Showing posts with label As You Like It. Show all posts
Showing posts with label As You Like It. Show all posts

Monday, April 25, 2016

Kumbukumbu ya Kifo cha Shakespeare

Wiki hii ni ya kumbukumbu ya kifo cha William Shakespeare. Ingawa siku ya kufariki kwake haijulikani kwa uhakika, mapokeo yameiteua tarehe 23 April, 1616, kuwa ndio siku ya kufariki kwake. Alizikwa tarehe 25 Aprili.

Sisi tuliosoma sekondari miaka ya sitini na kitu tuliweza kusoma maandishi ya Shakespeare na kuyafurahia. Tulisoma tamthilia kama Julius Caesar na The Merchant of Venice. Baada sekondari, sisi tuliokwenda "high school" tulipata fursa ya kusoma na kutafakari tamthilia zake ngumu zaidi, kama vile Hamlet na Othello.

Mwandishi maarufu wa ki-Swahili, Shaaban Robert, alimwenzi Shakespeare. Alisema kwamba akili ya Shakespeare ilikuwa kama bahari ambayo mawimbi yake yalitua kwenye fukwe duniani kote. Laiti kama wa-Tanzania tungefuata nyayo za Shaaban Robert, tukaachana na ufinyu wa fikra kuhusu umuhimu wa lugha mbali mbali na fasihi za ulimwengu, kwa kisingizio cha kukienzi ki-Swahili.

Maandishi ya Shakespeare yana kauli nyingi maarufu. Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Hamlet inayoanza hivi:

To be, or not to be: that is the question:
Whether 'tis nobler in the mind to suffer
The slings and arrows of outrageous fortune,
Or to take arms against a sea of troubles,
And by opposing end them? To die: to sleep;
No more; and by a sleep to say we end
The heart-ache and the thousand natural shocks
That flesh is heir to, 'tis a consummation
Devoutly to be wish'd.

Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Mark Antony iliyomo katika Julius Caesar, inayoanza hivi:

Friends, Romans, countrymen, lend me your ears;
I come to bury Caesar, not to praise him.
The evil that men do lives after them;
The good is oft interréd with their bones;
So let it be with Caesar. The noble Brutus
Hath told you Caesar was ambitious:
If it were so, it was a grievous fault,
And grievously hath Caesar answer'd it.

Kuna pia kauli maarufu katika tamthilia ya As You Like It, ambayo ni ya mhusika aitwaye Jaques. Anasema kuwa dunia ni jukwaa, ambapo kila binadamu ni kama mwigizaji:

All the world’s a stage,
And all the men and women merely players;
They have their exits and their entrances,
And one man in his time plays many parts,
His acts being seven ages.

Shakespeare aliona mbali. Kwa mfano, unaposoma The Merchant of Venice, unajionea jinsi Shakespeare alivyokuwa na upeo wa fikra wa kutambua tabia ya ubepari mapema kabisa, wakati ulipokuwa unachimbuka. Haishangazi kwa nini Mwalimu Nyerere, ambaye alikuwa katika harakati za kupambana na ubepari na kujenga ujamaa aliamua kuitafsiri tamthilia hii, akaiita Mabepari wa Venisi.

Shakespeare alizielezea kwa umakini tabia za binadamu, njema au mbaya. Katika tamthilia ya Macbeth, kwa mfano, tunashuhudia jinsi binadamu anavyoweza kuwa mbaya, na kama wewe ni msomaji wa Shaaban Robert utakumbuka jinsi naye alivyoielezea dhamira hii, kwa mfano katika Adili na Nduguze.

Shakespeare alikuwa mtunzi wa tamthilia na mashairi. Alitunga mashairi mengi, na baadhi ya hayo yako katika tamthilia zake. Haiwezekani kumtendea haki Shakespeare kwa kuelezea mchango wake katika makala ndogo kama hii. Kuna makala nyingi na vitabu juu yake na kazi zake, na maandishi yanaendelea kuchapishwa katika lugha nyingi. 

Kama Shaaban Robert alivyosema, akili ya Shakespeare ni kama bahari, ambayo mawimbi yake yanatua kwenye fukwe duniani kote. Ni miaka mia nne imepita tangu Shakespeare afariki, lakini mawimbi ya akili yake yataendelea kumwagika duniani kote.

Sunday, December 28, 2014

"As You Like It:" Kitabu cha Kumalizia Mwaka

Nimeanza kusoma As You Like It, moja ya tamthilia za Shakespeare. Ni wazi kuwa, nikizingatia kwamba leo ni tarehe 28 Desemba, hiki kitakuwa kitabu cha kumalizia mwaka.

Kama zilivyo tamthilia zingine za Shakespeare, As You Like It ni hazina kubwa ya mafundisho kuhusu mahusiano baina ya wanadamu na kuhusu maisha kwa ujumla. Tamthilia yoyote ya gwiji huyu, sawa na mashairi yake, ni hazina ya lugha ya ki-Ingereza.

Ningefurahi kama ningekuwa nimesoma angalau kitabu kimoja kwa kila wiki. Padre Lambert Doerr, OSB, mwalimu wetu wa ki-ingereza tulipokuwa tunasoma seminari ya Likonde, ambaye sasa ni abate askofu mstaafu, alitushinikiza kusoma angalau kitabu kimoja kwa wiki. Kila mmoja wetu alipewa daftari ambamo alitakiwa kuorodhesha vitabu alivyosoma, na alitegemewa kuweza kutoa maelezo mafupi kuhusu kila kitabu. Ningefurahi kama ningeweza kuendeleza jadi hii miaka yote.

Nirudi tena kwenye As You Like It. Simulizi inapoanza, tunamsikia Orlando akilalamika kuwa amedhulumiwa na kaka yake mkubwa, Oliver, kuhusu urithi. Anasema kuwa baba yao aliacha wosia kwamba Oliver amgawie yeye Orlando fungu fulani la mali yake na pia amsomeshe, lakini Oliver hakufanya hvyo. Dhuluma hii inamsononesha Orlando.

Mtindo huu wa kuanzia simulizi na mhusika akielezea masononeko tunauona pia katika tamthilia ya Shakespeare iitwayo The Merchant of Venice. Halafu katika sehemu hii ya mwanzo ya As You Like It kuna pia dhamira ya kiongozi kuporwa madaraka na ndugu yake, dhamira ambayo inajitokeza pia katika The Tempest, tamthilia nyingine ya Shakespeare. Hili suala la Shakespeare kurejea tena na tena kwenye dhamira au kipengele fulani cha sanaa yake nimeligusia kabla katika blogu hii.

Tangu mwanzoni mwa As You Like It, Shakespeare anatuweka katika hamaki ya kujua nini kitakachofuata katika mtiririko wa matukio. Vile vile, kama ilivyo kawaida yake, anatupeleka mbali katika ulimwengu wa fasihi na masimulizi na imani za zamani, kuanzia enzi za wa-Griki hadi wa-Ingereza wenyewe. Mifano ya wahusika wa masimulizi hayo ni Fortune na Robin Hood.

Sijui kama nitaweza kumaliza kusoma tamthilia hii kabla ya mwaka mpya kuanza, lakini nitajitahidi. Jambo moja linalonifanya nisome pole pole ni kuvutiwa na umahiri wa Shakespeare katika kutumia lugha kwa namna ambayo aghalabu haionekani katika ki-Ingereza cha leo. Ni aina ya chemsha bongo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...