Showing posts with label Mgeni bin Faqihi. Show all posts
Showing posts with label Mgeni bin Faqihi. Show all posts

Monday, April 6, 2015

Bemidji Yamwenzi Mary, Mke wa Hemingway

Jioni ya tarehe 4 Aprili, baada ya kurejea kutoka Leech Lake Tribal College karibu na mji wa Bemidji, niliingia mtandaoni nikiwa na lengo la kuona kama kuna taarifa zozote kuhusu mkutano wetu. Katika ukurasa wa Facebook wa Chuo, niliona taarifa na picha za mkutano ule:

Hilo lilinivutia. Lakini niliona pia taarifa nyingine, kuhusu namna mji wa Bemidji unavyomwenzi Mary Welsh, aliyekuwa mke wa nne na wa mwisho wa Ernest Hemingway. Mary Welsh alizaliwa karibu na Bemidji akakulia na kusoma mjini hapo.

Kisha alienda kusoma katika Chuo Kikuu cha Northwestern karibu na Chicago. Alikuja kuwa mwandishi katika magazeti hapo Chicago na hatimaye London, akajipambanua kama mwandishi wa habari za vita. Huko ndiko alikokutana na Ernest Hemingway na baadaye wakafunga ndoa.

Nilifahamu hayo yote na mengine mengi, kutokana na utafiti wangu wa miaka kadhaa. Nilifahamu tangu zamani kuwa Mary Welsh alizaliwa eneo la Bemidji, na nilikuwa nawazia kwenda kule kufanya utafiti juu yake. Mary Welsh Hemingway alitanguzana na Ernest Hemingway katika safari ya Afrika Mashariki mwaka 1953-54. Walizunguka Kenya, Tanganyika, hadi Uganda, ambako walipata ajali mbili za ndege, mfululizo.

Mary Hemingway alisafiri hadi Mbeya, na ameelezea hayo na mengi mengine katika kitabu chake kiitwacho How it Was. Nasikitika kuwa wa-Tanzania, kwa kukosa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu, hawafahamu hayo. Wangekuwa wana utamaduni huo, wangeweza kutumia habari na maandishi kama haya ya Mary Welsh Hemingway na Hemingway mwenyewe kwa manufaa makubwa, hasa katika utalii. Hali ni mbaya kwamba wa-Tanzania hawashtuki wakielezwa habari za vitabu namna hii. Nimethibitisha hayo, kama nilivyoandika katika blogu hii.

Wenzetu katika nchi kama Cuba, Hispania na Marekani wanafaidika sana na maandishi ya Hemingway. Cuba wanaitunza sana nyumba ya Hemingway, Finca Vigia, na hata baa alimokuwa anakunywa, mjini Havana, ni kivutio kikubwa cha watalii. Kule Hispania kuna mji wa Pamplona ambao ulipata umaarufu duniani na umaarufu huu unaendelea, baada ya Hemingway kuutembelea na kuangalia mchezo wa "bull fighting," akaandika juu yake katika riwaya iitwayo The Sun Also Rises. Maelfu ya watalii wanafurika Pamplona. Hapa Marekani, nyumba alimoishi Hemingway, kama vile kule Oak Park (Illinois)na Key West (Florida), ni vivutio vikubwa kwa watalii.

Hayo ndio yaliyonijia akilini wakati nasoma taarifa ya mji wa Bemidji kumwenzi Mary Welsh Hemingway. Jambo moja kubwa lililoelezwa katika taarifa ile ni utunzi wa tamthilia juu ya Mary Welsh Hemingway, unaofanywa na Catie Belleveau baada ya utafiti wa muda mrefu.

Hoja sio kwamba ni lazima nasi tujitose na kujishughulisha na Hemingway na mke wake, ingawa kufanya hivyo kungetuletea manufaa kama wanayopata wenzetu wa Cuba, Pamplona, Oak Park na Key West. Ninachotaka kusisitiza ni umuhimu wa kujifunza kutoka kwa hao wenzetu.

Sisi tunao waandishi maarufu kama Mgeni bin Faqihi wa Bagamoyo, aliyetunga Utenzi wa Ras il Ghuli. Je, tunajua habari zake? Tunaye Shaaban Robert. Je, ni wa-Tanzania wangapi wanajua angalau mahali alipozaliwa, sehemu alimoishi, na mahali alipozikwa? Je? wahusika katika wizara za utalii na utamaduni wanafahamu habari hizo? Na je, wanafahamu kuwa taarifa hizo ni hazina ambayo tungeweza kuitumi? Binafsi ninatekeleza wajibu wangu kwa kuandika kuhusu mambo haya, kama nilivyofanya katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, ambacho nitashangaa kikipata wasomaji Tanzania.

Saturday, April 2, 2011

Kitabu Kumhusu Hemingway

Leo nilipita tena katika duka la vitabu la Half Price Books la mjini Apple Valley. Kama kawaida, kutokana na ushabiki wangu wa maandishi ya Ernest Hemingway, nilianza kwa kwenda moja kwa moja kwenye sehemu vinapouzwa vitabu vyake: vile alivyoandika yeye mwenyewe au vilivyoandikwa juu yake.

Hadi sasa nina vitabu vingi vya Hemingway, lakini kila ninapoona kitabu kipya, au ambacho sina, napenda niwe nacho. Leo nimevikuta vitabu kadhaa vya aina hiyo, ila nilivutiwa zaidi ni Hemingway in Cuba, kilichoandikwa na Norberto Fuentes.

Sikuwa nimekiona kitabu hiki kabla. Nilikiangalia, nikaona kina utangulizi ulioandikwa na Gabriel Garcia Marquez. Hapo niliishiwa nguvu, kwani Marquez ni mmoja wa waandishi maarufu kabisa duniani.

Mawazo mengine yakafurika akilini mwangu. Ninajua kuwa Marquez ni rafiki mkubwa wa Fidel Castro, Castro ambaye watu wa kizazi changu tumemwenzi tangu tulipopata Uhuru. Najua pia kuwa Castro ni mshabiki wa maandishi ya Marquez. Cha zaidi ni kuwa najua kuwa Hemingway katika uhai wake alifahamiana na Castro, na pia kuwa Castro amekuwa shabiki wa Hemingway tangu miaka ile.

Pamoja na yote hayo, katika kusoma utangulizi wa Marquez, nimevutiwa kwa namna ya pekee na maelezo yake kuwa Hemingway ni mwandishi ambaye Castro anamsoma kuliko mwandishi mwingine yeyote. Hata anapozunguka nchini kwenye safari rasmi, Castro anakuwa na maandishi ya Hemingway. Marquez anatueleza kuwa Castro anaweza kuelezea maandishi ya Hemingway na kujibu masuali kwa uhodari wa kiwango cha juu.

Mimi kama shabiki mkubwa wa Hemingway najiandaa kukisoma kitabu hiki. Nimekipitia juu juu, nikaona kina mengi mapya kwangu, ingawa kilichapishwa mwaka 1984. Nina vitabu vingine vinavyoelezea maisha ya Hemingway Cuba, lakini hiki cha Fuentes kinazama zaidi katika maelezo yake.

Kwa wale ambao hawajui, Hemingway, ambaye ni m-Marekani aliyezaliwa mwaka 1899 karibu na Chicago, aliishi Cuba miaka 22. Hata alivyosafiri kuja Afrika Mashariki, mwaka 1933 na mwaka 1953, alitokea Cuba, na baada ya safari zake alirejea Cuba. Kuna vitu kadhaa alivyovipata Kenya na Tanganyika, kama vile vichwa vya wanyama aliowawinda, mikuki, na kinyago cha ki-Makonde. Vyote viko katika nyumba yake ya Finca Vigia, ambayo iko nje ya mji wa Havana, ambayo serikali ya Cuba inaihifadhi kwa heshima kubwa na vitu vyote vya Hemingway vilivyokuwamo humo, ingawa yeye alishaondoka na kurejea Marekani, ambako alijiua kwa bunduki mwaka 1961.

Cuba inamwenzi Hemingway kwa namna ambayo ingepaswa sisi wa-Tanzania tuwe tunawaenzi waandishi wetu kama vile Mgeni bin Faqihi wa Bagamoyo, aliyetunga Utendi wa Rasi l'Ghuli, au Shaaban Robert.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...