Showing posts with label blogu. Show all posts
Showing posts with label blogu. Show all posts

Monday, July 17, 2017

Nina Mashairi Yote ya John Donne

Nimegundua kuwa nina mashairi yote ya John Donne. Huyu ni mshairi mmoja maarufu sana katika ki-Ingereza, ambaye aliishi miaka ya 1572-1631, na niliwahi kumtaja katika blogu hii. Niliandika habari zake siku niliponunua kitabu kiitwacho The Works of John Donne.

Lakini wikiendi hii, katika kuangalia katika msitu wa vitabu vyangu ofisini, nimegundua kitabu kiitwacho The Complete English Poems of John Donne, kilichohaririwa na C.A. Patrides. Hiki kina mashairi yake yote.

Katika utangulizi wake, Patrides amesema mambo ambayo yamenifungua macho na kunifikirisha. Amesema, kwa mfano, "The text of Donne's poetry can vex an editor into nightmares." Anamaanisha kuwa maandishi ya Donne yanaweza kumchanganya akili mhariri akaishia katika majinamizi. Hii ni kwa sababu miswada ya mashairi ya Donne ni mingi na inahitilafiana.

Niliposoma utangulizi huu, nimewazia maandishi ya William Shakespeare, ambaye aliishi wakati ule ule wa John Donne. Maandishi ya Shakespeare, hasa tamthilia, nayo yanapatikana katika miswada inayohitilafiana, na kwa miaka yote wahariri wamekuwa wakijaribu kurekebisha na kuwasilisha kile ambacho wanaamini ni andiko sahihi la Shakespeare.

Tofauti hizi katika maandishi ya Donne na Shakespeare, haziko katika maneno na sentensi tu, bali pia katika alama kama vile nukta na mikato katika sentensi. Kwa hivyo, tunavyosoma andiko la Shakespeare, tunapaswa kuzingatia kuwa kuna vitu kadha wa kadha ambavyo vimeingizwa na wahariri wa karne moja hadi nyingine.

Hata hivi, kama nilivyosema katika ujumbe wangu wa mwanzo, nimeona nisome kwa makini mashairi ya Donne, hasa kwa kuzingatia kuwa nilikulia nikiwa nimesikia sana kwamba mashairi yake ni magumu. Nimepata mwamko mpya, wa kutaka kujipima akili kwa kuyakabili haya mashairi yanayosemekana ni magumu. Tena basi, nitapenda hata kujaribu kutafsiri baadhi ya mashairi haya kwa ki-Swahili, kama nilivyowahi kutamka katika blogu hii.

Friday, July 7, 2017

Wadau Wangu Wapya

Nina furaha kama mwandishi kuwa nimejipatia wadau wapya, na ninawatambulisha hapa kama ilivyo kawaida yangu. Hao ni Brian Faloon na mkewe Kristin, wenyeji wa Rochester, Minnesota. Brian ni rais wa Rochester International Association (RIA). Kristin na mimi ni wanabodi katika bodi ya RIA, ambamo nilijiunga mwaka jana kama nilivyoelezea katika blogu hii.

Baada ya mimi kujiunga na bodi, nilipata fursa ya kutoa mhadhara katika chuo kikuu cha Minnesota Rochester, mada ikiwa "Folklore as Expression of Ethics," kama nilivyoeleza katika blogu ya ki-Ingeeza. Brian alihudhuria.

Brian aliuongelea mhadhara ule katika mkutano uliofuata wa bodi ya RIA. Baada ya muda, nilipata mwaliko wa kutoa mhadhara chuo kikuu cha Winona, mwaliko ambao niliuelezea katika blogu hii. Kristin aliniuliza iwapo itawezekana yeye kuhudhuria. Niliwasiliana na waandaaji, kuwauliza iwapo ninaweza kumwalika mgeni kuhudhuria, nikajibiwa kuwa ni ruksa. Nilimweleza Kristin hivyo.

Nilisafiri tarehe 27 Juni hadi Winona, mwendo wa saa mbili. Nilivyoingia ukumbini, niliwakuta Kristi na Brian wameketi, pamoja na wasikilizaji wengine yapata 50. Nilitambulishwa na wenyeji wangu, nikatoa mhadhara kama nilivyoelezea katika blogu ya ki-Ingereza. Nilivyomaliza mhadhara na muda wa masuali na majibu, Kristin na Brian walinisogelea tukaongea. Walifurahia mhadhara. Nilivyowashukuru kwa kusafiri mwendo mrefu na kuhudhuria, walinijibu kuwa wao ni mashabiki wangu. Walichosema ni ukweli, kwani walianza kuwa wadau tangu waliposoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Tarehe 4 Julai, nilipata ujumbe kutoka kwa Kristin. Kati ya mambo aliyoandika ni haya:

We greatly enjoyed hearing your presentation and thought it was very good! Thank you for letting us attend! I believe it would be an excellent presentation to do in our community and schools here in Rochester as we have the same tensions between the two groups....I would like to coordinate something when we have time. We can discuss it at the next meeting if you're interested.

Ninajivunia hao wadau wangu wapya. Moyo wangu wa kutumia ujuzi wangu kwa manufaa ya walimwengu unaniletea fursa kama hii anayoongelea Kristin. Ninazipokea fursa hizi kwa moyo mkunjufu. Ninaamini ni mipango ya Mungu, wala sijali suala la kulipwa au kutolipwa fedha, kama nilivyoelezea katika blogu hii. Mungu ana mipango yake, na anasawazisha mambo.

Thursday, May 11, 2017

Shukrani kwa Msomaji

Msomaji mwingine wa kitabu cha Africans and Americans; Embracing Cultural Differences amejitokeza na kuandika maoni yake kuhusu kitabu hiki. Ameandika maneno matatu tu, "Short and sweet," katika mtandao wa Goodreads, ambao ni maarufu miongoni mwa wasoma vitabu. Humo wanaweka maoni yao kuhusu vitabu walivyosoma au vitabu wanavyopangia kusoma.

Kama ilivyo kawaida yangu katika blogu hii, ninamshukuru kwa kujipatia kitabu hiki, kukisoma, na kuwajuza walimwengu maoni yake. Amefanya hivyo kwa hiari yake, akijua kwamba kauli yake itasomwa na watu wengi. Namshukuru kwa hisani yake; amenifanyia kazi bila malipo wala kutegemea shukrani.

Maoni ya wasomaji yana manufaa makubwa. Kwanza yananiwezesha kufahamu kama ninafikisha ujumbe wangu na unaeleweka vipi. Kila msomaji anapotoa maoni, hutaja jambo fulani au mambo fulani yaliyomgusa kwa namna ya pekee. Wasomaji wanaweza kuwa wamekipenda kitabu hicho hicho, lakini kwa misingi au namna mbali mbali.

Pili, kuwepo kwa maoni ya wasomaji kunaniondolea jukumu la kukiongelea kitabu changu, kwa watu wanaokiulizia. Badala ya mimi kuwaelezea, ninawaelekeza watu wakasome maoni hayo, ambayo wasomaji wameyatoa kwa hiari yao, bila msukumo wa aina nyingine.

Siku nne zilizopita, kwa mfano, m-Tanzania moja aishiye Marekani, aliniandikia ujumbe binafsi katika Facebook akinielezea kuwa anatakiwa kuongea na waalimu kutoka Marekani katika kuwaandaa kwa safari ya Tanzania. Hiyo ni programu baina yao na walimu wa Tanzania kuhusu tamaduni na ufundishaji. Alihitaji pendekezo la kitabu kuhusu tamaduni.

Nilimtajia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na baadaye nimemshauri kuwa ili ajiridhishe, aangalie maoni ya wasomaji kwenye mtandao wa Amazon na pia mtandao wa Goodreads. Kuna sehemu zingine pia ambapo maoni yamechapishwa, kama vile blogu, tovuti, na majarida.

Friday, April 14, 2017

Neno Kuhusu Matokeo ya Kuchapisha Kitabu

Mimi kama mwandishi wa vitabu ninafurahi ninapopata wasaa wa kuelezea uzoefu wangu na kutoa ushauri kwa waandishi wengine au wale wanaowazia kuwa waandishi. Mara kwa mara ninaandika kuhusu mambo hayo kwa kujiamulia mwenyewe, lakini mara kwa mara ninaandika kuwajibu wanaoniulizia. Baadhi ya mawasiliano hayo huwa ni ya binafsi, na mengine hufanyika katika blogu hii.

Leo nimeona niseme neno kuhusu matokeo ya kuchapisha kitabu. Ninaandika kufuatia uzoefu wangu wa hapa Marekani. Kuchapisha kitabu ni aina ya ukombozi kwa mwandishi kutakana na jambo lilolokuwa linakusonga mawazoni. Ni kama kutua mzigo. Baada ya kumaliza kuandika, unajisikia mwenye faraja, tayari kuanza au kuendelea na majukumu mengine. Ni aina ya ukombozi.

Kuna waandishi chipukizi wanaoamini kuwa kuandika kitabu kutawaletea umaarufu au fedha. Wazo hili ni bora kuliweka kando. Fedha si jambo la kulipa kipaumbele; kwa kiasi kikubwa ni kubahatisha. Kwanza, kuna vitabu vingi mno vinavyochapishwa kila mwaka. Kwa hapa Marekani tu, vitabu zaidi ya milioni huchapishwa kila mwaka, kwa mujibu wa taarifa zilizopo. Sio rahisi mwandishi anayeanza safari ya uandishi ajipambanue na kuwa maarufu. Kwa wastani, nakala za kitabu zinazouzwa kwa mwaka ni 250, na ukomo wa mauzo kwa miaka yote ya kuwepo kitabu ni pungufu ya nakala 3,000.

Kwa hapa Marekani, kuna jadi kwamba waandishi, wakishachapisha kitabu, hufanya safari za kutangaza kitabu hicho. Safari hizi hupangwa na kuratibiwa na wadau wa vitabu kama vile wachapishaji wa vitabu, wauzaji wa vitabu, waendeshaji wa majarida yanayojihusisha na vitabu, na vikundi vya wasomaji katika miji na maeneo mbali mbali. Wote hao wanashiriki katika kufanikisha ziara ya mwandishi. Wanatangaza kwa namna yoyote ile ziara hiyo, magazetini, katika redio, katika televisheni, au mitandao ya kijamii.

Popote anapofika mwandishi, watu hujitokeza kumsikiliza akiongelea kitabu chake. Wanapata fursa ya kumwuliza masuali. Nakala za kitabu zinakuwepo, na watu wanapata fursa ya kununua na kusainiwa. Wenye maduka ya vitabu hupenda kuandaa mikusanyiko hiyo. Mbali na kwamba wanampa mwandishi fursa ya kukutana na wasomaji, na kutangaza kitabu chake, ni fursa kwa hayo maduka ya vitabu kujitangaza. Ni jadi iliyozoeleka kwamba nyakati hizo, kunakuwa na punguzo la bei ya kitabu kinachotangazwa, na hiki kinakuwa ni kivutio cha ziada kwa wateja.

Lakini jambo la msingi ni kuwa watu wa Marekani wanathamini sana fursa ya kukutana na mwandishi. Mimi mwenyewe, ingawa bado si mwandishi aliyetunukiwa tuzo maarufu kama Pulitzer, ninashuhudia jinsi watu wanavyovutiwa na fursa ya kukutana nami, iwe ni kwenye matamasha au kwenye mihadhara ninayotoa.

Hizi fursa za waandishi za kwenda kuongelea vitabu vyao ndio njia moja kuu ya waandishi kujijenga katika jamii. Mwandishi kuonekana na kusikilizwa moja kwa moja na wasomaji na wadau wengine wa vitabu ni njia ya kujijenga mioyoni mwao. Kukutana na mwandishi namna hiyo kunaleta picha na hisia ya pekee pale msomaji anaposoma kitabu cha mwandishi huyo. Bila shaka wote ambao tumewahi kukutana na waandishi tunajisikia hivyo tunaposoma maandishi yao.

Nimegusia hapo juu kuwa kuna watu wanaowazia kuwa kuchapisha kitabu kutawaletea umaarufu au fedha. Ni kweli, kutegemeana na kukubalika kwa kitabu katika jamii, mwandishi anaweza kupata umaarufu na fedha kiasi fulani. Lakini, kwa uzoefu wangu, ninapoalikwa kwenda kuongelea kitabu ndipo pana malipo makubwa, ukiachilia mbali kuwa vile vile nakala za vitabu zinauzwa hapo hapo. Vitabu ninavyoongelea hapa ni viwili: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na Matengo Folktales. Kipo kingine ambacho nimekuwa nikiandika kwa miaka kadhaa, kuhusu athari za tofauti za tamaduni, ambacho nina hakika kuwa kitawagusa watu kwa namna ya pekee.

Ningependa mambo hayo niliyoelezea yafanyike Tanzania. Ninatamani uje wakati ambapo, mwandishi akishachapisha kitabu muhimu, kiwe ni cha fasihi au maarifa, awe na fursa ya kuzunguka nchini kuongelea kitabu chake. Ninatamani uje wakati ambapo wananchi watakuwa na utamaduni wa kuvipenda vitabu na kupenda kukutana ana kwa ana na waandishi na kuongea nao.

Wednesday, April 12, 2017

Blogu Yangu Imepanda Chati Ghafla

Tangu wiki mbili zilizopita, blogu yangu hii imepanda chati ghafla. Ninaongelea kigezo cha "pageviews," ambazo ninaziangalia kila nitakapo. Kwa miaka na miaka, "pageviews" za blogu hii kwa siku zilikuwa kama 130, sio zaidi sana na sio pungufu sana.

Lakini, kuanzia wiki mbili hivi zilizopita, "pageviews" zimeongezeka ghafla kwa kiwango kikubwa, na sasa ni yapata 900 au zaidi kila siku. Sielewi ni nini kimesababisha ongezeko hilo. Mkondo wa mada zangu haujabadilika. Kwa kiasi kikubwa ninashughulika na masuala ya elimu na utamaduni.

Nimeona kuwa ongezeko hilo la "pageviews," limetokea hapa Marekani. Kwa nchi zingine, kama vile Tanzania na Kenya, hali haijabadilika. Ni ajabu kiasi kwamba blogu ya ki-Swahili inasomwa zaidi Marekani kuliko Afrika Mashariki.

Mtu unaweza kujiuliza ni watu gani wanaosoma hii blogu ya ki-Swahili kwa wingi namna hii hapa Marekani. Ukweli ni kuwa kuna watu wengi hapa, hasa kutoka Kenya na Tanzania, wanaokifahamu ki-Swahili. Wako pia watu kutoka Burundi, Uganda, Rwanda, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Vile vile, kuna wa-Marekani ambao wameishi Afrika Mashariki na wanakifahamu ki-Swahili. Pia kuna wa-Marekani wengi ambao wamejifunza au wanajifunza ki-Swahili katika vyuo vikuu mbali mbali hapa hapa Marekani. Ninahisi kuwa hao nao ni kati ya wasomaji wa blogu hii.

Ninavyowazia suala hili la ukuaji wa idadi ya "pageviews" katika blogu, ninawazia jinsi watu wanavyotumia blogu kwa matangazo, hasa ya biashara. Katika ulimwengu wa leo ambamo tekinolojia za mawasiliano zinaendelea kusambaa na kuimarika, wafanya biashara na wajasiriamali wanatumia fursa za mitandao kama vile blogu kutangaza shughuli zao.

Kwa upande wangu, sijajiingiza katika matumizi haya ya blogu, ukiachilia mbali matangazo ya vitabu vyangu na mihadhara ninayotoa au matamasha ninayoshiriki. Lakini, endapo nitabadili msimamo, bila shaka nitakaribisha matangazo ya waandishi, wachapishaji, na wauzaji wa vitabu, kwa sababu blogu yangu inajitambulisha kwa masuala ya aina hiyo.

Saturday, April 8, 2017

Mwaliko Chuo Kikuu cha Winona

Tangu mwaka uanze, nimetoa mihadhara au kufanyiwa mahojiano nje ya chuo ninapofundisha, mara nyingi kuliko kawaida. Nilitegemea kuwa kuanzia mwezi huu wa Aprili, hali ingebadilika. Lakini dalili hazionyeshi mabadiliko.

Tarehe 6, nilipata mwaliko kutoka kwa Alex Hines, mkuu wa idara ya Inclusion and Diversity katika Chuo Kikuu cha Winona, wa kwenda kutoa mhadhara:

We would like to extend an invitation for you to attend HOPE Academic & Leadership Academy during the week of June 26th through June 29th and conduct a two hour presentation from 7-9 p.m. on Embracing African and African American Culture.

Hii itakuwa ni mara ya tatu mimi kwenda kutoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Winona. Mara ya kwanza, niliongelea masuala ya utamaduni kama nilivyoyaeleza katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Mara ya pili, niliongelea mahusiano ya binadamu na uongozi, kwa kutumia kitabu cha Matengo Folktales, kama nilivyoandika katika blogu hii

Mwaliko huu wa sasa, kama ilivyoelezwa katika barua niliyonukuu hapa juu, msingi wake ni kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Alex Hines, tangu tulipofahamiana, miaka mingi iliyopita, amekuwa ni mmoja wa wale wanaonitegemea katika programu zao. Ninafurahi kwa imani ya wadau juu yangu, nami ninahamasika kufanya makubwa zaidi kwa ajili yao.

Blogu hii ni mahali ninapohifadhi kumbukumbu zangu, kama nilivyowahi kuandika katika blogu hii. Labda kuna siku nitapata wazo la kuandika kitabu kuhusu shughuli zangu. Ikitokea hivyo, kumbukumbu hizi zitanifaa.

Monday, January 2, 2017

Mazungumzo na Wanafunzi wa Chuo cha Gustavus Adolphus

Leo mchana nilikuwa Mount Olivet Conference & Retreat Center katika maongezi na wanafunzi wa chuo cha Gustavus Adolphus wanaokwenda Tanzania kimasomo. Profesa Barbara Zust, alikuwa amenialika, kama nilivyoandika katika blogu hii.

Wanafunzi wengi wa programu hii wanasomea uuguzi, na lengo la kwenda Tanzania ni kujifunza namna masuala ya afya na matibabu yalivyo katika mazingira tofauti na ya Marekani, kwa maana ya utamaduni tofauti. Kwa lengo hilo, wanafunzi husoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Kwa hivyo, hiyo jana, kama ilivyokuwa miaka iliyopita, niliwakuta wanafunzi wamesoma kitabu hiki na wamejizatiti kwa masuali ambayo yalinithibitishia kuwa ni wanafunzi makini wenye duku duku ya kujua mambo. Tulikuwa na mazungumzo ya kina yaliyodumu kwa zaidi ya saa mbili. Mwanafunzi mmoja, msichana, aliniambia kuwa yeye na mama yake walisoma kitabu changu pamoja. Taarifa hii imanigusa. Ni kama vile mzazi ametafuta namna ya kushiriki yale ambayo binti yake atayapitia atakapokuwa ugenini Tanzania.

Hiyo leo, nilipoanza kuongea na wanafunzi hao, niliwapongeza kwa uamuzi wao wa kwenda katika programu hii, ambayo itawapanua mtazamo na fikra, na hivyo kuwaandaa kukabiliana na dunia ya utandawazi wa leo. Baada ya mazungumzo yetu, tuliagana tukiwa tumefurahi, kama inavyoonekana pichani. Anayeonekana kulia kwangu kule nyuma kabisa ni Profesa Zust. Mbele yangu ni Mchungaji Todd Mattson.

Kwa taarifa zaidi kuhusu safari ya hao wanafunzi, fuatilia blogu yao With One Voice Tanzania

Friday, December 2, 2016

Ndugu wa Uganda Anataka Kitabu

Kama ilivyo kawaida katika blogu hii, ninapenda kujiwekea kumbukumbu mbali mbali. Jana niliwatembelea akina mama wawili wa-Kenya waishio Brooklyn Park, Minnesota, ambao walitaka tukutane ili niweze kuwapa ushauri kuhusu fursa za kujiendeleza kielimu ya juu na katika ajira. Wakati tulipokuwa katika maongezi, waliwasiliana na bwana mmoja wa kutoka Uganda, wakamwita kuja kuungana nasi.

Tulizungumza kuhusu masuala mbali mbali, yakiwemo masuali waliyoniuliza juu ya ufundishaji na uandishi wangu. Mmoja wa hao akina mama nilikuwa nimemwahidi kumpa nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Huyu jamaa wa Uganda aliniulizia namna ya kukipata kitabu kile, nikamweleza kuwa anaweza kukipata mtandaoni Amazon.com au lulu.com/spotlight/mbele, au kutoka kwangu. Nikamshauri kwamba kwa upnde wa gharama, ni rahisi zaidi kukinunua Amazon.com. Lakini yeye alisisitiza kuwa nimpelekee, akanipa na anwani yake.
,
M-Ganda huyu amenikumbusha wa-Ganda wengine niliokutana nao hapa Minnesota, wakajiptia kitabu changu. Mmoja ni Steven Kaggwa ambaye alikuwa anamiliki mgahawa wa Tam Tam. Baada ya kukisoma kitabu hiki, aliniambia kuwa aliwaelezea wafanya kazi wake. Mmoja wao, Sally, hakuishia tu kujinunulia nakala, bali alinunua nakala nyingine ambayo aliniambia alikuwa anampelekea mkuu wake wa kazi, ambaye ni m-Marekani. Niliguswa na taarifa ya huyu mama, kama nilivyoguswa miaka michache baadaye, wakati mama mmoja kutoka Togo alivyonunua nakala za kitabu hiki kwa ajili ya wakuu wa kazini kwake, kama nilivyoripoti katika blogu hii.

M-Ganda mwingine ninayemkumbuka nilikutana naye katika tamasha la vitabu ambalo nilikuwa ninashiriki. Alikuwa amefika kikazi hapa Minnesota, lakini alikuja kwenye tamasha hilo, na ndipo tulipofahamiana. Bila kusita alinunua kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differenes, akaenda zake. Yeye na hao wengine wameniacha nikitafakari jinsi hao wenzetu walivyo. Ninaona kuwa sio tu wameenda shule, bali wameelimika, kwani uthibitisho wa kuelimika ni kuwa na hamu ya kutafuta elimu hata baada ya kumaliza shule.

Thursday, September 8, 2016

Wasomaji Wangu Wa Nebraska Waendao Tanzania

Nina jadi ya kuwaongelea wasomaji wangu katika blogu hii, kama njia ya kuwaenzi. Ni jambo jema kwa mwandishi kufanya hivyo. Leo ninapenda kuwakumbuka wasomaji wangu wa sinodi ya Nebraska ya Kanisa la Kiluteri la Marekani, ambao tangu zamani wamekuwa na programu ya kupeleka watu Tanzania kuendeleza uhusiano baina yao na wa-Luteri wa Tanzania.

Hao wasafiri, sawa na wenzao wa sinodi zingine za Marekani, wamekuwa wakitumia kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika kujiandaa kwa safari, ili kuzielewa tofauti za tamaduni za Marekani na Afrika. Ni elimu muhimu katika ulimwengu wa utandawazi wa leo, ambayo nje ya ufundishaji wa darasani, ninashughulika nayo.


Wakati huu ninapoandika, waumini wa Nebraska wanajiandaa kwa safari ya Tanzania, ambayo itafanyika mwezi Februari mwaka 2017. Wameitangaza safari hii mtandaoni, na mratibu mojawapo wa safari, Martin Malley, ameniandikia ujumbe leo akisema, "We still recommend your book." Katika ukurasa wa 16 wa chapisho la maelezo na maandalizi ya safari, kitabu hicho kimetajwa.

Ninapowakumbuka wasomaji wangu wa Nebraska, ninakumbuka nilivyokutana katika uwanja wa ndege wa Amsterdam na kikundi cha watu wa Nebraska waliokuwa wanakwenda Tanzania, tukasafiri pamoja. Mimi sikuwajua, ila wao walinitambua, kama nilivyoelezea katika blogu yangu ya ki-Ingereza.


Saturday, April 23, 2016

Ujumbe Mzuri Kutoka kwa Mwanafunzi

Leo nimepata ujumbe mzuri kutoka kwa m-Tanzania ambaye simfahamu. Amejitambulisha kwamba alipokuwa mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule ya sekondari ya Namtumbo, alisoma mwongozo wangu juu ya Things Fall Apart na Song of Lawino. Nimefurahi kusikia habari hii ya kusomwa maandishi yangu sehemu ya mbali kama Namtumbo ambayo iko njiani baina ya Songea na Tunduru.

Inawezekana kuwa huyu mtu alimaanisha kijitabu changu ambacho kilikuwa na mwongozo wa Things Fall Apart na The African Child, ambao niliuelezea katika blogu hii. Ni hivi karibuni tu nimechapisha mwongozo wa Song of Lawino. Si hoja, ili mradi watu wasome ninayoandika.

Mimi ni mwalimu, na dhana yangu ya ufundishaji ni pana. Inajumlisha ninavyofundisha darasani, ninavyoandika na kuchapisha vitabu na makala, ninavyoblogu, ninavyoshiriki matamasha ya vitabu na utamaduni, ninavyoongea na watu ana kwa ana, kama vile mitaani, ninavyoendesha warsha, ninavyoshiriki mijadala mitandaoni, na kadhalika.

Mwalimu si mtu wa kuficha mawazo na mitazamo yake. Hachelei kujieleza. Ni wajibu wake. Mwalimu wa Chuo kikuu ana wajibu wa pekee wa  kufanya utafiti na kuandika vitabu na makala ili kuchangia taaluma. Anawajibika kwa wanataaluma wenzake na pia kwa jamii. Huu wajibu mpana ndio unanifanya nijishughulishe na jamii katika nyanja kama magazeti, blogu, mitandao. Miongozo ninayoandika juu ya kazi za fasihi ni sehemu ya azma hii ya kuisogeza taaluma katika jamii.

Mwongozo wangu wa Things Fall Apart alioongelea huyu mtu inaonekana ni wa mwanzo mwanzo. Nilifanya juhudi kuuboresha. Uthibitisho wa ubora wake ni kwamba unapendekezwa kwa wanafunzi hapa Marekani wanaosoma Things Fall Apart, kama ilivyofanywa na Chuo Kikuu cha Cornell. Ninafurahi kwamba ninatoa mchango wangu kwa namna hiyo, kuanzia Marekani hadi Namtumbo.

Thursday, December 3, 2015

Kuhusu Kublogu

Nimekuwa mwanablogu tangu mwaka 2008. Ninaendesha blogu hii ya Hapa Kwetu na nyingine ya ki-Ingereza. Kublogu kuna mambo mengi. Kublogu kunanipa fursa ya kujieleza kwa uhuru. Hili ni jambo la msingi, kama alivyoelezea mwanablogu Christian Bwaya.

Lakini kublogu kuna matokeo yenye manufaa. Kumeniwezesha kuwafikia watu mbali mbali ambao wanatembelea blogu zangu. Siwezi kujua wanapata ujumbe gani katika maandishi yangu. Kama taaluma inayotufundisha, hili ni suala tata.

Ujumbe wa andiko ni zao la kazi anayofanya msomaji juu ya andiko. Na kwa kuwa wasomaji wana akili zinazotofautiana, na wana nidhamu na uzoefu tofauti wa kusoma, kila mmoja anaibuka na ujumbe tofauti, kwa kiwango kidogo au kikubwa.

Niliwahi kuelezea kwa nini ninablogu, lakini sidhani kama nilikuwa na majibu ya uhakika. Baadaye, katika kutafakari suala hili, nilifikia hatua ya kutamka kwamba ninablogu kwa ajili yangu mwenyewe. Labda huu ndio ukweli wa mambo.

Imani iliyojengeka katika jamii ni kuwa mwandishi anawaandikia wasomaji. Tumezoea kuona waandishi wakiulizwa wanamwandikia nani, nao wanaelezea walengwa wao. Jadi hii na imani hii imekosolewa kwa uhodari na Roland Barthes katika makala yake, "The Death of the Author."

Makala hii ya Barthes naona inaipa uzito hoja yangu kuwa ninapoblogu ninajiandikia mwenyewe. Sijui ni nani atasoma au anasoma ninachoandika. Kusema kwamba ninawaandikia wasomaji ni kama kuota ndoto. Ni kujiridhisha kwa jambo ambalo halina uhakika bali ni bahati nasibu. Nikisema ninajiandikia mwenyewe ninasema jambo la uhakika.

Wednesday, October 28, 2015

Maprofesa na Wajibu wa Kuandika

Profesa ni mtu aliyefikia kiwango cha juu cha ufanisi katika ufundishaji, utafiti, uandishi, na kutoa ushauri kwa jamii katika masuala mbali mbali yanayohusiana na utaalam wake. Siwezi kuongelea hapa vipengele vyote vya suala hili, kama vile vigezo vinavyotumika katika kupima ufanisi wa mhusika hadi kumfikisha kwenye hadhi ya uprofesa. Ninakumbushia tu suala la wajibu wa profesa wa kuandika.

Baadhi yetu wa-Tanzania tumeliwazia na kuliongelea suala hili kwa miaka mingi, kwa manufaa ya jamii, tukiliunganisha na masuala kama sera ya elimu, matatizo ya uchapishaji, na kukosekana kwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu.

Kilichonifanya nirejeshe mada hii leo ni kwamba nimejikumbusha tamko la Rais Kikwete, "Maprofesa Wananisikitisha," ambalo lilijadiliwa katika blogu yangu hii na blogu ya Profesa Matondo. Mambo yaliyosemwa katika majadiliano yale ni muhimu na yataendelea kuwa muhimu. Wajibu wa profesa wa kuandika, kama njia mojawapo ya kufundisha na kuchangia maendeleo ya taaluma ni jambo lililo wazi.

Hata hivi, kwa kuzingatia kuwa dunia inabadilika muda wote, kuna umuhimu wa kulitafakari suala hili kwa mtazamo unaozingatia mabadiliko haya. Fikra zilizokuwa sahihi miaka michache iliyopita, huenda zimepitwa na wakati. Wataalam katika nyanja mbali mbali, kama vile ujasiriamali, elimu, na biashara wanatufundisha kuwa mabadiliko yanatulazimisha kuwa wabunifu na wepesi wa kubadilisha fikra, mahusiano, mbinu na utendaji wetu. Ndio maana ni muhimu kusoma daima na kujielimisha kwa njia zingine.

Katika dunia ya utandawazi wa leo, ambamo tekinolojia mbali mbali zinastawi, zikiwemo tekinolojia za mawasiliano, tunawajibika kuwa na fikra mpya kuhusu usomaji, uchapishaji na uuzaji wa vitabu, na kadhalika. Shughuli nyingi sasa zinafanyika mtandaoni, ikiwemo ufundishaji, kama nilivyowahi kugusia katika blogu hii. Tunawajibika kufunguka akili na kuacha kujifungia katika hiki tunachokiita sera ya elimu ya Tanzania. Je, inawezekana kuandika kitabu chenye umuhimu kwa Tanzania lakini si kwa ulimwengu? Taaluma inaweza kufungiwa katika mipaka ya nchi? Kuna dhana katika ki-Ingereza tunayopaswa kuitafakari: "The local is global."

Naona ni jambo jema kuirejesha mada hii, tuendelee kuitafakari katika mazingira ya leo. Lakini, naona tusome kwanza mjadala uliofanyika katika blogu hii na blogu ya Profesa Matondo.

Saturday, June 20, 2015

Msomaji Amenilalamikia

Leo alasiri nilikwenda Brooklyn Park, Minnesota, kuhudhuria mkutano wa bodi ya Afrifest Foundation ambayo mimi ni mwenyekiti wake. Tulifanyia mkutano wetu katika maktaba ya Brookdale.

Baada ya mkutano, nilipotoka nje kuelekea sehemu nilipopaki gari, alinikimbilia dada Latonya anayeonekana katika picha hapa kushoto, ambayo tulipiga miaka mitano iliyopita kwenye tamasha la Afrifest. Ni m-Marekani Mweusi kutoka Chicago, ila anaishi Minneapolis. Tulifahamiana miaka ile kwa kuwa naye alikuwa katika bodi ya Afrifest Foundation.

Hatukutegemea kama tungeonana leo, ghafla namna ile. Kwa hivi tulifurahi sana. Lakini hakupoteza muda, alianza kunihoji kwa nini siandiki sana katika blogu yangu ya ki-Ingereza kama zamani. Alisema, akimaanisha maandishi yangu ya kiSwahili, "Tunaona unaandika sana, na tunajua unaandika mambo ya maana, ila hatujui unachoandika. Inakuwa kama unatusahau marafiki zako wa-Marekani Weusi."

Kwa kweli, ingawa mazungumzo yalikuwa ya kirafiki, na hata kiutani, niliona kuwa alikuwa anaongea kwa dhati. Na sisi wa-Afrika ambao tunaishi Marekani tunafahamu kuwa wako wa-Marekani Weusi wengi ambao wanategemea sisi wa-Afrika tuwe na mshikamano nao, kama ndugu. Kwa hivi, sikuyachukulia malalamiko ya Latonya kama mzaha. Nilijikuta nikikiri kosa na kuahidi kuwa nitakuwa naandika kama zamani. Alivyowataja wa-Marekani Weusi hakuwa anatunga hadithi. Ninafahamu kuwa wanasoma maandishi yangu.

Latonya mwenyewe ni mmoja wa wafuatiliaji wa dhati wa maandishi yangu. Hapo pichani, anaonekana ameshika kitabu changu cha Africans and Americans:Embracing Cultural Differences, mara baada ya kukinunua. Maneno aliyoniambia leo yameniingia. Nilimwambia hivyo, nikaahidi kujirekebisha.

Thursday, June 11, 2015

Kesi ya Raif Badawi: Mwanablogu wa Saudi Arabia

Raif Badawi ni mwanablogu wa Saudi Arabia ambaye anafahamika sana duniani kutokana na kuhukumiwa kifungo cha miaka kumi gerezani na viboko 1000. Alihukumiwa kwa kile kilichoitwa kuitukana dini ya u-Islam. Amekaa gerezani miaka miwili na tayari alishapigwa viboko 50 nje ya msikiti mjini Jeddah. Adhabu hiyo si nyepesi; inaweza kusababisha kifo.

Watu wengi duniani wanalaani hukumu hiyo. Wengi hawaoni ni kwa vipi Raif Badawi ameutukana u-Islam. Wengi wamechukizwa na hukumu hiyo kwa kuwa ni hujuma dhidi ya uhuru wa kutoa mawazo.

 Mawazo ya Raif Badawi yaliyosababisha hukumu dhidi yake ni ya kawaida sana kwa vigezo vyetu wa-Tanzania na wengine duniani. Lakini wahusika nchini Saudi Arabia wameendelea kusisitiza kuwa Raif Badawi anastahili hukumu hiyo. Kuna tetesi kuwa huenda akashtakiwa upya ili apewe hukumu kali zaidi, kukatwa kichwa, hukumu ambayo hutekelezwa sana Saudi Arabia.

Kesi ya Raif Badawi imeibua masuala ya ukiukwaji wa haki za binadamu nchini Saudi Arabia. Kuna mengi yanayoongelewa. Kwa mfano, ni marufuku Saudi Arabia kutoa mawazo yanayopingana na yale ya watawala na viongozi wa dini. Ni marufuku kwa watu wasio wa-Islam kujenga nyumba za ibada zao, kama vile makanisa, katika ardhi ya Saudi Arabia. Ni marufuku kuhubiri dini tofauti na u-Islam. Ni marufuku kwa wanawake kuendesha gari. Ni marufuku kwa wanawake kusafiri bila kibali cha mume au ndugu wa kiume.

Kuna kampeni kubwa sehemu mbali mbali duniani kulaani hukumu dhidi ya Raif Badawi. Sisi wanablogu wa Tanzania tunasimama wapi? Ni vema kukumbushana kuwa ukiona mwenzako ananyolewa, wewe tia maji.

Monday, June 1, 2015

Blogu Zangu Zimenisaidia

Hapa Chuoni St. Olaf kuna utaratibu unaomtaka kila mwalimu kuandika ripoti ya shughuli alizofanya katika mwaka wa shule unaoisha. Hizo ni shughuli za kitaaluma, yaani vitabu ulivyochapishwa, makala ulizochapisha, ushiriki wako katika mikutano ya kitaaluma, kazi ulizofanya katika uongozi wa vyama vya kitaaluma, kozi ulizotunga na kufundisha, uhariri katika majarida ya kitaaluma. Vile vile unaorodhesha huduma ulizotoa katika jamii nje ya chuo, kama vile ushauri ("consultancy"), na mihadhara katika mikutano ya vikundi na jumuia.

Nimekuwa na jadi ya kuandika mambo ya aina hiyo katika blogu hii ya hapakwetu na blogu ya ki-Ingereza. Katika kuandika ripoti yangu ya mwaka unaoisha, blogu zangu zimekuwa hazina ya kumbukumbu na taarifa nilizohitaji. Huu ni uthibitisho wa manufaa ya shughuli ninayofanya ya kublogu. Ninakumbuka kuwa niliwahi kuelezea namna blogu ilivyonisaidia darasani.

Watu wengine wanaandika kumbukumbu zao katika "diary." Lakini mimi kwa vile sina mazoea ya kufanya hivyo, nitaendelea kublogu kama ninavyofanya. Lengo ni kuhifadhi kumbukumbu. Tena, kwa kuwa nimezoea kuelezea shughuli zangu kwa upana, tangu chimbuko hadi matokeo, taarifa zangu zitaweza kutumika hata kwa kuandika kitabu. Ndoto ya kuandika kitabu cha aina hiyo nimekuwa nayo kitambo. Panapo majaliwa, nitaitekeleza.

Wednesday, January 28, 2015

Katika Blogu, Sijui Ninamwandikia Nani Zaidi Yangu Mwenyewe

Je, mwandishi wa blogu anamwandikia nani? Kwa mtazamo wangu, hili ni suali gumu. Naliona gumu kulitafakari, achilia mbali kulijibu.

Baada ya kuona ugumu wa suali hili, nimeamua kukiri kuwa ninajiandikia mwenyewe. Ndio maana makala ninazoandika aghalabu zinanihusu mimi mwenyewe, shughuli zangu, matatizo na mafanikio yangu, mategemeo yangu na kumbukumbu zangu.

Sipendi sana kuwaongelea watu wengine, wala sipendi sana kuongelea mambo kinadharia, bila kujihusisha mwenyewe. Naweza kusema kuwa ndivyo nilivyoandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Sijajificha nyuma ya pazia la nadharia au taaluma. Nimejiweka wazi kwa namna nilivyoweza.

Mwandishi Ernest Hemingway aliongelea suala hili vizuri alipofafanua dhana ya ukweli katika uandishi. Nilivyomwelewa, anasema kuwa ukweli katika uandishi ni kwa mwandishi kuifungua na kuiweka bayana nafsi yake.

Ningependa sana niweze kuandika namna hii aliyoongelea Hemingway. Ni ndoto inayovutia, sawa na nyota inayong'aa mbali, ambayo mtu unaifuata kwa hamu ingawa haifikiki. Lakini, naona huku ndiko kujiandikia mwenyewe.

Kusema kuwa kuna hadhira ninayoiandikia katika blogu yangu ni kama kuota ndoto. Ni kujidanganya. Nasema hivi sio tu kutokana na tafakari yangu mwenyewe, bali ninakumbuka makala ya kufikirisha ya Walter J. Ong, "The Writer's Audience is Always a Fiction."

(Picha hapo juu nilijipiga mwenyewe jana, kwa ajili ya matangazo ya mihadhara yangu Mankato)

Tuesday, February 8, 2011

Blogu Imenisaidia Darasani

Leo wakati muhula mpya unaanza hapa Chuoni St. Olaf, nimekutana na wanafunzi nitakaowafundisha somo la kuandika kwa ki-Ingereza. Kama kawaida, siku ya kwanza huwa ni ya kujitambulisha, kuelezea habari za somo, maana yake, falsafa na maadili yangu kama mwalimu, maana na mikakati ninayotumia katika kufundisha.

Katika kujitambulisha, huwa nawaeleza wanafunzi kuhusu nyumbani kwangu, shule nilizosoma, na nilivyoingia katika kazi ya ualimu, na imani yangu kuwa Mungu alitaka niwe mwalimu.

Leo wakati naanza kuelezea habari za nyumbani kwangu, nilikumbuka kuwa nilishaandika kwenye blogu. Basi, niliwasha kompyuta iliyomo darasani nikafungua blogu na wao wenyewe wakasoma kwenye skrini kubwa habari za Litembo.

Blogu imenisaidia kufikisha ujumbe wangu kwa ufanisi, kwani mbali ya maelezo kuna picha. Picha zinajieleza vizuri kuliko pengine hata maneno, jambo linalosisitizwa katika ule usemi kuwa picha ni sawa na maneno elfu. Niliwaambia kuwa nina picha nyingi za nyumbani kwangu na Tanzania kwa ujumla. Ni wazi kuwa ninazo fursa tele za kuendelea kuwajulisha walimwengu habari za kwetu.

Thursday, September 16, 2010

Kwa Nini Ninablogu

Wiki kadhaa zilizopita, wanablogu watatu tulikutana Sinza, Dar es Salaam, tukaongea kuhuau masuala mbali mbali. Kati ya mambo mengi, tuliondoka na suali: kwa nini tunablogu? Bofya hapa. Baada ya kulitafakari suali hili kiasi, napenda kuelezea kidogo kwa nini ninablogu.

Kwanza, nakumbuka kuwa nilianza kublogu baada ya kuhamasishwa na ndugu Freddy Macha na Jeff Msangi, mmiliki wa Bongo Celebrity. Hao wawili walifahamu kuhusu maandishi yangu, wakanishawishi nianzishe blogu. Nami nilifuata ushauri wao.

Nilianzisha blogu mbili: ya ki-Swahili, na ya ki-Ingereza. Nilijifunza na naendelea kujifunza huku nikiblogu. Katika harakati hiyo, Dada Subi, mmiliki wa Wavuti amekuwa akinisaidia, kama anavyowasaidia wanablogu wengine.

Kwangu mimi blogu ni ukumbi wa kuelezea mawazo, hisia, fikra na mambo yangu mengine, na hivi kuyahifadhi na kuwashirikisha wengine. Siblogu kwa imani kuwa nina ujuzi au busara kuliko watu wengine. Blogu ni baraza inayonikutanisha na wengine kwa mazungumzo, mijadala na kubadilishana mawazo.

Vile vile, ninablogu kwa sababu nimeona umuhimu wa blogu kwa upande wa lugha. Ninavyoandika ki-Swahili najiongezea uzoefu wa kutumia lugha hiyo ipasavyo. Hiyo ndio jitihada yangu, na hili ndilo lengo langu.

Mazoezi ni mazoezi. Tunapofanya mazoezi ya viungo daima, tunajijengea afya bora, na tunaanza kuusikia mwili ukikaa sawa. Kwa namna hiyo hiyo, kuandika kwa ki-Swahili kumenifanya niisikie akili yangu ikizidi kukaa sawa, kwa upande huu wa matumizi ya lugha. Nazidi kujiamini katika utumiaji wa lugha hii.

Katika blogu yangu ya ki-Ingereza, naandika kwa lengo la kuonyesha uandishi bora wa ki-Ingereza. Ni lugha ambayo nimeipenda tangu nilipoanza kujifunza, darasa la tatu, na naifundisha hapa katika Chuo cha St. Olaf, Minnesota.

Kublogu kumeniunganisha na watu wengi ambao wanasoma blogu zangu, kutoka pande zote za dunia. Inaleta faraja, kwa mfano, ninapotambua kuwa kitu fulani nilichoandika katika blogu kimekuwa ni msaada kwa mtu fulani. Kwa mfano, miezi kadhaa iliyopita, nilipata ujumbe kutoka kwa mama mmoja aliyeko Ujerumani.

Aliulizia namna ya kufika Mbamba Bay na mahali pa kulala akishafika kule, kwani alikuwa anapangia kuja Tanzania. Alisema kuwa aliniuliza kwa vile alisoma habari za Mbamba Bay kwenye blogu yangu. Nilimpa maelezo aliyohitaji. Wakati huu wote yeye alikuwa Ujerumani na mimi nilikuwa Marekani. Alikuja Tanzania mwaka huu na familia yake, wakati nami niko nchini. Tulionana Ubungo, kwenye kituo cha mabasi, kama inavyoonekana katika picha hii, wakiwa wamefurahi kununua nakala ya Matengo Folktales.

Sunday, August 22, 2010

Kukutana kwa Wanablogu

Katika ziara yangu Tanzania mwaka huu, pamoja na mengi mengine, nilipata fursa ya kukutana na wanablogu. Tarehe 7 Agosti nilikutana na Kamala na Chacha pale Sinza kama inavyoonekana katika picha hii.
Tuliongea na kubadilishana mawazo ya aina aina, kama alivyoeleza Kamala katika blogu yake. Chacha naye aliandika ujumbe kuhusu mkutano wetu. Bofya hapa.

Tarehe 17 Agosti, hapo hapo Sinza, nilikutana na mwanablogu Maggid Mjengwa. Bofya hapa.Tuliongea kuhusu mambo mengi, kuanzia gazeti la Kwanza Jamii, masuala ya blogu, yakiwemo masuala ya faida na kero zake.

Tuliongelea, kwa mfano, namna ya kuyachukulia maudhi ya baadhi ya watoa maoni kwenye hizi blogu. Tangu tulipokuwa tunaandika katika Kwanza Jamii, sisi wawili tumekuwa na msimamo kwamba ni bora kuwaacha watu waseme hata kama wanachosema kinaudhi, kwa msingi kuwa labda wanahitaji kufanya hivyo kwa manufaa yao kisaikolojia, mbali na kwamba tunazingatia suala la uhuru wa kutoa maoni na fikra. Ni msimamo mgumu unaohitaji uvumilivu, lakini labda ni bora kuwa na msimamo huu kuliko msimamo wa kuwazuia watu uhuru. Msimamo huu nimeuelezea kinaganaga katika kitabu changu cha CHANGAMOTO.

Naona kuwa suala la kukutana na wanablogu wenzangu Tanzania linazidi kuwa jadi. Nilianza kufanya hivyo mwaka jana, nilipokutana na mwanablogu maarufu Issa Michuzi. Waliofanya juhudi kuniunganisha na Issa Michuzi ni Maggid Mjengwa na Frederick Mboma. Hatimaye, Ndugu Mboma ndiye aliyenifikisha ofisini kwa Michuzi, tukaongea kuhusu masuala ya aina aina, hasa blogu. Bofya hapa.

Mikutano hii ya wanablogu ina manufaa mengi, kama walivyosema wanablogu wengine. Ni fursa ya kufahamiana na kubadilishana mawazo kuhusu masuala ya blogu na mengine. Katika mkutano wangu na Chacha na Kamala, jambo moja lililosisitizwa ni suala la kujitambua. Hao wawili wanajibidisha katika kufuatilia mada hii wakijumuika na wengine. Nami niliona ni vema nasi wanablogu tuwe tunatakafakari suala hili la kujitammbua. Kwa hivi, niliuliza suali: kwa nini tunablogu? Bofya hapa.

Mwaka jana, wazo la kuwakutanisha wanablogu wa Tanzania lilipendekezwa na kujadiliwa. Ingawa mkutano huu haukufanyika, wazo linastahili kufanyiwa kazi na kutekelezwa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...