Showing posts with label Litembo. Show all posts
Showing posts with label Litembo. Show all posts

Friday, December 5, 2014

Kitabu cha "Siasa Hapo Kale"

Ninasoma Siasa Hapo Kale, kitabu ambacho nilikifahamu na kukipenda tangu nilipokuwa nasoma shule ya msingi kule nyumbani kwangu Litembo, katika mkoa wa Ruvuma. Mtunzi wa kitabu hiki ni Lucius Mabasha Thonya. Kama sikosei, nilikuwa na nakala ya kitabu hiki miaka ile kijijini kwangu. Ingawa sijui kilienda wapi, mara moja moja nimekikumbuka, hasa kwa vile mimi ni mtafiti katika fasihi simulizi. Hilo ni jambo moja katika utangulizi wa makala ya leo.

Jambo jingine ni kuwa kwa miaka kadhaa, nimevutiwa na juhudi za Dada Yasinta katika kudumisha lugha ya ki-Ngoni kwa kuanzisha na kuendesha blogu ya Vangoni. Ingawa ki-Ngoni sio lugha yangu, ninaielewa kiasi fulani nikiisikia au kuisoma, kwa vile inakaribiana na lugha yangu ya ki-Matengo.

Katika kusoma blogu ya Vangoni, nilipata wazo la kumwambia Dada Yasinta kuhusu kitabu hiki cha Siasa Hapo Kale. Hatimaye, nilimpelekea ujumbe, nikijua kuwa atapenda kusikia habari zake, na ndivyo ilivyokuwa. Kupitia maktaba ya hapa chuoni ninapofundisha, nilikipata kwa kutumia utaratibu unaotumiwa na maktaba wa kuazimishana vitabu na machapisho mengine, utaratibu uitwao "interlibrary loan."

Nilifurahi kukipata. Nilitengeneza nakala nikampelekea Dada Yasinta, naye aliandika habari hiyo katika blogu yake.

Siasa Hapo Kale ni mkusanyiko wa methali za ki-Ngoni, ambazo mtunzi amezitungia hadithi za kuzielezea. Katika maelezo yake, amefanikiwa vizuri kutupa maana na matumizi ya methali hizi, kwa kutumia maisha na mahusiano ya wahusika katika hadithi hizo. Anahitimisha kila hadithi kwa kusisitiza ujumbe muhimu uliomo katika methali. Kwa maneno yake mtunzi mwenyewe:

Hadithi zilizomo kitabuni humu zimesimuliwa kwa njia ya kubuniwa tu kupatana na mambo yalivyoweza kutokea katika maisha ya watu wa zamani zile. Hadithi hizo zimebuniwa ili kuwaangalisha wasomaji katika matukio ya namna mbalimbali yalivyopata kutokea katika kabila la Wangoni wa wilaya ya Songea iliyopo kusini mwa Tanganyika iliyo karibu na ziwa Nyasa.

Methali hizi zinathibitisha busara za wahenga, yenye falsafa, maadili, na mafundisho muhimu ya maisha. Napenda kunukuu baadhi ya methali, na tafsiri zilizomo kitabuni: "Njala likoko, yikoma na mhavi" (Njaa ni adui, hata mchawi inaua). "Mbanga kufwata manji kwegihamba" (Fuata maji yanakokwenda). "Katumbi ka ngolyongo ikwela mwe ngolyongo" (Utando wa buibui akwea yeye mwenyewe tu). "Mheka pangende kumwoyo lwitimba lungi" (Yu mcheshi machoni moyoni kuna mengine). "Imekela kandumba ka ngemelelu" (Ajivunia dawa ya bahati).

Mwandishi alifanya kazi kubwa ya kufikiri katika kuzitunga hadithi zilizomo kitabuni. Vile vile, ameandika kwa ki-Swahili sanifu, kinachovutia. Kitabu hiki kilichapishwa mwaka 1960, nami nakumbuka kuwa waandishi maarufu kama Shaaban Robert walikuwa bado hai. Miaka ile ya zamani, shirika la uchapishaji la East African Literature Bureau lilikuwa makini katika kuangalia matumizi ya lugha, kabla ya kuchapisha kitabu.

Monday, February 13, 2012

Mitaani Mbinga, 2011

Mwaka jana, tarehe 2 Agosti, nilipita Mbinga, mji mkuu wa wilaya yangu, nikapiga picha kadhaa. Hapa kushoto ni kituo cha mabasi. Hapo ndipo unapandia mabasi ya kwenda Mbamba Bay na Songea. Hapo pia unapanda mabasi au magari mengine yanayoenda vijijini katika wilaya hiyo.






Hapa kushoto ni mtaa mojawapo wa pembeni, karibu na kituo cha mabasi, upande wa barabara iendayo Songea.












Hapo ni mtaa mwingine, sehemu ya bondeni kutoka kituo cha mabasi.












Huo nao ni mtaa wa pembeni. Udongo wa Mbinga ni kama inavyoonekana pichani, sawa na ilivyo katika eneo lote kuanzia Songea hadi karibu na Mbamba Bay. Kahawa inastawi katika udongo huo, na hapa Mbinga kuna kiwanda cha kusindikia kahawa.

Siku zijazo ninapangia kuleta picha za mashamba ya kahawa, ngano, na kadhalika, ambayo yanazipendezesha sehemu za vijijini katika wilaya ya Mbinga.


Huo ni mtaa mwingine upande wa chini kutoka kituo cha mabasi. Mbinga ya leo sio kama ya miaka kumi au ishirini iliyopita. Ingawa nafika hapo karibu kila mwaka, daima naona mambo mapya. Kwa mfano, hoteli nzuri zinaongezeka. Mwaka jana nilifikia kwenye hoteli ambayo iko hapa kwenye dishi la satalaiti.






Mbinga ni mji ulio karibu na nyumbani kwangu Litembo. Kama unatoka Songea, ukitaka kufika Litembo, unapita hapa Mbinga na kuelekea mbele, juu milimani. Wilaya ya Mbinga kwa ujumla ina hali ya vuguvugu na pia baridi, na kadiri unavyoelekea milimani zaidi, baridi inaongezeka. Katika hiyo picha tumevaa kwa kufuata hali hiyo, nami nimejihami na jaketi la Shidolya Safaris ya Arusha.

Baadhi ya ndugu zangu wanaishi hapa Mbinga. Hapo kushoto niko na binamu yangu Remigius Komba ambaye anaishi hapo. Tulikutana hapo kituoni bila kutegemea. Hapa nyuma yetu unayaona magari yamepakia, tayari kwa safari. Hayo ndio magari ninayopanda kwa safari ya kutoka hapa Mbinga kwenda Litembo. Ingawa niko ughaibuni, ninapofika hapo Mbinga nagundua kuwa madereva na utingo wananifahamu vizuri.

Tuesday, February 8, 2011

Blogu Imenisaidia Darasani

Leo wakati muhula mpya unaanza hapa Chuoni St. Olaf, nimekutana na wanafunzi nitakaowafundisha somo la kuandika kwa ki-Ingereza. Kama kawaida, siku ya kwanza huwa ni ya kujitambulisha, kuelezea habari za somo, maana yake, falsafa na maadili yangu kama mwalimu, maana na mikakati ninayotumia katika kufundisha.

Katika kujitambulisha, huwa nawaeleza wanafunzi kuhusu nyumbani kwangu, shule nilizosoma, na nilivyoingia katika kazi ya ualimu, na imani yangu kuwa Mungu alitaka niwe mwalimu.

Leo wakati naanza kuelezea habari za nyumbani kwangu, nilikumbuka kuwa nilishaandika kwenye blogu. Basi, niliwasha kompyuta iliyomo darasani nikafungua blogu na wao wenyewe wakasoma kwenye skrini kubwa habari za Litembo.

Blogu imenisaidia kufikisha ujumbe wangu kwa ufanisi, kwani mbali ya maelezo kuna picha. Picha zinajieleza vizuri kuliko pengine hata maneno, jambo linalosisitizwa katika ule usemi kuwa picha ni sawa na maneno elfu. Niliwaambia kuwa nina picha nyingi za nyumbani kwangu na Tanzania kwa ujumla. Ni wazi kuwa ninazo fursa tele za kuendelea kuwajulisha walimwengu habari za kwetu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...