Showing posts with label Mwalimu Nyerere. Show all posts
Showing posts with label Mwalimu Nyerere. Show all posts

Tuesday, September 20, 2016

"The Dilemma of a Ghost:" Tamthilia ya Ama Ata Aidoo

The Dilemma of a Ghost ni tamthilia ya kwanza ya Ama Ata Aidoo wa Ghana. Aliitunga alipokuwa mwanafunzi katika chuo kikuu cha Ghana, Legon, ikaonyeshwa mara ya kwanza mwaka 1964, na kuchapishwa mwaka 1965. Ama Ata Aidoo aliendelea kuandika na bado anaandika, na kazi zake ni pamoja na tamthilia nyingine iitwayo Anowa, ambayo ilichapishwa mwaka 1970, hadithi fupi, na riwaya kadhaa.

The Dilemma of a Ghost inaongelea juu ya kijana wa Ghana aitwaye Ato aliyekwenda masomoni Marekani na huko akakutana na Eulalie, binti Mwamerika Mweusi. Huyu ni kati ya wale wa-Marekani Weusi wanaoiwazia Afrika kwa hamu kama mtu aliyeko ugenini anavyowazia nyumbani kwake.

Ato na Eulalie wanaoana na kurejea Ghana, ambako wanakumbana na mambo magumu. Kwanza ndugu zake Ato wanashtuka kusikia kuwa Ato ameoa bila kuwashirikisha. Halafu binti mwenyewe hana kabila wanalolitambua, na hata jina lake wanashindwa kulitamka, na kibaya zaidi, kwa mtazamo wao, ni kuwa binti huyo ni kizalia cha watumwa. Wanaukoo wanaona Ato amewasaliti.

Halafu, Eulalie naye anashindwa kuelewa na kufuata mila na desturi za hao ndugu. Wao wanamwona kama kizuka, kwa tabia zake, ikiwemo kukataa kunywesha dawa za kienyeji za kumwezesha kupata mimba. Mama mkwe wake, Esi Kom, anapofanya ukarimu wa kumletea konokono, ambao ni chakula cha heshima, Eulalie anashtuka, na haamini macho yake, na hatimaye anawatupilia mbali hao konokono. Jambo jingine linalowashangaza ndugu hao ni jinsi Eulalie anavyovuta sigara. Basi, inakuwa shida juu ya shida, na hatimaye binti anajikuta katika upweke na msongo wa mawazo.

Lakini, hatimaye, mama yake Ato anaridhia kumpokea huyu mkwe wake na anachukua hatua za kuwashawishi ndugu wote wampokee, kwa hoja kwamba mgeni hastahili kulaumiwa, bali mwenye lawama ni mwenyeji, yaani Ato. Ato anajikuta akiwa mpweke, aliyesongwa na mawazo, karibu kuchanganyikiwa. Ndivyo tamthilia inavyokwisha.

The Dilemma of a Ghost imejengeka katika mfumo wa hadithi za jadi ambazo huitwa "dilemma tales" ambao ni muundo unaowaacha wasikilizaji wakiwa na masuali yasiyojibika kirahisi. Katika tamthilia hii, suali moja muhimu ni nani wa kulaumiwa kwa matatizo yanayoibuka. Tamthilia hii inatumia pia aina nyingine za fasihi simulizi, kama vile nyimbo na methali. Vile vile kuna imani za jadi, kama vile juu ya mizimu na matambiko.

Ama Ata Aidoo ni mmoja wa waandishi wa ki-Afrika ambao ni hodari wa kutumia miundo na dhamira za masimulizi ya jadi. Hilo suala la kijana kujifanyia mwenyewe uamuzi wa kuoa au kuolewa bila kuwahusisha wazazi ni dhamira maarufu katika fasihi simulizi za Afrika, na matokeo ya kiburi hiki huwa si mema. Katika tamthilia ya Anowa, Ama Ata Aidoo ameiweka pia dhamira hiyo. Msichana Anowa anaamua kuolewa na kijana aliyemkuta bila wazazi kuhusika.

Tangu mwanzo, nilivutiwa na mtindo huu katika uandishi wa Ama Ata Aidoo, ambaye miaka ile alikuwa anajulikana kwa jina la Christina Ama Ata Aidoo. Ninakumbuka vizuri, kwa mfano, hadithi yake moja ya mwanzo kabisa iitwayo "In the Cutting of a Drink" ambayo niliisoma kwa mara ya kwanza miaka ya sitini na kitu, nilipokuwa mwanafunzi katika shule ya sekondari.

Nilivutiwa sana na hadithi hiyo kwa mtiririko wake sawa na wa mtambaji hadithi. Miaka ya baadaye, nilipojifunza somo la fasihi simulizi, nilianza kuelewa vizuri jinsi waandishi kama Ama Ata Aidoo wanavyotumia jadi hiyo.

Jambo muhimu sana jingine kuhusu Ama Ata Aidoo ni kuwa ni mwandishi mwenye kuchambua masuala ya jamii. Alivyokuwa anatunga The Dilemma of a Ghost, masuala kama ya mshikamano na mahusiano ya watu weusi ulimwenguni yaani "Pan-Africanism," yalikuwa yakivuma na kuwashughulisha viongozi maarufu kama George Padmore, W.B. Dubois, Kwame Nkrumah, Ahmed Sekou Toure, Jomo Kenyatta, na Julius Nyerere. Miaka iliyofuatia, Ama Ata Aidoo amekuwa akienda na wakati kama mwanaharakati katika masuala ya ukoloni mambo leo, haki za wanawake, na hata ujamaa. Sawa na ilivyokuwa kwa Mwalimu Julius Nyerere, Ama Ata Aidoo ni muumini wa fikra za kijamaa.

Monday, April 25, 2016

Kumbukumbu ya Kifo cha Shakespeare

Wiki hii ni ya kumbukumbu ya kifo cha William Shakespeare. Ingawa siku ya kufariki kwake haijulikani kwa uhakika, mapokeo yameiteua tarehe 23 April, 1616, kuwa ndio siku ya kufariki kwake. Alizikwa tarehe 25 Aprili.

Sisi tuliosoma sekondari miaka ya sitini na kitu tuliweza kusoma maandishi ya Shakespeare na kuyafurahia. Tulisoma tamthilia kama Julius Caesar na The Merchant of Venice. Baada sekondari, sisi tuliokwenda "high school" tulipata fursa ya kusoma na kutafakari tamthilia zake ngumu zaidi, kama vile Hamlet na Othello.

Mwandishi maarufu wa ki-Swahili, Shaaban Robert, alimwenzi Shakespeare. Alisema kwamba akili ya Shakespeare ilikuwa kama bahari ambayo mawimbi yake yalitua kwenye fukwe duniani kote. Laiti kama wa-Tanzania tungefuata nyayo za Shaaban Robert, tukaachana na ufinyu wa fikra kuhusu umuhimu wa lugha mbali mbali na fasihi za ulimwengu, kwa kisingizio cha kukienzi ki-Swahili.

Maandishi ya Shakespeare yana kauli nyingi maarufu. Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Hamlet inayoanza hivi:

To be, or not to be: that is the question:
Whether 'tis nobler in the mind to suffer
The slings and arrows of outrageous fortune,
Or to take arms against a sea of troubles,
And by opposing end them? To die: to sleep;
No more; and by a sleep to say we end
The heart-ache and the thousand natural shocks
That flesh is heir to, 'tis a consummation
Devoutly to be wish'd.

Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Mark Antony iliyomo katika Julius Caesar, inayoanza hivi:

Friends, Romans, countrymen, lend me your ears;
I come to bury Caesar, not to praise him.
The evil that men do lives after them;
The good is oft interréd with their bones;
So let it be with Caesar. The noble Brutus
Hath told you Caesar was ambitious:
If it were so, it was a grievous fault,
And grievously hath Caesar answer'd it.

Kuna pia kauli maarufu katika tamthilia ya As You Like It, ambayo ni ya mhusika aitwaye Jaques. Anasema kuwa dunia ni jukwaa, ambapo kila binadamu ni kama mwigizaji:

All the world’s a stage,
And all the men and women merely players;
They have their exits and their entrances,
And one man in his time plays many parts,
His acts being seven ages.

Shakespeare aliona mbali. Kwa mfano, unaposoma The Merchant of Venice, unajionea jinsi Shakespeare alivyokuwa na upeo wa fikra wa kutambua tabia ya ubepari mapema kabisa, wakati ulipokuwa unachimbuka. Haishangazi kwa nini Mwalimu Nyerere, ambaye alikuwa katika harakati za kupambana na ubepari na kujenga ujamaa aliamua kuitafsiri tamthilia hii, akaiita Mabepari wa Venisi.

Shakespeare alizielezea kwa umakini tabia za binadamu, njema au mbaya. Katika tamthilia ya Macbeth, kwa mfano, tunashuhudia jinsi binadamu anavyoweza kuwa mbaya, na kama wewe ni msomaji wa Shaaban Robert utakumbuka jinsi naye alivyoielezea dhamira hii, kwa mfano katika Adili na Nduguze.

Shakespeare alikuwa mtunzi wa tamthilia na mashairi. Alitunga mashairi mengi, na baadhi ya hayo yako katika tamthilia zake. Haiwezekani kumtendea haki Shakespeare kwa kuelezea mchango wake katika makala ndogo kama hii. Kuna makala nyingi na vitabu juu yake na kazi zake, na maandishi yanaendelea kuchapishwa katika lugha nyingi. 

Kama Shaaban Robert alivyosema, akili ya Shakespeare ni kama bahari, ambayo mawimbi yake yanatua kwenye fukwe duniani kote. Ni miaka mia nne imepita tangu Shakespeare afariki, lakini mawimbi ya akili yake yataendelea kumwagika duniani kote.

Wednesday, September 16, 2015

Filamu ya "Papa's Shadow:" Fursa ya Kuitangaza Tanzania

Nina furaha kuandika kuhusu filamu ambayo imeandaliwa iitwayo "Papa's Shadow," inayomhusu mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Katika filamu hiyo, ninaonekana nikiongea na Mzee Patrick Hemingway, ambaye ni mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye hai. Ana umri wa miaka 87. Tunaongelea maisha, safari, maandishi na fikra za Hemingway, hasa kuhusu Afrika.

Sehemu nyingi hapa duniani ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari zake, zimejipatia umaarufu. na zinafaidika hasa katika utalii. Mifano ni Cuba na mji wa Pamplona nchini Hispania. Watu wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla tuna bahati hiyo, kwani Hemingway alikuja na kuishi kwetu mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54, akaandika vitabu, hadithi, insha na barua kuhusu aliyoyaona.

Filamu ya "Papa's Shadow" ilitokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013 juu ya Hemingway. Kozi ile ilimhamasisha Jimmy Gildea, mmoja wa wanafunzi wangu, kutengeneza filamu hiyo. Alianzisha kampuni, Ramble Pictures, akaanza kutegeneza hiyo filamu ya kuelimisha. Anaendelea kutengeneza filamu zingine zenye kuelimisha.

"Papa's Shadow" inaitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Kuna kampeni ya kuchangisha fedha za kumalizia malipo ya usajili na taratibu zingine kabla ya filamu kuonyeshwa na kusambazwa. Naleta hapa ujumbe ambao umeandikwa na binti yangu Zawadi, mmoja wa watu wanaojitolea katika Ramble Pictures, unaoelezea kampeni hiyo.

Nitapenda ujumbe huu uwafikie wa-Tanzania popote duniani, hasa wanadiaspora, ofisi za ubalozi, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, na wadau wengine wote. Nilitumia miaka kadhaa kusoma maandishi ya Hemingway na kuandaa kozi ambayo ni chimbuko la filamu hii. Ninapangia kuendelea kufundisha kozi hiyo. Nawe m-Tanzania mwenzangu una fursa ya kutoa mchango wako. Tushirikiane. Tutafanikiwa. Sisi tuliokuwepo wakati Tanganyika ilipopata Uhuru tunakumbuka kauli mbiu ya Mwalimu Nyerere ya kuhimiza maendeleo ya Taifa jipya: "It can be done; play your part."

=====================================================

Hello!

My name is Zawadi Mbele, and I am contacting you today to let you know about an amazing project. Ramble Pictures, a Minneapolis-based, independent film company, recently launched a 30-day "Kickstarter" campaign in order to raise funds for the distribution of our completed documentary, Papa's Shadow.

Papa's Shadow is a personal film about Ernest Hemingway in East Africa. It explores his hunting expeditions and holds key dialogues on subjects such as race, language, and the cultures that distinguish us as citizens of the world. Featuring exclusive testimony by Ernest's only living son, Patrick Hemingway, as well as Tanzanian author and Hemingway scholar, Dr. Joseph Mbele, this documentary explores the integral role of two safaris in their shaping of an author and demise of a legend. 

Over the past four years, hard work and creative energy has been poured into making this feature-length documentary. The film has already been completed, however, we cannot show or distribute the film until we finish paying for copyright licensing. Again, please visit our Kickstarter webpage to learn more about how you can play an important role in bringing this documentary to distribution. Also, with Kickstarter, we are offering exclusive rewards with every donation, such as the new Hemingway Library Edition of "Greens Hills of Africa," signed by Patrick Hemingway. 

If there is someone else from your organization you would recommend contacting, we would be grateful to have our information passed along. If you can, please take the time to explore our webpage and let me know if you have any questions at all. You can email me directly or email Elizabeth Turner at elizabeth@ramblepictures.com.

Thank you for your time, and we look forward to hearing back from you!

Sincerely,

Zawadi Mbele
email: zawadi.mbele@gmail.com

Sunday, August 9, 2015

Shaaban Robert na Mbaraka Mwinshehe Waliongelea Umuhimu wa Shule

Nikiachilia mbali jinsi wazazi wangu walivyohimiza elimu, nikiachilia mbali jinsi Mwalimu Nyerere alivyohimiza elimu, naukumbuka kwa namna ya pekee mchango wa mwandishi Shaaban Robert na mwanamuziki Mbaraka Mwinshehe katika kuhimiza elimu.

Ninakumbuka jinsi baba yangu, nilipokuwa shule ya msingi, alivyokuwa ananitia msukosuko iwapo nilishindwa kupata 100% katika zoezi lolote au mtihani wowote. Ninakumbuka pia jinsi Mwalimu Nyerere alivyokuwa anahimiza elimu, kwa watu wote, kuanzia watoto hadi wazee, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Shaaban Robert ni mtu anayenifanya nimkumbuke baba yangu. Nilijionea hayo niliposoma kitabu kiitwacho Barua za Shaaban Robert, ambacho habari zake niliziandika katika blogu hii. Humo tunaona jinsi Shaaban Robert alivyokuwa anamhamasisha mdogo wake Yusuf Ulenge afanye bidii katika elimu, akimtimizia mahitaji yote ya shule. Kwa wazazi na walezi, Shaaban Robert ni mfano wa kuigwa.

Mbaraka Mwinshehe, mwanamuziki ambaye wakati wa ujana wangu alitingisha Afrika Mashariki, ya Kati, na Kusini kwa nyimbo na muziki wake, aliimba wimbo maarufu wa kuwaasa vijana wazingatie elimu. Wimbo huo, "Enyi Vijana Sikilizeni," unaweza kuusikiliza hapa:

https://archive.org/details/EnyiVijanaSikilizeni

Tuesday, March 3, 2015

Utamaduni wa Kuwasomea Watoto Vitabu

Nimeandika mara kwa mara kuhusu suala la elimu, sio tu katika blogu hii, bali pia katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, kitabu ambacho nilitegemea kitasomwa na wa-Tanzania wenzangu, lakini mambo yamekuwa kinyume.

Kati ya mambo ambayo nimekuwa nikiyaongelea ni umuhimu wa kuwasomea watoto vitabu, jambo ambalo limejengeka katika utamaduni wa wa-Marekani. Nimekumbuka yote hayo leo baada ya kusoma makala hii hapa
kama uthibitisho na changamoto.

Hili ni kati ya mambo ambayo wa-Tanzania tunapaswa kujifunza. Nimethibitisha mwenyewe kuwa watoto wa Tanzania wanapenda vitabu, bali, kadiri wanavyokua, mapenzi hayo huzimishwa na watu wazima na jamii kwa ujumla.

Kama wahenga walivyosema, mtoto umleavyo ndivyo akuavyo. Baada ya muda, watoto wa ki-Tanzania hufuata utamaduni wa jamii wa kutothamini vitabu, na Taifa linaendelea kuzorota kielimu., wakati wenzetu wa-Marekani wanawalea watoto wao katika kupenda vitabu.

Mwalimu Nyerere alikuwa mstari wa mbele katika kuwahamasisha watu wawe na tabia ya kutafuta elimu. Alikuwa mwandishi na msomaji makini. Alionyesha mfano kwa vitendo. Aliongoza njia.

Leo tuna watu ambao tunawaita viongozi ambao sielewi kwa nini wanaitwa viongozi. Wangekuwa ni viongozi, wangetambua kuwa elimu ni msingi wa maisha na maendeleo. Wangekuwa wanaihamasisha jamii kwa kauli na vitendo katika kutafuta elimu. Lakini, badala yake, hawaonekani kujali kabisa kwamba wanachangia katika kuliangamiza Taifa badala ya kuliongoza, yaani kulipeleka mbele.

Tuesday, December 9, 2014

Uhuru wa Tanganyika na Ukoloni Mamboleo

Siku hii ya leo, ambayo ni ya kumbukumbu ya siku ambapo Tanganyika ilijipatia Uhuru, nilitaka kuandika makala, "Uhuru wa Tanganyika na Ukoloni Mamboleo." Nilianzza kuandika, lakini nilijikuta naandika insha ndefu, sio makala fupi ambayo nadhani inatakiwa katika blogu. Kutokana na jambo hilo, nimeifuta ile makala na badala yake nimeandika kwa ufupi mambo yafuatavyo.

Uhuru tulipata tarehe 9 Desemba, 1961. Nilikuwa mwanafunzi wa darasa la tatu, na ninakumbuka msisimko, hata kule kijijini kwangu. Waalimu wetu, Charles Kinunda, John Pantaleon Mbonde, na Alois Turuka, walikuwa chanzo kikubwa cha ufahamu wetu wa mambo yaliyokuwa yanatokea.

Kati ya kumbukumbu ambazo haziwezi kutoweka akilini mwangu ni picha ya askari Alexander Nyirenda akiweka mwenge wa Uhuru juu ya Mlima Kilimanjaro. Sambamba na tukio hili la kihistoria ni hotuba ya Mwalimu Julius Nyerere, ambamo alisema:

Sisi tunataka kuwasha mwenge, na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro, ili umulike hata nje ya mipaka yetu, ulete tumaini pale ambapo hakuna matumaini, upendo mahali palipo na chuki, na heshima palipojaa dharau.

Mwalimu Nyerere, alifanya kila juhudi kuliongoza na kulielimisha hili Taifa huru, akisema kuwa tunaingia katika mapambano na maadui watatu: ujinga, umaskini na maradhi. Miaka ilivyopita, alifafanua vizuri malengo mengine ya Taifa hili: kujenga jamii ya usawa kwa wote, isiyo na matabaka; jamii yenye kutoa fursa sawa kwa wote, katika nyanja mbali mbali, kama vile uchumi, elimu, na afya; kuhakikisha kila mtu anatimiza wajibu wa kufanya kazi, chini ya kauli mbiu ya "Uhuru na Kazi," kujenga Taifa linalojitambua, kujiheshimu, na kujitegemea, Taifa huru lisilofungamana na upande wowote katika mazingira yale ya "Cold War," Taifa lenye kukaribisha urafiki na nchi yoyote kwa msingi wa kuheshimiana, Taifa ambalo halitamruhusu rafiki kutuchanguia marafiki au maadui, na tuwe mstari wa mbele kuunga mkono harakati za ukombozi Afrika na sehemu zingine duniani.

Hayo ndio yalikuwa malengo muhimu, ambayo Mwalimu Nyerere aliyaelezea katika hotuba zake, makala na vitabu mbali mbali. Alikuwa akienda na wakati, akizingatia mahitaji ya Taifa yalivyokuwa yanajitokeza. Kwa msingi huu, baada ya "Azimio la Arusha," aliendelea kuandika maandishi mengine, kama vile "Mwongozo," "Siasa ni Kilimo," "Elimu ya Kujitegemea," na "Binadamu na Maendeleo."

Hayo yote, tangu enzi za harakati za Uhuru hadi miaka ya mwisho mwisho ya sabini na kitu, yalifanyika chini ya uongozi wa chama cha TANU. Mtazamo na mwelekeo wa TANU ulikuwa wa kuongoza mapinduzi, kufuatana na mazingira ya kihistoria: kwanza ilikuwa kuwaunganisha wa-Tanganyika na kuwaongoza katika kupigania Uhuru, halafu, kuongoza harakati za kujenga ujamaa na kujitegemea.

Mwalimu Nyerere alifahamu fika kwamba Uhuru haukuwa mwisho wa safari. Kulikuwa na haja ya kupambana na urithi wa ukoloni, yaani ukoloni mamboleo na kuleta uhuru wa kweli, unaodhihirishwa na hali ya kujitegemea chini ya uongozi bora.

Miaka ilivyopita, baada ya chama kipya cha CCM kushika hatamu, hali ilikuwa hiyo kwa kipindi cha mwanzo. Lakini, pole pole, mwelekeo huu wa kuwa daima katika harakati za mapinduzi, ulianza kubadilika. Chini ya sera za CCM, kama vile "Azimio la Zanzibar," nchi imeendelea kuzama zaidi na zaidi katika mfumo wa matabaka na ukoloni mamboleo. Kwa lugha rahisi, CCM ni mhujumu wa Mapinduzi.

Ndoto na mategemeo ya Uhuru yametekwa nyara. Pamoja na kwamba tunasherehekea Uhuru tuliojipatia mwaka 1961, tutambue, kama TANU ilivyotambua, kuwa ule haukuwa mwisho wa safari. Enzi za TANU, tulitegemea kuwa tutajenga nchi ambayo iko chini ya mamlaka ya wakulima na wafanyakazi. Lakini, kama nilivyosema hapa juu, tunazidi kuzama katika ukoloni mamboleo. Wakulima na wafanyakazi, pamoja na washiriki wao, bado wana jukumu la kuendeleza harakati za kutafuta Uhuru wa kweli.

Thursday, August 28, 2014

Marekani Hata Wazee Wananunua na Wanasoma Vitabu

Kama nilivyoandika katika blogu hii, nilishiriki tamasha la tamaduni za kimataifa lililofanyika mjini Faribault tarehe 23 mwezi huu. Kati ya mambo niliyoelezea ni shughuli niliyofanya ya kusaini vitabu, na kati ya picha nilizoweka, ni hiyo inayoonekana hapa kushoto, ambayo inamwonesha mama mmoja mzee niliyekuwa namsainia nakala ya Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, aliyokuwa ameinunua hapo hapo.

Sijui kama jambo hili linaweza kutokea mahali kama Tanzania. Kule watu wanachojua ni kuwa vitabu ni kitu kinachowahusu wanafunzi, labda kiwe kitabu cha hadithi, hasa hadithi za kusisimua na za mapenzi. Vitabu vya maarifa ya aina yoyote vinachukuliwa kuwa ni kwa ajili ya wanafunzi, na hao wanafunzi wanatafuta vitabu vinavyotumika mashuleni.

Hapa Marekani, hali ni tofauti. Hata wazee hununua na husoma vitabu. Ukienda kwenye maduka ya vitabu, utawaona. Kwenye matamasha ya vitabu, utawaona. Nenda maktabani, utawaona.

Nasema hayo kutokana na uzoefu wangu. Nisiende mbali. Hapo hapo Faribault nimeshiriki matamasha, mwaka hadi mwaka, na baadhi ya watu waliofika kwenye meza yangu na kununua vitabu ni wazee.

Tarehe 11 Oktoba, kutakuwepo na maonesho makubwa ya vitabu mjini St. Paul. Nimeshiriki maonesho hayo mwaka hadi mwaka, na nimewaona wazee, sambamba na watu wazima, vijana, na watoto. Nina uhakika kuwa hiyo tarehe 11 Oktoba, wazee watakuwepo.

Kuna mambo ya kujifunza hapo. Jambo moja ni lile alilotufundisha Mwalimu Nyerere, kuwa elimu haina mwisho. Lakini, kwa ujumbe kama huu, sitegemei kuwa jamii yetu ya Tanzania itashtuka au kubadilika hima. Hali ni mbaya sana. Itachukua miaka mingi kutokea mabadiliko, ambayo yatabidi yaendane na malezi tofauti kwa watoto wetu. Itabidi wazazi kujijengea utamaduni wa kununua vitabu, kuvisoma, na kuwasomea watoto wao wanapokuwa wadogo kabisa, na kuwakuza katika utamaduni huo, ili hata watakapokuwa wazee, wawe na hamasa ya kununua na kusoma vitabu.

Monday, January 9, 2012

Mabepari wa Venisi: Tafsiri ya Julius Nyerere

Wiki kadhaa zilizopita, mawazo yangu yalitekwa sana na kumbukumbu za tafsiri za tamthilia za Shakespeare zilizofanywa na Julius Nyerere. Nilipata hamu ya kuziangalia na kuzisoma. Kwa kuanzia, niliagiza nakala ya Mabepari wa Venisi.

Kama nakumbuka sawa sawa, tulisoma The Merchant of Venice tulipokuwa kidatu cha nne. Tulikuwa tunafahamu ki-Ingereza kiasi cha kuweza kusoma na kuelewa maandishi hayo ya Shakespeare. Ni tofauti na leo, ambapo uvivu na uzembe vimesababisha ufahamu wa ki-Ingereza udidimie sana na hata kutoweka. Uvivu huo unajitokeza pia katika ufahamu wa ki-Swahili.

Nyerere aliichapisha tafsiri yake mwaka 1969, muda mfupi tu baada ya Azimio la Arusha. Kwa hivi, tafsiri yake ilikuwa na mvuto wa pekee miongoni mwetu, kwani tulikuwa tunavutiwa na nadharia za ujamaa. Hata neno mabepari lilikuwa likitumika sana, sambamba na maneno kama mabwanyenye. Ilikuwa rahisi kuelewa kwa nini Nyerere aliamua kuitafsiri tamthilia hii ya Shakespeare. Kwa kutumia tabia, fikra, na kauli za Shailoki, mfanyabiashara wa Venisi, Shakespeare alionyesha kwa umahiri mwenendo wa ubepari. Shailoki ni kielelezo bora cha dhana ya Nyerere kuwa ubepari ni unyama.

Mwanzoni mwa kitabu cha Mabepari wa Venisi kuna picha ya Shailoki, iliiyochorwa na Sefania Tunginie. Picha hii nayo inanikumbusha enzi za ujana wangu, nilivyokuwa naiangalia. Mimi mwenyewe nilikuwa mchoraji, na nilikuwa navutiwa na picha za wachoraji kama Sefania Tunginie, Sam Ntiro, na Elias Jengo.

Nimekumbuka hayo yote, na nimekitafuta kitabu cha Mabepari wa Venisi ili kujikumbusha umahiri wa Nyerere katika lugha ya ki-Ingereza na ki-Swahili. Kama kweli unakijua ki-Ingereza na ki-Swahili, huwezi ukasoma tafsiri ya Nyerere usikiri kuwa alikuwa na akili na ufahamu usio wa kawaida wa undani wa lugha hizo mbili. Hata hivi, kama wewe ni mtu makini sana, unaweza kubadili neno hapa au pale, katika tafsiri ya Nyerere. Angalia, kwa mfano, alivyotafsiri maneno ya Antonio, mwanzoni kabisa mwa tamthilia:



Ant. In sooth, I know not why I am so sad.
It wearies me; you say it wearies you;
But how I caught it, found it, or came by it,
What stuff 'tis made of, whereof it is born,
I am to learn;
And such a want-wit sadness make of me
That I have much ado to know myself.

Tafsiri ya Nyerere ni hii:

ANTONIO: Kusema kweli sijui kisa cha huzuni yangu;
Inanitabisha sana; wasema yakutabisha;
Bali nilivyoipata, au kuiambukizwa,
Au imejengekaje, imezawa jinsi gani,
Ningali sijafahamu,
Na huzuni yanifanya kuwa kama punguani,
Kunifanya nisiweze kujifahamu mwenyewe.

Kama nilivyosema, miaka ya ujana wetu, tuliweza kuelewa lugha ya Shakespeare, tena kwa undani. Leo sijui ni wa-Tanzania wangapi wanaoweza kumwelewa Shakespeare. Ngoja nilete kisehemu cha hotuba maarufu ya Portia, halafu ujaribu kutafsiri, uone unakifahamu ki-Ingereza na ki-Swahili kiasi gani:

Por. The quality of mercy is not strained,
It droppeth as the gentle rain from heaven
Upon the place beneath. It is twice blest--
It blesseth him that gives, and him that takes.
'Tis mightiest in the mightiest. It becomes
The throned monarch better than his crown.
His sceptre shows the force of temporal power,
The attribute to awe and majesty,
Wherein doth sit the dread and fear of kings;
But mercy is above this sceptred sway,
It is enthroned in the hearts of kings,
It is an attribute to God himself;
And earthly power doth then show likest God's
When mercy seasons justice.


Tuesday, April 5, 2011

Mwalimu Nyerere Aongelea Uongozi, 1995

Suala la uongozi lilikuwa moja ya vipaumbele vya Mwalimu Nyerere maisha yake yote. Tunasikia, kwa mfano, jinsi alivyolichukulia suala hili alipokuwa kiongozi wa wanafunzi katika shule ya Tabora. Wakati wa kupigania Uhuru na baada ya Uhuru aliliongelea suala hili tena na tena, kama vile katika "Azimio la Arusha" na "Mwongozo."

Mwalimu aliliongelea suala hili tena, kwa masikitiko, katika kitabu chake cha "Uongozi Wetu na Hatima ya Tanzania," akiihofia hatima ya Tanzania kutokana na uongozi mbovu wa CCM. Niligusia suala hilo katika makala hii hapa. Hata baada ya kuandika kitabu hiki, Mwalimu aliendelea kuongelea suala la uongozi. Hebu msikilize katika hotuba yake hii ya mwaka 1995.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...