Showing posts with label Utandawazi. Show all posts
Showing posts with label Utandawazi. Show all posts
Tuesday, January 14, 2020
Tuesday, December 17, 2019
Kofia ya CCM Nchini China
Naleta picha ya ujumbe wa CCM kwenye kikao na wenyeji wao mjini Shanghai, China, mwaka 2018. Hapo mezani upande wa kushoto kuna kofia ya CCM. Yawezekana walikwenda ziarani na magwanda yao na vikofia. Je, kuna sababu gani mimi kuandika ujumbe kuhusu kofia? Sina jambo la maana zaidi la kuongelea? Kwa nini nisiongelee madhumuni ya ziara na mafanikio yake?
Ninaandika ujumbe huu kama mtafiti, mwandishi, na mtoa ushauri juu ya masuala ya utamaduni na utandawazi. Nimekuwa nikifanya shughuli hizo hapa Marekani na Tanzania pia, ambako nimeendesha warsha mara kadhaa kuanzia mwaka 2008 katika miji ya Arusha, Tanga, na Dar es Salaam.
Ninajaribu kuwaelewesha watu kuwa tofauti za tamaduni zina athari kubwa, hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Tunapokutana na watu wa tamaduni tofauti na wetu, tuwe makini. Tunaweza tukaelewana vibaya, au tunaweza tusielewane. Ni muhimu tujielimishe kuhusu tofauti hizo kabla hayajatupata hayo.
Kofia ya CCM ni sehemu ya vazi rasmi la wana CCM. Ni utambulisho wao. Hata mimi ambaye sina chama ninawatambua kwa mavazi yao. Vyama vingine navyo vina mavazi yao. Kwa hapa nchini Tanzania, hakuna utata juu ya hayo mavazi. Lakini je, hali ni hiyo hiyo nje ya Tanzania kwenye tamaduni tofauti?
Nchini China, kofia ya kijani ni mkosi. Mwanaume kuvaa kofia ya kijani maana yake anatangaza kwamba mke wake ni mzinzi.
Kuhusu asili ya tafsiri hii ya waChina kuhusu kofia ya kijani, maelezo yanatofautiana. Baadhi ya maelezo ni kwamba zamani za kale, ndugu wa malaya walilazimishwa kuvaa kofia ya kijani wabebe aibu. Maelezo mengine ni kwamba zamani za kale, wahudumu katika madanguro walikuwa wanavaa kofia za kijani. Lakini kama nilivyogusia, maelezo yanahitilafiana. Ila jambo ambalo halina utata ni kwamba katika utamaduni wa China, kofia ya kijani ni mkosi kwani inatangaza habari ya uzinifu wa mke.
Sasa fikiria hiyo ziara ya ujumbe wa CCM China. Wafikirie wako sehemu mbali mbali kama wageni rasmi, wamevalia kofia za kijani. Bila shaka, wenyeji wao walifanya ukarimu na heshima kama ilivyo desturi. Lakini bila shaka, makada hao wa CCM watakuwa wameacha gumzo na taswira ambayo hawakutegemea.
Katika warsha ambazo nimeandaa Tanzania tangu mwaka 2008, waTanzania wachache sana wamekuwa wakihudhuria. Mbali ya warsha, nimekuwa nikielezea katika blogu zangu masuala ya athari za tofauti za tamaduni katika dunia ya utandawazi wa leo. Nimeandika hata kitabu, kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho kinapatikana Tanzania pia, kutoka katika maduka ya Kimahama (Arusha), Soma Book Cafe (Dar es salaam), na A Novel Idea (Arusha na Dar es Salaam).
Pamoja na kujaribu njia zote hizo, nimeona kuwa labda, kwa kuandika ujumbe huu kuhusu kofia ya CCM nchini China, waTanzania watanielewa vizuri na watachukua hatua stahiki katika masuala yote husikka, iwe ni mahusiano binafsi, biashara za kimataifa, utalii, diplomasia na kadhalika.
Ninaandika ujumbe huu kama mtafiti, mwandishi, na mtoa ushauri juu ya masuala ya utamaduni na utandawazi. Nimekuwa nikifanya shughuli hizo hapa Marekani na Tanzania pia, ambako nimeendesha warsha mara kadhaa kuanzia mwaka 2008 katika miji ya Arusha, Tanga, na Dar es Salaam.
Ninajaribu kuwaelewesha watu kuwa tofauti za tamaduni zina athari kubwa, hasa katika dunia ya utandawazi wa leo. Tunapokutana na watu wa tamaduni tofauti na wetu, tuwe makini. Tunaweza tukaelewana vibaya, au tunaweza tusielewane. Ni muhimu tujielimishe kuhusu tofauti hizo kabla hayajatupata hayo.
Kofia ya CCM ni sehemu ya vazi rasmi la wana CCM. Ni utambulisho wao. Hata mimi ambaye sina chama ninawatambua kwa mavazi yao. Vyama vingine navyo vina mavazi yao. Kwa hapa nchini Tanzania, hakuna utata juu ya hayo mavazi. Lakini je, hali ni hiyo hiyo nje ya Tanzania kwenye tamaduni tofauti?
Nchini China, kofia ya kijani ni mkosi. Mwanaume kuvaa kofia ya kijani maana yake anatangaza kwamba mke wake ni mzinzi.
Kuhusu asili ya tafsiri hii ya waChina kuhusu kofia ya kijani, maelezo yanatofautiana. Baadhi ya maelezo ni kwamba zamani za kale, ndugu wa malaya walilazimishwa kuvaa kofia ya kijani wabebe aibu. Maelezo mengine ni kwamba zamani za kale, wahudumu katika madanguro walikuwa wanavaa kofia za kijani. Lakini kama nilivyogusia, maelezo yanahitilafiana. Ila jambo ambalo halina utata ni kwamba katika utamaduni wa China, kofia ya kijani ni mkosi kwani inatangaza habari ya uzinifu wa mke.
Sasa fikiria hiyo ziara ya ujumbe wa CCM China. Wafikirie wako sehemu mbali mbali kama wageni rasmi, wamevalia kofia za kijani. Bila shaka, wenyeji wao walifanya ukarimu na heshima kama ilivyo desturi. Lakini bila shaka, makada hao wa CCM watakuwa wameacha gumzo na taswira ambayo hawakutegemea.
Katika warsha ambazo nimeandaa Tanzania tangu mwaka 2008, waTanzania wachache sana wamekuwa wakihudhuria. Mbali ya warsha, nimekuwa nikielezea katika blogu zangu masuala ya athari za tofauti za tamaduni katika dunia ya utandawazi wa leo. Nimeandika hata kitabu, kiitwacho Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho kinapatikana Tanzania pia, kutoka katika maduka ya Kimahama (Arusha), Soma Book Cafe (Dar es salaam), na A Novel Idea (Arusha na Dar es Salaam).
Pamoja na kujaribu njia zote hizo, nimeona kuwa labda, kwa kuandika ujumbe huu kuhusu kofia ya CCM nchini China, waTanzania watanielewa vizuri na watachukua hatua stahiki katika masuala yote husikka, iwe ni mahusiano binafsi, biashara za kimataifa, utalii, diplomasia na kadhalika.
Sunday, June 3, 2018
Vitendea Kazi vya Kampuni Yangu

Shughuli zangu hizi zimekuwa na mafanikio makubwa, kwa maana kwamba nimewasaidia watu kuelewa na kuepukana na mambo ambayo yanaweza kusababisha migogoro na kutoelewana. Wale ambao tayari walishakumbana na migogoro na kutoelewana nimewasaidia kufahamu kwa nini walijikuta katika migogoro na kutoelewana. Lakini mimi mwenyewe nimefanikiwa pia kujifunza mengi katika shughuli zote hizo.
Napenda kuelezea siri moja kubwa ya mafanikio haya. Siri hiyo ni kujielimisha kwa kutumia vitabu. Vitabu ndio vitendea kazi vyangu. Sichoki kununua na kusoma vitabu. Kulingana na shughuli za kampuni yangu, ninanunua na ninasoma vitabu kuhusu masuala kama utandawazi, utamaduni, na saikolojia. Jana, kwa mfano, bila kutegemea, nilikiona kitabu kiitwacho Riding the Waves of Culture, katika duka la Half Price Books, mjini Apple Valley. Nilipokiona tu, nilitambua kuwa kitakuwa kitendea kazi muhimu.
Mbali na kutumia vitabu vya wengine, ninatumia pia kitabu nilichoandika mwenyewe, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitabu hiki kilitokana na uzoefu nilioongelea hapa juu. Si mimi tu ambaye ninakichukulia kitabu hiki kama kitendea kazi muhimu. Mifano ni profesa na mwandishi maarufu Becky Fjelland Brooks, ambaye aliakiongelea kitabu katika blogu yake. Mzee Patrick Hemingway, ambaye aliwahi kuishi Tanzania miaka yapata ishirini na tano, aliwahi kuniambia kuwa kitabu hiki ni "a tool of survival" yaani kimbilio la usalama.
Hili suala la kuviona vitabu kama vitendea kazi ni muhimu. Hainiingii akilini mtu aanzishe biashara, kwa mfano, halafu asitafute na kusoma vitabu au maandishi mengine juu ya uendeshaji wa biashara. Atafanikishaje malengo yake kama hafahamu vitu kama saikolojia ya binadamu, ambao ndio wateja wake? Atafanikiwaje kama hafahamu namna ya kuwasiliana na watu? Kama wateja wake ni wa tamaduni tofauti na utamaduni wake, ni muhimu mno afahamu tofauti hizo.
Nilivutiwa na msimamo wa Mama Barbro Finskas Mushendwa, mmiliki wa kampuni ya utalii ya J.M Tours, yenye makao yake Arusha, Tanzania. Baada ya kusoma kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, aliamua kununua nakala kadhaa kwa ajili ya wafanyakazi wake, ambao walikuwa ni madreva wa watalii. Aliona haraka kuwa kitabu hiki kinafaa kama kitendea kazi na madreva wake walinithibitishia hivyo, kama nilivyoripoti katika blogu ya ki-Ingereza.
Mmiliki wa kampuni yoyote anajua ulazima wa vitendea kazi kama vile magari na kompyuta, sawa na mkulima navyojua ulazima wa jembe na shoka. Lakini sijui ni wamiliki wa makampuni na wafanya biashara wangapi wa Tanzania wenye mtazamo kama wa Mama Mushendwa, wa kutambua kuwa vitabu ni vitendea kazi. Ninaona wanaanzisha kampuni au biashara na kuziendesha kimazoea, au kwa kutegemea kudra ya Mungu au hata waganga wa kienyeji. Daima ninaona matangazo ya waganga wa kienyeji wakinadi dawa za mafanikio kibiashara.
Ninapoongelea mada hii ya vitabu kama vitendea kazi, ninakumbuka juhudi aliyofanya Mwalimu Nyerere katika kutekeleza kile alichoita elimu yenye manufaa. Aliwahimiza watu kujisomea ili kuboresha shughuli walizokuwa wanafanya. Chini ya uongozi wake, vilichapishwa na kusambazwa vitabu kuhusu kilimo, uvuvi, useremala, na kadhalika. Ninakumbuka kwamba kijijini kwangu, vitabu hivyo vilihifadhiwa katika nyumba ya baba yangu.
Pamoja na mimi kutumia vitabu vya wengine kama vitendea kazi, ninashukuru kwamba nami ni mwandishi. Ninapangia kuendelea kuandika ili kuchangia ufanisi katika shughuli zangu na za wengine.
Friday, February 17, 2017
Umuhimu wa Kuzifahamu Tamaduni za Wengine

Umuhimu wa kuzifahamu tofauti za tamaduni unaonekana wazi wazi wakati tunapokumbana na matatizo katika mahusiano yetu na watu wa tamaduni ambazo si zetu. Tusijidanganye kwamba jambo hilo ni la kinadharia tu na kwamba halituhusu. Miaka michache iliyopita, wafanya biashara wa Tanzania walikwenda Oman kushiriki maonesho ya biashara. Walipata shida kutokana na kutojua utamaduni wa watu wa Oman. Taarifa hiyo iliandikwa katika blogu ya Michuzi.
Suala hili haliwahusu wafanya bashara tu, bali wengine pia, kama vile wanafunzi wanaokwenda nchi za nje, wanadiplomasia, watu wanaokwenda mikutanoni, na kadhalika. Kwa kuzingatia hayo, na kwa kuwa nimekuwa nikifanya utafiti katika masuala hayo, nimekuwa nikipata mialiko ya kutoa ushauri kwa jumuia na taasisi mbali mbali hapa Marekani. Vyuo vya Marekani, kwa mfano, vinapopeleka wanafunzi nchi za nje, kama vile nchi za Afrika, vinazingatia suala la kuwaandaa wanafunzi kwa kuwaelimisha kuhusu utamaduni wa huko waendako. Mwaka hadi mwaka nimealikwa kutoa elimu hiyo.
Nimewahi pia kuendesha semina Tanzania, kwenye miji ya Arusha, Tanga, na Dar es Salaam. Vile vile, kwa kuombwa na ubalozi wa Marekani nchini Tanzania, niliwahi kutoa mihadhara Zanzibar na Pemba, juu ya utamaduni wa Marekani, kama nilivyoelezea katika blogu hii.
Kwa jinsi ninayofahamu umuhimu wa suala hili, nimekuwa nikikumbushia mara kwa mara kila ninapoweza. Kwa mfano, uhusiano ulipoanza kuimarika baina ya Tanzania na u-Turuki, nilikumbushia suala hilo katika blogu hii. Ningependa kuona suala hili la athari za tofauti za tamaduni linapewa kipaumbele katika maisha yetu kwani kulipuuzia ni kujitakia matatizo yasiyo ya lazima. Hii ndio sababu iliyonifanya nianzishe kampuni ya kutoa elimu na ushauri iitwayo Africonexion: Cultural Consultants.
Wednesday, January 18, 2017
Vitabu Nilivyojipatia Leo

Leo asubuhi, kama kawaida, nilienda chuoni St. Olaf kufundisha. Nilipoingia katika jengo la maktaba, ambamo pia ni makao ya idara yangu ya ki-Ingereza, nilipita kwenye meza ambapo huwekwa vitabu na makabrasha kwa ajili ya yeyote anayehitaji. Niliona meza imejaa vitabu kuliko siku nyingine yoyote iliyopita, nikaamua kuviangalia.
Niliona kuwa vyote vilikuwa vitabu vya taaluma, hasa masuala ya wanawake na jinsia. Niliamua kujichukulia vitatu, baada ya kuangalia ndani na kuona maelezo ya vitabu hivi. Kitabu kimojawapo ni Sex & Power, kilichotungwa na Susan Estrich. Niliona maelezo kuwa mwandishi alikuwa profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha Harvard na baadaye profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha California ya Kusini. Ameandika vitabu kadhaa na makala mbali mbali. Alikuwa mwanamke wa kwanza kuwa rais wa Harvard Law Review. Huenda msomaji wa taarifa hii utakumbuka kuwa hiki ni cheo ambacho Barack Obama aliwahi kushika. Kutokana na mada ya kitabu, na orodha ya sura zake niliona kuwa kitabu hiki kitanielimisha sana kuhusu nafasi ya wanawake katika jamii.
Kitabu cha pili kilichonivutia kwa namna ya pekee ni Globalization: The Making of World Society, ambacho kimetungwa na Frank J. Lechner. Kama tunavyofahamu, mada ya utandawazi inavuma sana miongoni mwa wanataaluma, wanasiasa, na jamii kwa ujumla. Hata hivi, mitazamo kuhusu nini maana ya utandawazi, chimbuko lake, faida na hasara zake, ni masuala ambayo yanajadiliwa na yamegubikwa na utata.
Mimi mwenyewe, kwa miaka kadhaa, nimetafakari suala la utandawazi, nikilihusisha na tofauti za tamaduni. Nimewahi hata kuendesha warsha kadhaa, nchini Tanzania, katika miji ya Arusha, Dar es Salaam, na Tanga. Kwa hivi, nilipokiona kitabu cha Globalization: The Making of World Society, nilikuwa na hamu ya kukisoma. Hiki kitaongeza idadi ya vitabu vyangu kuhusu utandawazi.
Kitabu cha tatu, Behind the Veil in Arabia: Women in Oman, kilichoandikwa na Unni Wikan, kilinivutia pengine zaidi ya hivi vingine. Nilipoona jina la kitabu hiki, nilikumbuka mara majina ya vitabu vingine, kama vile Beyond the Veil, cha Fatima Mernissi wa Morocco. Suala la wanawake katika nchi za ki-Arabu limeshika nafasi ya pekee kichwani mwangu kutokana na kozi niliyoanzisha na ninaifundisha, "Muslim Women Writers."
Simaanishi, na mtu asidhani, kwamba wa-Arabu wote ni wa-Islam, bali kuna suala la jinsi utamaduni unavyoingiliana na dini kiasi kwamba pamoja na tofauti za dini, kuna mambo kama mila, desturi, na lugha, ambayo yanawaungamisha wa-Arabu.
Katika kufundisha kozi ya "Muslim Women Writers" imedhihirika kuwa vazi kama hijab ni suala la utamaduni zaidi kuliko dini. Qur'an inasema wanawake wajisitiri na wainamishe macho, lakini haisemi wavae nini. Hili ni suala la kila utamaduni, na ndio maana mavazi ya wanawake wa ki-Islam katika tamaduni mbali mbali yanahitilafiana.
Maktaba yangu imetajirika leo kwa kuongezewa vitabu hivi muhimu. Ni raha iliyoje kujipatia hazina kubwa namna hii bila gharama yoyote kwa upande wangu.
Monday, October 10, 2016
Ki-Ingereza Kama Lugha ya Ulimwengu

Nilikumbuka kwamba nina kitabu cha David Crystal, English as a Global Language, ambacho nilikinunua miaks michache iliyopita, ila nilikuwa nimekipitia juu juu tu. Leo nimeamua kukisoma, na ninaona jinsi maelezo yake kuhusu lugha ya ki-Ingereza yanavyofungamana na suala la utandawazi. Kwa mfano, katika utangulizi wake, mwandishi anasema,
"We have as yet no adequate typology of the remarkable range of language contact situations which have emerged as a consequence of globalization, either physically (e.g. through population movement and economic development or virtually (e.g. through Internet communication and satellite broadcasting)." (xi)
Kitu kimoja kilichonifanya nikumbuke kitabu cha David Crystal ni kuwa huyu ni mtaalam maarufu ulimwenguni wa masuala ya lugha. Nilipokuwa mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuanzia mwaka 1973, nikisomea "Literature" na "English," ndipo niliposoma maandishi ya Crystal, sambamba na mabingwa wengine, kama vile Frank R. Palmer, John Lyons, Noam Chomsky, Sydney Greenbaum, na Randolph Quirk. Kumbukumbu hiyo ndiyo ilinifanya ninunue kitabu cha Crystal, English as a Global Language miaka michache iliyopita. Sasa, kwa kuwa ninafuatilia suala la utandawazi, ninaona nilifanya vizuri kununua kitabu hiki.
Pamoja na kuelezea jinsi ki-Ingereza kilivyofanikiwa kuenea duniani na kinavyoendelea kuiteka dunia kama lugha ya mawasiliano ulimwenguni iliyo muhimu kuliko zote, Crystal anabainisha pia kuwa hatuwezi kuwa na uhakika kama hali hii itaendelea hivi siku za usoni. Kama nilivyoeleza katika ujumbe wa jana, nikinukuu kitabu cha People Before Profit, utandawazi hausambai bila upinzani kutoka katika jamii na tamaduni mbali mbali zinazotaka kulinda jadi na misingi yao.
Ni hivi hivi katika kuenea kwa ki-Ingereza. Crystal anatuelekeza kwenye kitabu cha Tom McArthur, The English Language, na anatumabia kuwa McArthur
"adopted a more synchronic perspective, moving away from a monolithic concept of English. His primary focus was on the kinds of variation encountered in the language as a consequence of its global spread. He suggested that English was undergoing a process of radical change which would eventually lead to fragmentation into a 'family of languages.'" (x)
Hilo wazo la ki-Ingereza kugawanyika katika vilugha mbali mbali linasisimua akili. Lakini, hata kama ki-Ingereza kitaishia kuwa vilugha vingi, ninategemea kuwa bado kutakuwa na misingi itakayodumu katika vi-Ingereza hivyo na kuendelea kuwawezesha watumiaji kuwasiliana na kuelewana. Hata wakati huu, tayari ki-Ingereza kina lahaja nyingi, sawa na ki-Arabu, ki-China, ki-Swahili, na lugha zingine.
Jambo la muhimu la kuzingatia, kwa nchi kama Tanzania, ni hoja ya msingi ya English as a Global Language, kwamba hakuna namna ya kukizuia ki-Ingereza kutawala dunia kama lugha ya mawasiliano. Tupende tusipende, lazima tutafute namna ya kuhakikisha kuwa tunaijua lugha hiyo. Tusipumbazwe na siasa reja reja zilizovaa gwanda la utaifa, tukasahau kwamba ki-Ingereza ndiyo nyenzo na silaha itakiwayo katika mapambano ya ulimwengu wa utandawazi wa leo na kesho.
Saturday, October 8, 2016
People Before Profit: Kitabu Kuhusu Utandawazi

Kwanza, niseme kuwa kitabu hiki kina utangulizi ulioandikwa na Noam Chomsky. Hilo pekee ni ishara ya thamani ya kitabu hiki, kwani Chomsky ni mchambuzi maarufu wa masuala ya ulimwengu kwa mtazamo wa kimaendeleo. Ninamheshimu sana, kama ninavyowaheshimu wachambuzi kama Seymour Hersh na Amy Goodman.
People Before Profit ni hazina ya elimu. Kinafafanua dhana ya utandawazi. Kwanza kinaelezea ukale wa utandawazi, na kwamba utandawazi una historia ndefu. Haukuanza zama zetu hizi, bali umekuwepo kwa miaka maelfu na maelfu, ukibadilika katika kila zama.
Pili kitabu kinaelezea uhusiano wa utandawazi na tekinolojia, kama vile mapinduzi ya miundombinu na viwanda. Tatu, kitabu kinaelezea mahusiano ya utandawazi na utamaduni, na hasa katika mazingira ya leo, kuna suala la mahusiano ya utandawazi na itikadi, kama vile demokrasia.
Kuna dhana kadhaa juu ya utandawazi ambazo tunapaswa kuzihoji, kwa mfando dhana ya kwamba utandawazi unaondoa tofauti miongoni mwa nchi na jamii mbali mbali, na kuifanya dunia iwe na sura moja. Dhana hii imekuwa ikijadiliwa sana.
Inahojiwa, kwa mfano na watu wanaosema kwamba pamoja na juhudi za utandawazi kuufunika ulimwengu, kuna pia nguvu za jamii na tamaduni mbali mbali zinazopambana ili kujilinda, kujihami, na kuendelea kuwepo kwa misingi tofauti na ile ya utandawazi. Nami, katika warsha zangu, kama zile nilizowahi kuendesha Arusha na Dar es Salaam, nilijaribu kuibua masuala haya.
Kifupi ni kwamba kitabu hiki kinaibua masuala muhimu ya kuelimisha kuhusu hiki kinachoitwa utandawazi. Ninakipendekeza kwa yeyote anayethamini elimu.
Thursday, September 22, 2016
David Robinson Ahutubia Chuo Kikuu cha Minnesota

David Robinson aliamua kwenda kuishi Tanzania, kwenye kijiji cha Bara wilaya ya Mbozi. Alijitambulisha kwa wanakijiji akajieleza kuwa ni mtoto wa Afrika aliyepotezewa ughaibuni kwa karne kadhaa, katika utumwa, na sasa ameamua kurudi nyumbani. Wanakijiji walimpa shamba akaanza kulima kahawa. Aliungana na wanakijiji wengine, wakaanzisha chama cha ushirika kiitwacho Sweet Unity Farms

Pichani hapa kushoto anaonekana David Robinson, Limi Simbakalia, mwanafunzi m-Tanzania wa Chuo cha St. Olaf ambapo ninafundisha, na mimi.
Kuna taarifa nyingi mtandaoni juu ya David Robinson na Sweet Unity Farms, yakiwemo mahojiano naye. Taarifa moja nzuri kabisa ni hii hapa. Aidha, kuna taarifa nyingi juu ya baba yake, mwanariadha Jackie Robinson. Mfano mmoja ni filamu hii hapa chini, inayoonyesha magumu aliyopitia na alivyopambana kishujaa katika mazingira ambayo yalikuwa mabaya sana kwa wa-Marekani Weusi.
Wednesday, October 28, 2015
Maprofesa na Wajibu wa Kuandika

Baadhi yetu wa-Tanzania tumeliwazia na kuliongelea suala hili kwa miaka mingi, kwa manufaa ya jamii, tukiliunganisha na masuala kama sera ya elimu, matatizo ya uchapishaji, na kukosekana kwa utamaduni wa kununua na kusoma vitabu.
Kilichonifanya nirejeshe mada hii leo ni kwamba nimejikumbusha tamko la Rais Kikwete, "Maprofesa Wananisikitisha," ambalo lilijadiliwa katika blogu yangu hii na blogu ya Profesa Matondo. Mambo yaliyosemwa katika majadiliano yale ni muhimu na yataendelea kuwa muhimu. Wajibu wa profesa wa kuandika, kama njia mojawapo ya kufundisha na kuchangia maendeleo ya taaluma ni jambo lililo wazi.
Hata hivi, kwa kuzingatia kuwa dunia inabadilika muda wote, kuna umuhimu wa kulitafakari suala hili kwa mtazamo unaozingatia mabadiliko haya. Fikra zilizokuwa sahihi miaka michache iliyopita, huenda zimepitwa na wakati. Wataalam katika nyanja mbali mbali, kama vile ujasiriamali, elimu, na biashara wanatufundisha kuwa mabadiliko yanatulazimisha kuwa wabunifu na wepesi wa kubadilisha fikra, mahusiano, mbinu na utendaji wetu. Ndio maana ni muhimu kusoma daima na kujielimisha kwa njia zingine.
Katika dunia ya utandawazi wa leo, ambamo tekinolojia mbali mbali zinastawi, zikiwemo tekinolojia za mawasiliano, tunawajibika kuwa na fikra mpya kuhusu usomaji, uchapishaji na uuzaji wa vitabu, na kadhalika. Shughuli nyingi sasa zinafanyika mtandaoni, ikiwemo ufundishaji, kama nilivyowahi kugusia katika blogu hii. Tunawajibika kufunguka akili na kuacha kujifungia katika hiki tunachokiita sera ya elimu ya Tanzania. Je, inawezekana kuandika kitabu chenye umuhimu kwa Tanzania lakini si kwa ulimwengu? Taaluma inaweza kufungiwa katika mipaka ya nchi? Kuna dhana katika ki-Ingereza tunayopaswa kuitafakari: "The local is global."
Naona ni jambo jema kuirejesha mada hii, tuendelee kuitafakari katika mazingira ya leo. Lakini, naona tusome kwanza mjadala uliofanyika katika blogu hii na blogu ya Profesa Matondo.
Wednesday, July 22, 2015
Mdau Kanikumbuka

Mwanzoni mwa wiki hii, tarehe 19, nilipata ombi la urafiki katika Facebook. Nilivyoona jina la mhusika, Sandy, nilihisi kuwa si jina geni. Nilipoangali picha yake, nilikumbuka kuwa ni mama aliyewahi kunitembelea hapa Chuoni St. Olaf akiwa na rafiki yake, Desemba 2011. Niliandika habari za ujio wao katika blogu hii. Bila kuchelewa, nilikubali mwaliko wa urafiki.
Jana nimepata ujumbe wa mama huyu katika Facebook. Wakati tulipoonana, huyu mama na mwenzake walinunua vitabu vyangu, na aliniambia kuwa nakala ya Africans and Americans: Embracing Cultural Differences alikuwa anamnunulia rafiki yake ambaye alikuwa anapanga safari ya kwenda Afrika.
Kwa bahati mbaya tulipoteana kwa miezi mingi. Hatukuwa na mawasiliano. Baada ya kuungana tena katika Facebook, jana huyu mama ameniandikia ujumbe mfupi: My friend loved your book about the African culture. She had a wonderful experience.
Nimefurahi. Ni jambo la kushukuru kukumbukwa na mdau namna hii. Inaonyesha kuwa tulivyokutana mara ya kwanza tulikutana kwa uzuri na kumbukumbu zikabaki. Nashukuru pia kusikia kuwa rafiki ya huyu mama amekifurahia kitabu changu na safari yake ya Afrika.
Taarifa za aina hii kutoka kwa wadau wangu nazipata muda wote. Zinanipa raha maishani na hamasa ya kuendelea kufanya ninayofanya kama mwandishi na mtoa ushauri. Kuridhika na kufurahi kwa wadau ni tunu kubwa kwangu kuliko malipo ya fedha. Ninamshukuru Mungu kwa yote. Ninamwomba aendelee kunipa uzima siku hadi siku, na akili timamu, niweze kuendelea na majukumu.
Wednesday, January 14, 2015
"Leading Beyond the Walls:" Kitabu Murua

Kwenda na wakati kunahitaji wepesi wa kubadilika kifikra, kimwenendo, kimfumo na hali zingine, ili kumudu mahitaji na hali halisi ya mabadiliko yanayotokea ulimwenguni, ambayo hayakwepeki. Mafanikio ya shirika, taasisi, au kampuni
yanategemea utayari wa kujibadili. Mazoea ni kipingamizi kikubwa cha mafanikio; ni kama kuta ambazo tumejizungushia. Jukumu letu, ambalo halikwepeki, ni kuvunja hizo kuta, tuwe na uwanja na upeo usio na mipaka.
Wengi wa watunzi wa makala zilizomo kitabuni humu nilikuwa sijawahi hata kuwasikia, isipokuwa Joseph S. Nye, Jr., Stephen R. Covey, na Peter F. Drucker, ambaye niliwahi kusoma andiko lake mojawapo. Kati ya makala ambazo nilivutiwa nazo hata kabla ya kuzisoma ni "And the Walls Came Tumbling Down" (Jim Collins), "Dissolving Boundaries in the Era of Knowledge and Custom Work" (Sally Helgesen), "Culture is the Key" (Regina Herzlinger, "New Competencies for Tomorrow's Global Leader" (Marshall Goldsmith, Cathy Walt), na "Creating Success for Others" (Jim Belasco).
Kila makala ambayo nimesoma katika kitabu hiki imenipanua mawazo. Nimegundua mambo ya maana ambayo yataboresha mihadhara ninayotoa kwa jumuia, taasisi na makampuni. Nawazia, kwa mfano, mihadhara niliyotoa kwenye kampuni ya RBC Wealth Management.
Ninashukuru kuwa nilinunua kitabu hiki, ingawa sikumbuki ilikuwa lini. Nina ari kubwa ya kumaliza kusoma insha zote zilizomo, na nina hakika kuwa, Mungu akinijalia uzima, nitazisoma tena na tena.
Sunday, December 21, 2014
Kitabu Kingine: "A Goal is a Dream With a Deadline"

Kitabu hiki ni tofauti na vingine kwani ni mkusanyo wa misemo ya busara kuhusu mambo kama kujiwekea malengo, kustahimili matatizo, kutafuta masoko au wateja, kujiwekea maamuzi na kuyatekeleza kwa dhati na bila kuchelewa, kuwasikiliza wateja kwa makini na kuwahudumia vizuri, kuzingatia ubunifu, kupunguza urasimu, na kujiamini. Hayo ni baadhi ya yaliyomo katika kitabu hiki.
Sura zote za kitabu hiki zina mambo muhimu. Kwa vile mimi ninashughulika na kutoa ushauri kwa jumuia, taasisi, makampuni, na watu binafsi kuhusu tofauti za tamaduni na athari zake, nimevutiwa sana na sura ya kitabu hiki iitwayo "Going Global." Baadhi ya mawaidha yaliyomo katika sura hii ni haya: "Never assume that business is conducted in a foreign country just as it is at home" (uk. 146), "Learn about your host's people by reading about their history and culture" (uk. 147), " "Always assume that time will be handled differently in a foreign country" (uk. 147), "Latin Americans may refuse to do business with you if you are too serious. So lighten up and slow down" (uk. 151), "In Asia, learn when "maybe" really means "no" (uk. 151).
Mawaidha haya yanafanana na yale ninayotoa na kuyafafanua katika mihadhara na warsha zangu. Yamo katika kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, na pia mara moja moja katika blogu hii.
Nimejifunza mambo kadhaa muhimu katika kusoma A Goal is a Dream With a Deadline, na nakipendekeza kwa yeyote anayetaka mabadiliko yenye manufaa katika fikra, shughuli, maisha yake na ya jamii.
Thursday, December 29, 2011
Mahojiano na Profesa Mbele, "Kombolela Show"
Nimeona niwaletee wadau mahojiano niliyofanyiwa katika "Kombolela Show," Oktoba 2, 2010. Mwendesha mahojiano alikuwa Metty Nyang'oro. Kwa jinsi mtandaoni kunavyofurika taarifa, nimeona si vibaya kuyaleta tena mahojiano haya, ili wadau wayasikie na kuyatafakari na kuchangia, endapo watajisikia kufanya hivyo, kwani elimu haina mwisho, wala haina mwenyewe.
Tuesday, July 5, 2011
Ugali wa Yanga

Wa-Tanzania walipolalamikia unga huo, Mwalimu Nyerere alijibu kwa ukali kuwa wasiotaka Yanga ni watu wasio na shida. Naomba wadau wenzangu wa wakati ule wanisahihishe kama nimepotosha.
Sio kwamba tulikula Yanga miaka yote ya utawala wa Mwalimu Nyerere, na sio kwamba Mwalimu Nyerere alitaka Yanga ndio iwe chakula cha wa-Tanzania, au kwamba aliifurahia hali hiyo. Nawaomba wadau wanikumbushe ni mwaka upi au miaka ipi ambayo tulipata dhiki hiyo ya kula Yanga.
Je, tunalitafsiri vipi suala la unga wa Yanga? Kwa mtazamo wangu, kuna kipengele muhimu cha tofauti za tamaduni. Tofauti hizi zinajitokeza katika mambo mengi, na kwa namna nyingi, likiwamo hili suala la vyakula.
Tofauti za tamaduni zinaweza kuathiri kukubalika au kutokukubalika kwa bidhaa. Kwa mfano, namna bidhaa inavyotangazwa katika jamii au utamaduni fulani na kuwavutia watu inaweza ikawachefua watu wa jamii na utamaduni tofauti.
Hata rangi zinaweza kuibua hisia tofauti katika tamaduni mbali mbali. Rangi ya bidhaa inayowavutia watu wa utamaduni fulani inaweza kuwachefua watu wa utamaduni tofauti. Mfanyabiashara anaweza kuhujumu biashara yake kwa vile tu ameitangaza kwa kutumia rangi fulani au bidhaa yenyewe ina rangi isiyokubalika katika jamii fulani.
Katika utamaduni wetu wa-Swahili, ambao tunakula ugali, unga wa manjano haukubaliki. Kama ni unga wa mahindi, tunataka uwe mweupe. Hii ndio jadi tuliyozoea. Ni sehemu ya utamaduni wetu. Wengine wanatumia unga wa muhogo au ulezi. Lakini Yanga haikubaliki.
Lakini Marekani, Yanga iko kila mahali, sambamba na unga mweupe. Mwanzoni, katika kuishi kwangu Marekani, nikienda dukani, nilikuwa naikwepa kabisa Yanga. Lakini kidogo kidogo nilianza kuitumia, hadi nikafikia hatua ya kuupenda kabisa ugali ya Yanga.
Uamuzi wa kuleta Yanga Tanzania haukuzingatia suala la tofauti za tamaduni. Sijui ni nani aliyefanya uamuzi ule, lakini naamini haukuwa kwa nia mbaya. Kilichokosekana ni elimu sahihi. Nahisi wangejua wangeweza kubadilisha na kuleta unga mweupe. Hapangetokea manung'uniko, wala jazba za Mwalimu Nyerere.
Suala la ugali wa Yanga ni kielelezo kidogo cha masuala yanayoikabili dunia katika utandawazi wa leo, na masuala haya yatazidi kuongezeka kwa kadri dunia inavyozidi kuwa kijiji. Katika maandishi, warsha na mihadhara, najaribu kuelezea masuala hayo. Ni muhimu sana, kama ninavyosisitiza katika kitabu cha Africans and Americans. Elimu hii kama ingefanyika ipasavyo, ingetuepushia matatizo yaliyojitokeza wakati wa Mwalimu Nyerere, na pia ingepunguza jazba ambazo bado zipo kuhusiana na suala la kulishwa Yanga.
Wednesday, January 19, 2011
Andika ki-Swahili; ki-Ingereza Hatuelewi
Kuna tabia katika jamii ya wa-Tanzania ya kulalamika pale mtu anapoandika ki-Ingereza. Malalamiko haya yanaonekana mara kwa mara katika blogu ya Michuzi, kwa mfano, ambayo inasomwa sana na wa-Tanzania, pale inapotokea makala iliyoandikwa kwa ki-Ingereza.
Walalamikaaji wanakumbushia kuwa wa-Tanzania wengi hawajui ki-Ingereza, na kwa hivi wanataka mwandishi awafikirie hao kwa kuandika kwa ki-Swahili, lugha wanayoifahamu. Ujumbe unaojitokeza katika malalamiko hayo ni kwamba ni jambo la uzalendo kwa mwandishi kuwafikiria hao wa-Tanzania walio wengi, ili nao wapate kufaidika na yale yanayoandikwa.
Sijawahi kuona malalamiko hayo yakipingwa. Inaonekana kuwa hoja inayotolewa katika malalamiko hayo inakubalika miongoni mwa wa-Tanzania.
Katika kulitafakari suala hili, naona kuna haja ya kuwakosoa hao walalamikaji. Ingawa ni kweli kuwa mtu akiandika kwa ki-Swahili anawafikia wananchi wasiojua ki-Ingereza, kuna pia tatizo la uvivu katika jamii yetu.
Malalamiko hayo ni sehemu ya tatizo hili la uvivu ambalo naliongelea tena na tena katika blogu hii na zingine, na pia katika maandishi mengine. Wa-Tanzania wanapenda kutafuta visingizio na kuwalaumu wengine. Kwa nini wa-Tanzania waridhike na hali yao, ya kujua ki-Swahili tu, badala ya kujifunza lugha zingine?
Kama wa-Tanzania wanataka kudekezwa, ni bora wajue kuwa dunia hii ya ushindani haidekezi mtu. Wasipojituma katika masuala ya elimu, ikiwemo elimu ya lugha mbali mbali, sio tu watabaki nyuma, bali wataumia. Mawasiliano ya kimataifa yatakuwa mtihani mkubwa ambao watashindwa. Mikataba ya nje watashindwa kuielewa.
Wakati huu tunanyoosheana vidole kutokana na mikataba tunayohisi waTanzania wenzetu wanaisaini kifisadi. Lakini, kwa jinsi tunavyoendekeza uvivu ninaoongelea, tutaendelea kusaini mikataba mibovu kwa kutojua lugha. Nchi itaendelea kuumia.
Hata kama watu hawana vitabu, kuna maktaba katika miji mbali mbali. Mtu yeyote anaweza kujipangia utaratibu wa kwenda kusoma vitabu vilivyomo, akajiongezea angalau ufahamu wa ki-Ingereza. Lakini wa-Tanzania wako radhi kukaa kwenye kijiwe nje ya maktaba, siku hadi siku, wiki hadi wiki, mwezi hadi mwezi, mwaka hadi mwaka, bila kuingia humo maktabani. Hili ni tatizo kubwa katika nchi yetu.
Walalamikaaji wanakumbushia kuwa wa-Tanzania wengi hawajui ki-Ingereza, na kwa hivi wanataka mwandishi awafikirie hao kwa kuandika kwa ki-Swahili, lugha wanayoifahamu. Ujumbe unaojitokeza katika malalamiko hayo ni kwamba ni jambo la uzalendo kwa mwandishi kuwafikiria hao wa-Tanzania walio wengi, ili nao wapate kufaidika na yale yanayoandikwa.
Sijawahi kuona malalamiko hayo yakipingwa. Inaonekana kuwa hoja inayotolewa katika malalamiko hayo inakubalika miongoni mwa wa-Tanzania.
Katika kulitafakari suala hili, naona kuna haja ya kuwakosoa hao walalamikaji. Ingawa ni kweli kuwa mtu akiandika kwa ki-Swahili anawafikia wananchi wasiojua ki-Ingereza, kuna pia tatizo la uvivu katika jamii yetu.
Malalamiko hayo ni sehemu ya tatizo hili la uvivu ambalo naliongelea tena na tena katika blogu hii na zingine, na pia katika maandishi mengine. Wa-Tanzania wanapenda kutafuta visingizio na kuwalaumu wengine. Kwa nini wa-Tanzania waridhike na hali yao, ya kujua ki-Swahili tu, badala ya kujifunza lugha zingine?
Kama wa-Tanzania wanataka kudekezwa, ni bora wajue kuwa dunia hii ya ushindani haidekezi mtu. Wasipojituma katika masuala ya elimu, ikiwemo elimu ya lugha mbali mbali, sio tu watabaki nyuma, bali wataumia. Mawasiliano ya kimataifa yatakuwa mtihani mkubwa ambao watashindwa. Mikataba ya nje watashindwa kuielewa.
Wakati huu tunanyoosheana vidole kutokana na mikataba tunayohisi waTanzania wenzetu wanaisaini kifisadi. Lakini, kwa jinsi tunavyoendekeza uvivu ninaoongelea, tutaendelea kusaini mikataba mibovu kwa kutojua lugha. Nchi itaendelea kuumia.
Hata kama watu hawana vitabu, kuna maktaba katika miji mbali mbali. Mtu yeyote anaweza kujipangia utaratibu wa kwenda kusoma vitabu vilivyomo, akajiongezea angalau ufahamu wa ki-Ingereza. Lakini wa-Tanzania wako radhi kukaa kwenye kijiwe nje ya maktaba, siku hadi siku, wiki hadi wiki, mwezi hadi mwezi, mwaka hadi mwaka, bila kuingia humo maktabani. Hili ni tatizo kubwa katika nchi yetu.
Thursday, December 30, 2010
Utamaduni na Utandawazi: Tunawafahamu wa-Turuki?

Wasomaji wa blogu zangu wanafahamu kuwa suala la utamaduni na utandawazi ni moja ya masuala ninayoyatafakari sana. Ninaelezea umuhimu wa suala hili kwa namna ya pekee katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii.
Dhana ya utamaduni ina maana nyingi, na ni muhimu kwa mtumiaji wa dhana hii kuelezea anaitumia kwa maana ipi. Ili nieleweke vizuri na kiurahisi, singependa kuleta nadharia na mambo ya kufikirika. Badala yake, nimeamua kuuliza suali: Tunawafahamu wa-Turuki?
Leo hii, Tanzania na u-Turuki zinajenga uhusiano kwa kiwango ambacho hatujawahi kuona kabla, katika nyanja kama biashara, utalii, na elimu. Shirika la ndege la u-Turuki linapiga hatua katika kuimarisha safari baina ya Tanzania na u-Turuki. Ni wazi kuwa watu wa nchi hizi mbili wataendelea kuwa na mahusiano ya karibu katika nyanja mbali mbali.
Kama ninavyosema mara kwa mara, naamini kuwa mahusiano yoyote baina ya watu wa tamaduni mbali mbali yanaathiriwa moja kwa moja na tofauti za tamaduni hizo. Ndio maana ninauliza iwapo tunawafahamu wa-Turuki.
Sambamba na kuanzisha uhusiano na watu wa utamaduni tofauti na wetu, kuna umuhimu wa kujielimisha. Jambo moja ni kusoma vitabu. Nikiendelea na mfano huu wa u-Turuki, kuna waandishi maarufu wa ki-Turuki, kama vile Nazim Hikmet na Orhan Pamuk, ambaye alipata tuzo ya Nobel mwaka 2006. Kuna masimulizi ya kale, kama yale ambayo mhusika wake ni Nasreddin Hodja, maarufu kwa wa-Turuki na wasomaji wengine duniani.
Kwa miaka kadhaa nilifahamu kuhusu utungo maarufu unaojulikana kama The Book of Dede Korkut. Nilinunua nakala, lakini sikupata fursa ya kuisoma. Wiki hii nimeanza kuisoma, nikiwa nimesukumwa na hili suala la kukua kwa uhusiano baina ya Tanzania na u-Turuki. Lakini vile vile ni kwa sababu nimeamua kufundisha kitabu hiki katika kozi ya fasihi nitakayofundisha kuanzia wiki ijayo.
Kama nilivyotegemea, kitabu hiki ni hazina kubwa na njia nzuri ya kuwafahamu wa-Turuki: mtazamo wao wa maisha na mahusiano ya jamii, maadili yao na kadhalika. Kitabu hiki ni maarufu duniani. Wenzetu wa Brazil kwa mfano, ambao tunawaona kama rafiki zetu, wanakienzi kitabu hiki. Soma hapa.
Katika makala hii, juu ya kupokelewa kwa tafsiri ya The Book of Dede Korkut Brazil, tunaona wenzetu wanavyoelewa umuhimu wa kujisomea vitabu ili kujenga maelewano na watu wa nchi zingine na kuboresha mahusiano. Ni elimu ambayo inatufaa sote, kuanzia wafanya biashara, wadau wa elimu, diplomasia, utalii na kadhalika. Hayo ni baadhi ya mambo muhimu ninayomaanisha ninapoongelea suala la utamaduni na utandawazi.
Ingawa nimewataja wa-Turuki, siwaongelei wao tu. Tujiulize kama tunawafahamu wa-Hindi, wa-Australia, wa-China, wa-Marekani, wa-Rusi, na kadhalika. Jambo la kuzingatia ni kuwa dunia ya utandawazi wa leo inakuja na mitego na mitihani mingi, si ya kuivamia kichwa kichwa, bila elimu.
Sunday, December 19, 2010
Kitabu Kimetua St. Cloud, Minnesota

Nafanya shughuli hizi si kwa ajili ya kutafuta umaarufu, bali naamini ni wajibu kwa wanadamu kusaidiana katika maisha na kuifanya dunia iwe bora kuliko ilivyo.
Miezi ya karibuni nimejishughulisha sana na matatizo yanayowapata wahamiaji wa ki-Somali katika jimbo la Minnesota, ambalo linaongoza kwa idadi ya wahamiaji wa ki-Somali. Wasomaji wa blogu zangu watakumbuka taarifa za shughuli zangu katika mji wa Faribault.
Matatizo kama haya ya Faribault yako pia katika miji mingine, kama vile St. Cloud. Kutokana uzoefu nilioupata Faribault, nimeanzisha mawasiliano na ndugu Mohamoud Mohamed, mkurugenzi wa SASSO, jumuia inayoshughulikia masuala ya wa-Somali mjini St. Cloud.
Nilimpelekea nakala ya kitabu cha Africans and Americans, kama mchango wangu na changamoto. Jana ameniambia kuwa kitabu amekipata, anaendelea kukisoma, na anakipenda. Atawaonyesha wadau wa St. Cloud: halmashauri ya mji, shule na vyuo, idara ya polisi, mahospitali, na kadhalika. Nami nilimhakikishia kuwa ni jambo bora. Badala ya watu kununiana tu au kugombana, ni vema wakaanza utaratibu wa kuzungumzia matatizo kama ilivyofanyika Faribault, na ikapokelewa vizuri.
Kama ninavyosema katika mihadhara, blogu na maandishi mengine, matatizo ya aina hii yanayoikumba miji ya Faribault na St. Cloud yanajitokeza katika miji na jamii nyingine duniani: Afrika, Asia, Australia, Marekani, Ulaya, na kwingineko, na yataongezeka, kutokana na mwenendo wa utandawazi wa leo. Ninapokuwa Dar es Salaam, kwa mfano, nasikiliza na kutafakari minong'ono na majungu kuhusu wa-China, ambao wanaendelea kuja katika mji ule. Niliwahi pia kuongelea tafrani iliyotokea Zanzibar. Kinachobaki ni sisi kujizatiti kwa kuelimishana kuhusu tofauti zetu na kutafuta namna ya kuishi bila matatizo.
Najiandaa kushiriki katika masuala ya St. Cloud. Mbali ya umuhimu wake kwa jinsi hali ilivyo, ni fursa ya mimi kujiongezea ujuzi na uzoefu nitakaoutumia katika kuwasaidia wengine.
Monday, October 4, 2010
Mahojiano Yangu "Kombolela Show"
Tarehe 2 Oktoba, nilihojiwa katika "Kombolela Show." Hiki ni kipindi cha redio kinachoendeshwa na Jaduong Metty, ambaye pia ni mmiliki wa blog ya Metty's Reflections. Kusikiliza mahojiano, bofya hapa au hapa
Wednesday, September 29, 2010
Programu za Kupeleka Wanafunzi Tanzania
Tunafanya hivyo mara moja kwa mwaka.
Pamoja kazi yangu ya kufundisha katika idara ya ki-Ingereza hapa St. Olaf, ninashughulika katika program zinazopeleka wanafunzi nchi za ki-Afrika, ikiwemo Tanzania. Nimefanya shughuli hii kwa miaka yote niliyofundisha hapa ughaibuni, katika programu kama LCCT, ACM Tanzania, na ACM Botswana. Leo nilijipanga kwenye meza kama inavyoonekana katika picha, nikingojea wanafunzi, nimwage sera.
Saturday, June 5, 2010
Warsha Zangu Hazina Posho
Tangu mwaka juzi, nimeendesha warsha Tanzania, kuhusu masuala ya utamaduni, utandawazi, na maendeleo. Nina malengo kadhaa katika kufanya hivyo.
Lengo moja ni kuwapa wa-Tanzania ujuzi ambao ninaendelea kuupata huku ughaibuni, kutokana na kusoma vitabu, kuongea na watu, na kuendesha warsha kuhusu masuala niliyotaja hapo juu. Natambua umuhimu wa kutoa fursa kwa wa-Tanzania kuyaelewa masuala hayo, waweze kujizatiti kwa ushindani wa dunia ya leo. Hakuna msingi bora na imara kuliko elimu.
Lengo la pili la kuendesha warsha hizi Tanzania ni kuleta mwamko mpya katika mfumo na uendeshaji wa warsha. Kwanza, kuna mtindo wa kutegemea wafadhili. Watu wamezoea kuona warsha zikifanyika kwa kutegemea fedha kutoka kwa wafadhili au taasisi fulani. Wahudhuriaji wa warsha wanategemea kulipiwa gharama za ushiriki, pamoja na posho. Vibahasha vya posho ni sehemu ya utamaduni wa warsha katika Tanzania.
Ninapinga utamaduni huu. Sitafuti wafadhili wa kulipia warsha zangu, na warsha zangu hazina posho. Badala yake, wanaohudhuria wanalipia.
Kwa mtazamo wangu, warsha ni fursa ya kujielimisha. Elimu ni mtaji mkubwa, pengine muhimu kuliko mitaji yote. Kama mtu analipia trekta limzalishie mazao shambani, kwa nini asilipie mtaji huu mkubwa kuliko yote, yaani elimu?
Huku Marekani, ninaona utaratibu huu wa kulipia warsha. Mimi mwenyewe nimeshalipia hela nyingi kuhudhuria warsha hizi. Ninajua umuhimu wake. Niligusia kidogo jambo hili katika blogu hii, nilipoongelea suala la kununua vitabu.
Ninanunua pia vitabu na kuvisoma. Kati ya vitabu nilivyonunua hivi karibuni ni Global Literacies. Kwa kusoma vitabu na kuhudhuria warsha, ninajiongezea mtaji wa elimu. Ufanisi wangu kama mtoa mada na mwendesha warsha unaendelea kuongezeka.
Katika kuendesha warsha zangu Tanzania, nataka kujenga utamaduni wa kuthamini elimu. Msimamo huu unanipa wajibu mkubwa. Nawajibika kujielimisha kwa uwezo wangu wote, ili niweze kuwa mwelimishaji bora. Ndio maana ninafanya bidii kuhudhuria warsha, kununua vitabu na kuvisoma, na pia kuendesha warsha. Ninaelimika hata ninapoendesha warsha.
Nawakaribisheni kwenye warsha zangu za mwaka huu:
Juni 12, "Culture, Globalization and Development," Meeting Point Tanga.
Julai 3, "Culture and Globalization," Arusha Community Church.
Julai 10, "Cultural Tourism," Arusha Community Church.
Natarajia kupanga warsha nyingine moja au mbili. Wasiliana nami: info@africonexion.com
Lengo moja ni kuwapa wa-Tanzania ujuzi ambao ninaendelea kuupata huku ughaibuni, kutokana na kusoma vitabu, kuongea na watu, na kuendesha warsha kuhusu masuala niliyotaja hapo juu. Natambua umuhimu wa kutoa fursa kwa wa-Tanzania kuyaelewa masuala hayo, waweze kujizatiti kwa ushindani wa dunia ya leo. Hakuna msingi bora na imara kuliko elimu.
Lengo la pili la kuendesha warsha hizi Tanzania ni kuleta mwamko mpya katika mfumo na uendeshaji wa warsha. Kwanza, kuna mtindo wa kutegemea wafadhili. Watu wamezoea kuona warsha zikifanyika kwa kutegemea fedha kutoka kwa wafadhili au taasisi fulani. Wahudhuriaji wa warsha wanategemea kulipiwa gharama za ushiriki, pamoja na posho. Vibahasha vya posho ni sehemu ya utamaduni wa warsha katika Tanzania.
Ninapinga utamaduni huu. Sitafuti wafadhili wa kulipia warsha zangu, na warsha zangu hazina posho. Badala yake, wanaohudhuria wanalipia.
Kwa mtazamo wangu, warsha ni fursa ya kujielimisha. Elimu ni mtaji mkubwa, pengine muhimu kuliko mitaji yote. Kama mtu analipia trekta limzalishie mazao shambani, kwa nini asilipie mtaji huu mkubwa kuliko yote, yaani elimu?
Huku Marekani, ninaona utaratibu huu wa kulipia warsha. Mimi mwenyewe nimeshalipia hela nyingi kuhudhuria warsha hizi. Ninajua umuhimu wake. Niligusia kidogo jambo hili katika blogu hii, nilipoongelea suala la kununua vitabu.
Ninanunua pia vitabu na kuvisoma. Kati ya vitabu nilivyonunua hivi karibuni ni Global Literacies. Kwa kusoma vitabu na kuhudhuria warsha, ninajiongezea mtaji wa elimu. Ufanisi wangu kama mtoa mada na mwendesha warsha unaendelea kuongezeka.
Katika kuendesha warsha zangu Tanzania, nataka kujenga utamaduni wa kuthamini elimu. Msimamo huu unanipa wajibu mkubwa. Nawajibika kujielimisha kwa uwezo wangu wote, ili niweze kuwa mwelimishaji bora. Ndio maana ninafanya bidii kuhudhuria warsha, kununua vitabu na kuvisoma, na pia kuendesha warsha. Ninaelimika hata ninapoendesha warsha.
Nawakaribisheni kwenye warsha zangu za mwaka huu:
Juni 12, "Culture, Globalization and Development," Meeting Point Tanga.
Julai 3, "Culture and Globalization," Arusha Community Church.
Julai 10, "Cultural Tourism," Arusha Community Church.
Natarajia kupanga warsha nyingine moja au mbili. Wasiliana nami: info@africonexion.com
Subscribe to:
Posts (Atom)
Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault
Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...

-
Leo ni kumbukumbu ya siku ya kuzaliwa kwangu, ambayo ni tarehe 17 Agosti, 1951. Familia yangu, ndugu, na marafiki wamejumuika nami kushereh...
-
Kutafsiri kazi ya fasihi ni kazi ngumu ya kuchemsha bongo. Inahitaji ufahamu wa hali ya juu wa lugha husika, na pia hisia makini za kifasih...
-
Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...