Showing posts with label dhamira. Show all posts
Showing posts with label dhamira. Show all posts

Saturday, November 19, 2016

"Ozymandias:" Shairi la Shelley na Tafsiri Yangu

Percy Bysshe Shelley ni mmoja kati ya washairi maarufu kabisa katika ki-Ingereza, ambaye nilimtaja jana katika blogu hii. Alizaliwa mwaka 1792 akafariki mwaka 1822. Ni mmoja wa washairi wanaojumlishwa katika mkondo uitwao "Romanticism," ambamo wanaorodheshwa pia washairi wa ki-Ingereza kama William Blake, William Wordsworth, Samuel Taylor Coleridge, na Lord Byron. "Romanticism" ni mkondo uliojitokeza katika mataifa na lugha zingine pia, kama vile Ujerumani na Ufaransa. Kwa waandishi wa Afrika au wenye asili ya Afrika waliotumia ki-Faransa, "Romanticism" ilijitokeza kama "Negritude," jambo ambalo nimeelezea katika mwongozo wa Song of Lawino.

"Ozymandias" ni shairi mojawapo maarufu la Shelley. Ninakumbuka kuwa nililisoma kwa mara ya kwanza nilipokuwa sekondari, miaka ya kuanzia 1967. Kitu kimoja kinacholitambulisha shairi hili kuwa ni la mkondo wa "Romanticism" ni ule mtazamo wake ambao Edward Said aliuita "Orientalism." Lengo langu hapa si kuongelea "Romanticism" wala "Orientalism," bali kutaja mambo mawili matatu yanayohusu shairi la "Ozymandias" na suala la tafsiri.

Suala la kutafsiri kazi za fasihi nimeliongea tena na tena katika blogu hii. Pamoja na ugumu wake, ninaona kuwa baada ya mahangaiko yote, inakuja raha ya aina yake. Sio raha au furaha inayotujia tunaposhinda shindano au mtihani, kwani katika kutafsiri hakuna ushindi. Kinachotokea ni kuwa mtu unafanikiwa kuuzalisha upya utungo unaowania kuutafsiri.

"Ozymandias" ni shairi ambalo ninalielewa vizuri kabisa lilivyo katika ki-Ingereza. Lakini, nilivyojaribu kulitafsiri, tangu jana, limenihangaisha. Nimejionea jinsi ufahamu wangu wa ki-Swahili unavyopwaya. Nimejikuta nikijiuliza iwapo madai yetu wa-Tanzania kuwa tunakifahamu vizuri ki-Swahili ni ya kweli au ni porojo. Nilipata taabu zaidi kutafsiri mstari wa tano na mistari mitatu ya mwisho. Pamoja na kwamba nimeweka tafsiri yangu hapa, siridhiki nayo.

Kuhusu dhamira, shairi la "Ozymandias" lina mengi ya kujadiliwa. Kwa mtazamo wa fasihi linganishi, dhamira ya kisa cha msafiri inajitokeza katika tungo nyingi za tangu zamani. Mfano moja ni hadithi ya Misri ya kale iitwayo "The Tale of the Shipwrecked Sailor." Kuna pia hadithi za baharia Sindbad. Pia kuna shairi la Samuel Taylor Coleridge, "The Rime of the Ancient Mariner." Tungo zote hizi zina mambo ya ajabu na mtazamo juu ya ulimwengu na tabia za binadamu.

Vile vile, "Ozymandias" ni shairi lenye ujumbe mzito. Ni onyo kwa wanadamu kuwa utukufu wa hapa duniani, uimara wa himaya au udikteta ni vitu ambavyo vina mwisho. Ujumbe huu umo pia katika tungo zingine maarufu, kama vile utenzi wa Al Inkishafi. Naishia hapo.
--------------------------------------------------------------------------------------------------------

Ozymandias

Percy Bysshe Shelley, 1792-1822

I met a traveller from an antique land,
Who said: "Two vast and trunkless legs of stone
Stand in the desert.... Near them, on the sand,
Half sunk, a shattered visage lies, whose frown,
And wrinkled lip, and sneer of cold command,
Tell that its sculptor well those passions read
Which yet survive, stamped on these lifeless things,
The hand that mocked them, and the heart that fed;
And on the pedestal, these words appear:
'My name is Ozymandias, King of Kings;
Look on my Works, ye Mighty and despair!'
Nothing beside remains. Round the decay
Of that colossal Wreck, boundless and bare
The lone and level sands stretch far away."

Tafsiri

Nilimkuta msafiri kutoka nchi ya kale
Ambaye alisema, "Miguu miwili ya mawe mikubwa sana isiyo na kiwiliwili
Imesimama jangwani....Karibu nayo, mchangani,
Ukiwa umezama nusu, uso uliopasuka vipande umelala, mnuno wake,
Na mdomo uliokunyata, na dhihaka ya mamlaka yabisi
Vyabainisha kwamba mchongaji alizifahamu sawasawa hisia zile
Ambazo bado zimedumu, zikiwa zimebandikwa katika vitu hivi visivyo hai,
Mkono uliovidhihaki, na moyo uliovilisha,
Na kwenye sehemu ya kusimamia yanaonekana maneno haya:
'Jina langu ni Ozymandias, Mfalme wa Wafalme:
Yaoneni niliyofanikisha, enyi wenye mamlaka makuu, mkate tamaa!'
Hakuna kilichosalia, pembeni mwa uharibifu
Wa ile sanamu kuu iliyoporomoka, bila upeo bila chochote
Mchanga mpweke umetanda hadi mbali kabisa."

Monday, April 25, 2016

Kumbukumbu ya Kifo cha Shakespeare

Wiki hii ni ya kumbukumbu ya kifo cha William Shakespeare. Ingawa siku ya kufariki kwake haijulikani kwa uhakika, mapokeo yameiteua tarehe 23 April, 1616, kuwa ndio siku ya kufariki kwake. Alizikwa tarehe 25 Aprili.

Sisi tuliosoma sekondari miaka ya sitini na kitu tuliweza kusoma maandishi ya Shakespeare na kuyafurahia. Tulisoma tamthilia kama Julius Caesar na The Merchant of Venice. Baada sekondari, sisi tuliokwenda "high school" tulipata fursa ya kusoma na kutafakari tamthilia zake ngumu zaidi, kama vile Hamlet na Othello.

Mwandishi maarufu wa ki-Swahili, Shaaban Robert, alimwenzi Shakespeare. Alisema kwamba akili ya Shakespeare ilikuwa kama bahari ambayo mawimbi yake yalitua kwenye fukwe duniani kote. Laiti kama wa-Tanzania tungefuata nyayo za Shaaban Robert, tukaachana na ufinyu wa fikra kuhusu umuhimu wa lugha mbali mbali na fasihi za ulimwengu, kwa kisingizio cha kukienzi ki-Swahili.

Maandishi ya Shakespeare yana kauli nyingi maarufu. Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Hamlet inayoanza hivi:

To be, or not to be: that is the question:
Whether 'tis nobler in the mind to suffer
The slings and arrows of outrageous fortune,
Or to take arms against a sea of troubles,
And by opposing end them? To die: to sleep;
No more; and by a sleep to say we end
The heart-ache and the thousand natural shocks
That flesh is heir to, 'tis a consummation
Devoutly to be wish'd.

Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Mark Antony iliyomo katika Julius Caesar, inayoanza hivi:

Friends, Romans, countrymen, lend me your ears;
I come to bury Caesar, not to praise him.
The evil that men do lives after them;
The good is oft interréd with their bones;
So let it be with Caesar. The noble Brutus
Hath told you Caesar was ambitious:
If it were so, it was a grievous fault,
And grievously hath Caesar answer'd it.

Kuna pia kauli maarufu katika tamthilia ya As You Like It, ambayo ni ya mhusika aitwaye Jaques. Anasema kuwa dunia ni jukwaa, ambapo kila binadamu ni kama mwigizaji:

All the world’s a stage,
And all the men and women merely players;
They have their exits and their entrances,
And one man in his time plays many parts,
His acts being seven ages.

Shakespeare aliona mbali. Kwa mfano, unaposoma The Merchant of Venice, unajionea jinsi Shakespeare alivyokuwa na upeo wa fikra wa kutambua tabia ya ubepari mapema kabisa, wakati ulipokuwa unachimbuka. Haishangazi kwa nini Mwalimu Nyerere, ambaye alikuwa katika harakati za kupambana na ubepari na kujenga ujamaa aliamua kuitafsiri tamthilia hii, akaiita Mabepari wa Venisi.

Shakespeare alizielezea kwa umakini tabia za binadamu, njema au mbaya. Katika tamthilia ya Macbeth, kwa mfano, tunashuhudia jinsi binadamu anavyoweza kuwa mbaya, na kama wewe ni msomaji wa Shaaban Robert utakumbuka jinsi naye alivyoielezea dhamira hii, kwa mfano katika Adili na Nduguze.

Shakespeare alikuwa mtunzi wa tamthilia na mashairi. Alitunga mashairi mengi, na baadhi ya hayo yako katika tamthilia zake. Haiwezekani kumtendea haki Shakespeare kwa kuelezea mchango wake katika makala ndogo kama hii. Kuna makala nyingi na vitabu juu yake na kazi zake, na maandishi yanaendelea kuchapishwa katika lugha nyingi. 

Kama Shaaban Robert alivyosema, akili ya Shakespeare ni kama bahari, ambayo mawimbi yake yanatua kwenye fukwe duniani kote. Ni miaka mia nne imepita tangu Shakespeare afariki, lakini mawimbi ya akili yake yataendelea kumwagika duniani kote.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...