Showing posts with label Othello. Show all posts
Showing posts with label Othello. Show all posts

Monday, April 25, 2016

Kumbukumbu ya Kifo cha Shakespeare

Wiki hii ni ya kumbukumbu ya kifo cha William Shakespeare. Ingawa siku ya kufariki kwake haijulikani kwa uhakika, mapokeo yameiteua tarehe 23 April, 1616, kuwa ndio siku ya kufariki kwake. Alizikwa tarehe 25 Aprili.

Sisi tuliosoma sekondari miaka ya sitini na kitu tuliweza kusoma maandishi ya Shakespeare na kuyafurahia. Tulisoma tamthilia kama Julius Caesar na The Merchant of Venice. Baada sekondari, sisi tuliokwenda "high school" tulipata fursa ya kusoma na kutafakari tamthilia zake ngumu zaidi, kama vile Hamlet na Othello.

Mwandishi maarufu wa ki-Swahili, Shaaban Robert, alimwenzi Shakespeare. Alisema kwamba akili ya Shakespeare ilikuwa kama bahari ambayo mawimbi yake yalitua kwenye fukwe duniani kote. Laiti kama wa-Tanzania tungefuata nyayo za Shaaban Robert, tukaachana na ufinyu wa fikra kuhusu umuhimu wa lugha mbali mbali na fasihi za ulimwengu, kwa kisingizio cha kukienzi ki-Swahili.

Maandishi ya Shakespeare yana kauli nyingi maarufu. Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Hamlet inayoanza hivi:

To be, or not to be: that is the question:
Whether 'tis nobler in the mind to suffer
The slings and arrows of outrageous fortune,
Or to take arms against a sea of troubles,
And by opposing end them? To die: to sleep;
No more; and by a sleep to say we end
The heart-ache and the thousand natural shocks
That flesh is heir to, 'tis a consummation
Devoutly to be wish'd.

Sijui kama kuna msomaji wa Shakespeare ambaye hakumbuki ile hotuba ya Mark Antony iliyomo katika Julius Caesar, inayoanza hivi:

Friends, Romans, countrymen, lend me your ears;
I come to bury Caesar, not to praise him.
The evil that men do lives after them;
The good is oft interréd with their bones;
So let it be with Caesar. The noble Brutus
Hath told you Caesar was ambitious:
If it were so, it was a grievous fault,
And grievously hath Caesar answer'd it.

Kuna pia kauli maarufu katika tamthilia ya As You Like It, ambayo ni ya mhusika aitwaye Jaques. Anasema kuwa dunia ni jukwaa, ambapo kila binadamu ni kama mwigizaji:

All the world’s a stage,
And all the men and women merely players;
They have their exits and their entrances,
And one man in his time plays many parts,
His acts being seven ages.

Shakespeare aliona mbali. Kwa mfano, unaposoma The Merchant of Venice, unajionea jinsi Shakespeare alivyokuwa na upeo wa fikra wa kutambua tabia ya ubepari mapema kabisa, wakati ulipokuwa unachimbuka. Haishangazi kwa nini Mwalimu Nyerere, ambaye alikuwa katika harakati za kupambana na ubepari na kujenga ujamaa aliamua kuitafsiri tamthilia hii, akaiita Mabepari wa Venisi.

Shakespeare alizielezea kwa umakini tabia za binadamu, njema au mbaya. Katika tamthilia ya Macbeth, kwa mfano, tunashuhudia jinsi binadamu anavyoweza kuwa mbaya, na kama wewe ni msomaji wa Shaaban Robert utakumbuka jinsi naye alivyoielezea dhamira hii, kwa mfano katika Adili na Nduguze.

Shakespeare alikuwa mtunzi wa tamthilia na mashairi. Alitunga mashairi mengi, na baadhi ya hayo yako katika tamthilia zake. Haiwezekani kumtendea haki Shakespeare kwa kuelezea mchango wake katika makala ndogo kama hii. Kuna makala nyingi na vitabu juu yake na kazi zake, na maandishi yanaendelea kuchapishwa katika lugha nyingi. 

Kama Shaaban Robert alivyosema, akili ya Shakespeare ni kama bahari, ambayo mawimbi yake yanatua kwenye fukwe duniani kote. Ni miaka mia nne imepita tangu Shakespeare afariki, lakini mawimbi ya akili yake yataendelea kumwagika duniani kote.

Sunday, January 24, 2016

Nimemkumbuka Shakespeare

Leo, bila kutegemea, nimemkumbuka Shakespeare. Nimeona niandike neno juu yake, kama nilivyowahi kufanya. Nimekumbuka tulivyosoma maandishi yake tukiwa vijana katika shule ya sekondari.

Katika kiwango kile, tulisoma tamthilia tulizozimudu, kama The Merchant of Venice na Julius Caesar. "High school," ambayo kwangu ilikuwa Mkwawa, tulisoma tamthilia ngumu zaidi, kama Othello na Hamlet. Othello ilikuwa katika silabasi ya "Literature."

Nakumbuka sana kuwa hapo hapo Mkwawa High School tuliangalia filamu ya Hamlet, ambamo aliyeigiza kama Hamlet alikuwa Sir Lawrence Olivier. Huyu ni mmoja wa waigizaji maarufu kabisa wa wahusika wakuu wa Shakespeare. Niliguswa na uigizaji wake kiasi cha kujiaminisha kwamba sitaweza kushuhudia tena uigizaji uliotukuka namna ile. Nilipoteza hamu ya kuangalia filamu yoyote baada ya pale, kwa miaka mingi.

Ninavyomkumbuka Shakespeare, ninajikuta nikikumbuka mambo mengi. Kwa mfano, nakumbuka tafsiri murua za Mwalimu Julius Nyerere za tamthilia mbili za Shakespeare: The Merchant of Venice na Julius Caesar. Nakumbuka pia jinsi Shaaban Robert alivyomsifu Shakespeare, kwamba akili yake ilikuwa kama bahari pana ambayo mawimbi yake yalikuwa yanatua kwenye fukwe zote duniani.

Shaaban Robert alitoboa ukweli; Shakespeare ni mwalimu asiye na mfano. Aliingia katika nafsi za wanadamu akaelezea silika na tabia zao kwa ustadi mkubwa, na alitafakari uhalisi wa maisha yetu akatuonyesha maana na mapungufu yake. Alitukumbusha kwamba dunia ni kama jukwaa la maigizo, ambapo kila mmoja wetu anakuja na kutimiza yanayomhusu na kisha anatoweka.

Ningeweza kusema mengi juu ya Shakespeare. Ninapenda tu kuleta moja ya tungo zake ziitwazo "sonnets." Hii ni "sonnet" namba 2. Labda kuna siku nitapata hamu ya kuutafsiri utumgo huu, kujipima uwezo wangu wa kutafsiri na ufahamu wangu wa ki-Swahili.

Sonnet 2

When forty winters shall besiege thy brow
And dig deep trenches in thy beauty’s field,
Thy youth’s proud livery, so gazed on now,
Will be a tattered weed, of small worth held.
Then being asked where all thy beauty lies,
Where all the treasure of thy lusty days,
To say within thine own deep-sunken eyes
Were an all-eating shame and thriftless praise.
How much more praise deserved thy beauty’s use
If thou couldst answer, “This fair child of mine
Shall sum my count and make my old excuse,”
Proving his beauty by succession thine.
  This were to be new made when thou art old,
  And see thy blood warm when thou feel’st it cold.

Sunday, November 30, 2014

Kuhusu "Macbeth"

Makala hii nilianza kuiandika mara tu baada ya kuanza kusoma Macbeth, tamthilia ya Shakespeare, ambayo niliitaja hapa na hapa. Jana usiku nimefika mwisho wake. Inafurahisha kujisomea namna hii, bila msukumo kutoka popote.

Hapa na pale katika Macbeth nimejikuta nikiyakumbuka maandishi mengine ya Shakespeare ambayo niliyasoma zamani, kama vile The Merchant of Venice, Othello, The Tempest, na Twelfth Night. Hii ni kwa sababu kuna mawazo ambayo yanajitokeza tena na tena katika maandishi ya Shakespeare. Wazo mojawapo ni kwamba dunia ni jukwaa ambapo sisi wanadamu ni waigizaji. Kuna misemo pia ambayo inajitokeza tena na tena.

Kwa mfano, nilivyosoma katika Macbeth kauli ya mchawi kuhusu meli kukumbwa na dhoruba (I, III, 25-26) nimekumbuka The Tempest. Nilivyokutana na usemi huu wa mfalme kwa kapteni shujaa: "So well thy words become thee as thy wounds; They smack of honor both," (I, II, 47-48) nimekumbuka hotuba ya Portia katika The Merchant of Venice, ambamo anaelezea thamani ya huruma.

Kati ya mambo anayosema kuhusu thamani ya huruma ni kwamba "It becomes the throned monarch better than his crown." Kwa tahadhari, niseme kuwa neno "becomes" anavyolitumia Shakespeare, lina maana tofauti kabisa na ile tunayoijua. Jambo hilo nilishaligundua katika kusoma tamthilia za Shakespeare.

Unaposoma Macbeth, sawa na kazi nyingi maarufu za fasihi, mahusiano ya namna hii hujitokeza, sio tu baina ya maandishi ya mwandishi mmoja, bali pia baina ya maandishi ya waandishi mbali mbali. Katika nadharia ya fasihi, mahusiano hayo huitwa "intertextuality" kwa ki-Ingereza.

Kufafanua zaidi wazo hili, napenda kusema kuwa jambo moja lililonistua katika Macbeth ni pale Fleance anaposema, "The moon is down; I have not heard the clock" (II, I, 2). Hapo nilikumbuka riwaya ya John Steinbeck, The Moon is Down, nikapata shauku ya kufuatilia kama kuna uhusiano. Lo, nimegundua kuwa Steinbeck alipata jina la riwaya yake hapo kwenye tamthilia ya Macbeth.

Ni wazi kuwa kusoma vitabu kunasisimua akili. Unaposoma masimulizi ya aina hii, ubongo unafanya kazi muda wote, kukumbuka hiki au kile, kuelewa kile unachosoma, na pia kubashiri kinachofuata katika mtiririko wa matukio.Kuelewa huko na kukumbuka vimefungamana. Akili hailali; inapata mazoezi, sawa na mazoezi ya viungo vyovyote vya mwili. Manufaa yake ni makubwa.

Ninavyosoma Macbeth, nakumbuka vizuri taarifa niliyosoma miaka kadhaa iliyopita kuhusu onesho la Macbeth lililofanywa Uingereza na kikundi cha waigizaji cha wa-Zulu. Niliisosoma makala hiyo, "The Zulu Macbeth," katika jarida la The New African, kama sikosei. Kuna ripoti kadhaa mtandaoni kuhusu onesho hilo la tamthilia ya Macbeth ya ki-Zulu, ambayo ilitungwa na Welcome Msomi na kupewa jina la "Umabatha." Kwa mfano, soma makala hii.

Ningeweza kuandika makala ndefu kuhusu Macbeth, nikijadili masuala kama dhamira, wahusika, mawaidha, falsafa, na umahiri wa Shakespeare katika kutumia lugha. Pamoja na mengine yote, Shakespeare ni mwanafalsafa anayefikirisha. Kwa mfano, tafakari kauli hii maarufu ya Macbeth mwenyewe, mhusika mkuu wa tamthilia hii, anapoambiwa kuwa mke wake amefariki:

She should have died hereafter;
There would have been a time for such a word.
Tomorrow, and tomorrow, and tomorrow
Creeps in this petty pace from day to day
To the last syllable of recorded time;
And all our yesterdays have lighted fools
The way to dusty death. Out, out, brief candle!
Life's but a walking shadow, a poor player,
That struts and frets his hour upon the stage
And then is heard no more. It is a tale
Told by an idiot, full of sound and fury,
Signifying nothing (V, V, 19-30).

Kwa kuhitimisha, napenda kusema kuwa nimefurahi sana kuisoma Macbeth hadi mwisho. Najisikia raha kuwa nimeongeza kitu cha thamani katika akili yangu. Ndivyo inavyokuwa katika kusoma vitabu vyenye thamani.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...