Saturday, April 2, 2011

Kitabu Kumhusu Hemingway

Leo nilipita tena katika duka la vitabu la Half Price Books la mjini Apple Valley. Kama kawaida, kutokana na ushabiki wangu wa maandishi ya Ernest Hemingway, nilianza kwa kwenda moja kwa moja kwenye sehemu vinapouzwa vitabu vyake: vile alivyoandika yeye mwenyewe au vilivyoandikwa juu yake.

Hadi sasa nina vitabu vingi vya Hemingway, lakini kila ninapoona kitabu kipya, au ambacho sina, napenda niwe nacho. Leo nimevikuta vitabu kadhaa vya aina hiyo, ila nilivutiwa zaidi ni Hemingway in Cuba, kilichoandikwa na Norberto Fuentes.

Sikuwa nimekiona kitabu hiki kabla. Nilikiangalia, nikaona kina utangulizi ulioandikwa na Gabriel Garcia Marquez. Hapo niliishiwa nguvu, kwani Marquez ni mmoja wa waandishi maarufu kabisa duniani.

Mawazo mengine yakafurika akilini mwangu. Ninajua kuwa Marquez ni rafiki mkubwa wa Fidel Castro, Castro ambaye watu wa kizazi changu tumemwenzi tangu tulipopata Uhuru. Najua pia kuwa Castro ni mshabiki wa maandishi ya Marquez. Cha zaidi ni kuwa najua kuwa Hemingway katika uhai wake alifahamiana na Castro, na pia kuwa Castro amekuwa shabiki wa Hemingway tangu miaka ile.

Pamoja na yote hayo, katika kusoma utangulizi wa Marquez, nimevutiwa kwa namna ya pekee na maelezo yake kuwa Hemingway ni mwandishi ambaye Castro anamsoma kuliko mwandishi mwingine yeyote. Hata anapozunguka nchini kwenye safari rasmi, Castro anakuwa na maandishi ya Hemingway. Marquez anatueleza kuwa Castro anaweza kuelezea maandishi ya Hemingway na kujibu masuali kwa uhodari wa kiwango cha juu.

Mimi kama shabiki mkubwa wa Hemingway najiandaa kukisoma kitabu hiki. Nimekipitia juu juu, nikaona kina mengi mapya kwangu, ingawa kilichapishwa mwaka 1984. Nina vitabu vingine vinavyoelezea maisha ya Hemingway Cuba, lakini hiki cha Fuentes kinazama zaidi katika maelezo yake.

Kwa wale ambao hawajui, Hemingway, ambaye ni m-Marekani aliyezaliwa mwaka 1899 karibu na Chicago, aliishi Cuba miaka 22. Hata alivyosafiri kuja Afrika Mashariki, mwaka 1933 na mwaka 1953, alitokea Cuba, na baada ya safari zake alirejea Cuba. Kuna vitu kadhaa alivyovipata Kenya na Tanganyika, kama vile vichwa vya wanyama aliowawinda, mikuki, na kinyago cha ki-Makonde. Vyote viko katika nyumba yake ya Finca Vigia, ambayo iko nje ya mji wa Havana, ambayo serikali ya Cuba inaihifadhi kwa heshima kubwa na vitu vyote vya Hemingway vilivyokuwamo humo, ingawa yeye alishaondoka na kurejea Marekani, ambako alijiua kwa bunduki mwaka 1961.

Cuba inamwenzi Hemingway kwa namna ambayo ingepaswa sisi wa-Tanzania tuwe tunawaenzi waandishi wetu kama vile Mgeni bin Faqihi wa Bagamoyo, aliyetunga Utendi wa Rasi l'Ghuli, au Shaaban Robert.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...