, hapo nimeona lazima niingie mzigoni na kuwachangamkia hao Lonely Planet. Sio kuwalazia damu; ni kuwavalia njuga tu. Nimefanya hivyo tayari, kwa kumpa yule mteja taarifa anazohitaji. Bofya hapa. Heshima na shukrani kwa Dada Subi, kama kawaida, na blogu yake maarufu hii hapa.

Wednesday, July 15, 2009

Mafanikio ya Mradi wa Utalii: Mto wa Mbu

Nimesoma taarifa ya kufurahisha katika Arusha Times kuwa mradi wa utalii Mto wa Mbu, umeteuliwa kuwa mfano wa kuigwa nchini Tanzania. Ni heshima kubwa, nami natoa pongezi kwa vijana wanaoendesha mradi huu.

Nimewafahamu vijana hao kwa miaka kadhaa, tukizungumzia masuala mbali mbali muhimu. Katika kupita kwangu Mto wa Mbu na wanafunzi wa kiMarekani, vijana hao wamekuwa wenyeji wetu wa kutueleza masuala ya tamaduni za mji ule.

Nimeandika habari zao kwenye blogu yangu. Nao katika blogu yao wameandika habari ya ushirikiano wetu.

Ni jambo la kufurahisha kuwaona vijana wakijituma katika shughuli za maendeleo namna hii, na nawatakia mafanikio makubwa zaidi siku za usoni.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...