Showing posts with label Shaaban Robert. Show all posts
Showing posts with label Shaaban Robert. Show all posts

Monday, April 25, 2016

Kumbukumbu ya Kifo cha Shakespeare

Wiki hii ni ya kumbukumbu ya kifo cha William Shakespeare. Ingawa siku ya kufariki kwake haijulikani kwa uhakika, mapokeo yameiteua tarehe 23 April, 1616, kuwa ndio siku ya kufariki kwake. Alizikwa tarehe 25 Aprili.

Sisi tuliosoma sekondari miaka ya sitini na kitu tuliweza kusoma maandishi ya Shakespeare na kuyafurahia. Tulisoma tamthilia kama Julius Caesar na The Merchant of Venice. Baada sekondari, sisi tuliokwenda "high school" tulipata fursa ya kusoma na kutafakari tamthilia zake ngumu zaidi, kama vile Hamlet na Othello.

Mwandishi maarufu wa ki-Swahili, Shaaban Robert, alimwenzi Shakespeare. Alisema kwamba akili ya Shakespeare ilikuwa kama bahari ambayo mawimbi yake yalitua kwenye fukwe duniani kote. Laiti kama wa-Tanzania tungefuata nyayo za Shaaban Robert, tukaachana na ufinyu wa fikra kuhusu umuhimu wa lugha mbali mbali na fasihi za ulimwengu, kwa kisingizio cha kukienzi ki-Swahili.

Maandishi ya Shakespeare yana kauli nyingi maarufu. Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Hamlet inayoanza hivi:

To be, or not to be: that is the question:
Whether 'tis nobler in the mind to suffer
The slings and arrows of outrageous fortune,
Or to take arms against a sea of troubles,
And by opposing end them? To die: to sleep;
No more; and by a sleep to say we end
The heart-ache and the thousand natural shocks
That flesh is heir to, 'tis a consummation
Devoutly to be wish'd.

Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Mark Antony iliyomo katika Julius Caesar, inayoanza hivi:

Friends, Romans, countrymen, lend me your ears;
I come to bury Caesar, not to praise him.
The evil that men do lives after them;
The good is oft interréd with their bones;
So let it be with Caesar. The noble Brutus
Hath told you Caesar was ambitious:
If it were so, it was a grievous fault,
And grievously hath Caesar answer'd it.

Kuna pia kauli maarufu katika tamthilia ya As You Like It, ambayo ni ya mhusika aitwaye Jaques. Anasema kuwa dunia ni jukwaa, ambapo kila binadamu ni kama mwigizaji:

All the world’s a stage,
And all the men and women merely players;
They have their exits and their entrances,
And one man in his time plays many parts,
His acts being seven ages.

Shakespeare aliona mbali. Kwa mfano, unaposoma The Merchant of Venice, unajionea jinsi Shakespeare alivyokuwa na upeo wa fikra wa kutambua tabia ya ubepari mapema kabisa, wakati ulipokuwa unachimbuka. Haishangazi kwa nini Mwalimu Nyerere, ambaye alikuwa katika harakati za kupambana na ubepari na kujenga ujamaa aliamua kuitafsiri tamthilia hii, akaiita Mabepari wa Venisi.

Shakespeare alizielezea kwa umakini tabia za binadamu, njema au mbaya. Katika tamthilia ya Macbeth, kwa mfano, tunashuhudia jinsi binadamu anavyoweza kuwa mbaya, na kama wewe ni msomaji wa Shaaban Robert utakumbuka jinsi naye alivyoielezea dhamira hii, kwa mfano katika Adili na Nduguze.

Shakespeare alikuwa mtunzi wa tamthilia na mashairi. Alitunga mashairi mengi, na baadhi ya hayo yako katika tamthilia zake. Haiwezekani kumtendea haki Shakespeare kwa kuelezea mchango wake katika makala ndogo kama hii. Kuna makala nyingi na vitabu juu yake na kazi zake, na maandishi yanaendelea kuchapishwa katika lugha nyingi. 

Kama Shaaban Robert alivyosema, akili ya Shakespeare ni kama bahari, ambayo mawimbi yake yanatua kwenye fukwe duniani kote. Ni miaka mia nne imepita tangu Shakespeare afariki, lakini mawimbi ya akili yake yataendelea kumwagika duniani kote.

Sunday, January 24, 2016

Nimemkumbuka Shakespeare

Leo, bila kutegemea, nimemkumbuka Shakespeare. Nimeona niandike neno juu yake, kama nilivyowahi kufanya. Nimekumbuka tulivyosoma maandishi yake tukiwa vijana katika shule ya sekondari.

Katika kiwango kile, tulisoma tamthilia tulizozimudu, kama The Merchant of Venice na Julius Caesar. "High school," ambayo kwangu ilikuwa Mkwawa, tulisoma tamthilia ngumu zaidi, kama Othello na Hamlet. Othello ilikuwa katika silabasi ya "Literature."

Nakumbuka sana kuwa hapo hapo Mkwawa High School tuliangalia filamu ya Hamlet, ambamo aliyeigiza kama Hamlet alikuwa Sir Lawrence Olivier. Huyu ni mmoja wa waigizaji maarufu kabisa wa wahusika wakuu wa Shakespeare. Niliguswa na uigizaji wake kiasi cha kujiaminisha kwamba sitaweza kushuhudia tena uigizaji uliotukuka namna ile. Nilipoteza hamu ya kuangalia filamu yoyote baada ya pale, kwa miaka mingi.

Ninavyomkumbuka Shakespeare, ninajikuta nikikumbuka mambo mengi. Kwa mfano, nakumbuka tafsiri murua za Mwalimu Julius Nyerere za tamthilia mbili za Shakespeare: The Merchant of Venice na Julius Caesar. Nakumbuka pia jinsi Shaaban Robert alivyomsifu Shakespeare, kwamba akili yake ilikuwa kama bahari pana ambayo mawimbi yake yalikuwa yanatua kwenye fukwe zote duniani.

Shaaban Robert alitoboa ukweli; Shakespeare ni mwalimu asiye na mfano. Aliingia katika nafsi za wanadamu akaelezea silika na tabia zao kwa ustadi mkubwa, na alitafakari uhalisi wa maisha yetu akatuonyesha maana na mapungufu yake. Alitukumbusha kwamba dunia ni kama jukwaa la maigizo, ambapo kila mmoja wetu anakuja na kutimiza yanayomhusu na kisha anatoweka.

Ningeweza kusema mengi juu ya Shakespeare. Ninapenda tu kuleta moja ya tungo zake ziitwazo "sonnets." Hii ni "sonnet" namba 2. Labda kuna siku nitapata hamu ya kuutafsiri utumgo huu, kujipima uwezo wangu wa kutafsiri na ufahamu wangu wa ki-Swahili.

Sonnet 2

When forty winters shall besiege thy brow
And dig deep trenches in thy beauty’s field,
Thy youth’s proud livery, so gazed on now,
Will be a tattered weed, of small worth held.
Then being asked where all thy beauty lies,
Where all the treasure of thy lusty days,
To say within thine own deep-sunken eyes
Were an all-eating shame and thriftless praise.
How much more praise deserved thy beauty’s use
If thou couldst answer, “This fair child of mine
Shall sum my count and make my old excuse,”
Proving his beauty by succession thine.
  This were to be new made when thou art old,
  And see thy blood warm when thou feel’st it cold.

Sunday, August 9, 2015

Shaaban Robert na Mbaraka Mwinshehe Waliongelea Umuhimu wa Shule

Nikiachilia mbali jinsi wazazi wangu walivyohimiza elimu, nikiachilia mbali jinsi Mwalimu Nyerere alivyohimiza elimu, naukumbuka kwa namna ya pekee mchango wa mwandishi Shaaban Robert na mwanamuziki Mbaraka Mwinshehe katika kuhimiza elimu.

Ninakumbuka jinsi baba yangu, nilipokuwa shule ya msingi, alivyokuwa ananitia msukosuko iwapo nilishindwa kupata 100% katika zoezi lolote au mtihani wowote. Ninakumbuka pia jinsi Mwalimu Nyerere alivyokuwa anahimiza elimu, kwa watu wote, kuanzia watoto hadi wazee, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii.

Shaaban Robert ni mtu anayenifanya nimkumbuke baba yangu. Nilijionea hayo niliposoma kitabu kiitwacho Barua za Shaaban Robert, ambacho habari zake niliziandika katika blogu hii. Humo tunaona jinsi Shaaban Robert alivyokuwa anamhamasisha mdogo wake Yusuf Ulenge afanye bidii katika elimu, akimtimizia mahitaji yote ya shule. Kwa wazazi na walezi, Shaaban Robert ni mfano wa kuigwa.

Mbaraka Mwinshehe, mwanamuziki ambaye wakati wa ujana wangu alitingisha Afrika Mashariki, ya Kati, na Kusini kwa nyimbo na muziki wake, aliimba wimbo maarufu wa kuwaasa vijana wazingatie elimu. Wimbo huo, "Enyi Vijana Sikilizeni," unaweza kuusikiliza hapa:

https://archive.org/details/EnyiVijanaSikilizeni

Wednesday, June 3, 2015

Nadharia ya Uandishi

Uandishi ni nini? Je, kila uandishi ni uandishi wa kweli? Uandishi wa kweli ni nini? Naona haya ni masuali ya msingi. Ningependa tuyatafakari. Waandishi wengi maarufu wameandika kuhusu masuala hayo. Katika kitabu chake, Letters to a Young Novelist, Mario Vargas Llosa, mwandishi maarufu kutoka Peru, aliandika:

The defining characteristic of the literary vocation may be that those who possess it experience the exercise of their craft as its own best reward, much superior to anything they might gain from the fruits of their labors. That is one thing I am sure of amid my many uncertainties regarding the literary vocation: deep inside, a writer feels that writing is the best thing that ever happened to him, or could ever happen to him, because as far as he is concerned, writing is the best possible way of life, never mind the social, political, or financial rewards of what he might achieve through it.

Nitafsiri kwa ki-Swahili:

Utambulisho mahsusi wa wito wa uandishi labda ni kwamba wale wenye wito huo huutambua uandishi kama tunu kubwa kuliko zote, bora kuliko chochote wanachoweza kukipata kutokana na juhudi yao. Hiki ni kitu kimoja ambacho nina uhakika nacho ingawa nimezingirwa na masuali yaletayo wasiwasi kuhusu wito wa uandishi: ndani ya nafsi yake, mwandishi hujisikia kuwa uandishi ni kitu bora kabisa kumtokea au kinachoweza kumtokea, kwa sababu kwa mtazamo wake, uandishi ni mkondo bora kabisa wa maisha, bila kujali manufaa ya kijamii, kisiasa, au kifedha anayoweza kuyapata kwa uandishi.

Kama ilivyo tafsiri yoyote, tafsiri yangu hainasi kila kipengele cha ujumbe wa mwandishi, hasa tukizingatia kuwa tafsiri yangu ni tafsiri ya tafsiri, kwani Mario Vargas Llosa aliandika kwa ki-Hispania. Hata hivi naamini kuna mambo muhimu yanayojitokeza. Mfano ni msisitizo kuwa uandishi kwa wenyewe ni tunu ya thamani kuliko zote. Ni kama kusema kuwa uandishi wa kweli ni ule unaomletea mwandishi faraja kamili na kumfanya asijali matokeo mengine ya uandishi wake, kama vile sifa na fedha.

Nilipokinunua kitabu hiki cha Mario Vargas Llosa, miaka michache iliyopita, nilianza kukisoma nikakutana na dhana fulani ambazo nilishakutana nazo katika maandishi ya Shaaban Robert. Waandishi maarufu wa lugha yoyote ni watu wenye utajiri wa fikra. Hili ni fundisho kwa waandishi chipukizi.

Wakati huu ninaposoma Letters to a Young Novelist, ninasoma pia The Naïve and the Sentimental Novelist, kitabu cha Orhan Pamuk, ambacho nilikinunua hivi karibuni. Orhan Pamuk ni mwandishi maarufu wa U-Turuki, ambaye alipata tuzo ya Nobel. Kitabu chake hiki nacho kinaelezea mtazamo wake kuhusu uandishi. Niliwahi kumtaja mwandishi huyu katika blogu hii, katika kulalamika kuwa maisha hayaturuhusu kusoma vitabu vyote muhimu.

Tuesday, May 12, 2015

Vitabu vya Shaaban Robert

Jina la Shaaban Robert ni maarufu miongoni mwa wa-Tanzania na wengine wa nchi zingine wanaokijua ki-Swahili. Lakini, tujiulize ni wa-Tanzania wepi ambao wamesoma angalau vitabu vichache vya Shaaban Robert. Ni wangapi wamesoma au wanasoma mashairi yake, tenzi zake, insha zake, barua zake, na riwaya zake?

Ni wangapi wamesoma vitabu vyake vingine, kama vile Wasifu wa Siti Binti Saad, Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini, na tafsiri yake ya mashairi ya Omar Khayyam? Kama hatuna majibu ya kuridhisha, tuache kujigamba, kujidanganya na kudanganyana kuwa tunamwenzi mwandishi wetu huyu maarufu.

Ingawa kulikuwa na kipindi cha uhaba, leo vitabu vya Shaaban Robert vinapatikana kirahisi Tanzania, baada ya kampuni ya uchapishaji ya Mkuki na Nyota kuanza kuvichapisha upya. Mwaka hadi mwaka, ninapokwenda Tanzania, nimekuwa nikijinunulia vitabu hivyo, kama hivi vinavyoonekana pichani, sambamba na vitabu vya waandishi wengine maarufu katika lugha ya ki-Swahili.

Imekuwa ni faraja kwangu kuvisoma, baada ya kuzinduka kutoka katika mazoea ya kusoma zaidi maandishi ya ki-Ingereza. Ninajiona kama vile nimeanza kujikomboa kimawazo. Lugha yako ni utambulisho wako, na kuifahamu na kuitumia vizuri ni ishara ya kuiheshimu lugha hiyo. Ni ishara ya kujiheshimu.

Pamoja na kununua na kusoma vitabu alivyoandika Shaaban Robert, ninajitahidi kupanua akili yangu kwa namna nyngine pia. Ninayo maandishi yanayochambua maandishi ya Shaaban Robert. Mfano ni vitabu vinavyoonekana hapa pichani, kimoja cha A.G. Gibbe, na kingine cha Clement Ndulute. Maandishi mengine yamo katika majarida na vitabu vingine ambavyo baadhi ninavyo pia.

Ninajitahidi, kwa uwezo wangu, kushiriki katika kuandika kuhusu kazi za Shaaban Robert. Nimechapisha insha juu ya Shaaban Robert katika Encyclopaedia of African Literature iliyohaririwa na Simon Gikandi. Katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, kuna pia insha yangu iitwayo "Shaaban Robert: Mwalimu wa Jamii." Kadiri nitakavyokuwa naendelea kusoma maandishi yake, nategemea kuandika zaidi. Nina nafasi nzuri ya kufanya hivyo kwa kuwa ni mwalimu wa fasihi za kimataifa na nadharia ya fasihi.

Monday, April 6, 2015

Bemidji Yamwenzi Mary, Mke wa Hemingway

Jioni ya tarehe 4 Aprili, baada ya kurejea kutoka Leech Lake Tribal College karibu na mji wa Bemidji, niliingia mtandaoni nikiwa na lengo la kuona kama kuna taarifa zozote kuhusu mkutano wetu. Katika ukurasa wa Facebook wa Chuo, niliona taarifa na picha za mkutano ule:

Hilo lilinivutia. Lakini niliona pia taarifa nyingine, kuhusu namna mji wa Bemidji unavyomwenzi Mary Welsh, aliyekuwa mke wa nne na wa mwisho wa Ernest Hemingway. Mary Welsh alizaliwa karibu na Bemidji akakulia na kusoma mjini hapo.

Kisha alienda kusoma katika Chuo Kikuu cha Northwestern karibu na Chicago. Alikuja kuwa mwandishi katika magazeti hapo Chicago na hatimaye London, akajipambanua kama mwandishi wa habari za vita. Huko ndiko alikokutana na Ernest Hemingway na baadaye wakafunga ndoa.

Nilifahamu hayo yote na mengine mengi, kutokana na utafiti wangu wa miaka kadhaa. Nilifahamu tangu zamani kuwa Mary Welsh alizaliwa eneo la Bemidji, na nilikuwa nawazia kwenda kule kufanya utafiti juu yake. Mary Welsh Hemingway alitanguzana na Ernest Hemingway katika safari ya Afrika Mashariki mwaka 1953-54. Walizunguka Kenya, Tanganyika, hadi Uganda, ambako walipata ajali mbili za ndege, mfululizo.

Mary Hemingway alisafiri hadi Mbeya, na ameelezea hayo na mengi mengine katika kitabu chake kiitwacho How it Was. Nasikitika kuwa wa-Tanzania, kwa kukosa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu, hawafahamu hayo. Wangekuwa wana utamaduni huo, wangeweza kutumia habari na maandishi kama haya ya Mary Welsh Hemingway na Hemingway mwenyewe kwa manufaa makubwa, hasa katika utalii. Hali ni mbaya kwamba wa-Tanzania hawashtuki wakielezwa habari za vitabu namna hii. Nimethibitisha hayo, kama nilivyoandika katika blogu hii.

Wenzetu katika nchi kama Cuba, Hispania na Marekani wanafaidika sana na maandishi ya Hemingway. Cuba wanaitunza sana nyumba ya Hemingway, Finca Vigia, na hata baa alimokuwa anakunywa, mjini Havana, ni kivutio kikubwa cha watalii. Kule Hispania kuna mji wa Pamplona ambao ulipata umaarufu duniani na umaarufu huu unaendelea, baada ya Hemingway kuutembelea na kuangalia mchezo wa "bull fighting," akaandika juu yake katika riwaya iitwayo The Sun Also Rises. Maelfu ya watalii wanafurika Pamplona. Hapa Marekani, nyumba alimoishi Hemingway, kama vile kule Oak Park (Illinois)na Key West (Florida), ni vivutio vikubwa kwa watalii.

Hayo ndio yaliyonijia akilini wakati nasoma taarifa ya mji wa Bemidji kumwenzi Mary Welsh Hemingway. Jambo moja kubwa lililoelezwa katika taarifa ile ni utunzi wa tamthilia juu ya Mary Welsh Hemingway, unaofanywa na Catie Belleveau baada ya utafiti wa muda mrefu.

Hoja sio kwamba ni lazima nasi tujitose na kujishughulisha na Hemingway na mke wake, ingawa kufanya hivyo kungetuletea manufaa kama wanayopata wenzetu wa Cuba, Pamplona, Oak Park na Key West. Ninachotaka kusisitiza ni umuhimu wa kujifunza kutoka kwa hao wenzetu.

Sisi tunao waandishi maarufu kama Mgeni bin Faqihi wa Bagamoyo, aliyetunga Utenzi wa Ras il Ghuli. Je, tunajua habari zake? Tunaye Shaaban Robert. Je, ni wa-Tanzania wangapi wanajua angalau mahali alipozaliwa, sehemu alimoishi, na mahali alipozikwa? Je? wahusika katika wizara za utalii na utamaduni wanafahamu habari hizo? Na je, wanafahamu kuwa taarifa hizo ni hazina ambayo tungeweza kuitumi? Binafsi ninatekeleza wajibu wangu kwa kuandika kuhusu mambo haya, kama nilivyofanya katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, ambacho nitashangaa kikipata wasomaji Tanzania.

Monday, February 23, 2015

Mihadhara ya Mankato ni Kesho

Siku zinakwenda kasi. Naona kama ndoto, kwamba safari yangu ya kwenda Chuo cha South Central, mjini Mankato, kutoa mihadhara ni kesho asubuhi.

Ninangojea kwa hamu kutekeleza majukumu yaliyoko mbele yangu, ambayo ni kwanza kuongea na wanafunzi wanaojiandaa kwa safari ya Afrika Kusini kimasomo, na pili ni kutoa mhadhara kwa jumuia ya chuo ambao mada yake itakuwa "Writing About Americans."

Maongezi yote hayo yatahusu masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake ulimwenguni. Wanafunzi wanaokwenda Afrika Kusini wanajiandaa kuishi na kushughulika na wa-Afrika, katika utamaduni ambao ni tofauti na ule wa Marekani. Utaratibu huu wa maandalizi, ambao umeshakuwa jambo la kawaida hapa Marekani, ingekuwa bora ufuatwe na wengine, kama nilivyowahi kuwaasa wa-Tanzania wenzangu.

Katika maandalizi hayo, hao wanafunzi wanasoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kitabu ambacho, japo kidogo, kinawagusa watu, tangu nilipokichapisha, tarehe 5 Februari, 2005. Namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kukiandika kama nilivyoandika, hadi kimekuwa msingi wa mialiko ya kwenda kuongelea yaliyomo na yatokanayo.

Katika mhadhara wa "Writing About Americans," ninapangia kuelezea mchakato wa kuandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kuanzia chimbuko la wazo la kukiandika, mchakato wa kukiandika, mambo muhimu niliyojifunza katika kuandika huku, hadi jinsi kitabu kilivyopokelewa na jamii, hasa wa-Marekani, ambao ndio wanaoongoza katika usomaji wake.

Jambo moja kubwa nililojifunza katika kutafakari na kuandika ni kuheshimu tamaduni, pamoja na tofauti zake. Shaaban Robert angeishi miaka mingi zaidi ya ile aliyoishi, angetufundisha mengi kuhusu suala hilo.

Panapo majaliwa, nikikamilisha ziara ya kesho, nitaandika taarifa katika hii blogu yangu.

Friday, December 5, 2014

Kitabu cha "Siasa Hapo Kale"

Ninasoma Siasa Hapo Kale, kitabu ambacho nilikifahamu na kukipenda tangu nilipokuwa nasoma shule ya msingi kule nyumbani kwangu Litembo, katika mkoa wa Ruvuma. Mtunzi wa kitabu hiki ni Lucius Mabasha Thonya. Kama sikosei, nilikuwa na nakala ya kitabu hiki miaka ile kijijini kwangu. Ingawa sijui kilienda wapi, mara moja moja nimekikumbuka, hasa kwa vile mimi ni mtafiti katika fasihi simulizi. Hilo ni jambo moja katika utangulizi wa makala ya leo.

Jambo jingine ni kuwa kwa miaka kadhaa, nimevutiwa na juhudi za Dada Yasinta katika kudumisha lugha ya ki-Ngoni kwa kuanzisha na kuendesha blogu ya Vangoni. Ingawa ki-Ngoni sio lugha yangu, ninaielewa kiasi fulani nikiisikia au kuisoma, kwa vile inakaribiana na lugha yangu ya ki-Matengo.

Katika kusoma blogu ya Vangoni, nilipata wazo la kumwambia Dada Yasinta kuhusu kitabu hiki cha Siasa Hapo Kale. Hatimaye, nilimpelekea ujumbe, nikijua kuwa atapenda kusikia habari zake, na ndivyo ilivyokuwa. Kupitia maktaba ya hapa chuoni ninapofundisha, nilikipata kwa kutumia utaratibu unaotumiwa na maktaba wa kuazimishana vitabu na machapisho mengine, utaratibu uitwao "interlibrary loan."

Nilifurahi kukipata. Nilitengeneza nakala nikampelekea Dada Yasinta, naye aliandika habari hiyo katika blogu yake.

Siasa Hapo Kale ni mkusanyiko wa methali za ki-Ngoni, ambazo mtunzi amezitungia hadithi za kuzielezea. Katika maelezo yake, amefanikiwa vizuri kutupa maana na matumizi ya methali hizi, kwa kutumia maisha na mahusiano ya wahusika katika hadithi hizo. Anahitimisha kila hadithi kwa kusisitiza ujumbe muhimu uliomo katika methali. Kwa maneno yake mtunzi mwenyewe:

Hadithi zilizomo kitabuni humu zimesimuliwa kwa njia ya kubuniwa tu kupatana na mambo yalivyoweza kutokea katika maisha ya watu wa zamani zile. Hadithi hizo zimebuniwa ili kuwaangalisha wasomaji katika matukio ya namna mbalimbali yalivyopata kutokea katika kabila la Wangoni wa wilaya ya Songea iliyopo kusini mwa Tanganyika iliyo karibu na ziwa Nyasa.

Methali hizi zinathibitisha busara za wahenga, yenye falsafa, maadili, na mafundisho muhimu ya maisha. Napenda kunukuu baadhi ya methali, na tafsiri zilizomo kitabuni: "Njala likoko, yikoma na mhavi" (Njaa ni adui, hata mchawi inaua). "Mbanga kufwata manji kwegihamba" (Fuata maji yanakokwenda). "Katumbi ka ngolyongo ikwela mwe ngolyongo" (Utando wa buibui akwea yeye mwenyewe tu). "Mheka pangende kumwoyo lwitimba lungi" (Yu mcheshi machoni moyoni kuna mengine). "Imekela kandumba ka ngemelelu" (Ajivunia dawa ya bahati).

Mwandishi alifanya kazi kubwa ya kufikiri katika kuzitunga hadithi zilizomo kitabuni. Vile vile, ameandika kwa ki-Swahili sanifu, kinachovutia. Kitabu hiki kilichapishwa mwaka 1960, nami nakumbuka kuwa waandishi maarufu kama Shaaban Robert walikuwa bado hai. Miaka ile ya zamani, shirika la uchapishaji la East African Literature Bureau lilikuwa makini katika kuangalia matumizi ya lugha, kabla ya kuchapisha kitabu.

Monday, December 24, 2012

Shaaban Robert na Nyerere: Waandishi Muhimu kwa Kila m-Tanzania

Kwa miaka michache iliyopita, wakati nimejitosa katika kusoma maandishi ya Shaaban Robert, nimejiwa na mawazo mbali mbali ambayo naona ni muhimu. Kwa bahati nzuri, nimechapisha makala mbili juu ya Shaaban Robert, moja katika Encyclopedia of African Literature, na nyingine katika CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Napenda kunukuu machache niliyoandika katika Encyclopedia of African Literature:

Shaaban Robert displayed profound awareness of the human condition; he opposed injustice, championed freedom, and extolled the dignity of labour. He was sensitive to the condition of women. He wrote poems celebrating women, and a biography of Siti Binti Saad, the famous female taarab singer, recounting the meteoric rise to fame of this woman from a humble rural background in a male-dominated world which put incredible obstacles in her path. He was proud of his Swahili language and culture, which he understood very well, appropriated, and celebrated in and through his writings. However, he deeply respected other languages and cultures and appropriated whatever he could from them. If colonialism had not limited his educational opportunities, he would have explored this dimension to the fullest. He greatly admired world writers like Shakespeare, whose artistic mind he described as a great ocean whose waves touched the shores of the whole world....[Shaaban] Robert's poetic sensibility was deep and intertwined with his moral and ethical principles. Sensitive to the condition and plight of all creatures, he held that all things moved with the rhythm of poetry: the birds, streams, the sea, the wind and the thunderstorms, the seasons....His vision of a just society was part of the shaping of the dream for an egalitarian society, which became his country's policy. (p. 463)

Katika kusoma na kutafakari maandishi ya Shaaban Robert, ilifikia wakati nikajenga wazo kuwa kuna uwiano mzito baina ya mafundisho ya Shaaban Robert na yale ya Mwalimu Nyerere. Wakati Nyerere anaongelea sana masuala ya siasa, uchumi, nadharia mbali mbali kuhusu jamii na maendeleo yake, Shaaban Robert aliongelea masuala ya aina hiyo hiyo kwa kutuingiza katika hisia na mahusiano baina ya binadamu na binadamu mwenzake.

Kama Nyerere, Shaaban Robert alikuwa mchambuzi wa jamii na mwanafalsafa, lakini aliongelea masuala kwa kutumia wahusika maalum na matendo na masahibu yao, na hivi kutugusa moja kwa moja. Ningekuwa na madaraka ya kuamua masuala ya mfumo wa elimu Tanzania, ningehakikisha kuwa Shaaban Robert na Nyerere wamekuwa nguzo ya elimu ya kila m-Tanzania.

Wednesday, December 5, 2012

Barua za Ernest Hemingway, 1907-1922

Leo nimekipata kitabu cha barua za Hemingway ambacho nilikitaja katika blogu hii siku chache zilizopita. Kama nilivyoandika, nilikiona kwa mara ya kwanza katika duka la vitabu hapa Chuoni St. Olaf. Lakini nakala ile ilinunuliwa hima, ikabidi niagize.

Hemingway alikuwa mwandishi makini wa barua. Hata mwanae, Mzee Patrick Hemingway, amethibitisha hivyo. Kwa ujumla, Hemingway hakutaka wala kutarajia kuwa barua zake zichapishwe. Alikuwa na mazoea ya kuandika barua zake kwa uwazi na hata kutumia lugha ambayo inaonekana kali au yenye kukiuka maadili.

Baada ya Hemingway kufariki, mwaka 1961, suala la kuchapisha au kutochapisha maandishi ya Hemingway ambayo alikuwa hajayachapisha lilijitokeza na kuwa kubwa. Maandishi yake mengine alikuwa hajamaliza kuyarekebisha. Barua zake alikuwa hajaazimia zichapishwe. Suala likawa nini kifanyike.

Wasomaji wa maandishi ya Hemingway walisukumwa na kiu ya kutaka kusoma maandishi yake yote. Wahariri na watafiti walitaka hivyo pia. Familia yake ilikuwa katika mtihani mgumu. Lakini hatimaye, iliamuliwa kuwa bora kuchapisha maandishi hayo, hata barua zake. Ndivyo tulivyovipata vitabu vya Hemingway kama vile The Garden of Eden, Islands in the Stream, A Moveable Feast, na Under Kilimanjaro. Ni matokeo ya maamuzi magumu, na juhudi za wahariri kuhariri miswada aliyoicha Hemingway ikiwa haijakamilika, wakiongozwa na wazo kwamba bila shaka Hemingway mwenyewe angeafiki uhariri huo.

Tunaposoma vitabu hivi bado tunajiuliza iwapo kama Hemingway angeishi zaidi, angerekebisha vipi maandishi haya, hasa ikizingatiwa kuwa alikuwa mwandishi mwenye nidhamu ya hali isiyo ya kawaida katika kusahihisha na kuboresha maandishi yake. Alitaka kila neno liwe mahali pake na liwe kweli ni neno hilo, si jingine, na kila sentensi iwe imekamilika kwa kiwango cha juu kabisa.

Leo nilitaka nikumbushie pia kitabu cha barua za Shaaban Robert, ambacho niliandika habari zake katika blogu hii. Nilitaka nivijadili vitabu hivi vya barua kwa pamoja, kuelezea umuhimu wa vitabu vya aina hii, ambamo tunapata kuwafahamu waandishi hao maarufu kupitia njia ya barua walizoandika. Barua hizi ni kioo muhimu cha kutuwezesha kuyafahamu mambo ambayo pengine hatungeyafahamu kwa kuangalia tu vitabu vyao vingine. Nangojea nipate wasaa wa kuandika na kuzihusianisha barua za Hemingway na zile za Shaaban Robert.

Saturday, April 2, 2011

Kitabu Kumhusu Hemingway

Leo nilipita tena katika duka la vitabu la Half Price Books la mjini Apple Valley. Kama kawaida, kutokana na ushabiki wangu wa maandishi ya Ernest Hemingway, nilianza kwa kwenda moja kwa moja kwenye sehemu vinapouzwa vitabu vyake: vile alivyoandika yeye mwenyewe au vilivyoandikwa juu yake.

Hadi sasa nina vitabu vingi vya Hemingway, lakini kila ninapoona kitabu kipya, au ambacho sina, napenda niwe nacho. Leo nimevikuta vitabu kadhaa vya aina hiyo, ila nilivutiwa zaidi ni Hemingway in Cuba, kilichoandikwa na Norberto Fuentes.

Sikuwa nimekiona kitabu hiki kabla. Nilikiangalia, nikaona kina utangulizi ulioandikwa na Gabriel Garcia Marquez. Hapo niliishiwa nguvu, kwani Marquez ni mmoja wa waandishi maarufu kabisa duniani.

Mawazo mengine yakafurika akilini mwangu. Ninajua kuwa Marquez ni rafiki mkubwa wa Fidel Castro, Castro ambaye watu wa kizazi changu tumemwenzi tangu tulipopata Uhuru. Najua pia kuwa Castro ni mshabiki wa maandishi ya Marquez. Cha zaidi ni kuwa najua kuwa Hemingway katika uhai wake alifahamiana na Castro, na pia kuwa Castro amekuwa shabiki wa Hemingway tangu miaka ile.

Pamoja na yote hayo, katika kusoma utangulizi wa Marquez, nimevutiwa kwa namna ya pekee na maelezo yake kuwa Hemingway ni mwandishi ambaye Castro anamsoma kuliko mwandishi mwingine yeyote. Hata anapozunguka nchini kwenye safari rasmi, Castro anakuwa na maandishi ya Hemingway. Marquez anatueleza kuwa Castro anaweza kuelezea maandishi ya Hemingway na kujibu masuali kwa uhodari wa kiwango cha juu.

Mimi kama shabiki mkubwa wa Hemingway najiandaa kukisoma kitabu hiki. Nimekipitia juu juu, nikaona kina mengi mapya kwangu, ingawa kilichapishwa mwaka 1984. Nina vitabu vingine vinavyoelezea maisha ya Hemingway Cuba, lakini hiki cha Fuentes kinazama zaidi katika maelezo yake.

Kwa wale ambao hawajui, Hemingway, ambaye ni m-Marekani aliyezaliwa mwaka 1899 karibu na Chicago, aliishi Cuba miaka 22. Hata alivyosafiri kuja Afrika Mashariki, mwaka 1933 na mwaka 1953, alitokea Cuba, na baada ya safari zake alirejea Cuba. Kuna vitu kadhaa alivyovipata Kenya na Tanganyika, kama vile vichwa vya wanyama aliowawinda, mikuki, na kinyago cha ki-Makonde. Vyote viko katika nyumba yake ya Finca Vigia, ambayo iko nje ya mji wa Havana, ambayo serikali ya Cuba inaihifadhi kwa heshima kubwa na vitu vyote vya Hemingway vilivyokuwamo humo, ingawa yeye alishaondoka na kurejea Marekani, ambako alijiua kwa bunduki mwaka 1961.

Cuba inamwenzi Hemingway kwa namna ambayo ingepaswa sisi wa-Tanzania tuwe tunawaenzi waandishi wetu kama vile Mgeni bin Faqihi wa Bagamoyo, aliyetunga Utendi wa Rasi l'Ghuli, au Shaaban Robert.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...